Riwaya: 'hofu'

Riwaya: 'hofu'

Willy Gamba 1

JF-Expert Member
Joined
Jan 5, 2015
Posts
352
Reaction score
377
HOFU
SEHEMU YA KWANZA
PORT ELIZABETH
Ilikuwa tarehe 24 Machi, baada ya mauaji ya
kikatili ya waafrika 19, katika kitongoji cha
Langa, karibu na Vitenhage; mji ulio karibu na
ule mji wa viwanda wa Port Elizabeth, katika
Jimbo la Cape Mashariki. Mauaji hayo yalikuwa
yamefanyika tarehe 21 Machi, siku ya
kukumbuka mauaji ya kikatili kwenye mji wa
Sherpville mnamo mwaka 1960. Wakati
wazalendo 69 walipouawa kikatili. Mnamo
tarehe hiyo ya 24 Machi, huko mjini Port
Elizabeth kulifanyika mkutano katika ofisi ya
Mkuu wa Polisi mnamo saa sita usiku.
Ndani ya chumba cha mkutano huo walijumuika
watu ambao wamekuwa chanzo cha vilio na
malalamiko mengi kutoka kwa wazalendo wa
Afrika Kusini dhidi ya makaburu. Katika mkutano
huo alikuwemo waziri wa sheria na usalama wa
makaburu, Kamishna wa Polisi, Mkurugenzi wa
shirika la Ujasusi la makaburu na Kamanda wa
kikosi cha Jeshi kiitwacho 'KULFUT'yaani
'Gongo la Chuma' wote hao walikuwa ni
makaburu. Lakini vile vile mkutano huo
ulihudhuliwa na watu weusi ambao walikuwa
wameitwa haraka haraka.
Hawa walikuwa wamefanyiwa mipango maalumu
ya usafiri ili mladi wafike kwenye mkutano huo
muhimu. Walikuwa wamesafiri kwa kutumia
ndege ya Jeshi la Anga la makaburu. Weusi
hawa walikuwa ni Mkuu wa Magaidi wa UNITA,
wenye kupinga Serikali ya Angola, Mkuu wa
Magaidi wa MNR wenye kupinga Serikali ya
Msumbiji na Mkuu wa Magaidi wa LLA wenye
kupinga Serikali ya Lesotho, kwa kifupi tu ni
kwamba, Magaidi wote hawa ni vibaraka wa
Serikali ya Makaburu na ilikuwa ni serikali ya
makaburu iliyowagharamia kufanya ujahili dhidi
ya nchi zilizo mstari wa mbele katika Ukombozi
wa Afrika Kusini, ili kuzizorotesha kisiasa na
kiuchumi kwa nia ya kuziangusha hatimaye.
Waziri wa sheria, ambaye alikuwa Mwenyekiti
wa mkutano huo, alianza kwa kusema;
"Kwanza lazima nitoe shukrani zangu kwa nyinyi
wote kuweza kufika hapa kwa muda uliopangwa,
shukrani zangu za dhati ziwaendee nyinyi
wageni wetu ambao mmetoka nje ya nchi hii.
Pili tumeitana hapa usiku wa manane
kuzungumzia suala muhimu sana. Ningependa
tufanye na kumaliza mazungumzo yetu usiku
huu ili muweze kuondoka kabla
hapajapambazuka, kwani shughuli hii ni ya siri
sana. Mimi nikiwa mwana siasa nitazungumza
tu kwa ujumla kuhusu nia ya mkutano. Halafu
nitawaachia wataalamu wa utekelezaji walio
hapa kuchambua vipengele vinavyohusika kwa
undani zaidi".
"Nafikiri nyote mnaelewa kwamba kumekuwa na
wimbi la maasi la waafrika katika nchi nzima ya
Afrika Kusini. Wimbo hili, kwa kiasi fulani
limetutia wasiwasi. Migomo imeongezeka katika
sehemu za kazi kiasi cha kutishia uchumi wa
nchi yetu. Maandamano yameongezeka kiasi cha
kutishia utulivu na amani ya wananchi. Vitendo
vya hujuma vinavyofanywa na magaidi
wanaojiita wapigania uhuru'wa Afrika Kusini
vimeongezeka kiasi cha kutishia mashirika ya
nje yenye raslimali zao humu nchini.
"Sasa Serikali imeamua kukomesha vitendo
vyote hivi. Serikali ilikuwa na nia ya kulegeza
vipengele fulani fulani katika sheria zetu kwa
manuafaa ya weusi. Lakini imegundulika kuwa
kufanya hivyo kutawafanya watu hawa kuwa
kichwa ngumu zaidi. Na kama alivyosema Rais
wetu, hakuna mtu yeyote Ulimwenguni
atakaetuzuia kulinda usalama wa nchi yetu na
watu wake wapendao amani!'. Na hapa
nasisitiza tena hatutaki mchezo.
"Ghasia hizi ambazo zimekuwa zinaendelea
zimefanya mashirika na makampuni kutoka nje
kuwa na mtazamo mpya. Yanaanza kuwa
wasiwasi juu ya uwezo wetu na pia kuelekea
kuwa na imani katika vyama vinavyodai
vinapigania uhuru. Hali hiyo siyo nzuri na ni
tishio kubwa kwetu".
"Uchumi wetu umeanza kuanguka. gharama za
maisha zimepanda kwa kadri asilimia kumi na
saba!, ukame umeathiri uzalishaji wa chakula.
Bei ya dhahabu imeanguka saba mwaka huu na
kufanya bei za vitu muhimu, kama vile Petroli,
kuongezeka kufuatana na kushuka kwa thamani
ya fedha yetu, ukilinganisha na thamani ya dola
ya kimarekani. Jumuia ya Kimataifa inapiga
kelele na kuyataka makampuni yasiweke
raslimali na vitegauchumi vyao nchini mwetu".
"Mambo yote haya yanatokana na mwamko wa
Ulimwengu dhidi ya siasa yetu ya ubaguzi. suala
la kuzungumzia ni nini kufanyike ili kulekebisha
hali hii ndio sababu leo mko hapa kutafuta
ufumbuzi. kuanzia sasa tunataka kufanya
macho ya Jumuia ya Kimataifa kuelekea
sehemu nyingine ili sisi tupate nafasi ya
kurekebisha mambo humu nchini. Macho yao
yanataka yaelekee kwenye nchi zilizo mstari wa
mbele na vile vile Namibia. Tutafanya vitendo
katika nchi hizo vitaifanya Jumuia ya Kimataifa
kushughulikia sana; ikitafuta njia za kuwasaidia
wananchi wa hizo. Wakati Jumuia ya Kimataifa
inashughulika kiasi hicho, sisi tutaanza kuwapa
fundisho hawa watu weusi wanaoleta ghasia
hapa nchini. Jumuia ya Kimataifa ikija kugeuza
macho yake kuyaelekeza kwetu. tutakuwa
tumeisha wakomesha hawa watu weusi ambao
ni wakorofi watakuwa wamenyooka kama
mpini".
"Hivyo tumeamua kuanzisha 'UTAWALA WA
HOFU' dhidi ya weusi walio humu nchini na pia
walio katika nchi zilizo mstari wa mbele kwa
ujeuri. Ni imani yangu kuwa mmenielewa na
ninawashukru tena kwa kunisikiliza. Wakuu wote
wa usalama wako hapa. watawaeleza jinsi
utekelezaji wa jukumu hili utakavyokuwa.
Ahsanteni sana".
Alipomaliza kusema hayo, Waziri wa sheria na
usalama alifunika jalada lake, kisha akasimama
na wengine wakasimama pia. Huku akiwapungia
mkono wa kwaheri, Waziri alisindikizwa na
Kamishina wa Polisi mpaka kwenye mlango.
Alifunguliwa mlango huo na kutokomea gizani.
Baada ya Kamishina wa Polisi kurudi kwenye
nafasi yake, Mkurugenzi wa shirika la Ujasusi la
Makaburu alichukua uwanja kueleza namna ya
utekelezaji wa mpango huo.
"Nafikiri nyinyi wote mmemsikiliza waziri kwa
makini. Mambo ni kama hayo na hatuna budi
kutekeleza, nyinyi wenzetu wa UNITA, MNR na
LLA tunahitaji msaadawenu kikamilifu.
Tumesaidiana mambo mengi sana. Bila sisi
kusingekuwepo na UNITA, MNR au LLA", alisema
huku akiwakazia macho viongozi wa vyama
hivyo vya magaidi.
Wote walimwemwesa huku wakionyesha kwa
vichwa vyao ishala ya kukubaliana nae.
"Kuanzia sasa misaada kwenu inaongezwa
mara dufu". Wote walishangilia kwa kupiga
makofi.
"Lakini", aliendelea Mkurugenzi wa Shirika la
Ujasusi la Makaburu, "Misaada hii haikuongezwa
bure. Kutakuwa na kazi kubwa ya kufanya.
Alinyamaza huku akiwaangalia viongozi wa
magaidi kujua kama walikuwa wanampata.
"Mmesikia kuwa tunaanzisha utawala wa hofu'
dhidi ya watu weusi waliomo humu nchini na pia
nchi zilizoko mstari wa mbele pamoja na
Namibia. Utekelezaji wa mpango huo utakuwa
kama ifuatavyo.
"Kwanza sisi tutajitangazia uhuru nchini
Namibia. Baada ya kufanya hivyo tutapambana
na SWAPO. Kama ikibidi tutauwa watu Namibia
kwani nchi ile ni lazima kuitawala. Tumeanzisha
Jeshi linaloitwa KULFUT, yaani Gongo la
Chuma'. Hili ndilo Jeshi litakalosababisha Hofu
huko Namibia na nchi fulani fulani zinazojidai
kuwa mstari wa mbele. Jeshi hili limeundwa na
Makomandoo watupu na lenye uwezo mkubwa.
Limefundishwa kwa kipindi cha miaka kumi
sehemu mbali mbali Ulimwenguni na sasa liko
tayari kabisa kutia hofu popote litakapotumwa.
Upande wetu umejiweka tayari. Baadhi ya vikosi
vya Jeshi hili vitaletwa kwenu".
Wajumbe walipiga makofi.
"UNITA", aliendelea "Kazi yenu itakuwa kutia
hofu huko Angola. Hakuna mazunguzo na
Serikali ya Angola tena. Mtapewa kila msaada
wa hali na mali. Lazima kuhakikisha kuwa
uchumi wa nchi hiyo unaanguka kabisa.
Kamanda wa KULFUT yupo hapa atapewa kikosi
cha Jeshi hilo kusaidia katika dhima hiyo,
wapiganaji wenu wasiwe na huruma, bali
kuchinja na kuua kiumbe chochote kilicho mbele
yenu. Hakikisha mnawaangamiza wale wote
wanaojiita wapigania uhuru wa Namibia. Sisi
tuko nyuma yenu kwa lolote lile litakalotokea.
Nguvu zetu mnazijuwa. Kwa hoyo hakuna
atakayechezea".
"Nyinyi MNR", alimgeukia kiongozi wa MNR,
"Kazi yenu mnaijuwa. Kama watakavyofanya
hawa watu wa UNITA. Fanyeni vurugu ndani ya
Msumbiji. Watu wapate hofu kuliko wale
walioishi wakati wa NAAzI iliyosababishwa na
Wajerumani".
Mara alimuona Kamanda wa MNR amenyoosha
kidole akitaka kuzungumza.
"Eh, unasemaje?, aliuliza kwa shauku kubwa.
"Sisi tuko tayari kabisa", alisema Kamanda wa
MNR, "Lakini lazima niseme kwamba mkataba
wenu wa Nkomati unatutatanisha. Ni mkataba
wa amani kati ya Msumbiji na Afrika Kusini.
Sasa kwetu sisi kuendeleza mapambano
inakuwa vigumu ingawa mnatusaidia. Mkataba
huo unatuathiri sana".
Mkurugenzi wa Shirika la Ujasusi la Makaburu
alijibu. "Achana na siasa. Mkataba wa Nkomati
ni siasa tu. Sahau kabisa. Tangu uwekwe saini
hakuna mtu ambaye ameutekeleza. Ndio sababu
misaada kwenu imeendelea. Kazi yenu ni kama
nilivyosema: fanya hali ya Msumbiji iwe ya hofu
tupu. Lengo la mkataba wa Nkomati ilikuwa
kuwachota akili viongozi wa serikali ya
Msumbiji. Tumegundua kwamba wanawaogopa
sana nyinyi watu wa MNR. Nyinyi ndio mlikuwa
chanzo cha mkataba huo. Walitaka amani. Sasa
kinachohitajika ni kuwatia hofu zaidi kwa vita na
si ajabu mkachukuwa madaraka. La sivyo,
angalau waje kusujudu kwetu na kutulamba
miguu. Kwa hivyo sahau kitu kama mkataba wa
nkomati".
"Nakuapia", alisema Kamanda wa MNR,
"Watakiona cha mtemakuni".
Ndipo Mkurugenzi wa shirika la Ujasusi la
Makaburu alipoendelea, "Kazi ya LLA haina
tofauti na wengine askari kutoka jeshi la KULFUT
watawasaidia kuleta vurugu na hofu kubwa huko
Lesotho na Botswana. Sisi tuachieni Zimbabwe,
Zambia na Tanzania. Vikosi vyetu maalumu vya
uhujumu katika Jeshi la KULFUT vitazionyesha
cha mtemakuni nchi hizo. Ili kuonyesha nguvu
zetu, sisi tutaanzia Tanzania. Tunataka tutie
vurugu na kuleta rindi la hofu katika nchi hiyo
dunia itashangaa. Tanzania haijawahi kupewa
fundisho kwa sababu hiyo nchi ina kiburi na ndio
shina la hawa wanaojiita wapigania uhuru".
"Bila Tanzania, hawa watu wasingetupa taabu
kiasi hiki. Nchi hiyo inawapa hifadhi watu hao
na kuwapatia mafunzo ya kijeshi. Baadae
inawapenyeza kwetu na kutupa shida,
shambulizi tutakalofanya huko Tanzania.
litawatia hofu hao wanaojiita wapigania uhuru
na kuwafanya wasambae bila mpango,
itawachukua karne nzima kuweza kujikusanya
tena. Litakuwa pigo takatifu ambalo litaiacha
dunia nzima inagwaya. Mipango ya awali juu ya
kipigo hicho iko tayari na hatuna wasiwasi".
Mkuu wa UNITA aliamusha mkono ikiwa ni
ishara yake ya kuomba kusema.
"Eh, unasemaje?". Mkurugenzi wa Shirika la
Ujasusi la Makaburu alimuuliza Mkuu wa UNITA.
"Mimi nasikia moyo wangu unakwenda mbio
kwa shauku", alisema Mkuu wa UNITA. "Kama
kweli mtaipa kipigo Tanzania mpaka ikakoma
kutamba, basi sisi kazi yetu itakuwa rahisi kama
kunywa maji. Nchi hiyo ina kiburi na ndio
inayowapa kichwa ngumu wale wanaodai
kupigania uhuru, na nchi nyingine za mstari wa
mbele. Iwapo Tanzania itashika adabu, basi
vyama vyetu vitapata ushindi wa kutawala.
Lakini napenda kukutahadhalisha kuwa nchi
hiyo ni imara sana. Mimi nimewahi kuishi huko
na ninajua kazi yenu haitakuwa rahisi".
Mara alikatizwa na Mkurugenzi.
"Usiwe na wasiwasi", Mkurugenzi alianza
kujitapa. "Hakuna nchi itakayonusurika. Na
Tanzania itakuwa ya kwanza. Nyinyi mtasikia.
Kusema kweli baada ya kipigo hicho, hao
wapigania uhuru; na pia nchi nyingine zilizo
mstari wa mbele watabaki wanagwaya".
"Ili yakutoke mashaka", alidakiza Kamanda wa
KULFUT, "Matayarisho ya kipigo hicho yalianza
siku nyingi. Jeshi la KULFUT likishikiana na
Shirika la Ujasusi hakuna wasiwasi kuhusu
kipigo hicho, nakuhakikishia kuwa Tanzania na
wenzake watakipata cha mtemakuni. Tumetumia
miaka kumi kujitayarisha na muda huo siyo
mchezo".
"Saa zimekwenda sana. Tumetumia muda
