Riwaya; Mauaji ya kasisi

Dam55

JF-Expert Member
Oct 8, 2015
5,592
11,831
RIWAYA: MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE
Simu: +255 766 974865

UTANGULIZI

MAUAJI YA KASISI
© Richard Richard Mwambe

Ni kizaazaa katika jiji la Nairobi, Kasisi wa kanisa katoliki anauawa katika lango kuu la kuingilia kanisani hapo mapema alfajiri. Sajini Maria na wasaidizi wake wanaingia kazini kuwasaka wauaji.

Nyuma ya pazia la mauaji hayo, jasusi linalotafutwa na idara mbalimbali za usalama duniani ikiwemo ile ya Tanzania (TSA), Bill Van Getgand, anahusishwa na mauaji hayo kwa kuwakodi majambazi ambao anawalipa pesa nyingi kumuua kasisi huyo na kisha kuiba monstrance iliyotoka makao makuu ya kanisa hilo, Vatican, kwa ajili ya adhimisho la jubilee ya miaka 100 ya Ukristo nchini Kenya.
Idara mbalimbali za usalama duniani ikiwemo ile ya Tanzania zinatambua uwepo wa jasusi huyo, hivyo msako unaanza ndani ya jiji la Nairobi na viunga vyake.
Kamanda Amata anajikuta tena katika sakata hili gumu ambalo linaihatarisha kazi yake na maisha yake kwa ujumla. Anarudishwa Tanzania akiwa hoi, hajitambui. Anapopata fahamu anaamua kumrudia jasusi huyo ili kumfunza adabu wakati huo akiwa hatambuliki na idara yake ya usalama.

Bill anatoroka baada ya kuipata ile monstrance na kuwaua walio jirani nae ili wasije kutoa siri endapo watajikuta mikononi mwa polisi. Baada ya kazi nzuri ya Kamanda Amata mpaka kugundua ni wapi jasusi huyo yupo, idara yake inamrudisha kazini na kumtuma ama kumkamata au kumuua kabisa jasusi huyo anayesumbua dunia.
Ndani ya mji wa Aachen, Ujerumani Kamanda Amata anafanya kazi ngumu akipata vikwazo kutoka shirika la upelelezi la USA…. Nini kilijiri huko Ujerumani?
Soma riwaya hii tamu MAUAJI YA KASISI na mwenyewe utasema hakika hii ni riwaya kali kuliko zote…

*****************************************************

SEHEMU YA KWANZA

1
HOLY FAMILY BASILICA
NAIROBI – saa 01:00 asubuhi

HAKUNA mtu aliyeamini anachokiona mbele yake, kila aliyepita njia alitikisa kichwa na wengine kuangusha machozi. Polisi kutoka kituo cha kati cha Nairobi walikuwa hapo mbele ya kanisa hilo kubwa wakifanya uchunguzi wa hili na lile. Mwili usio na uhai ulikuwa umelala chini na majeraha makubwa kifuani yakiwa yameganda damu nzito. Hakuna asiyejua mwili ule ni wa nani, kila aliyepita alisikitika, wengine hata walighairisha safari zao za kazini, vilio vilitawala eneo lile. Kila mtu alionekana kuguswa kwa namna moja au nyingine na mauaji ya Kasisi huyu wa kanisa la Roman Catholic, Rev Fr Frederick Gichuru, hakuna aliyejua kwa nini na ni nani aliyetekeleza mauaji haya ya kinyama. Baada ya kumsachi hakuna cha ziada walichokikuta katika kanzu ya kasisi huyo zaidi ya rozari iliyokuwa mkononi mwake.

“Bila shaka alikuwa katika sala zake za asubuhi” sauti ya kukwaruza kutoka kwa koplo Otholong’ong’o ilipenya sikioni mwa sajenti Maria Kariuki ambaye kwa muda huo alikuwa bado amepigwa na butwaa. Sajenti Maria alisikitika na kujutia nafsi yake, alijiona kama mwenye makosa mbele ya Mungu kwa kifo hicho.
“Ndiyo, afande, daima asubuhi kabla ya misa makasisi wa kikatoliki huwa na wajibu wa kusali kwanza wao weyewe” Sajenti Maria alimjibu koplo Otholong’ong’o huku ukungu mzito ukimtoka kinywani mwake kuashiria baridi kali ya mwezi wa sita hapo Nairobi. Bado sajenti Maria alikuwa kajiinamia jirani kabisa na mwili ule akiuangalia kwa makini jinsi ulivyoharibiwa kwa risasi, maganda saba ya Colt 45 yalikuwa mkononi mwake, huku akiyarusharusha alijinyanyua taratibu na kuamuru mwili ule uondolewe na kupelekwa chumba cha maiti cha hospitali ya rufaa.

§§§§§

Inspekta Simon Saitoti alimkazia macho sajenti Maria aliyekuwa ameketi mbele yake akiwa na jalada moja la khaki lililoandikwa juu ‘MAUAJI YA KASISI’, alionekana kama mtu ambaye haelewi anachoelezwa, alilivuta jalada lile na kuliperuzi kurasa zake chache kwa dakika kadhaa, kisha akainua macho yake kutazama ukutani ambako kulipambwa kwa picha ya muasisi wa taifa hilo, hayati Jomo Kenyatta.

“Umesema paroko wa kanisa hilo hamjamkuta, sivyo?” Inspekta Saitoti alimtwanga swali sajenti Maria.
“Ndiyo afande, na tulipowauliza masista walisema kuwa kawaida wanakuwa na zamu ya kufanya misa za asubuhi vigangoni, hivyo paroko alikuwa amekwenda kigangoni” Maria alijibu kwa ukakamavu wa kipolisi.
“Ok, mauaji kama haya hayajawahi kutokea hapa kwetu hii ni mara ya kwanza, na naomba sana iwe mara ya mwisho, endelea kufanya uchunguzi wa tukio hili kwa kina ukishirikiana na koplo Otholong’ong’o na mnipe taarifa za kina, ili tuwatie mbaroni wauaji.”
“Sawa afande” sajenti Maria alisimama na kurudi nyuma hatua mbili na kupiga saluti ikiwa ni kitendo cha kuonesha heshima kwa mkubwa wake kadiri ya nidhamu za kipolisi.

§§§§§

Kijua cha haja kililing’aza jiji kubwa la Nairobi, jiji lenye pilikapilika za kila aina katika ukanda wa Afrika ya Mashariki. Watu walionekana wakitembea na kuvuka barabara kwa haraka haraka kuashiria kuwa ukichelewa tu matatu itakugonga. Bado hali ya ubaridi ilikuwa ikiendelea na kila mtu alionekana kujidhatiti kwa hali hiyo.
Kwenye kituo kimoja cha basi, mwanaume mmoja mrefu alikua amesimama akisubiri matatu, mara tu matatu moja ikafika na muziki mkubwa ndani yake, akaikaribia na kupanda ndani yake, mkononi alikuwa na mfuko wa plastiki ulioandikwa UCHUMI, bila shaka alikuwa akitoka supermarket, safari yake kwa matatu hiyo iliishia katika kitongoji cha Uthiru Kenoo barabara kuu ya kwenda Uganda. Kwa mwendo wa wastani alivuka kwa kupitia daraja kubwa na kufika upande wa pili wa barabara hiyo ambapo kuna biashara nyingi, aliliendea gari aina ya Hammer lililokuwa limepaki hapo, ndani yake hakukuonesha dalili yoyote ya kuwapo mtu, alifungua mlango kwa kidubwasha maalum na kuuweka ule mfuko katika kiti cha mbele kisha akatokomea kusikojulikana.
Takribani nusu saa hakuna aliyeisogelea gari ile, mara akaja mtu mwingine mnene wa haja pamoja na mwanamke mmoja mrefu na mwenye mwii ulioumbika vizuri, wakaingia ndani ya gari ile na kujifungia milango.
“Shit, washakosea tena” alisikika Yule mtu mnene akimwambia Yule mwanamke
“Nini tena?”
“Hawako makini na kazi yao, tunawalipa pesa nyingi lakini hawajui nini cha kufanya, nguruwe wakubwa hawa”
“Kwani nini?” Yule mwanamke alizidi kudadisi
“Ah, we yaache tu, hutakiwi kujua”
“Aaa jamani, yani umelala na mimi umenambia vingapi mpaka hili usinambie?”
“Mambo ya kazi haya, achana nayo”.
Ile gari ilitiwa moto na kurudi mjini, hakuna ambaye angekaa bila kulitupia macho gari hilo kwa jinsi lilivyo na uzuri wa aina yake na gharama yake ndiyo iliyotia kiwewe.
Moja kwa moja gari ile ilisimama karibu kabisa na mtaa wa Koinange, mtaa unaosifika kwa machangudoa hapo Nairobi.

“Nitakucheki usiku twende club” mtu mnene mwenye asili ya kihindi alimwambia Yule mwananmke na kumpa noti za shilingi elfu moja moja tano za Kikenya.

§§§§§

Askofu mkuu wa jimbo kuu la Nairobi, Mhashamu Gregory Julius Maina, akiwa ofisini kwake alishikwa na huzuni kubwa kwa habari ya mauaji ya Fr Gichuru, alimlilia na kumuombea lakini hakujua ni nini hasa chanzo cha kifo hicho. Alitafakari na kuumiza kichwa, kisha akainua macho yake na kutazama jopo lile la makasisi lililokuwa mbele yake, kila mmoja alikuwa ama akiangusha au akijifuta machozi, ukumbi wa parokia ya Maria Consolatha katika eneo la Westland ulikuwa umetulia kimya kabisa kana kwamba hakukuwa na watu ndani yake.
“Nawasalimu katika jina la Bwana” Askofu aliwasalimu makasisi wale wapatao kama mia mbili weupe kwa weusi.
“Amen” waliitikia.
“Nina masikitiko moyoni, kuwatangazia rasmi kifo cha kasisi mwenzetu padre Frederick Gichuru, paroko msaidizi wa parokia ya Familia Takatifu, kilichotokea leo alfajiri kwa kupigwa risasi tatu kifuani na kupoteza uhai papo hapo” alifuta machozi na kukaa kimya kidogo, kisha akaendelea “Tunalaani vikali kabisa mauaji haya yasiyo na sababu inayoeleweka, hatuna cha kusema zaidi ila sisi kama kanisa tunaiomba serikali na vyombo vyake vya dola vifanye kazi ya kuwatia nguvuni wote wanaohusika, na tunawaomba raia wema wanaojua tetesi yoyote ya kifo hiki kutoa taarifa polisi au hata kwetu ili kusaidia katika kupambana na kadhia hii. Zaidi ya yote Bwana awasamehe kwa maana hawajui watendalo. Ibada ya mazishi itafanyika keshokutwa katika Basilica la Familia Takatifu” alimaliza Askofu kutoa tamko kwa niaba ya kanisa, kisha kuwapatia Baraka na wote wakatawanyika.
“Baba, pole kwa msiba” Kasisi mmoja alimsalimu paroko wa Basilica la Familia Takatifu ambaye msaidizi wake ndiye aliyeuawa asubuhi hiyo.
“Tumeshapoa, Mungu mwenyewe anajua”
Mara gari ya polisi aina ya Land Cruiser iliingia katika viwanja vya kanisa hilo la Consolata, sajenti Maria alikuwa wa kwanza kuteremka, akiwa ndani ya suruali yake ya buluu na shati la buluu bahari alipendeza kwelikweli. Alifanya juu chini kumpata Padre Joe Smith, raia wa Marekani ambaye ni paroko wa Basilica lililotokea mauaji, alipompata alimuomba kuongea naye machache na wote wakaelekea katika ofisi ya parokia hapo Consolatha.
“Pole sana baba kwa msiba, naitwa sajenti Maria kutoka kituo cha polisi cha kati Nairobi”
“Asante, tumeshapoa” alijibu Fr Joe Smith kwa Kiswahili chake kinachopendwa na wengi hasa anapotoa mahubiri.
“Wakati tukio linatokea, wewe ulikuwa wapi asubuhi hiyo?”
“Mimi nilikuwa nimekwenda kufanya misa ya asubuhi kigangoni”
“Siku hiyo ni wewe ulitakiwa uende kigangoni?”
“Hapana, kadiri ya ratiba siku hiyo haikuwa zamu yangu”
“Enhe sasa ilikuwaje ukaenda?”
“Fr Gichuru, usiku wa jana alinambia kuwa yeye hajisikii vizuri, hivyo angependa kubaki parokiani” alimjibu sajenti Maria ambaye alionekana kuandika vitu Fulani kwenye kitabu chake.
“Je unafahamu lolote kama marehemu alikuwa na ugomvi na mtu, au hali yoyote tofauti iliyokuwa katika maeneo yenu kama wachungaji?”
“Kwa kweli katika siku hizi, kumekuwa na mambo ya ajabu kabisa, kuna watu walikuwa wanakuja sana pale parokiani na kuuliza mambo mengi kwa watoto watumishi, wakati Fulani tulimkuta mtu anapekua Sacristia, walipomuuliza akawachapa makofi.”
“Mlichukua hatua gani?”
“Niwaulize ninyi polisi, mimi nilipiga simu polisi na mkaahidi kuja kufanyia uchunguzi lakini bho! Sikuwaona”
“Sawa, msaidizi wako alikuwa na mahusiano ya kimapenzi na mtu yeyote awe sista au mwingine yeyote?”
Fr Joe alishtuka kidogo kwa swali hilo. Sajenti Maria akatoa tabasamu lake lisilo nahisia hata kidogo mbele ya watu.
“Mbona umeshtuka baba?”
“Eh nikikuuliza wewe kama una mahusiano na kasisi hautashtuka?” wote wakacheka kisha Joe akaendelea “Hakuna kitu kama hicho, kama kipo basi mimi sijui”
“Haya, asante sana baba, kama nikikuhitaji nitakutafuta” wakapeana mikono na kuagana.

Sista Rose alikuwa akibubujikwa na machozi mbele ya sajenti Maria.
“Usilie Sista, ni maswali machache tu nataka kukuuliza”
“Sawa afande”
“Wakati mauaji yanatokea wewe ulikuwa wapi?”
“Muda huo mimi nilikuwa natoka nyumbani kwetu naenda kuandaa misa kanisani…

Ilivyokuwa

…Ilikuwa yapata saa kumi na moja na nusu alfajiri, sista Rose alikuwa na zamu ya kwenda kuandaa misa, aliamka na kujiandaa, kisha akiwa ndani ya mavazi ya kitawa alitoka nje ya nyumba ‘coventi’ yao na kwa mwendo wa taribu na rozari yake mkononi alikatisha kauwanja kanakotenganisha nyumba yao na kanisa, mara alisimama ghafla moyo wake ulifanya paaah! Hakujua kwa nini, kwa mbali alimuona Fr Gichuru akiingia kwenye uwanja wa kanisa hilo akiwa kwenye vazi lake jeusi na kofia nyeusi yenye nyoya katikati, alivaa kikasisi hasa na si mara nyingi kuonekana katika mavazi haya. Alikuwa akitembea taratibu na mara walikutana na sista Rose katikati ya uwanja, wakasalimiana kwa ishara lakini Fr Gichuru alibaki kasimama akimwangalia sista Rose, akamuonesha ishara ya kuwa ainamishe kichwa chake, sista Rose akafanya hivyo na Fr Gichuru akamuwekea mikono kichwani kumbariki, mara mwanga wa taa za gari ukawamulika kutoka getini, hakuna liyejua ni gari ya nani, Fr Gichuru akamuacha Sr Rose aendelee na shughuli yake yeye akaliendea geti…

Sista Rose alikuwa kajibanza kwenye ua kubwa lililo karibu kabisa na mlango wa kuingilia sakristia, akiangalia kinachoendelea, baada ya mabishano mafupi kati ya Fr Gichuru na wale jamaa waliokuja na ile gari mara alishuhudia kasisi yule akianguka chini kwa kishindo na sauti ya kike iliamuru wengine kupanda garini na kuondoka kwa kasi. Sista Rose alibaki akitetemeka huku machozi yakimwagika na si kumbubujika, alishindwa afanye nini, awaamshe wenzake au aende kumsaidia Fr Gichuru, alikuwa njia panda hakujua afanye nini. Gari ile ilipoondoka alirudi nyumbani kwao akilia na kuwapa taarifa wenzake ambao wote waliamka na kwenda kuona tukio hilo kisha kupiga simu polisi na kwa paroko ambaye alikuwa ameenda kigangoni kwa misa ya alfajiri…

“Poleni kwa msiba huo mzito” sajenti Maria alitoa pole akiwa na macho makavu kabisa, “Labda sista niambie, unaweza kukumbuka aina ya gari walilokuja nalo?”
“Kwa kweli ni shida kulikumbuka kwa kuwa kulikuwa na giza na mi nilikuwa mbali kidogo” sista alijibu.
“Kipi cha pekee unachokumbuka katika tukio hilo?”
“Sauti ya mwanamke iliyokuwa ikimhimiza mwenzake kumaliza kazi, nilisikia wakitamka jina ‘Black Cheetah’” alimaliza na kutungua kilio.
“Ok waweza kwenda tutakapokuhitaji tutakupa taarifa.

§§§§§

Black Cheetah, jambazi sugu linalotafutwa na polisi ukanda wote wa Africa Mashariki, linajikuta katika sakata jipya, sakata la mauaji ya kasisi. Kila mtu aliamini kuwa jambazi hilo si bure tu bali linatumia hata nguvu za giza kwa jinsi linavyoweza kuwatoroka polisi katika mazingira ya kutatanisha hata wenyewe kushindwa kujielewa inakuwakuwaje. Hakuna aliyekuwa halijui jina hili, si mtoto wala mtu mzima, jina la Black Cheetah halikuisha midomoni mwao.

Sajenti Maria alishtushwa kusikia jina hilo likitajwa na sista Rose kuwa aliisikia sauti ya kike ikilitamka katika tukio hilo. Alitafakari akaona kibarua hicho si cha kitoto ni kucheza na mtu au watu waliokomaa kwenye taaluma.
Black Cheetah, kama anavyojiita ni kijana mtukutu, mkakamavu, muasi aliyetoroka katika kundi lao la M23 huko mashariki mwa Congo, aliyetokea kuwa jambazi sugu na tishio katika ukanda wote wa Afrika ya mashariki, alikuwa akikodiwa na matajiri wakubwa kutekeleza mauaji au wizi wa kutumia silaha. Mara kadhaa ameshahusishwa na wizi wa benki uliotokea Dar es salaam Tanzania miaka michache iliyopita, mlipuko wa bomu uliotokea Kampala wakati watu wakiangalia mpira na matukio mengi yaliyotukia huko Kenya ambayo hata hatuwezi kuyaainisha hapa, kwa ujumla alikuwa gaidi.

Mwezi mmoja uliopita
Ngong Hills Hotel-Nairobi

GARI AINA ya Hammer nyeusi ilisogea taratibu katika maegesho ya hoteli ya Ngong Hills, watu watatu, wanaume, wakashuka wakiwa ndani ya suti nyeusi zilizotanguliwa na shati nyeupe, mmoja kati yao mwenye mwili mnene alikuwa akitembea kwa msaada wa fimbo maalum, taratibu waliingia hotelini hapo na moja kwa moja wakaelekea sehemu ya chakula na kuchukua meza yenye viti vine na kuketi, kiti kimoja kilibaki wazi wakaagiza vyakula na vinywaji na kuanza maongezi yao. Maongezi yaliendelea na baada ya muda kidogo kijana mmoja aliingia mahali pale akiwa kavalia koti kubwa la bluu nyeusi akiwa na kofia kubwa aina ya pama, kwa hatua za maringo aliijongea meza hiyo, kila mtu alimuangalia kwa mwendo wake hususan camera za usalama. Alifika katika meza ile na kuvuta kiti kimoja kilichobaki kikimsubiri yeye, akaketi na kuiweka bilauri yake vizuri kabla ya kuimiminia kinywaji kilichokuwa hapo.

“Yes, Cheetah…” yule bwana anaetembea kwa msaada wa fimbo alimkaribisha
“Nimeitika wito wako, bwana Bill” Cheetah alijibu.
“Vizuri, hawa ni wadau wenzangu ambao sote tumekuita ili tukupe kazi maalum” aliendelea
“Nawasikiliza”
“Kuna kazi ndogo tunataka utufanyie” alizungumza bwana Wambugu, akajikohoza na kuendelea “Tunataka kitu kinachoitwa Monstrance, kimehifadhiwa katika kanisa kuu la Familia Takatifu hapa Nairobi, of course ni kazi ndogo tu”
“Hakuna kazi ndogo kama itahitaji kumwaga damu, hasa damu ya watu wasio na hatia” Cheetah alimjibu Wambugu
“No! hatumwagi damu, ni kujua ilipo na kuichukua basi”
“Unafikiri tutaipata kwa urahisi kama unavyofikiria? Maana ingekuwa hivyo basi hata wewe ungeenda pale na kuichukua, lakini kama umeniita mimi maana yake ni kwamba hiyo si kazi ndogo kwa vyovyote lazima vyuma vitaongea” Cheetah alimaliza kauli yake na kuinua bilauri iliyojaa kilevi na kujimiminia kinywani mwake baada ya kulishuighulikia pande la nyama lililokuwa ndani ya sahani hiyo.

“Hilo nalo neno bwana Cheetah. By the way wewe utajua la kufanya, sisi tunachotaka ni Monstrance basi” alimaliza bwana Wambugu.
“Ok, tusipoteze muda, mimi nitaunda kikosi kazi kitakachoweza kufanikisha kazi hiyo, lakini mjue kule ni kanisani, wale makasisi wana mazindiko yao, hivyo lazima mnipatie fedha iliyotakata”
“Ha ha ha ha ha hilo usitie shaka bwanaaa bwana Cheetah” cheko la kivivu lilimtoka yule bwana anyetembea kwa fimbo, kisha akainua simu yake na kubofya namba kadhaa, punde tu vijana wawili waliingia pamwe na briefcase ndogo mkononi, ikawekwa mezani, kwa ishara ya mkono ya mkono yule bwana alimuomba Wambugu kuifungua, baada ya kuzungusha vijinamba Fulani mara yenyewe ilifyatuka kuashiria kuwa kilichopo kiljaa ndani yake kwa kukandamizwa hasa. Naam manoti yenye sura za Moi na Kenyatta yalipangwa na kubanwa katika mabandali kibao, Black Cheetah macho yalimtoka pima.
“Ukifanikisha kazi basi hata briefcase hii ni mali yako” yule bwana alizungumza kivivu.

Black Cheetah alitikisa kichwa juu chini juu chini kuashiria amekubaliana nao. Kwa kuanzia alipewa mabandali kadhaa katika mfuko wa plastiki. Waliagana wane hao na Cheetah akaondoka zake akiwaacha wao wakiendelea kutumbua mavyakula yaliyojaa mezani hapo.
Katika maegesho ya magari, Cheetah aliisogelea gari yake na kusimama kidogo kisha akaangalia uku na huku, hakuona yeyote wala chochote cha kushuku, akaingia na kukaa nyuma ya usukani, milango ikafungwa na vyoo vyote vikabaki juu. Aliufungu ule mfuko wa karatasi na kuhesabu burungutu zile, si haba takribani laki mbili za Kenya, alikenua kwa furaha na kulazimisha tabasamu ambalo halikuendani na uso wake khasilan. Alitia gia na kuyaacha maegesho, baada ya kulivuka geti moja kwa moja aliningia barabara ya Ngong na kurudi katikati ya jiji la Nairobi.

“Hivi unafikiri tutafanikiwa kuipata?”Wambugu alimwuliza yule bwana anyetembelea fimbo
“Ha ha ha ha Wambugu unanichekesha sana, kazi iko kwa Cheetah lazima atararua mpaka tuipate, na tukishaitia mkononi yule Don kule Ujerumani atatukatisha kwa pesa nyingi, si ya kitoto” aliongea kwa sauti yake ya kivivu huku mdomoni akitafuna vyakula aina aina.
“Don!” Wambugu alishangaa
“Yeah, Don, anaitwa Don Fredrick Schurmann, ni tajiri sana katika mji wa Achen, yeye ndiye anayetaka hiyo Monstrance, amesema tukiifikisha mikononi mwake tutapata pesa nyingi sana, ha ha ha ha !” alimaliza kwa kucheka na kunyanyua bilauri yake iliyojaa mnvinyo wa Sant Raphael.

§§§§§

Katika bar kubwa ya Dagoreti Corner super pub, watu walijaa sana wakiburudika kwa vinywaji, nyama choma huku muziki laini wa The Mushroom ukisikika kutoka katika spika kubwa zilizozunguka eneo hilo. Hakuna aliyefikiria kesho kila mmoja alijiachia kwa starehe zake alizoziona kuwa zinamfaa, ilimradi siku ilipita katika mtindo huo. Katika kona moja ya pub hiyo watu watatu waliketi katika mtindo wa mzunguko mmoja wao alikuwa mwanamke walionekana kana kwamba wana mazungumzo mazito sana, hivyo hakuna mtu ambaye alisogelea eneo lile zaidi ya mhudumu wa pub hiyo, naye alikuja tu kuleta alichoagizwa na kuondoka zake.

“Ndiyo vijana, kuna kazi ya kuifanya haraka iwezekanavyo” Cheetah alianzisha mazungumzo.
“Tunakusikia mkuu” sauti pekee ya kike iliiitikia kauli hiyo.
“Tunatakiwa kuchukua mzigo pale Holy Family Basilica”
“Mapesa mangapi tukachukue?” aliuliza kijana mwingine aliyeketi hapo.
“Siyo pesa Bwana Gichui, kuna kitu kinaitwa Monstrance, mnakijua?” Cheetah aliwauliza na wote wakatazamana.
“Monstrance!?” Mellina Wanjiku alishtuka na kujishika kifua kwa mshangao.
“Unashtuka nini, unaijua?” Cheetah aliuliza, na yeye alionekana kushtuka kidogo na kuanza kujiuliza kama kapokea mbuzi kwenye gunia safari hii.
“Naijua Monstrance, ni chombo kitakatifu sana, kukishika kwa hila inaweza kuwa matatizo kwetu” Mellina alijibu kwa upole sana, akatulia kidogo kisha akaendelea “Pamoja na ujambazi ninaoufanya sikuwa kufikiri kuligeukia kanisa, kuna nini kwenye Monstrance hiyo?” aliuliza Mellina
“Ah vile vitu vya wakatoliki huwa vinatengenezwa kwa dhahabu tu, itakuwa ndiyo wanayoitaka” alijibu Gichui.
Black Cheetah alijikuta kwenye mtihani mgumu, kama kuna vitu aliviogopa ni miujiza ya Kimungu ambayo mara nyingi aliisoma kati vitabu vitakatifu, mtihani mkubwa! Alijiona amefanya ujinga kutokuuliza nini kilichomo katika monstrance hiyo, je kama wakizikuta nyingi ni ipi ya kuichukua, utata!

“Cheetah!” aliita Mellina.
Black Cheetah alishtushwa na wito huo kutoka katika lindi la mawazo, akawatazama wanakikundi wenzake ambao yeye aliona wangefaa kwa kazi hiyo lakini sasa walimfanya hata yeye kushikwa na wasiwasi.
“Ok, tunafanya kazi au hatufanyi tuchague moja” aliwapa mtego. Baada ya kutafakari mara mbili mara tatu wote waliamua kuingia kazini kuisaka hiyo monstrance.

ITAENDELEA...
 
RIWAYA: MAUAJI Y KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE
Simu: +255 766 974865

Black Cheetah alishtushwa na wito huo kutoka katika lindi la mawazo, akawatazama wanakikundi wenzake ambao yeye aliona wangefaa kwa kazi hiyo lakini sasa walimfanya hata yeye kushikwa na wasiwasi.
“Ok, tunafanya kazi au hatufanyi tuchague moja” aliwapa mtego. Baada ya kutafakari mara mbili mara tatu wote waliamua kuingia kazini kuisaka hiyo monstrance.

SEHEMU YA 2

Miaka kumi nyuma… Al-hamis kuu 1996

KANISA la Holy Family lilisheheni watu mpaka nje wakifuatilia misa takatifu ya alhamis kuu ambapo yalifanyika maadhimisho ya karamu ya mwisho. Hakukuwa hata na njia ya kupita kuelekea popote kila mtu alipo basi ni hapohapo.
Katika madhabahu makasisi wapatao sita pamoja na baba Askofu walikuwa wakiendesha misa hiyo kubwa ambayo mwisho wake huwa inakuwa na maandamano ya kuhamisha mwili wa Bwana kuupeleka mahali pengine ili waumini wapate kuabudu. Watu waliketi kimya kumsikiliza baba Askofu Njue mara baada ya misa hiyo kuhitimika
“Tuna furaha kuwatangazia kuwa mwaka huu tumepokea Monstarnce maalum kwa maadhimisho ya misa maalum. Monstrance hii ambayo ina historia kubwa katika kanisa ilitengenezwa miaka ya 1878 huko Tanzania katika abasia kubwa ya Wabenedictin iliyopo Peramiho. Na ilitolewa zawadi kwa Baba Mtakatifu Leo XIII na kuhifadhiwa pale Roma. Leo hii imeletwa hapa kwetu kwa ajili ya maadhimisho ya jubilee ya miaka mia moja ya Ukristu hapa Kenya. Na itahifadhiwa hapa mpaka tukio hilo litakapokwisha ndipo tutairudisha Roma” alimaliza maelezo yake na kujongea madhabahuni, akainyanyua juu ile Monstrance kubwa iliyokuwa iking’aa kwa rangi ya dhahabu hasa ilipomulikwa na taa zilizowekwa kwa umaridadi ndani ya kanisa hilo, kengele zililia na kisha maandamano kutoka nje ya kanisa yalifanyika mpaka kwenye kikanisa kingine kidogo, ikahifadhiwa hapo na kuacha watu wakipeana zamu za kufanya ibada usiku huo.

1878
Mahali Fulani huko Tanzania

VIBARUA wa wakolono walikuwa wakichimba mashimo makubwa kuingia chini ya milima iliyozunguka eneo hilo, huku wakiwa wamesimamiwa na askari hatari wa kijerumani. Kazi ilikuwa ngumu lakini walifanya hivyo hivyo, walitoa mchanga na kuuchekecha kwenye chekeche maalum na wale wazungu waliondoka na udongo walioutaka na kuingia nao katika chumba maalumu na kuuhifadhi.

Katika milima ile baadaye kulijengwa majengo makubwa na yale mashimo yakawa ndani yake, kila kukicha wazungu wengi walikuwa wakiingia hapo, hawa wakisafiri na hawa wakifika ilimradi shughuli zilikuwa nyingi katika eneo hilo.

Peter Schurmann alikuwa busy kugongagonga chuma kimoja kilichokuwa katika mtindo wa samaki, jasho lilimtoka mwili mzima lakini yeye hakujali aliendelea na kazi yake, na aliporidhika na kile alichokitengeneza alichukua kitu kama uji mzito wa moto na kumwagia ndani yake kisha akauacha upoe kwa muda. Alipokuja kutoa baadae alipata kituchenye umbo la samaki, akaketi na kuanza kukifanyia nakshinaksh. Hakika kazi ya mhunzi yule ilikuwa safi sana chombo kile kilikuwa kiking’aa sana hasa wakati ambapo kinapigwa na mwanga, kishapo akatengeneza mkitako safi kikubwa na kukiunganisha kwa chini ya chombo kile ili kiweze kusimama chenyewe na kweli ilikuwa hivyo, kisha wakakihifadhi katika kanati maalumu. Yake mashimo yaliyopo kule ndani yote yakafukiwa lakini kilibakishwa chumba kimoja ambacho hicho haruhusiwi kuingia mtu yeyote mpaka leo hii. Katika milima iliyozunguka walisimika vitu kama misalaba mikubwa na kuijengea kwa sementi kali sana ambayo si rahisi kuivunja kwa zana za kawaida tulizozizoea. Kile chombo baada ya kukamilika kilihamishwa na kupelekwa kwao.

Chombo kile kilipelekwa huko Italia na kuhifadhiwa kati chumba maalum ndani kabisa ya kanisa la Mtakatifu Petro, Vatican. Chombo hicho kilichojulikana kwa jina la Monstrance kilitolewa mara moja tu kwa mwaka na daima kiliwekwa sehemu maalumu ambayo kila mmoja angeweza kwenda kuadudu huko.

Wiki chache nyuma
Jomo Kenyatta International Airport

Rev. Fr Frederick Gichuru aliketi katika viti vya kupumzikia akisubiri muda wake ufike aingie ndegeni kuelekea Roma kwa kazi maalumu. Watu walikuwa ni wengi uwanjani hapo na kila mmoja wao alikuwa na safari yake, hakuna aliyefuatilia mwenzake anafanya nini au anataka nini.
Tangazo lilisikika kwenye chombo cha kupaaza sauti kuwataka abiria wanaosafiri kwa ndege ya shirika la ndege la uswiss kuingia ndegeni tayari kwa safari. Pembeni ya Fr Gichuru alikaa mtu mmoja mnene aliyeshiba vizuri, inaonekana ndege hiyo yeye aliipanda kutokea Dar es salaam au Kilimanjaro, alimsalimia Fr Gichuru kwa kumpa mkono wake wa kuume.

§§§§§

Na baada ya ndege hiyo kuwa angani mazungumzo baina yao yalichukua nafasi. Mtu huyu mnene alikuwa akielekea Ujerumani kwa shughuli za kikazi na Fr Gichuru nae alikuwa akielekea Roma kwa shughuli za kikazi vilevile. Ndege ilipotua katika uwanja wa kimataifa wa Geneva, ndipo Fr Gichuru alipogundua kuwa yule mtu mnene mwenye sauti ya kivivu alikuwa akitembea kwa msaada wa fimbo. Waliagana na kila mmoja kuchukua njia yake.

Akiwa kwenye gari iliyokuja kumchukua Fr Gichuru alididimia kwenye kisima kirefu cha mawazo, alijaribu kuyarudisha maongezi yale aliyokuwa akiongea na yule mtu mnene kwenye ndege, ilionekana alikuwa akifahamu vitu vingi labda katika kuzunguka sna nchi mbalimbali za dunia hii, lakini alishtushwa kwa jinsi alivyoizungumzia kwa tuo monstrance ile ambayo Fr Gichuru alikuwa akienda kuifuata ili kuileta Nairobi, Kenya.

Baada ya itifaki zote za kikanisa kukamilika Fr Gichuru alikabidhiwa ile monstrance, aliitazama kwa udadisi na kuigeuzageuza ‘Kile ni chombo cha thamani sana, hata pale kilipo hakuna aneujua uthamani wake’, maneno ya yule bwana yalimrudiarudia kichwani mwake. Aliiweka juu ya kijimeza kidogo na kufanya ishara ya msalaba kisha akaitumbukiza kwenye kisanduku maalumu kwa kazi hiyo tayari kwa safari. Baada ya chakula cha jioni Fr Gichuru alikuwa katika mazungumzo na makasisi mbalimbali katika ukumbi maalum, wakibadilishana mawazo na pia akiwaalika katika adhimisho la jubilee hiyo.

Fr Gustav Macker, alikuwa akizungukazunguka katika bustani ndogo iliyo karibu na lango kuu akiongea na simu bila kuchoka kwa lugha yao ya kijerumani, alionekana mara kama anatoa melekezo Fulani, wakati mwingine kama anajibishana na mtu kwa ukali. Alipomaliza alimuona Fr Gichuru akiwa tayari ameketi ndani ya gari akimngoja kwa safari ya uwanja wa ndege.
“Oh Father, nilikuwa naongea na nyumbani kidogo, tunaweza kwenda?”
“Ndiyo nipo tayari.”
Fr Gustav aliondoa gari na kuelekea uwanja wa ndege, njia nzima hakuna aliyeongea na mwenzake, mara kwa mara Fr Gichuru alikuwa akistuka kila alipokumbuka mzigo alioubeba aliingiwa na giza la hofu.
“Haya Father , mi nakutakia safari njema na Bwana akutangulie” Fr Gustav alimuaga Fr Gichuru, akamkumbati na kumpa mkono kisha yeye akageuza gari na kurudi alikotoka.
Akiwa ndani ya ndege alikuwa akisoma kitabu chake cha riwaya ya ‘Msitu wa Solondo’ kilitungwa huko Tanzania, kilimvutia sana hasa alipojua kuwa kwa nini wazungu hupenda sana kudadisi mambo, alikuwa mara ancheka mwenyewe, mara anakunja uso, mara anajishika moyoni kuonesha mshtuko basi ilimradi riwaya hiyo ilimkamata vilivyo.

Baada ya takribani masaa nane angani, ndege ya shirika la ndege la Uswiss ilikanyaga ardhi ya Nairobi na kujiegesha vyema katika maegesho yake. Watu walishuka mmoja baada ya mwingine na mwisho kabisa Fr Gichuru alishuka akiwa na kijisanduku kile mkononi mwake. Alilakiwa na paroko wake Fr Joe Smith na kumuongoza kuelekea kwenye gari aina ya Land Rover 110 Defender mali ya jimbo kuu la Nairobi. Wakati wanatoka pale uwanja wa ndege na kushika barabara kubwa ya kurudi mjini waliipita gari aina ya Hammer iliyokuwa imeegeshwa na mara tu ile gari iliingia barabarani. Ikiwa nyuma kama gari ya tatu hivi ilikuwa aikiifuatilia ile Land Rover 110.
“Karibu sana Fr Gichuru, safari yako imekuwaje?”
“Safari imekuwa nzuri sana, lakini kuna kitu Fr kinanitia mashaka sana”
“Ooh kitu gani tena Fr?”
Fr Gichuru alimsimulia mazungumzo yote aliyozungumza na yule mtu mnene kule kwenye ndege, juu anavyoijua ile monstrance na jinsio alivyomueleza mara ngapi amewahi kuiona na ni nchi tofauti tofauti na ameahidi kuja Nairobi katika adhimisho hilo la jubilee.
“Ananitia mashaka sana, kwa nini kila inapokwenda na yeye anaenda, ni kipi kinamvutia?” Fr Gichuru alimuuliza Fr Joe
“Inategemea kabisa, lakini labda anapenda kuiona inavyopendeza au ni Mkristo kwelikweli anayedumu sana katika imani”
Walipokaribia katika geti la kanisa ile Hammer iliwapita kwa kasi na kusimama mbele sana. Fr Joe aliichukua monstrance ile na kuihifadhi katika chumba maalumu kilichopo ndani ya nyumba yao.

2
1961
Munichen – Ujerumani

“ULE NI URITHI wa ukoo wetu, babu wa baba yangu alisema lazima tufanye juu chini tukauchukue popote utakapokuwepo” mzee wa zaidi ya miaka themanini alikuwa akiongea na mjukuu wake wakiwa shambani juu ya trekta aina ya Massey Furgasson.
“Ha, kumbe eee!” Mjukuu wa miaka saba alikuwa akimsikiliza babu yake kwa makini sana.
“Sasa, wewe mjukuu ndiyo unatakiwa ufanye kazi hiyo, wewe unaonekana mjanja sana”
“Mimi, ah! Naogopa.”
“Usiogope, muda ukifika utajua la kufanya. Ila mjukuu wangu wewe unapenda kufanya nini ukiwa mkubwa?”
“Mimi ningependa kuwa mwanajeshi, nipigane vita.”
“Ha ha ha ha Mjukuu wangu Gustav, vita si jambo jema. Unajua ni kitu gani nilikuwa nafikiria juu yako?”
“Hapana niambie babu”
“Wewe uwe Padre, uongoze kanisa, uchunge kondoo wa Bwana”
“Ha! Nitakuwa nakunywa divai yote” mjukuu alimjibu babu yake na babu mtu alitungua kicheko kadiri ya mawazo ya mjukuu wake.

Miaka michache baadae
Munichen – Ujerumani

GUSTAV Macker alimaliza masomo yake na kujiunga na seminari kuu ya Mt Augustino iliyopo kati jimbo la Munichen, alikuwa mtii kwa viongozi wake na hata kupendwa na waalimu na walezi wake katika seminari yao. Alimaliza miaka mitano ya falsafa na baada ya kupata stashahada yake alichaguliwa kwenda mji wa Achen hukohuko Ujerumani kuendelea kusoma teolojia kwa miaka mingine mitano, alikuwa ni kijana mpole, mnyenyekevu na mtii kwa kila jambo, daima kila alipoonekana al;ikuwa katika hali ya unyenyekevu wa hali ya juu.
Siku moja alitembelewa na mtu asiyemjua, baada ya mazungumzo marefu sana walifahamiana kuwa kumbe wao ni ndugu, na sasa huyu ambaye angetakiwa kumwita kaka alikuwa ni mtu mkubwa kwatika mji huo wa Achen.
“Ndiyo, mimi ni Andreas Schurmman, baba yangu mimi mzee Ernst Schurmman alizaliwa tumbo moja na mama yako Angela Schurmman, wakati wa vita ya pili ya dunia ndipo walipopoteza maisha katika mazingira tofauti na wewe ulichukuliwa ukiwa mdogo na babu yako aliyemzaa mama yako, mimi nililelewa na msamalia mwema tu mpaka nimekuwa hivi nilivo.”
Gustav alitikisa kichwa juu chini kuonesha kuwa aliielewa hiyo safari ya maisha jinsi ilivyokuwa.
“Umejuaje kama nipo hapa?”
“Nina rafiki yangu ambaye ni mfanya kazi hapa ndiye aliyeniambia lakini hata yeye hajui kuwa mimi na wewe tuna undugu, ila mimi nilijua kwa kuwa ninalikumbuka jina hili Gustav Macker, karibu sana nyumbani uje unitembelee”.
Baada ya mazungumzo yao waliagana na kila mtu kubaki na na hamsini zake, ‘Sasa ishu yangu itakamilika’, Don Andreas Schurmann alijiwazia wakati akiingia kwenye gari yake aina ya Mercedes Benz na kuuacha uwanja wa seminari hiyo.

§§§§§

“Hutakiwi kushangaa wala kushtuka” Don Andreas alimweleza Gustav Macker.
“Sishangai kwa unachoniambia, bali nashangaa kwa nini babu aliweka utajiri huo huko?! Inatia uchungu”
“Hapana babu yangu alikuwa na akili sana, alikuwa anatafuta mahali salama pa kuihifadhi siri ile ya utajiri kwa kizazi chake cha sasa” Don Andreas akajimiminia glass yake ya pombe kali na kusafisha koo kwa kujikohoza kidogo, kisha akaendelea, “Vatican, ni sehemu yenye usalama sana duniani, na si uongo. Mzee Peter Schurmann aliiweka pale siri ile ya utajiri mkubwa kwa ukoo wake. Sikia Gustav, utakapokuwa Padre nitafanya kila njia uhamishiwe Vatican ili ufanye uchunguzi ujue jinsi gani tunaweza kuipata Monstance ile irudi mikononi mwetu.”
Gustav aliinama kwa sekunde chache akiangalia sakafu ile ya marumaru safi ambayo ilimruhusu kuiona taswira yake mwenyewe kwa jinsi ilivyokuwa safi.
“Gustav!” Don aliita, “Usihofu, haya ni mambo madogo sana, na nina hakika tutafanikiwa na kuishi kifalme”. Maneno matamu ya Don Andreas yalianzisha mapigano ya nafsi na roho ndani ya kijana huyu ambaye kanisa liliridhia kumpa ukasisi miezi michache ijayo, ama kweli kwenye mkono wa Mungu hapakosi mguu wa shetani. Mazungumzo ya wawili hao yalikuwa marefu sana na mwishowe makubaliano yalifanyika na mpango mahsusi ukapangwa na tajiri huyo, Don Andreas, kama alivyojulikana.

Baada ya miezi sita Gustav Macker alipewa daraja la upadre na kuwa kasisi rasmi katika kanisa Katoliki, hakuamini masikio yake alipopata taarifa kuwa kituo chake cha utume kitakuwa Vatican, katika makao makuu ya kanisa hilo.

Dagoreti Corner Super Pub

BLACK Cheetah alinyanyuka na kusimama wima na wengine wakafanya hivyo hivyo.
“Vijana tuingie kazini, tutengeneze pesa” Cheetah aliwaeleza wenzake na wote wakahafiki.

Walipomaliza vinywaji hivyo waliliendea gari ya Black Cheetah aina ya Subaru na kupotelea mjini. Ilikuwa tayari majira ya saa nne usiku Subaru ile ilipoegeshwa katika maegesho ya viwanja vya Uhuru, wote wakateremka na kupotelea katika club kubwa inayojulikana kama Nairobi by night, humo starehe za aina zote zilikuwa zikipatikana, walijichanganya na wadau wengine wakisubiri mida yao ya kazi ifike ili wafanye wanalolihitaji.

* * *
Ilitimu saa sita ya usiku, Cheetah na wenzake walipoegesha gari yao karibu kabisa na jingo la kanisa hilo na kushuka.
“Hivi nyie mnaosali, hiyo monstrance sijui nini huwa inahifadhiwa wapi?” Cheetah aliwauliza wenzake
“Kawaida kwenye chumba cha kuvalia makasisi, ambacho huwa ni kanisani” alijibu Mellina wakati Gicui akiliangalia jingo lile kubwa lililojengwa kwa kuta nene ajabu likiwa katikati ya mji wa Nairobi.
“Ok, nafikiri mmoja wetu aingie huko kwenye hicho chumba halafu wengine waangali usalama wa ndani na nje” Cheetah alitoa oda.
“Sawa Cheetah!” Gichui aliitikia kama aliyekurupushwa usingizini.

Dakika chache baadae Gichui alikuwa ndani ya wigo wa kanisa hilo akitalii hapa na pale, akiangalia hiki na kile, usiku mnene usio na mbala mwezi, aliifanya kazi hiyo kwa ustadi hata walinzi hawakugundua chochote, Mellina na Cheetah walibaki nje lakini kila mmoja upande wake, Mellina katika ulinzi wa nje na Cheetah akiwa makini na tayari kumuokoa Gichui kama itatokea la kutokea. Akiwa ndani ya wigo ule Gichui alitembea kwa uangalifu sana akichungulia kwenye vitundu vidogo vilivyojengewa kwenye ukuta huo wa kanisa, ndani aliona tu kataa kekundu kakiwakawaka mithili ya mshumaa, alikaangalia na kukumbuka kuwa pale huwa makasisi wanawekaweka vikombe Fulani, labda ni penyewe. Aliendelea na kutokea upande wa nyuma wa kanisa hilo, milango kadhaa ilikuwako hapo na yote imefungwa imara kabisa kwa vitasa vya kiitaliano, kila aliyoutikisa ulikuwa imara kabisa, akatoa funguo zake zinazofungua kotekote akatumbukiza moja na kujaribu ikagoma, akachukua nyingine akatumbukiza mlango ukakutii amri na kufunguka, akiwa na sox yake kichwani akaingia ndani ya chumba hicho ambako alikutana na makabati mengi ambayo yalimchanganya, kabati kubwa la mbele liliunganishwa na meza kubwa sana iliyofunikwa kwa Formica safi, akatulia na kuatafakari, kabati lipi hasa analolihitaji, kwake aliiona kazi hiyo ikiwa rahisi kabisa ni kiasi cha kufungua makabati tu na kubeba anachotaka kisha kuondoka. Alilijongea kabati hilo kubwa na kujaribu milango yake, ilikuwa wazi, ndani kulikuwa na nguo tu za ibada zinazotumiwa na makasisi.

§§§§§

Fr Frederick Gichuru, alishtuka usingizini, ndoto mbaya ilimsongasonga hata kuufanya moyo wake kwenda mbio, alikaa kitandani na kuitafakari ndoto hiyo hakupata maana, machozi yalimtoka, alipiga magoti mbele ya msalaba na kutulia kimya, baada ya dakika kadhaa alishtuka na kusikia kelele za mlango kama mtu anaufungua kwa kutumia nguvu, alisikiliza kwa makini na kukuguundua kuwa ulikuwa mlango wa Sakristia (sakristia ni chumba kinachojengwa pamoja na kanisa ambacho uhifadhiwa mavazi na vitu mbalimbali vya ibada), mlango ambao Gichui alikuwa akiufungua taratibu sana lakini Fr Gichuru aliusikia kwa kelele. Aliinuka na kuchuku kanzu lake zito jeusi ili kujistiri na baridi kali ya Nairobi, alienda mpaka chumba cha Fr Joe, akamkua mzee huyo anakoroma kwa usingizi mzito akaamua kumuacha, akatoka nje kuelekea kanisani kushuhudia nini kinafanyika, alishtuka na kusimama ghafla alipoona mlango wa sakristia uko wazi, alikibanza kwenye ua kubwa la yugiyugi lililomficha vizuri, ‘wanataka nini?’ alijiuliza asipate jibu, aliangalia lakini hakuona mtu kutoka, alivuta hatua ndogindogo na kuufikia mlango huo, akazipanda ngazi na kuingia ndani, aligeuka huku na huku hakuona mtu isipokuwa milango wazi ya makabati.
“Tulia apo hapo, usijitikise” sauti ilitoka upande wa makabati ya nyuma.
Fr Frederick alitulia na kunyoosha mikono yake juu kujisalimisha.
“Wanaume wanapokuwa kazini wewe hutakiwi kuamka amka” Gichui alimwambia Fr Gichuru, Fr Gichuru aling’ata meno kwa hasira, hakujali kama mtu huyo ana silaha gain alishusha mikono na kugeuka na kutazamana na domo la bastola aina ya Smith and Wesson.
“Wewe ni nani?” Fr Gichuru aliuliza
“Usitake kujua” alijibiwa
Fr Gichuru alimkazia macho Gichui, Gichui alijikuta akiishiwa nguvu na kushusha bastola yake.
“Kwa nini mnataka kulidhulumu kanisa?” akauliza Fr Gichuru, “Nani aliyekutuma? Na mnataka nini?” kimya kilitawala kati yao, “Sema nitakusaidia, kazi ya kanisa ni kusaidia wahitaji na wenye shida, sema.” Gichui aliinua bastola yake tena na kuondoa kiguu cha usalama kuruhusu risasi ipande juu tayari kabisa kufyatuliwa.
“Siogopi risasi, maana risasi itaua mwili lakini kamwe haiwezi kuuwa roho” Fr Gichuru alimueleza jambazi yule. Gichui alishusha pumzi bado akimnyoshea bastola kasisi huyo.
“Sikiliza kijana, weak bastola yako mahali pake uende kwa amani, maadam sijakuona sura yako na hii itabaki kuwa siri yetu mimi na wewe tu,” Fr Gichuru alimaliza na kuanza kufunga makabati yake. Alipogeuka baadae hakumuona yule jambazi mahali pale, akafanya ishara ya msalaba na kurudi nyumbani kwake. Usingizi haukuwako tena mpaka kulipokucha.

ITAENDELEA....
 
Kwa mahitaji ya Riwaya nyingine kali kutoka kwa Richard Mwambe kama vile
TUFAA JEKUNDU
CRONOC 7
KITISHO
HARUFU YA KIFO
MPATANISHI n.k
Walisiana nae kwa namba
+255 766 974 86
 
MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE
WHATSAPP: 0766 974865
“Sikiliza kijana, weak bastola yako mahali pake uende kwa amani, maadam sijakuona sura yako na hii itabaki kuwa siri yetu mimi na wewe tu,” Fr Gichuru alimaliza na kuanza kufunga makabati yake. Alipogeuka baadae hakumuona yule jambazi mahali pale, akafanya ishara ya msalaba na kurudi nyumbani kwake. Usingizi haukuwako tena mpaka kulipokucha.
SEHEMU YA 3
§§§§§
“Uuuuh!” Gichui alipumua kwa nguvu baada ya kuingia kwenye gari yao akiwa na wenzake tayari kuondoka.
“Tupe ripoti” Cheetah alitoa ombi kwa Gichui
“Haaaa, siamini”
“Huamini nini, umeona nini huko?” Cheetah alidadisi
“Makabati makubwa na nguo za kasisi, sijaona monstrance”
“Lakini Gichui unaonekana kuna kitu hutaki kusema” mellina alidakia kutokapale nyuma ya usukani alikpokaa.
“Kanisani, si pa kuiba” alijibu, “Nimekutana na Kasisi Gichuru ana kwa ana pale kanisani” akaweka tuo kidogo na kuendelea “Nilijikuta naishiwa nguvu, sikuweza kufanya lolote, akaniruhusu kuondoka”.
“We bwege kweli, ungembana huyohuyo akueleze” Meliina aling’aka.
“Mellina mi nashindwa kukueleza, wale jamaa sijui wana dawa!” aliongea kwa mshangao Gichui.
“Basi, tutarudi kwa nguvu mpya” Cheetah aliwapoza wenzake na kuondoka zao.
“Una uhakika kuwa hiyo monstrance ipo huku?” Cheetah alimuuliza mtu mnene kwa njia ya simu.
“Mi siyo mtoto Cheetah, najua na nina uhakika na hilo, hakikisha tunaipata” alijibiwa.
“Maana jana tumefanya upekuzi mle kanisani hatukuiona” aliendelea kuongea Cheetah
“hata kama haipo kanisani, lakini ipo maeneo hayo, fanya kila unaloweza uipate” alimaliza mtu mnene na kukata simu.
“Sasa wajukuu, hapa kilichobaki ni kufanya mbinu zote kumteka Fr Gichuru tumbane mpaka atueleze maana yeye ndiye aliyeuleta ule mzigo” Cheetah aliwaelezawenzake na wote wakaafikiana na kupanga mikakati.
§§§§§
“Baba Joe, leo usiku nimeota ndoto mbaya sana hata nikaamka usiku kusali” Fr Frederick alimueleza Fr Joe walipokuwa mezani wakipata chai.
“Ni nini tena umeota Fr?” Joe aliuliza
“Ah, ndoto mbaya sana” alisema huku akitua slesi za mkate katika sahani na kuiinamia meza akitegemeshwa na mikono yake miwili. Fr Joe aliona matone kama matone ya maji yakidondoka juu ya meza hiyo.
“Fr, ni nini, nieleze nikusaidie” Fr Joe aliinuka kitini na kulmuendea Fr Gichuru huku akimueleza maneno hayo, alitoa kitambaa chake na kumfuta machozi. Fr Gichuru aliinuka kitini pamoja na Fr Joe wakatoka nje kwenye kabustani kadogo na kutembeatembea wakiwa na rozali zao mikononi.
“Fr Joe! Nililala kama kawaida mara baada ya masifu ya jioni, katikati ya usiku huo niliota nipo Roma makao makuu ya kanisa, nipo juu kabisa ya mnara wa jengo hilo, niliangalia chini palikuwa parefu sana, isingekuwa rahisi hata kuruka, sikuwa na msaada, nililia na machozi yangu yalikuwa ni machozi ya damu, yalitirirka na kulowesha kanzu yangu nyeupe lakini hayakufika chini bali yote yalituama kifuani upande wa moyo wangu. Nilimuona Malaika kasimama mbele yangu mkononi kashika kikombe, akanisogelea akanipa kikombe hicho ambacho ndani yake kulikuwa na divai nyekundu lakini cha kushangaza mlikuwa na risasi ndani yake, akanambia
‘Kunywa’, nikasita akanambia kuwa ‘yakupasa unywe’, nilikiangalia kikombe kile, mwsho nilikitwaa na kunywa, nilipomaliza tu nilihisi kizunguzungu na kuanguka kutoka juu ya mnara ule kuelekea chini, lakini kabla sijafika chini nilishtuka kutoka usingizini.
Mara moja niliitafakari ile ndoto lakini sikupata maana yake, nikapiga magoti kusali, wakati nasali niakaanza kusikia kelele za mlango wa Sakristia ukifunguliwa, kelele zile zilikuwa kubwa mno hata kuyasumbua masikio yangu, nilinyanyuka na kuitwaa kanzu yangu kisha nikaja chumbani kwako nikakukuta umelala, nikakuacha na kwenda kungalia nini kinachotukia huko, lo! Fr Frederick alijishika kifuani na kukumbuka ahadi yake na yule jambazi ‘ibaki kuwa siri yetu’…”
“Oh Bill, aaaah, uuuuh” sauti ya kimahaba iliyoashiria kuwa viumbe hao wapo kwenye ulimwengu mwingine zilitawala chumba kimojawapo katika hotel kubwa inayojulikana kama Plazza Hotel iliyopo katikati ya jiji la Nairobi.
Bill, mtu mnene alikuwa kitandani akipewa raha na msichana wa Kikikuyu kutoka North Kinangop, binti huyo alihakikisha anampagawisha mzee huyo mpaka ammalize kabisa, na hivyo ndivyo ilivyokuwa, Bill alikuwa nyang’anyang’a kwa penzi alilopewa na msichana huyo aliyembeba usiku uliopita katika mtaa wa Koinange hapo hapo Nairobi kwa dau la kulipana dola za kimarekani, alimfurahia jinsi alivyomkatia kiuno kwa mitindo ya ajabu hata akafanywa kusahau adhma ya kumtaka msichana huyo kimapenzi.
Rosemary Wangui alihakikisha anamkamua Bill mtu mnene mpaka tone la mwisho akiwa na lengo moja tu la kuchota madola yake yaliyojaa katika mkoba maalumu wa ngozi.
Penzi la uongo na muda mfupi liliendelea katika kitanda cha hotel hiyo, hakuna aliyekiogopa kifo, baada ya kuona hawafaidi utamu wa maumbile yao ndipo walipokubaliana kutokutumia kinga ili kutiana hasara roho, hapo sasa ndipo mtu mnene alipoahidi donge nono kwa shughuli aliyopewa na msichana huyo aliahidi kufanya lolote kwa jinsi alivyopagawisha na mtu mnene, Bill.
“Rose, you are so sweet baby!” Bill alitamka maneno hayo huku akijifunga taulo kuelekea maliwato.
“Same to you my cock” Rose alimsindikiza Bill kwa macho wakati akielekea maliwatoni huku moyo wake ukimuenda mbio kwa kuuona ule mkoba wa Bill ulioshiba manoti. Dakika chache baadae Bill alitoka maliwato na kuketi juu ya kitanda na kuruhusu minyama ya mwili wake kutikisika kwa jinsi alivyojitupa hapo.
“Rose!” Bill aliita
“Yes, Sir!” Rose aliitika kwa adabu ya uongo.
“Unauona ule mkoba wenye pesa?” Bill alimtupia swali Rose
“Yeah nauona, vipi?”
“Nitakupa ule mkoba kama ulivyo, na pesa yake ndani” Bill alizungumza hayo na kumwangalia Rose usoni, Rose hakuamini anayoyasikia kutoka mtu mnene, tabasamu pana lilichanua usoni mwa mrembo huyu, tabasamu la kuuaga umasikini, tabasamu la utajiri wa dharula.
“Sijaelewa darling” Rose alisema kuonesha kuwa hajaelewa aliloambiwa.
“Nini hujaelewa? Kwenye ule mkoba kuna dola za kimarekani nyingi tu, nahitaji kukupa wewe pamoja na mkoba wake kama ulivyo”. Rose alibaki kimya, kisha akafungua kinywa chake na kumwambia mtu mnene “Asante,” akamkumbatia na kukutanisha ndimi zao ambazo zilichukua muda kidogo kila moja kuonja ladha ya nyingine. Kisha Bill akamtoa Rose kinywani mwake.
“Sikia, hakuna ujira usiyo na kazi kwanza” Bill aliongea, akainua glass yake ya pombe ya kirusia ‘Pushkin’ akapiga funda moja na kumtupia jicho Rose aliyejilaza kitandani na kuegamia upande wa mbele wa kitanda hicho kwa kutumia mto wa kulalia.
“Nakusikiliza” Rose alimwambia Bill mtu mnene.
“Unamjua huyu?” Bill alimuuliza Rose na kumpa picha ndogo iliyoonekana kwenye kioo cha simu yake kubwa, Rose aliipokea na kuiangalia kwa makini sana kisha akatikisa kichwa kuashiria ameifahamu.
“Mmh! Namfahamu, kafanyaje?”
“Namtaka huyu mtu nizungumze nae kirefu, na wewe nataka unifanikishie hilo”
Rose alibaki midomo wazi, alimwangalia Bill mtu mnene hakummaliza
“Kivipi?” akauliza
“Nataka ufanye kila hila ya kike, umlete mahali halafu vijana wangu watawateka wote wawili ila wewe watakuacha nay eye tutamchukua kwa kuwa tuna shida naye” Bill alimueleza kinagaubaga, Rose alionesha woga sana katika hilo, alijifikiria kwa kina, pesa anazitamani, kulitekeleza hilo ni vigumu, ugomvi mkubwa kati ya nafsi yeke ulizuka haikuwa rahisi kwake kuuamua, alinyanyuaka kutoka pale kitandani alipokaa na kuvuta hatua chache kuelekea maliwato alipita mbele ya Bill akiwa mtupu kama alivyozaliwa, Bill alibaki hoi na kushuhudia jogoo lake likiinua taulo kuashiria network imerudi.
3
SAJENT Maria na koplo Othorong’ong’o walibaki kutazamana hawakuwa na jibu sahihi juu ya mauaji yale, waliperuzi kwa pamoja faili lile walilokabidhiwa na Inspekta Simon Saitoti
“Kwa maelezo ya Fr Joe, yule paroko, nafikiri tuifanyie kazi hiyo taarifa tuliyopewa” koplo Othorong’ong’o alimueleza sajent Maria aliyekuwa ameketi kwenye benchi huku akiwa na redio call yake mkononi.
“Uko sahihi, lakini haya maelezo yangekuwa timilifu sana kama tungeonana na marehemu lakini haikuwa hivyo” sajenti Maria alionesha ugumu wa kazi ulipo.
“Sajenti, hivi tukifanya uchunguzi kwenye mitaa ya vibaka kama Kawangware kule hatuwezi kupata habari yoyote ya huyu Cheetah, ili tupate kwa kuanzia?” koplo Othorong’ong’o aliuliza.
“Unafikiri Cheetah kwa hadhi yake atakuwa anjificha kule ambako kila mara tunaenda kwa msako, kule wamejaa wahamiaji haramu koplo” sajenti Maria alimjibu koplo Othorong’ong’o, kisha kimya kifupi kikatawala.
“Nafikiri litakuwa jambo la busara sana tukijaribu njia hiyo, ila twende kiraia zaidi ili tuchangamane nao kisha tuweze kupata habari yoyote inayoweza kutuanzishia game hii.” Walikubaliana kuingia mtaa huo jioni ya siku hiyo kujichanganya ili kupata lolote la kuanzia katika kesi hiyo iliyoonekana kuwatoa kijasho kidogo.’
Walikubaliana kukutana baada ya muda kidogo wa mapumziko ambapo kila mmoja wao aliutumia kwa jinsi anavyojua yeye.
‘A Catholic priest murdered after returning from Rome’. Kilikuwa ni kichwa cha habari kilichosomeka juu kabisa katika ukurasa wa mbele wa gazeti la Daily Nation la siku hiyo, mwandishi wa gazeti hilo alieleza kwa kina habari hiyo aliyoifanyia uchunguzi wa kutosha na wa kuridhisha. Sajenti Maria alilishusha gazeti lile lililokuwa limeuficha uso wake na kulitua magotini pake na kuruhusu wazo moja lipite kidogo kisha akaendelea tena kuisoma habari ile iliyomsisimua sana kama riwaya tamu za Richard Mwambe, alipojiridhisha na habari hiyo aliandika vitu fulani katika kijitabu chake cha kumbukumbu kisha akalifunga na kuingia ofisini kwake ambako alimkuta koplo Otho’ amesinzia kitini, akamshtua na kumueleza juu ya gazeti lile kwa jinsi lilivyoandika kwa kina juu ya habari.
“Sajenti, turudi kwa Fr Joe kwa mahojiano kidogo ili tujue kwa undani juu ya safari yake ya Roma na kama kulikuwa na uadui wowote na mtu,”
“Positive, koplo” Maria alijibu na mara moja wakaelekea katika kanisa kuu la Familia takatifu kwa kazi hiyo.
ITAENDELEA.
 
MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: Richard MWAMBE.
SEHUMU YA 4
ILIPOISHIA…Akalifunga na kuingia ofisini kwake ambako alimkuta koplo Otho’ amesinzia kitini, akamshtua na kumueleza juu ya gazeti lile kwa jinsi lilivyoandika kwa kina juu ya habari.
“Sajenti, turudi kwa Fr Joe kwa mahojiano kidogo ili tujue kwa undani juu ya safari yake ya Roma na kama kulikuwa na uadui wowote na mtu,”
“Positive, koplo” Maria alijibu na mara moja wakaelekea katika kanisa kuu la Familia takatifu kwa kazi hiyo.
Songa nayo….

“Marehemu Fr Gichuru hakuwa na mazoea ya kuhifadhi kumbukumbu sehemu? Ama kwa maandishi au njia yoyote ile?” lilikuwa ni swali kutoka kwa koplo Otho’
“Yeah, alikuwa anaandika sana, daima alikuwa na diary yake” Fr Joe alijibu hukua akinyanyuka na kuingia kwenye chumba cha marehemu Fr Gichuru, kisha akarudi na diary ndogo mkononi mwake na kuiweka mezani, sajenti Maria aliichukua mikononi mwake
“Fr, samahani kwa kukusumbua mara kwa mara lakini nafikiri ndani ya diary hii tunaweza kupata chochote kitakachotusaidia, kama unaturuhusu tuondoke nayo ili kuendelea na upelelezi”
“Oh ninyi mpo kazini, usijali mama, nenda nayo ukimaliza kazi nayo uirejeshe kwa kumbukumbu hapa” Fr Joe aliwakabidhi ile diary na kuagana nao, akawasindikiza mpaka getini, walipokuwa wanaagana pale getini, mwanamke mmoja mnene lakini aliyeonekana ana mwili wa mazoezi akiwa kavalia sketi nyeusi, iliyobeba blauzi nyeupe na juu yake ikafunikwa na kijikoti cheusi, aliingia getini na kuwapita sajenti Maria na koplo Otho’ wakati wakiagana na Fr Joe. Jicho la sajenti Maria halikuondoka kwa yule dada aliyekuwa akitembea kwa mwendo wa wastani akielekea kanisani kulikokuwa kukiendelea na maombolezo. Baada ya maagano yale, sajenti Maria alirudi garini pamoja na koplo Otho’
“Koplo, umemuona yule dada aliyetupita pale?” Maria aliuliza
“Nimemuona, halafu sura yake si ngeni kichwani mwangu” koplo Otho’ alijibu na kuongezea. Sajenti Maria alitulia kwa nukta kadhaa, akavuta kijidroo cha dashboard ya gari na kutoa kamera ndogo ambayo unaivaa kama saa mkononi, akateremka garini.
“Nakuja koplo, Linda mkia wangu tafadhali” Maria alitamka hayo huku akiurudishia mlango wa gari ile na kurudi kule kanisani kwa kutumia njia ile aliyopita yule dada wakati huo akiivaa ile camera mkononi mwake. Ilikuwa ni hatua chache tu alimuona yule dada akiwa katikati ya watu akijipenyeza ili kupata eneo zuri la kumuezesha kujua kinachojir katika kanisa hilo ambalo lilijawa na waumini waliokuwa wakiomboleza kwa nyimbo na zaburi. Sajent Maria aliendelea kumuangalia kwa makini, alimuona akitoa simu yake na kuandika kitu kama ujumbe mfupi kisha kuirudisha kotini, na muda huohuo alijipenyeza tena kuelekea upande mwingine ndipo alipogongana kikumbo na sajenti Maria ambaye kwa uzoefu wake wa kazi ya kipolisi alikuwa tayari amekwisha mpekua kwa kumgusagusa.
“Dada, we vipi? Mbona unagonga watu ovyo, huoni njia?” yule dada aliuliza
“Samahani nilikuwa nasoma saa hata sikukuona, samahani sana” sajenti Maria aliomba radhi, kila mtu aliyekuwa pale aliawaangalia wanawake hawa. Sajenti Maria alikua amehisi kitu kigumu katika ubavu wa kushoto wa mwanadada yule na kwa uzoefu wake aligundua kuwa yule dada amehifadhi bastola katika ubavu wake, aliishusha saa yake machoni na kutazama kama picha aliyoipiga imetoka vizuri, akaridhika nayo kisha akajiondoa na kurudi garini.
“Vipi?” koplo Otho’ aliuliza
“Ah, clear, nina wasiwasi na yule dada, kwanza inaonekana ana bastola kiunoni mwake” Maria alijibu
“Tumsubiri?”
“Haina haja lumsubiri, huyo hapo anakuja, hakikisha hatumpotezi kwenye sight yetu.”
Yule mwanadada alitoka getini na kupinda kushoto kwenye maegesho ya magari na kuingia kwenye moja ya magari yaliyopo hapo, na gari ile taratibu iliyaacha maegesho yale kuingia barabarani kuelekea upande wa Westland. Koplo Otho’ naye aliiondosha gari yao aina ya Peugeot 308, gari ya kisasa kutoka Uingereza, baada ya dakika kadhaa waikuwa kwenye foleni kubwa za Nairobi lakini macho yao yalikuwa makini kuitazama gari aliyopanda mwanadada yule isipotee. Kwa mwendo wa taratibu walikuwa katika barabara ya Mombasa kisha wakaiacha ile iendayo Nairobi central na wao kuifuata ile gari aliyokuwa sasa imekamata barabara ya Waiyaki kuelekea Westland, baada ya mwendo kidogo ile gari ilikunja kulia na kufuata barabara ya vumbi iliyoingia katikati ya nyumba zilizojengwa kwa mpangilio mahsusi kama quarter za shirika Fulani, Otho’ nae aliingia na gari yake kuifuata, sasa ailibaki gari mbili tu mbele aliyopanda yule dada na nyuma ya kina koplo Otho’ na sajenti Maria…
Otho’ aliegesha gari yake mbele kidogo karibu na duka kubwa lililokuwa likiuza bidhaa muhimu kwa binadamu. Sajenti Maria alishuka kutoka katika gari na kutembea taratibu kuelekea kule aliko yule mwanadada, Otho’ alibaki kwenye gari akiangalia kwa mbali tukio hilo. Yule mwanadada aliongeza mwendo kidogo alipogundua kuwa anafuatwa, alitembea huku akitoa simu yake ya mkononi na kuongea na mtu Fulani, sajenti Maria aliona tayari kagundulika kama anamfuata huyo mwanadada, na yeye alitoa simu yake na kwasiliana na Otho’ ili amlinde katika hilo. Otho’ aliiacha gari pale dukani na kufuata ule mtaa kama mtu aliye na shughuli nyingine kabisa, kwa mbali alimuona sajenti Maria kasimama akitazamana na yule mwanadada, kati yao kulikuwa na nafasi kama ya mita mia moja hivi, Otho’ alimpita sajent Maria na kumsalimu kama hamjui huku akiendelea upande ule aliko yule mwanadada na alipomfikia alimsalimu vilevile na kuendelea na safari yake na kumpita yule mwanadada, baada ya mwendo kama wa mita hamsini alikunja kona na kusimama kuona nini kinaendelea.
Sajenti Maria alibaki akitazamana na yule mwanadada kila mmoja akiwa na simu mkononi, mara nyuma ya Sajenti Maria ulisikika mlio wa pikipiki, Sajenti Maria alipogeuka nyuma kuipisha pikipiki ile alichelewa, dereva wa ile pikipiki alimgonga Maria na kumuangusha chini, sajenti Maria alijaribu kujiinua lakini kabla hajakamilisha zoezi hilo aligongwa tena eneo la mbavu na kuanguka chini, kisha yule muendesha pikipiki aliteremka na kuiegesha ile pikipiki huku ikiwa inanguruma na taratibu alimfuata sajenti Maria pale chini, alimtazama kwa dharau na kupandisha juu kile kioo cha kofia ngumu aliyoivaa.
“Wewe ndiyo unajua kufatilia nyendo za watu siyo?” alimuuliza huku akimsogele karibu zaidi. Sajenti Maria alimwangalia kwa hasira mpaka uso wake ulipoteza kabisa ile haiba ya uanamke, yule jamaa alipomkaribia alichuchumaa ili kumsaili vizuri sajenti Maria, kwa kushtukiza sajenti Maria alirusha teke la nguvu lililotua katikati ya mapaja ya yule jamaa na kupiga sawasawa sehemu zake za siri, yule jamaa kabla hajajielewa teke lingine lilitua upande wa kulia wa shingo yake na kumpeleka chini, sajenti Maria alijiinua kwa haraka na kusimama kidete na kumuacha yule jamaa akiwa chini. Yule mwanadada alipoona mchezo ule wa kiufundi kutoka kwa sajenti Maria aligeuka ili apotee eneo lile, lakini hamad alijikuta akitazamana uso kwa uso na bastola ya Othorong’ong’o, alisimama ghafla na kujikuta hana la kufanya, Otho’ akatoa pingu zilizokuwa mifukoni mwake ili kumfunga yule mwanadada.
“Weka mikono yako nyuma!” alimuamuru ili amfunge pingu hizo, yule mwanadada akaishikanisha mikono yake nyuma ya mgongo akiwa anatazamana na Otho.
“Geuka” Otho alimuamuru, na yule mwanadada aligeuka na mkononi mwake tayari alikuwa na bastola amabayo aliificha upande wa nyuma kwenye sketi yake, aligeuka na kufyatua risasi iliyoenda na kupiga mguu wa Otho, yowe la maumivu lilimtoka Otho huku akiiachia bastola yake ikidondoka chini, sajenti Maria alichanganyikiwa afanye nini akiwa bado katika kuhamaki pikipiki nyingine ilitokea nyuma ya Otho na yule mwanadada akaidandia katika kiti cha nyuma, sajenti Maria alirusha risasi kwa bastola yake lakini hakuweza kupata shabaha nzuri kwani ile pikipiki ilikuwa imekwishakunja kona na kumuacha Otho akiwa chini mguu ukivuja damu, aligeuka kumwangalia yule mwenye pikipiki ya kwanza lakini hakumuona pale badala yake watu walianza kujaa eneo lile, sajenti Maria akavua shati lake alilovaa juu na kumfunga koplo Otho jeraha lake ili kuzifanya damu zisiendelee kumwagika kisha akajitahidi kumyanyua kutoka pale chini akisaidiwa na watu wachache walifanikiwa kumfikisha kwenye gari, sajenti Maria aliwasha gari na kuondoka eneo lile.
Siku mbili
Kabla ya mauaji ya Fr Gichuru
MTAWA wa kike alikuwa amesimama katika kituo cha matatu akisubiri usafiri kuelekea mjini, kila mara alionekana akiiangalia simu yake, huku akiwa na kikapu mkononi alionekana kama anayekwenda sokoni. Mara gari moja Land Rover Defender ilikuwa ikitoka katika geti la kanisa hilo na kukunja kulia kuelekea mjini, ikasimama jirani kabisa na mtawa yule.
“Sista, twende nikusaidie” ilikuwa ni sauti ya Fr Gichuru akimpa lifti yule mtawa, alipokwishakuketi sawia kitini waliondoka kuelekea upande wa mjini na Fr gichuru alianzisha maongezi.
“Sista safari ya wapi saa hii?”
“Nakwenda Kileleshwa estate, kusalimia jamaa kwani leo nina ruhusa kutoka kwa mama mkuu” yule mtawa alijibu.
“Ooh, vizuri kuwatembelea ndugu siku mojamoja” Fr Gichuru alimueleza huku akiwa anakaribia katikati ya jiji la Nairobi
“Ila kwanza nataka kwenda pale shule ya msingi Nairobi, ningeshukuru kama unganisaidia kufika pale maana usafiri wa kwenda kule ni mgumu” yule mtawa aliomba huku akimlegezea macho Fr Gichuru. Siku zote kumnyima mwanamke ombi lake siyo rahisi sana, Fr Gichuru aliiacha barabara kubwa na kuufuata barabara ndogo inayopita katika majumba ya watu kuelekea huko shule ya msingi, alipoyamaliza majumba na kuteremka kibonde kidogo kuliendea daraja ili kuvuka na kutokea upande wa pili, alikuta mtu aliyeanguka na pikipiki.
“Oh God!” yule sista alihamaki, Fr Gichuru akasimamisha gari akataka kushuka kwenda kumsaidia yule jamaa aliyeanguka.
“No usiende Fr ni hatari, huwezi jua nini kilichopo huko chini” Sista alimbembeleza Fr Gichuru, lakini haikuwa rahisi kwani moyo wa huruma wa kikasisi ulimsukuma kushuka.
“Hapo hapo ulipo tulia” sauti ilitoka nyuma ya gari yake, alipogeuka alikutana na mtu aliyeshika bastola akimnyooshea yeye.
“Nini tena jamani? Mbona sielewi kinachoendelea?” Fr Gichuru alilalamika
“Tulikuwa tunakusubiri wewe na tunashukuru huyo sista wako amekuleta mahali pema peponi” yule jambazi alizungumza, “Haya haraka ingia katika gari iyohiyo siti ya nyuma” aliamuriwa, na bila kubisha alijipakia ndani yake na nyuma ya usukani yule mtawa aliyepewa lifti alikuwa tayari nyuma ya usukani kwa kuondoka.
“Ha! Sista!” Fr Gichuru alipigwa na mshangao alipomkuta yule sista tayari ameketi kwenye usukani.
“Aliyekwambia mi sista ni nani!?” alijibu yule mtawa huku akitoa kilemba chake kichwani na kuruhusu rasta zake ndefu kumwagika mabegani “Mimi nilikuwa nakutafuta wewe, naitwa kahaba Rose” alijitambulisha. Fr Gichuru alivalishwa soksi usoni ili asione anapopelekwa na safari ilianza. Mwendo wa muda kadhaa waliisimamisha ile gari na kumshusha Fr Gichuru kisha wakachukua gari nyingine na kuitelekeza ile ya mission palepale eneo la Madaraka estate pembeni mwa barabara ya Mbagathy, kisha wao wakaendelea na safari yao kuelekea barabara ya Mombasa na mpaka karibu na kiwanda cha saruji cha Bamburi na kupinda kushoto kuelekea kwenye eneo la viwanda, moja kwa moja waliingia kwenye godown kubwa na kumteremsha Fr Gichuru. Ndani ya chumba kidogo chenye vikorokoro vingi walimuhifadhi akiwa amefungwa kamba kwa nyuma.
Yule mwanamke aliyejifanya mtawa alimvua ile soksi usoni na kumuacha huru akiweza kuona kwa mbali kutokana na giza lililotanda ndani humo
ITAENDELEA….
 
MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE
WHATSAPP: 0766974865
Ndani ya chumba kidogo chenye vikorokoro vingi walimuhifadhi akiwa amefungwa kamba kwa nyuma.
Yule mwanamke aliyejifanya mtawa alimvua ile soksi usoni na kumuacha huru akiweza kuona kwa mbali kutokana na giza lililotanda ndani humo
SEHEMU YA 5
.
§§§§§
“Kazi uliyonituma nimeimaliza, nipe changu” Rose alimwambia mtu mnene walipokutana tena katika chumba chao kilekile katika Plazza Hotel.
“Usijali, mzigo wako upon a asante kwa kazi nzuri, lakini ole wako uitoe siri hii, nakuua” Bill mtu mnene alimpatia pesa nyingi kahaba Rose na kuagana nae.
“Asante Bill” alishukuru huku akitoa machozi, machozi yenye pande mbili, furaha ya kukamata pesa nyingi ambazo hajawahi kuzishika maishani, na uchungu wa kumsaliti kasisi asiye na hatia. Alitoka na kubamiza mlango nyuma yake, moja kwa moja akaiendea lifti na kuteremka chini kabla ya kupotelea mitaani.
Bill akiwa na swahiba zake waliingia katika gari aina ya hammer na kuelekea kumuona mateka wao mioyoni mwao wakijua kazi imekwisha.
Ukimya ulitawala katika lile godown isipokuwa kweny kijichumba kimoja kimoja tu ambako Fr Gichuru alikuwa akisali kwa kilatini kwa sauti tulivu ambayo kama ungekuwa karibu na dirisha lake ungeisikia vizuri tu.
Mara mlango ulifunguliwa kwa ghafla na watu sita waliingia ndani ya kijichumba kile. Fr Gichuru aliendelea na sala yake kana kwamba hakuna mtu aliyeingia humo ndani.
“Mmmh Sali sana tu mpaka milango ifunguke!” sauti hiyo ilimshtua Fr Gichuru na kuinua macho yake juu na kugongana na yale ya ya Bill mtu mnene
“Bill!” aliita kwa mshangao
“Unashangaa nini? Habari za Roma?” Bill alimuuliza Fr Gichuru
“Nzuri tu, habari za ulikokwenda”
“Salama tu Fr, leo tumeonana tena, sina mazungumzo mengi na wewe leo ila ninachohitaji ni ile Monstrance, tuambie ilipo tukaichukue usiku huu kisha tutakuachia huru, mimi sipendi kumwaga damu isiyo na hatia kama yako Reverent Father Frederick Gichuru” Bill aliongea kwa pozi huku akiruhusu pumzi zake kumtoka kwa shida. Fr Gichuru alimtazama mtu huyu mnene na kisha kuwatazama wale wengine watano, mara moja akamtambua Gichui, yule jambazi waliyekutana naye kanisani akipekuwa makabati.
“Muulizeni huyu kama ameiona” alimueleza Bill huku akimtazama Gichui, “Ile ni mali ya kanisa ninyi mnaitakia nini?” akawauliza. Wote wakatazamana.
“Gichuru, kama hutaki kutueleza utataulazimisha kufanya kitu tusichokitaka, haya mi natoka nawaacha vijana wangu utawaelekeza” Bill mtu mnene alizungumza na kutoka katika kile chumba akifuatiwa na wengine wawili, pale ndani wakabaki watatu. Cheetah na wenzake walimuadhibu vikali Fr Gichuru kwa mapigo makali sana kumlazimisha aseme, lakini Fr Gichuru hakufungua mdomo wake badala yake alikuwa akisali kwa kilatini ambacho wale jamaa hawakuelewa kitu. Mateke ya tumboni, mbavuni, mikanda ya kijeshi vyote vilikuwa ni masluub kwa Fr Gichuru.
Lakini baada ya kumtesa kwa zaidi ya lisaa limoja Fr Gichuru alipoteza fahamu kabisa na kulala kama mfu.
“Amekufa?” Mellina aliuliza
“Hajafa huyu kazirai tu, lete maji baridi” Wambugu alimueleza Mellina, ndoo ya maji ikafika na kummwagia mwilini Fr Gichuru, akashtuka na kuhema kwa nguvu, akawatazama wale watesi wake mmoja baada ya mwingine.
“Baba uwasamehe maana hawajui watendalo” baada ya kusema maneno hayo alianguka na kupoteza fahamu kwa mara nyingine…
Kwa mbali alisikia mlango ukifunguliwa, ilikuwa ni ndoto tamu iliyomfariji moyo, alimuona Malaika akija pale alipolala na kumfungua zile kamba. Haikuwa ndoto kiuhalisia, mlinzi wa godown lile aliingia kwa kunyata ndani ya kile chumba kidogo alimfungua kamba na kumbeba mabegani mwake Fr Gichuru aliyekuwa hana fahamu na kujaribu kutoroka nae, alipita kandokando ya magari mabovu ili walinzi wenzake wasimuone kasha kwa kutumia kijimlango kidogo cha nyuma alitoka nje huku akiwa kambeba fr Gichuru kwa mtindo ule ule, baada ya mwendo mfupi alimuhifadhi katika nyumba ndogo jirani tu na eneo hilo, kasha yeye akaenda zake tena lindoni kwake, hakuna mtu aliyemgundu kwa hicho alichokifanya aliingia tena kimyakimya na kuendelea na majukumu yake kama kawaida.
Baada ya masaa machache Fr Gichuru alirudiwa na fahamu zake na kujikuta mahali tofauti na mwanzo, alijitazama na kujikuta hana zile kamba mikononi, yuko huru isipokuwa maumivu makali katika maeneo ya tumbo na mbavu yalikuwa yakimsumbua, hakujua ni jinsi gani amefika eneo lile, alijaribu kuinuka kutoka pale alipokuwa amelala, akaketi na kuegemea kabati kuukuu lililokuwa ndani ya kijichumba hicho na kushusha pumzi ndefu alipogundua kuwa hapo kwa vyovyote ni mahali salama. Akiwa katika tafakari hiyo alisikia nyayo za mtu zilizokuwa zikipitapita huku na huko upande wa nje, akajituliza kimya na kubaki kusubiri kuona ni nani huyo; mara kelele za mlango ambao bawaba zake zimekosa mafuta zilisikika na mlango ule uliacha kijinafasi cha kupenya mtu mwembamba, na punde tu mtu mmoja alijipenyeza na kuurudishia huo mlango nyuma yake.
Kutoka ndani ya koti lake alitoa mfuko wa plastiki uliondikwa UCHUMI na kuuvirigua kisha akatoa kachombo ka plastiki na kufungua mfuniko wake.
“Father, kula chakula, najua una njaa sana” yule mtu alimwambia Fr Gichuru. Ndani ya kichombo kile kulikuwa na chakula aina ya mokimo (mchanganyiko wa maharage, mahindi na viazi kisha husongwa kama ugali), Fr Gichuru alikula na kunywa maji yaliyokuwa jirani hapo bila kuangalia yana hali gani.
Baada ya kumaliza kile chakula, akajiweka vizuri na kumtazama yule mtu, sasa akagundua kuwa alikuwa ni mzee sana lakini bado likuwa na nguvu zake.
“Wewe ni nani?” Fr Gichuru alimuuliza
“Mimi ni bwana Melchior Ndege, mtu wa huko Iriyamurahi”
“Hapa nimefikaje na ni wapi?”
“Tangu unafikishwa pale godown mimi nilikuona na sura yako si ngeni kwangu, nakufahamu sana, wewe ni Fr Gichuru wa kanisa kuu siyo?”
“Sawa kabisa! Zaidi ya hapo wewe ni Malaika kwangu, hakika Mungu amekutuma”
“Napenda tuzungumze kidogo” yule mzee alimwambia Fr Gichuru. Fr Gichuru alimwangalia kwa makini yule mzee aliyekaa mbele yake juu ya kiti kidogo cha miguu mitatu.
“Father, kwa nini hawa jamaa wamekuteka wewe? Maana kama hela huna!”
“Bwana Ndege, hii ni hadithi ndefu sana” Fr Gichuru akatulia kidogo kisha akaanza kumueleza kila kitu mzee yule, hakumficha hata jambo moja, kuanzia safari yake ya Roma mpaka aliporudi, mpaka alivyotekwa na jinsi ilivyokuwa. Mzee Melchior Ndege alitulia tuli kama maji ya mtungini, alimwangalia yule kasisi asiye na kosa kisha akakohoa kidogo.
“Father, mimi ndiyo niliyekuleta humu ndani, ndiye niliyekutoa kule, wala si mbali ni mtaa wa tatu tu hapo, nimekufuatilia kwa muda mrefu sana na hata mpango wa wewe kutekwa mi niliujua mapema.” Maelezo yale yalimshtua sana Fr Gichuru, alishindwa kuelewa inakuwaje mzee huyo kumfuatilia na kujua hata kutekwa kwake.
“Sijakuelewa bado bwana Melchior!” Fr Gichuru aliuliza kwa mshangao
“Na hiyo nayo ni hadithi ndefu father Gichuru, nitakwambia jiweke tayari” akachukua chupa yake ya maji na kupiga mafunda kadhaa kisha akaiweka chini na kuendelea, “Bill, ni mtu anayetafutwa sana kila kona ya dunia hii, ni jasusi la kutisha la kimataifa linalotumiwa na makundi mengi kuekeleza mauaji au wizi wa kimataifa, hapa ninavyokwambia tayari FBI wameshafika Kenya kwa ajili ya kumnasa mtu huyu, Bill hawezi kuja hapa kwa kuitaka hiyo monstrance tu kama alivyosema, ama kuna kitu kingine nyuma yake au hiyo monstrance ina jambo lingine ambalo ninyi hamlijui, mimi hapa usinione mzee, mi siyo mzee” yule mzee aliposema hayo aliingiza mkono wake ndani ya kofia aliyojifunika ambayo ilikuwa imeunganishwa na jacket lake na kwa kutumia nguvu alivua kitu kama gozi nene usoni mwake na kulitupa chini kisha akajifuta vizuri na kumtazama Fr Gichuru ambaye alikuwa amepigwa na butwaa akmtazama kijana huyo mtanashati kwa sura, kumbe alivaa sura bandia.
Siku chache zilizopita
SIMU ya mezani kwa Melchior Ndege iliita, mara moja aliacha kazi aliyokuwa akiifanya na kuitazama simu hiyo alisita kidogo kuipokea, lakini kelele za simu ile zilimfanya aipokee
“Hello!” aliita
“…aa! Ok, sawa (…) sasa hivi nashughulikia”
Melchior aliinuka kwenye kiti chake na kuingia kwenye lift iliyompeleka juu kama ghorofa tano hivi katika jengo la KICC, aliuendea mlango Fulani na kuufungua kisha kuingia ndani
“Karibu sana Ndege, keti, maana kwa jinsi unavyohema itakuwa unahabari nzito” Gallus Shikuku alimkaribisha Ndege ofisini kwake.
“Nimepata simu kutoka ofisi ndogo ya uwanja wa ndege” Melchior alianza kuzungumza
“Mh niambie kijana!” alijiweka vizuri kitini na kuiegemea meza yake kubwa akimtazama Melchior Ndege.
“Mtu tunayentafuta kwa udi na uvumba ameingia nchini, Bill”
Gallus Shikuku hakuamini anachokisikia kwa kijana huyo alimkazia macho na kumuuliza tena swali lilelile, naye akapata jibu lilelile.
“Bill…” Gallus Shikuku alilirudia jina hilo, “Kaja kufanya nini tena? Kajileta mwenyewe” aliongea peke yake.
“Ok! Ndege nimeisikia hiyo habari, sasa vijana kazini, naomba umchunguze Bill anavyoketi na anvyosimama na wakati huo mimi nawasiliana na vyombo vyote vinavyomsaka ili tupate usaidizi maana huyu mtu ni wa hatari sana na tukienda vibaya anatumaliza.”
Melchior alitoka ofisini kwa boss wake bwana Gallus Shikuku na kurudi ofisini kwake kujipanga kwa kazi aliyopewa. Bwana Gallus Shikuku alijishika kichwa na kuzunguka kutoka huku na huku, aliiona sasa bahati imekuja kwao ya kumtia mkononi mkorofi huyu, Bill, aliyeshindikana, FBI wanamtafuta, Interpool wanamsaka kila kona ya dunia, lakini jinsi anavyowatoroka ni utata mtupu, wengine wakadiriki kusema ni mchawi lakini haikuwa hivyo.
Gallus Shikuku aliketi kitini na kuvuta laptop yake na kufungua sehemu ya kuandika ujumbe, baada ya kuhakikishiwa kuwa aliyeonekana ni Bill na watu wake walio uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta kumtumia picha za haraka na yeye kuzifikisha katika kitengo maalumu cha utambuzi, picha hizo zilitoa jibu lilelile, Bill Van Getgand. Shikuku alitoa taarifa kwa vyombo husika vya usalama ambavyo tayari vilisambaza habari na picha ya jasusi huyo popote duniani atakapoonekana basi mara moja wataarifiwe ili atiwe nguvuni.
Melchior Ndege aliondoka na kuliacha jengo la KICC na kujichanganya mjini kadiri ya maelekezo aliyopewa na watu wanaomfuatilia Bill, ili kujua ni wapi amefikia. Haikuwa kazi kwani alimuaona mtu huyu mnene akiwa na ile fimbo yake ya kutembelea, mara hii Ndege alishtuka kidogo, hakuambiwa kuwa huyu jamaa anatembea kwa msaada wa fimbo, alichukua kamera yake kubwa aina ya Cannon Cibershot na kumpiga picha kadhaa akiwa pale nje ya Plazza Hotel akilipana na muendesha tax, mara moja zile picha aliziingiza katika computer yake ndogo na kuzituma kwa bosi wake na maelezo machache.
Bill Van Getgand alipanga chumba namba 207 katika hotel hiyo, akiwa kaja Nairobi kwa kazi moja tu ndogo ya kuhakikisha anaipata monstrance aliyotumwa na tajiri wake kutoka Ujerumani, Don Andreas, kwa pesa nyingi sana.
Melchior Ndege, aliweka vijana eneo lile kuhakikisha wanapata nyendo zote za Bill mchana huo ili wajue jinsi ya kumtega.
§§§§§
Melchior Ndege aliendelea kubaki pale nje ya hotel hiyo akifuatilia kujua ni wakati gani bwana Bill atatoka ili na yeye afanye kazi yake, alilolisubiri likatimia, muda kama wa saa nne usiku hivi Bill alitoka na kwenda kusikojulikana, alipopotelea na gari hilo alilolikodi, Melchior alitoka katika gari yake na kuchukua vifaa vyake vichache na kuelekea katika hoteli ile, moja kwa moja hakupitia katika ofisi ya mapokezi, aliingia katika lifti na kupanda mpaka ghorofa ya pili, alikitafuta chumba namba 7, haikuchukua muda alikipata, kwa kutumia funguo zake maalum alicheza na kitasa kile na mlango ule ukafunguka, akaingia na kuurudisha nyuma yake. Akatazama kile chumba kwa macho ya kiintelijensia kisha akakiendea kile kitanda kikubwa na kuivuta droo ya kitanda hicho kisha kwa upande wa chini akabandika kidubwasha maalum kisha akafanya hima kutoka katika chumba hicho.
Alipofika chini, pale alipoegesha gari lake aliingia na kuketi ndani, kisha akawasha chombo Fulani kama simu na kuweka vidubwasha Fulani masikioni mwake alibonyabonya vitu Fulani na kutulia, haikuchukua muda Bill alirudi na mwanamke fulani wakikokotana na kuingia ndani ya hotel hiyo. Melchior aliwasha kile kidude chake na kujiwek tayari kisha akalaza kiti cha gari yake na kusubiri, mara baada ya sekunde kadhaa akaanza kusikia mazungumzo ya mahaba yaliyokuwa yakitoka katika chumba hicho, mara alisikia mikoromo ya raha za dunia, akabonyeza kitufe cha kurekodi kila kinachozungumzwa kisha yeye akajitupa katika usingizi akiwa ndani ya gari hiyo.
Katikati ya usiku melchior ndege alishtuka kwa simu iliyomuita ndani ya gari, aliitazama saa yake ilikuwa tayari imetimu saa tisa kasoro robo usiku, aliwasha mashine yake na kusikiliza machache yaliyoongelewa chumbani humo, Melchior alipata habari nyingi ambazo Bill alimshirikisha yule kahaba Rose na kumshawishi aweze kumfanyia kwa malipo ya pesa nyingi za kigeni. Mazungumzo yote melchior alikuwa ameyapata katika chombo chake kile. Alipogundua kuwa tayari ulikuwa ni usiku sana aliamua kuondoka eneo lile.
Asubuhi siku iliyofuata aliwasilisha ripoti kwa boss wake Bw Shikuku na kwa pamoja waliisikiliza kwa makini na kupanga mikakati ya kazi ikiwamo Melchior kusafiri katika ndege ambayo Fr Gichuru angeitumia kwenda Roma kwani huyo bwana Bill naye alipanga kusafiri kwa ndege hiyo ikiwa ni moja ya njama zake za kujiweka karibu na kasisi huyo.
Mpango ukasukwa na kila kitu kikawa sawa kabisa, Melchior Ndege akawa tayari kwa safari hiyo.
Akiwa ujerumani aliweza kumfuatilia vizuri sana mtu mnene Bill nyendo zake zote na kujua ni nini na ni nani aliyekuwa akionana nae mara kwa mara na kwa nia gani, alipolijua na kuhakikisha kuwa hapo cha kuhitaji, Melchior Ndege alichukua ndege na kuelekea Roma Italy ambako alijichanganya na watalii mbalimbali katika viwanja vya Vatican lakini yeye akiwa na lengo tofauti kabisa, alipopata nafasi ya kuingia ndani ya jengo hilo la kihistoria alijariu kutafuta kama anaweza kuona muhusika yoyote labda angemuuliza habari fulani fulani juu ya hiyo Monstrance ambapo sasa ndicho alichogundua kuwa Bill, mtu mnene ndicho hasa kilichomleta.
§§§§§
Yule mzee aliyekuwa sasa kijana alimtazama Fr Gichuru aliyekuwa amepigwa na butwaa kwa habari hiyo ambayo kwake ilikuwa kama riwaya nzuri masikioni mwake, alimtazama kijana huyu na kumuona hakika ni Malaika kwake.
“Na kuhusu kutekwa kwangu we ulijuaje?” Fr Gichuru alimtupia swali yule kijana.
“Ndiyo maana nakwambia ni stori ndefu sana, mimi nilijua kila kitu mpaka mpango wa wewe kuletwa hapa, anyway, hatuwezi kumaliza yote hapa maana muda nao unatuacha, mpango uliopo sasa kwanza, tunataka tumnase huyu mtu mnene kwani yeye ni jasusi linalotafutwa kila kona ya ulimwengu, kisha wewe tukuweke kwenye usalama, hivyo basi mimi na wewe tutatoka hapa na nitakupeleka sehemu ambayo utakaa huko mpaka amri nyingine itakapotolewa” Melchior Ndege alimaliza kuzungumza na kuinuka pale alipoketi kisha kujikung’uta vumbi katika zile nguo kuukuu.
“Sasa, unajua mimi ni Kasisi, hata kama nakwenda huko lazima viongozi wangu wajue na kuna zana ambazo ni muhimu kuondoka nazo kutokana na mfumo wa maisha yangu” Fr Gichuru alitoa ombi.
“Yeah, najua sana juu ya hilo, lakini kwa sasa kama wameshakuteka ujue hawatashindwa kukuua, kwa hiyo wewe twende na taarifa kwa viongozi wako sisi tutazipeleka kwa njia tunayoijua, maana kwa sasa hatuamini mtu” Melchior aliendelea. Japokuwa alijaribu kumbembeleza fr Gichuru lakini alikataa katakata, alipendekeza arudi kwanza parokiani kwake ndipo afanye taratibu kama hizo. Melchior Ndege hakuona haja ya kupoteza muda, alimchukua fr Gichuru na kupita nae katika vichocjoro kadhaa kisha wakafika nyuma ya jingo moja kubwa, kulikuwako hapo kituka kibanda lakini kilichofunikwa na manyasi marefu yaliyorundikwa baada ya kukatwa.
Ndege akapekua pekua na ndani yake kulikuwa na pikipiki kubwa iliyofichwa hapo, akaitoa na kuwasha, muungurumo wake ulieleweka kabisa kuwa pikipiki hilo ni bidhaa ya Mjerumani BMW. Wote wawili wakakaa juu yake na Melchior Ndege akaliongoza kuelekea mjini. Moja kwa moja walifika mbele ya kanisa kuu la familia takatifu, Nirobi mjini na kumuacha hapo,
“Sasa, ukiwa tayari unifahamishe maana tunataka usalama wako fr,” Melchior Ndege alimuasa.
“Sawa Melchior, na Mungu akubariki sana katika hili,” alimalizia fr Gichuru na kuingia ndani ya wigo wa kanisa hilo, wakati Melchior Ndege akiondoka eneo lile na kurudi katika majukumu yake.
ITAENDELEA
 
MAUAJI YA KASISI
MTUNZI; Richard MWAMBE
SEHEMU YA 6

ILIPOISHIA…. Sasa, ukiwa tayari unifahamishe maana tunataka usalama wako fr,” Melchior Ndege alimuasa.

SONGA NAYO.....

“Sawa Melchior, na Mungu akubariki sana katika hili,” alimalizia fr Gichuru na kuingia ndani ya wigo wa kanisa hilo, wakati Melchior Ndege akiondoka eneo lile na kurudi katika majukumu yake.
Kijua cha asubuhi kilianza kuchomoka katika maeneo ya viwanda ya Nairobi kandokando ya barabara ya Mombasa, walinzi waliopewa kazi ya kumchunga Fr Gichuru walikwenda kumtazama ili kuhakikisha kuwa yupo salama, walipofika hawakuamini wanachokiona, mlango ulikuwa wazi katika mtindo uleule kama Maria Magdalena alipofika katika kaburi la Yesu alfajiri. Wakatazamana, hawakuwa na lakufanya, wakatoa taarifa haraka kwa wakubwa waliomleta mateka huyo.
“Yaani aisee msilete ujinga, tunakuja sasa hivi” ilikuwa ni sauti ya Blach Cheetah kwenye simu hiyo, na mara simu ile ikakatwa.
Dakika kumi na tano, Black Cheetah, Mellina Wanjiku na Bwana Gichui walifika pale godown na kushuhudia hali hiyo, waliwaita walinzi wote pale laikini mmoja hakuonekana,
“Mwenzenu yuko wapi?” lilikuwa swali kutoka kwa Gichui kwenda kwa wale walinzi, hawakuwa na jibu, walibaki kutazamana tu, “Nawauliza ninyi, walinzi gain mpo hapa na mtu anatoroka? Ninyi mmekula njama,” aliongeza kisha akawasukumia wote kwenye kile kichumba na kuufunga mlango kwa nje.
Taarifa za kutoweka kwa fr Gichuru hazikumfurahisha Bill mtu mnene hata kidogo, alihisi kuwa hiyo ni njama na hasa kwa kuwa mlinzi mmoja hakuonekana kati ya hao.
Pamoja na adhabu walizowapa walinzi wale lakini hakuna kilichozaa matunda.
Bill aliwaita vijana wa kazi katika kivhumba kidogo ndani ya godown hilo na kuwapa kazi ya kumsaka popote alipo Fr Gichuru na atakapoonekana hakuna cha kusubiri ni kumuondoa uhai tu na mambo mengine yatafuatia.
“Sasa tukimuua ndiyo tutapata hiyo monstrance?” Mellina aliuliza.
Bill alibaki kimya kwa swali hilo kisha akamtazama Cheetah na Gichui, akimaanisha watoe wazo hapo cha kufanya.
“Sikia, yule Gichuru ameshajua mengi juu yetu, sasa tukimuacha atatoa siri polisi, halafu mission itashindikana. Hivyo tunamuua kisha tunavamia kanisa ki-ambush na kuchukua tunachokitaka” Black Cheetah aliwaeleza wanzake.
“Safi!” Bill mtu mnene alimpongeza.
Baada ya kikao hicho kifupi, walitawanyika na kuanza kazi ya kumsaka kasisi huyo.
Alfajiri ya siku iliyofuata…
“Baba, mimi leo sijisikii vizuri, mwili wote unaniuma sana, naomba unisaidie kigangoni kwa misa mimi nitabaki hapa” fr Gichuru alimuomba paroko wake fr Joe Simith
“Kwa kweli fr inabidi ubaki, kwani hawa maharamia wanaweza kukukamata njiani, ubaki hapa mimi nitakwenda kigangoni”. Baada ya makubaliano hayo fr Joe alichukua gari ya mission na kuondoka zake na kumuacha Fr Gichuru akisubiri muda wa ibada saa kumi na mbili kamili asubuhi.
Fr Gichuru alivalia kanzu yake nyeusi na kofia ya kikasisi nyeusi yenye nyoya jeusi katikati, mkononi akiwa na rozali yake aliterenka ngazi taratibu ili apate muda wa kusali alfajiri hiyo kabla hajaingi katika misa. ‘Moyo wangu una huzuni kiasi cha kufa’ alijiwazia wakati amesimama kwenye ngazi za nyumba yao, kisha kwa hatua za taratibu aliteremka na kukanyaga uwanja wa kanisa hilo kongwe, ‘Baba ikiwezekana kikombe hiki kinipitie mbali,’ aliendelea kupata tafakari hii ya uchungu, hatua chache alisimama, ‘ Lakini si kwa mapenzi yangu bali yako yatimizwe.’
Subaru ya kijivu ilikuwa imesimama karibu kabisa na barabara ipitayo mbele ya kanisa hilo kubwa, hata fr Joe alipopita hapo aliiona lakini hakuitilia maanani. Nadni ya gari hiyo kulikuwa na watu watatu, awili wanaume na mmoja mwanamke.
Black Cheetah aliitazama saa katika dashboard ya gari hiyo, ilikuwa tayari ni saa kumi na moja alfajiri akamwambia Gicui aliyekuwa nyuma ya usukani huo, “Twende sasa, mlinzi atafungua tu huu muda ni sawa,” kwa mwendo wa taratibu Gichui aliielekea geti kuu na alipofika getini kwa mbali aliona vivuli kama vya watu, akawasha taa katika mtindo wa full na kuwamulika, alikuwa ni sista na fr, akawasha tena taa mara kadhaa katika mtindo huo. Yule kasisi akalisogelea geti kutazama kulikoni, alifika getini na kusimama akilitazama gari hilo. Milango ikafunguliwa, Black Cheetah akatoka akiwa ndani ya koti lake jeusi na kulielekea geti, sasa uso kwa uso na fr Gichuru.
“Kwa kosa ulilolifanya la kututoroka, jua la leo si halali wewe kuliona” Black cheetah, alimueleza fr Gichuru huku akiondoa usalama wa bastola yake na kuruhusu risasi niingie katika chemba, fr Gichuru aliutazama mdomo wa bastola ile,
“Si kwa mapenzi yangu, bali yako yatimizwe” Fr Gichuru alisema mara hii kwa sauti iliyoweza kusikiwa na Black Cheetah pekee, mkono wa jambazi huyo ulikuwa ukitetemeka hata kutaka kupoteza nguvu.
“Black Cheetah, unachelewaaa!” ilikuwa sauti ya Mellina ikimstua Black Cheetah na bila ajizi vidole vyake vikapata nguvu na kufyatua trigger ya ile bastola, risasi mbili zilipenye katika kifua cha kasisi huyo na kumnyayua kabla ya kumbwaga chini chali na mifereji ya damu kuanza kuchuruzika kutoka mgongoni alaikolalia.
Kwa mwendo wa kasi ile Subaru iliondolewa mahali pale na kusababisha kelele za tairi pindi ilipoingia barabarani.
Fr Gichuru hakuwa na nafasi hata ya kuomba maji, “Yametimia, Baba mikononi mwako naiweka roho yangu” alitamka maneno hayo kwa shida huku damu nyingine zikitoka kinywani na kisha kichwa chake kikaelemea uapnde wa kushoto na kukata roho.
4
INSPEKTA Saitoti alikuwa akigongagonga kalamu yake mezani kwake huku akionekana wazi kuwa kichwa chake kilikuwa na mambo mengi sana ambayo kwa namna moja au nyingine yalimchanganya kichwa., mara alivuta kabrasha hili mara lile lakini hakujua anachotaka kufanya kwa muda huo, akiwa katika hali hiyo aligutushwa na hodi iliyogongwa mlangoni mwake kisha mwanamama mmoja aliyevalia kiraia aliingia kwa ukakamavu na kubana miguu yote miwili kuonesha nidhamu ya kijeshi.
“Jambo afande?” Inspekta asitoti alisabahi
“Jambo!” alijibu yule mwanamke au kana anavyojullkana Sargeant Maria, “Afande natoa taarifa ya kuumia afande Otho’ katika mapano na moja kati ya majambazi tunayoyatafuta”
“Oh! Pole sana afande, nieleze kwa kina,” Inspekta Saitoti aliomba aelezwe huku akimpa ishara ya kuketi kitini sergeant Maria.
Alipokwishakueleza kinagaubaga kila kilichojiri, alitulia kitini kimya akisubiri amri ya boss wake itasema nini, mara Inspekta Saitoti alikohoa kuashiria kuuvunja ukimya ule.
“Ok! Sasa kutokana na hilo, naomba afande Otho nimuondoe kwenye operesheni hii na nikupe kijana mwingine machachri wa kukusaidia, koplo Kariithi, au we unasemaje?” alimuuliza huku akimkazia macho,
“Sina neno afande, kijana yupo kamili na anaweza kazi,” Maria alijibu kwa sauti ya ukakamavu hasa.
“Ok basi nitampa taarifa na mara moja ataungana na wewe katika hili, hakikisheni tunawatia mbaroni wauaji ili sheria ichukue mkondo wake,” sergeant Maria alisimama na kubana miguu yake sawia, “Sawa afande!” alijibu, akageuka na kutoka nje.
Inspekta Saitoti alibaki tena peke yake mle ofisini, sasa hakuwa anagongagonga ile peni tena pale mezani bali alikuwa akibofya namba za simu yake ya mezani na kuweka kile kisikilizio sikioni mwake kusubiri sauti ya upande wa pili iongee lolote.
Alipokwisha kuongea na mtu wa upande wa pili alitulia tena kitini na kufungua runinga yake ndogo iliyowekwa ofisini humo na kufuatilia habari za kimataifa. Mara mlango uligongwa na alipomkaribisha mgongaji, aliingia kijana wa makamo, mwenye kadiri ya miaka kama ishirini na minane hivi, mwenye siha nzuri ya kuvutia, aliyejengeka kimazoezi, alisimama mbele ya Inspekta kikakamavu, Inspekta Saitoti alimtazama kijana huyu, kisha akavuta motto wa meza na kutoa bahasha ya khaki akamkabidhi, na maneno machache yakafuatia ya kumpa majukumu ya afande Otho ambaye kwa kipindi hicho alikuwa hospitalini akiuguza jeraha lake. Kariithi alirudi nyuma hatua mbili na kupiga mguu chini kisha akageuka kikakamavu na kutoka nje ya ofisi ile.
§§§§§
Sergeant Maria alikuwa akimuelekeza mambo Fulani Fulani koplo Kariithi juu ya wapi wameishia na nini cha kufanya juu ya sakata hilo la mauaji ya Kasisi.
“Ok, mi nafikiri sasa cha kufanya ni kufuatilia nyendo za hawa jamaa ili tuweze kuwatia mkononi” Kariithi alitoa ushauri.
“Ni sawa, lakini bado hatujajua adui yetu anapenda kuonekana wapi,” Maria alieleza dukuduku lake katika hilo.
“Nimekuelewa afande, hapa kuna sehemu kubwa nne za kufanya doria, Dagoreti Corner, Kawangware, Korogocho na Uthiru Kenoo, nafikiri tukifanya doria kali pande hizo tunaweza kama si kuwatia mkononi basi kupata japo harufu yao” koplo Kariithi alieleza kwa kujiamini na mkakati ukapangwa wa kufanya doria ya kimyakimya maeneo hayo yote.
Ulikuwa ni usiku wa balaa katika mitaa hiyo, hakuna aliyekamatwa kwa maana polisi hao waliwajua wanaowatafuta, hawakufanya kamatakamata kama za huku kwetu Bongo.
Uthiru Kenoo…
“Leo hii lazima tumalize kazi!” Cheetah aliwaambia wenzake huku aking’ata pande kubwa la mutura na kulishushia na tusker, akabeua na kuwatazama wenzake kwa zamu, “Maisha hayana guarantee, hasa haya yetu, Bill atatulipa pesa nyingi sana ukizingatia pesa tu aliyomlipa yule kahaba Rose ni ndefu itakuwaje kwetu sisi?”
Mellina alionekana kuwa mbali kabisa kimawazo, walipomgutusha wenzake alionekana kama mtu aliyetoka katika usingizi,
“We vipi? Mbona hauko nasi kabisa?” Wambugu alimuuliza
“Ah! Nafsi yangu inanisuta sana, hivi kwa nini tunafanya unyama huu kwa sababu ya pesa? Tumemuua kasisi wa watu bila kosa,” Mellina alionekana kusikitika sana.
“Aaa ha ha ha ha Mellina, wewe ni jambazi wa kike, muuaji ambaye hata Mungu hana muda wa kukusamehe, leo hii ujutie kifo cha mtu mmoja, mtu asiye na faida, hana watu wanaomtegemea wala nini, pesa pesa Mellina, hata Yuda Iskariote alimtoa Yesu auawe kwa vipande thelathini vya fedha, nini wewe!!!” Cheetah aliongea huku akiwa amesimama akigonga meza yake kwa ngumi, tayari pombe ilikuwa imekwishafanya kazi yake kichwani, alihema kwa nguvu na kuwatazama tena kwa zamu, “Ninawaamini sana vijana wangu, kwa kuwa Mellina ameonesha mashaka sasa nabadili program, leo hii tunaenda kuibeba hiyo Mostrance, lazima ipatikane, kwa udi na uvumba, kama jina la riwaya ya Innocent Ndayanse, leo hii ili kesho Bill atupe dolari zetu na kila mtu atawanyike kivyake, kama kukamatwa na akamatwe kivyake,” amakweli pombe mwana haramu, Cheetah alitoa bastola yake na kuifutafuta vumbi hakujali kama watu walikuwa wakimwangalia, Wambugu akainuka na kumnyang’anya ile bastola kisha kumvutia nje na kumuingiza kwenye gari, alishaona kuwa sasa Cheetah hakuwa yeye.
Mellina alikaa nyuma ya usukani na kutaka kuiondoa gari ile lakini alikuta mbele yake kuna watu wawili wamesimama wakimtazama, ‘Polisi’ alijiwazia huku akikanyaga clutch na kutumbukiza gia ya kwanza, alipoanza kukanyaga accelerator wale polisi wakatoa bastola zao tayri kwa mashambulizi,
“Shiiittt!” Mellina alikanyaga mafuta kwa nguvu na huku bado mguu haujatoka sawasawa katika clutch na kuuzungusha usukani, norinda iliyotokea hapo haikuwa ya kawaida, vumbi lilitimka usiku huo na watu walio jirani walisikika wakipiga mayoe ya woga, Cheetah na Wambugu tayri bastola mikononi wakishambulia upande ule walipo wale askari, lakini umahiri wa Mellina katika usukani uliwafanya wakose shabaha, ile Subaru iliizunguka na kuingia barabarni kisha Mellina akatumbukiza gia ya pili mara ya tatu na kuwaacha watu midomo wazi. Mwendo haukuwa wa kawaida kuelekea mjini huku baadhi ya gari ya polisi zikifuata nyuma kwa kupiga ving’ora ili kupisha njia kumbe kwa jinsi hiyo walimpa mwanya Mellina kuchanja mbuga, dakika kama tano kulikuwa na pengo kubwa kati ya polisi na Mellina.
“Weka gari pembeni,” aliamuru Cheetah kisha akafungua mlango na kuwaamuru wenzake kumfuata, wote walitoka na moja kwa moja wakaenda katika maegesho ya NAKUMATT supermarket maeneo ya Westland na kuingi kwenye Toyota Prado, kwa kutumia funguo za bandia waliiwasha ile prado na kuitoa pale maegeshoni na kuileta barabara kubwa, waliyaacha mafgari ya polisi yapite kisha wao wakaingia nyuma yao na kufuata taratibu.
“Sasa tunakwenda moja kwa moja kuchukua ile Mostrance sasa” Cheetah aliamuru na kila mmoja akajiweka sawa kwa hilo, bastola zilizoshindiliwa risasi za kutosha zilikuwa tayari mikononi na viunoni mwao.
§§§§§
“Ah!” koplo Kariithi alitikisa kichwa kwa kuchelewa kufika eneo la tukio,
“Vipi koplo?” sergeant Maria alimuuliza huku akiweka vizuri jacket lake.
“Yaani ningewapata hawa leo, nakuhakikishia afande ungeijua shabaha yangu leo” Kariithi alimueleza huku akivuta hatua fupifupi kuwaelekea wale polisi wawili waliokuwa pale kwa doria ambao ndiyo waliwapigi redio ili wafike hapo.
“Siku yao ipo! Usiku huu halali mtu mpaka tuwatie mkononi kwa gharama yoyote ile” sergeant Maria alimueleza koplo Kariithi. Kishapo wote wakaingia garini na akabla hawajatoka eneo lile walipata taarifa kuwa gari aina ya Subaru forester iliyotumiwa na majambazi hao imeonekana maeneo ya Westaland imetelekezwa, nao wote wakaenda hapo kuiona, kama walivyoambiwa waliikuta pale imetulia.
“Koplo, tunapambana na watu makini, tujiweke vyema” Maria alimtahadaharisha Kariithi.
Wakiwa wanajiandaa kuondoka wakati huohuo polisi wakifanya mchakato wa kuiwekea mtego ile gari labda watarudi kuichukua, mara walikatishwa na kelele kutoka katika maegesho ya supermarket hiyo.
“Oooh my car my car” (Oooh gari yangu, gari yangu), Sergeant Maria alitega sikio na kushuka katika gari yao kisha akaelekea kule kwenye ile kelele, mama mmoja wa kizungu alikuwa akilia kwa uchungu kuwa gari yake imeibwa, sergeant Maria alimtuliza na kumuuliza maswali machache kisha akamchukua na kwenda nae kituo cha karibu kwa ajili ya kuanza uchunguzi, alipokwishamkabidhi kwa wahusika, akarudi garini na kumkuta Kariithi akiwa bize kusikiliza muziki uliokuwa ukipigwa ndani ya gari hiyo, aliingia na kujifungia mlango.
“Koplo, kwa vyovyote Cheetah na wenzake wameiba ile gari,”
“Nilikuwa nafikiri hivyo pia, afande huu lazima uwe usiku wa kazi” Kariithi alisisitiza.
“Endesha gari!” Maria aliagiza
“Twende wapi afande?”
“Twende tukabane karibu na kanisa kuu kwa muda kidogo tukisubiri taarifa nyingine, labda tutaokota kitu huko.” Kariithi akaitoa ile gari kujiunga na magari mengine kuelekea katikati ya mji. Ilikuwa imetimu saa nne usiku, bado foleni ilikuwa kubwa ya magari katika jiji la Nairobi.
ITAENDELEA….
 
Kwa mahitaji ya Riwaya nyingine kali kutoka kwa Richard Mwambe kama vile
TUFAA JEKUNDU
CRONOC 7
KITISHO
HARUFU YA KIFO
MPATANISHI n.k
Walisiana nae kwa namba
+255 766 974 86
 
MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE

“Koplo, kwa vyovyote Cheetah na wenzake wameiba ile gari,”
“Nilikuwa nafikiri hivyo pia, afande huu lazima uwe usiku wa kazi” Kariithi alisisitiza.
“Endesha gari!” Maria aliagiza
“Twende wapi afande?”
“Twende tukabane karibu na kanisa kuu kwa muda kidogo tukisubiri taarifa nyingine, labda tutaokota kitu huko.” Kariithi akaitoa ile gari kujiunga na magari mengine kuelekea katikati ya mji. Ilikuwa imetimu saa nne usiku, bado foleni ilikuwa kubwa ya magari katika jiji la Nairobi.

§§§§§
SEHEMU YA 7

Ngumi ya hasira ilitua juu ya meza ya chuma katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali kuu ya Nairobi, huku akiuma meno aliuangalia mwili wa Fr Gichuru uliolala kwenye kitanda hicho ukiwa ndani ya mfuko maalum wa plastiki.
“Bill, Bill, Billllllllll !!!!! lazima ulipe kifo hiki kwa gharama yoyote,” Melchior Ndege alijikuta akiongea peke yake mle ndani ya chumba kile kidogo cha kuhifadhia maiti.

Hali ya utulivu ilitawala nje ya eneo la jingo hilo kubwa, watu waliokaa kwa utulivu kwenye vibenchi vidogo vilivyowekwa maalumu kwa kazi hiyo. Melchior Ndege alitoka akiwa kama mtu asiyejielewa na moja kwa moja aliingia kwenye gari yake na kuliacha eneo hilo kurudi ofisini.
Aliketi na kutulia akiwa na mawazo mengi sana juu ya hili sakata, sasa aliona kuwa kazi inaanza rasmi, kumsaka Bill na genge lake, kujua ni nani yuko nyuma ya Bill katika hili.
Mlio wa simu ulimshtua Melchior mawazoni, akaitazama simu ile iliyokuwa ikipiga kelele bila kunyamaza, akainyanyua na kuiweka sikioni, hakuongea kitu bali alijaribu kusikiliza sauti ya upande wa pili, nako kulikuwa kimya, walitegeana. Zaidi ya kusikia pumzi inayopanda na kushuka kutoka upande wa pili, melchior hakuna alichosikia kutoka kwa mpiga simu, akaitua taratibu na kuiweka mezani bila kuirudisha kwenye kitako chake na kuifanya iendelee kuwa hewani, zaidi ya hilo alibofya kitufe cha kuruhusu sauti isikike kwa nguvu ‘loud speaker’ kisha akajituliza kitini. Akishika hiki na kile juu ya meza yake mara mlango uligongwa na kufunguliwa na mgongaji aliyejitoma ndani bila kukaribishwa, hakuwa mwingine ni yule boss wake bwana Shikuku aliyeingia akiwa amefura kwa hasira ambayo ilimtisha hata Melchior, akajitupa kwenye kiti cha upande wa pili na kushusha pumzi ndefu,
“Mr Ndege, FBI wapo hapa” alimwambia Melchior ambaye alionekana kushtushwa kidogo kwa taarifa hiyo
“Oh shit, wataharibu mipango yetu” Ndege alimjibu huku akiiweka kalamu yake mezani na mkono kuuelekeza shavuni.
“Sio wataharibu, wameshaharibu,” bwana Shikuku alitamka hayo huku akitikisa kichwa, kisha akamuangalia melchior na kumwambia, “Wameshatuomba tujitoe kwenye huu mkakati ili wao wafanye kazi ya kumnasa bwana Bill, wameniuzi”
“What?!” bwana Ndege aliuliza kwa mshangao mkuu.
“Ndiyo hivyo,” Shikuku akajibu kwa mkato huku akiangalia pembeni.
“Bill hawezi kuondoka mikononi mwetu kijingajinga wakati tunajua wazi jinsi alivyoendesha mambo ya kijasusi katika Afrika Mashariki, na sasa yupo kwetu tena, kule Tanzania alitoroka hatukuweza kumtia mkononi kwa sababu hizi hizi, sasa na leo tena haiwezekani,” Melchior aliongea kwa uchungu, kisha akatulia na baadaye kumtazama boss wake, “Bill nitamtia mkononi kabla ya wao kufanikisha hilo” alimwambia boss wake huku akifungafunga vitabu vyake, akasita kidogo na kusema, “Lazima tujue nyuma ya mauaji ya kasisi kuna nini, mpaka Bill ahusike, tusipompata Bill hatutaweza kutatua juu ya kifo hiki cha utata, mimi nina mwanzo wa mkasa na Bill ana hatima ya mkasa, lazima nimpate mimi na siyo FBI.
5
DAR ES SALAAM
TANZANIA

MVUA kubwa iliendelea kunyesha katikati ya jiji la Dar es salaam, maji yalizijaza barabar zote na kufanya ugumu wa watembea kwa miguu kuonekana dhahiri, akina mama viatu mkono wakizikunja nguo zao kwa juu huku mifuko ya plastiki ikiwa imefunika vichwa vyao ili kuokoa nywele za gharama zisiharibike, magari nayo yalipita shida kwa namna moja au nyingine, yakitumbukia kwenye mashimo ya liyojitengeneza kutokana na mvua hiyo, basi jiji lote lilikuwa vururuvururu. Kila mtu alionekana kuchukia hali ile ambayo serikali inaifumbia macho mara zote, shida kubwa ikawa kwa wale waishio mabondeni waliokuwa wakifukuzwa kila siku tangu enzi za mheshimiwa Makamba lakini waling’ang’ana utafikiri walizaliwa hapo, huyu akisonya, yule akimkashifu kiongozi Fulani wa chama na serikali.
“Bora tuwachague wapinzani mwaka ujao” mwingine alisikika akisema hayo huku akiwa juu ya moarobaini uliokuwa ndani ya maji nusu nzima. Ilhali anasahau kuwa mvua hizo ni mabadiliko ya tabia nchi ambayo mimi na wewe ndio visababishi.
“Ila mi Mabwepande ndio siendi” alijibiwa na yule aliyekuwa juu ya paa lanyumba iliyochoka ambayo kwayo uhai wake ulifika tamati, alisahau kabisa kuwa haikomoi serikali bali anawaumiza watoto wake ambao hakuhusika katika kuchagua eneo la kuishi.
Wakati upande mwingine watu wakiwa wamejazana katika daraja kubwa la Tabata Matumbi wakivumilia harufu kali ambayo ilisemekana ni ya mwili wa binadamu uliokwama katika maji yam to Msimbazi huku jeshi la polisi likisaidi kazi hiyo, wengine walikuwa wakichanganya vichwa, akili na mawazo yao vikiwa tofauti na matakwa ya mioyo yao.
Ndani ya jengo la JM MALL, ghorofa ya saba mlango namba 705 ni watu wawili tu mwanamke na mwanaume walikuwa wameketi wakitazamana mmoja akishindwa kuamua na mwingine akishindwa kushauri nini cha kuamua. Wakiwa bado katika kushangaana wawili hawa mara mlango ulifunguliwa na bibi mmoja wa makamo ambaye nywele zake zilishahitilafiana na weusi wake wa asili na kuubeba weupe ambao wengi hupenda kuuita mvi, aliingia moja kwa moja na kuketi kwenye kiti kikubwa ambacho kilikuwa pembeni kidogo ya meza ile safi iliyozungukwa na mapambo murua ambayo ukiketi basi yatakupa burudani ya macho na kuondosha ile ambayo muandishi wa kitabu cha SHIDA, Ndyanao Balisidya aliita ‘kiwi cha macho’.
“Karibu Madam S” Kamanda Amata alisimama na kupeana mkono na mwanamama huyu aliyebobea kwenye kazi za kikachero tangu usichana wake.
“Nimekaribia Kamanda” akajibu huku akijiweka vizuri pale kochini ambapo aliweza kuonana na mrembo aliyemkuta ofisini humo. Mara baada ya kujiweka sawa alimtzama Amata na kumpa bahasha moja ya khaki ambayo juu yake imeandikwa maandishi yanayoitambulisha kuwa ni mali ya serikali, akaitupia mezani na Kamanda Amata akaichukua na kuifungua, baada ya kuisoma akaitupia mezani,
“Nairobi tena! Kuna nini madam?” Kamanda Amata aliuliza
“Mauaji ya Kasisi, jasusi Bill Van Getgand yuko Nairobi, FBI na taasisi nyingine za kikachero zimetuma watu wao kumnasa, lakini sifikiri kama ni vyema wakamchukua ndani ya ardhi yetu wenyewe, huyu ameshatekeleza mambo Fulani ya kijasusi katika nchi yetu na zingine za Afrika Mashariki” madam S alikuwa akiongea bila mapumziko akionekana wazi amehamanika kwa hilo.
“Madam, mi niko safarini,” kamanda Amata alitoka katika meza yake na kuchukua vifaa vyake vichache vya kiofisi, akamwita Gina na kumpa maagizo Fulani Fulani ya kiofisi kisha akatoka na madam S, boss wake wa miaka mingi na kuondoka zake.

§§§§§

BOEING 737 ilishuka katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta. Ilikuwa alasiri tulivu uwanjani hapo palipoonekana kuwa na ulinzi mkali wa polisi na ule wa vyombo binafsi vya ulinzi.
Baada ya itifaki zote kukamilika, kamanda Amata alitoka nje na kukamata tax moja kabla ya kuamua wapi anataka kwenda mchana huo. Alijiweka katika saiti ya nyuma na kumwambia dereva ampeleke katika hoteli kubwa ya nyota tano katikati ya jiji hilo la Nairobi.
Kamanda Amata alifika katika Hotel Intercontinental, katika mtaa wa Posta na kuweka kambi yake hapo akiwa naa kazi moja tu aliyotumwa na serikali yake ama kumkamata Bill ili ajibu kwa yale aliyoyafanya siku za nyuma au uhai wake ubaki Afrika Mashariki na mwili wake urudi kwao, ilikuwa ni moja kati ya hayo lililotakiwa kutekelezwa. Amata alitupia begi lake kitandani na kuchukua kifaa chake maalum kilichoweza kung’amua kama humo ndani kuna aina yoyote ya mlipuko au chombo chochote kitakachoweza kuhatarisha maisha yake, aliporidhika na usalama wake, akalisogelea dirisha kubwa na kuvuta kidogo pazia lake na kutupa macho yake nje upande wa chini ambako pilikapilika za wakazi wa Nairobi waliokuwa wakirudi majumbani kutokea makazini zilikuwa kubwa, kana kwamba hakuridhika na kile alichokua akikitazama alivuta kibegi chake na kutoa kiona mbali na kukisogeza karibu na macho yake, naam kile alichokiangali kilikuwa kikionekana kwa uzuri wa hali ya juu, vijana waliokuwa wakijidunga madawa ya kulevya katika moja ya mitaa hiyo ulioonekana wazi kuwa haukuwa ukitumika na wapita njia, alitazama kwa makini vijana wale walivyojidunga mpaka kuanza kusinzia pale chini, Amata alitikisa kichwa kwa masikitiko, ‘Nguvu kazi ya taifa inatoweka’. Akiwa katika kutafakari hayo mara alisikia ving’ora vya polisi na kufuatiwa na gari mbili zilizopita kwa kasi kuelekea upande wa pili wa eneo hilo, ‘Shughuli za kiusalama hizo’, alijiwazia kwa mara nyingine na kutoka pale dirishani kisha kuketi katika kochi moja lililopo pale chumbani. ‘Bill Van Getgand, umekuja tena, sasa hakika hutoponyoka kwenye mikono hii,’ akaivuta laptop yake na kuanza kuperuzi habari mbalimbali za jasusi huyo, akirejea hasa yale matukio yaliyofanywa na mtu huyu pale Dar es salaam …

Miaka mitano iliyopita
Kilimanjaro Hotel

KAMANDA Amata aliuangalia mwili usiokuwa na uhai uliokuwa ukielea katika bwawa la kuogelea la hoteli hiyo kubwa ya kimataifa iliyopo pembezozi mwa bahari ya Hindi. Watu kadhaa walizunguka eneo hilo wote wakiwa wametokwa na hamu ya kujiburudisha kwa maji hayo ambayo sasa yalikuwa mekundu kwa damu ya mtu huyo aliyeonekana kuwa na asili ya America. Akiwa amepiga goti moja pale katika ukingo wa bwawa hilo, kamanda Amata aliinua kichwa chake na kutazama uelekeo ambao labda muuaji alikuwapo, kwa maana mtu huyo aliuawa kwa risasi iliyotoka katika bunduki aina ya Sniper Rifle ya Kimarekani, naam macho yake yalitua mahali sawia, dirisha moja lililokuwa katikati kama ghorofa ya nane hivi katika jingo lililokuwa na benki ya Meridian Biao enzi hizo. Alipotuiliza macho yake alishuhudia pazia la dirisha hilo likifungwa ghafla kana kwamba aliyekuwa hapo dirishani alikuwa akimtazama Amata pia. Ili asimpoteze maboya mtu huyo Kamanda Amata kwa kutumia simu yake maalum iliyounganishwa na saa ya mkononi alipeleka ujumbe wa sauti kwa Madam S aliyekuwa upande wa pili wa jingo hilo, nae bila kusita alituma kikosi cha watu wanne kwenda kufanya uchunguzi katika ghorofa hiyo.

Hisia za Amata hazikuwa bure, jasusi Bill Van Getgand lilikamilisha kazi yake kupitia ofisi ya mtu Fulani ndani ya jingo hilo kwa kutumia bunduki ya Sniper Rifle, wakati vijana wale wakigawana majukumu mmoja apande kwa lift, mwingine kwa ngazi ya kawaida na wengine wabaki nje kutazama kinachoendelea, ndipo yule aliyepanda kwa ngazi alipopishana na Bill aliyekuwa akishuka huku akitanguliwa na mwanadada mmoja mwenye umbo dogo aliyekuwa amebeba koba kubwa la kuhifadhia guitar lakini akiwa kwenye hali ya kutojiamini, yule afisa usalama alitulia kidogo na kuwaangali huku akipishana nao na mara hiyo akatoa taarifa kwa walio nje kumwafuatilia watu hao bila kuwapoteza.
Kwa uchunguzi wa muda mfupi uliofanyika katika chumba kilekile ambacho Amata alikihisi tangu mwanzo liliokotwa ganda moja la risasi ambayo ni ile iliyotumika kumuua bwana yule.
Kamnda Amata alilitazama ganda lile na kutikisa kichwa kukubali hisia zake.
“Mnasema mmeweka watu wawafuatilie hao mnaowahisi?” aliwauliza wale vijana chipukizi katika kazi hiyo.
“Ndiyo na tunatumaini bado wanawafuatilia” alijibu mmoja wao. Kamanda Amata akainua simu yake ya upepo na kuwauliza vijana wale waliopewa kazi,
“Ndiyo, tupo hapa Red Carpet Upanga, wameingia ndani na bado hawajatoka, gari yao ipo hapa nje inawasubiri,” jibu lilimridhisha Amata, aliingia garini na mara moja kuelekea Upanga, akawakuta vijana wake wakiwa wametega pa si kuwaona watu hao, masaa mawili yalikuwa yamepita, Amata aliteremka na kuzunguka lile jingo la ghorofa mbili na alipofika nyuma yake alitikisa kichwa kwa kuugundua upumbavu wa vijana hao waliobaki ndani ya gari wakati nyuma ya jingo kuna ngazi zinazoweza kumtoa mtu yoyote aliye ndani ya jingo hilo, akarudi mpaka mbele na kuwapa taarifa hiyo ambayo iliwafanya wafadahaike sana kwa ujinga walioufanya.
Hakika Bill Van Getgand alikuwa ametokea upande wa pili pamoja na yule mwanadada na kuchukua tax iliyokuwa imeegeshwa huko nyuma na kuondoka zao mpaka uwanja wa ndege ambako walichukua ndege na kuelekea Nairobi.
Baada ya kumsukasuka yule dereva wa tax aliyewabeba Bill na yule mwanadada hakuna jibu la maana walilopata zaidi ya kubaki na lile koba la gitaa ambalo ndani yake kulikuwa na bunduki kubwa iliyotumika kwa mauaji yale lakini hakukuwa na guitar, baada ya uchunguzi wa hali ya juu kufanyika uliohusisha vyombo mbalimbali vya kiintelijensia ilionekana Bill amehusika na mauaji hayo na si sehemu moja tu basil maeneo mbalimbali duniani, nah ii iliifanya nchi yetu kuingia kwenye matatizo ya kimahusiano na nchi husika ya mrehemu yule kwani iligundulika alikuwa ni mtu muhimu serikalini ambaye alikuja kwa shughuli za kiserikali na kufikia hapo hoteli ya Kilimanjaro.

Rejea Nairobi Intercontinental Hotel…

Kamanda Amata aliishusha picha ndogo ya Bill aliyokuwa akitumbulia macho na kuirudisha kwenye kikoba maalum. Mara kengele ya mlango wa chumba chake ikagongwa, akanyanyuka taratibu na kuuendea mlango huo huku bastola yake ndogo ikiwa mkononi mwake, akiwa kaificha kwa nyuma alimruhusu mtu huyo kuufungua mlango. Mwanadada mwembamba, mrefu wa wastani aliupenyeza mwili wake ndani ya chumba cha Amata, Amata alimeza mate ya uchu hasa alipokutana macho na paja mwororo la mwanadada huyo ambalo lilibaki wazi baada ya sketi yake iliyofungwa kwa vifungo upande wa kulia kulipa nafasi paja hilo kuonekana, kiuno chake kidogo kilibeba kajiumbo ka wastani, si kanene sana, lakini kenye mvuto mahsusi kwa mwanaume yoyote rijali, mikono ya Amata ilipoteza nguvu na kuiruhusu ile bastola yake kurudi mfukoni bila kutarajia, macho yake yalikuwa yakitalii kifua cha mwanadada huyo ambapo blauzi aliyoivaa yenye vifungo vichache mbele iliruhusu nusu ya titi lake ambalo halikuhifadhiwa kwa sidiria kuonekana na kumfanya kamanda kuinuka kutoka pale alipoketi na kumjongelea mwanadada huyu, kabla hajamfikia, yule msichana aliweka magazeti aliyokuwa nayo mkononi juu ya meza ya kioo iliyokuwa hapo ndani.
“Wakati unasubiri kuonana na mwenyeji wako, usome magazeti haya!” sauti tamu ya yule dada iliyapenya masikio ya Kamanda Amata. Baada ya kuyaweka magazeti hayo pale mezani, aligeuka na kutoka nje huku macho ya Amata yakimsindikiza kwa kila hatua aliyoivuta, alitoka na kuurudishia mlango nyuma yake. Amata alibaki kapigwa na bumbuwazi, ‘Mwenyeji, mwenyeji wangu,’ alijiuliaza, kengele za hatari zikalia kichwani mwake, akainama kuchukua yale magazeti lakini kabla hajayachukua kutoka pale mezani, akasita, akatazama saa yake, muda ulikuwa umekwenda sana, akaachana nay ale magazeti na kujiandaa kwenda kuoga.
Dakika chache zilimpita akiwa maliwato na alipomaliza, aakaufungua mlango, akasimama ghafla, akatupa macho yake juu ya kitanda kikubwa kilichopo katika chumba hicho hakuamini anachokiona, akafikicha macho kana kwamba anachokiona ni kiini macho.
“Come to me boy..” sauti ya msichana yule aliyekuja na magazeti ilimfikia tena Amata masikioni, akamtazama kwa makini msichana huyu mrembo aliyejilaza kitandani na kujifunika shuka mpaka maeneo ya kifuani na kuishika kwa mkono mmoja huku mwingine ukifanya ishara ya kumuita Amata kitandani. Lilikuwa ni jicho baya na kali la Amata lililomfanya yule msichana kuurudisha mkono wake chini na kupatwa na sura ya woga. Amata akautazama mlango ambao yeye aliufunga lakini alishangaa huyu msichana kapita vipi mpaka kujitoma ndani ya chumba hicho, kisha akarudisha macho yake pale kitandani, “Toka!” alimuamuru yule msichana, lakini hakuonekana kuitii amri hiyo, “Mmmm boy, kwa nini unanifukuza wakati nimekuja kukuburudisha?” alianza kutumia silaha ya sauti yake kumlainisha Amata, “Tokaaaa!” Amata aling’aka kwa hasira huku akimfuata yule msichana pale kitandani, yule msichana akanyanyuka haraka na kukiacha kitanda kile, akasimama pembeni akiwa uchi wa mnyama, akachukua nguo zake na kuzivaa kisha akaufungua mlango na kutoka nje. Kamanda Amata akakiendea kioo cha ukutani na kujitazama kisha akaanza kuvaa suti yake nadhifu aliyoichagua kwa siku hiyo. Akiwa pale kiooni alihisi mlango ukifunguliwa kwa mara nyingine, kabla hajageuka aksikia sauti kutoka nyuma yake, “Tulia hivyohivyo, ukijifanya mjuzi, tunaondoka na pumzi yako,” Amata akaona sasa mambo si mambo, akaendelea kujiandaa huku mtutu wa bastola yenye kiwambo cha sauti ikimtazama.
“Ok, umependeza, sasa utaondoka na sisi, bwana Bill anataka kukukona usiku huu kwa maana hana uhakika kama jua la kesho utaliona,” yule jamaa alimwambia Amata huku akimruhusu kutangulia mlangoni ambapo palikuwa na watu wengine wawili, hamna ujanja. Kamanda Amata aliongoza taratibu nje ya chumba kile na kuifikia korido ndefu, mbele yake kulikuwa na mtu mmoja, nyuma yake kulikuwa na mwingine yule mwenye bastola ambayo sasa alikuwa ameifunika kwa koti lake la suti kiasi kwamba kwa mtu mwingine hasingeweza kujua kama mkoni hapo kuna mguu wa kuku. Waliingi ndani ya lifti kwa mtindo huo huo, hakuna aliyeongea kati yao, wakateremka mpaka chini na kuongoza kwenye gari moja la kifahari aina ya Cardilac, gari ya kifahari na gharama ya hali ya juu, Amata alitangulizwa kuingia ndani kiti cha nyuma kisha wawili kati ya wale watatu wakaingia mmoja huku na mwingine kule, yule mwenye bastola akiwa mmoja wao, mwingine wa tatu akaingia siti ya mbele.
“Karibu sana Amata,” ilikuwa sauti ile tamu ya mrembo aliyeongea huku akigeuka nyuma na kumtolea tabasamu pana Kamanda. Taratibu waliyaacha maegesho ya hotele ile na kutokomea mjini, barabara chache na foleni za hapa na pale katika jiji hilo la Nairobi ziliwafanya wachukue muda kidogo kufika wanapopakusudia, mwanadada yule aliyekuwa akiendesha gari hiyo kwa umahiri mkubwa alikatiza kwatika vichochoro mbalimbali na kutimiza kusudio lake.
Mguu wa kulia wa mwanadada yule ulihama kutoka katika pedeli ya mafuta na kukanyaga ile ya breki huku mikono yake ikiuzungusha usukani kwa kidole kimoja kuingia katika maegesho ya hoteli ya Safari Park.
Wote wakashuka na yule mwanadada alitangulia kuelekea ndani ya hotel ile akifuatiwa na wale wengine wakati Kamanda Amata alikuwa katikati ya wote, wakaingia na kupita mapokezi kisha kuingia upande mwingine na kuchukua lifti kushuka ghorofa moja chini, walipotoka walikaribishwa na maandishi makubwa ya kuwakawaka yaliyosomeka, Safari Park Casino, casino ya kisasa iliyojengwa chini ya ardhi katika hotel hiyo, mlangoni walisimama wazaume wawili waliovalia suti nyeusi na kuonekana wameshiba kimazoezi, walikuwa wamesimama mithili ya sanamu ya bismini.
“Clean!” mmoja wa wale waliomtangulia Amata alitamka neon hilo akimaanisha hakuna shida, mara mlango wa kioo ukafunguka na wote wakaingia ndani. Taa za rangi mbali mbali ziliujaza ukumbi huo ambao ulionekana kuwa na shughuli nyingi, wanaocheza kamali walikuwapo, wacheza uchi nao walilipamba jukwaa wakicheza miziki yao michafu, waliokuwa wakinyonyana ndimi hadharani nao hawakukosa, wale waliokana jinsia zo hawakuwa mbali, ilimradi tu dhambi zote zilihifadhiwa ndani ya casino hilo.
“Huku tafadhali,” Amata alielekezwa ngazi ndefu zilizokuwa zikipanda juu, akazifuata bila ubishi mpaka juu, pale wale wasindikizaji wakamuacha na kupokelewa na wengine kisha akaingizwa ndani ya chumba safi na nadhifu kilichoja samani za gharama ya hali ya juu, mbele yake kulikuwa na mtu mnene amaye alisimama na kuja kumlaki kwa bashasha, “Oooh Kamnda Amata, karibu sana, nisingefurahi kama nisingeonana nawe leo hii, karibu sana,” Bill alimkaribisha Amata na kumuongoza kitini, kisha akampatia glass yenye kinywaji na kuketi katika mtindo wa kutazamana.

§§§§§

Akiwa kwa mwendo wa miguu huku akipiga mruzi usiku huo, Melchior Ndege alikuwa akipita mbele ya hotel hiyo ya Safari Park, mara akapitwa na gari moja ya kupendeza inayovutia macho, akasimama kuitazama gari ile, Cardillac ya bluu nyeusi, iliyokwenda na kuegeshwa kwa utulivu. Lakini alipata mshtuko baada ya kuwaona wale walioshuka kutoka garini, aliwatazama kwa makini na kuoamua kubadili uelekeo wa safari yake. Melchior aliyaamini macho yake yaliyomwambia kuwa umuonaye ndiye Kamanda Amata, ‘Shiiit, amefika lini?’ alijiuliza na kusukuti kwa sekunde chache kabla kuruhusu miguu yake kuamriwa na ubongo juu ya lile linalopaswa kutendwa kwa wakati huo. Alipotazama vizuri, kwa macho yake ya kipelelezi akajua wazi kuwa Kamanda alikuwa kwenye hatari, akavuka kijibarabara kidogo na kuelekea mlango mkubwa wa hotel ile kisha akaingia ndani, alipofika mapokezi hakutaka kupoteza muda kwani aliwaona wapi wameingilia, akafuata, wakati wao wakifunga mlango wa lifti kuteremka chini yeye akazifuata ngazi zinazoelekea hukohuko chini. Alizuiliwa mlangoni na kupekuliwa, “Haturuhusu kuingia na silaha, weak pale unapotoka utaichukua.” Melchior alisogea kwenye meza ndogo ambayo ilikaliwa na mwanadada mrembo akaichukua bastola ya Melchior na kumpatia kadi maalum ya kumbukumbu. Akaelekea kaunta na kuketi juu ya kiti kimoja kirefu mbele ya kaunta hiyo. Akiwa anakunywa kinywaji chake taratibu huku macho yake akiwa kayaongoa kule wlikopelekwa Kamanda Amata, ambapo palitenganishwa na ukumbi mkubwa kwa vioo maalum vinavyoruhusu mtu wa ndani kuweza kuona kinachoendelea ukumbini lakini yule wa ukumbini asiweze kujua nini kinaendendele ndani ya chumba kile. Melchior akatoa miwani yake maalumu na kuipachika usoni, miwani hii ilikuwa na madini ambayo yaliweza kupenya kwenye kioo cha aina yoyote pia yaliweza kukuruhusu kuona mtu kama amebeba silaha au vipi, maana iliruhusu kuona vitu vigumu tu vilivyo mwilini mwa mtu. Alimuona Kamnda Amata akiwa na Bill wakizungumza, lakini hakuweza kujua wanazungumza nini, aliwatazama walinzi wa mlango wakuingia kule juu aliwaona wakiwa na bastola mbili kila mmoja, kisha akawatazama wafanyakazi wa casino hiyo na kuona kila mmoja alivyoipachika silaha yake, kisha akayarudisha macho yake na kuyatuliza kule aliko Kamanda Amata na kuendelea kuona kinachojiri, huku akiendelea kunywa kinywaji chake. Mara alihisi, akipapaswa kwa nyuma maeneo ya kiunoni, akageuka na kukutana macho na mwanamke mshumami, aliyejiremba akarembeka, yule mwanamka aliyeonekana ana kila dalili ya ulevi machoni mwake alizunguka na kusimama mbela ya Melchior, akamrembulia macho, Melchior hakuonesha hata kumjali kwani yeye alitaka kujua tu nini kitatokea kule ndani, “Mwanamke unataka nini? Kama kinywaji chukua uende, mi sihitaji mwanamke saa hii,” Melchior alimwambia yule mwanamke, akamnunulia kinywaji kisha kwa akapewa shukrani ya sonyo kali na refu, “Go fish!” yule mwanamke alimwambia Melchior.
§§§§§

ITAENDELEA..
 
MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE

Melchior hakuonesha hata kumjali kwani yeye alitaka kujua tu nini kitatokea kule ndani, “Mwanamke unataka nini? Kama kinywaji chukua uende, mi sihitaji mwanamke saa hii,” Melchior alimwambia yule mwanamke, akamnunulia kinywaji kisha kwa akapewa shukrani ya sonyo kali na refu, “Go fish!” yule mwanamke alimwambia Melchior.

SEHEMU YA 8

“Bado mnanifuata Kamanda!” Bill alimwambia Amata huku akimimina kinywaji katika glass yake.
“Kwanza nashangaa kukuona huku, umekuja kufanya nini?” Amata alimuuliza Bill, cheko kali lilimtoka mpaka walinzi wake waligeuka kutazama ndani.
“Kamanda Amata, mimi si motto mdogo au punguani, najua ninachofanya na ninajua kila anayeingia katia wigo wangu popote pale katika pepo zote nne za dunia,” Bill aliongea kwa kujiamini, “Nina macho Kamanda, siyo haya mawili, mengi tu, na nilijuwa kuwa utakuja, maana una kiu na mimi, lakini ujue hata mimi nina kiu na wewe, umeshaniharibia mambo mengi sana,” akapiga fuinda moja kinywaji chote kikaishia tumboni mwake, akabeua kwa shibe ya kinywaji.
“Bill Van Getgand, unajua unachokizungumza? Nimekuja Nairobi, nashangaa naambiwa wewe unanihitaji, nisingeshindwa kuwararua hawa nyau wako hata kama wangekuwa hamsini, lakini kwa heshima yako nikawaacha na kuwatii kwa kuwa umeniita, na ungependa kuniona kabla ya jua la kesho kwa kuwa unajua kuwa jua la kesho sitaliona, ok, niambie ulichotaka kuniambia, unataka kunipa deal?” Kamanda Amata aliuliza.
“Oh, Kamanda, mi nipo hapa takribani wiki mbili sasa, nimekuja kibiashara, lakini nilijuwa safari yako ya kuja hapa Nairobi, nikajua wazi kuwa wewe ni mgeni wangu, ndo maana nikakukaribisha uje tustarehe, lakini nataka uniambie umekuja kufanya nini hapa Nairobi,” Bill alihoji kijanja.
“Bill, maswala yangu ya kikazi siwezi kukwambia wewe kuwa nimekuja kufanya nini, kama hilo ndilo uliloniitia basi hutopata jibu,”
“Hivi unajua kuwa upo mikononi mwangu?” Bill aliuliza
“Hata kama, lakini huwezi kunilazimisha nikwambie nimekuja kufanya nini,”
Bill akachomoa bastola yake na kumnyooshea Amata, “Utaniambia tu, maana hata nikikuua hapa hakuna atakayejua kama umekufa zaidi ya mimi na wewe mwenyewe,”
“Sitishiki na hiyo bastola ya Kirussi Bill,” Amata alijibu kijeuri, lakini kabla hajakaa vizuri, bastola ya Bill ikafyatuliwa, risasi ikapenye katikati ya paja na paja la Amata, ile sofa ikatimua vinyoya kidogo, Amata alitetemeak ka hofu, kijasho chembachemba kikamtiririka, akaona kuwa kumbe hapo hakuna usalama wala mzaha, hakuna urafiki kama upo basi ni wa mashaka.
“Usifikiri nakutania, nataka unieleze lile lililokuleta, na ukijifanya mjanja nakuua,” Bill aliongea huku akimlenga na ile bastola yake iliyoonekana wazi iko tayari muda wowote kufanya itakachoamuliwa, kabla hajajaibu, Bill alifyatua risasi kadhaa, moja katikati ya mapaja ya Amata, ya pili upande wake wa kushoto nay a tatau upande wa kulia, hali ile ilimfanya Amata aweweseke na kushindwa kujua atfanye nini, alibaki kutetemeka na kulowa jasho mwili mzima, akabana meno kwa hasira, “Nimekuja kukufuata wewe hayawani, na nakupa muda mchache tu utakuwa mikononi mwangu, Bill, ndipo dunia itakapojua kuwa roho moja dhalimu imeondoka duniani.”
“Aaaaaaa ha ha ha ha ha!” Cheko la Bill lilipasua anga la chumba kile, “Kamanda Amata, Tanzania Secret Agency, hapa mmefika, nitawaacha hapa na mi nitaondoka na kile kilichonileta. Kama hauamini hujiulizi nimejuaje kuwa huko hapa! Ujue kuwa muda wowote nitaitwaa roho yako kabla ya jua la asubuhi inayofuata.” Bill akamalaiza risala yake na kugugumia tena glass nyingine ya kinywaji kikali, “Nimefurahi kukuona!” alimalizia na kuichukua fimbo yake ya kutembelea kisha kuondoka eneo lile.
“Tutaonana tena soon,” Amata alijibu kijeuri na kunyanyuka kuelekea mlango, kabla hajatoka mlangoni alisimama na kugeuka nyuma akagongana macho na Bill, wakatazamana, “Siku yetu inakuja,” alimwambia na mara wale walinzi wakamvuta kumtoa katika mlango ule alioutumia kuingilia na kwenye ngazi alikutana na yule mwanadada aliyemjia chumbani akiwa ameweka pozi akitazama yanayoendelea ukumbini mle, wakatazamana kwa sekunde, “Unahitaji lifti yangu?” yule mwanadada alimuuliza Amata huku tayari akiongozana nae kumsindikiza, mara simu ya yule mwanadada ikaita, “Yes Boss…” aliitika, sauti ya upande wa pili ilisikika vizuri masikioni mwa Amata japo ilikuwa ndogo, “Nakupa usiku huu tu ukamstareheshe Kamanda, maana ana msongo wa mawazo, kisha urudi kabla jua alijachomoza,”
“Sawa boss, umesomeka,” alijibu kisha akamwangalia Amata, “Leo mimi na wewe mpaka kuchee, boss ameruhusu,” kisha akamshika mkono Amata na kujichnganya nae katikati ya watu ndani ya casino ile.
§§§§§

Nyimbo za masifu ya jioni zilikuwa zikirindima katika masikio ya walio jirani na eneo hilo la kanisa la Holy Family, masista waliokuwa kanisani mida hiyo walikuwa wakimalizia sala zao za jioni kabla ya kwenda kulala, kusubiri siku inayofuatia, ikiwa ni siku chache tu tangua mazishi ya Fr Gichuru yamalizike, bado mioyo yao ilikuwa imejawa na huzuni ukizingatia kwao kasisi huyo alikuwa ni mtu wa pekee sana, mwenye karama ya uponyaji ya hali ya juu, mpole, mcheshi, mwenye upendo na mcha Mungu.
Ibada ilimalizika na watawa hao wa kike walianza kutoka kuelekea nyumbani kwao, nyumba iliyo umbali wa kama mita mia mbili kutoka kanisa hilo, taa za nje zenye mwanga wa njano zilipendezesha eneo hilo, maua na miti michache ilifanya kabaridi kawe kakali kiasi. Masista wote walimalizika isipokuwa sista Rose ambaye alikuwa akimalizia kupanga vitu vya ibada itakayofuatia, kisha afunge sakristia. Haikumchukua muda alimaliza na kujianda kutoka ndani ya jengo hilo ili akaungane na wenzake. Alipoukaribia mlango tu alijikuta akibanwa na mkono wenye nguvu, uliombana barabara katika shingo yake hata akajikuta anakosa pumzi na mwili wake kukosa nguvu, mkono ule ulilegezwa kidogo na kumruhusu sista Rose kuweza kufurukuta kidogo, akataka kupiga kelele lakini alibadili mawazo ghafla baada ya kukutana na bisu kubwa na kali lililoshikwa na mkono wa mwanamke, Mellina alimkazia macho mwanamke mwenzake kana kwamba anamwangalia kuku au sungura.
“Monstrance! Onesha haraka iliko,” ilikuwa sauti ya Mellina ikimtoka huku mkononi bado kalishikilia lile jisu lake tena akiwa kalinyooshea kwa sista Rose. Ilikuwa ni wakati mgumu sana kwa mtawa yule wa kike, hakuwa na ujanja, hatari zote zilimkabiri, “Tuoneshe ilipo monstrance, tunaitaka monstrance sasa hivi, ukileta ujuaji nakutumbua na hili bisu,” Mellina alimwambia Sista Rose huku akiwa bisu lake kaliegesha nchaye katika ziwa moja la mtawa yule aliyekuwa akitetemeka kwa hofu kuu huku akilisukuma kama anayetaka kutoboa.
“Utaonesha au tukumalize kama yule kasisi wenu? Maana na ye alikuwa mbishi kama wewe” Cheetah alimuuliza kutoka nyuma yake, ndipo yule sista akajua kuwa aliyemkaba alikuwa ni mwanaume. “Ni ni nitawaonesha!” alijibu yule sista. Kisha wote kwa pamoja wakaongozana kuelekea milango mingine iliyotengenezwa vizuri kabisa ndani ya vyumba hivo vya kanisa hilo kubwa. Baada ya kupita milango kadhaa mara waliteremka ngazi kuelekea chini na huko walikuta stoo kubwa lakininzuri yenye vitu vingi tena vya thamani kubwa, sista Rose akawaonesha kabati moja kubwa lililofungwa ukutani, Mellina akaliendea na kufungua milango yake, “Waoh!” alijisemea kwa sauti ambayo kila mmoja alisiikia. “Nini Mellina?” Cheetah aliuliza, alipokaza macho yake alishuhudia monstrance kubwa ya dhahabu safi ikiwa imetulia kabatini, akamuacha yule mtawa na kuliendea kabati akainyanyua ile monstrance kwa umakini wa hali ya juu na kuiweka mikononi mwake, kisha kwenye begi walilokuja nalo maalumu kwa kazi hiyo. Sista Rose alikuwa akitetemeka sana akiangalia walivyokuwa wanaichuku bila heshima yoyote kwa chombo hicho kitakatifu.
“Tafadhali muiache hiyo monstrance,” sista Rose aliwasihi Cheetah na Mellina.
“Acha ujinga wako,” alijibiwa na mellina huku akipata pigo moja la ubapa wa kile kisu kikubwa. Sista Rose akabaki kimya huku machozi yakimtoka baada ya pigo lile, walipohakikisha wameiweka sawa katika begi lile la ngozi, Cheetah akalibeba na kumtazama sista Rose, akacheka cheko la dharau, “Kazi yetu imekwisha, kwa heri msalimie paroko,” Cheetah alimwambia sista Rose huku akimpita na kuuelekea mlango waliouingilia. Pigo moja la judo lilitua mwilini mwa sista Rose, akapepesuka, kabla hajajitambua, mellina akampa pigo lingine lililompoteza akili na kumbwaga chini kama mzigo, kisha guu nene la Mellina lilikanyaga koromeo la sista yule kwa sekunde kadhaa likimkandamiza chini na kumfanya kurusharusha miguu na mikono huku na kule na kuzimika. Ilikuwa tabu kuujua mlango waliongilia, kila walipoufungua huu walijikuta eneo lingine kabisa, walipojaribu huu hali ilikuwa ileile, Cheetah alionekana kuchanganyikiwa maana alipoingia aliona milango michache lakini sasa anaona milango mingi kuliko ile ya kwanza, iliwachukua dakika nyingi kuutafuta mlango ule bila mafanikio.

§§§§§

Melchior Ndege, aliendelea kupepesa macho yake maangavu ndani ya casino lile lililosheheni watu wa kila aina, muda ulivyozidi kwenda ndivyo watu walivyoongezeka ndani yake, alihakikisha hampotezi Amata machoni pake, na liona wazi jinsi alivyokuwa amegandwa na mwanadada yule. Melchior alijaribu kuvuta kumbukumbu ni wapi amekwisha wahi kumuona yule mwanadada lakini jibu hakulipata kirahisi japokuwa sura ilikuwa ikimjia.
Alimuona Kamanda Amata akiwa anakunywa kinyaji kikali huku mwanamke yule akiwa pembeni yake na akionekana kumhamasisha, mara amsike kiunoni mara ambusu mara ampapase hapa na pale, kisha aliwaona wakikokotana kutoka nje ya casino ile.
Melchior alishusha glass yake taratibu na kuiweka katia meza ya kaunta kisha akateremka kutoka katika kile kiti kirefu na kuuendea mlango wa casino kutoka nje, akachukua bastola zake pale mlangoni nakuiendea lift iliyompandisha hadi juu na kutoka mlango mkubwa wa hoteli. Katika maegesho ya magari alimuona Amata akiwa na yule mwanamke, sasa ilionekana wazi kuwa mapenzi yanachukua nafasi yake, akajifanya anapiga simu, ili kupoteza muda ajue kitachoendelea. Muda si mrefu, ikasimama gari pembeni yao, Jeep Cherokee ya kibuluu hivi, yule mwanamke akamvutia ndani Amata na gari ile ikatoweka. Melchior alitazama hapa na pale na kuona gari nyingi zilizokuwa zimeegeshwa na wamiliki wake walikuwa wakila starehe ndani ya hoteli ile, akaiendea moja wapo, Toyota Celica, akatoa funguo yake, wengi huiita Malaya, funguo inayoweza kufungua takribani lock zaidi elfu kumi za magari bila shida achana na switch zake. Alizungusha mara mbili tu mult lock zikaachia akaingia nyuma ya usukani na kulitekenya nalo likacheka, taratibu akaingia barabarani na kuifuata ile Jeep Cherokee, alikanyaga mafuta na kuhakikisha haiachi mbali gari ile, kati yake aliacha gari kama mbili hivi na kuendelea kuifuata, baada ya barabara tatu nne na vichochoro kadhaa ilianza kuuacha mji na kuchukua barabara ya kuelekea Thika, Melchior aliendelea kuwafuata na walipokaribia maeneo ya Kalimoni, akaona hapana, akaongeza mwendo na kuifikia ile Jeep, akaipita na kukaa mbele yao. Kila dereva wa ile jeep alipoijitahidi kuipita ile gari ya Ndege haikuwa rahisi, Melchior akaongeza kasi na kuiacha kama mita ishirini hivi kisha akafunga breki kali sana na ile jeep ilikuja na kuigonga ile Toyota kwa nyuma, kutoka katika ile jeep, mtu mmoja akateremka na kuifuata ile Toyota akaangalia ndani lakini hakuona dalili ya mtu, alitazama huku na kulea asione kitu, akarudi garini mwake na kuingia, alipofunga mlango tu alihisi kitu cha baridi kikigusa shingo yake, “Tulia hivyohivyo,” sauti ilimwambia, kisha Ndege akaunyoosha mkono wake na kuichomoa bastola ya yule dereva, wakati huo tayari kipigo cha haraka kilishampa usingizi wa muda yule mwanamke aliykuwa na Amata, “Toa gari barabarani, weka kando ile,” Melchior Ndege aliamuru na amri ikafuatwa, mbele kabla ya mahali alipoambiwa aiegeshe gari ile palikuwa na daraja kubwa sana la mpishano wa barabara, wao sasa walikuwa barabara ya juu, yule dereva akafanya hila kwa kugongesha ile gari katika ukingo wa daraja, ile gari ikayumba kidogo, Melchior, mle ndani ya gari akaangukia upande wa pili na kumpa nafasi yule dereva kufanya lolote, lakini kabla hajafanya hivyo, maana Melchior alimuona akichomoa bastola nyingine sehemu Fulani ya dashboard yake, kitendo bila kuchelewa, kwa kutumia miguu yake miwili alimbana kabali njema, gari iliyumba lakini Melchior hakujali, mara akasikia kishindo kikubwa, ile gari ilijipiga kwenye ukingo wa daraja, ikahamia upande wa pili ikakutana na Toyota prado na kujibamiza kisha akaangukia nje ya barabara. Kamanda Amata akiwa hajui lolote linaloendelea kutokana na usingizi mzito alioulala mara tu baada ya kuingia mle garini, alijigonga kichwa kwenye muhimo wa dirisha, akshtuka na kuanza kushangaashangaa, huku damu zikimtiririka kutoka kwenye jeraha dogo lililotokea katika kichwa chake baada ya kujigonga kule.
Melchior alitoka kwa shida kidogo katika gari ile baada ya kuvunja kioo cha mbele, kisha akamsaidia Kamanda Amata kutoka nje, bado Kamanda alikuwa hajarudiwa na akili sawasawa alikuwa kama zezeta hivi, Melchior akamshika mkono na kutembea nae kuelekea pale alipoiacha ile gari alioichukua kule hotelini, aliwakuta polisi wawili akiitazama ile gari huku wakiwa na wanaandikaandika vitu Fulani wakisaidiwa na taa za barabarani. Melchior aliufungua mlango wa mbele na kumtumbukiza Kamanda kiti cha kushoto kisha yeye akazunguka kiti cha kulia, “Halo, vipi, mbona unakuwa kama hauheshimu mamlaka?” mmoja wa wale askari akauliza, Melchior akawasha gari huku akimwangalia yule askari, “Nenda pale karibu na njia panda utakuta ajali ya gari aina ya Jeep Cherokee, hiyo ndiyo ukaipime, hii sio ajali,” kisha akaondoka kwa kasi mpaka kwenye mzunguko mkubwa na kuhama njia kuchukua njia inayorudi mjini, kwa mwendo uleule wa kasi ya ajabu.

AGA KHAN HOSPITALI
Parkland Avenue-Nairobi

MELCHIOR ndege aliegesha gari katika lango la hospitali ile na daktari mmoja alikuwa pale tayari na kitannda cha magurudumu, akisaidiwa na manesi wawilli walimlaza kamnda Amata na kuingia naye ndani, moja kwa moja wakamuweka kitandani kwemye chumba cha peke yake, wodi maalumu, daktari alipomuangalia vizuri aliona wazi hali yake si nzuri, hivyo akaamuru awekewe drip ya glucose ili iweze kumrejeshea nguvu japo kidogo. Wale wauguzi wakafanya hivyo lakini pia walicheki mapigo ya moyo na kuweka kumbukumnbu zake kati faili maalumu lililokuwa pale, Kamanda Amata alilala kimya akiwa hajitambui tena, jeraha lake lilishonwa na kuwekwa katika hali ya usafi.
Melchior Ndege, alipekuwa kwenye mifuko ya Amata lakini hakuona chochote, akabaki kumtazama pale kitandani alipozungukwa na mitambo tiba ya kisasa ambayo ilikuwa inaangalia mwenendo wa mwili kwa ujumla kama mapigo ya moyo na mambo mengine. Melchior Ndege alitoka nje na kufunga mlango mkubwa kioo kisha kurudi ofisini kwa daktari.
“Rafiki yako inaonekana amepewa sumu kali sana ambayo imempotezea fahamu na kuathiri mfumo wa urendaji kazi wa mwili wake, itamchukua masaa mengi sana kuirudia hali yake ya kawaida,” Daktari alimweleza Melchior Ndege, haikuwa rahisi kulielewa swala hilo, lakini aligundua kuwa Bill alidhamiria kummaliza Amata. Akashusa pumzi ndefu na kumtazama daktari.
“Huyu ni mtu wetu, katoka Tanzania,” akamwambia kwa kifupi, daktari akatikisa kichwa kuashiria kuwa ameelewa, kisha Melchior akampa habari nzima jinsi alivyomuona kuanzia pale hotel ya Safari park mpaka kule kwenye ajali.
Hasira zilizidi kumtawala Melchior na moyoni akaapa lazima Bill alipe yote ayafanyayo, hapo akagundua kuwa Bill ni jasusi la kimataifa lenye mbinu za kuua bila kutumia silaha na kuwafanya watu kutojua ni nini chanzo cha kifo. Aliagana na daktari na kuomba kurudi baadaye kidogo lakini apewe taarifa ya kila kinachoendelea.
Safari yake na gari ile ya kukodi iliishia katika mtaa wa Riara, akashuka na kuilipa tax hiyo kisha akaliendea geti kubwa jeusi lilofungwa sawia, akabofya kengele, mara likafunguka naye akajitoma ndani, “Karibu sana kijana!” alikaribishwa na sauti ya boss wake bwana Shikuku, “Vipi mbona usiku sana ?” akaongeza swali, ndipo Melchior alipoinua mkono wake kuitazama ile saa yake iliyomuonesha kuwa ni saa nane kasoro robo usiku. Wakaingia sebuleni na kuzungumza machache, Melchior alimpa habari yote ya Kamanda Amata. Shikuku alisikitishwa sana na habari hiyo, kisha wote wawili usiku huo wakatoka na kuelekea kule hospitali kumuona Kamanda, walimkuta katika hali ileile isipokuwa sasa ilikuwa mbaya zaidi kwani mapigo ua moyo yalishuka sana, hata daktari alikuwa na wasi wasi juu ya hilo maana hayakuonekana kupata unafuu wowote.
“Shiiiittt!!!!” aliinua simu yake na kubofya namba Fulani kisha kusikiliza sauti ya upande wa pili, baada ya mazungumzo mafupi aliikata na kuiweka mezani, akajishika kichwa kwa masikitiko, mara simu yake ikapata uhai na kujitikisatikisa pale mezani, aliinyakuwa na kusikiliza, “Yeah… ndiyo… ee. Fanyeni haraka tafadhali,” akakata simu na kuitia mfukoni.
“Vipi, ni nani hao?” Ndge alimuuliza bosi wake.
“Nilikuwa nawapa taarifa juu ya mtu wao huko Tanzania, ili wajue ni nini watafanya, sasa wamesema wayanijibu haraka iwezekanavyo,” Shikuku alijibu.
“Hivi Bill amedhamiria haswa kufanya mauaji ya mtindo huu sivyo?” Ndege alimuuliza Shikuku.
“Yule ni shetani, sio binadamu, hivi umesema yuko wapi saa hii?” Shikuku aliuliza swali kwa Ndege.
“Niliwaacha, Safari Park casino, lakini sidhani kama bado wako hapo, ngoja tufatilie wale watu wa kwenye ile gari ili tujue kwa undani juu ya sakata hili na nini kipo nyuma yake, simpendi kabisa Bill, na aombe Kamnda Amata asiamke milele, lakini Shikuku nakuhakikishia, Kamanda akiamka atavunja mpaka miiko ya kazi yake ili amtafute huyu hayawani na kwanza atamuua kisha amuulize maswali anayoyataka,” melchior Ndege aliongea kwa hasira na kutoka nje ya chumba cha daktari.
Mkono wa bwana Shikuku ulimshika bega Melchior Ndege pale alipokuwa ameegemea ukuta akiwa amewaka hasira zilizojaa uchungu.
“Malchior, punguza jazba, pamoja na FBI kuwa hapa, isiturudishe nyuma, ingia kazini, mimi nakuamuru, kama kuna swali mi nitajibu; Kamanda atapona tu, najua walimuwahi katika namna ambayo hakuitegemea,” yalikuwa ni maneno ya Shikuku kwa Melchior, akageuka kumtazama mtu huyo mwenye mwili mkubwa, mkuu wa idara ya usalama wa Taifa hapo Kenya, Melchior alitabasamu kwa bashasha baada ya kuambiwa ‘Ingia kazini’, alitoka pale alipo na kuelekea tena chumba cha daktari kisha akaingia kumuona Kamanda, alimutoa alama ya saluti ya heshima, na kumuhakikishia Kamnda kuwa sasa analipiza kisasi kwa ajili yake, kishapo akatoka nje na kuagana na Shikuku.

DAR ES SALAAM
Saa 9:15 Usiku

KELELE za simu ya mezani ya Madam S ilipiga kelele usiku huo, mlio wa dharula ulimshtua kutoka katika usingizi mzito, “Aaaa nini tena saa hizi?” aliongea kwa sauti ya hasira na kuinyakua ile simu masikioni mwake, “Hallo nini saa hii?” aliipokea na kutupa swali hilo; huku akisikiliza sauti ya upande wa pili, “Madam, kuna taarifa kutoka Nairobi kuhusu Kamanda Amata, hali yake ni mbaya sana yuko kufani,” sauti hiyo iliongea kwa upole, ilikuwa ni simu kutoka ofisi ya usalama wa Taifa ikimpa taarifa hiyo Madam, mkuu wa kitengo maalum chenye watu wachache makini wanaofanya kazi za umakini kwa umakini wa kimakini. Aliishika ile simu bila kuongea. “Unasemaje?” akauliza, akajibiwa tena jibu lilelile. Madam S alishikwa na kigugumizi, midomo ilimchezacheza, hakuamini anachoambiwa, ni jana tu mchana alipoagana na Kamanda wake pale JNIA na kumpa usia wa nguvu, Madam alibaki kimya na simu ikiwa hewani nab ado hajaishusha kutoka sikioni mwake, akashusha pumzi kisha akafungua kinywa chake, “OK, asante kwa taarifa, fanya kila kinachowezekana Kamanda afike hapa mara moja,” akakata simu na kurudisha mkono wake mahali pake, “Uuuuhhhhh!!!!” akashusha pumzi nzito kwa mara nyingine, akajilaza kitandani kwake huku mawazo lukuki yakiwa yamemtawala kichwani mwake. Akafikiri la kufanya na kumpigia daktari wao pale Muhimbili, ushauri aliopewa aliuona una maana sana, yule daktari alimshauri ikodiwe ndege ya haraka kutoka Nairobi imlete Dar, badala ya kukodi kutoka Dar. Utaratibu ukaandaliwa haraka kwa ushirikiano na Bwana Shikuku kule Kenya. Usingizi haukuja tena kwa Madam S, akaifungua kompyuta yake ya kazini ambayo imeunganishwa moja kwa moja katika kitanda chake, alipojaribu kuingiza password yake, ikagoma, haikufuka, akajaribu tena na tena, wapi. Alipoona imeshindikana, akampigia simu Chiba, mtaalamu wa ICT wa kitengo chao, naye akajaribu kuifungua lakini ikawa ngumu, akatumia mbinu zote kuitafuta maana alishajua kuwa wajanja wameiiba kimtandao, na kwa maana hiyo siri zote za usalama wa Tanzania ziko hatarini kuvuja, kijasho kilimtoka Chiba, usingizi ulikatika, akiwa mezani kwake alikuwa akishindana na mtandao kuloitatua tatizo hilo huku Madam S akimuahidi kufika hapo mapema ili kujua kulikoni. Majibu yalikuja na kugundua kuwa kompyuta ya Madam S imekuwa ‘Hiked’ sehemu Fulani huko Nairobi, mchezo ukaanza kunoga, sasa mapigano ya kimtandao, Chiba hakukubali, alifanya juu chini kuinusuru, ‘Kamanda Amata wanataka kumuua na mtandao wanataka kuukamata, shiit,” alijiwazia kisha akaiacha kompyuta yake na kuelekea kwenye kabati lake, akavaa nguo haraka haraka na kuibeba ile kompyuta kisha kuchukua gari yake haraka akawahi katika ofisi ya mawasiliano ya Usalamawa Taifa, pale kuna kompyuta kubwa zaidi inayoweza kujua vizuri sana, ni wapi na ni nani aliyefanya hivyo, haikuchukua muda aliinasa, na kuifunga kabisa kwa namba ambazo mwingine asingeweza kuzifungua. Akasimama na kumtazama kijana aliyekuwa akisaidiana naye kazi hiyo, Frank Masai.
“Dah, hatujui ni kiasi gani wamepata siri zetu,” Chiba alimueleza Frank Masai aliyekuwa kasimama karibu na meza kubwa yenye screen kubwa sana ya kompyuta inayoweza kuzileta kompyuta nyingi za ulimwenguni na kutafuta kila wanachokitaka.
“Sasa Bro, cha kufanya ni kiunguza kabisa hiyo kompyuta yao waliyotumia kutu ‘hike’,” Frank alisema.
“Tutafanyaje, maana inabidi tupate namba ya BIOS,” Chiba alisema
“Ah no, siku hizi huwezi kuua kompyuta kwa kuiharibu BIOS maana technolojia imepanda kaka, Operating System za sasa zina uwezo wa kutest kila hardware na software zilizopo kati kompyuta bila kupitia kwenye BIOS, cha kufanya hapa tufuondoe taarifa zetu kisha mi nitaweka kirusi kibaya sana kwa jina la faili moja, najua kwa vyovyote watafungua tena, maana kwa sasa wanaonekana wapo offline, kisha huyo kirusi atavuruga system yote ya kompyuta yao,” Frank Masai alijibu kwa kujiamini, kijana mwenye elimu ya ICT kutoka chuo kikuu cha Dar es salaam.
“Ok, fanya hivyo wakati mi nafanya mengine,” Chiba alimalizia. Kijana Frank Masai alikaa makini kwenye laptop yake akitengeneza shetani hilo alilolipa jina TOP SECRET, kazi iliyochukuwa kama lisaa limoja hivi na kuifanikisha akiwa kachoka sana. Kisha akamwendea Chiba na kumwambia kazi tayari ili apate ruhusa ya kufanya mlipuko huo, akakubaliwa, kazi ndogo, akaingiza kile kirusi kwenye mfumo wa kompyuta ya Madam S na kukiacha hapo, wakati document zingine zote akiwa zimebanwa na Chiba kwa pin ngumu.

§§§§§

REJEA NAIROBI… kanisa la familia Takatifu…

Ilikuwa ni kazi ngumu kwa Black Cheetah na Mellina kutoka ndani ya wigo wa kanisa maana tayari sergeant Maria na koplo Kariithi walikuwa pale na wengine wanne wenye silaha, walitanda kila upande kuhakikisha majambazi hao hawatoki bila kuacha roho zao.
Gichui, aliyekua akiendesha gari siku hiyo aliwapa taarifa kwa simu kuwa jamaa wamejipanga vipi huko nje, wakamuamuru, aanzishe show kwa kupiga risasi za hewani. Naye akafanya hivyo, mlio wa risasi zile ukawafanya wale askari kuchanganyikiwa kidogo, Black Cheetah alitoka katika mlango mkubwa akiwa na lile begi na kukimbilia upande wa pili wa ukuta huo ambako ndiko waliokoingilia, huku Mellina akitambaa mwendo wa nyoka kulifuata geti kubwa akiwa na bastola yake aina ya revolver mkononi mwake.
Gichui alipiga norinda na kutimua vumbi liliwachanganya Mellina na Kariithi ambao walikuwa tayari kujibu mashambulizi, Sargeant Mellina alijitupa chini na kubingirika kwa usatadi mpaka kwenye ukuta wa wigo wa kanisa hilo huku akishuhudia vijana wake wakijiweka tayari, “Freeze!!!!!!” sauti ya askari mmoja lisikika upande wa pili, Kariithi bado alikuwa akijaribu kuona afanye nini, akajitoa na kukimbilia upande wa sauti ile ilipotokea, akiwa anakata kona ya ule ukuta alisikia mlio wa risasi na kushuhudia mwili wa yule askari ukijibwaga chini kama kiroba, “Shiittt!” akng’aka kwa hasira, alimuona Cheetah, aliyeifanya kazi hiyo akiishia gizani, akajaribu kulenga na kufyatua risasi mbili lakini hakumpata, mara ile gari yao ilipita kwa kasi na kuelekea upande ule alipo Cheetah, haikuhitaji kusimama, kawani Cheeta alirusha begi ndani ya gari na kujirusha kupitia dirishani, lakini kabla hajamalizi miguu risasi moja ilipita katikati ya mguu wake na kufumua mifupa ya ugoko, Gichui aliizungusha gari kwa ustadi na kumfanya Cheetah kutumbukia ndani, “Aaaaaaaaiiiiggggghhhhhh!!!!” ulikuwa ukelele wa maumivu kutoka kwa Cheetah.
“Vipi brother?” Gichui aliuliza huku akiizungusha tena ile gari na kumgonga askari mwingine, sasa alikuwa akilielekea geti kuu la kanisa lile.
“They have shot me, bastards!” wamenipiga wanaharamu alimwambia Gichui, huku akiiweka tayari bastola yake. Sergeant Maria akiwa pale chini aliilenga sawia ile gari na kabla hajapiga risasi alihisi kama kitu kimenguka pale alipolala kwa nyuma yake alipogeuka aliona mwanamke kibonge akitua juu ardhi kavu na bastola mkononi, akiwa pale chini alijigeuza na kupiga mtama mmoja maridadi, Mellina alilipokea pigo hilo na kubwagwa chini, alijitahidi kujiinua kisarakasi lakini kabla hajawa wima mtama mwingine wa Mellina ulimrudisha chini na kumfanya hoi pale ardhini, sasa alishindwa kujiiunua. Bastola ya Mellina ilicheua na risasi ikapita mililmita chache kwenye uso wa Maria aliyekuwa pale chini, teke moja kali la afande Maria lilipeperusha bastola ile kutoka mikono ya Mellina ikapaa juu, kisha aliushusha mguu wake na kuutuza juu ya uso wa Mellina.
Koplo Kariithi alijitoa mhanga na kucukua ile SMG ya askari ambaye aliku marehemu, kuilenga gari ya Gichui, ‘nice shot’ risasi moja alipiga tairi ya nyuma na kuipotezea muelekeo ile gari, ikayumba na kuyumba lakini ikakaa tena barabarani, risasi ya pili kutoka kwa Kariithi ikakishusha kioo cha nyuma na bila kukosea ikafumua kisogo cha Gichui na ile gari ikayumba myumbo mkuu na kugonga mti. Wakati Kariithi akiifuta, ghafla nyuma yake kulitokea gari aina ya BMW kwa kasi ya ajabu ikafunga breki kali karibu kabisa na ule mti ilipogonga ile gari ya Gichui, kwa haraka watu wawili walishuka na kuifungua milango wakamtoa Cheetah na kulibeba begi kisha kurudi ndani, ile gari nayo ikazungushwa kwa mtindo wa U turn na risasi moja iliyotoka ndani ya gari ile ilimpata koplo kariithi mkononi, na ukelele wa maumivu, ulimchanganya sergeant Maria, akamsahau Mellina na kumkimbilia Kariithi, “Soldier!!!” Askari, sergeant Maria aliita kwa sauti na askari wote wakaja eneo hilo na kumbeba mwenzao wakimpakia kwenye gari, wengine wakabaki kufanya utaratibu wa kumuondoa Gichui ambaye alikuwa hana maisha tena na kichwa chake kikiwa kimevurugika kwa risasi ya Kariithi, moja kwa moja walimfikisha katika hospitali ya taifa ya Nairobi.

ITAENDELEA ....
 
RIWAYA: MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE

“Koplo, kwa vyovyote Cheetah na wenzake wameiba ile gari,”
“Nilikuwa nafikiri hivyo pia, afande huu lazima uwe usiku wa kazi” Kariithi alisisitiza.
“Endesha gari!” Maria aliagiza
“Twende wapi afande?”
“Twende tukabane karibu na kanisa kuu kwa muda kidogo tukisubiri taarifa nyingine, labda tutaokota kitu huko.” Kariithi akaitoa ile gari kujiunga na magari mengine kuelekea katikati ya mji. Ilikuwa imetimu saa nne usiku, bado foleni ilikuwa kubwa ya magari katika jiji la Nairobi.

§§§§§
SEHEMU YA 9

Ngumi ya hasira ilitua juu ya meza ya chuma katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali kuu ya Nairobi, huku akiuma meno aliuangalia mwili wa Fr Gichuru uliolala kwenye kitanda hicho ukiwa ndani ya mfuko maalum wa plastiki.
“Bill, Bill, Billllllllll !!!!! lazima ulipe kifo hiki kwa gharama yoyote,” Melchior Ndege alijikuta akiongea peke yake mle ndani ya chumba kile kidogo cha kuhifadhia maiti.

Hali ya utulivu ilitawala nje ya eneo la jingo hilo kubwa, watu waliokaa kwa utulivu kwenye vibenchi vidogo vilivyowekwa maalumu kwa kazi hiyo. Melchior Ndege alitoka akiwa kama mtu asiyejielewa na moja kwa moja aliingia kwenye gari yake na kuliacha eneo hilo kurudi ofisini.
Aliketi na kutulia akiwa na mawazo mengi sana juu ya hili sakata, sasa aliona kuwa kazi inaanza rasmi, kumsaka Bill na genge lake, kujua ni nani yuko nyuma ya Bill katika hili.
Mlio wa simu ulimshtua Melchior mawazoni, akaitazama simu ile iliyokuwa ikipiga kelele bila kunyamaza, akainyanyua na kuiweka sikioni, hakuongea kitu bali alijaribu kusikiliza sauti ya upande wa pili, nako kulikuwa kimya, walitegeana. Zaidi ya kusikia pumzi inayopanda na kushuka kutoka upande wa pili, melchior hakuna alichosikia kutoka kwa mpiga simu, akaitua taratibu na kuiweka mezani bila kuirudisha kwenye kitako chake na kuifanya iendelee kuwa hewani, zaidi ya hilo alibofya kitufe cha kuruhusu sauti isikike kwa nguvu ‘loud speaker’ kisha akajituliza kitini. Akishika hiki na kile juu ya meza yake mara mlango uligongwa na kufunguliwa na mgongaji aliyejitoma ndani bila kukaribishwa, hakuwa mwingine ni yule boss wake bwana Shikuku aliyeingia akiwa amefura kwa hasira ambayo ilimtisha hata Melchior, akajitupa kwenye kiti cha upande wa pili na kushusha pumzi ndefu,
“Mr Ndege, FBI wapo hapa” alimwambia Melchior ambaye alionekana kushtushwa kidogo kwa taarifa hiyo
“Oh shit, wataharibu mipango yetu” Ndege alimjibu huku akiiweka kalamu yake mezani na mkono kuuelekeza shavuni.
“Sio wataharibu, wameshaharibu,” bwana Shikuku alitamka hayo huku akitikisa kichwa, kisha akamuangalia melchior na kumwambia, “Wameshatuomba tujitoe kwenye huu mkakati ili wao wafanye kazi ya kumnasa bwana Bill, wameniuzi”
“What?!” bwana Ndege aliuliza kwa mshangao mkuu.
“Ndiyo hivyo,” Shikuku akajibu kwa mkato huku akiangalia pembeni.
“Bill hawezi kuondoka mikononi mwetu kijingajinga wakati tunajua wazi jinsi alivyoendesha mambo ya kijasusi katika Afrika Mashariki, na sasa yupo kwetu tena, kule Tanzania alitoroka hatukuweza kumtia mkononi kwa sababu hizi hizi, sasa na leo tena haiwezekani,” Melchior aliongea kwa uchungu, kisha akatulia na baadaye kumtazama boss wake, “Bill nitamtia mkononi kabla ya wao kufanikisha hilo” alimwambia boss wake huku akifungafunga vitabu vyake, akasita kidogo na kusema, “Lazima tujue nyuma ya mauaji ya kasisi kuna nini, mpaka Bill ahusike, tusipompata Bill hatutaweza kutatua juu ya kifo hiki cha utata, mimi nina mwanzo wa mkasa na Bill ana hatima ya mkasa, lazima nimpate mimi na siyo FBI.
5
DAR ES SALAAM
TANZANIA

MVUA kubwa iliendelea kunyesha katikati ya jiji la Dar es salaam, maji yalizijaza barabar zote na kufanya ugumu wa watembea kwa miguu kuonekana dhahiri, akina mama viatu mkono wakizikunja nguo zao kwa juu huku mifuko ya plastiki ikiwa imefunika vichwa vyao ili kuokoa nywele za gharama zisiharibike, magari nayo yalipita shida kwa namna moja au nyingine, yakitumbukia kwenye mashimo ya liyojitengeneza kutokana na mvua hiyo, basi jiji lote lilikuwa vururuvururu. Kila mtu alionekana kuchukia hali ile ambayo serikali inaifumbia macho mara zote, shida kubwa ikawa kwa wale waishio mabondeni waliokuwa wakifukuzwa kila siku tangu enzi za mheshimiwa Makamba lakini waling’ang’ana utafikiri walizaliwa hapo, huyu akisonya, yule akimkashifu kiongozi Fulani wa chama na serikali.
“Bora tuwachague wapinzani mwaka ujao” mwingine alisikika akisema hayo huku akiwa juu ya moarobaini uliokuwa ndani ya maji nusu nzima. Ilhali anasahau kuwa mvua hizo ni mabadiliko ya tabia nchi ambayo mimi na wewe ndio visababishi.
“Ila mi Mabwepande ndio siendi” alijibiwa na yule aliyekuwa juu ya paa lanyumba iliyochoka ambayo kwayo uhai wake ulifika tamati, alisahau kabisa kuwa haikomoi serikali bali anawaumiza watoto wake ambao hakuhusika katika kuchagua eneo la kuishi.
Wakati upande mwingine watu wakiwa wamejazana katika daraja kubwa la Tabata Matumbi wakivumilia harufu kali ambayo ilisemekana ni ya mwili wa binadamu uliokwama katika maji yam to Msimbazi huku jeshi la polisi likisaidi kazi hiyo, wengine walikuwa wakichanganya vichwa, akili na mawazo yao vikiwa tofauti na matakwa ya mioyo yao.
Ndani ya jengo la JM MALL, ghorofa ya saba mlango namba 705 ni watu wawili tu mwanamke na mwanaume walikuwa wameketi wakitazamana mmoja akishindwa kuamua na mwingine akishindwa kushauri nini cha kuamua. Wakiwa bado katika kushangaana wawili hawa mara mlango ulifunguliwa na bibi mmoja wa makamo ambaye nywele zake zilishahitilafiana na weusi wake wa asili na kuubeba weupe ambao wengi hupenda kuuita mvi, aliingia moja kwa moja na kuketi kwenye kiti kikubwa ambacho kilikuwa pembeni kidogo ya meza ile safi iliyozungukwa na mapambo murua ambayo ukiketi basi yatakupa burudani ya macho na kuondosha ile ambayo muandishi wa kitabu cha SHIDA, Ndyanao Balisidya aliita ‘kiwi cha macho’.
“Karibu Madam S” Kamanda Amata alisimama na kupeana mkono na mwanamama huyu aliyebobea kwenye kazi za kikachero tangu usichana wake.
“Nimekaribia Kamanda” akajibu huku akijiweka vizuri pale kochini ambapo aliweza kuonana na mrembo aliyemkuta ofisini humo. Mara baada ya kujiweka sawa alimtzama Amata na kumpa bahasha moja ya khaki ambayo juu yake imeandikwa maandishi yanayoitambulisha kuwa ni mali ya serikali, akaitupia mezani na Kamanda Amata akaichukua na kuifungua, baada ya kuisoma akaitupia mezani,
“Nairobi tena! Kuna nini madam?” Kamanda Amata aliuliza
“Mauaji ya Kasisi, jasusi Bill Van Getgand yuko Nairobi, FBI na taasisi nyingine za kikachero zimetuma watu wao kumnasa, lakini sifikiri kama ni vyema wakamchukua ndani ya ardhi yetu wenyewe, huyu ameshatekeleza mambo Fulani ya kijasusi katika nchi yetu na zingine za Afrika Mashariki” madam S alikuwa akiongea bila mapumziko akionekana wazi amehamanika kwa hilo.
“Madam, mi niko safarini,” kamanda Amata alitoka katika meza yake na kuchukua vifaa vyake vichache vya kiofisi, akamwita Gina na kumpa maagizo Fulani Fulani ya kiofisi kisha akatoka na madam S, boss wake wa miaka mingi na kuondoka zake.

§§§§§

BOEING 737 ilishuka katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta. Ilikuwa alasiri tulivu uwanjani hapo palipoonekana kuwa na ulinzi mkali wa polisi na ule wa vyombo binafsi vya ulinzi.
Baada ya itifaki zote kukamilika, kamanda Amata alitoka nje na kukamata tax moja kabla ya kuamua wapi anataka kwenda mchana huo. Alijiweka katika saiti ya nyuma na kumwambia dereva ampeleke katika hoteli kubwa ya nyota tano katikati ya jiji hilo la Nairobi.
Kamanda Amata alifika katika Hotel Intercontinental, katika mtaa wa Posta na kuweka kambi yake hapo akiwa naa kazi moja tu aliyotumwa na serikali yake ama kumkamata Bill ili ajibu kwa yale aliyoyafanya siku za nyuma au uhai wake ubaki Afrika Mashariki na mwili wake urudi kwao, ilikuwa ni moja kati ya hayo lililotakiwa kutekelezwa. Amata alitupia begi lake kitandani na kuchukua kifaa chake maalum kilichoweza kung’amua kama humo ndani kuna aina yoyote ya mlipuko au chombo chochote kitakachoweza kuhatarisha maisha yake, aliporidhika na usalama wake, akalisogelea dirisha kubwa na kuvuta kidogo pazia lake na kutupa macho yake nje upande wa chini ambako pilikapilika za wakazi wa Nairobi waliokuwa wakirudi majumbani kutokea makazini zilikuwa kubwa, kana kwamba hakuridhika na kile alichokua akikitazama alivuta kibegi chake na kutoa kiona mbali na kukisogeza karibu na macho yake, naam kile alichokiangali kilikuwa kikionekana kwa uzuri wa hali ya juu, vijana waliokuwa wakijidunga madawa ya kulevya katika moja ya mitaa hiyo ulioonekana wazi kuwa haukuwa ukitumika na wapita njia, alitazama kwa makini vijana wale walivyojidunga mpaka kuanza kusinzia pale chini, Amata alitikisa kichwa kwa masikitiko, ‘Nguvu kazi ya taifa inatoweka’. Akiwa katika kutafakari hayo mara alisikia ving’ora vya polisi na kufuatiwa na gari mbili zilizopita kwa kasi kuelekea upande wa pili wa eneo hilo, ‘Shughuli za kiusalama hizo’, alijiwazia kwa mara nyingine na kutoka pale dirishani kisha kuketi katika kochi moja lililopo pale chumbani. ‘Bill Van Getgand, umekuja tena, sasa hakika hutoponyoka kwenye mikono hii,’ akaivuta laptop yake na kuanza kuperuzi habari mbalimbali za jasusi huyo, akirejea hasa yale matukio yaliyofanywa na mtu huyu pale Dar es salaam …

Miaka mitano iliyopita
Kilimanjaro Hotel

KAMANDA Amata aliuangalia mwili usiokuwa na uhai uliokuwa ukielea katika bwawa la kuogelea la hoteli hiyo kubwa ya kimataifa iliyopo pembezozi mwa bahari ya Hindi. Watu kadhaa walizunguka eneo hilo wote wakiwa wametokwa na hamu ya kujiburudisha kwa maji hayo ambayo sasa yalikuwa mekundu kwa damu ya mtu huyo aliyeonekana kuwa na asili ya America. Akiwa amepiga goti moja pale katika ukingo wa bwawa hilo, kamanda Amata aliinua kichwa chake na kutazama uelekeo ambao labda muuaji alikuwapo, kwa maana mtu huyo aliuawa kwa risasi iliyotoka katika bunduki aina ya Sniper Rifle ya Kimarekani, naam macho yake yalitua mahali sawia, dirisha moja lililokuwa katikati kama ghorofa ya nane hivi katika jingo lililokuwa na benki ya Meridian Biao enzi hizo. Alipotuiliza macho yake alishuhudia pazia la dirisha hilo likifungwa ghafla kana kwamba aliyekuwa hapo dirishani alikuwa akimtazama Amata pia. Ili asimpoteze maboya mtu huyo Kamanda Amata kwa kutumia simu yake maalum iliyounganishwa na saa ya mkononi alipeleka ujumbe wa sauti kwa Madam S aliyekuwa upande wa pili wa jingo hilo, nae bila kusita alituma kikosi cha watu wanne kwenda kufanya uchunguzi katika ghorofa hiyo.

Hisia za Amata hazikuwa bure, jasusi Bill Van Getgand lilikamilisha kazi yake kupitia ofisi ya mtu Fulani ndani ya jingo hilo kwa kutumia bunduki ya Sniper Rifle, wakati vijana wale wakigawana majukumu mmoja apande kwa lift, mwingine kwa ngazi ya kawaida na wengine wabaki nje kutazama kinachoendelea, ndipo yule aliyepanda kwa ngazi alipopishana na Bill aliyekuwa akishuka huku akitanguliwa na mwanadada mmoja mwenye umbo dogo aliyekuwa amebeba koba kubwa la kuhifadhia guitar lakini akiwa kwenye hali ya kutojiamini, yule afisa usalama alitulia kidogo na kuwaangali huku akipishana nao na mara hiyo akatoa taarifa kwa walio nje kumwafuatilia watu hao bila kuwapoteza.
Kwa uchunguzi wa muda mfupi uliofanyika katika chumba kilekile ambacho Amata alikihisi tangu mwanzo liliokotwa ganda moja la risasi ambayo ni ile iliyotumika kumuua bwana yule.
Kamnda Amata alilitazama ganda lile na kutikisa kichwa kukubali hisia zake.
“Mnasema mmeweka watu wawafuatilie hao mnaowahisi?” aliwauliza wale vijana chipukizi katika kazi hiyo.
“Ndiyo na tunatumaini bado wanawafuatilia” alijibu mmoja wao. Kamanda Amata akainua simu yake ya upepo na kuwauliza vijana wale waliopewa kazi,
“Ndiyo, tupo hapa Red Carpet Upanga, wameingia ndani na bado hawajatoka, gari yao ipo hapa nje inawasubiri,” jibu lilimridhisha Amata, aliingia garini na mara moja kuelekea Upanga, akawakuta vijana wake wakiwa wametega pa si kuwaona watu hao, masaa mawili yalikuwa yamepita, Amata aliteremka na kuzunguka lile jingo la ghorofa mbili na alipofika nyuma yake alitikisa kichwa kwa kuugundua upumbavu wa vijana hao waliobaki ndani ya gari wakati nyuma ya jingo kuna ngazi zinazoweza kumtoa mtu yoyote aliye ndani ya jingo hilo, akarudi mpaka mbele na kuwapa taarifa hiyo ambayo iliwafanya wafadahaike sana kwa ujinga walioufanya.
Hakika Bill Van Getgand alikuwa ametokea upande wa pili pamoja na yule mwanadada na kuchukua tax iliyokuwa imeegeshwa huko nyuma na kuondoka zao mpaka uwanja wa ndege ambako walichukua ndege na kuelekea Nairobi.
Baada ya kumsukasuka yule dereva wa tax aliyewabeba Bill na yule mwanadada hakuna jibu la maana walilopata zaidi ya kubaki na lile koba la gitaa ambalo ndani yake kulikuwa na bunduki kubwa iliyotumika kwa mauaji yale lakini hakukuwa na guitar, baada ya uchunguzi wa hali ya juu kufanyika uliohusisha vyombo mbalimbali vya kiintelijensia ilionekana Bill amehusika na mauaji hayo na si sehemu moja tu basil maeneo mbalimbali duniani, nah ii iliifanya nchi yetu kuingia kwenye matatizo ya kimahusiano na nchi husika ya mrehemu yule kwani iligundulika alikuwa ni mtu muhimu serikalini ambaye alikuja kwa shughuli za kiserikali na kufikia hapo hoteli ya Kilimanjaro.

Rejea Nairobi Intercontinental Hotel…

Kamanda Amata aliishusha picha ndogo ya Bill aliyokuwa akitumbulia macho na kuirudisha kwenye kikoba maalum. Mara kengele ya mlango wa chumba chake ikagongwa, akanyanyuka taratibu na kuuendea mlango huo huku bastola yake ndogo ikiwa mkononi mwake, akiwa kaificha kwa nyuma alimruhusu mtu huyo kuufungua mlango. Mwanadada mwembamba, mrefu wa wastani aliupenyeza mwili wake ndani ya chumba cha Amata, Amata alimeza mate ya uchu hasa alipokutana macho na paja mwororo la mwanadada huyo ambalo lilibaki wazi baada ya sketi yake iliyofungwa kwa vifungo upande wa kulia kulipa nafasi paja hilo kuonekana, kiuno chake kidogo kilibeba kajiumbo ka wastani, si kanene sana, lakini kenye mvuto mahsusi kwa mwanaume yoyote rijali, mikono ya Amata ilipoteza nguvu na kuiruhusu ile bastola yake kurudi mfukoni bila kutarajia, macho yake yalikuwa yakitalii kifua cha mwanadada huyo ambapo blauzi aliyoivaa yenye vifungo vichache mbele iliruhusu nusu ya titi lake ambalo halikuhifadhiwa kwa sidiria kuonekana na kumfanya kamanda kuinuka kutoka pale alipoketi na kumjongelea mwanadada huyu, kabla hajamfikia, yule msichana aliweka magazeti aliyokuwa nayo mkononi juu ya meza ya kioo iliyokuwa hapo ndani.
“Wakati unasubiri kuonana na mwenyeji wako, usome magazeti haya!” sauti tamu ya yule dada iliyapenya masikio ya Kamanda Amata. Baada ya kuyaweka magazeti hayo pale mezani, aligeuka na kutoka nje huku macho ya Amata yakimsindikiza kwa kila hatua aliyoivuta, alitoka na kuurudishia mlango nyuma yake. Amata alibaki kapigwa na bumbuwazi, ‘Mwenyeji, mwenyeji wangu,’ alijiuliaza, kengele za hatari zikalia kichwani mwake, akainama kuchukua yale magazeti lakini kabla hajayachukua kutoka pale mezani, akasita, akatazama saa yake, muda ulikuwa umekwenda sana, akaachana nay ale magazeti na kujiandaa kwenda kuoga.
Dakika chache zilimpita akiwa maliwato na alipomaliza, aakaufungua mlango, akasimama ghafla, akatupa macho yake juu ya kitanda kikubwa kilichopo katika chumba hicho hakuamini anachokiona, akafikicha macho kana kwamba anachokiona ni kiini macho.
“Come to me boy..” sauti ya msichana yule aliyekuja na magazeti ilimfikia tena Amata masikioni, akamtazama kwa makini msichana huyu mrembo aliyejilaza kitandani na kujifunika shuka mpaka maeneo ya kifuani na kuishika kwa mkono mmoja huku mwingine ukifanya ishara ya kumuita Amata kitandani. Lilikuwa ni jicho baya na kali la Amata lililomfanya yule msichana kuurudisha mkono wake chini na kupatwa na sura ya woga. Amata akautazama mlango ambao yeye aliufunga lakini alishangaa huyu msichana kapita vipi mpaka kujitoma ndani ya chumba hicho, kisha akarudisha macho yake pale kitandani, “Toka!” alimuamuru yule msichana, lakini hakuonekana kuitii amri hiyo, “Mmmm boy, kwa nini unanifukuza wakati nimekuja kukuburudisha?” alianza kutumia silaha ya sauti yake kumlainisha Amata, “Tokaaaa!” Amata aling’aka kwa hasira huku akimfuata yule msichana pale kitandani, yule msichana akanyanyuka haraka na kukiacha kitanda kile, akasimama pembeni akiwa uchi wa mnyama, akachukua nguo zake na kuzivaa kisha akaufungua mlango na kutoka nje. Kamanda Amata akakiendea kioo cha ukutani na kujitazama kisha akaanza kuvaa suti yake nadhifu aliyoichagua kwa siku hiyo. Akiwa pale kiooni alihisi mlango ukifunguliwa kwa mara nyingine, kabla hajageuka aksikia sauti kutoka nyuma yake, “Tulia hivyohivyo, ukijifanya mjuzi, tunaondoka na pumzi yako,” Amata akaona sasa mambo si mambo, akaendelea kujiandaa huku mtutu wa bastola yenye kiwambo cha sauti ikimtazama.
“Ok, umependeza, sasa utaondoka na sisi, bwana Bill anataka kukukona usiku huu kwa maana hana uhakika kama jua la kesho utaliona,” yule jamaa alimwambia Amata huku akimruhusu kutangulia mlangoni ambapo palikuwa na watu wengine wawili, hamna ujanja. Kamanda Amata aliongoza taratibu nje ya chumba kile na kuifikia korido ndefu, mbele yake kulikuwa na mtu mmoja, nyuma yake kulikuwa na mwingine yule mwenye bastola ambayo sasa alikuwa ameifunika kwa koti lake la suti kiasi kwamba kwa mtu mwingine hasingeweza kujua kama mkoni hapo kuna mguu wa kuku. Waliingi ndani ya lifti kwa mtindo huo huo, hakuna aliyeongea kati yao, wakateremka mpaka chini na kuongoza kwenye gari moja la kifahari aina ya Cardilac, gari ya kifahari na gharama ya hali ya juu, Amata alitangulizwa kuingia ndani kiti cha nyuma kisha wawili kati ya wale watatu wakaingia mmoja huku na mwingine kule, yule mwenye bastola akiwa mmoja wao, mwingine wa tatu akaingia siti ya mbele.
“Karibu sana Amata,” ilikuwa sauti ile tamu ya mrembo aliyeongea huku akigeuka nyuma na kumtolea tabasamu pana Kamanda. Taratibu waliyaacha maegesho ya hotele ile na kutokomea mjini, barabara chache na foleni za hapa na pale katika jiji hilo la Nairobi ziliwafanya wachukue muda kidogo kufika wanapopakusudia, mwanadada yule aliyekuwa akiendesha gari hiyo kwa umahiri mkubwa alikatiza kwatika vichochoro mbalimbali na kutimiza kusudio lake.
Mguu wa kulia wa mwanadada yule ulihama kutoka katika pedeli ya mafuta na kukanyaga ile ya breki huku mikono yake ikiuzungusha usukani kwa kidole kimoja kuingia katika maegesho ya hoteli ya Safari Park.
Wote wakashuka na yule mwanadada alitangulia kuelekea ndani ya hotel ile akifuatiwa na wale wengine wakati Kamanda Amata alikuwa katikati ya wote, wakaingia na kupita mapokezi kisha kuingia upande mwingine na kuchukua lifti kushuka ghorofa moja chini, walipotoka walikaribishwa na maandishi makubwa ya kuwakawaka yaliyosomeka, Safari Park Casino, casino ya kisasa iliyojengwa chini ya ardhi katika hotel hiyo, mlangoni walisimama wazaume wawili waliovalia suti nyeusi na kuonekana wameshiba kimazoezi, walikuwa wamesimama mithili ya sanamu ya bismini.
“Clean!” mmoja wa wale waliomtangulia Amata alitamka neon hilo akimaanisha hakuna shida, mara mlango wa kioo ukafunguka na wote wakaingia ndani. Taa za rangi mbali mbali ziliujaza ukumbi huo ambao ulionekana kuwa na shughuli nyingi, wanaocheza kamali walikuwapo, wacheza uchi nao walilipamba jukwaa wakicheza miziki yao michafu, waliokuwa wakinyonyana ndimi hadharani nao hawakukosa, wale waliokana jinsia zo hawakuwa mbali, ilimradi tu dhambi zote zilihifadhiwa ndani ya casino hilo.
“Huku tafadhali,” Amata alielekezwa ngazi ndefu zilizokuwa zikipanda juu, akazifuata bila ubishi mpaka juu, pale wale wasindikizaji wakamuacha na kupokelewa na wengine kisha akaingizwa ndani ya chumba safi na nadhifu kilichoja samani za gharama ya hali ya juu, mbele yake kulikuwa na mtu mnene amaye alisimama na kuja kumlaki kwa bashasha, “Oooh Kamnda Amata, karibu sana, nisingefurahi kama nisingeonana nawe leo hii, karibu sana,” Bill alimkaribisha Amata na kumuongoza kitini, kisha akampatia glass yenye kinywaji na kuketi katika mtindo wa kutazamana.

§§§§§

Akiwa kwa mwendo wa miguu huku akipiga mruzi usiku huo, Melchior Ndege alikuwa akipita mbele ya hotel hiyo ya Safari Park, mara akapitwa na gari moja ya kupendeza inayovutia macho, akasimama kuitazama gari ile, Cardillac ya bluu nyeusi, iliyokwenda na kuegeshwa kwa utulivu. Lakini alipata mshtuko baada ya kuwaona wale walioshuka kutoka garini, aliwatazama kwa makini na kuoamua kubadili uelekeo wa safari yake. Melchior aliyaamini macho yake yaliyomwambia kuwa umuonaye ndiye Kamanda Amata, ‘Shiiit, amefika lini?’ alijiuliza na kusukuti kwa sekunde chache kabla kuruhusu miguu yake kuamriwa na ubongo juu ya lile linalopaswa kutendwa kwa wakati huo. Alipotazama vizuri, kwa macho yake ya kipelelezi akajua wazi kuwa Kamanda alikuwa kwenye hatari, akavuka kijibarabara kidogo na kuelekea mlango mkubwa wa hotel ile kisha akaingia ndani, alipofika mapokezi hakutaka kupoteza muda kwani aliwaona wapi wameingilia, akafuata, wakati wao wakifunga mlango wa lifti kuteremka chini yeye akazifuata ngazi zinazoelekea hukohuko chini. Alizuiliwa mlangoni na kupekuliwa, “Haturuhusu kuingia na silaha, weak pale unapotoka utaichukua.” Melchior alisogea kwenye meza ndogo ambayo ilikaliwa na mwanadada mrembo akaichukua bastola ya Melchior na kumpatia kadi maalum ya kumbukumbu. Akaelekea kaunta na kuketi juu ya kiti kimoja kirefu mbele ya kaunta hiyo. Akiwa anakunywa kinywaji chake taratibu huku macho yake akiwa kayaongoa kule wlikopelekwa Kamanda Amata, ambapo palitenganishwa na ukumbi mkubwa kwa vioo maalum vinavyoruhusu mtu wa ndani kuweza kuona kinachoendelea ukumbini lakini yule wa ukumbini asiweze kujua nini kinaendendele ndani ya chumba kile. Melchior akatoa miwani yake maalumu na kuipachika usoni, miwani hii ilikuwa na madini ambayo yaliweza kupenya kwenye kioo cha aina yoyote pia yaliweza kukuruhusu kuona mtu kama amebeba silaha au vipi, maana iliruhusu kuona vitu vigumu tu vilivyo mwilini mwa mtu. Alimuona Kamnda Amata akiwa na Bill wakizungumza, lakini hakuweza kujua wanazungumza nini, aliwatazama walinzi wa mlango wakuingia kule juu aliwaona wakiwa na bastola mbili kila mmoja, kisha akawatazama wafanyakazi wa casino hiyo na kuona kila mmoja alivyoipachika silaha yake, kisha akayarudisha macho yake na kuyatuliza kule aliko Kamanda Amata na kuendelea kuona kinachojiri, huku akiendelea kunywa kinywaji chake. Mara alihisi, akipapaswa kwa nyuma maeneo ya kiunoni, akageuka na kukutana macho na mwanamke mshumami, aliyejiremba akarembeka, yule mwanamka aliyeonekana ana kila dalili ya ulevi machoni mwake alizunguka na kusimama mbela ya Melchior, akamrembulia macho, Melchior hakuonesha hata kumjali kwani yeye alitaka kujua tu nini kitatokea kule ndani, “Mwanamke unataka nini? Kama kinywaji chukua uende, mi sihitaji mwanamke saa hii,” Melchior alimwambia yule mwanamke, akamnunulia kinywaji kisha kwa akapewa shukrani ya sonyo kali na refu, “Go fish!” yule mwanamke alimwambia Melchior.
§§§§§

ITAENDELEA
 
RIWAYA: MAUAJI YA KASISI
MTUNZI: richard MWAMBE

Melchior hakuonesha hata kumjali kwani yeye alitaka kujua tu nini kitatokea kule ndani, “Mwanamke unataka nini? Kama kinywaji chukua uende, mi sihitaji mwanamke saa hii,” Melchior alimwambia yule mwanamke, akamnunulia kinywaji kisha kwa akapewa shukrani ya sonyo kali na refu, “Go fish!” yule mwanamke alimwambia Melchior.

SEHEMU YA 10

“Bado mnanifuata Kamanda!” Bill alimwambia Amata huku akimimina kinywaji katika glass yake.
“Kwanza nashangaa kukuona huku, umekuja kufanya nini?” Amata alimuuliza Bill, cheko kali lilimtoka mpaka walinzi wake waligeuka kutazama ndani.
“Kamanda Amata, mimi si motto mdogo au punguani, najua ninachofanya na ninajua kila anayeingia katia wigo wangu popote pale katika pepo zote nne za dunia,” Bill aliongea kwa kujiamini, “Nina macho Kamanda, siyo haya mawili, mengi tu, na nilijuwa kuwa utakuja, maana una kiu na mimi, lakini ujue hata mimi nina kiu na wewe, umeshaniharibia mambo mengi sana,” akapiga fuinda moja kinywaji chote kikaishia tumboni mwake, akabeua kwa shibe ya kinywaji.
“Bill Van Getgand, unajua unachokizungumza? Nimekuja Nairobi, nashangaa naambiwa wewe unanihitaji, nisingeshindwa kuwararua hawa nyau wako hata kama wangekuwa hamsini, lakini kwa heshima yako nikawaacha na kuwatii kwa kuwa umeniita, na ungependa kuniona kabla ya jua la kesho kwa kuwa unajua kuwa jua la kesho sitaliona, ok, niambie ulichotaka kuniambia, unataka kunipa deal?” Kamanda Amata aliuliza.
“Oh, Kamanda, mi nipo hapa takribani wiki mbili sasa, nimekuja kibiashara, lakini nilijuwa safari yako ya kuja hapa Nairobi, nikajua wazi kuwa wewe ni mgeni wangu, ndo maana nikakukaribisha uje tustarehe, lakini nataka uniambie umekuja kufanya nini hapa Nairobi,” Bill alihoji kijanja.
“Bill, maswala yangu ya kikazi siwezi kukwambia wewe kuwa nimekuja kufanya nini, kama hilo ndilo uliloniitia basi hutopata jibu,”
“Hivi unajua kuwa upo mikononi mwangu?” Bill aliuliza
“Hata kama, lakini huwezi kunilazimisha nikwambie nimekuja kufanya nini,”
Bill akachomoa bastola yake na kumnyooshea Amata, “Utaniambia tu, maana hata nikikuua hapa hakuna atakayejua kama umekufa zaidi ya mimi na wewe mwenyewe,”
“Sitishiki na hiyo bastola ya Kirussi Bill,” Amata alijibu kijeuri, lakini kabla hajakaa vizuri, bastola ya Bill ikafyatuliwa, risasi ikapenye katikati ya paja na paja la Amata, ile sofa ikatimua vinyoya kidogo, Amata alitetemeak ka hofu, kijasho chembachemba kikamtiririka, akaona kuwa kumbe hapo hakuna usalama wala mzaha, hakuna urafiki kama upo basi ni wa mashaka.
“Usifikiri nakutania, nataka unieleze lile lililokuleta, na ukijifanya mjanja nakuua,” Bill aliongea huku akimlenga na ile bastola yake iliyoonekana wazi iko tayari muda wowote kufanya itakachoamuliwa, kabla hajajaibu, Bill alifyatua risasi kadhaa, moja katikati ya mapaja ya Amata, ya pili upande wake wa kushoto nay a tatau upande wa kulia, hali ile ilimfanya Amata aweweseke na kushindwa kujua atfanye nini, alibaki kutetemeka na kulowa jasho mwili mzima, akabana meno kwa hasira, “Nimekuja kukufuata wewe hayawani, na nakupa muda mchache tu utakuwa mikononi mwangu, Bill, ndipo dunia itakapojua kuwa roho moja dhalimu imeondoka duniani.”
“Aaaaaaa ha ha ha ha ha!” Cheko la Bill lilipasua anga la chumba kile, “Kamanda Amata, Tanzania Secret Agency, hapa mmefika, nitawaacha hapa na mi nitaondoka na kile kilichonileta. Kama hauamini hujiulizi nimejuaje kuwa huko hapa! Ujue kuwa muda wowote nitaitwaa roho yako kabla ya jua la asubuhi inayofuata.” Bill akamalaiza risala yake na kugugumia tena glass nyingine ya kinywaji kikali, “Nimefurahi kukuona!” alimalizia na kuichukua fimbo yake ya kutembelea kisha kuondoka eneo lile.
“Tutaonana tena soon,” Amata alijibu kijeuri na kunyanyuka kuelekea mlango, kabla hajatoka mlangoni alisimama na kugeuka nyuma akagongana macho na Bill, wakatazamana, “Siku yetu inakuja,” alimwambia na mara wale walinzi wakamvuta kumtoa katika mlango ule alioutumia kuingilia na kwenye ngazi alikutana na yule mwanadada aliyemjia chumbani akiwa ameweka pozi akitazama yanayoendelea ukumbini mle, wakatazamana kwa sekunde, “Unahitaji lifti yangu?” yule mwanadada alimuuliza Amata huku tayari akiongozana nae kumsindikiza, mara simu ya yule mwanadada ikaita, “Yes Boss…” aliitika, sauti ya upande wa pili ilisikika vizuri masikioni mwa Amata japo ilikuwa ndogo, “Nakupa usiku huu tu ukamstareheshe Kamanda, maana ana msongo wa mawazo, kisha urudi kabla jua alijachomoza,”
“Sawa boss, umesomeka,” alijibu kisha akamwangalia Amata, “Leo mimi na wewe mpaka kuchee, boss ameruhusu,” kisha akamshika mkono Amata na kujichnganya nae katikati ya watu ndani ya casino ile.
§§§§§

Nyimbo za masifu ya jioni zilikuwa zikirindima katika masikio ya walio jirani na eneo hilo la kanisa la Holy Family, masista waliokuwa kanisani mida hiyo walikuwa wakimalizia sala zao za jioni kabla ya kwenda kulala, kusubiri siku inayofuatia, ikiwa ni siku chache tu tangua mazishi ya Fr Gichuru yamalizike, bado mioyo yao ilikuwa imejawa na huzuni ukizingatia kwao kasisi huyo alikuwa ni mtu wa pekee sana, mwenye karama ya uponyaji ya hali ya juu, mpole, mcheshi, mwenye upendo na mcha Mungu.
Ibada ilimalizika na watawa hao wa kike walianza kutoka kuelekea nyumbani kwao, nyumba iliyo umbali wa kama mita mia mbili kutoka kanisa hilo, taa za nje zenye mwanga wa njano zilipendezesha eneo hilo, maua na miti michache ilifanya kabaridi kawe kakali kiasi. Masista wote walimalizika isipokuwa sista Rose ambaye alikuwa akimalizia kupanga vitu vya ibada itakayofuatia, kisha afunge sakristia. Haikumchukua muda alimaliza na kujianda kutoka ndani ya jengo hilo ili akaungane na wenzake. Alipoukaribia mlango tu alijikuta akibanwa na mkono wenye nguvu, uliombana barabara katika shingo yake hata akajikuta anakosa pumzi na mwili wake kukosa nguvu, mkono ule ulilegezwa kidogo na kumruhusu sista Rose kuweza kufurukuta kidogo, akataka kupiga kelele lakini alibadili mawazo ghafla baada ya kukutana na bisu kubwa na kali lililoshikwa na mkono wa mwanamke, Mellina alimkazia macho mwanamke mwenzake kana kwamba anamwangalia kuku au sungura.
“Monstrance! Onesha haraka iliko,” ilikuwa sauti ya Mellina ikimtoka huku mkononi bado kalishikilia lile jisu lake tena akiwa kalinyooshea kwa sista Rose. Ilikuwa ni wakati mgumu sana kwa mtawa yule wa kike, hakuwa na ujanja, hatari zote zilimkabiri, “Tuoneshe ilipo monstrance, tunaitaka monstrance sasa hivi, ukileta ujuaji nakutumbua na hili bisu,” Mellina alimwambia Sista Rose huku akiwa bisu lake kaliegesha nchaye katika ziwa moja la mtawa yule aliyekuwa akitetemeka kwa hofu kuu huku akilisukuma kama anayetaka kutoboa.
“Utaonesha au tukumalize kama yule kasisi wenu? Maana na ye alikuwa mbishi kama wewe” Cheetah alimuuliza kutoka nyuma yake, ndipo yule sista akajua kuwa aliyemkaba alikuwa ni mwanaume. “Ni ni nitawaonesha!” alijibu yule sista. Kisha wote kwa pamoja wakaongozana kuelekea milango mingine iliyotengenezwa vizuri kabisa ndani ya vyumba hivo vya kanisa hilo kubwa. Baada ya kupita milango kadhaa mara waliteremka ngazi kuelekea chini na huko walikuta stoo kubwa lakininzuri yenye vitu vingi tena vya thamani kubwa, sista Rose akawaonesha kabati moja kubwa lililofungwa ukutani, Mellina akaliendea na kufungua milango yake, “Waoh!” alijisemea kwa sauti ambayo kila mmoja alisiikia. “Nini Mellina?” Cheetah aliuliza, alipokaza macho yake alishuhudia monstrance kubwa ya dhahabu safi ikiwa imetulia kabatini, akamuacha yule mtawa na kuliendea kabati akainyanyua ile monstrance kwa umakini wa hali ya juu na kuiweka mikononi mwake, kisha kwenye begi walilokuja nalo maalumu kwa kazi hiyo. Sista Rose alikuwa akitetemeka sana akiangalia walivyokuwa wanaichuku bila heshima yoyote kwa chombo hicho kitakatifu.
“Tafadhali muiache hiyo monstrance,” sista Rose aliwasihi Cheetah na Mellina.
“Acha ujinga wako,” alijibiwa na mellina huku akipata pigo moja la ubapa wa kile kisu kikubwa. Sista Rose akabaki kimya huku machozi yakimtoka baada ya pigo lile, walipohakikisha wameiweka sawa katika begi lile la ngozi, Cheetah akalibeba na kumtazama sista Rose, akacheka cheko la dharau, “Kazi yetu imekwisha, kwa heri msalimie paroko,” Cheetah alimwambia sista Rose huku akimpita na kuuelekea mlango waliouingilia. Pigo moja la judo lilitua mwilini mwa sista Rose, akapepesuka, kabla hajajitambua, mellina akampa pigo lingine lililompoteza akili na kumbwaga chini kama mzigo, kisha guu nene la Mellina lilikanyaga koromeo la sista yule kwa sekunde kadhaa likimkandamiza chini na kumfanya kurusharusha miguu na mikono huku na kule na kuzimika. Ilikuwa tabu kuujua mlango waliongilia, kila walipoufungua huu walijikuta eneo lingine kabisa, walipojaribu huu hali ilikuwa ileile, Cheetah alionekana kuchanganyikiwa maana alipoingia aliona milango michache lakini sasa anaona milango mingi kuliko ile ya kwanza, iliwachukua dakika nyingi kuutafuta mlango ule bila mafanikio.

§§§§§

Melchior Ndege, aliendelea kupepesa macho yake maangavu ndani ya casino lile lililosheheni watu wa kila aina, muda ulivyozidi kwenda ndivyo watu walivyoongezeka ndani yake, alihakikisha hampotezi Amata machoni pake, na liona wazi jinsi alivyokuwa amegandwa na mwanadada yule. Melchior alijaribu kuvuta kumbukumbu ni wapi amekwisha wahi kumuona yule mwanadada lakini jibu hakulipata kirahisi japokuwa sura ilikuwa ikimjia.
Alimuona Kamanda Amata akiwa anakunywa kinyaji kikali huku mwanamke yule akiwa pembeni yake na akionekana kumhamasisha, mara amsike kiunoni mara ambusu mara ampapase hapa na pale, kisha aliwaona wakikokotana kutoka nje ya casino ile.
Melchior alishusha glass yake taratibu na kuiweka katia meza ya kaunta kisha akateremka kutoka katika kile kiti kirefu na kuuendea mlango wa casino kutoka nje, akachukua bastola zake pale mlangoni nakuiendea lift iliyompandisha hadi juu na kutoka mlango mkubwa wa hoteli. Katika maegesho ya magari alimuona Amata akiwa na yule mwanamke, sasa ilionekana wazi kuwa mapenzi yanachukua nafasi yake, akajifanya anapiga simu, ili kupoteza muda ajue kitachoendelea. Muda si mrefu, ikasimama gari pembeni yao, Jeep Cherokee ya kibuluu hivi, yule mwanamke akamvutia ndani Amata na gari ile ikatoweka. Melchior alitazama hapa na pale na kuona gari nyingi zilizokuwa zimeegeshwa na wamiliki wake walikuwa wakila starehe ndani ya hoteli ile, akaiendea moja wapo, Toyota Celica, akatoa funguo yake, wengi huiita Malaya, funguo inayoweza kufungua takribani lock zaidi elfu kumi za magari bila shida achana na switch zake. Alizungusha mara mbili tu mult lock zikaachia akaingia nyuma ya usukani na kulitekenya nalo likacheka, taratibu akaingia barabarani na kuifuata ile Jeep Cherokee, alikanyaga mafuta na kuhakikisha haiachi mbali gari ile, kati yake aliacha gari kama mbili hivi na kuendelea kuifuata, baada ya barabara tatu nne na vichochoro kadhaa ilianza kuuacha mji na kuchukua barabara ya kuelekea Thika, Melchior aliendelea kuwafuata na walipokaribia maeneo ya Kalimoni, akaona hapana, akaongeza mwendo na kuifikia ile Jeep, akaipita na kukaa mbele yao. Kila dereva wa ile jeep alipoijitahidi kuipita ile gari ya Ndege haikuwa rahisi, Melchior akaongeza kasi na kuiacha kama mita ishirini hivi kisha akafunga breki kali sana na ile jeep ilikuja na kuigonga ile Toyota kwa nyuma, kutoka katika ile jeep, mtu mmoja akateremka na kuifuata ile Toyota akaangalia ndani lakini hakuona dalili ya mtu, alitazama huku na kulea asione kitu, akarudi garini mwake na kuingia, alipofunga mlango tu alihisi kitu cha baridi kikigusa shingo yake, “Tulia hivyohivyo,” sauti ilimwambia, kisha Ndege akaunyoosha mkono wake na kuichomoa bastola ya yule dereva, wakati huo tayari kipigo cha haraka kilishampa usingizi wa muda yule mwanamke aliykuwa na Amata, “Toa gari barabarani, weka kando ile,” Melchior Ndege aliamuru na amri ikafuatwa, mbele kabla ya mahali alipoambiwa aiegeshe gari ile palikuwa na daraja kubwa sana la mpishano wa barabara, wao sasa walikuwa barabara ya juu, yule dereva akafanya hila kwa kugongesha ile gari katika ukingo wa daraja, ile gari ikayumba kidogo, Melchior, mle ndani ya gari akaangukia upande wa pili na kumpa nafasi yule dereva kufanya lolote, lakini kabla hajafanya hivyo, maana Melchior alimuona akichomoa bastola nyingine sehemu Fulani ya dashboard yake, kitendo bila kuchelewa, kwa kutumia miguu yake miwili alimbana kabali njema, gari iliyumba lakini Melchior hakujali, mara akasikia kishindo kikubwa, ile gari ilijipiga kwenye ukingo wa daraja, ikahamia upande wa pili ikakutana na Toyota prado na kujibamiza kisha akaangukia nje ya barabara. Kamanda Amata akiwa hajui lolote linaloendelea kutokana na usingizi mzito alioulala mara tu baada ya kuingia mle garini, alijigonga kichwa kwenye muhimo wa dirisha, akshtuka na kuanza kushangaashangaa, huku damu zikimtiririka kutoka kwenye jeraha dogo lililotokea katika kichwa chake baada ya kujigonga kule.
Melchior alitoka kwa shida kidogo katika gari ile baada ya kuvunja kioo cha mbele, kisha akamsaidia Kamanda Amata kutoka nje, bado Kamanda alikuwa hajarudiwa na akili sawasawa alikuwa kama zezeta hivi, Melchior akamshika mkono na kutembea nae kuelekea pale alipoiacha ile gari alioichukua kule hotelini, aliwakuta polisi wawili akiitazama ile gari huku wakiwa na wanaandikaandika vitu Fulani wakisaidiwa na taa za barabarani. Melchior aliufungua mlango wa mbele na kumtumbukiza Kamanda kiti cha kushoto kisha yeye akazunguka kiti cha kulia, “Halo, vipi, mbona unakuwa kama hauheshimu mamlaka?” mmoja wa wale askari akauliza, Melchior akawasha gari huku akimwangalia yule askari, “Nenda pale karibu na njia panda utakuta ajali ya gari aina ya Jeep Cherokee, hiyo ndiyo ukaipime, hii sio ajali,” kisha akaondoka kwa kasi mpaka kwenye mzunguko mkubwa na kuhama njia kuchukua njia inayorudi mjini, kwa mwendo uleule wa kasi ya ajabu.

AGA KHAN HOSPITALI
Parkland Avenue-Nairobi

MELCHIOR ndege aliegesha gari katika lango la hospitali ile na daktari mmoja alikuwa pale tayari na kitannda cha magurudumu, akisaidiwa na manesi wawilli walimlaza kamnda Amata na kuingia naye ndani, moja kwa moja wakamuweka kitandani kwemye chumba cha peke yake, wodi maalumu, daktari alipomuangalia vizuri aliona wazi hali yake si nzuri, hivyo akaamuru awekewe drip ya glucose ili iweze kumrejeshea nguvu japo kidogo. Wale wauguzi wakafanya hivyo lakini pia walicheki mapigo ya moyo na kuweka kumbukumnbu zake kati faili maalumu lililokuwa pale, Kamanda Amata alilala kimya akiwa hajitambui tena, jeraha lake lilishonwa na kuwekwa katika hali ya usafi.
Melchior Ndege, alipekuwa kwenye mifuko ya Amata lakini hakuona chochote, akabaki kumtazama pale kitandani alipozungukwa na mitambo tiba ya kisasa ambayo ilikuwa inaangalia mwenendo wa mwili kwa ujumla kama mapigo ya moyo na mambo mengine. Melchior Ndege alitoka nje na kufunga mlango mkubwa kioo kisha kurudi ofisini kwa daktari.
“Rafiki yako inaonekana amepewa sumu kali sana ambayo imempotezea fahamu na kuathiri mfumo wa urendaji kazi wa mwili wake, itamchukua masaa mengi sana kuirudia hali yake ya kawaida,” Daktari alimweleza Melchior Ndege, haikuwa rahisi kulielewa swala hilo, lakini aligundua kuwa Bill alidhamiria kummaliza Amata. Akashusa pumzi ndefu na kumtazama daktari.
“Huyu ni mtu wetu, katoka Tanzania,” akamwambia kwa kifupi, daktari akatikisa kichwa kuashiria kuwa ameelewa, kisha Melchior akampa habari nzima jinsi alivyomuona kuanzia pale hotel ya Safari park mpaka kule kwenye ajali.
Hasira zilizidi kumtawala Melchior na moyoni akaapa lazima Bill alipe yote ayafanyayo, hapo akagundua kuwa Bill ni jasusi la kimataifa lenye mbinu za kuua bila kutumia silaha na kuwafanya watu kutojua ni nini chanzo cha kifo. Aliagana na daktari na kuomba kurudi baadaye kidogo lakini apewe taarifa ya kila kinachoendelea.
Safari yake na gari ile ya kukodi iliishia katika mtaa wa Riara, akashuka na kuilipa tax hiyo kisha akaliendea geti kubwa jeusi lilofungwa sawia, akabofya kengele, mara likafunguka naye akajitoma ndani, “Karibu sana kijana!” alikaribishwa na sauti ya boss wake bwana Shikuku, “Vipi mbona usiku sana ?” akaongeza swali, ndipo Melchior alipoinua mkono wake kuitazama ile saa yake iliyomuonesha kuwa ni saa nane kasoro robo usiku. Wakaingia sebuleni na kuzungumza machache, Melchior alimpa habari yote ya Kamanda Amata. Shikuku alisikitishwa sana na habari hiyo, kisha wote wawili usiku huo wakatoka na kuelekea kule hospitali kumuona Kamanda, walimkuta katika hali ileile isipokuwa sasa ilikuwa mbaya zaidi kwani mapigo ua moyo yalishuka sana, hata daktari alikuwa na wasi wasi juu ya hilo maana hayakuonekana kupata unafuu wowote.
“Shiiiittt!!!!” aliinua simu yake na kubofya namba Fulani kisha kusikiliza sauti ya upande wa pili, baada ya mazungumzo mafupi aliikata na kuiweka mezani, akajishika kichwa kwa masikitiko, mara simu yake ikapata uhai na kujitikisatikisa pale mezani, aliinyakuwa na kusikiliza, “Yeah… ndiyo… ee. Fanyeni haraka tafadhali,” akakata simu na kuitia mfukoni.
“Vipi, ni nani hao?” Ndge alimuuliza bosi wake.
“Nilikuwa nawapa taarifa juu ya mtu wao huko Tanzania, ili wajue ni nini watafanya, sasa wamesema wayanijibu haraka iwezekanavyo,” Shikuku alijibu.
“Hivi Bill amedhamiria haswa kufanya mauaji ya mtindo huu sivyo?” Ndege alimuuliza Shikuku.
“Yule ni shetani, sio binadamu, hivi umesema yuko wapi saa hii?” Shikuku aliuliza swali kwa Ndege.
“Niliwaacha, Safari Park casino, lakini sidhani kama bado wako hapo, ngoja tufatilie wale watu wa kwenye ile gari ili tujue kwa undani juu ya sakata hili na nini kipo nyuma yake, simpendi kabisa Bill, na aombe Kamnda Amata asiamke milele, lakini Shikuku nakuhakikishia, Kamanda akiamka atavunja mpaka miiko ya kazi yake ili amtafute huyu hayawani na kwanza atamuua kisha amuulize maswali anayoyataka,” melchior Ndege aliongea kwa hasira na kutoka nje ya chumba cha daktari.
Mkono wa bwana Shikuku ulimshika bega Melchior Ndege pale alipokuwa ameegemea ukuta akiwa amewaka hasira zilizojaa uchungu.
“Malchior, punguza jazba, pamoja na FBI kuwa hapa, isiturudishe nyuma, ingia kazini, mimi nakuamuru, kama kuna swali mi nitajibu; Kamanda atapona tu, najua walimuwahi katika namna ambayo hakuitegemea,” yalikuwa ni maneno ya Shikuku kwa Melchior, akageuka kumtazama mtu huyo mwenye mwili mkubwa, mkuu wa idara ya usalama wa Taifa hapo Kenya, Melchior alitabasamu kwa bashasha baada ya kuambiwa ‘Ingia kazini’, alitoka pale alipo na kuelekea tena chumba cha daktari kisha akaingia kumuona Kamanda, alimutoa alama ya saluti ya heshima, na kumuhakikishia Kamnda kuwa sasa analipiza kisasi kwa ajili yake, kishapo akatoka nje na kuagana na Shikuku.

DAR ES SALAAM
Saa 9:15 Usiku

KELELE za simu ya mezani ya Madam S ilipiga kelele usiku huo, mlio wa dharula ulimshtua kutoka katika usingizi mzito, “Aaaa nini tena saa hizi?” aliongea kwa sauti ya hasira na kuinyakua ile simu masikioni mwake, “Hallo nini saa hii?” aliipokea na kutupa swali hilo; huku akisikiliza sauti ya upande wa pili, “Madam, kuna taarifa kutoka Nairobi kuhusu Kamanda Amata, hali yake ni mbaya sana yuko kufani,” sauti hiyo iliongea kwa upole, ilikuwa ni simu kutoka ofisi ya usalama wa Taifa ikimpa taarifa hiyo Madam, mkuu wa kitengo maalum chenye watu wachache makini wanaofanya kazi za umakini kwa umakini wa kimakini. Aliishika ile simu bila kuongea. “Unasemaje?” akauliza, akajibiwa tena jibu lilelile. Madam S alishikwa na kigugumizi, midomo ilimchezacheza, hakuamini anachoambiwa, ni jana tu mchana alipoagana na Kamanda wake pale JNIA na kumpa usia wa nguvu, Madam alibaki kimya na simu ikiwa hewani nab ado hajaishusha kutoka sikioni mwake, akashusha pumzi kisha akafungua kinywa chake, “OK, asante kwa taarifa, fanya kila kinachowezekana Kamanda afike hapa mara moja,” akakata simu na kurudisha mkono wake mahali pake, “Uuuuhhhhh!!!!” akashusha pumzi nzito kwa mara nyingine, akajilaza kitandani kwake huku mawazo lukuki yakiwa yamemtawala kichwani mwake. Akafikiri la kufanya na kumpigia daktari wao pale Muhimbili, ushauri aliopewa aliuona una maana sana, yule daktari alimshauri ikodiwe ndege ya haraka kutoka Nairobi imlete Dar, badala ya kukodi kutoka Dar. Utaratibu ukaandaliwa haraka kwa ushirikiano na Bwana Shikuku kule Kenya. Usingizi haukuja tena kwa Madam S, akaifungua kompyuta yake ya kazini ambayo imeunganishwa moja kwa moja katika kitanda chake, alipojaribu kuingiza password yake, ikagoma, haikufuka, akajaribu tena na tena, wapi. Alipoona imeshindikana, akampigia simu Chiba, mtaalamu wa ICT wa kitengo chao, naye akajaribu kuifungua lakini ikawa ngumu, akatumia mbinu zote kuitafuta maana alishajua kuwa wajanja wameiiba kimtandao, na kwa maana hiyo siri zote za usalama wa Tanzania ziko hatarini kuvuja, kijasho kilimtoka Chiba, usingizi ulikatika, akiwa mezani kwake alikuwa akishindana na mtandao kuloitatua tatizo hilo huku Madam S akimuahidi kufika hapo mapema ili kujua kulikoni. Majibu yalikuja na kugundua kuwa kompyuta ya Madam S imekuwa ‘Hiked’ sehemu Fulani huko Nairobi, mchezo ukaanza kunoga, sasa mapigano ya kimtandao, Chiba hakukubali, alifanya juu chini kuinusuru, ‘Kamanda Amata wanataka kumuua na mtandao wanataka kuukamata, shiit,” alijiwazia kisha akaiacha kompyuta yake na kuelekea kwenye kabati lake, akavaa nguo haraka haraka na kuibeba ile kompyuta kisha kuchukua gari yake haraka akawahi katika ofisi ya mawasiliano ya Usalamawa Taifa, pale kuna kompyuta kubwa zaidi inayoweza kujua vizuri sana, ni wapi na ni nani aliyefanya hivyo, haikuchukua muda aliinasa, na kuifunga kabisa kwa namba ambazo mwingine asingeweza kuzifungua. Akasimama na kumtazama kijana aliyekuwa akisaidiana naye kazi hiyo, Frank Masai.
“Dah, hatujui ni kiasi gani wamepata siri zetu,” Chiba alimueleza Frank Masai aliyekuwa kasimama karibu na meza kubwa yenye screen kubwa sana ya kompyuta inayoweza kuzileta kompyuta nyingi za ulimwenguni na kutafuta kila wanachokitaka.
“Sasa Bro, cha kufanya ni kiunguza kabisa hiyo kompyuta yao waliyotumia kutu ‘hike’,” Frank alisema.
“Tutafanyaje, maana inabidi tupate namba ya BIOS,” Chiba alisema
“Ah no, siku hizi huwezi kuua kompyuta kwa kuiharibu BIOS maana technolojia imepanda kaka, Operating System za sasa zina uwezo wa kutest kila hardware na software zilizopo kati kompyuta bila kupitia kwenye BIOS, cha kufanya hapa tufuondoe taarifa zetu kisha mi nitaweka kirusi kibaya sana kwa jina la faili moja, najua kwa vyovyote watafungua tena, maana kwa sasa wanaonekana wapo offline, kisha huyo kirusi atavuruga system yote ya kompyuta yao,” Frank Masai alijibu kwa kujiamini, kijana mwenye elimu ya ICT kutoka chuo kikuu cha Dar es salaam.
“Ok, fanya hivyo wakati mi nafanya mengine,” Chiba alimalizia. Kijana Frank Masai alikaa makini kwenye laptop yake akitengeneza shetani hilo alilolipa jina TOP SECRET, kazi iliyochukuwa kama lisaa limoja hivi na kuifanikisha akiwa kachoka sana. Kisha akamwendea Chiba na kumwambia kazi tayari ili apate ruhusa ya kufanya mlipuko huo, akakubaliwa, kazi ndogo, akaingiza kile kirusi kwenye mfumo wa kompyuta ya Madam S na kukiacha hapo, wakati document zingine zote akiwa zimebanwa na Chiba kwa pin ngumu.

§§§§§

REJEA NAIROBI… kanisa la familia Takatifu…

Ilikuwa ni kazi ngumu kwa Black Cheetah na Mellina kutoka ndani ya wigo wa kanisa maana tayari sergeant Maria na koplo Kariithi walikuwa pale na wengine wanne wenye silaha, walitanda kila upande kuhakikisha majambazi hao hawatoki bila kuacha roho zao.
Gichui, aliyekua akiendesha gari siku hiyo aliwapa taarifa kwa simu kuwa jamaa wamejipanga vipi huko nje, wakamuamuru, aanzishe show kwa kupiga risasi za hewani. Naye akafanya hivyo, mlio wa risasi zile ukawafanya wale askari kuchanganyikiwa kidogo, Black Cheetah alitoka katika mlango mkubwa akiwa na lile begi na kukimbilia upande wa pili wa ukuta huo ambako ndiko waliokoingilia, huku Mellina akitambaa mwendo wa nyoka kulifuata geti kubwa akiwa na bastola yake aina ya revolver mkononi mwake.
Gichui alipiga norinda na kutimua vumbi liliwachanganya Mellina na Kariithi ambao walikuwa tayari kujibu mashambulizi, Sargeant Mellina alijitupa chini na kubingirika kwa usatadi mpaka kwenye ukuta wa wigo wa kanisa hilo huku akishuhudia vijana wake wakijiweka tayari, “Freeze!!!!!!” sauti ya askari mmoja lisikika upande wa pili, Kariithi bado alikuwa akijaribu kuona afanye nini, akajitoa na kukimbilia upande wa sauti ile ilipotokea, akiwa anakata kona ya ule ukuta alisikia mlio wa risasi na kushuhudia mwili wa yule askari ukijibwaga chini kama kiroba, “Shiittt!” akng’aka kwa hasira, alimuona Cheetah, aliyeifanya kazi hiyo akiishia gizani, akajaribu kulenga na kufyatua risasi mbili lakini hakumpata, mara ile gari yao ilipita kwa kasi na kuelekea upande ule alipo Cheetah, haikuhitaji kusimama, kawani Cheeta alirusha begi ndani ya gari na kujirusha kupitia dirishani, lakini kabla hajamalizi miguu risasi moja ilipita katikati ya mguu wake na kufumua mifupa ya ugoko, Gichui aliizungusha gari kwa ustadi na kumfanya Cheetah kutumbukia ndani, “Aaaaaaaaiiiiggggghhhhhh!!!!” ulikuwa ukelele wa maumivu kutoka kwa Cheetah.
“Vipi brother?” Gichui aliuliza huku akiizungusha tena ile gari na kumgonga askari mwingine, sasa alikuwa akilielekea geti kuu la kanisa lile.
“They have shot me, bastards!” wamenipiga wanaharamu alimwambia Gichui, huku akiiweka tayari bastola yake. Sergeant Maria akiwa pale chini aliilenga sawia ile gari na kabla hajapiga risasi alihisi kama kitu kimenguka pale alipolala kwa nyuma yake alipogeuka aliona mwanamke kibonge akitua juu ardhi kavu na bastola mkononi, akiwa pale chini alijigeuza na kupiga mtama mmoja maridadi, Mellina alilipokea pigo hilo na kubwagwa chini, alijitahidi kujiinua kisarakasi lakini kabla hajawa wima mtama mwingine wa Mellina ulimrudisha chini na kumfanya hoi pale ardhini, sasa alishindwa kujiiunua. Bastola ya Mellina ilicheua na risasi ikapita mililmita chache kwenye uso wa Maria aliyekuwa pale chini, teke moja kali la afande Maria lilipeperusha bastola ile kutoka mikono ya Mellina ikapaa juu, kisha aliushusha mguu wake na kuutuza juu ya uso wa Mellina.
Koplo Kariithi alijitoa mhanga na kucukua ile SMG ya askari ambaye aliku marehemu, kuilenga gari ya Gichui, ‘nice shot’ risasi moja alipiga tairi ya nyuma na kuipotezea muelekeo ile gari, ikayumba na kuyumba lakini ikakaa tena barabarani, risasi ya pili kutoka kwa Kariithi ikakishusha kioo cha nyuma na bila kukosea ikafumua kisogo cha Gichui na ile gari ikayumba myumbo mkuu na kugonga mti. Wakati Kariithi akiifuta, ghafla nyuma yake kulitokea gari aina ya BMW kwa kasi ya ajabu ikafunga breki kali karibu kabisa na ule mti ilipogonga ile gari ya Gichui, kwa haraka watu wawili walishuka na kuifungua milango wakamtoa Cheetah na kulibeba begi kisha kurudi ndani, ile gari nayo ikazungushwa kwa mtindo wa U turn na risasi moja iliyotoka ndani ya gari ile ilimpata koplo kariithi mkononi, na ukelele wa maumivu, ulimchanganya sergeant Maria, akamsahau Mellina na kumkimbilia Kariithi, “Soldier!!!” Askari, sergeant Maria aliita kwa sauti na askari wote wakaja eneo hilo na kumbeba mwenzao wakimpakia kwenye gari, wengine wakabaki kufanya utaratibu wa kumuondoa Gichui ambaye alikuwa hana maisha tena na kichwa chake kikiwa kimevurugika kwa risasi ya Kariithi, moja kwa moja walimfikisha katika hospitali ya taifa ya Nairobi.

ITAENDELEA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom