RIWAYA: Mkakati wa kuelekea Ikulu

RIWAYA: Mkakati wa kuelekea Ikulu

SEHEMU YA KUMI NA NANE

Habari hizi ambazo wengi ziliwaacha midomo wazi,
baadhi wakishika vichwa kutoamini wakisikiacho,
kwa Masurufu zilikaribia kuondoka na roho yake
kwa kuwa alijikuta akishikwa Shinikizo la damu
baadae kizunguzungu kikali kabla hajaanguka chini
na kuzirai ambapo alikimbizwa hospitali ya Ocean
Road zilikoanza juhudi za kuokoa maisha yake.
Habari za ugonjwa wake zikatakiwa kuwa siri
kubwa hata watumishi wake ofisini hawakujua
yupo wapi!
* * ***********

Malumbano haya baina ya John Tengeneza na Dr.
Masurufu ambayo wengine hawakuyatilia uzito
sana yakawa yamempatia uhakika Samson wa ile
hofu iliyokuwa ikimkabili. Hofu kwamba uchaguzi
huu ulikuwa na jambo zaidi ya uchaguzi.
Awali kabla ya malumbano haya ya Tengeneza na
Masurufu, alikuwa amewatembelea kwa siri
wagombea Urais wasiopungua sita kwa kuwatumia
vijana wake shupavu. Michael na Raymond. Akawa
amejua mambo kadha wa kadha kuwahusu.
Mambo ambayo pia hakuona kama yalikuwa na
athari hasi kwa taifa.
Mgombea ambaye alikuwa amemvutia alikuwa Dr.
Masurufu Huyu alimvutia kwa jinsi alivyoishi kama
kinyonga kwa kuudanganya umma mahala
anakolala.Awali alikuwa amefikiria kwamba
Masurufu anafanya haya kwa sababu za
kiusalama, hii ni kwa vile alifika zaidi ya mara
moja katika maeneo yake na kutoona hitilafu
yoyote.
Kuibuka kwa madai ya Masurufu dhidi ya
Tengeneza na baadae ya Tengeneza dhidi
Masurufu kukawa kumeifanya hofu yake itimie.
Kwamba staili ya kinyonga ya Dr Masurufu ilikuwa
inalenga kuficha mambo ambayo baadhi
yametajwa na Tengeneza
Kama mpelelezi anayotegemewa na serikali,
Samson Kidude aliona kuwa anawajibika kutafuta
uthibitisho wa madai hayo ya Masurufu kama
ambavyo alikuwa anahitimisha kupata ushahidi wa
Tengeneza, ili mwisho wa siku aweze kuwakabidhi
katika vyombo vya usalama wakapate malipo ya
uhalifu wao.
Haraka akainua simu na kuwaita vijana wake
machachari Raymond Kalolelo na Michael
Kilibhaha, ambapo walifika ndani ya dakika kumi.
“Nimewaita kwa kazi moja ya haraka!” Samson
akawaambia mara waliopoingia na kuketi. “Kazi
ambayo nitapenda muifanye kwa uwezo wenu
wote!” Akatua na kuwaruhsia nakala za magazeti
yenye habari za Dr Masurufu.
Wakiwa wameshazisoma habari hizo tayari, Ray na
Michael walizipitia tena haraka haraka kabla
hawajayatua magazeti kando na kumtumbulia
macho Samson, macho yao yakidai maelezo zaidi!
“Nahitaji uthitibitisho wa madai hayo!” Samson
akasema kama aliyeyasoma macho hayo.
“Ikiwezekana na ushahidi kabisa. Wakati nyie
mnafanya hayo, mie nakwenda kumbana
Tengeneza anieleze alikoyatoa madai haya mazito.
Natumai ipo cheni ndefu nyuma yake. Cheni
ambayo itatuongoza hadi penye mzizi wa tatizo
ambapo tutaufukua na kuondoa utata kabisa.
Naomba mwenye swali aulize!” Akatua.
Yafuatia maswali madogo madogo tu kama
Masurufu aliishi wapi, mahala anakofanyia kazi
familia na kadha wa kadha maswali ambayo
Samson aliyajibu vizuri tu kwa kuwa alikuwa
amemtembelea mara mbili na aliyajua fika
mazingira ya Dr. Masurufu.
“Raymond!” Samson akaita waliposimama tayari
kwa kuondoka. Raymond akamuangalia.
“Ingawa Dr Masurufu amepata kuwa mwanajeshi,
sitarajii kama mtapata upinzani wa maana hasa
ukizingatia alivyoacha madaraka yamlevye na
kumjaza mafuta mwilini kitambi kikiwemo, Naomba
mjihadhari na muwe makini!”
Ray na Michael wakatabasamu. Moyoni
wakifarijika kuona Samson anavyojali maisha yao
“Usihofu kaka!” wakageuka na kuondoka.
Mazungumzo mafupi waliyoyafanya yakawafanya
waifuate moja ya kanuni ya kazi zao.
Kutoongozana kama maandazi.
Wakagawana
Raymond akaelekea ofisini kwa Dr Masurufu wakati
Michael akaelekea nyumbani kwake. Kila mmoja
alisisimkwa na mwili jambo lililowaashiria kuwa
walikuwa wanaingia kazini rasmi!
* * *
Dr Masurufu alizinduka masaa machache baada ya
madaktari kumaliza kumtibu na kuondoka baada
ya kuitaka familia yake kutomsumbua. Glady
mkewe aliyekuwa akiombea mumewe aamke,
akamsimamia kumkabili mithili ya jini la kutumwa.
Habari alizozipata toka kwa wapambe wa Dr.
Masurufu ambao nao walikuwa mapandikizi ya
John Tengeneza; kuwa Dr. Masurufu alikuwa na
nyumba ndogo tofauti na yeye na kwamba ndiyo
iliyokuwa ikishirikishwa katika mipango yote
zilikuwa zimemchanganya vibaya hata akose simile
na busara za kawaida za mwanadamu.
“Niko wapi Hapa?” Masurufu akauliza. Glady
akamtazama kwa jicho la chuki na kumjibu, “Uko
hospitali! Umeponea chupu chupu na tabia yako ya
kuficha ficha!.”
“Kuficha ficha?! Mungu wangu, kumejiri kitu gani
tena!” Masuruf akaweweseka akili yake ilikuwa
bado hajaweza kuunganisha mambo sawa sawa na
alikuwa akijitahidi kukumbuka mambo kwa uwezo
wa hali ya juu.
“Kimejiri kitu gani?! Subiri tu. Na polisi wataanza
kukutafuta sasa hivi!” Akapumua kwa hasira!
“Lakini Mama Masurufu…!” Steve mlinzi wao
ambaye alikuwa kimya muda wote akaingilia, “…
ungemuacha kwanza aji…!”
“Shut up you Idiot!” Glady akakemea.
Likawa jibu lililomkera Steve. Akaruka kutoka
alipokuwa mpaka kwa Mama Masurufu, “Je,”
Akamuuliza kwa hasira baridi, “unawezaje kunijibu
kijeuri hali hukuniajiri wewe?”
“I don’t care!”
“Hujali siyo? Haya toka nje!”
“Sitoki!”
“Tokaah!!”
“Sitoki nakwambia!”
“Basi utatoka tu!” Steve akamshika mikono na
kuanza kumvuta atoke nje. Ikatokea purukushani
kidogo mpaka Dr Masurufu alipmkataza amri Steve
kwa sauti dhaifu, ndipo alipomuachia na wote
wakabakia wakihema kama madume ya bata
yaliyotoka kupigana.
“Ahsante sana Masurufu!” Akaanza mkewe
Masurufu akihema “Unanificha hata mie? Mimi
mimi?!” Akajipigapiga kifuani eneo ulipo moyo na
kuangua kilio. Kilio kikuu. Masurufu akashangaa
maajabu haya. Swali likamtoka! “ Nimekuficha nini
mpenzi wangu?”
“Hebu toka hapa na Unafiki waka, nani mpenzio?
Ningekuwa mpenzio ungeweza kufanya uliyofanya
bila walau kunijulisha? Mbona mimi ni mkeo?
Liwazo la moyo wako, mama wa watoto wako?
Mangapi nimeweza kuyaficha na kuyatunza hadi
leo tuko hapa?”
“Bado sijakuelewa mama Rose?”
“Unanielewa vizuri sana, kwani nini umemtuma
Steve anifukuze? Sawa, sistahili kuwa na wewe.
Kwa sababu unakwenda kuwa rais wa Tanzania.
Na Rais hapaswi kuwa na mke mshamba
mshamba kama mimi si ndiyo?, Nashukuru sana.
Nashukuru sana Masurufu!” Glady akatua na kulia
tena.
Masurufu akaendelea kushangaa kwa dhati,
asielewe chochote.
“Usijitie kushangaa wakati umefanya tambiko na
upuuzi wako mwingine bila kuniambia. Umeingia
hata katika malumbano ya kijinga na kipuuzi
mpaka kufikia hatua ya kumwaga damu pasipo
kunishauri. Kwa akili zako finyu wadhani ndio
wapalilia Barabara yako ya Ikulu. Vyema sana!
Nenda salama. Najua sina thamani tena kwako na
ndio maana umepata mwanamke mwingine
ambaye kwako wadhani anastahili kuwa mkeo na
First Lady pindi ukiwa Rais.
Hongera kwa hilo, Ila kwa kuwa umemwaga mboga
mie namwaga ugali. Nakwenda kuwa upande wa
John Tengeneza na ninajua kwa taarifa zilizotoka,
polisi watataka kukutembela. usijidanganye
kwamba nitawaficha, nitawaeleza ukweli mtupu
ikiwa ni pamoja na kuwasaidia kukwamisha ndoto
zako.
Kama hiyo haitoshi nitawaeleza juu ya mkakati
wako na mkataba uliofanya na akina Chris halafu
tuone kama hayo unayoyataka yatatimia shenzi
Taip!!”
Mama Masurufu akahitimisha na kuondoka kwa
kasi kweli!
“Mama Roseeeh…!” Masurufu akaita kwa taabu.
Alikuwa ameogopa kwelikweli “Mama Dani…, mke
wanguuuh!” Mkewe hakumsikia na pengine
alimdharau. Ilikuwa wakati huu Glady alipoufikia
mlango, akaufungua kwa nguvu kabla hajaubamiza
kwa hasira nyuma yake hali sauti ya “Sitakiih!”
Ikiwafikia kwa taabu.
Masurufu akasikia mapigo ya moyo yakipanda tena
kwa kasi hali pumzi zikimpaa “Nii…nii…niitie
daktari...!” Akafaulu kusema kwa taabu na
kuongeza, “Na…na… umzuie …umzuie Glady asilete
madhara……madhara!”
***Ama hakika Ikulu si mchezo! Masurufu atafika
kweli ikulu huyu!!!
 
SEHEMU YA KUMI NA TISA
Masurufu akasikia mapigo ya moyo yakipanda tena
kwa kasi hali pumzi zikimpaa “Nii…nii…niitie
daktari...!” Akafaulu kusema kwa taabu na
kuongeza, “Na…na… umzuie …umzuie Glady asilete
madhara……madhara!”
Kitendo bila kuchelewa Steve akaruka nje, dakika
ya pili akarejea na Daktari na kukuta Dr Masurufu
ameshazirai tena.
Wakati daktari ameanza kumshughulikia Dr.
Masurufu, Steve alikuwa ndani ya Toyota
Landcruiser VX akipangua gia na kukanyaga
mafuta mpaka alipofika katika mtaa ya Ohio
ambapo aliliona Toyota Nissan gari la Glady
Stevenson Ombwe, mke wa Dr Masurufu likiacha
barabara ya Bibi titi na kuchukua ile ya Ally
Hassani Mwinyi.
Akaiandama kwa busara kwa kuacha magari
kadhaa mbele yake safari yao iliishia Mbezi Beach
nyumbani kwa Dr Masurufu, ambako Glady
alishuka na kuingia ndani kama mtu
aliyechangikiwa haswaa.
“Sitaki mtu anibughudhi kabisa!” Mama Masurufu
aliwaambia wafanyakazi wa ndani wakati
akipitiliza ndani alikoingia na kuanza kulia.
Steve aliipaki gari yake pembeni ya gari ya Mama
Masurufu naye akashuka na kuingia.
“Mama amesema hataki kusumbuliwa na mtu
yoyote!” Eliza mtumishi wa ndani alikuwa
amekumbuka kumwambia Steve mara alipomuona
akielekea chumbni kwa Mama Masurufu. Kauli
iliyomfanya Steve asimame na kutengeneza
tabasamu.
“Oh! sorry” Akasema kama aliyekumbuka kitu.
“Mama hajisikii vizuri, mie nataka nikachukue cheti
nikamnunulie dawa!” Akawaambia.
“Ohh! Kumbe!” Alikuwa Eliza kwa unyenyekevu
“Samahani, unaweza kuendelea!”
“Msijali!”
Steve akaingia ndani alikochukua dakika chache tu
zilizotosha kumfaya Glady asiwe na madhara wala
tishio kwa Dr Masurufu.
* * *
Sekunde chache baadae, Michael naye alikuwa
anapaki gari katika viunga vya Dr Masurufu pale
Mbezi Beach pembeni ya gari ya Steve na Glady.
Akashuka akaukabili mlango na kubonyeza
kengele.
“Karibu!” Eliza aliitika na kwenda kufungua mlango
tena. “Karibu! Karibu ndani!” Akamkaribisha zaidi.
“Ahsante!” Michael akaingia ndani “Naitwa Michael
ni mwandishi wa Habari, natokea Daily News!”
Michael akatua na kutoa kitambulisho, akampa
kitambulisho Eliza huku macho yake ya kazi
yakisawiri hapa na pale kwa kasi ya ajabu.
“Shikamoo!” Alikuwa Eliza tena baada ya Michael
kuketi na kumrejesha kitambilisho.
“Marahaba!
“Utakunywa nini? Soda, Juisi, Maji au kahawa?”
“Ahsante. Baba yuko wapi? Nina shida na baba
kwanza. Nilikuwa ofisini nikaambiwa yuko
nyumbani! Niitie nizungumze nae!”
“Baba hayupo! Na hutaweza kuzungumza nae
kabisa!”
“Kwa nini?” Michael akauliza kwa pupa na kihoro
“Kuna mambo yalitokea. Sijui mambo gani vile,
baba akawa ameshikwa na Presha na kukimbizwa
hospitali. Wakati fulani mama alitupigia simu
kwamba anaendelea vizuri. Labda atatoka
baadae!”
“Oooh! Poleni sana!”
“Ahsante Tumeshapoa! Michael akavuta tafakuri
akijaribu kuhusianisha presha ya Dr Masurufu na
zile habari za Ufisadi. Inaweza kuwa sababu?
Akajiuluza kabla hajajirudi kuwa jibu la swali hilo
liko kwa Masurufu. Akamtazama tena Eliza na
kumuuliza
“Je amelazwa hospitali gani?”
“Nilisikia wanasema kama Ocean Road vile?! Sina
hakika lakini.”
Wakati Eliza anajibu hivi, mlango wa chumba cha
kulala wa cha Dr. Masurufu ukafunguliwa na Steve
akatoka akiwa ameisikia Ocean Road Vizuri kabisa.
Kwa sekunde kadhaa wakatazamana kila mmoja
akimsoma mwenzake. Michael alipoona muda
unapita pasipo kutambulishwa akasimama na
kusema “Ahsante Eliza, Nitarudi tena baadae.
Mzee atakapotoka Hospitali!”
“Haya!”
Michael akamtupia jicho Stevu na kumuaga kwa
kusema “Kaka Ahsante”
Steve akanyanua kichwa kukubali. Michael
akatoka. Steve akamkabili Eliza na kumkazia
macho mpaka Eliza akaogopa. “Yule nani”
Akamuuliza.
“Ni mwandishi wa habari wa Daily News!”
“Amekuja kufanya nini?”
“Anataka kuzungumza na baba, nikwamwambia
baba anaumwa yuko hospitalini Ocean Road.”
“Kwanini umemwambia yuko Ocean Road? Nani
alikutuma kusema hivyo?”
Eliza akatetemeka asijue la kusema. “Nisamehe
kaka, sikujua!”
“Pumbavu!” Steve akabweka kwa ghadhabu.
“Usirudie tena mchezo huu sawa? Hujui kama
mzee ana maadui wengi na wanaweza kumdhuru?
Ukome kabisa!”
“Ndiyo kaka!” Alikuwa Eliza tena kwa woga. Steve
akamuaru awaite wafanyakazi wote sita wa kasri
hilo, Wakaitwa! Walipatikana wanne, wengine
walikuwa nje ya nyumba kikazi.
Steve akawaonya wasithubutu tena kutoa habari
za Dr Masurufu na kwamba atakayejaribu atakiona
cha moto. Akawaacha wameduwaa na kutoka
sekunde chache baadae akarudi na kuwaambia
tena
“Mama amepumzika. Msimsumbue hata kidogo!
Muacheni mpaka atakapoamka mwenyewe Sawa?!”
“Sawa!”
Akatoka na kuingia chumba chake cha kazi
alikojipanga kwa muda mfupi sana kabla
hajapanda gari na kurudi Ocean Road Hospitali
kwa Dr Masurufu.
* * *
Njiani Michael alimpigia simu Raymond na
kumtaka aje Ocean Road Hospitali kwamba Dr
Masurufu alikuwa amelazwa huko baada ya
kushikwa na presha.
“Nashukuru kaka, maana ilibaki sentimita chache
niingine ofisini kwake! Usijali nitakuwa nawe baada
ya muda mfupi tu!”
“Uje bwana, kuna njemba imenitia shaka pale
nyumbani kwa Dr Masurufu! Nataka tuijadili kwa
kina maana Samson hakuwahi kusema kama pale
kuna mtu wa ziada. Na yule jamaa haelekei kuwa
house boy!”
“Unataka kusema umetoka msambweni?”
“Hapana. Ila angalia yake kwangu kama jasusi
fulani hivi! Kama vile hakufurahia mie kwenda
pale!”
“Nakuja, tutaongea mengi nikifika!
“Poa!”
Ray akakata simu. Michael akampigia Samson na
kumpa taarifa hizo, Samson akampongeza na
kumtaka aendelee. Ulikuwa mwanzo mzuri.
Hakupata taabu kuiona wodi aliyolazwa Dr
Masurufu, vile alikuwa Maarufu pale hospitali, na
vile alizijua wodi za watu mashuhuri maarufu
kama VIP; Michael alipitiliza moja kwa moja
mpaka katika vyumba hivyo ambapo alianza
kuingia chumba kimoja baada ya kingine.
Chumba cha tatu akawa amekutana na Daktari
aliyekuwa akimaliza kumtibu Dr Masurufu “Ohh
Michael!” Daktari akaita na kuongeza. “Hujambo?”
“Sijambo kabisa! Haya niambie Dokta Makete,
Shikamoo Kwanza!”
“Marahaba. Vipi, huyu mtu wetu nini? Maana nyie
mkionekana mahala kuna jambo!” Akauliza Dr
Makete, mzee mwenye miaka hamsini hivi ambaye
naye alikuwa mtu wa usalama
“Ni mtu wetu Dokta! Kama uvujuavyo ni mmoja wa
wagombea habari zake ndizo zinazotamba.
Tumenusa kitu kumhusu na ndio maana tuko
hapa!”
“Ooh! Vizuri!”
“Uhakikishe anapona!”
“Hilo halina shaka.
“Na je, Itamchukua muda gani kuamka?”
“Kama masaa sita hivi. Huu mshtuko wa mara ya
pili ndio umekuwa mbaya maana alikwishapata
nafuu kabisa, haiweleweki ni kitu gani
kilichomshitua tena na kumtia hatarini. Wengine
wanaposhtuka hivi huwa wanapoteza maisha
kabisa!”
Ukimya mfupi ukapita wakati Dr. Makete
akimpachika dripu ya maji, alipohakikisha
yanaenda vizuri akamuuliza Michael.
“Sasa?”
“Nahitaji kufanya kazi kidogo, then nitarejea baada
ya hayo masaa sita atakapokuwa amerejewa na
fahamu zake!”
“Haina Shida!” Makete akakubali na kutoka.
Michael akaanza upeke upeke wake. Alikagua
hapa, akapachika hiki pale kabla hajuvuta droo hii
na ile. Aliporidhika na kazi yake, akajiweka sawa
na kuelekea mlangoni tayari kuondoka.
Alipofungua mlango tu, hamad! Uso kwa macho na
Steven Lawrance Marvin ambaye alikuwa hatua
kama nne hivi toka alipokuwa kitendo bila
kuchelewa Steve akawa na bastola mkononi na
haraka akampa Michael ishara ya kurudi
alikokuwa.
Michael akajilaani na kuilaani bahati yake.
Nimekuwa mzembe? Akajiuliza hali akiangalia huku
na huko kama kulikuwa na raia waliokuwa
wakiwangalia. Hakuna aliyewaangalia ingawa
kulikuwa na watu wachache, vitendo hivyo
vilifanyika ndani ya muda mfupi sana.
Michael akapima itamchukua sekunde ngapi
kuingiza mkono wake chini ya kitovu na kuchukua
bastola, kuondoa usalama, kumlenga Steve na
kuifyatua risasi. Na itamchukua sekunde ngapi
steve kukivuta kiwambo cha kufyatulia risasi. Jibu
likaufanya mwili umsisimke.
Akainua mikono na kuanza kurudi ndani taratibu.
Steven akamfuata kitemi kabisa na kuufunga
mlango nyuma yake kwa kutumia mguu. Kwa
maringo kabisa, akamwambia
“Hatimaye nimekupata mshenzi mkubwa haya
niambie ukweli wewe ni nani na unataka nini kwa
Dr Masurufu, Usijidanganye kuniongopea kuwa
wewe ni mwandishi wa habari na unatoka Daily
News!”
***Patamu
 
SEHEMU YA ISHIRINI
Michael akapima itamchukua sekunde ngapi
kuingiza mkono wake chini ya kitovu na kuchukua
bastola, kuondoa usalama, kumlenga Steve na
kuifyatua risasi. Na itamchukua sekunde ngapi
steve kukivuta kiwambo cha kufyatulia risasi. Jibu
likaufanya mwili umsisimke.
Akainua mikono na kuanza kurudi ndani taratibu.
Steven akamfuata kitemi kabisa na kuufunga
mlango nyuma yake kwa kutumia mguu. Kwa
maringo kabisa, akamwambia
“Hatimaye nimekupata mshenzi mkubwa haya
niambie ukweli wewe ni nani na unataka nini kwa
Dr Masurufu, Usijidanganye kuniongopea kuwa
wewe ni mwandishi wa habari na unatoka Daily
News!”
“Halafu ukishajua mimi ni nani ikusaidie nini?”
Michael akaanza kununua muda kutafuta makosa
ya Steve ili amshughulikie wakati huo huo
akimsubiria Raymond.
Kabla Steve hajajibu swali la Michael, simu ya
Steve ikaanza kuita. Wakati steve anahangaika
kuitoa kwa mkono mmoja, Michael akaona nafasi
aliyokuwa akiingojea ndio hii. Haraka akaishusha
mikono na kuupleka mkono chini ya kitovu
kulikokuwa na bastola yake.
Hakuwahi!
Bastola ya Steve iliyokuwa na kiwambo cha kuzuia
sauti ikakohoa mara moja. Risasi ikapiga nyuma
ya kiganja cha mkono wa kulia wa Michael,
ikatoboa tumbo na mgongo na kutokea upande wa
pili.
Michael akajikunja kwa maumivu makali na
kwenda chini hali akimtolea Steve jicho la
kutoamini. Bastola ya Steve ilipokohoa mara ya pili
risasi ikatua katika paji la uso na kumuua Michael
moja moja.
“Shenzi type!” Steve akasonya akiipeleka simu
sikioni.
SURA YA NANE
VIUNGO NA DAMU ZA ALBINO
Muda si muda polisi nao wakawa wamefika
nyumbani kwa Dr Masurufu na kuanza kumhoji
kwa vitisho kila waliyemuona, wakitaka kujua
Masurufu yuko wapi ili wamuhoji juu ya tuhuma
zilizotolewa na John Tengeneza dhidi yake.
Maonyo ya Steve yakiwa yangali mabichi vichwani
mwao, wafanyakazi wale wa ndani waliendelea
kung’anga’ania hawajui kilichompata Dr Masurufu,
wala hawajui alipo. Polisi walipodadisi zaidi, ishara
za mwili zikawasaliti watumishi wa Dokta
Masurufu.
Polisi wakagundua wanadanganywa ndipo
walipowazoa wote na kuwapeleka Kituo cha Polisi
ambapo walieleza kitu baada kulambwa vibao
viwili vitatu na kutishiwa kutupwa ndani.
Wakaruhusiwa baadae baada ya kueleza ukweli na
ya kuandikisha maelezo yao.
* * *
Ramond aliwasili katika wodi aliyolazwa Dr
Masurufu na kuingia ghafla bila hodi dakika tano
baadae. Hii ilikuwa baada ya kumpigia simu
Michael, na simu hiyo ikaishia kuita tu bila
kupokelewa, hali gari lake lilikuwa katika maegesho
ya pale Ocean Road Hospitali.
Kabla hajaifikia wodi hii alikuwa amekutana na Dr
Makete kama nasibu wakati alipokuwa amekuja
kuchukua dawa zilizoletwa na Lori la MSD ambalo
lilipaki hatua chache toka walipokuwa wamepaki.
Ni yeye aliyemwambia kwamba Michael yuko ndani
kwa Dr Masurufu na akamuelekeza wodi hiyo ilipo
ambapo alianza kupiga hatua ndefu ndefu kuifuata.
Alifika anamkuta Steven amemaliza kuongea na
simu.
Maiti ya Michael ilikuwa imeondolewa na
kusukumiwa mvunguni mwa kitanda cha Dr
Masurufu. Ile damu iliyotapakaa pale sakafuni
inamtisha na haraka anapeleka mkono nyuma ya
mgongo kwa minajili ya kutoa bastola. Lakini
anachelewa kwani tayari alikuwa anachungulia
mdomo wa Bastola ndogo ya kisasa aina ya 36
Calibre iliyotengenezwa na Mrusi.
Tabasamu la uchungu likamtoka moyoni
akistaajabu wepesi usio wa kawaida wa Steve.
Kwa wepesi ule ule, Raymond nae akafyatua teke
kali kwa kutumia mguu wake wa kulia akaipigia
teke bastola ya Steve nayo ikarushwa kando.
Wanaume wakaanza kuzungukana
Raymond akatisha kushoto na kurusha pigo la
kwanza katika mtindo wa karate. Steve
akalikwepa. Pigo la pili Hola! La tatu na la nne.
Yote yakakata upepo. Raymond akashangaa zaidi
asijue kakutana na mtu gani. Akabadili mtindo wa
mapigano na kuanza kuruka kama bondia mwenye
uzito mwepesi akitupa mapigo mazito mazito kwa
staili ya kung-fu. Mapigo ya kifo.
Bado steve aliendelea kuyapoteza mapigo yake
kama mzaha, hali akitabasamu kwa dharau. Mara
Raymond akarusha pigo la kininja, mara
Taekwondo, mara KickBoxer! Ilikuwa kazi bure.
Hakuingiza hata pigo moja katika mwili wa steve.
Steve alipoona amemchosha vilivyo Ramond, ndipo
alipoikamata mikono yake ambayo ilikuwa imekuja
kwa lengo la kumpiga karate katika chembe ya
moyo, akaizungusha na kumnyanyua Ramond kwa
kasi ya ajabu na kwa njia ya Judo amshusha na
kumbwaga chini kwa nguvu. Maumivu makali
yakampata mgongoni.
Akamfuata na kumnyanyua tena kwa njia ilele ile
ya Judo akampigiza tena chini kwa nguvu “Mama
nakufaaah!” Ramond akapiga unyende mkali wa
maumivu.
“Unakufakweli” Akamwambia kwa dhihaka wakati
akimkusanya na kumnyanyua tena. Akamwambia
“Ni wachache sana waliowahi kupambana na mimi
na wakatoka salama. Wasalimie kuzimu!”
Alipomtua tena mara ya tatu, uti wa mgongo wa
Raymond ukavunjika! Raymond akalia kama mtoto
mdogo. Steve akamsogelea pale chini na
kumnyuka makonde kadhaa ya haja, Ray
alipotepeta kabisa, Steve akakiinua kichwa chake
na kumvunja shingo.
Baada ya kumuua Raymond ndipo Steve
alipotambua kuwa mahali pale hapakuwa salama
hata kidogo, Hii ni kwa vile kama watu aliowaua
walikuwa wametumwa, basi lazima aliyewatuma
atataka kujua matokeo ya kazi yake.
Na vile Dr Masurufu alikuwa angali amepoteza
fahamu, Steve akaona mambo yanaweza kuwa
magumu zaidi kama Polisi watafika hapo na
kumkuta anang’aa ng’aa macho. Akatoka nje na
kuchukua kigari cha kubebea wagonjwa,
akakiingiza wodini na kumpakia Dr Masurufu.
Akampeleka mpaka katika gari lake na kumuingiza.
Madaktari na walinzi walipomuulizia majibu ya
kina yalikuwa yanawasubiri, kwamba wameamua
kwenda kumuuguzia nyumbani chini ya uangalizi
wa Daktari wa familia. Wakamruhusu.
Walipoumuuliza ilipo hati ya ruhusa, discharge
card. Akaingiza mkono mfukoni, ukatoka ukiwa na
noti kadhaa. Akamkabidhi mmoja wao.
“Za nini?!” Mmoja akasaili kwa macho.
“Tusaidiane ndugu zangu, nyumbani wanamuhitaji
haraka!”
Wale walinzi wakatazamana. Halafu wakaelewa na
kutabasamu. Wakamfungulia geti akatoka taratiibu
kwa amani na kutokomea zake.
Ni mtu mmoja tu aliyeingiwa na mashaka baada
ya kuambiwa Dr Masurufu ameondoka. Mtu huyu
Dr. Keneth Makete ambaye alikuwa maliwato
wakati Steve alipoondoka na Dr. Masurufu; yeye
alikimbilia moja kwa moja katika chumba
alichokuwa Dr Masurufu ambapo damu zililimlaki.
Alipoangalia chini ya mvungu, Maiti ya Raymond
yalikuwa bado hata hayajapoa wakati ile ya
Michael damu zilikuwa zimeanza kuganda. Haraka
akainuka na kurudi ofisini kwake ambako alijua cha
kufanya.
* * *
Frank aliingia hima katika hospitali hiyo ya Binafsi
ambayo ilikuwa Sinza kijiweni ambako alimkuta
Steve amejiinamia. Akamsogelea na kumsaili.
“Vipi Master?!”
“Mambo sio hata kidogo, hata naanza kupata
mashaka kama harakati zetu zitafanikiwa”.
“Kwani kumezidi kitu gani tena?”
“Tengeneza ametuweza kweli! Sijui zile ziri za
Masurufu alizipata wapi? Yaelekea Polisi
wamezipata na kuamua kuzifuatilia, Taasisi ya
kuzuia Rushwa hali kadhalika. Wachilia mbali
usalama wa Taifa ambao nahisi wapo nyuma!
Naona matumaini yamepungua sana!”
“Mungu wangu!” Frank John akamudu kutamka.
“Sasa tutafanyeje maana naona kama vile tunanza
kuwa wakimbizi ndani ya nchi yetu wenyewe!”
“Ndiyo maana nimekuita tushauriane”
“Mie nadhani tungesubiri kwanza Masurufu aamke
ili tujadiliane nae kwa kina, kwa sababu namna
mambo anavyoyaendesha anajua mwenyewe. We
siri kama zile unaweza kuzipata wapi kama sio
mtu wake wa karibu sana. Mie mwenyewe kuna
Baadhi ya mambo ndio nayaona mle. Pengine
akiamka anaweza kuwa na hisia nani amehusika.
Pengine mkewe. Tutajuaje?”
“Inawezekana, maana jinsi Mama Masurufu
alivyompandishia mumewe pale hospitali, inatia
mashaka kama wangali wanazungumza lugha
moja.”
“Eti? Wamegombana na mkewe? Hebu nipe
habari!” Frank aliomba.
Steve akamsimulia yote. Frank akabaki ameshika
kichwa kwa mshangao. Kutokea hapo walijadiliana
kwa muda lakini baadae waligundua kuwa
hawaendi mbele wala kurudi nyuma. Wakawa
hawana budi kusubiri Masurufu aamke wamuulize.
Wakaendelea kusubiri.
Masurufu alizinduka masaa manne baadae na
baada ya huduma zaidi za hapa na pale, Dr
Masurufu alijikuta akiwa na nafuu kabisa kiasi cha
akili yake kutulia na kutafakari mambo kwa upana
wake. Na katika hali hiyo waliweza kufanya
majadiliano ya kina pia.
Ambapo mwisho walikubaliana Masurufu aendelee
kujificha hapo hospitali kwa muda wakati Frank
akisawazisha mambo kwa kuwanunua wanahabari
ili wasiendelee kukuza mambo, kununua viongozi
wa hospitali na ikiwezekana hata polisi ili mambo
yafunikwe na Dr. Masurufu atakapojitokeza hali iwe
shwari kabisa kabisa.
Masurufu pia alipendekeza John Tengeneza auawe
ili kukishawishi chama kupeleka uteuzi wa
wagombea mbele kwa kuwa hili litasaidia wao
kupata muda wa kujipanga vizuri kuondoa makosa
yote na kurejesha imani ya jamii iliyotoweka juu
yake.
Kitu ambacho walikikubali.
* * *
Taarifa kwamba Raymond na Michael wameuawa
na Dr Masurufu kutoweka zilikaribia kumfanya
Samson Kidude awehuke kwa kihoro. Akakanyaga
mafuta ya gari kwa hasira akivunja na kukiuka
sheria za usalama barabarani hadi pale alipojikuta
amewasili katika viunga vya Ocean Road Hospital
ambako Dk Makete alikuwa Akimsubiri.
Akampokea na kumpa maelezo machache kabla
hajamuongoza mpaka katika chumba alichokuwa
amelazwa Dr Masurufu, ambacho wakati huu
kilikuwa kimesheheni damu na harufu ya maiti.
Wakainua kitanda na kukisogeza pembeni, maiti ya
Raymond na Michael zikaonekana.
Roho ilimuuma kuona vijana wake walivyouawa
kikatili. Akafumba macho na kutoa heshima za
mwisho kwa vijana wake hawa aliowapenda na
kuwaamini, moyoni akijilaani ni kwa nini hakujipa
yeye jukumu la kuja kukabiliana na Masurufu,
akiwaacha vijana wake wakienda kwa Tengeneza.
Akainama na kuchukua miwani ya Michael
iliyokuwa hatua chache toka ilipo maiti ya Michael,
akanyofoa vitendea kazi kadhaa katika shati la
Raymond halafu akazifunika shuka maiti zile na
kutoka, akimtaka Dk Makete awaite Polisi ambao
Awali walikuwa wamezuiliwa wasifanye chochote ili
wapige picha na kuchukua alama halafu azihifadhi
maiti hizo mochwari.
Kutoka pale Ocean Road, safari yake iliishia katika
maabara yake ambako alifika anavitumbukiza vifaa
vile katika mashine yake. Picha za matukio
waliyopitia Michael na Raymond zikatokea, picha
ya Steve ikijionyesha vizuri zaidi. Akai-print na
kuihifadhi.
Dakika chache alikuwa katika simu akitoa maagizo
haya na yale kwa Mzee Chilonga ambaye naye
alijua cha kufanya.
Kiza kilipoanza kubisha hodi kilimkuta akiwa katika
sebule ya jumba la kifahari la Dk Masurufu, mbele
yake akiwepo Eliza na watumishi wengine watano.
Hofu kwamba huyu ni polisi uliwazidishia wasiwasi
hata wasijue familia yao inakabiliwa na kitu gani
hata polisi waizingire mara kwa mara.
“Mnaweza kuniambia huyu ni nani?”Akawauliza
huku akiwapa picha ya Steve. Watumishi wale
wakaitazama kwa zamu na kubakia na hofu huku
wakitegeana nani aongee. Hii ni kwa kuwa maonyo
ya Steve yalikuwa yangali mabichi vichwani mwao.
“Je” Akawauliza tena “Mnamfahamu?”
Baadhi wakatikisa kichwa kukubali, wengine
wakikataa.
“Ni nani?”
“Ni... ni... ni mlinzi wa baba aliyerejea nae toka
Ulaya!”. Joyce ambaye alipata msukosuko kuzidi
wenzake pale walipochukuliwa na polisi mara ya
kwanza akaamua kusema, akihofu kwamba
pengine ile hadithi ya kuchukuliwa tena mpaka
Polisi inaweza kujirudia tena.
“Anaitwa nani?
“Sisi tumemzoea kwa jina moja la Anko Steve!”
“Yuko wapi?”
“Humu huwa haingii mara kwa mara, huingia kwa
dharura tu na mara nyingi anapoingia huwa
ameitwa na baba. Nyumba yake ni ile pale!”
Akajibu tena Joyce akiisota nyumba ya Steve
ambapo kwa hapo walipokaa, ilikuwa mgongoni
kwa Samsoni.
Samsoni akageuka na kutazama nyuma, akakiona
kijumba kidogo mfano wa nyumba yenye vyumba
viwili na sebule pembeni sana ya geti la kuingilia
na kutokea ndani. Ilizungukwa na maua mengi
kiasi cha kufanya isionekane sawa sawa nyakati za
mchana, ingawa kwa jioni hii ikiwa inawaka taa
ilionekana vizuri zaidi. Akashangaa kwa nini
hakuwa ameiona nyumba hii katika mara zote
alizofanya safari za siri hapo nyumbani kwa Dk
Masurufu.
ITAENDELEA.
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA
Samsoni akageuka na kutazama nyuma, akakiona
kijumba kidogo mfano wa nyumba yenye vyumba
viwili na sebule pembeni sana ya geti la kuingilia
na kutokea ndani. Ilizungukwa na maua mengi
kiasi cha kufanya isionekane sawa sawa nyakati za
mchana, ingawa kwa jioni hii ikiwa inawaka taa
ilionekana vizuri zaidi. Akashangaa kwa nini
hakuwa ameiona nyumba hii katika mara zote
alizofanya safari za siri hapo nyumbani kwa Dk
Masurufu.
“Ndio kusema yupo nyumbani kwake?”Akaendelea
kusaili.
“Sidhani!” Sasa akajibu Eliza.
“Kwa nini?” Samsoni akamgeukia.
“Mara ya mwisho ilikuwa mchana wakati mama
aliporejea kutoka hospitali akiwa hajisikii vizuri na
kuomba asisumbuliwe. Anko Steve akaja baadae,
akazungumza nae na kwenda kumnunulia dawa
huku akituonya tusimsumbue mama wala kutoa
habari za mahali alikolazwa Baba.”
Samsoni akasikia moyo wake unapiga kwa nguvu.
“Je,” Akauliza “ Na toka muda huo, mama
hajaamka na Steve hajarudi?”
“Hatujui kama ni hivyo au lah!”
“Kwa nini?”
“Kwa kuwa baada ya yule mwandishi wa habari
kutoka, na anko Steve kutukemea, na yeye
kuondoka, Polisi waliingia hapa na kuanza kutafuta
habari za mzee, ambapo walitusomba wote baada
ya kuwaambia hatujui alipo mzee, wenyewe
wakisema tunawaongopea.
Kituoni tulilazimika kusema ukweli ambapo
tuliachiwa baada ya kuandika maelezo. Nyakati za
jioni polisi walikuja tena kutaka kuongea na mama
lakini mlango wake ulikuwa bado umefungwa kitu
kilichotufanya tuhisi kuwa kama mama hakutoka
wakati sisi tulipokuwa polisi; basi atakuwa bado
amelala.
“Chumba chake kiko wapi?”
“Kile pale! Lakini huwa haruhusu kabisa
kuamshwa, anaweza kutufukuza kazi, mama ni
mkali sana!”
“Hatawafukuza!” Samsoni akawatia moyo akiinuka
na kwenda kuukabili mlango. Akaugonga mara
kadhaa bila jibu. Akarudi nyuma na kuurukia kwa
miguu yote miwili. Lilikuwa pigo takatifu. Mlango
ukatii na kufunguka na kufanya Samsoni atue
ndani.
Kile alichokihofia ndicho kilichokuwa. Mama
Masurufu alikuwa amefariki kwa risasi ya kichwa.
Alilala kwa utulivu juu ya kitanda chake hali
dimbwi la damu likijitenga pembeni nae juu ya
kitanda hicho hicho.
Kushoto kwake kulikuwa na bastola ndogo ambayo
Samson alihisi pengine mama Masurufu alikuwa
anataka kupambana na Steve muda mfupi kabla ya
kifo chake. Samson akachoka.
Mama Masurufu alifanya nini mpaka Steve na
Masurufu wake wampe adhabu kali hivi? Akajiuliza
asipate jibu. Akatoka nje na kuwapigia simu Polisi.
Wakati Polisi wanakuja yeye akatoka nje na
kwenda kuyakabili makazi ya Steve ambako
mshangao ulikuwa unamsubiri.
Nyumba ya Steve ilijengwa imara na kitu mfano wa
zege kama sio chuma. Milango na madirisha yake
vilikuwa imara kiasi kwamba pengine ungehitaji
silaha mfano wa RPG kufungua. Samson alifanya
kila alichoweza kufungua bila mafanikio.
Polisi wakafika na kuichukua maiti ya mama
Masurufu baada ya taratibu nyingine kufuatwa.
Familia nzima ikasombwa na kupelekwa Polisi
ambako walijikuta wakihenyeshwa kwa maswali
ambayo majibu yake hawakuyajua.
Samsoni aliendelea kuitafiti nyumba ya Steve
mpaka pale alipopokea simu kwamba mmoja wa
watu waliotangaza nia ya kugombea urais kupitia
chama Tawala alikuwa ameuawa kikatili.
Samsoni akalazimika kuwaita vijana wake wengine
wawili ambao aliwataka walinde tu nyumba ya Dk
Masurufu na pale watakapomuona Steve amerudi
wasimfanye chochote badala yake wampigie simu
na atakuja mara moja
Wakakubali, Samsoni akaondoka.
* * *
Leo Profesa Zonga alikuwa tofauti na siku zote.
Uso wote ulikuwa mwekundu na alikuwa
akitetemeka kwa hasira huku macho yote
ameyatoa kwa namna iliyotisha na kuogofya
kabisa, hali msaidizi wake Mwile wa Mwilenga
akiwa na kazi ya kuwatuliza waungwana
waliopanda kichwani kwa Profesa Zonga na
kutishia amani.
“Umefanya makosa Masuuuuh! Makosa makubwa
Masurufu. Sasa waungwana wamekasirika
wanataka kuitoa roho yangu, wanataka
kuangamiza familia Masurufu. Umefanya nini
sasa!”Zonga aliendelea kulalamika akitikiswa kwa
nguvu.
“Basi waungwana muwasamehe! Ni watoto,
wangali wanajifunza bado!” Mwilenga akasihi
akimgeukia Dr Masurufu aliyekuwa amejiinamia
kwa hofu hali akitetemeka kwa uoga.
“Sema tawire!” Mwilenga akamfokea Masuru kwa
sauti kali na kuongeza “Utakufa wewe!”
Masurufu akakurupuka na kubweka “Tawire”
Profesa Zonga akasikitika na kulia. “Sasa mimi
nitafanya nini kukusaidia wewe hali umevunja
masharti eeh Masurufu?!”
“Tusaidie baba, tumekosa!”
“Haya nipe jini langu!” Profesa Zonga akaomba.
“Jini?” Masurufu akashangaa akiogopa zaidi.
Akauliza
“Je, Uliwahi kunipa jini Profesa?”
“Mwileeeh!” Sauti ya Profesa sasa ikawa kama
mwangwi!” Mwile akakurupuka na kuanguka
kifudifudi mbele ya Zonga!
“Rabaika Sayid yangu!”Akajibu akitetemeka kwa
uoga.
“Huyu anaongea kitu gani?”
Mwile akainuka na kumtazama Dk Masurufu kwa
jicho kali. Masurufu akazidi kuogopa. Akamwambia
akingali amemtumbulia macho. “Hukumbuki
kupewa kitu chochote na Sayid yangu?!”
“Kitu.... kitu...!” Dr Masurufu akavuta tafakuri.
Hakukumbuka chochote.
“Sikumbuki maulana. Mungu na mtume sikumbuki
kabisa!”
Mwile akatikisa kichwa kwa masikitiko kufuatia jibu
hili. Akisema, “Siku ile ya kazi ulipovunja nazi
sabini kwenye tendegu la mlango hukupewa kitu
wewe?”
Ndiyo kwanza akakumbuka! Kwamba baada ya
zoezi lile lililomchosha sana, mwisho wa siku
alipewa karatasi iliyoandikwa maneno ya kiarabu
na kuambiwa ahakikishe anatembea nayo kila
anapokwenda ila asiingie nayo chooni wala
msikitini na aliweke mbali pindi anapomkaribia
mkewe.
“Ile karatasi?”Akauliza kizembe zembe.
“Ndilo jini linaloombwa na Sayid yangu hilo!”
Machozi yakamtoka Masurufu. Ni kweli alikuwa
amevunja masharti, siku chache tu toka atoke kwa
Profesa alijisahau na kuingia nalo chooni,
alipojitahidi kujilinda na hilo, siku nyingine mkewe
akambana akajikuta akifanya mapenzi naye hali
karatasi hilo limo mfukoni mwake.
Ni kutokea hapo ndipo aliponunua mkebe maaalum
akaliweka katika gari na kutembea nayo kila
alipokwenda. Ukweli huu ukamfanya aone dunia
ikimuinamia hali walimwengu wakimdhihaki na
kumkebehi.
“Nipe jini langu haraka!” Alikuwa Profesa tena kwa
makelele.
“Lipo katika gari yangu ambayo ipo nyumbani, toka
niliposhikwa na presha sijalitumia tena. Labda
nimtume Frank akalilete!”
“Haina haja... Haina haja Masu!! Mwanangu
umemtenda na ametoroka. Shida zote hizi
anazileta yeye kwa kuwa tu hukuheshimu
makubaliano yetu! Umenitenda Masu, Umenitenda
Masuuh!” Profesa Zonga akatetemeka na kulia
zaidi, Mwile akimpoza hali Dr Masurufu akiomba
msamaha.
Ilikuwa ni baadae sana jini lililomtoroka Masurufu
lilipokubali kurudi kumsaidia tena Dr Masurufu
lakini kwa sharti la kupatiwa lita kumi na tano ya
damu ya albino, viganja vitano vya mikono, mikono
minne, nyayo mbili na moyo mmoja!
Yalikuwa masharti yaliyomtisha Dr Masurufu kupita
kiasi. Ilibakia sentimita chache arejewe na presha
tena. Kwa dakika kadhaa aliomboleza akitaka
abadilishiwe masharti au atoe fedha badala yake,
hakukubaliwa.
“Hapa una mawili tu, “Profesa Zonga alimwambia
baadae baada ya mashetani wake kuondoka.
Akaendelea, ama utimize masharti uupate urais au
uache kiti wangu aitafune familia yako na wewe
mwenyewe!”
Yote yalikuwa magumu. Masurufu hakujua
afanyeje.
Kikao baina yake na Steve na Frank hakikuwa na
matunda ya kujivunia kabisa. “Frank!”Akaita
baadae baada ya kuona hawaendi popote.
“Itakubidi ushughulikie hili!
Frank akajamba. “Eti… eti nini vile?!!” Hakuamini.
“Ndiyo Frank! There is no way. Jitahidi kadiri ya
uwezo wako, mahitaji ya Profesa yapatikane
haraka iwezekanavyo ndani ya siku chache tu
ikiwezekana tatu tu!”
“Lakini Dokta... lakini!”
“Naelewa unachotaka kusema. Naelewa pengine
kuliko unavyotaka nielewe. Lakini kumbuka hakuna
lisilowezekana chini ya jua. Usione watu
wanakuwa wasemaji wa Ikulu au wanampangia
rais cha kufanya, mamlaka hayo hutokana na
majukumu kama haya.
Kama unavyojua Steve hawezi kusimamia hili kwa
kuwa sio kazi yake, lakini pia baada ya kuwaua
wale makachero wa polisi kule hospitali, hatuoni
kama ni busara aendelee kuzagaa zagaa mitaani.
Mimi pia sitaweza kwa kuwa natafutwa na vyombo
vya usalama kujibu tuhuma alizotoa Tengeneza.
Ndio maana nimeomba fursa ya kujificha hapa
kwa Profesa Zonga ili aweke mambo sawa ndipo
nijitokeze. Nikiwa na waungwana wa Profesa
Zonga baada ya kulishughulikia hili vizuri
nitajitokeza kifua mbele nikiwa na majibu ya hoja
zote, tena majibu timilifu kabisa!”
Akatua kwa muda kuona Frank anayapokeaje
maelezo yale. Alipoona kimya akaendelea.
“Hii ni kadi yangu ya ATM, niliamua kuzigawanya
kadi hizi kwa ajili ya dharura kama hizi. Humo
kuna milioni ya mia moja, neno la siri ni mkakati.
Chukua fedha unazoweza, kodi watu unaowataka
ili mradi tu zoezi hilo litimie ndani ya siku mbili au
tatu.
Kingine unachopaswa kukumbuka ni kuwa maji
tumeshayavulia nguo, hatuna budi kuyaoga. Hivyo
ni lazima tupambane bila kuinua mikono wala
kurudi nyuma. Na ole wao tuitie Tanzania
mikononi…!”
Masurufu akahitimisha. Ikawa hotuba iliyomjaza
mori na kumtia hamasa Frank. Akapokea kadi ya
ATM na kuondoka.
* * *
“Stupid! Stupid! Bastard! Christopher McDonald
alilalama kwa sautii kali kiasi cha kuyaumiza
masikio ya Steve. Uso ukambadilika na kuwa
mwekundu mithili ya papai bivu.
“Nani alimtuma aingie katika siasa za kuchafuana
hali anajielewa fika si msafi, ilikuaje aanze ugomvi
wa mawe hali nyumba yake ni ya vioo? Sie tulimpa
fedha akanunue uongozi yeye kanunua matusi!
Shiit!”Aliendelea kulalamika wakati Steve
akimueleza hali halisi na karata ya mwisho
anayoicheza Masurufu.
“Sikiza Steve!” Alikuwa McDonald kwa hasira
mwisho wa maongezi yake na Steve.
“Endelea kuangalia upepo ukoje. Hakikisha
humwachi hata hatua moja. Ukiona mambo huku
saa nane huku saa tisa, hakikisha unamrejesha
mikononi mwetu haraka iwezekanavyo na lazima
arejeshe gharama zetu zote! Okay?!”
“Haina shida!”
“Huo Mkakati wake mwingine unauonaje?”
“Wa kutafuta viungo vya Albino?”
‘Ndiyo!”
“Hata mie umenishangaza. Sioni ni vipi damu au
viungo vya mtu vinaweza kurekebisha hali hii Ndio
maana alipotaka kunishirikisha nikamwambia hiyo
siyo kazi iliyonileta!”
“Na huyo anaeishughulikia anaweza kuiendesha
vizuri maana isije kuwa mnachota maji kisimani ili
kwenda kujaza bahari!”
“Nadhani anaweza. Awali alikuwa na hofu lakini
baadae akatuliza akili na kuanza kuitekeleza.
Nahisi atafanikiwa. Na unajua nini,huyu mtabiri
sijui mnajimu huku anakubalika sana. Ana timu
kubwa ya viongozi na watu wengine mashuhuri.
Ngoja tuone, pengine atafanikiwa!”
“Katika hilo hakikisha huchezi pata potea Steve!”
“Usihofu bosi, ninajua ninachokifanya!”
Wakaagana.
***Haya...
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI
“Endelea kuangalia upepo ukoje. Hakikisha
humwachi hata hatua moja. Ukiona mambo huku
saa nane huku saa tisa, hakikisha unamrejesha
mikononi mwetu haraka iwezekanavyo na lazima
arejeshe gharama zetu zote! Okay?!”
“Haina shida!”
“Huo Mkakati wake mwingine unauonaje?”
“Wa kutafuta viungo vya Albino?”
‘Ndiyo!”
“Hata mie umenishangaza. Sioni ni vipi damu au
viungo vya mtu vinaweza kurekebisha hali hii Ndio
maana alipotaka kunishirikisha nikamwambia hiyo
siyo kazi iliyonileta!”
“Na huyo anaeishughulikia anaweza kuiendesha
vizuri maana isije kuwa mnachota maji kisimani ili
kwenda kujaza bahari!”
“Nadhani anaweza. Awali alikuwa na hofu lakini
baadae akatuliza akili na kuanza kuitekeleza.
Nahisi atafanikiwa. Na unajua nini,huyu mtabiri
sijui mnajimu huku anakubalika sana. Ana timu
kubwa ya viongozi na watu wengine mashuhuri.
Ngoja tuone, pengine atafanikiwa!”
“Katika hilo hakikisha huchezi pata potea Steve!”
“Usihofu bosi, ninajua ninachokifanya!”
Wakaagana.
* * *
Milioni thelathini alizopewa Emanuel Kuho na Frank
John yakiwa ni malipo ya awali zilimchanganya
akili, akajifungia ndani akipanga mpango mzima
wa kutekeleza matakwa ya Frank. Katika hili
alijikuta akisafiri mikoa michache tu kwa kutumia
ndege ya kukodi na aliporidhika na uchunguzi wake
ndipo alipokuja tena kwa Frank na kuchukua
theluthi nyingine ya fedha, tayari kwa utekelezaji.
* * *
Siku mbili za kusubiria zikaanza kumchosha
Samson. Hata hivyo hakuchoka. Aliendelea kusubiri
tu. Kitu fulani kiliendelea kumwambia kuwa lazima
tu Steve au Masurufu watarudi katika nyumba hiyo
kukamilisha masuala yao fulani fulani.
Hakutaka kuamini mara moja kuwa baada ya
mauaji yale yaliyopelekea kupotea kwa Steve na
Masurufu hata wakasakwa katika viunga vyote bila
kupatikana kwamba watakuwa wameyeyuka moja
kwa moja. Na hili alilipa nguvu kufuatia lile
angalizo.
Naam! Angalizo alilotoa kwa mzee Anderson
Chilonga, ambalo kwa hakika lilikuwa limefanya
kazi ipasavyo. Mipaka yote ilikuwa imefungwa kwa
ajili ya Masurufu na Steve, askari wenye picha zao
waliwekwa kila palipohisiwa kuwa panaweza
kumtoa mtu nje ya Dar es salaam.
Tishio kwamba uchaguzi huu utakuwa na tatizo
liliwasumbua vichwa takribani maafisa wote wa
usalama pamoja na maafisa wa jeshi la polisi kiasi
cha kila mmoja kuhaha kutaka kuweka hali sawa.
Akiwa anapata taarifa zote toka kwa rafiki zake
waliomo ndani ya jeshi la polisi na vyombo vingine
vya usalama, Samson alijiona kama aliye hatua
moja mbele katika mapambano hayo kwa kule
kumfahamu kwake Steve na ofisi yake yake Siri.
Ofisi ambayo alikuwa amejaribu kuifungua kwa
mbinu zake na kutofanikiwa.
“Maadamu taarifa zinasema hajatoroka nje, na
kwamba inawezekana kuwa wameamua kujificha
kwa dharura, basi watarudi tu na hapo ndipo
kiama chao kitakapotukia!” Samsoni aliamua na
kuendelea kusubiri.
* * *
Kipindi kilichofuatia kilikuwa kigumu zaidi kwa jeshi
la polisi, vyombo vya usalama na serikali kwa
ujumla. Maisha ya raia wenye ulemavu wa ngozi
maarufu kama Albino yalianza kuwa hatarini na
kuwafanya waishi kwa mashaka mazito.
Ilianzia Kigoma, mmoja akauawa na kunyofolewa
baadhi ya viungo vyake, kabla hili halijaisha
ikafuatia Tabora kabla Mwanza nako mambo
hayajaharibika.
Nchi ikatikisika na kuzomewa na mataifa ya nje.
Wanaharakati wakaandama na kulaani, hali Albino
wenyewe wakianza kuishi kwa hofu pasipo kujua
nani atafuata kesho. Wakahaha kuomba Serikali
iwasaidie na kuwalinda. Ulinzi miongoni mwao
ukaongezwa. Polisi wakaapa kuwakamata wote
walioendesha unyama huo..
Alipouawa Albino mwingine kule Shinyanga na
maiti yake kuonekana siku ya pili ikiwa imeharibika
vibaya, ndipo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania aliposimama na kutoa hotuba kali na
kutaka watuhumiwa wa vitendo hivi wawe
wamekamatwa na kufikishwa mbele ya sheria
haraka iwezekanavyo. Akamtaka Mkuu wa Jeshi la
Polisi aiongoze oparesheni hiyo na kumpelekea
moja kwa moja taarifa.
Hatua hii ilifuatiwa na ile ya Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kububujikwa
na machozi wakati alipokuwa akisikiliza kisa cha
mmoja wa Albino walionusurika katika kadhia hiyo
ambaye hata hivyo alikatwa viganja vya mikono
yake miwili. Akamuagiza Mkuu wa Polisi
kuhakikisha maharamia hao wanakamatwa.
Mkuu wa Polisi akamuahidi kulifanyia kazi. Ahadi
ambayo aliitimiza.
* * *
Wakati hali ikiwa tete hivi Emanuel Kuho, wakala
wa Frank aliyekuwa amepanga Mwanza Hotel;
alikuwa amepungukiwa na lita tatu tu za damu,
pamoja na kiganja kimoja kutimiza yale mahitaji ya
Bosi wake Frank.
Kwa mujibu wa wa Robinson mtu aliyempa jukumu
la kumtekelezea kazi hiyo kwa shilingi milioni tatu
kwa kila kiungo, laki tisa kwa kila lita moja ya
damu alikuwa amehakikishiwa kwamba upungufu
huu wa leo ungeweza kumalizwa kabisa.
Kiasi alijisikia mwenye furaha isiyo kifani. Hii ni
kwa vile ndege ya kukodi ilikuwa ikimsubiri
uwanjani. Hivyo alijua muda si muda Robinson
atamletea amana yake naye ataondoka usiku huo
huo na kurejea Dare s salaam ambako atamkabidhi
Frank mali yake naye atamaliziwa fedha zilizosalia
na kuwa miongoni mwa mamilionea.
Hakuona ni kwa nini asipambe na kusherehekea.
Naam, akainua simu na kumwita mmoja wa
wahudumu wa Hotel ile ambapo alimuagiza
chakula, vinywaji na kitu kingine kimoja zaidi.
Mhudumu akaondoka amekenua baada ya kupewa
ahsante ya shilingi elfu ishrini.
Dakika chache baadae Emanuel alikuwa katikati ya
maguberi mawili ya kike wakiogelea katika msitu
wa vinywaji na makulaji. Alikula, kunywa na
kufanya mapenzi na malaya wale mpaka pale
alipopigiwa simu kwamba mzigo wake ulikuwa
tayari. Ni hapo alipowatimua wale vyangudoa .
“Nawashukuruni sana, sasa mnaweza kwenda!”
“Jamani mara hii”, Mmoja akalalamika kwa
geresha hali moyo ukimpaa kwa furaha baada ya
kukabidhiwa kibunda cha shilingi laki moja kwa
kazi ya kipuuzi kabisa.
“Msijali, mie naingia katika majukumu mengine na
nikiwahitaji tena, nitamjulisha Peter nae
atawaleta!”
“Kweli?”
“Kabisa!”
“Usijali, tukikutana tena utafurahi mara mbili ya
hapa!”
“Nitashukuru!”
Wanawake wakavaa na kuondoka. Naye akaingia
bafuni, kuoga na kuvalia nadhifu. Malipo ya
Robinson akayaandaa na kuyaweka kwenye
bahasha kabisa.
Hakika, Robinson alifika baadae. Na hakuwa
pekee. Alikuwa na Polisi ambao walimkamata
Emanuel Kuho kama kuku, na kumpeleka kituoni
ambako aliminywa vizuri na kurupoka kila kitu
ikiwemo ndege ya kukodi aliyokuja nayo kutoka
Dar es salaam ambayo ilikuwa ikimsubiri Uwanja
wa ndege.
Polisi wakabaki wanashangaa, mtu kukodi ndege
kutoka Dar es salaam hadi Mwanza kwenda
kufanya mauaji tu.
Dakika chache baadae, Robinson, Kuho, maafisa
wa Polisi pamoja na watuhumiwa wengine zaidi
wa matukio ya mauaji ya Albino, walikua hewani
kurejea Dar es salaam wakitumia ndege ile ile ya
kukodi iliyokuwa ikimsubiri Emanuel Kuho.
Moyoni, maafisa wale wa polisi walikuwa
wamkimshukuru Mungu kuona kwamba zoezi
lililokuwa kubwa kiasi cha kupigiwa kelele mpaka
na Rais mwenyewe, licha ya kuwa gumu, lakini
limekuwa fupi na lenye manufaa kwao.
Ilikuwa ni baada ya jitihada za kuwapeleleza
waliofanya mauaji na vitendo vya ukatili dhidi ya
Albino kutozaa matunda ndipo lilipokuja wazo la
kuimarisha Ulinzi dhidi ya Raia wenye ulemavu huo
kwa polisi wenye silaha kujichanganya katika
familia zenye raia hao.
Wazo ambalo limekuwa na manufaa kwa kuwa
watu waliokuja kufanya uhalifu walikamatwa
kirahisi na walipobanwa wakawa wamewaleta
mpaka kwa Robinson ambaye aliwapeleka mpaka
kwa Kuho ambaye naye alikuwa mbioni
kuwafikisha miguuni kwa Frank.
Kama ilivyokuwa kwa Kuho, Frank nae alikamatwa
siku hiyo hiyo.
SURA YA TISA
HATI YA KUMKAMATA MASURUFU
Ilikuwa ni lazima arejee katika makazi yao ili
kukamilisha jukumu moja zito aliloagizwa na
Christopher McDonald. Hivyo akiwa anajua fika
kuwa nyumba ya Dr Masurufu imeshakuwa eneo la
makachero, Steve alichukua kila aina ya tahadhari
ikiwemo hii ya kuingia usiku akitumia moja ya
milango ambayo hutumika kwa nadra sana.
Bahati haikuwa yake, kwani eneo aliloamua
kulitumia kwa kuingilia lilikuwa jirani sana na eneo
alilojificha Samson kidude ambaye wakati huu
alikuwa ameanza kusinzia. Zile kukuru kakara
ambazo zilifanyika kwa utaratibu uliolenga
kuzifanya zisitoe ukelele zikawa zimemuamsha.
Akasimama imara sambamba na ukuta, mavazi
yake meusi yakimfanya awe sehemu ya kiza hicho.
Alitulia kwa utulivu mpaka Steve alipomaliza
kukuru kakara zake na kuanza kupiga hatua fupi
fupi zenye umakini wa aina yake kuelekea jengo
kuu ndipo Samson alipomwambia.
“Karibu nyumbani shujaa!”
Steve akashtuka na kugeuka haraka kwa kasi
mkono wake ukisafiri kwa kasi kuelekea kule iliko
bastola yake. Akajikuta amechelewa kwani tayari
alikuwa anatazamana na mdomo wa bastola ya
kisasa aina ya Colt 50 iliyotengenezwa na Mjapani.
Kwa kila hali Samson alikuwa amemuwahi.
“Unanishangaza! Uliwezaje kuwaua vijana wangu
kijasiri kule hospitali, halafu ushindwe kuja mchana
katika makazi yako tena utumie milango
isiyotumika!”
“Wewe ni nani?” Steve akauliza akiwa na lengo la
kumvizia Samson aweze kumpotezea silaha yake.
Lengo ambalo Samson pia alilijua! Samson
akatabasamu. Akimwamuru Steve asogee mbele
kulikokuwa na uwanja na mwanga wa kutosha.
Steve akatii.
“Unataka kunijua siyo, utanijua tu. Lakini kwanza
niambie kwa nini ulimuua mama Masurufu?”
“Siyo mimi niliyemuua!”
“Ni wewe! Watumishi wote wa Dr Masurufu
walikuona. Wewe ndiye uliyekuwa mtu wa mwisho
kuingia chumbani kwake, na toka ulivyotoka
hakuna yeyote aliyeingia mpaka maiti yake
ilipoonekana juzi!”
“Nakwambia sio mimi niliyemuua, hutaki shauri
yako!”
“Unajifanya jeuri siyo? Utafika wakati utatapika kila
kitu. Na Dr Masurufu umemficha wapi?”
“Sijui unaongea nini! Mimi ni mlinzi tu!”
“Unakuaje mlinzi mpumbavu kiasi hicho usiyejua
wapi alipo bosi wako?
Kimya.
“Mikono juu!” Akaamrisha. Steve akatii.
Samson akamsogelea. Ilikuwa fursa adhimu
ambayo Steve alikuwa akiisubiri kwa hamu. Kwa
uangalifu wa hali ya juu Samson akaanza
kumkagua Steve akichukua silaha hii na ile na
kifaa hiki na kile toka katika mwili wa Steve na
kukitupa kushoto.
Ulikuwa ni wakati huu Steve aliposhusha mikono
yake kwa nguvu, ikatua katika kichwa cha Samson
na hapo hapo akaachia teke kali lililopiga bastola
ya Samson ikapotelea kizani. Wakati huo huo
akapeleka mapigo mawili ya karate ambayo licha
ya Samson kuyakinga, bado yalimpeleka chini.
Steve akamuacha Samson ainuke. Tukio hili
likamshangaza Samson, Steve alikuwa na nafasi
nzuri ya kuendelea kumshambulia lakini
akamuacha. Steve akamuhimiza ainuke.
“Inuka ujiandae. Bila shaka ni Samson Kidude.
Nimekuwa nikisikia sifa zako tu, pamoja na
kwamba nimetumwa na bosi, nataka nihakiki, je ni
kweli sifa hizi unazo au wamekuwa wakikuvisha
kilemba cha ukoka. Inuka Samson, inuka!”.
Samson akainuka. “Bosi wako ni nani?” Akauliza.
“Haikuhusu!” Steve akajibu kijeuri huku
akimzunguka “Mind your business!” Akaongeza
akitupa pigo la kungfu. Samson akaliona na
kulipoteza. Akarusha lingine na lingine. Samson
akayapoteza.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU
“Haikuhusu!” Steve akajibu kijeuri huku
akimzunguka “Mind your business!” Akaongeza
akitupa pigo la kungfu. Samson akaliona na
kulipoteza. Akarusha lingine na lingine. Samson
akayapoteza.
Alipoona amepoteza mapigo ya kutosha ya Steve
na Steve anaelekea kuchoka , ndipo naye alipoanza
kutupa pigo moja moja. La kwanza Steve
akalikwepa, Samson aliporusha teke, Steve
akalidaka na wakati anajiandaa kuunyonga mguu,
Samson alijipindua na kumpiga teke jingine zito
katika shavu la kushoto kwa kutumia mguu
uliobaki chini na Steve akaenda chini pamoja na
Samson.
Wakati huu Samson alikuwa ameshaweza
kumsoma vizuri Steve na kugundua mitindo yote
anayotumia, hivyo yeye aliyapoteza mapigo ya
Steve katika mitindo ya Steve na kutoa ya kwake
mitindo tofauti kabisa.
Mitindo ambayo ni aghalabu kwa wanafunzi wa
kawaida kuijua kutoka kwa walimu wao. Yeye
Samson aliijua mitindo hii kwa kuwa mwalimu
wake wa Tai-chi kule Hong Kong alimpenda kupita
kiasi, akawa amemfundisha kila alilolijua huku
akimpa siri za ndani za kushinda mapambano
magumu.
Na kila Samson alipozitumia mbinu hizo, hakuwahi
kushindwa. Na hapa wakati anaziutumia mbinu
hizi, alifaulu kumnyuka Steve kama mtoto. Hili
lilimshangaza na kumuumiza sana Steve pengine
kuliko kipigo alichopokea maana kila alivyojitahidi
ajikurupushe na kuonyesha uwezo, ndiyo alivyozidi
kuchezea kichapo.
Kutahamaki akawa hoi pale sakafuni, uso ukiwa
hautamaniki.
“Haya inuka na uniongoze ndani, nione
mlichokifungia mle. Natumai sasa unaweza kujibu
maswali yangu vizuri!” Samson alitamba baada ya
kuhakikisha amempokonya Steve silaha zote
vikiwemo vidonge vya sumu ambavyo labda
pengine Steve angevitumia kujiua akizidiwa kabisa
na Samson.
Steve akajizoazoa pale na kuinuka. Roho ikimuuma
kuona namna alivyonyanyaswa na kudhalilishwa na
mtu mweusi kutoka Afrika. Akaapa kumuua
Samson kidogo kidogo kwa mateso makali mara tu
atakapomtia Samson mikononi.
Akanza kuongoza kuelekea lilipo jumba la Dokta
Masurufu!
“Siyo huko!” Akafoka Samson. “Nipeleke katika kile
kijumba chako!
Yes! Steve akafurahi kimoyomoyo akimuongoza
Samson. Nakuonea huruma kaka, akaendelea
kusema kimoyomoyo. Kunirudisha katika chumba
kile ni sawa na kumrejesha mamba mtoni baada ya
kumshinda katika nchi kavu!
Hatua chache toka kilipo kijumba kile, Steve
aliinama na kuutoa mfuniko fulani uliokuwa sawa
sawa na ardhi. Samson akamtazama vizuri zaidi
bastola mkononi huku akiwa tayari kuzuia hila
zozote ambazo Steve angeweza kuzifanya.
Steve hakufanya hila, badala yake alibonyeza
bonyeza pale chini kulikokuwa na mfuko ule,
kutahamaki mlango wa kile kijumba ukaanza
kufunguka kidogo kidogo kwa kuzama ardhini.
Lango la kijumba kile lilipobaki wazi, Steve akawa
wa kwanza kuingia ndani. Samson akamfuata
kidogo kidogo kwa hadhari zote, naye alipoingia
ndani tu mlango ukaanza kujifunga.
“Nani kakuruhusu ufunge mlango?” Akafoka
Samson “Fungua mlango haraka!” Akaamuru
macho yake yakizunguka huku na huko.
Yakalakiwa na mandhari ya kupendeza na kuvutia.
Kijumba kile kilikuwa kimejengwa kwa mtindo wa
namna yake, hali ndani kukiwa na nafasi kubwa ya
kutosha kuingia hata Fuso mbili na zikaenea bila
tabu.
Samson akashangaa kwa nini muda wote aliokuwa
anakuja hapa kumpeleleza Masurufu hakujiwa na
wazo la kukitembea kijumba hiki. Kijumba
ambacho kilielekea kubeba kila kitu. Samson
akafoka zaidi “Fungua mlango nakwambia!”
Steve akatabasamu, nguvu zikiwa zimeanza
kumrejesha akauliza kwa maringo.
“Unaogopa nini na hali umeshanishinda katika
mapambano ya mikono? Na hali ukingali umeshika
bastola?!”
“Nimesema fungua mlango!”
“Na nikikataa je?”
“Nakupa nafasi moja ya mwisho!” Samson akatua
na kumeza mate. Safari hii mlango ukiwa
umejifunga kabisa. “Ukileta ujeuri zaidi nitajua la
kufanya na hutapata zaidi ya hasara. Haya fungua
mlango!”
“Okay nitafanya upendandavyo!” Alikuwa Steve
kwa maringo akivuta hatua kuelekea ukutani
kulikokuwa na swichi mfano wa zile za kuwashia
umeme. “Mlango unafunguka sasa hivi Sir!” Steve
akasema akibonyeza mojawapo ya zile swichi.
Kilichotokea Samson hakukitegemea.
Alijishtukia akigongwa na kitu kizito kisogoni mfano
wa kitako cha Bunduki ambacho kilimfanya
ashindwe kujihimili akajikuta akianguka kifudifudi
hali bastola ikimtoka mkononi na kuangukia mbele.
Akajitahidi kuamka kadiri alivyoweza ili apambane
na Steve, akashindwa, akaona nguvu zikipungua
kwa kiasi mwilini mwake hali macho yakiona giza.
“Shit!” Akaguta kwa nguvu akiilani bahati yake.
Sauti pia haikutoka.
Akapoteza fahamu!
“Shenzi taip!” Steve akasonya wakati akiokota
bastola ya Samson aliyelala kama mzoga hatua
chache mbele yake. Akamtazama Samson na
kutikisa kichwa kwa masikitiko “Umekwisha
Samson! Akasema kwa mnong’ono mzito akiondoa
kiwambo cha kuzuia usalama katika bastola yake.
* * *
Baada ya kupokea simu hii, Inspekta Kimaro
alilazimika kuondoka katika hafla ya kumpongeza
Askari mwenzao wa ngazi za juu aliyerejea toka
Masomoni ambapo alikuwa amepata alama nzuri
kiasi cha kuipa sifa Tanzania. Na jeshi liliamua
kumuandalia hafla kumpongeza. Miongoni mwa
watu walioalikwa na kuhudhuria alikuwa Inspekta
Kimaro ambaye wakati huu aliwaomba radhi
wenzie kwa maelezo kuwa kuna dharura, akapanda
gari yake na kuelekea ofisini kwake ambako alikuta
wageni wawili wakimsubiri, Kachero Inspekta
Mathias na Sub Inspekta Mina.
Hawa walisimama mara tu Kimaro alipoingia,
wakakakamaa huku wakiinua mikono na kupiga
saluti miguu yao ikiwa sawa kabisa. Sauti
zikawaponyoka kwa pamoja,
“Jambo Afande!”
“Jambo!” Inspekta Kimaro akajibu akizunguka
nyuma ya meza yake na kuketi. “Enhe?” akasema
hali akiitoa kofia kichwani na kuitua mezani.
“Leteni taarifa. Nimelazimika kuacha sherehe kuja
kuwasikiliza kwa ajili ya unyeti wa kazi
niliyowatuma. Nawasikiliza!” Akatua.
“Tunaomba utayarishe hati ya kumkamata Dr
Masurufu!” Akasema Mina na kuongeza “Na zoezi
hili lifanyike haraka iwezekanavyo, ikiwezekana
usiku huu huu atiwe mbaroni!”
“Kitu gani? Msiniambie kama Masurufu anahusika!”
“Tunakwambia Mkuu. Masurufu anahusika kwa kila
hali na yupo kila mahali. Kwanza mali zake nyingi
ni za wizi na magendo. Uchunguzi tulioufanya kwa
kutembelea miradi iliyoanishwa katika kashfa
zilizotolewa dhidi yake na Marehemu John
Tengeneza unathibitisha hivyo.
Ameshiriki pia kuiba fedha zilizo katika akaunti ya
madeni ya ndani na nje, ana hisa katika kampuni
zote zilizoshiriki katika kulihujumu Shirika hata
likapata hasara ya mamilioni ya Shilingi. Baadhi
ya hasara hizo, taifa lingali linaendelea kuzipata
hadi leo hii tena kwa kulipa mamilioni ya shilingi.
Hapana Inspekta, masurufu anatakiwa kusimama
kizimbani akapate malipo ya uhalifu wake!”
Mathias akatua.
“Kama hiyo haitoshi”, Mina akaongezea “Ameshiriki
pia kusababisha vifo vya Michael na Raymond wa
Usalama wa Taifa, amemuua mkewe pia kwani
alama za vidole zilikutwa katika wodi aliyokuwa
amelazwa Masuruf pale Ocean Road, ndizo
ambazo pia zimekutwa katika kitasa cha mlango
wa ndani wa chumba cha Dr Masurufu ambapo
mkewe alikutwa amekufa.
Alama hizo hizo zipo pia katika usukani wa baadhi
y magari. Tunaamini alama hizi ni za Steve kama
tulivyoambiwa na Samson na kuthibitishiwa na
Frank ambaye amesema ni Steve aliyemuua pia
John Tengeneza. Kwa hiyo utaona kama Steve ni
mlinzi wa Masurufu na ndiye anayetokea kila
penye mauaji, yanayoambatana harakati zake za
kutaka kwenda Ikulu, Masurufu hawezi kukwepa
tuhuma na ukweli huu!”
****Heh!
ITAENDELEA...
 
duh hii story bwana. kama ina ukweli vile lkn ni riwaya means hakuna ukweli japo baadhi ya matukio yanayojadiliwa ni real
 
jaman mambo gani haya ya kuwekana viporo siku zote hizi?
 
Labda mleta uzi kapata dharura kwa kasi alioanza nayo usein nati angesubiri tumpe muda.
 
MWISHO SEHEMU YA KWANZA

...
Alama hizo hizo zipo pia katika usukani wa baadhi
y magari. Tunaamini alama hizi ni za Steve kama
tulivyoambiwa na Samson na kuthibitishiwa na
Frank ambaye amesema ni Steve aliyemuua pia
John Tengeneza. Kwa hiyo utaona kama Steve ni
mlinzi wa Masurufu na ndiye anayetokea kila
penye mauaji, yanayoambatana harakati zake za
kutaka kwenda Ikulu, Masurufu hawezi kukwepa
tuhuma na ukweli huu!”
Mina anaye akatua. Inspekta Kimato akauliza.
“Na kuhusu yule mtuhumiwa wa jana?”
“Frank siyo?” Mathias akajibu kwa Swali
Kimaro akatikisa kichwa akakubali
“Ni huyo aliyetufanya tuje tuombe hati ya
kumkamata Masurufu. Jana tumemminya kiasi cha
kutosha na ametapika kila kitu. Kwamba hata vifo
vya Albino vilivyokuwa vimeshamiri, vinatokana na
mahitaji ya Dr Masurufu ambaye anatimiliza
matakwa ya Profesa Zonga ili hatimaye Dr
Masurufu aweze kwenda Ikulu.
“Mungu wangu!” Inspekta akamudu kutamka
“Profesa Zonga pia yumo?!”
“Kwa mujibu wa Frank ambaye ilifikia mahali
akashindwa kabisa kuyavumilia mateso tuliyokuwa
tukimpa, amesema Albino hawa wasingeuwawa
kama Dr Masurufu asingevunja masharti ambapo
ilitakiwa dawa na viungo vya Albino kumsafisha, na
ndipo yeye alipopewa jukumu hili pamoja na kitita
cha milioni mia moja, ambapo naye alilikabidhi
jukumu la kutafuta viungo vya Albino kwa
Emmanuel Kuho!” Akatua Mathias.
“Isitoshe,” Mina akaendelea “Frank amethibitisha
pia kuwa ni Masurufu aliyetoa amri ya Tengeneza
kuuawa, na kwamba sasa hivi Dr Masurufu na
Steve wamejificha nyumbani kwa Profesa Zonga
wakingojea damu ya Albino ili wasafishe mambo
na kujitokeza hadharani wakiwa na nguvu mpya!”
Mina akamalizia.
Ilitosha! Inspekta akachoka. Mikono akaitua
mezani na kujiinamia.
Ilimuumiza kuona Masurufu Hussein Masurufu,
mtoto wa mpigania Uhuru maskini, aliyesoma na
kukua chini ya ulezi wa baba wa taifa ndiye
aliyeangukiwa na tuhuma zote hizi. Hakuweza
kuunganisha mambo mara moja na kuweza
kuupata mzizi kuwa ilikuwaje hata mtu kama
Masurufu aliyetegemewa kuwa hazina na rasilimali
ya taifa ageuke kuwa mwiba kwa taifa.
Alishindwa kutambua mara moja pia nini huwa
kinatokea kwa watu mpaka wengine wanakuwa
waadilifu sana kama alivyo yeye ambapo starehe
yake ni kuona watu wote wanaishi kwa haki na
usawa chini ya amani, utulivu na upendo
wakifanya kazi zao kwa uhuru na furaha; Na
inakuwaje wengine wanakuwa wahalifu sana kiasi
cha kutaka kukwapua hata kile kidogo ambacho
wananchi wa kawaida wamekipata kwa ngama
baada ya kukitolea jasho jingi.
Watu kama hawa hakujua walipaswa kupewa
adhabu gani kati ya kunyongwa, kufungwa maisha
na kuachiwa huru kama alivyofayika Mengistu
Haile Maryamu
Kama ningekuwa mimi… Akawaza …ningemfunga
kifungo cha maisha mahala pa wazi ili kila mmoja
aweze kumuona na kumsusuika. Pengine
ingesaidia kuifanya mioyo ya vijana wetu ambayo
kwa sasa ni kama imeandaliwa kujengwa na
kumea ndani ya ufisadi, kuweza kuhofia na
kuuacha mfumo huo.
Naam! Inspekta Kimaro aliendelea kuona athari ya
maisha wanayoishi watanzania kama hatua
madhubuti hazitachukuliwa kuizuia hali hii.
Kwamba ukabila unarejea kwa kasi ya ajabu,
vyama vya makabila baadhi vikiachwa vichipue
kama uyoga na kumea kila nafasi ilipopatikana.
Watu wakijisikia kama wana wajibu wa kutoa
rushwa hata baada ya kupewa huduma inayostahili
ambayo ni haki yao kimsingi. Hali ambayo
imewafikisha watanzania mahala ambapo
wameamini kama hujulikani kwa maana ya kuwa
mtoto au mtu mwenye nasaba na kigogo au
mfanyabiashara fulani na huna chochote kitu
mfukoni, huwezi kupata msaada au huduma yoyote
ile.
Hili pamoja na lile ma mgawanyo usio sawa wa
rasilimali za taifa, pengo kati ya masikini na
matajiri ambao licha ya kuishi katika sayari moja,
bado matajiri wamekuwa na maisha yao wakimiliki
dunia yao yenye kila kitu chao kama makazi, shule,
hospitali, magari na hata starehe zao.
Maskini pia nao wamekuwa na makazi kwenye
dunia yao, wakichangia huduma duni kutoka katika
shule zao almaarufu kama shule za akina
Kayumba. Si hilo tu wamekuwa pia na Hospitali
zao, usafiri wao wa daladala na starehe zao
ambazo ni aghalabu sana kutofutiana na ile
starehe anayoipata mbwa kwa kukalia mkia wake.
Inspekta Kimaro aliendelea kuiona hatari kubwa
inayoinyemelea Tanzania zaidi ya hii ya Dr
Masurufu. Hatari ya nchi kugeuka kuwa ya kifisadi
na kila mwenye kinafasi chake anataka ale na kula
na kula hadi asaze! Na pengine amalize chote na
kingine akaweke akiba nje ya nchi ili atakapostaafu
na kuzeeka aishi kama yuko peponi.
Kwa ujumla hatari ilikuwa kubwa sana. Kubwa
mno! Na kama mkereketwa wa uhuru wa kweli,
amani ya kweli na upendo wa kweli, Inspekta
Kimaro alikuwa anaamini kwa dhati kwamba
ilitakiwa kuchukuliwa hatua. Hatua madhubuti
ambayo ingeizuia Tanzania kutumbukia katika
shimo la kupoteza dira na mwelekeo inakoelekea
sasa, yenyewe ikidhani inaelekea katika maziwa na
asali.
Lakini nani na kuchukua hatua hiyo? Akajiuliza na
kuendelea …wakati kila mmoja anaona kwamba hili
ni jukumu la mwenzake? Lilikuwa swali gumu kwa
kila hali. Akaachana mawazo hayo na kuusogelea
mkonga wa simu. Akampigia mkuu wa Jeshi la
Poisi kwa ajili ya kupata kibali cha kumkamata Dr
Masurufu.
Kama ilivyokuwa kwake, IGP anae alishtuka kusikia
habari za Dr Masuruf na Profesa Zonga, hata hivyo
baada ya kujadiliana na watu anaofanya nao kazi
hatimaye aliidhinisha na muda mwingi baadae, hati
ya kukamatwa kwa Dr Masurufu, ikawa imetolewa
rasmi.
* * *$$$$****

Wakati Steve anainua bastola ili ampige Samson
risasi ya mguu kwa lengo la kumpunguza makali ili
aweze kumtesa vizuri, simu yake ikaita.
Christopher MacDonald alikuwa upande wa pili
akitaka kujua mambo yanakwendaje na kama
jukumu alilompa Steve lilikuwa limemalizika au lah.
“Nalikamilisha sasa hivi mkuu, baada ya dakika
ishirini hivi utapata majibu!”
Akamjibu akificha kueleza hali halisi ikiwemo kipigo
alichokipata toka kwa Samson. Akiwa mtu
asiyependa kukata tamaa haraka alimuhakikishia
kuwa mambo bado sio mazuri sana ingawa
hatarajii kuwa yanaweza kuwa mabaya zaidi ya
hapo.
“Nakutegema Steve, muangalie sana Masurufu,
binafsi naanza kukosa imani nae!”
“Namuangalia vizuri bosi, na angalizo lako lingali
hai akilini mwangu. Ninachokuahidi ni kitu kimoja
tu Cris, sitakuangusha bosi wangu. Sijawahi
kumuangusha mteja wangu na sitakaa niangushe
mtu!” Akatua. Ilikuwa sawa na kiapo.
“Vizuri Steve, kuna la ziada?”
“Hakuna!”
Wakaagana
Steve akainamana na kumuangalia Samson vizuri
akiukubali na kustaajabia uwezo wake wa
kupigana. Ile dhana kwamba afrika hakuna
wapiganaji wazuri, akaifuta. Wazo la kumpiga risasi
ya mguu kumpunguza makali likiondoka.
Akajikuta akitaka kumjua vizuri na kujua anajua
mangapi kuwahusu! Habari za yeye kuhusika na
vifo vya mama Masurufu na akina Michael huyu
alizipata vipi na kwa nini aliitilia mashaka nyumba
hii ambayo ni kweli imehifadhi kila kitu. Je
amewahi kuitembelea kabla, na kwanini amsumbirie
yeye tu hadi usiku?
Ni haya yaliyomfanya atamani kumuhoji Samson.
Akamgeuza kuangalia pale alipopigwa na kile
chuma kilichopachikwa ukutani kiufundi. Jeraha
lilikuwa kubwa kiasi, damu ikiwa imetoka kwa
uchache. Kwa kadiri alivyojua, mtu aliyepigwa na
chumba ile huchukua kati ya dakika arobaini na
tano na saa moja kurejewa na fahamu tena.
Hivyo kabla ya muda huo, alihitaji kufanya
maandalizi kadhaa ikiwa ni pamoja na kumchoma
Samson sindano ya kumpunguza nguvu ili asiweze
kuleta ushindani wa maana na kumfanya ashindwe
kutimiza lengo. Na baada ya hapo ndipo
angeitimiza ile ahadi yake ya kumuua kikatili kwa
mateso makuu ili Samson ajutie kitendo cha
kujiingiza katika mambo yasiyomuhusu, ikiwa ni
pamoja na kumuadhibu yeye steve.
Ni hapa alipoanza kumpekua Samson na kumsachi
hapana na pale na kutoa kila alichokuwa nacho
Samson zikiwemo zile silaha ambazo zilikuwa
mbali kabisa ambazo macho au mikono ambayo
haijafuzu isingweza kuziona kamwe.
“Yu nani mtu huyu!” Steve akajikuta akijiuliza.
Maana silaha na vifaa nilivyokuwa vimefichwa
katika mwili wa Samson vikamfanya ajue kuwa
hachezi na mtoto kama alivyokuwa amefikiria
awali, bali anacheza na wazoefu wanaojua kit
gani wanafanya. Majasusi kama yeye.
Kabla hajaendelea zaidi, simu yake ikaita tena
Masurufu alikuwa upande akikabiliwa na hatari ya
kukamatwa. Steve akaikumbuka ahadi yake kwa
Christopher MacDonald ambayo ilikuwa sawa na
kiapo. Akamtamzama samson na kufikiria kama
anaweza kupata fahamu karibuni. Uwezekano
ulikuwa mdogo.Hata hivyo akajikumbusha uimara
wa jingo hili. Akajiuliza kama atamfungia Samson
kwa nje, kamwe samson asingweza kufungua
mlango na kutoroka kwa kuwa mlango ule ulihitaji
tarakimu za siri ambazo alizijua yeye tu.
Akazificha silaha na zana za Samson, akamvuta na
kumuhifadhi mahala pazuri akimfunga kamba kwa
tahadhari akatoka, akaiparamia gari na kukimbilia
kwa Profesa Zonga kumuokoa Dr Masurufu katika
hatari ya kukamatwa na polisi.

SURA YA KUMI
MAMBO HADHARANI

Aliwahi dakika kadhaa kabla polisi hawajafika.
Akamkuta Dr Masurufu akitetema hovyo huku
akiwa anashindwa hata kufikiria vizuri. Nusura
Steve aangue kicheko pale alipoona Suruali ya Dr
Masurufu ikiwa imelowana. Hata hivyo akajizuia na
kuuliza.
“Kumezidi kitu gani tena?”
“Frank amekamatwa!”
“Mungu wangu!” Moyo wa Steve ukapiga kite na
kuanza kudunda vibaya.
“Amekamatwa lini na kwa nini?” Akauliza kwa
kihoro hali akijitahidi kuirudisha akili yake katika
hali ya kawaida ili aweze kufikiria na kuamua
vizuri. Alikuwa na hakika kuwa akiiruhusu hofu na
woga vimtawale itafika mahala atashindwa
kujihimili na matokeo yake ni kujikojolea kama
alivyofanya Masurufu na kuishia mikononi mwa
Polisi ambapo mchezo utakuwa umekwisha.
“Amekamtwa jana. Ni kuhusu ile issue ya Albino!”
“Mie nilijua tu…” Steve akalaumu. Hata hivyo
akajirudi. Huu haukuwa wakati wa lawama.
Alichotakiwa kufanya ni kuiepusha hatari
inayowakabili, huku akifiria umuhimu wa kurudi
nyumbani kwa Dr Masurufu kumuua Samson na
kuchukua vifaa vyake muhimu tayari kwa kutoweka
nchini.
“Sasa ninyi mmejuaje kama mnakuja kukamatwa”
“Kuna kiongozi mmoja wa vyombo vya usalama,
ngazi ya juu amempigia Simu Profesa Zonga.
Akamwambia ajihadhari polisi wanajua kama
amemficha Dokta Masurufu na wanakuja kumkata
usiku huu!.
“Ni huyo pia aliyewapa habari za Frank
kukamatwa?”
“Ndiyo. Alimueleza Profesa Zonga kuwa Frank
amekamatwa baada ya kutajwa na watuhumiwa
wa mauaji ya Albino na baada ya kuteswa Frank
ametamka kila kitu. Ilikuwa ni baada ya hati ya
kukamatwa kwangu kutolewa ndipo kigogo huyo
alipompigia simu Profesa ili kumtahadharisha! Na
hili nahisi lilijiri kwa kuwa Profesa ana timu kubwa
viongozi wa ngazi za juu anaowahudumia.
“Kwa nini wakukamate kwa hati?”
“Nina historia na nchi hii Steve, mimi ni mtoto wa
mpigania Uhuru kwa Baba. Pamoja na baba
nimelelewa pia na muasisi wa Taifa hili
anayeheshimika sana. Isitoshe nimekuwa Mbunge,
Waziri na baadae Balozi na ningali Balozi hadi leo
hii. Ndio maana nahisi wameona siwezi
kukamatwa kienyeji! Kwa upande wa pili ni bahati
mbaya sana kuona kwamba mkakati wangu
hauelekei kuzaa matunda. Nasikitika sana.
Nauonea aibu mwisho wangu!”
“Hutakamatwa Dokta!” Akamjibu kumpa moyo.
Akaendelea “Believe me or not! Uko na Steve
Lawrance Marvin. Ukiwa mimi daima uko salama!”
“Kiasi naamini Steve. Nakuamini! Ila… Ila….!” Dr
Masurufu akakwama, Steve akamuelewa “Usijali”
Akamwambia na kumuuliza tena. “Kwa hiyo
Profesa Zonga yuko wapi?”

ITAENDELEA
 
MWISHO SEHEMU YA PILI
SIMU: 0755-697 335
“Ndiyo. Alimueleza Profesa Zonga kuwa Frank
amekamatwa baada ya kutajwa na watuhumiwa
wa mauaji ya Albino na baada ya kuteswa Frank
ametamka kila kitu. Ilikuwa ni baada ya hati ya
kukamatwa kwangu kutolewa ndipo kigogo huyo
alipompigia simu Profesa ili kumtahadharisha! Na
hili nahisi lilijiri kwa kuwa Profesa ana timu kubwa
viongozi wa ngazi za juu anaowahudumia.
“Kwa nini wakukamate kwa hati?”
“Nina historia na nchi hii Steve, mimi ni mtoto wa
mpigania Uhuru kwa Baba. Pamoja na baba
nimelelewa pia na muasisi wa Taifa hili
anayeheshimika sana. Isitoshe nimekuwa Mbunge,
Waziri na baadae Balozi na ningali Balozi hadi leo
hii. Ndio maana nahisi wameona siwezi
kukamatwa kienyeji! Kwa upande wa pili ni bahati
mbaya sana kuona kwamba mkakati wangu
hauelekei kuzaa matunda. Nasikitika sana.
Nauonea aibu mwisho wangu!”
“Hutakamatwa Dokta!” Akamjibu kumpa moyo.
Akaendelea “Believe me or not! Uko na Steve
Lawrance Marvin. Ukiwa mimi daima uko salama!”
“Kiasi naamini Steve. Nakuamini! Ila… Ila….!” Dr
Masurufu akakwama, Steve akamuelewa “Usijali”
Akamwambia na kumuuliza tena. “Kwa hiyo
Profesa Zonga yuko wapi?”
“Ameenda Ikulu!” Ameenda kumuomba Rais
amlinde na kadhia hii! Mwenyewe akidai
anasingiziwa na maadui zake!”
Ilikuwa kauli iliyofamfanya Steve acheke kwa
uchungu
“ Na Rais naye anaweza kumsaidia?!”
“Sasa mimi nitajuaje Steve”
“Okay! Tuna muda mchache sana. Jiandae
tuondoke”
“Tunakwenda wapi?”
“Vita vyetu tumezidiwa hatuna budi kukimbia ili
tukaongeze nguvu!”
“Na Polisi Je?” Masurufu aliendelea kuwa na
wasiwasi.
“Hilo niachie mimi!”
“Lakini bado hujaniambia tunakwenda wapi?”
“Nje ya nchi! Ila tunapitia nyumbani mara moja
kuna kazi ya kufanya kabla hatujaondoka!” Steve
akahitimisha.
“Mie sina neno!” Masurufu akakubali. Kumbe
angefanya nini? Wakaondoka. Dakika tano baadae,
gari ya polisi ikaingia. Maelezo waliyoyapata
yakawafanya waelekee Mbezi Beach, nyumbani
kwa Dr Masurufu.
* * *
Samson Kidude alizinduka dakika kumi baada ya
Steve kuondoka. Chumba kilikuwa na giza na
kichwa kilikuwa kikimuuma vibaya. Aliposema
ajigeuze ndipo alipogundua pia alikuwa amefungwa
imara kabisa. Akatulia na kutuliza akili hali
akijitahidi kutafakari kwa nguvu.
Kwa mbali macho yake yalianza kuzoea giza,
akaweza kuziona kamba alizofungwa. Akili yake
ilipotulia na kuanza kufanya kazi vizuri, ikawa
imemchukua dakika tano tu kujifungua kamba na
kuipata swichi ya taa.
Akiwa katika nuru ile, sasa aliweza kukikagaua
chumba kile vizuri. Alikwishagundua kwamba vitu
vingi katika chumba kile vilikuwa vikiendeshwa kwa
kutumia mitambo maalumu inayotumia umeme.
Kwa maana hii ilihitajika akili zaidi, kuliko nguvu.
Akitembea hapa na pale , Samson alianza kuona
mitambo mbalimbali ambayo hakujua kazi yake
mara moja, akajikuta akiwa na kazi mbili ya
kusoma na kujaribu katika kujaribu akagundua
kwamba nyingi zilikuwa silaha, baadhi zilitupa hata
risasi. Ndipo akagundua ni kwanini alipigwa na kitu
kilichomfanya azirai.
Akijua kwamba ugunduzi na pengine kutoka kwake
ndani ya jela hii kunaongozwa na kujaribu, Samson
hakukoma. Aliendelea kugusa hapa na pale na
katika kugusa gusa hivi mara ukuta uliokuwa
unamkinga mbele asione kitu, ukaachana na mbele
yake inatokea ofisi nzuri sana. Ofisi ya kifahari
hasa.
Udadisi unamshika, anasahau maumivu na kupiga
hatua za taratibu kuisogelea. Mbele yake juu ya
meza ile aghali, mbali ya kompyuta, simu ya
mezani, kitufe cha ramani, mafaili na vifaa vingine
vya kiofisi; pia kulikuwa na maandishi
yaliyochongwa kisanifu kabisa kwa kutumia
dhahabu yaliyosomeka Hon. E. Dr Masurufu. H.
Masurufu, President of United Republic of
Tanzania.
Samson akatabasamu kwa uchungu. Ile dhahabu
iliyotumika kuchonga jina lile ingeweza kujenga
Hospitali kama sio shule kadhaa za Sekondari.
Nyuma ya meza ile aghali kabisa kulikuwa na kiti
maridhawa kilichozidia vile vinavyoitwa Executive
chair kwa uzuri. Ukiacha hivi kulikuwa na makabati
kadhaa, mashubaka ya vitabu, droo za chuma za
mafaili na vingine kadha wa kadha.
Vyote viliashiriia kitu kimoja dhahiri, ukwasi
uliokithiri.
Samson akajikuta juu ya kiti kile cha kifahari na
meza ile aghali, akaanza kupekua mafaili kadhaa
yaliyojazana pale juu ya meza. Mihutasari ya
mikutano, hati za ukodashaji helkopta, Orodha ya
timu ya kampeni na mipango mbalimbali ya
ushindi vilikuwa baadhi ya vitu alivyoviona na
kuvipitia kwa haraka, baadhi vikiusisimua moyo
wake.
Hatosheki na nyaraka za juu ya meza, anavuta
droo moja baada ya nyingine na kupitia kila
nyaraka kwa umakini na wepesi wa hali ya juu.
Nyaraka mbalimbali zinatokea na hizi zinakuwa
msaada mwingine kama sio ushahidi wa
kuyathititisha madai ya Tengeneza dhidi ya
Masurufu.
Anapohitimisha zoezi hili, anarudi mezani na
kuwasha kompyuta inamdai neno la siri
anapoingiza jina la Masurufu kompyuta inafunguka.
Anaanza kuita faili moja baada ya jingine.
Anasoma na kusoma na kusoma. Akiwa katika
zoezi hili anagundua kuwa kompyuta
imeunganishwa na mtandao wa Internet. Hili
linamfanya ajitumie kila anachikiona kinafaa katika
barua pepe yake.
Kutahamaki likaja faili la Mkakati wa Kuelekea
Ikulu, Samson akafanya kulifungua kwa pupa.
Haikuwa rahisi. Lilimdai neno la siri. Akajaribu
majina yote ya Dr Masurufu na vitu alivyohisi vina
uhusiano naye bado haukufunguka “Shit!” Samson
akaguta na kusonya.
Akakata tamaa na kuachana na mkakati huo,
akaendelea kuita na kusoma mafaili mengine.
Kulikuwa na mafaili mengi tu na kila moja lilikuwa
na umuhimu wake. Ni katika moja ya mafaili hayo
alipokuta nambari za siri za kufungulia sefu.
Akahamisha macho kutoka katika kompyuta na
kuyazungusha tena humo ndani. Hakukuwa na
sefu. Wakati anajiaanda kupuuza akakumbuka.
Kwamba masefu ya siku hizi ili kubana matumizi
ya nafasi na pengine kuyaficha, huwa
yanayejengwa sambamba na kuta, wakati
mwingine hupigwa rangi moja na ukuta kabisa.
Jambo ambalo hukuwia vigumu kujua kama kuna
sefu humo ndani.
Ni wazo hili lililomfanya anyanyuke pale kitini
akaanza kuusanifu ukuta akifunua hiki na kile. Na
pale kulipokuwa na picha ya Mlima Kilimanjaro
ambayo ilikuwa imekaa kama pambo, akakuta
vinamba kama vile viliyovyopo juu ya Briefscase.
Akazibonyeza nambari za siri, alipomaliza tu sefu
lile maridhawa likafunguka.
Masalalee! Hayo mamilioni ya shilingi na dola za
kimarekani yaliyojipanga na kulala kwa utulivu
yalikaribia kumpofusha macho hata akajikuta
akimeza mafunda kwa mafunda ya mate.
Zilikuwa fedha nyingi mno na kiasi Samson
hakujisumbua hata kufikiria kukisia thamani yake.
Chini kabisa ya fedha zile kulikuwa na droo
ambapo ndani yake kulikuwa na Suitcase ndogo
iliyoandikwa siri. Moyo ukamdunda Samson
Alipoifungua Suitcase hiyo, ndipo alipoikuta nakala
ngumu ya Mkakati wa kuelekea Ikulu pamoja na
mkataba baina yake na G-8 Original.
Samson akivitwaa na kuvisoma.
Akakutana na mambo mazito mazito ambayo
hakuyafikiria kama mtanzania wa kawaida wachilia
mzalendo kama anaweza kufikiria kuvitenda kwa
nchi yake. Ukatili ulioje. Alipomaliza kuusoma
mkakati na mkataba wake, alikuwa akitetembeka
kwa hasira na uoga. Hakutaka kufikiria kama yale
aliyoyaona yakitekelezwa Tanzania itakuwaje.
Naam! Kwa mawazo yake huu haukuwa mkakati
wa kuelekea Ikulu tu bali mkakati wa kuiuza
Tanzania ukiwa umeambatana na mkataba wake!
Hujuma iliyoje kwa Taifa hili maskini!
“Hapana!” Samson akaamua kwa dhati “Nitakuwa
radhi kufa kuliko kuiacha Tanzania ichukuliwe na
manyang’au!” Kama hiyo haitoshi akaapa
kuwapeleka kuzimu wote walio nyuma ya mkakati
huu.
Muda si mrefu Samson, kupitia dirishani akaona
gari, Toyota Land Cruiser VX likiingia na kusimama
hatua chache mbele kidogo ya kijumba
alichokuwemo. Kupitia dirisha lile ambalo
lilimuwezesha wa ndani kumuona wa nje na wa
nje kutomuona wa ndani, Samson akashuhudua Dr
Masurufu na mlinzi wake Steve wakishuka.
“Naam…!” Akajiambia “Kazi imeanza!”
Ingawa hakuwa na silaha. Alijijasirisha na
kujitayarisha kuwapokea akidhamiria kupambana
nao kufa na kupona mpaka atakapowashinda
nguvu na kuwatia mbaroni. Alipokuwa akihifadhi
vitu vile vizuri ndipo jicho lake lilipotua juu ya
meza kwa mara nyingine tena akawa ameiona
simu.
Akajilaumu kwa nini hakupiga simu ofisini kwake,
polisi au kwa Anderson Chilonga kumuomba
msaada. Wazo likamjia kwamba akimbilie simu na
kupiga kuomba msaada. Wazo hili lilizidi kupata
nguvu kutokana na ukweli kwamba atakuwa
akipambana na watu wawili wakiwa katika chumba
chenye mitambo yenye silaha nyingi ambayo
wapinzani wake wanazijua vizuri kuliko yeye.
Hata hivyo akapima uharaka wa kila jambo.
Kwamba itamchukua dakika ngapi kuiendea meza,
kupiga simu na kupokelewa na yeye kueleza shida
yake, na itawachukua sekunde ngapi Steve na Dr
Masurufu kumfikia yeye pale alipo.
Akaachana na wazo hili na kujikusuru kupambana
nao.
Wakati Steve na Masurufu wanaanza kuifuata ile
nyumba, gari nyingine Landlover Difender ikaingia
kwa fujo. Askari wenye silala zaidi ya kumi na
mbili ambao walikuwa wamejificha katika bodi ya
gari, sasa wakajitokeza wakizipunga silaha zao
hewani huku mmoja wao akibweka “Mko chini ya
ulinzi!”
Steve akaduwaa kwa sekunde mbili hivi.
Ulikuwa ni wakati huu pia baadhi ya askari
walipoanza kuruka na kuchukua nafasi. Samson
akiendelea kuchungulia katika dirisha akamshukuru
mungu kuona amemuelewa na kumletea msaada.
Kwa askari wale wenye silaha zile, Samson akajua
ingewawia vigumu Steve na Masurufu kuwashinda.
Maskini kumbe hakumjua Steve vizuri.
Sekunde iliyofuata, Steve alimkamata mkono
Masurufu na kwa kasi ya ajabu akafungua mlango
wa VX na kumsukumia ndani, wakati huo huo
akaruka mpaka upande wa pili wa dereva,
akafungua mlango na kuingia garini kwa kasi ile ile
vitendo vyote hivyo vilitokea ndani ya nukta tatu
au nne hivi.
Akawasha Land Cruiser na kuirudisha nyuma kwa
nguvu na kwa spidi kali kabisa ambapo aliwagonga
askari wanne kati ya sita waliokuwa pale mbele.
Wawili waliosalia akawamaliza kwa Bastola na
haraka haraka akawageukia wengine waliokuwa
wakishangaa na kuwadonoa mmoja baada ya
mwingine kwa kutumia bastola yake yenye
kiwambo cha kuzuia sauti.
Ni pale polisi walipokuja kutahamaki wamebaki
wawili ndipo walipokurupuka na kuanza
kummiminia risasi Steve. Walimimina risasi za
kutosha hasa muda si muda wakasikia Steve
akipiga yowe baada ya kupigwa risasi mkononi.
Pamoja na maumivu, Steve akaing’oa tena
Landcruiser VX na kuitoa kwa kasi kubwa kuelekea
ilipo nyumba ya kuishi ya Dr Masurufu ambako
aliugonga ukuta, ukabomoka na kuingia ndani.
Askari wale waliendelea kumimina risasi hadi
zilipowaishia kulipokuwa kimya, ndipo walipiga
simu kituoni na kuomba waongezewe nguvu. Muda
si muda gari nyingine iliyokuwa na askari wa
kutosha wenye silaha ikafika.
Polisi waliokuwepo wakawapa wenzao taarifa kwa
ufupi, ambapo kundi la askari wenye silaha
wakaizunguka nyumba ya Dr Masurufu ili
kuimarisha ulinzi. Wengine wakaingia ndani
kwenda kumkamata Steve na Masurufu, .
Kule ndani Samson alijitahidi alivyoweza kupiga
kelele za kuomba msaada na kufungua mlango
haikuwezekana. Alipochoka kabisa akampigia simu
Mkuu wake wa kazi Anderson Chilonga pamoja na
msaidizi wake Assia na kuwaeleza kinachojiri
katika nyumba ya Dr. Masurufu na kule
alikofungwa yeye.
Hawa wakamtoa hofu na kumwambia wanakwenda
huko mara moja. Samson akashukuru na kuendelea
kuangalia sinema ile kupitia dirishani.
Ndani askari wale walilikuta gari likiwa tupu.
Wakiongozwa na michinzi ya damu ambayo bila
shaka ilitoka katika jeraha la Steve, Polisi wale
waliingia mpaka katika chumba fulani ambacho
kulikuwa kama stoo hivi.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA MWISHO
SIMU: 0755-697 335
Askari wale waliendelea kumimina risasi hadi
zilipowaishia kulipokuwa kimya, ndipo walipiga
simu kituoni na kuomba waongezewe nguvu. Muda
si muda gari nyingine iliyokuwa na askari wa
kutosha wenye silaha ikafika.
Polisi waliokuwepo wakawapa wenzao taarifa kwa
ufupi, ambapo kundi la askari wenye silaha
wakaizunguka nyumba ya Dr Masurufu ili
kuimarisha ulinzi. Wengine wakaingia ndani
kwenda kumkamata Steve na Masurufu, .
Kule ndani Samson alijitahidi alivyoweza kupiga
kelele za kuomba msaada na kufungua mlango
haikuwezekana. Alipochoka kabisa akampigia simu
Mkuu wake wa kazi Anderson Chilonga pamoja na
msaidizi wake Assia na kuwaeleza kinachojiri
katika nyumba ya Dr. Masurufu na kule
alikofungwa yeye.
Hawa wakamtoa hofu na kumwambia wanakwenda
huko mara moja. Samson akashukuru na kuendelea
kuangalia sinema ile kupitia dirishani.
Ndani askari wale walilikuta gari likiwa tupu.
Wakiongozwa na michinzi ya damu ambayo bila
shaka ilitoka katika jeraha la Steve, Polisi wale
waliingia mpaka katika chumba fulani ambacho
kulikuwa kama stoo hivi.
Ndani ya kile chumba kulikuwa na vikorokoro vingi
na mfuniko wa kitu kama chemba ya choo hivi.
Pembeni ya chemba hiyo kulikuwa na kidimbwi
kidogo cha damu ambacho askari wale walihisi
kama Steve aliitumia sehemu ile kujiganga. Askari
walipojiridhisha kuwa hakukuwa na mahala
pengine ambapo mtu angeweza kujificha,
wakaifunua chemba ile ambayo haikuwa
imefunikwa vizuri
Ngazi zinazoelekea chini zikawalaki.
Handaki! Wakapigwa na butwaa la mshangao
wakati wakiingia chini Haraka. Ndani kulikuwa na
vyumba vinne, vyenye shehena mbalimbali za
mizigo ambayo hawakuitambua mara moja.
Hakukuwa na muda wa ukaguzi, silaha zao zikiwa
tayari tayari wakaongoza kukifuata kijinjia
chembamba chenye kiza kilichokuja kuwatoa
ufukweni mwa bahari ya Lindi.
Mahala walioibukia kulikuwa na boti mbili speed
boat! Katikati ya Boti hizo kulikuwa na uwazi
mkubwa ulioashiria kuwa Speed boat moja ilikuwa
imeondoka. Walipotupa macho Baharini
hawakuweza kuona chochote zaidi ya giza
lililotamalaki na kufunika bahari nzima.
Mawasiliano yakafanyika haraka kuwataka askari
walio mjini waagize boti za Doria zilizomo katika
Bahari ya Hindi waitafute, kuifukuza na kuikamata
haraka boti hiyo ambayo ilikuwa ikiwatorosha
watuhumiwa wao Dr Masurufu Hussein Masurufu
na mlinzi wake Steve.
Wao wakarudi kuwapa taarifa wenzao.
Wakakuta tayari Inspekta Kimaro ameshafika,
alikuwa anawaangalia askari wake waliouawa na
Steve kwa uchungu na masikitiko makuu, hali
majeruhi wakimueleza ilivyokuwa. Inspekta Kimaro
hakuwa pekee, alikuwa pamoja na Mkurugenzi
msaidizi wa Usalama wa Taifa Chilonga Anderson
Chilonga, Msaidizi wa Samson Assia Khalifa
pamoja na maafisa wengine wa polisi.
Vitu aina kwa aina vya Dr Masurufu vikiwa
vimekusanya pamoja baada ya kumfungulia
Samson kwa kutumia Mtaalamu wa mitambo ya
kijasusi kutoka jeshi la Polisi la Tanzania.
Kutoka hapo safari ya kuelekea Makao makuu na
baadae Usalama wa Taifa ilianza ambako Samson
kidude alikuwa na mengi ya kueleza mbele ya
Inspetka Kimaro, Anderson Chilonga, Mkurugenzi
wa Usalama wa Taifa, Katibu Mkuu wa chama,
Mwenyekiti wa Chama Tawala pamoja na Rais
anayemaliza muda wake.
Mwisho wa maelezo yake, Samson aliwakabidhi
Mkakati wa Dr Masurufu wa kuelekea Ikulu, ule
mkataba wa kishetani baina ya Dr Masurufu na
G-8 Original, pamoja na taarifa za uwepo wa
mabilioni kwa mabilioni ya shilingi katika Ofisi na
handaki la Dr Masurufu kule Mbezi Beach.
Viongozi wa usalama pamoja na Rais
walibubujikwa na machozi ya furaha wasiamini kile
wakisikiacho. Kwa mara nyingine tena Samson
kidude kwa kushirikiana na jeshi la Polisi na
Vyombo vya Usalama alikuwa wameliepusha taifa
toka katika hujuma hizo nzito.
Kwao hizi zilikuwa taarifa za ushindi kwa kila hali.
Taarifa za matumaini. Taarifa ambazo zingetoa
onyo kwa G-8 Original na kuwajulisha kuwa huu
ulikuwa mwanzo wa Tanzania kujinasua toka
katika ukoloni mamboleo. Ukoloni wa kifikra,
ukoloni wa kuandaliwa sera na mifumo isiyokuwa
na tija kwa wananchi wa kawaida.
Naam! Taarifa hizi zilikuwa sawa na pigo
lililonyooka.
Rais aliwataka wakuu wa vyombo vya ulinzi na
usalama kuhakikisha Dr Masurufu anakamatwa na
kurejeshwa kizimbani ili sheria ichukue mkondo
wake pamoja na wote walioshiriki katika kadhia la
Dokta Masurufu. Akawaamrisha viongozi wa
chama kumchukulia hatua za kinidhamu ndani ya
chama kwa jinsi alivyoshiriki kukichafua na
kukipaka matope na akataka hatua hizo
zichukuliwe haraka.
Akawataka wakurugenzi wa Usalama waiboreshe
ofisi ya Samson na kuhakikisha anapata kila
anachohitaji. Kwa upande wa rasilimali fedha
zilizokamatwa nyumbani kwa Masurufu, Rais
aliamua kuwa zitaelekezwa katika shughuli za
maendeleo ya jamii ili kuchangia katika harakati za
kupunguza umasikini wa kipato na kuboresha
maisha.
Ilikuwa ni baada ya kila mmoja kuahidi kuyafanyia
kazi maagizo ya Rais ndipo, Samson Kidude
alipoanza kupokea pongezi za dhati kutoka kwa
kila mmoja. “Sidhani kama nastahili pongezi hizi
peke yangu!” Akasema kwa upole na kuendelea
“Kila mmoja amefanya kazi, hivyo yafaa
tujipongeze wote hasa jeshi la Polisi!”
Wakampigia makofi.
* * *
SURA YA KUMI NA MOJA
MALIPO YA UHALIFU
Tarehe mbili, mwezi Mei, Kamati kuu ya Chama
ilikutana katika kikao chake cha dharura, na
pamoja na mambo mengine. Ililiondoa jina la Dr
Masurufu Hussein Masurufu kutoka miongoni mwa
watu wanaotarajiwa kuwa wagombea Urais kupitia
Chama cha Mapinduzi.
Kamati pia ilichuja baadhi ya majina na kumfuta
John Tengeneza ambaye alikuwa amepoteza
maisha hata hivyo haya hayakuvuruga ratiba ya
uchaguzi.
Akiongea na vyombo vya habari katika ukumbi wa
mikutano wa Dodoma Hotel, Katibu Mkuu wa
Chama alisema walikuwa na wajibu wa kuondoa
jina la Dokta Masurufu toka miongoni mwa
wagombea kwa kuwa alikiuka, miiko maadili na
kanuni za chama cha Mapinduzi wakati akishiriki
katika kinyang’anyiro hicho.
Katibu alisema Dr Masurufu amekiuka kanuni hizo
kwa kuingia mkataba wa kihuni na mabepari
wanaotaka kufaidi rasilimali za Tanzania bila
jasho, kushiriki kwa vitendo vya ufisadi na kupora
rasilimali za taifa na kujilimbikizia mali toka wakati
wa vita vya Kagera, Azimio la Arusha, Uhujumu
Uchumi hadi katika misamaha ya kodi zaidi akiwa
mshirikiana.
Hata hivyo aliwataka wananchi kutoihukumu CCM
kwa vitendo vya Dokta Masurufu kwamba hivyo
vilikuwa vitendo binafsi vya mtu na kwamba licha
ya kila dini kuhubiri mema na kukataza mabaya,
bado baadhi ya waumini wa dini hizo wamezama
katika mambo yote waliyokatazwa kama ulevi,
uzinzi, uongo, ulaghai, wizi, usenganyaji na
kadhalika. Kwa hiyo huwezi kuihukumu dini kwa
kuwa na watu kama hawa.
Alisema watu kama Dr Masurufu waliingia katika
chama kwa bahati mbaya kama vile jiwe lipatavyo
fursa ya kuingia katika sahani ya ubwabwa na
katu huu sio mpango wa chama kuwa na watu
kama hawa na ndio maana kila wanapobainika
hutemwa mara moja kam jiwe liliko katika
ubwabwa linavyotemwa pindi likiingia kinywani na
kutafunwa.
Akifafanua zaidi alisema safari ya jiwe kuelekea
katika sahani ya ubwabwa ilianzia mbali toka
shambani. Ambapo mpunga ulivunwa na
kukusanywa. Ni pale tu ulipoanikwa ndipo jiwe
lilipojiingiza kinyemela! Hata ulipoanuliwa juani na
kupigwa au kutwangwa na pengine kukobolewa
jiwe liliendelea tu kung’ang’ania.
Safari ya kuupeleka mchele sokoni, mama akaja
kuununua na kuuchagua, kuupepeta na kuuchuja,
Bado tu jiwe liliendelea kuwemo. Hatimaye mchele
unapikwa na kugeuka wali, unapakuliwa katika
sahani, jiwe bado limo tu. Na lilivyo na tabia
mbaya, jiwe hili hukimbia katika sahani ya baba au
ya mgeni na kutoa tafsiri kwamba mama hajui
kupika.
Akawataka wananchi wajue kuwa hata katika CCM
bado kuna mawe mengi na wataendelea kuyatoa
kadri yatakapobainika kwani sio matarajio ya
chama kuwa na mawe! Akawataka wananchi
wajitokeze kwa wingi siku ya uchaguzi na
kuichagua CCM kura nyingi.
Hotuba yake iliwasisimua na kuwavutia wengi.
Habari hizo zilipotoka zikawafanya watu washike
vichwa kwa uchungu na mshangao. Wasiamini
kama Masurufu huyu, aliyezaliwa na mpigania
Uhuru, akasomeshwa na kulelewa na baba wa
Taifa ndiye anayefanya haya.
“Laiti Mwalimu angelikuwepo na kujionea kizazi
alichokilea na kukisimamia kinavyopotoka?” Baadhi
waliwaza kwa hitimisho, wakisikitika na kuondoka.
Naam! Siku chache baadae Profesa Zonga, Frank,
Kuho, Robison na wauaji wenzao wa raia wenye
ulemavu wa ngozi nao walifikishwa mahakamani.
Ushahidi wao ukiwa dhahiri na mwingine wakiwa
nao, upelelezi ulifanyika haraka na muda mfupi
baadae wakawa wamehukumiwa kifungo cha
maisha na kazi ngumu jela.
* * *
Baada ya chenga za hapa na pale zilizowachukulia
muda na fedha za kutosha, hatimae Steve na
Masurufu walifika Afrika Kusini wakiwa
wamemaliza akiba yao yote. Steve akampigia simu
Christopher McDonald ambaye aliwatumia ndege
ya kukodi iliyowafikisha Uingereza.
Christopher aliwapokea vizuri akaenda nao mpaka
ofisini kwake na wakampa habari za kina kwa
mara nyingine, habari ambazo zilikuwa zaidi ya zile
alizozipata kupitia vyombo vya habari vya BBC na
CNN.
“Hongera Steve!”Akamwambia baadae. “Umefanya
kazi nzuri kumleta Masurufu. Hii ni theluthi
nyingine ya malipo yako. Kesho utamaliziwa
theluthi iliyobakia na tutakuruhusu urudi zako
Miami! Tayari tumekuandalia hoteli nzuri ya
kufikia”.
Akatua na kujiwashia sigara, akatoa moshi mwingi
na kupuliza hewani. Halafu akamgeukia Masurufu,
“Wewe nenda kapumzike bila shaka G-8
watapenda kuyasikia haya unayonieleza.
“Chris naomba tena, niko chini ya miguu yenu. I’m
very very sorry Chris!” Machozi yakamtoka.
“Najua! Lakini kesho tutaongea mengi zaidi!”
Alipomaliza kusema hayo walikuja watu wawili,
mmoja akamchukua Masurufu na mwingine
akamchukua Steve wakaondoka nao hadi katika
Hotel ya nyota tano pale Uingereza. Kila mmoja
akakabidhiwa chumba chake.
Steve alipobaki peke yake akainua ile briefcase
yake yenye fedha na kuifungua. Badala ya fedha,
ukatoka moshi fulani mweupe. Ulikuwa na harufu
nzuri hujaona na ulimuingia Steve moja kwa moja
puani.
Steve alipokuja kutahamaki kwamba anavuta sumu,
tayari alikuwa amekwisha chelewa, nguvu zilikuwa
zikipungua mwilini mwake kwa kasi ya ajabu.
Akajitahidi kuinuka akimbilie bafuni akapate maji
ambayo yalikuwa dawa ya sumu hii, hakuweza,
akaanguka vibaya, mwili ukikosa nguvu hata ya
kujikokota.
“Shiit!” Akajitahidi kujuta akijilaani na kuilani
bahati yake. Sauti pia haikutoka. Akili ikapoteza
uwezo wa kufikiri akaanza kudidimia katika shimo
lefu la kiza ambalo halikuwa na mwisho. Ukawa
mwisho wake.
* * *
Dr Masurufu alikuja kuchukuliwa siku ya pili
asubuhi na kupelekwa katika chumba fulani
ambako alikuta timu yote ya G-8 Original
ikimsubiri.
Hapo tena akatakiwa kueleza kilitokea nini, hata
mpango wao ukafeli licha ya wao kuwekeza
mamilioni kwa mamilioni ya shilingi. Akijua hii
ndiyo nafasi yake ya mwisho, Masurufu alieleza
hatua kwa hatua mpaka hali ilipofikia.
“Umenisikitisha sana Masurufu!” Akasema
Christopher mwisho wa simulizi. “Ulishindwa nini
kuomba ushauri kabla? Kwa hasara uliyotuingiza
tuambie ni kwa nini hustahili kufa!”
“Kufa?” Masurufu akashtuka. “Oh! Hapana jamani…
No… Nooooh! Nina mipango mbadala ambayo
itarejesha fedha mliyotoa na faida. Nina familia na
wazazi wanaonitegemea! Nina… Nina…!”Alisema
mengi ambayo hayakuwaelea G-8 Original, zaidi
akiomba msamaha na kwamba katika mpango
mwingine atakuwa makini zaidi. Ataomba ushauri
na kadhalika.
“Okay!Unaweza kwenda!” Akaambiwa alipomaliza
kusema.
Masurufu hakuyaamini masikio yake, kirahisi hivi.
Akawaza na kuuliza kutaka uhakika “Eti
umesema?”
“Unaweza kwenda!”
“Je” Akatua akiwatazama mmoja baada ya
mwingine “Mmenisamehe?”
Wajumbe wakatikisa kichwa juu na chini kukubali.
Dr Masurufu akaomba dua, kumshukuru Mungu na
kuwashukuru Christopher McDonald na wenzake.
Kabla hajainuka akaanza kuvuta hatua na
kuondoka.
Alipoukaribia mlango tu, Christopher McDonald
akatoa bastola na kumpiga Dr Masurufu risasi ya
kisogo ambayo ilimpaisha na kumsomba mzima
mzima, ikampigiza ukutani kwa nguvu. Alipotua
chini alikuwa maiti.
“Number one!” Masurufu akasema baada ya
kubonyeza mahala ukutani. Dakika hiyo hiyo
akaingia mwanaume mmoja mwenye asili ya
kichina aliyechanganya damu na mjapani. Huyu
alikuwa Ben Tapeli.
“Niko hapa Sir!”
“Vipi kazi ya hotelini?” Akamsaili.
“Imekwenda vizuri sana. Steve ameingia kuzimu
jana jioni kwa kutumia ileile sumu hatari tuliyoipata
South Korea. Hakukuwa na upinzani kabisa. Alikufa
mara moja. Bila shaka anamkaribisha mwenzie
sasa hivi!” Akihitimisha kwa utani.
Akina Christopher wakacheka.
“Ilikuwa ni lazima afe. Uzembe wake wa
kutomsimamia Masurufu vyema umemgharimu!”
“Kabisa bosi!”
“Tafadhari tuondolee huu mzoga ndani. Unastahili
kuwa chakula cha samaki baharini!” Akaamrisha.
Jamaa akaanza kutekeleza kazi aliyotumwa,
akiacha Christopher akiwaomba radhi wenzie kwa
kufeli kwa mpango wao.
Walipomsamehe ndipo walipoanza kuumiza vichwa
kutafuta namna ya kulipiza kisasi kwa watanzania
na serikali yao kufidia hasara waliyoingia.
Walidhamiria kutoka na mkakati ambao utakuwa
sawa na pigo takatifu sana. Pigo lenye nguvu
kupita kiasi. Pigo litakalofanya sio tu Tanzania na
Afrika ilie pekee bali na kusaga meno!
Waliendelea kutafuta.
* * *
Maiti ya Dr Masurufu yaliokotwa kando kando mwa
ufukwe wa Bahari katika jimbo moja nchini
Ufaransa. Iliwachukua muda mfupi tu Polisi
kugundua kuwa walikuwa wameuokota mwili wa
aliyekuwa anataka kugombea urais wa Tanzania
kutokana na nyaraka zilizokutwa mfukoni mwake.
Habari hizi zilipofika Tanzania, hakuna aliyelia!
MWISHO.

KITABU HIKI KINAPATIKANA MITAANI, KWA
MAELEZO ZAIDI WASILIANA NA MTUNZI KWA
NAMBA ZAKE HAPO JUU.
 
Back
Top Bottom