mwingi sana kuzungumzia suala hili wakati
ambapo nyie mnapaswa kuondoka kwa siri sana
kabla ya mapambazuko". Hapa Mkurugenzi
alinyamaza kidogo kisha akaendelea kusema.
"Kamanda wa KULFUT' atawapatia msaada
mnaohitaji katika kutekeleza mpango huo.
Hatuwezi kukubali kushindwa kwani hiyo ina
maana kuwa huo utakuwa ndio mwisho wetu -
kitu ambacho hakiwezekani. Lazima nipate ripoti
ya maendeleo ya mpango huu kila siku ili niweze
kuipa taarifa serikali. Kamishina wa Polisi
anasema hana wasiwasi juu ya weusi wa hapa
kwani atawatia vurumai mpaka wajute
kuzaliwa".
:Nafikiri mmesikia kuwa mwezi Februali
tuliwakamata vingozi wa vyama vya upinzani.
Hao tumewaweka kiporo na baada ya kuipa
kipigo Tanzania. Nyinyi mtasikia vurumai
tutakavyoifanya, au uongo Kamishina?".
Akionyesha majivuno, Kamishina wa Polisi
alijibu, "Watajuta kuzaliwa kwani walikuwa
wanaleta mchezo. walikuwa wamediliki
kusababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe
hapa nchini. Kitu kama hicho hakiwezi kutokea
wakati bado niko hai".
Mkurugenzi alifunga mkutano huo kwa dharura
kwa kusema, "Ahsanteni sana. Ni mategemeo
yangu kuwa mmeelewa hali halisi na hivyo
mtatekeleza itasavyo. Naamini tutakapokutana
tena kwenye mkutano kama huu hali haitakuwa
hivi, bali kusherekea ushindi dhidi ya adui. Sura
ya Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara
itabadilika kwa kupata tawala mpya".
Mkutano ulifungwa saa kumi na moja alfajiri.
ITAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA PILI
HARARE
Ilikuwa tarehe 1 Aprili, Juma moja baada ya
mkutano uliofanywa na maafisa wa Makaburu
na vikaragosi vyao mjini Port Elizabeth. Siku
hiyo kulifanyika mkutano mwingine. Mkutano
huo ulikuwa kati ya watu tofauti na wale
Makaburu, mikutano yao ilikuwa na uhusiano.
Mkutano huu ulifanyika mjini Harare, Zimbabwe,
katika ofisi za wapigania uhuru wa Afrika Kusini.
Tofauti na ule mkutano wa Makaburu uliofanyika
usiku, mkutano wa wapigania uhuru ulifanyika
mnamo saa nne hivi asubuhi. Mkutano huo
ulifanyika katika ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa
Chama cha kupigania uhuru. Waliohudhuria
mkutano huu ni yeye Mkuu wa Upelelezi,
Mkurugenzi wa Upelelezi na Serikali ya
Zimbabwe pamoja na kijana mmoja aitwae Bon
Sipele.
Huenda itakuwa kwa faida yako kama
nitakueleza kidogo juu ya kijana huyu mradi
usiniite mmbeya. Lakini kwa kuwa mimi huwa
sisengenyi, fahamu kwamba mambo
nitakayokueleza ni kweli tupu. Kijana Bon Sipele
alikuwa na umri yapata miaka ishirini na nane.
Kijana huyu alikuwa mzalendo wa Afrika Kusini
ambaye alizaliwa katika kijiji cha Soweto. Kijana
huyu alianza kujulikana kama mwana mapinduzi
akiwa bado mbichi. Alipokuwa na umri yapata
miaka kumi na tisa, yeye na wenzake baada ya
kumaliza darasa la kumi na nne walivamia mitaa
wakiwa na mawe na chupa kuupinga utawala
wa kibaguzi wa Makaburu. Serikali ilijibu kuwa
kuwauwa baadhi ya vijana hao na kuwatia ndani
wengine. Bon pamoja na wenzake walipata
bahati ya kutoroka. Huku wakisaidiwa na
wapigania uhuru, waliweza kuingia Zambia na
hatimaye Tanzania. Bon alijaa uchungu
kutokana na vitendo vya kikatili vya Makaburu.
Hivyo aliapa kuwa angejitoa mhanga kupigania
uhuru wa nchi yake.
Bon alipewa nafasi ya kwenda nje ambapo
alipata mafunzo ya kijeshi kijana huyu alipitia
mafunzo magumu huko Urusi, China, Cuba na
Korea Kasikazini. Aliporudi kutoka kwenye
mafunzo alikuwa na ujuzi wa hali ya juu.
Aliombwa kukaa katika ofisi za wapigania uhuru
zilizo Tanzania ili awe mkuu wa idara ya
uendeshaji vita. Lakini, Bon alikataa kazi hiyo
kwani alitaka kuishi katika hali halisi ya vita.
Hivyo alikwenda moja kwa moja mpaka
Msumbiji kupambana na Wareno na Makaburu
huko msituni. Baadaye aliweza kuhujumu
viwanda kadhaa, mitambo ya umeme pamoja na
Reli ndani ya Afrika Kusini. Bon aliwatia homa
Makaburu.
Vyama vya wapigania uhuru viliona Bon alikuwa
anafaa kuwa mpelelezi ili awakabiri majasusi wa
Makaburu kutokana na ujasili wake na mafunzo
aliyokuwa nayo. Baada ya muda siyo mrefu Bon
alitokea kuwa mpelelezi aliyesifika na kuogopwa
katika sehemu hii ya Kusini mwa Afrika.
Makaburu walimhala kutokana na hasara kubwa
aliyowatia. Serikali ya Afrika Kusini ilikuwa
inamtafuta bila kufanikiwa. Kijana huyu ndiye
Bon Sipele.
Tunarudi kwenye mkutano uliokuwa ukifanywa
na watu hao watatu.
Mkurugenzi wa upelelezi wa Zimbabwe ndiye
alikuwa mtu wa kwanza kutoa hoja yake.
Alisema, "Tumekusanyika hapa ili niweze
kuwaeleza ama sote kuzungumza suala muhimu.
Habari kuhusu suala hilo nimezipata kutokana
na kazi yangu, suala hili linawahusu nyinyi pia.
Ndio sababu nimeona ni vizuri niwahusishe".
Alimeza mate kulainisha koo akaendelea,
"Mnakumbuka kuwa hapa majuzi watu wetu
walifanya operesheni kwenye sehemu ya
Beitbridge katika mpaka wetu na Makaburu.
Mtakumbuka pia kuwa watu wetu waliweza
kuvunja kundi la Majasusi waliokuwa wanafanya
ujahili dhidi ya nchi yetu kutokana na amri za
Makaburu".
"Tunakumbuka", walijibu kwa pamoja.
"Katika operesheni hiyo", Mkurugenzi aliendelea,
"Tuliweza kuwakamata Majasusi ishirini. Baada
ya kuyakamata, vijana wetu kama mjuavyo
walishughulika kikamilifu. Baada ya kuhojiwa
mmoja wao alitoa taarifa ambayo imetufanya
tuwe macho. Kwa sababu hiyo nimelazimika
kuwapa habari hizi. Kutokana na ripoti niliyopata
ofisini kwangu ni kwamba, Makaburu wamebuni
mpango wa kukomesha mashambulizi dhidi yao.
Utekelezaji wa mpango huo ni kwamba
Makaburu watatoa kipigo kitakatifu ambacho
kitamaliza kabisa nguvu za wapigania uhuru
kiasi kwamba wale watakaobahatika kubaki
hawatathubutu kufanya mashambulizi dhidi yao.
Vile vile kuna mpango wa kushambulia nchi yetu
baada ya kipigo dhidi ya wapigania uhuru. Sasa
kama inavyofahamika, viongozi wa wapigania
uhuru wamesambaa katika nchi mbali mbali.
Wako kwenye nchi zilizo katika mstari wa
mbele. Vilevile wako katika nchi kadhaa za
Afrika na hata nchi rafiki za Ulaya. Hivi
tumefikiri sana juu ya hali hii lakini hatujapata
ufumbuzi. Ndio sababu imeonekana ni vizuri
tutafute ufumbuzi wote kwa pamoja".
Mkurugenzi wa upelelezi wa Zimbabwe
alipomaliza kusema chumba kikajaa ukimya.
Baada kimya kirefu kilichoambatana na
kutafakari maelezo hayo, Bon alisema,
"mtakumbuka tarehe 21 machi, siku ambayo
yalitokea mauaji ya kikatili katika kitongoji cha
Langa. Siku mbili baadaye niliweza kujipenyeza
na kuingia Afrika kusini. Wakati huo wazalendo
walikua wamepamba moto wakiwaua polisi wa
kiafrika waliomo katika jeshi la polisi makaburu.
Mimi na watu wetu walio ndani ya Afrika kusini
tuliweza kumpata mmoja wa polisi weusi
aliyekuwa anakimbia. Kabla wazalendo
hawajamfikia sisi tulimkimbiza na kumshika.
Lakini tulimfanya asituogope kwani tulimridhisha
na akaamini tulikua upande wake. Tulimchukua
na kumficha.
"Tulipomwuliza maswali alitwambia kuwa watu
weusi walikuwa hawajui kwamba Makaburu
walikuwa hawawezekani. Kwamba weupe
walishaamua kuua weusi bila kujali mpaka
ghasia ikome kabisa. Vile vile nchi zote
zinazosaidia wapigania uhuru zitakiona cha
mtema kuni kwani sasa hivi makaburu walo
jeshi liitwalo Gongo la chuma'ambalo halijawahi
kutokea duniani. Sasa hivi jeshi hilo lipo tayari
kufagia aina yeyote ya upinzani baada ya
kutayarishwa kwa muda wa miaka kumi.
Nakumbuka niliporudi nilileta ripoti hii. Sasa
ukilinganisha ripoti yangu na maelezo aliyotoa
mkurugenzi sasa hivi ni dhahiri kwamba
yanaoana. Hii inaonyesha ni kwamba ni kweli
Makaburu wanao mpango huo."
"Hata mimi naafiki kuwa yaliyosemwa ni kweli,"
alisema mkuu wa upelelezi wa wapigania uhuru.
"Lakini kitu ambacho ni lazima kukiweka
maanani ni hicho kipigo wanachotishia
watakifanya. Je kipigo hicho kitafanywa wapi;
lini na kwa namna ipi?"
Hapo mkurugenzi wa upelelezi wa Zimbabwe
aliinua kichwa akasema, Hata mimi jambo hilo
ndilo linalonipa wasiwasi maana kutokana na
maneno ya jasusi tuliyemteka, nchi zetu
zitaanza kushambuliwa mara tu baada ya kipigo
hicho. Huenda wanataka kutupumbaza ili
watushambulie wakati sisi tunasubiri watoe
kipigo kwa wapigania uhuru kwanza . Hata
hivyo ni lazima tupate ufumbuzi wa suala hili."
"Mnajua kwamba sasa hivi makaburu wana
wasiwasi mkubwa na wanatuogopa. Hivyo sasa
hivi hawana njia yeyote ile bali kutafuta njia za
kututeketeza. Uchumi wao umeanguka. Hivi juzi
juzi tu wafanyabiashara wa Uingereza waliitisha
mkutano huko mjini Leeds na kuwataka wafanya
biashara wa Afrika Kusini wajaribu kutetea haki
za wafanyakazi weusi. Waliwataka pia waibane
Serikali yao ili iwaruhusu weusi kufanya biashara
kwenye sehemu wanazoishi weupe. Vile vile
waliwataka wapinge vikali siasa ya kibaguzi ili
Waingereza waendelee kupeleka rasilimali zao
huko Afrika kusini. Hivyo makaburu wamehaha
kwani msimamo huo umewauma sana. Ni kama
mjuavyo, mtu anayehaha anaweza kufanya
jambo lolote. Hatuna budi kuwa macho kabisa
kwani hali hii imewafanya makaburu kujizatiti.
Sasa hivi wamebanwa sana ndani na nje".
"Nilikuwa nikifikiri sana sasa hivi", Bon alianza
kusema na hapo hapo wale Wakuu wawili
wakageuka kumsikiliza yeye. Walikuwa
wanajuwa kuwa Bon alikuwa kijana mwenye
akili sana na ubongo wake ulifanya kazi kama
komputa. Kila lilipotokea tatizo, Bon aliweza
kutoa ufumbuzi sahihi. Ndio sababu alihusishwa
katika mikutano ya ngazi za juu kama huu.
"Mnajuwa kuwa mwezi ujao kutafanyika
mkutano wa pekee wa wapigania uhuru wote wa
Afrika Kusini huko Tanzania, baada ya ule
uliofanyika mwaka 1969. Kuna uwezekano
kwamba Makaburu wameshapata habari na
wanajitayarisha kutushambulia huko. Maana
kama wakiweza kutekeleza tishio lao hilo la
kipigo, wakateketeza wajumbe wote kwenye
mkutano huo. Basi hivyo wanavyojigamba
itakuwa ni sahihi kabisa. Viongozi wetu wote
kutoka sehemu mbalimbali duniani watakuwapo
pamoja na watu wale wanaotuunga mkono".
Wakuu wale walimwangalia Bon na kumsikiliza
kwa makini.
"Bila hata kuzungumza zaidi, nafikiri Bon
amesema ukweli kabisa", Mkurugenzi alisema
huku akikiri rohoni kuwa kweli Bon alikuwa
kijana mwenye akili za kuzaliwa. "Hata mimi
nafikiri hilo ndilo jawabu lake, asante sana Bon.
Lakini kuna jambo moja, Tanzania iko mbali
sana. Sijui watatumia mbinu gani?", aliuliza
Mkuu wa Idara ya Upelelezi huku akiwaangalia
wale wajumbe wawili.
Akidakia haraka kujibu swali hilo, Mkurugenzi wa
Upelelezi wa Zimbabwe alisema, "Usiwachezee
hawa Makaburu. Wanao uwezo wa kufanya
jambo lolote. Wako mbali na Tanzania ndio,
lakini wakijigamba ujuwe wanao mpango
madhubuti. Hivyo ni juu yetu kujiweka tayari
kutekeleza jukumu letu".
"Jibu tumeshalipata", alipaza sauti Mkuu wa
Idara ya Upelelezi. "Hakuna haja ya kuhangaisha
vichwa vyetu zaidi. Lililobaki ni kwamba mimi
nitaitisha mkutano wa wenzangu niwaeleze
tuliyogundua. Halafu tuzungumzie nini la
kufanya kabla ya mkutano huo kuanza.
Makaburu wasije wakatuchezea kama watoto
wadogo".
"Hata mimi nafikiri hilo ndilo wazo la busara
wazee wenzangu. Tusipochukua hatua za
tahadhari tutaadhirika." Bon alijibu huku akili
yake ikiwa mbali kwani alishachekecha akilini
mwake na kuona jinsi jukumu hili lilivyokuwa
gumu na la hatari sana.
"Yote niachie mimi alirukia mkuu wa idara ya
upelelezi. Leo hii nitaitisha mkutano ili mpango
yote ya tahadhari ikamilike. Ahsanteni sana.
Mimi nitawajulisha kila hatua ambayo tutafikia.
Nitawapa habari zote kuhusu matokeo ya
mkutano. Bon usiondoke hapa mjini. Kila wakati
nataka kujua mahali utakapokuwa. Ninaweza
kukuhitaji ghafla. Kuhusu wewe ndugu
mkurugenzi, mimi nitakujulisha tarehe ya
mkutano hapo baadaye kwani ni lazima uwepo."
Mkutano ulifungwa na watu watatu hao
wakaagana.
INAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA TATU

NAIROBI

Mike Maina aliingia ofisini kwa mkubwa wake wa kazi akiwa ameshika jalada mkononi. Maina alikuwa ofisa upelelezi katika idara ya upelelezi nchini kenya. Kijana huyu alikuwa anategemewa sana na serikali ya Kenya kwa kazi yake kubwa ya kulinda usalama dhidi ya hujuma za kisiasa, kijeshi na kiuchumi. Alikwisha tokomeza mipango mingi dhidi ya serikali.

"Ehe, hebu nieleze Maina ." Mkurugenzi wa upelelezi alisema, "Ingawa nimeitwa huko Ikulu, afadhali tuzungumze kwanza ndiyo nielekee huko baadaye."

Katika kumkumbusha mkubwa wake wa kazi, Mike alitasua midomo yake na kusema, "Unakumbuka mwaka 1981 wakati mamluki, wakiongozwa na Michael Hoare, walipojaribu kuiangusha serikali ya visiwa vya Shelisheli; halafu wakashindwa?"

"Ndivyo, kwani vipi? Wanataka kuishambulia Shelisheli tena?"

"Hapana. Unakumbuka serikali ya Shelisheli iliilaumu serikali ya Kenya kwa kuhusika; na serikali yetu ikakanusha vikali madai hayo? Unakumbuka serikali hata hivyo, ilituamuru tuchunguze suala hilo. Unakumbuka kuwa mimi ulinipa kazi hiyo?".

"Nakumbuka sana, mike."

Ripoti yangu ilionyesha kwamba, ingawa serikali haikuhusika, kuna watu binafsi au hata wakazi tu waliohusika. Kutokana na ushahidi tulioupata watu wengine wenye heshima wamepoteza kazi zao. Wakazi wengine hata wamefukuzwa nchini."

"Nakumbuka."

"Wakati wa upelelezi wetu kuna mtu ambaye tulimshuku sana. Lakini kutokana na kukosa ushahidi thabiti, hakuchukuliwa hatua. Hata hivyo jalada lake lilibaki wazi. Niliweka kijana kuchunguza mienendo yake. Vile vile nilikuwa nimemwagiza achimbe historia ya maisha yake toka kuzaliwa kwake mpaka hivi leo. Mtu huyu anaitwa Peter Gerrit. Yeye ni mfanya biashara. Anayo kampuni ya kuhudumia watalii ijulikanayo kama Kinyonga Tours and Safaris."

"Lo, jina lenyewe linasisimua," alisema kwa mzaha mkurugenzi.

"Sasa jana huyu kijana wetu aliniletea ripoti ambayo ilinifanya niwe na wasiwasi mkubwa kiasi kwamba lazima nikueleze. Kwa muda wote huu kijana wetu alikuwa anampeleleza mtu huyu."

"Mtu huyu anajulikana katika idara ya uhamiaji kama Mjerumani. Vile vile Idara ya uhamiaji inayo taarifa kwamba biashara hii ya kuhudumia watalii aliianza huko huko Ujerumani. Baadae aliamua kuja kuianzisha hapa nchini Kenya. Hayo tu ndiyo wanayoyafahamu maafisa wa Uhamiaji. Lakini sisi kitu kinachotugutua ni kwamba siku ambayo askari wa kukodiwa walipovamia Visiwa vya Shelisheli, huyu Peter alikuwapo. Na wakati askari hao walipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Victoria. Maana ripoti inasema Peter alikuwa uwanjani hapo. Ni baada tu ya kugutushwa na mapigano yaliyotokea pale wakati Peter alipojisalimisha kwa majeshi ya usalama ya shelisheli.

"Wakati wa kuhojiwa Peter alieleza kwamba alikuwa hapo uwanjani kusindikiza rafiki zake waliokuwa kwenye ndege ya shirika la ndege la India ambayo ilitekwa nyara. Askari wa Shelisheli walipoangalia pasipoti yake na kuona kuwa yeye ni mkazi wa Kenya na mfayabiashara ya utalii walimwachia mara moja. Wakati wa uchunguzi wetu tulipata fununu kuwa huyu Peter alikuwa kwenye uwanja wa ndege kwa nia ya kuwapokea askari wa kukodiwa. Lakini kwa kuwa tulikosa ushahidi wa kutosha, hatukuweza kumchukulia hatua, bali tulibaki tunamtuhumu tu. Wewe unajua tena jinsi mahakama zetu pamoja na serikali vinavyotaka haki itekelezwe. Heri kumwachia huru mhalifu kuliko kumwadhibu yule asiye na hatia.

"Sasa katika uchunguzi uliofanywa na kijana huyu kwa muda wa miaka yote hii. umegundua mambo yenye kututia wasiwasi. Kwanza kijana wetu amegundua kwamba Peter hakuzaliwa Ujerumani, bali yeye ni mzaliwa wa Afrika kusini. Ila mjomba wake alikuwa anaishi Ujerumani. Ndiye huyo huyo aliyemchukua Peter na kumpeleka huko. Aliishi na kukulia huko ambako alipata masomo. Alipofikia umri wa miaka ishirini alirudi Afrika kusini katika mji wa kwao wa Pietermaritzburg. Inasemekana aliisha fanya kazi kwa Michael Hoare kama askari wa kukodiwa. Baada ya hapo alipotea na kisha akaibuka huko Ujerumani. Wakati huo mjomba wake alikuwa ameanzisha kampuni ya kuhudumia watalii ambayo alijiunga nayo. Baada ya muda kitambo, ndipo akaja Kenya. Sasa unaweza kuona kuwa kuwako kwake Shelisheli hakukuwa kwa bahati tu ila kwa sababu maalumu.

"Zaidi ya hayo, kijana wetu amegundua kitu ambacho kimetia wasiwasi na pia kunifanya mimi nifanye hima . Nikwamba kwa muda wa majuma mawili sasa kumekuwa kunakuja wazungu wanaume wawili wawili kila baada ya siku tatu. Wazungu hao wanakwenda nyumbani kwa Peter huko Red hill kwenye njia ya kwenda Limuru. Kijana wetu anahisi kwamba baada ya hao wazungu kuingia nyumbani hawatoki nje tena. Wako kama watu sita sasa. Unajua kuwa analo shamba kubwa na pia nyumba kubwa. Katika shaba hilo kuna nyumba za wafanyakazi. Sasa tunajiuliza hivi: kama kweli hawa ni wageni wa kawaida, kwa nini hawaonekani angalau kutembea tembea au hata kwenda mjini? kwa nini wasithubutu hata kuzurura hapo kwenye shamba?"

"Huenda wanatembea usiku," alipendekeza mkurugenzi.

"Kama kweli ni usiku, kwa nini usiku? aliuliza Mike.

"Nafikiri unayo sababu nzuri ya kuwa na wasiwasi. Kufuatana na maelezo yako inabidi mtu huyu apelelezwe kikamilifu zaidi kwani huenda akawa na jambo. Bali kama mtu huyu anayo mahusiano na serikali ya makaburu, yafaa apelelezwe kwa uangalifu na tahadhari zaidi. Akigundua kuwa anachunguzwa si ajabu akateleza tena kama alivyofanya hapo kwanza. Hivyo, kwa baraka zangu, nakuruhusu uendelee na kazi ya kumpeleleza ili tujuwe hasa anapanga kufanya kitu gani. Umesema kuwa kipindi fulani alikuwa haonekani na haikujulikana alikuwa wapi. Basi ni dhahili kuwa anaweza kuwa jasusi wa makaburu ambaye alikuwa mafunzoni. Hapa inawezekana kaja kikazi, kwa hiyo chunga sana mtu huyu kwani anaweza kuwa hatari|".

"Asante. Nitafanya hivyo na kisha nitakujulisha maendeleo ya kila siku".

Mike Maina alichukuwa jalada na kutoka nje ya ofisi ya mkubwa wake.

Mike alipofika ofisini kwake alimwambia Katibu Muhitasi wake amuite kijana Mwaura. Kwa muda wa miaka yote hii Mwaura ndiye alikuwa akimpeleleza Peter.

"Mwaura", Mike alisema mara Mwaura alipoingia ofisini kwake. "Nimezungumza na Mzee na tumekubaliana kwamba tuendelee na upelelezi wetu. Sasa nitakuongezea vijana wengine na ninataka ripoti juu ya maendeleo yote ya mtu huyu, kila kitu atakachofanya, na mahali atakapokwenda".

"Nashukru sana, Bosi". Mwaura alijibu. "Nafikiri ukinipa vijana wawili, kama vile Onyango na Kipukoachi, kazi itafanyika vizuri".

"Maombi yako yatatimizwa mara moja, unafanya kazi nzuri Mwaura. Kuna haja ya idara kufikiria kuongeza maslahi yako".

"Asante sana, Bosi, kazi kwanza".

"Ningependa kazi hii ianze mara moja leo hii na mhakikishe kwamba Peter hapati mwanya wa kufanya jambo lolote dhidi yetu", alisema Mike.
"Kitu ambacho nimekosea bosi ni kwamba tangu asubuhi sikuweka mtu wa kuendelea na uchunguzi juu ya maendeleo ya mtu huyu. Katika muda huu wa masaa tisa huende amefanya majambo", Mwaura alijilaumu.

"Tusililie maji yaliyomwagika. Kuanzia sasa hivi fanya kazi kama kawaida".


ITAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA TATU

II
Wakati Mike anazungumza na Mkurugenzi wa Upelelezi, ofisini mwa Peter Gerrit, katika mtaa wa Koinange, ambako ndiko yaliko Makao ya Kinyonga Tours and Safaris, simu ya siri ilikuwa ikilia. Simu hii ilikuwa inajulikana na watu wachache sana. Kila simu ilipokuwa inalia moyo wa Peter ulishtuka kidogo.

"Hallo, Peter hapa,"Peter alisema mara baada ya kuunyakua mkono wa simu na kuupachika katika sikio lake la kulia.

"Masoga hapa," upande mwingine wa simu ulimwitikia.

Masoga alikuwa ni afisa mwingine katika kurugenzi ya upelelezi. Lakini alikuwa kwenye orodha ya kulipwa na Peter Gerrit. Masoga alikuwa ni msaliti wa serikali ya wananchi wa Kenya kwa sababu ya tamaa ya pesa. Hivyo alikuwa anampa habari muhimu sana Peter ambazo alikuwa anzitumia dhidi ya wanamapinduzi wa Afrika.

Wajati Mwaura alipokuwa anamweleza Mike asubuhi ile jinsi alivyokuwa na wasiwasi juu ya wageni waliokuwa wakiingia nyumbani kwa Peter, Masoga alikuwa amepitia ofisini kwa Mike akiomba ruhusa kwenda nje. Na kwa vile hawakuwa na wasiwasi nae, Mwaura aliendelea kueleza wasiwasi wake kuhusu Peter Gerrit na wageni wake. Ndipo Mike aligeuka na kutaka kujuwa Masoga alikuwa na shida gani. Lakini Masoga alikuwa amesikia sehemu ya mwisho ya taarifa ya Mwaura juu ya wazungu walikuwa wakienda kwa Peter.

"Ehee, kuna nini?. Peter aliuliza kwa sauti kali.

Masoga alikuwa anapiga simu kwenye kibanda cha posta kando ya posta kuu, alisema, "Kuna habari ofisini kwetu kuwa unao wageni nyumbani kwako ambao wanaingia tu lakini hawatoki, idara yetu inao wasiwasi, vipi?".

Bila kujua umuhimu wa habari alizokuwa akizitoa kwa Peter, Masoga alitabasamu.

"Wana wazimu! naona sasa idara yenu haina kazi ya kufanya. Mimi sina wageni wa namna hiyo. Kama wana wasiwasi, kwanini wasije kuona?". Hivi ni nani anasema maneno hayo?", Peter aliuliza kana kwamba hajali kitu ingawa kwa kweli moyo wake ulikuwa ukidunda vibaya kwa hofu aliyokuwa nayo.

"Kijana mmoja anayeitwa Mwaura".

"Acha nae". Peter alimjibu. "Huenda anapalilia cheo".

"Huenda. Lakini mimi niliona ni vizuri kukwambia.

"Hivyo ni sawa. Lakini hakuna chochote wala usiwe na wasiwasi. Hata hivyo, asante. Njoo umuone Kanabhai. Utakuta anayo bahasha yako.

"Asante", alijibu Masoga huku anasikia raha alipojuwa kuna bahasha yake.

Baada ya Peter kuweka simu chini, alianza kufikiri. Alikuwa ameshangazwa na habari hizi kwani hakutarajia kabisa kuwa idara ya upelelezi ya Kenya ilikuwa na uwezo wa kufanya kazi kwa kiwango cha juu kiasi hicho. Ni kweli kwamba Peter alikuwa na makomandoo maarufu kumi na wawili nyumbani kwake kutoka kwenye jeshi hatari la makaburu liitwalo KULFUT. Watu hawa walikuwa wameingia nchini Kenya kwa siri na ni yeye aliyetayarisha mpango huo. walikuwa wameingia nchini Kenya kupitia Mombasa. Walisafiri kwa mashua mpaka kwenye Bandari ya Mombasa baada ya kushushwa katika Bahari ya Hindi kutoka kwenye Meli moja ya makaburu walikuwa wamefika kwenye ufuko wa Nyali walipojifanya wao ni watalii waliokuwa wakicheza tu na mashua. Peter alikuwa ametayarisha kila kitu.

Akitumia wadhifa wake kama mfanyabiashara wa kuhudumia watalii, aliweza kuwasafirisha. Awamu kwa awamu, hadi Nairobi. Aliamua kutowasafirisha kwa mkupuo ili asije kugutukiwa. Hivyo watu hawa walikuwa nchini Kenya kinyume cha sheria. Idadi yao ya watu kumi na wawili kuwa yenye nguvu sawa na kikosi kizima cha jeshi. Vile vile walikuwa wamepewa mafunzo ya kila aina kuhusu kuua. Wawili kati ya hao walikuwa NINJA. Ninja ni mtu aliyehitimu mafunzo ya pekee ya karate na kung fu huko Ujapani na Korea. Kuelezea ninja kwa kirefu inaweza kuchukua siku nzima. Hivyo ridhika na ukweli huu kwamba ninja anakuwa amejifunza zaidi ya njia elfu moja za kuua. Mtu mmoja anaweza akakiangusha kikosi kizima. Ni watu wachache katika ulimwengu huu ambao wamehitimu mafunzo hayo. Askari jeshi mia moja na silaha zao hawawezi kufua dafu kwa ninja mmoja.

Makomando hawa wa makaburu walikuwa bado kufika mwisho wa safari yao. Walikuwa wanaelekea Tanzania. Hivyo kama wangegutukiwa bado wakingali Kenya, Peter angepata matatizo makubwa kutoka kwa wafadhili wake. Hivyo ilibidi abadili mpango haraka ili aweze kuingia Tanzania ambako ndiko walikuwa wakafanye kazi. Peter aliendelea kujifikiria yeye mwenyewe. Yeye pia alikuwa ni komando katika jeshi la KULFUT kwenye kikosi cha ujasusi. Alikuwa amehitimu kila aina ya mafunzo ya upiganaji na ujasusi. Alikuwa ameletwa Kenya kusubiri wakati wake wa kufanya kazi. Alikuwa tayari kufanya kazi wakati wowote alipohitajiwa na wakubwa wake. Na wakati huo sasa ulikuwa umewadia. Wakubwa zake Peter walikuwa wameamua kufanya kazi sehemu hii ya Afrika mashariki.

Kila wakati alipofikiria mpango huu na utekelezaji wake, Peter alisisimkwa na damu. Alikuwa amefikiri sana juu ya siasa za nchi huru za afrika na kuona vyema kuzitokomeza ili Afrika kusini iweze kulitawala bara zima la Afrika. Aliamini kabisa kwamba mtu mweusi hakuwa na haki ya kujitawala. Mtu mweusi alipaswa kuwa mtumwa wa wazungu. Kwake Peter mtu mweusi alikuwa kama paka au kwani hata mbwa anayo thamani. Mara nyingine alishangaa aliposikia mtu mweusi anazungumza neno la busara. Kwake yeye kama makaburu na pia kufuatana na walivyofunzwa na kulelewa, aliona mtu mweusi kama kitu kisichokuwa na thamani yoyote. Kwa sababu hiyo Peter alisisimkwa damu alipofikiri kuwa yeye mwenyewe angeshiriki kuwaangamiza watu weusi katika nchi zao ambazo walidai ni huru.

Ili mipango yake isije ikaharibika, Peter aliinua simu akazungusha namba kazaa, kisha kusubiri kuitikiwa.

"Hallo, hapo ni Arusha ?" Peter aliuliza baada ya kuitikiwa.

"Ndiyo. Habari gani, P. G.?"

"Nzuri, F. K."

"Mipango imebadilika. Tungoje mpakani saa mbili usiku. Naamini mipango yote iko shwari mpakani."

"Nimeisha suka kila mpango kama tulivyozungumza. Hakuna tabu kamwe."

"Ahsante F. K."

"Ahsante P G."

ITAENDELEA
 
shusha kiongozi, riwaya hii niliisoma mwaka 1997 lkn napata uhonde kama vili sijawahi kuisoma vile. safi sana.
 
imetulia imeanza kunoga sasa japo mwanzoni ilinipa usingizi
 
mkuu Willy Gamba 1 tafadhali tushushie vitu kwanza tunashukuru kwa sehemu hii ya kwanza...sasa inaanza kunoga nakumbuka ni ndefu ya kutisha tu kama unayo nzima itakuwa poa sana
 
Last edited by a moderator:
HOFU
SEHEMU YA NNE

F. K

"Nyoka Tours and Safaris," Tondo aliitika kwenye simu.

"Njoo nyumbani haraka." Tondo alisikia sauti ya tajiri wake ikimwamrisha.

"Sawa mzee," aliitika kwa unyenyekevu.

Tondo aliweka simu chini na kuinuka. Bila hata kuaga alielekea kwenye gari lake ili aende kwa tajiri yake. Alipoangalia saa yake aliona inaonyesha saa nane na nusu mchana.

Chris Tondo alikuwa meneja mkuu wa kampuni ya Nyoka tours and Safaris ya mjini Arusha ambayo ilikuwa ni mali ya Mhindi mmoja. Mhindi huyo alikuwa anajulikana kwa jina la Firozali Kassam na watu wengi walimwita F. K. Yeye alikuwa tajiri sana. Alikuwa akiishi sehemu ya Them Hill ambako alijenga nyumba kubwa sana ambayo mashabiki waliita "White House" au Ikulu ya Arusha.

F. K alipendwa sana na wakazi wa Arusha kutokana na tabia yake ya kuwasaidia watu wenye uwezo mdogo wa kipesa. Alikuwa mtu mkarimu sana. Inasemekana nusu ya teksi zote za Arusha zilinunuliwa na wenyewe kwa mkopo usio na riba kutoka kwa F. K. Inasemekana kuwa alifuta madeni mengi ya watu walioonekana hawana uwezo wa kulipa. Ingawa hakuwa muumini wa dini ya kikristo, F. K alisaidia kujenga makanisa mengi ya madhehebu mbalimbali mjini Arusha.

Kwa muda mrefu F.K alikuwa mstari wa mbele katika kusaidia Chama na serikali katika mkoa huo, kufanya shughuli zake nyingi. Inasemekana. Kwa mfano alichanga pesa nyingi kwa ajili ya ujenzi wa makao makuu ya chama cha mkoa. Hivyo alipewa heshima kubwa sana na wakuu wa chama na serikali hapo mkoani Arusha. Kusema kweli kama angetokea mtu akasema kwamba F.K alikuwa ni mtu mbaya, basi angeuawa kwa kupigwa mawe hadhalani.

F.K alijulikana kama mtu wa watu, raia mwema na mpenzi wa watu wa rika zote. Alikuwa mtu maarufu na murua. Watu wote walimwelewa hivyo. Sifa zake zilizidi kuvuma kwani F. K alikuwa mfadhili, asiyebagua mtu awe mweupe au mweusi, masikini, fukala au tajiri. Watu wote mbele ya F.K walijiona sawa. Huo ulikuwa upande mmoja tu wa F.K.

Lakini F.K alikuwa na upande mwingine ambao ni watu wachache sana walioujuwa. Hata mtu kama Chris Tondo nae alimjuwa F.K juu juu tu.

F.K alikuwa mzaliwa wa Dar es Salaam, Tanzania, baba yake alikuwa mfanyabiashara maarufu sana Jijini Dar es Salaam, alikuwa na maduka makubwa matatu ya vipuri vya magari na alikuwa wakala wa makampuni mengi ya nchi za nje hapa Tanzania. Hivyo huyo mzee Kassam alikuwa tajiri sana. F.K alizaliwa mnamo mwaka 1945. Baada ya kusoma shule ya msingi hapo nchini, baba yake alimpeleka Uingereza ambako alipata elimu ya sekondari na chuo kikuu. Hii ilitokana na kwamba baba yake alikuwa na uwezo wa kumlipia F.K ada ya shule.

Mnamo mwaka 1967 serikali ya Tanzania ilitaifisha makampuni makubwa ya watu binafsi na kuyaweka katika mikono ya wananchi. Hatua hiyo ilifuatia kutangazwa kwa siasa za ujamaa na kujitegemea katika Azimio la Arusha. Mnamo mwaka 1972 serikali ilichukuwa hatua nyingine zaidi. Majumba makubwa ya watu binafsi yaliyaifishwa vilevile.

Wakati huo F.K alikuwa anasoma chuo kikuu huko Uingereza. Baba yake alimpigia simu na kumweleza mkasa uliokuwa umewapata nyumbani. Alimfahamisha kuwa nyumba zao therathini ambazo walikuwa wamejenga na nyingine kununua vile vile zilikuwa zimetaifishwa. Aliposikia vile F.K alipatwa na wazimu. Aliilaani serikali kiasi ambacho hajapata kusikia.

Siku hiyo jioni alienda kwenye baa na kuchapa mtindi barabara. Mara alisikika akiapa, "Naapa kwa jina la Mungu, kuna siku nitalipiza kisasi dhidi ya serikali ya Tanzania", Kwa bahati mbaya au nzuri katika baa ile kulikuwemo jasusi mmoja kutoka Afrika Kusini lililokuwa kwenye shughuri zake lenyewe. Liliposikia hivyo lilikumbuka kuwa shirika la ujasusi la Afrika Kusini lilikuwa linamtafuta mtu raia wa Tanzania ambaye angelifanyia kazi ya kijasusi huko.

Hivyo ndivyo alivyopatikana F.K na kuwekwa katika orodha ya kulipwa na shirika la ujasusi la Afrika Kusini. Pamoja na kulipwa ili afanye kazi ya ujasusi, F.K aliahidiwa kuwa angepewa msaada kulipiza kisasi dhidi ya serikali ya Tanzania. Inasemekana kuwa baadae alipotea kwa muda wa miaka mitatu na haikujulikana mahali alipokuwa. Lakini habari zilisema kuwa alikuwa huko Afrika Kusini akipewa mafunzo ya kijasusi kwenye makambi mbali mbali.

Aliporudi Tanzania alikuta wazazi wake wako kwenye pilikapilika za kuhama na kwenda Canada F.K alikataa kuondoka na wazazi wake na kusema kwamba yeye alikuwa mzaliwa wa Tanzania hivyo hakuwa na sababu ya kuihama nchi yake na kwenda nchi nyingine. Hivyo familia yake ilimugawia sehemu ya mali iliyobaki naye akaamua kuhamia mjini Arusha. Huko ndiko alikoanzisha kampuni yake ya kuhudumia watalii iliyojulikana kwa jina la nyoka tours and safaris.

Alichagua jina hilo kwa sababu alizozijua mwenyewe. Mabwana zake walimpa fedha nyingi ambazo alizitumia kufanya mambo niliyoyaeleza na pia kujenga white house. Kutokana na utajiri wake F.K aliweza kuisarti nchi bila mtu yeyote kumshuku. Fedha zake ziliwafumba watu macho. Nyumba hiyo iliyoitwa White House ilikuwa imejengwa kwa aina yake. Ilikuwa imejengwa kwa shabaha ya kufanya ujasusi. Nyumba hiyo ilikuwa na vyumba vingine chini ya ardhi. Kulikuwa na barabara kadhaa chini kwa chini ambazo zilitokea nje ya sengenge ilizunguka ekali kumi na mbili za kiwanja cha nyumba hiyo.

F.K alikuwa hajaowa wala kuwa na watoto. Hivyo aliishi katika nyumba hii peke yake. Watumishi wake waliishi kwenye nyumba kando kando ya jumba lake. Kwa muda wote huo F.K alifanikiwa kujenga kwa nje, akaonekana kama mbwa mwitu aliyevaa ngozi ya kondoo. Alionekana mzuri kwa nje lakini alikuwa hatari kwa ndani.

Dhamila yake kubwa ilikuwa ni kulipiza kisasi. Kwa kufanya hivyo F.K angekuwa amefanya kazi katika upande wa adui namba moja wa Afrika huru na Ulimwengu mzima kwa ujumla. Hii ndiyo ilikuwa upande wa pili wa F.K ambayo ilikuwa sura yake halisi.

Chris Tondo ambaye sasa alikuwa anaelekea Themi Hill ndiye aliyejuwa F.K hakuwa mtu mzuri kama watu wengine wa mjini Arusha walivyoamini. Yeye Tondo walikuwa wakionana na kufahamiana kiajabu. Tondo alikuwa na umri karibu sawa na F.K. Walionana mara tu baada ya Tondo kustaafishwa kutoka Jeshi la Polisi kwa manufaa ya umma. Alikuwa tayari amefikia cheo cha Kamishna Msaidizi, akiwa kati ya waafrika wa kwanza kufikia ngazi hiyo. Tondo alichukulia kustaafishwa kwake kama kitendo cha fitina na hivyo alikuwa na chiki dhidi ya serikali. Aliamini kuwa alionewa wivu kwani alikuwa na nafasi nzuri ya kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba huyu Chris Tondo alikuwa akitumia cheo chake kusaidia wahujumu uchumi. Aliwasaidia kutorosha vipusa vyote vya thamani kwa njia ya magendo. Alipostaafishwa jina lake lilitolewa kwenye magazeti ya kila siku. Kwa njia hiyo F.K ambaye alishaambiwa habari za Tondo na wale wahujumu aliowasaidia, alijuwa kuwa amepata mtu aliyekuwa akimuhitaji. F.K alijuwa Tondo hakuwa mwaminifu kwa serikali. Vile vile alishakuwa mtu mkubwa na hivyo mwenye uzito katika jeshi la polisi. Huyu ndiye mtu aliyefaa katika mpango wake waliokuwa nao F.K pamoja na wafadhili wake.

Siku moja F.K alimfuata Tondo Jijini Dar es Salaam. Alimdanganya kwamba kuna mtu amemwelekeza kwake. Alimwambia kuwa kama ingewezekana alipenda wafanye kazi pamoja kwa kuwa hakuwa na kazi. Bila kusita Tondo alikubali akaona ni bahati iliyoje. Siku hiyo Chris Tondo alimweleza jinsi alivyoichukia serikali ya Tanzania akidaiwa kuwa ilimstaafisha bila sababu ya msingi.

"Wewe tulia tu, kuna siku mtu atalipa", F.K alimhakikishia.

Baada ya kusikia maelezo ya Tondo, F.K alijuwa amempata mtu aliyekuwa akimtafuta. Tondo aliteuliwa kuwa Meneja Mkuu wa Nyoka Tours and Safaris. Kusema kweli kampuni hiyo ilikuwa ni kisingizio. Mambo ambayo F.K na Tondo walifanya kwa siri katika kuhujumu uchumi aliyejuwa ni Mungu peke yake.

Tondo alisimama na kuegesha gari nyumbani kwa F.K. F.K alifungua mlango na kumkaribisha ndani Tondo.

"Karibu ndani.

"Asante", alijibu Tondo.

"Nimekuita ghafla kwa sababu nimepata habari sasa hivi kutoka kwa yule rafiki yangu wa Nairobi kwamba wale wageni waliokuwa wafike kesho wataingia leo jioni. Kitu ninachotaka ufanye ni kwenda kubadiri mipango huko mpakani. Kama nilivyokuwa nimekueleza awali, watu hawa wataingia bila kupitia sehemu za kawaida. Wageni hao wanayo mizigo ambayo sitaki ikaguliwe wala wao wasionekane na mtu yeyote", alieleza F.K na kisha akaelekea kwenye chumba fulani. Aliporudi alikuwa amebeba pasporti kumi na mbili na bahasha moja.

"Pasporti hizi ni za hawa wageni. Nenda nazo huko mpakani kwa mtu wetu akugongee mihuri ya idara ya uhamiaji. Unajuwa ni siku nyingi hatujaangalia maslahi yake. Hivyo mpelekee hii bahasha yake".

F.K alimkabidhi Tondo hivyo vitu.

"Aidha nenda kwa Hasanali mwambia kuwa wale wageni watakwenda nyumbani kwake kwa kupitia njia ya porini mnamo saa mbili usiku. Mimi nitafika hapo kuwachukuwa mnamo saa mbili na nusu usiku, na yeey tuonane hapo. Kazi ifanyike kama kawaida Tondo".

"Sawa nitatekeleza yote kama ulivyosema".

Tondo alibeba mzigo wake akaelekea nje huku akisindikizwa na mwenyeji wake.

Wakati akielekea nyumbani kwake alifikiri kwamba wakati mwingine mambo waliyofanya yalikuwa ya ajabu kama sasa alishangaa alipoona F.K anazo pasporti za watu ambao walikuwa bado kuingia nchini hata hivyo Tondo alijuwa haikuwa juu yake kuuliza maswali. kazi yake kubwa ilikuwa utekelezaji.

Tayari alikuwa amejenga nyumba tatu. Nyumba moja ilikuwa Dar es Salaam na aliipangisha kwa Ubalozi kwa elfu hamsini kwa mwezi. Nusu ya kodi hiyo Tondo alilipwa kwa fedha za kigeni. Nyumba nyingine alikuwa amejenga nyumbani kwao Njombe ambayo kwa viwango vya huko nyumba hiyo ilikuwa ya hali ya juu. Nyumba ya tatu ni hiyo aliyojenga Arusha. Tondo alikuwa hajawahi kuoa lakini alikuwa na watoto watatu aliowapata nje ya ndoa. Watoto wake wawili wakubwa walikuwa wanasoma shule ya msingi huko London, wakati yule mdogo alikuwa anakaa na mama yake huko Njombe.

"Tangu nistaafishwe na kuungana na F.K mafanikio yangu yamekuwa ya makubwa kuliko ya mtanzania wa hali ya juu. Kweli kazi hii inanifaa shauri yao watanikoma", Tondo alijisemea kimoyomoyo.

Mara alikutana na gari lilimumulika kwa taa zake. Kabla ya kupishana alitambua ni Nyaso, hivyo akapunga mkono, Nyaso naye akampungia mkono pia.

Nyaso alikuwa ni msichana mrembo sana. Hapakuwepo msichana mwingine mjini Arusha ambaye wangeweza kushindana naye kwa urembo. Nyaso alikuwa hawala yake F.K. Watu waliojuwa penzi lao walisema kuwa Nyaso alikuwa saizi ya F.K kutokana na utajiri wake. Bali tu walishindwa kufahamu kwanini hawakuoana. Hata hivyo rafiki zake na F.K ndoa ingekuwa kinyume cha mila za wahindi. Kwa kuamua kuishi na Nyaso kama hawala kulionyesha watu unafiki wa F.K na Wahindi wengine. Waliopenda kufanya mapenzi na waafirika lakini ilikuwa mwiko kuwaoa. Wahindi walitembea na wasichana wa kiafrika na baadaye kuwatupa jalalani.

Kila wakati Tondo alipofikiria uhusiano wa watu hawa wawili aliona kuwa Nyaso hakumhitaji sana F.K. Alijuwa msichana yule alitaka pesa zake tu. Hii ilionyeswa na majibu ya mkato aliyompa F.K mara kwa mara. Lakini hata hivyo F.K alikuwa amemjengea Nyaso nyumba nzuri sana. Nyaso alikuwa haruhusiwi kwenda kwa F.K. Hivyo F.K alikuwa akienda kulala kwa Nyaso. Hata Tondo hakujuwa kwanini F.K hakupenda Nyaso aende kwake bali alilidhika alipoambiwa na F.K kwamba hiyo ingekuwa kukiuka mila za Kihindi.

"Acha mtoto wa Kitanzania amule kidogo Mhindi huyu", Tondo alijisemea.

Aliegesha gari yake nyumbani kwake halafu akajitayarisha kwa safari ya kuelekea mpakani.

ITAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA NNE

F. K


III

"Nyoka Tours and Safaris," Tondo aliitika kwenye simu.

"Njoo nyumbani haraka." Tondo alisikia sauti ya tajiri wake ikimwamrisha.

"Sawa mzee," aliitika kwa unyenyekevu.

Tondo aliweka simu chini na kuinuka. Bila hata kuaga alielekea kwenye gari lake ili aende kwa tajiri yake. Alipoangalia saa yake aliona inaonyesha saa nane na nusu mchana.

Chris Tondo alikuwa meneja mkuu wa kampuni ya Nyoka tours and Safaris ya mjini Arusha ambayo ilikuwa ni mali ya Mhindi mmoja. Mhindi huyo alikuwa anajulikana kwa jina la Firozali Kassam na watu wengi walimwita F. K. Yeye alikuwa tajiri sana. Alikuwa akiishi sehemu ya Them Hill ambako alijenga nyumba kubwa sana ambayo mashabiki waliita "White House" au Ikulu ya Arusha.

F. K alipendwa sana na wakazi wa Arusha kutokana na tabia yake ya kuwasaidia watu wenye uwezo mdogo wa kipesa. Alikuwa mtu mkarimu sana. Inasemekana nusu ya teksi zote za Arusha zilinunuliwa na wenyewe kwa mkopo usio na riba kutoka kwa F. K. Inasemekana kuwa alifuta madeni mengi ya watu walioonekana hawana uwezo wa kulipa. Ingawa hakuwa muumini wa dini ya kikristo, F. K alisaidia kujenga makanisa mengi ya madhehebu mbalimbali mjini Arusha.

Kwa muda mrefu F.K alikuwa mstari wa mbele katika kusaidia Chama na serikali katika mkoa huo, kufanya shughuli zake nyingi. Inasemekana. Kwa mfano alichanga pesa nyingi kwa ajili ya ujenzi wa makao makuu ya chama cha mkoa. Hivyo alipewa heshima kubwa sana na wakuu wa chama na serikali hapo mkoani Arusha. Kusema kweli kama angetokea mtu akasema kwamba F.K alikuwa ni mtu mbaya, basi angeuawa kwa kupigwa mawe hadhalani.

F.K alijulikana kama mtu wa watu, raia mwema na mpenzi wa watu wa rika zote. Alikuwa mtu maarufu na murua. Watu wote walimwelewa hivyo. Sifa zake zilizidi kuvuma kwani F. K alikuwa mfadhili, asiyebagua mtu awe mweupe au mweusi, masikini, fukala au tajiri. Watu wote mbele ya F.K walijiona sawa. Huo ulikuwa upande mmoja tu wa F.K.

Lakini F.K alikuwa na upande mwingine ambao ni watu wachache sana walioujuwa. Hata mtu kama Chris Tondo nae alimjuwa F.K juu juu tu.

F.K alikuwa mzaliwa wa Dar es Salaam, Tanzania, baba yake alikuwa mfanyabiashara maarufu sana Jijini Dar es Salaam, alikuwa na maduka makubwa matatu ya vipuri vya magari na alikuwa wakala wa makampuni mengi ya nchi za nje hapa Tanzania. Hivyo huyo mzee Kassam alikuwa tajiri sana. F.K alizaliwa mnamo mwaka 1945. Baada ya kusoma shule ya msingi hapo nchini, baba yake alimpeleka Uingereza ambako alipata elimu ya sekondari na chuo kikuu. Hii ilitokana na kwamba baba yake alikuwa na uwezo wa kumlipia F.K ada ya shule.

Mnamo mwaka 1967 serikali ya Tanzania ilitaifisha makampuni makubwa ya watu binafsi na kuyaweka katika mikono ya wananchi. Hatua hiyo ilifuatia kutangazwa kwa siasa za ujamaa na kujitegemea katika Azimio la Arusha. Mnamo mwaka 1972 serikali ilichukuwa hatua nyingine zaidi. Majumba makubwa ya watu binafsi yaliyaifishwa vilevile.

Wakati huo F.K alikuwa anasoma chuo kikuu huko Uingereza. Baba yake alimpigia simu na kumweleza mkasa uliokuwa umewapata nyumbani. Alimfahamisha kuwa nyumba zao therathini ambazo walikuwa wamejenga na nyingine kununua vile vile zilikuwa zimetaifishwa. Aliposikia vile F.K alipatwa na wazimu. Aliilaani serikali kiasi ambacho hajapata kusikia.

Siku hiyo jioni alienda kwenye baa na kuchapa mtindi barabara. Mara alisikika akiapa, "Naapa kwa jina la Mungu, kuna siku nitalipiza kisasi dhidi ya serikali ya Tanzania", Kwa bahati mbaya au nzuri katika baa ile kulikuwemo jasusi mmoja kutoka Afrika Kusini lililokuwa kwenye shughuri zake lenyewe. Liliposikia hivyo lilikumbuka kuwa shirika la ujasusi la Afrika Kusini lilikuwa linamtafuta mtu raia wa Tanzania ambaye angelifanyia kazi ya kijasusi huko.

Hivyo ndivyo alivyopatikana F.K na kuwekwa katika orodha ya kulipwa na shirika la ujasusi la Afrika Kusini. Pamoja na kulipwa ili afanye kazi ya ujasusi, F.K aliahidiwa kuwa angepewa msaada kulipiza kisasi dhidi ya serikali ya Tanzania. Inasemekana kuwa baadae alipotea kwa muda wa miaka mitatu na haikujulikana mahali alipokuwa. Lakini habari zilisema kuwa alikuwa huko Afrika Kusini akipewa mafunzo ya kijasusi kwenye makambi mbali mbali.

Aliporudi Tanzania alikuta wazazi wake wako kwenye pilikapilika za kuhama na kwenda Canada F.K alikataa kuondoka na wazazi wake na kusema kwamba yeye alikuwa mzaliwa wa Tanzania hivyo hakuwa na sababu ya kuihama nchi yake na kwenda nchi nyingine. Hivyo familia yake ilimugawia sehemu ya mali iliyobaki naye akaamua kuhamia mjini Arusha. Huko ndiko alikoanzisha kampuni yake ya kuhudumia watalii iliyojulikana kwa jina la nyoka tours and safaris.


Alichagua jina hilo kwa sababu alizozijua mwenyewe. Mabwana zake walimpa fedha nyingi ambazo alizitumia kufanya mambo niliyoyaeleza na pia kujenga white house. Kutokana na utajiri wake F.K aliweza kuisarti nchi bila mtu yeyote kumshuku. Fedha zake ziliwafumba watu macho. Nyumba hiyo iliyoitwa White House ilikuwa imejengwa kwa aina yake. Ilikuwa imejengwa kwa shabaha ya kufanya ujasusi. Nyumba hiyo ilikuwa na vyumba vingine chini ya ardhi. Kulikuwa na barabara kadhaa chini kwa chini ambazo zilitokea nje ya sengenge ilizunguka ekali kumi na mbili za kiwanja cha nyumba hiyo.

F.K alikuwa hajaowa wala kuwa na watoto. Hivyo aliishi katika nyumba hii peke yake. Watumishi wake waliishi kwenye nyumba kando kando ya jumba lake. Kwa muda wote huo F.K alifanikiwa kujenga kwa nje, akaonekana kama mbwa mwitu aliyevaa ngozi ya kondoo. Alionekana mzuri kwa nje lakini alikuwa hatari kwa ndani.

Dhamila yake kubwa ilikuwa ni kulipiza kisasi. Kwa kufanya hivyo F.K angekuwa amefanya kazi katika upande wa adui namba moja wa Afrika huru na Ulimwengu mzima kwa ujumla. Hii ndiyo ilikuwa upande wa pili wa F.K ambayo ilikuwa sura yake halisi.

Chris Tondo ambaye sasa alikuwa anaelekea Themi Hill ndiye aliyejuwa F.K hakuwa mtu mzuri kama watu wengine wa mjini Arusha walivyoamini. Yeye Tondo walikuwa wakionana na kufahamiana kiajabu. Tondo alikuwa na umri karibu sawa na F.K. Walionana mara tu baada ya Tondo kustaafishwa kutoka Jeshi la Polisi kwa manufaa ya umma. Alikuwa tayari amefikia cheo cha Kamishna Msaidizi, akiwa kati ya waafrika wa kwanza kufikia ngazi hiyo. Tondo alichukulia kustaafishwa kwake kama kitendo cha fitina na hivyo alikuwa na chiki dhidi ya serikali. Aliamini kuwa alionewa wivu kwani alikuwa na nafasi nzuri ya kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba huyu Chris Tondo alikuwa akitumia cheo chake kusaidia wahujumu uchumi. Aliwasaidia kutorosha vipusa vyote vya thamani kwa njia ya magendo. Alipostaafishwa jina lake lilitolewa kwenye magazeti ya kila siku. Kwa njia hiyo F.K ambaye alishaambiwa habari za Tondo na wale wahujumu aliowasaidia, alijuwa kuwa amepata mtu aliyekuwa akimuhitaji. F.K alijuwa Tondo hakuwa mwaminifu kwa serikali. Vile vile alishakuwa mtu mkubwa na hivyo mwenye uzito katika jeshi la polisi. Huyu ndiye mtu aliyefaa katika mpango wake waliokuwa nao F.K pamoja na wafadhili wake.

Siku moja F.K alimfuata Tondo Jijini Dar es Salaam. Alimdanganya kwamba kuna mtu amemwelekeza kwake. Alimwambia kuwa kama ingewezekana alipenda wafanye kazi pamoja kwa kuwa hakuwa na kazi. Bila kusita Tondo alikubali akaona ni bahati iliyoje. Siku hiyo Chris Tondo alimweleza jinsi alivyoichukia serikali ya Tanzania akidaiwa kuwa ilimstaafisha bila sababu ya msingi.

"Wewe tulia tu, kuna siku mtu atalipa", F.K alimhakikishia.

Baada ya kusikia maelezo ya Tondo, F.K alijuwa amempata mtu aliyekuwa akimtafuta. Tondo aliteuliwa kuwa Meneja Mkuu wa Nyoka Tours and Safaris. Kusema kweli kampuni hiyo ilikuwa ni kisingizio. Mambo ambayo F.K na Tondo walifanya kwa siri katika kuhujumu uchumi aliyejuwa ni Mungu peke yake.

Tondo alisimama na kuegesha gari nyumbani kwa F.K. F.K alifungua mlango na kumkaribisha ndani Tondo.

"Karibu ndani.

"Asante", alijibu Tondo.

"Nimekuita ghafla kwa sababu nimepata habari sasa hivi kutoka kwa yule rafiki yangu wa Nairobi kwamba wale wageni waliokuwa wafike kesho wataingia leo jioni. Kitu ninachotaka ufanye ni kwenda kubadiri mipango huko mpakani. Kama nilivyokuwa nimekueleza awali, watu hawa wataingia bila kupitia sehemu za kawaida. Wageni hao wanayo mizigo ambayo sitaki ikaguliwe wala wao wasionekane na mtu yeyote", alieleza F.K na kisha akaelekea kwenye chumba fulani. Aliporudi alikuwa amebeba pasporti kumi na mbili na bahasha moja.

"Pasporti hizi ni za hawa wageni. Nenda nazo huko mpakani kwa mtu wetu akugongee mihuri ya idara ya uhamiaji. Unajuwa ni siku nyingi hatujaangalia maslahi yake. Hivyo mpelekee hii bahasha yake".

F.K alimkabidhi Tondo hivyo vitu.

"Aidha nenda kwa Hasanali mwambia kuwa wale wageni watakwenda nyumbani kwake kwa kupitia njia ya porini mnamo saa mbili usiku. Mimi nitafika hapo kuwachukuwa mnamo saa mbili na nusu usiku, na yeey tuonane hapo. Kazi ifanyike kama kawaida Tondo".

"Sawa nitatekeleza yote kama ulivyosema".

Tondo alibeba mzigo wake akaelekea nje huku akisindikizwa na mwenyeji wake.

Wakati akielekea nyumbani kwake alifikiri kwamba wakati mwingine mambo waliyofanya yalikuwa ya ajabu kama sasa alishangaa alipoona F.K anazo pasporti za watu ambao walikuwa bado kuingia nchini hata hivyo Tondo alijuwa haikuwa juu yake kuuliza maswali. kazi yake kubwa ilikuwa utekelezaji.

Tayari alikuwa amejenga nyumba tatu. Nyumba moja ilikuwa Dar es Salaam na aliipangisha kwa Ubalozi kwa elfu hamsini kwa mwezi. Nusu ya kodi hiyo Tondo alilipwa kwa fedha za kigeni. Nyumba nyingine alikuwa amejenga nyumbani kwao Njombe ambayo kwa viwango vya huko nyumba hiyo ilikuwa ya hali ya juu. Nyumba ya tatu ni hiyo aliyojenga Arusha. Tondo alikuwa hajawahi kuoa lakini alikuwa na watoto watatu aliowapata nje ya ndoa. Watoto wake wawili wakubwa walikuwa wanasoma shule ya msingi huko London, wakati yule mdogo alikuwa anakaa na mama yake huko Njombe.

"Tangu nistaafishwe na kuungana na F.K mafanikio yangu yamekuwa ya makubwa kuliko ya mtanzania wa hali ya juu. Kweli kazi hii inanifaa shauri yao watanikoma", Tondo alijisemea kimoyomoyo.

Mara alikutana na gari lilimumulika kwa taa zake. Kabla ya kupishana alitambua ni Nyaso, hivyo akapunga mkono, Nyaso naye akampungia mkono pia.

Nyaso alikuwa ni msichana mrembo sana. Hapakuwepo msichana mwingine mjini Arusha ambaye wangeweza kushindana naye kwa urembo. Nyaso alikuwa hawala yake F.K. Watu waliojuwa penzi lao walisema kuwa Nyaso alikuwa saizi ya F.K kutokana na utajiri wake. Bali tu walishindwa kufahamu kwanini hawakuoana. Hata hivyo rafiki zake na F.K ndoa ingekuwa kinyume cha mila za wahindi. Kwa kuamua kuishi na Nyaso kama hawala kulionyesha watu unafiki wa F.K na Wahindi wengine. Waliopenda kufanya mapenzi na waafirika lakini ilikuwa mwiko kuwaoa. Wahindi walitembea na wasichana wa kiafrika na baadaye kuwatupa jalalani.

Kila wakati Tondo alipofikiria uhusiano wa watu hawa wawili aliona kuwa Nyaso hakumhitaji sana F.K. Alijuwa msichana yule alitaka pesa zake tu. Hii ilionyeswa na majibu ya mkato aliyompa F.K mara kwa mara. Lakini hata hivyo F.K alikuwa amemjengea Nyaso nyumba nzuri sana. Nyaso alikuwa haruhusiwi kwenda kwa F.K. Hivyo F.K alikuwa akienda kulala kwa Nyaso. Hata Tondo hakujuwa kwanini F.K hakupenda Nyaso aende kwake bali alilidhika alipoambiwa na F.K kwamba hiyo ingekuwa kukiuka mila za Kihindi.

"Acha mtoto wa Kitanzania amule kidogo Mhindi huyu", Tondo alijisemea.

Aliegesha gari yake nyumbani kwake halafu akajitayarisha kwa safari ya kuelekea mpakani.

ITAENDELEA
 
HOFU

SEHEMU YA TANO

DAR ES SALAAM

Jijini Dar es Salaam, Tanzania, siku hiyo watu walikuwa wanasherehekea Sikukuu ya Iddy El Fitri kwa hoi hoi na vifijo. Mchana huo watu walikuwa wamejaa katika hoteli ya Kunduchi. Baadhi yao walikuwa wanaogelea, wakati wengine wakitafuna na kula vitu laini. Watu wengine walikuwa wanacheza disco la mchana. Vile vile kuna wale ambao walibaki nyumbani kwa kujuwa wangekosa nafasi kwani hoteli ya Kunduchi ilikuwa imejaa kibati.

Nje ya hoteli hiyo, karibu na ufukwe, kulikuwepo na meza moja kubwa. Kwenye meza hiyo walikaa vijana wanane. Wanaume wanne na wasichana wanne hii ina maana kuwa kila mtu alikuwa na kitu chake. Wote hawa walikuwa wamefika kusherehekea Iddy pia. Walikuwa wamekaa wakibishana huku wanauchapa mtindi. Wakati huo walikuwa wanabishana juu ya siasa ya ujamaa nchini Tanzania.

"Mimi nawaambieni, hii siasa ndio inayoturudisha nyuma. Mbona kabla ya siasa hii mambo hayakuwa hivi?", Eddy aliuliza.

"Lakini nchi nyingine zina shida vile vile", alijibu Khadija, "Siyo. Sisi peke yetu".

"Shida za nchi nyingine siyo kama zetu. Ukienda nchi za jirani, utaona wana kila kitu. Kwanini?, kwa sababu hawana siasa hii, bwana. Tusidanganyane", Eddy alisisitiza.

"Hata mimi nakubaliana na wewe Eddy", Rashid aliunga mkono.

"Mimi nilikulia kijijini. kulikuwepo mabasi manne kila siku, lakini juzi nimekwenda huko sikukuta basi hata moja. nilitembea kwa miguu umbali wa kilometa arobaini. Hivi sasa sina hata hamu ya kwenda likizo nyumbani".

"Sikilizeni jamani", Esther alianza kutoa nasaha zake, "Dunia nzima ina matatizo. Mimi naamini siasa yetu ni nzuri, ila kuna mahali ambako makosa yamefanyika. Mnajuwa kila kitu kina uzuri na ubaya wake. Inawezekana siasa hii imeleta madhala ya kiuchumi, lakini tumefaidika kwa upande mwingine watanzania tumekuwa watu wanaopendana na kuheshimiana. Tunao umoja, na mtu mkubwa hamnyanyasi mdogo. Hatuna ukabila. Katika nchi nyingine mnazozungumzia, kama wewe ni mtu mdogo kama sisi wengine hapa unaonekana huna thamani hata kidogo. Achani jamani, siasa hii imetuletea hadhi na haki kwa kila kitu".

"Kwenda zako! wewe utakula au kuvaa heshima?, hii siasa inatuumiza, bwana, acheni", alijibu Rukia kwa hasira.

Mmoja wa vijana hao aliyekuwa anasikiliza maendeleo ya mabishano alimwemwesa, kisha akasema, "Rukia, usikasilike. Hapa tunazungumza tu na kila mtu anatoa mawazo yake. Hivyo poa mtoto, ngoja mimi niwaelezeni jinsi nyinyi mnavyobishana bila msingi. Mnajuwa, kama mtu anataka kubishana juu ya jambo fulani, lazima alielewe kwa undani jambo lenywe. Kila mtu hapa anasema ujamaa ndio umeleta hali ngumu. Lakini hali hiyo imesababishwa vipi na siasa hii?".

"Haya basi, tueleze kama unafahamu", Sammy alichokoza. "Wewe si unajiita mchumi?", Kwanza nyinyi mliosomea uchumi ndio mnatoa ushauri mbaya kwa wanasiasa hapa nchini".

Hapa vijana wote waliangua kicheko.

Kijana huyu alitabasamu kisha akawaashiria wanyamaze na yeye akaendelea kusema. "Azimio la Arusha lilitangazwa mnamo mwaka 1967. Kutokana na tangazo hilo, makampuni makubwa ya binafsi yalitaifishwa. Hatu hiyo ilifanya siasa ya ujamaa ianze kuonekana. Lakini utaona kwamba tangu kutaifishwa kwa makampuni hayo uchumi wa nchi uliendelea kukua kwa kiwango kilichoridhisha. Uchumi ulikua kwa asilimia tano kila mwaka, hadi mwaka 1977. Tulikuwa na fedha za kigeni kiasi cha kutuwezesha kuagiza bidhaa za kukidhi mahitaji ya taifa kwa muda wa miezi mitano. Wakati huo wote sisi tulikuwa hatupati msaada wa fedha kutoka benki ya dunia wala shirika la fedha la kimataifa".

"Hao wenzetu mnaowasema, uchumi wao wakati huo ulikuwa ukikuwa kwa asilimia mbili tu kwa mwaka. Na kukuwa kwa uchumi wao huo kulitokana tu na misaada ya fedha kutoka benki ya dunia na shirika la fedha la kimataifa. La sivyo hali yao ingekuwa mbaya zaidi kuliko sisi. Kwa muda wa miaka kumi ya kwanza ya siasa ya ujamaa, uchumi ulikuwa vizuri sana. Ni muhimu kukumbuka kuwa mnamo miaka ya 1973 - 1976 bei ya mafuta ilipanda. Vile vile kulitokea ukame. Lakini uchumi wa nchi uliendelea vizuri hii inaonyesha wazi kuwa siasa ya ujamaa haikuwa chanzo cha kuanguka kwa uchumi wa taifa letu".

"Ngoja nikukate kilimi", Sammy alimkatiza yule kijana.

"Sasa unafikiri nini kimetokea kama kweli sababu zako ni sawa sawa?".

"Nilikuwa naelekea huko", yule kijana aliendelea kusema.

"Kuanzia mwaka 1978 mambo yalikwenda mrama. Na mambo yote yalitokana na chanzo kilizho nje ya siasa ya aina yoyote. Kwanza Jumuia ya Afrika Mashariki ilivunjika. nyinyi mnajuwa kuwa hiyo ilitifanya tukose vitu kadhaa pamoja na huduma kutoka nchi wanachama wa jumuia hiyo. Bei ya mafuta iliongezeka sana kiasi cha kuathiri uwezo wetu utokanao na fedha za kigeni. Ukame pia uliathiri uchumi wetu. Zaidi ya hayo kulitokea vita kati yetu na majeshi ya uvamizi ya Nduli Iddy Amin. Mambo hayo ndiyo yalifanya uchumi wetu kuyumba. Na mbali na hayo, kumetokea hali fulani ndani kwa ndani. Ari ya mfanyakazi imedhorota".

"Hali ngumu ya maisha imewafanya maafisa wa ngazi za juu kuendekeza rushwa. Ni dhahiri kuwa kuna maamuzi yanafanywa na maafisa wa serikali bila kujali maslahi ya umma. Si ajabu kuona vibari vinatolewa kuhusu matumizi ya fedha za kigeni kwa shughuri ambazo siyo muhimu. Wakati ule ule sekta za uzalishaji kama kilimo na viwanda zinanyimwa fedha za kigeni za kununulia pembejeo na kadharika siyo sahihi, kwa kweli, kusema kwa njia ya mkato kwamba mambo haya yamesababishwa na siasa ya ujamaa. Na kama nilivyokuwa nimesema hapo awali, shirika la fedha la kimataifa na benki ya dunia havikutupatia hata senti tano. Wakati huo huo wenzetu walipewa mamilioni ya fedha za kigeni".

"Nia ya vyombo hivi ilikuwa kuhakikisha kuwa uchumi wetu unaanguka kwani vilichukia siasa ya ujamaa ambayo ni ya kimapinduzi. Walikataa kutusaidia huku wakifahamu fika kuwa matatizo yetu hayakutokana na siasa ya ujamaa. Lakini iliwafaa kutusingizia. Sasa pia na nyinyi mmejiunga na mabepari katika kulaumu badala ya kujiimarisha...".

"Mara muhudumu mmoja wa hoteli hiyo alifika hapo mezani na kuuliza, "Wewe si ndiye Willy Gamba?".

"Ndio", yule kijana alimjibu haraka muhudumu.

"Kuna simu yako mapokezi".

"Ahsante. Hebu nikasikilize simu halafu nitakuja tuendelee".

Yule kijana aliondoka na kuwaacha wameduwaa kutokana na maelezo yake mazito na yenye msingi.

Pale mapokezi alimkuta muhudumu wa kike.

"Wewe mwanamume, hapo ulipokaa una bibi na bado unatafutwa na bibi mwingine", muhudumu wa kike alimtania yule kijana. "Hutosheni mwenzetu?".

"Nifanye nini, bibie, na wakati ndio huu! lazima niutumie ujana wangu, sitaki kuujutia nikishazeeka", Willy alijibu, kisha akauchukua mkono wa simu na kuupachika kwenye sikio lake.

"Unauchapa tu mwenzetu", sauti ya Maselina ilisikika waziwazi sikioni mwa Willy Gamba.

"Unataka kuja?", Willy aliuliza.

"Unataka huyo bibi yako anikate masikio?" Sina haja ya kuharibiwa sura mwenzako.

"Sasa unasemaje?".

"Nasema hivi: niko ofisini pamoja na Chifu. Unatakiwa kama ulifikili mambo yamekunyookea na huyo msichana uliyenae, basi ulie tu. Unatakiwa sasa hivi. Umenielewa?", Maselina alisema kwa kebehi.

"Hamniachii angalau sikukuu hii nikala raha kidogo?".

"Njoo umweleze mwenyewe maneno hayo huyu babu yako, kwani mimi hiyo raha siitaki? Au kwa kuwa umenizoea unafikiri mabwana hawanitaki. Hata mimi nimechomolewa kutoka kwenye raha na pilika pilika safi za Iddy El Fitri.

"Wacha utani; nakuja sasa hivi".

Willy aliyakata mazungumzo, kisha akaiweka simu chini.

"Vipi huyo mkeo?", yule msichana wa mapokezi alimuuliza Willy mara alipokata simu.

"Afadhali ningekuwa na mke", alijibu Willy huku akielekea kwa wenzake.

Alipofika mezani ilibidi anywe pombe yake haraka ili aweze kuondoka. Jambo zuri ni kwamba vijana wote walikuwa wanafanyakazi ofisi moja na Willy ndiye alikuwa mkubwa wao wa kazi.

"Samahani", Willy aliwataka radhi vijana wenzake. "Imenilazimu nikitoe. Kuna mZee wangu ameshikwa na ugonjwa wa ngiri. Lazima nimpeleke hospitali".

Wale vijana wenzake walielewa ana maana gani ila wale wasichana masikini walidhani maneno ya Willy yalikuwa ya kweli.

"Oh pole sana," Rukia na Esther walisema kwa pamoja.

"Ahsante. Mwana, tunakwenda au unabaki? Willy alimwuliza mpenzi wake.

"Nibaki vipi?" Mwana alihamaki, "huoni kitu mtu hapa? Je, ukiniacha halafu wenzangu wakaamua kuchukua vyumba vya kulala, mimi nitafanyaje?"

"Kwangu wawili ni saizi," Sammy alitania" usiwe na wasiwasi".

"Rukia mwenzetu, mbona unayo shida."

"Maneno tu. Atawahi? kila siku jasho linamtoka," Rukia alijibu huku Mwana na Willy wakiinuka kuondoka.

ITAENDELEA
 
HOFU
SEHEMU YA TANO

DAR ES SALAAM
II

Willy Gamba alikuwa ni mpelelezi maarufu aliyekuwa akifanya kazi katika idara ya upelele ya Tanzania. Sifa zake zilitapakaa katika Bara zima la Afrika. Kutokana na ujasiri wake, watu wengi walifikiri mtu huyu alikuwa wa kubuniwa tu maanaa watu walifikiri kuwa vitendo vya Willy Gamba vilikuwa kama mchezo wa sinema.

Lakini ukweli ni kwamba huyu mtu yupo na vitendo vyake ni vya kweli tupu. Kijana huyu alikuwa amefanyakazi kubwa sana katika kusaidia harakati zinazoendeshwa na umoja wa nchi huru za Afrika. Kwa sababu hiyo yeye alijulikana katika Afrika nzima. Watu wengi waliohusika na kazi yake na wale waliobaki waliishia kusoma na kusikia habari zake bila kuamini.

Wakati akiendesha gari lake kuelekea mjini, Willy alikuwa na mawazo mengi. Maswali mengi yalimjia kichwani. Kwanini, kwa mfano, Chifu alikuwa anamhitaji wakati wa sikukuu kama hii?, lakini alihisi kulikuwako na kazi muhimu, kwani haikuwa kawaida ya Chifu kumbugudhi wakati wa mapumziko kama hayo. Chifu, kama alivyoitwa, ndiye alikuwa mkubwa wake wa kazi. Alikuwa Mkurugenzi wa upelelezi nchini Tanzania. Alikuwa Mzee wa miaka mingi katika kazi hiyo na sifa zake zilitapakaa mahali pengi, hasa kwa kumtoa kijana shupavu kama Willy.

Willy alipofika njia panda kati ya New na Old Bagamoyo ndipo mawazo yake yaliporudi kwa huyu msichana ambaye alikuwa pamoja nae kwenye gari. Msichana huyu alikuwa ameanza kusinzia. Mwana alikuwa anaishi sehemu za Mwenge, sehemu iliyo nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

"Mwana", Willy alisema. "Nitakupeleka nyumbani kwako halafu mimi nitaendelea na safari".

"Aka, babu, twende wote", Mwana alilalamika.

"Kwani huyo Mzee wako mimi siwezi kumpeleka Hospitali?".

"Wewe unajuwa Mzee anayeumwa ngili anakuwaje?, unataka kukosa radhi kwa kuangalia vitu vya wazee, nini?", Willy alimwasa huku akipinda kona kuingia barabara ya New Bagamoyo.

"Hukosi sababu wewe. si ajabu ni mwanamke mwingine unayemfuata huku ukinidanganya, maana wewe umezidi", Mwana alijibu huku machozi yanamlengalenga.

"Wacha wivu usiokuwa na msingi mama, haukusaidii kitu. Kama ningekuwa na bibi mwingine kwanini nikuchukue wewe tangu asubuhi?, na huyo bibi ana nini mpaka nikurudishe na kumfuata yeye wakati wewe kwangu ndio mipango inanyooka?", Willy aliuliza huku akicheka.

"Eh, huenda mipango yake ni zaidi. Nitajuaje mie?", MWana alisema kwa kejeli.

"Afadhali ningekuwa na bibi kama huyo. Lakini hawajaanza kuzaliwa. Nasikia wataanza kuzaliwa mwaka Elfu mbili", Willy alijibu.

"Wacha maneno mengi, utarudi?".

"Usiwe na wasiwasi. Nikimaliza shughuri na mzee nitarudi".

"Au ukaniache nyumbani kwako", Mwana aliomba kwa sauti nyororo.

"Mimi nitakuja kwako, si mzee yuko nyumbani au hunielewi?".

"Si mimi nitampikia?".

"Asante, lakini bado sijakutambulisha rasmi. Subiri mpaka nifanye hivyo kwani wazee hawa wana nyadhifa zao", Willy alisema huku akikata kona kuelekea nyumbani kwa Mwana. Walipofika Mwana alimvuta Willy na kumpa busu kali kisha kumwachia huku akisema, "Usiporudi usishangae kusikia kuwa nimekula kulolokwini kumi, wala usinilaumu".

"Nitarudi", Willy aliahidi.

Baada ya Mwana kutelemka, Willy aliondoa gari, moyoni alikuwa anashangaa jinsi wasichana walivyo. Hii ilikuwa miadi ya pili tu kati yake na Mwana. Hata hivyo msichana huyu alikuwa amekufa hasa kwa Willy. Willy aliendesha moja kwa moja hadi ofisini kwake katika mtaa wa Samora, katikati ya Jijini. Baada ta kuegesha gari alipanda ngazi. Aliongoza moja kwa moja mpaka kwenye ofisi ya Chifu. Alipofungua mlango kuingia kwa Katibu Muhtasi wa Chifu, alimkuta Maselina ameng'ang'ana na simu.

"Pole mwenzangu, nakwambia kazi hii itakuja kutuua siku moja", Maselina alimkebehi Willy.

"Inatufaa lakini. Yupo?", Willy aliuliza.

"Aende wapi!, leo kawa mzee ile mbaya, sijui nini kinamtia homa mzee wako", Maselina alimwalifu.

"Basi ukiona hivyo ujuwe mambo ni yale yale. Asipostaafu huyu mzee atakuja kutufia humo ofisini kutokana na ugonjwa wa moyo".

"Afe kwa ugonjwa wa moyo?, kwa ugonjwa huo utakufa wewe kabla yake. Mzima kweli huyo", Maselina alisema.

"Umeshajaribu kutingisha kiberiti na kujua ziko njiti ngapi nini?", Willy alitania.

Maselina alichukua rula na kutaka kumpga nayo. Willy aliepa huku akikimbilia mlango wa ofisi ya Chifu.

"Muhuni mkubwa, we!", hayo ndio maneno aliyoyasikia Willy yakitoka kinywani mwa Maselina.

Watu hawa wawili walikuwa wamefanyakazi pamoja kwa muda mrefu. walikuwa wakielewana kiasi kwamba walikuwa kama kaka na dada mtu au hata mpenzi.

Willy alipofungua mlango wa kuingia ndani alimkuta Chifu anasoma gazeti la Daily News.

"Shikamoo mzee", Willy alisalimia.

Chifu aliinua kichwa na kumtazama usoni.

"Marahaba. Imebidi nikuite maana nimepata habari ambazo zinahitaji sisi kuzishughulikia mara moja", Chifu alieleza.

"Nimepata habari kutoka Lusaka kuwa kumefanyika mkutano kati ya wakurugenzi wa upelelezi wa Zambia, Zimbabwe, Angola, Msumbiji na Botswana, pamoja na wakuu wa upelelezi wa wapigania uhuru. Sisi hatukuweza kuwakilishwa kutokana na sababu ambazo hazikuweza kuzuilika. Mazungumzo yao yalihusu mkutano wa wapigania uhuru ambao utafanyika kesho kutwa huko Arusha. Nafikiri unazo habari".

"Ndio ninazo".

"Kuna habari za kuaminika kwamba makaburu wana nia ya kuleta maafa makubwa na kuvuruga mkutano huo. Habari hizi ni za kipelelezi. Sasa sisi tunaombwa tuwe macho. Ingawa idara ya Polisi ilishajidhatiti kwa ulinzi huko Arusha, ni lazima na sisi tushughulikie suala hili kikamilifu. Hii ni kwamba kama kweli makaburu wamenuia kutenda kitendo hicho, bila shaka watatumia majasusi wa hali ya juu ambao wana uwezo mkubwa. Tayari wapigania uhuru wameshatuma mpelelezi wao maarufu Bon Sipele. Serikali ya Zimbabwe nayo imetuma mpelelezi wake mashuhuri Rocky Malele. Hao watawasili hapa leo jioni wakiwa njiani kuelekea Arusha...".

"Kwa hiyo hatuna budi kuungana nao leo hii ili kuimalisha usalama wa mkutano huu. Wakuu wa nchi wamekwisha julishwa. Vile vile Kamati ya ukombozi wa nchi huru za Afrika pamoja na wapigania uhuru wameaziimia mkutano huo lazima ufanyike. La sivyo, litakuwa pigo kubwa kwa wapigania uhuru na Afrika nzima na ushindi kwa makaburu. Kwa hiyo Willy hatuna uhakika makaburu watatumia mbinu gani. Ni dhahiri kuwa makaburu hawatatumia Jeshi ingawa Jeshi letu tayari limewekwa katika hali ya tahadhari tunahisi makaburu watatumia majasusi ili kuhujumu mkutano na ikibidi kuua wajumbe wengi kadiri inavyowezekana...".

"Kazi yako wewe na wenzako ni kuhakikisha kwamba jambo hili halitokei na mkutano utafanyika kama ulivyopangwa. Huo ndio utakuwa ushindi kwa Bara la Afrika na vile vile kuwatia hamasa wapigania uhuru. Baada ya mkutano huo wapigania uhuru watakuwa na nguvu mpya. Hivyo makaburu watakiona cha mtema kuni. Nafikiri umenielewa", alimalizia Chifu.

"Hatua gani za tahadhari zimechukuliwa awali, kwani inawezekana majasusi na makaburu wameshaingia nchini tayari", Willy aliasa.

"Walinzi wote kwenye mipata wameshatahadhalishwa na jeshi la polisi linafanya kazi yao. Viwanja vya Ndege vya Dar es Salaam na Kilimanjaro viko kwenye hali ya tahadhari. Wana usalama wanapekuwa vikali kila mtu anayeingia na kutoka. Wote wako macho. Kama ni kuingia nchini Majasusi hawawezi kuingia nchini mapema kwa kuogopa kugutukiwa", alijibu Chifu.

"Je wajumbe wameshawasili?", Willy aliuliza.

"Kufuatana na ripoti ya Polisi baadhi ya wajumbe wameshaanza kuingia. Wengine wako Arusha tayari. Ndio sababu lazima nyinyi muondoke leo. Tuketi yako iko tayari kwani Maselina kaishaandaa kila kitu kwa ajili ya safari yako", Chifu alimwambia Willy.

"Ni nani tutashughulika nae huko Arusha?".

"Hatutaki Polisi huko Arusha wajuwe kuwa nyinyi mnakwenda huko. Wakijuwa hivyo wanaweza kuridhika kuwa usalama upo halafu wasifanye kazi yao barabara. Hata hivyo Afisa Usalama wa mkoa anayo habari. Hivyo huyo ndiye mtu wa kumuona. Ndiye mtu wa kumwamini".

"Ni sawa kabisa, Hamisi ni mtu wa kuaminika. Lakini mbali na Hamisi, nisingependa mtu mwingine ajuwe kwani mimi nafahamu majasusi wa makaburu wanavyofanya kazi yao", Willy aliongezea.

"Sasa nenda ukajitayarishe. Vile vile nataka ripoti kutoka kwako kila wakati unapogundua kuna kitu kipya. Kama utahitaji msaada wa vijana wako uko huru kufanya hivyo, kwani watakaa hapa ofisini katika hali ya tahadhali", alisema Chifu.

"Ahsante, tuombe Mungu", Willy alijibu.

Alipofika karibu na mlango Chifu alimwita tena.

"Willy, chunga sana kwani makaburu siyo watu wa kawaida", Chifu alionya.

"Nitajihidi na Mungu atatusaidia". Willy alijibu na kutokea kwenye ofisi ya Katibu Muhtasi.

"Kwanini ukunibonyeza kwamba ninasafiri na wewe ndiye uliyekata tiketi, una visa wewe", Willy alimwambia Maselina.

"Nikwambie nini, mimi ndiye niliyekuajiri?. Mimi siyo mmbeya, bwana wewe", Maselina alisema.

"Najua unafurahi rohoni kwa kuwa mimi nasafiri. Wacha roho mbaya".

"Wewe Willy, wacha kuniumiza roho. Unajuwa jinsi gani ninavyojisikia ovyo unaposafiri. Mimi siyo kama hao wahuni wako, leo ukienda usirudi kesho wanao wengine. mimi kwangu wewe ni rafiki ambaye hana kifani na siwezi hata kufikiri ninaweza kuishi vipi bila wewe", Maselina alieleza kwa masikitiko makubwa.

"Niombee na Mola atanisaidia", Willy alijibu.

"Nakuombea kila siku", alimwambia Willy huku akimpa tiketi yake, "Chunga sana".

"Ahsante Maselina, nitajitahidi", Willy alijibu akainama akambusu kwenye shavu halafu akaondoka.

ITAENDELEA
 
Mkuu Willy Gamba 1 asante sana utamu ndo huoooo

CC Khantwe RR kidi kudi na wengineo

tupe uhondo mkuu naona mambo ndo kwaaanza yananoga mzee wa kazi Willy Gamba anaingia mzigoni
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom