Riwaya: Barua Kutoka Jela

Riwaya: Barua Kutoka Jela

Rushwaaa ni adui wa haki Mrs Masawe.......unaona sasa
 
MTUNZI: GAMA Ibrahim


SEHEMU YA KUMI NA SABA


Kilichotokea Mke wa Dokta Masawe hakukitegemea kabisa katika mawazo yake kama kingeweza kutokea!
Inspekta Jamila aliangaliwa na Afande Kubuta usoni, na Inspekta Jamila akakilaza kichwa chake kidogo pembeni ikiwa ni ishara ya kuruhusu jambo fulani kutendeka, hivyo kufumba na kufumbua Mke wa Dokta Masawe alikuwa ana Pingu mikononi mwake, huku Afande Kubuta akimwambia.
“Nakufungulia shitaka la kutoa Rushwa, ili kutaka kupindisha sheria huku ukiwa unafahamu kuwa ni kosa la Jinai katika Serikali ya jamuhuri ya muungano wa Tanzania!”
“Ama kwa hakika huu ni mtego wa panya.”


Inspekta Jamila alijisemea kimoyomoyo huku akiihakiki kama simu yake yenye Video Camera kama ilikuwa inafanya kazi yake sawasawa, na akathibitisha kuwa kweli alichokuwa akikirecodi kimeingia barabara.
Mke wa Dokta Masawe alipokuja kutanabahi, alikuwa yumo ndani ya gari ya polisi akiwa na pingu mikononi, akipelekwa kituo cha Polisi cha Daraja la Salenda akawekwe Rumande.
Inspekta Jamila na Afande Kubuta walikuwa hawana Msalie mtume, katika kufanya kazi yao.
*******


Kijana mrefu wa wastani aliejengeka kimazoezi, mweye misuli imara iliyotokeza anapotembea.
Alikuwa pahala ambapo mwenyewe hupendelea kupaita Chimbo, akimaanisha ni sehemu iliyojificha.
Alikuwa yupo katika himaya yake kule maeneo ya Vingunguti nyuma ya kiwanda cha kutengeneza kandambili cha Fida Hussein, akiwa anatafakari namna alivyowaacha wale maaskari kule maeneo ya Tabata Baracuda.
Alijipongeza kwa kitendo chake cha kuchelewa kufika katika eneo alilopanga kukutana na Dokta Masawe kwa dakika takribani kumi tu, lau kama angewahi kufika kama kawaida yake anapokuwa na ahadi na mtu, pengine siku ile angekuwa “Amelosti” (angekamatwa) kama watu wa Jamii yake wanavyopenda kulitamka neno lile!
Lakini kilichokuwa kinamuumiza kichwa zaidi ni pale kila anapoipiga simu ya Dokta Masawe, ilikuwa haipatikani kitu ambacho kilimtia mashaka zaidi.
Kupitia simu maalum ya Dokta Masawe ilikuwa haikosekani kwa siku zote zinazokwenda kwa Mungu.
Lakini leo nayo kila anapoipigia simu ile, ikawa pia haipatikani!
Akafikiri mambo mengi, yakiingia na kutoka, mara akasikia simu yake ikiita,na alipoitazama namba ya mpigaji alipatwa na kihoro, na wahka wa hali ya juu sana.
Akaipokea simu ile, ilikuwa ni simu ya Dokta Masawe!
Kwa sauti ya kunong’ona, Dokta Masawe alisema.
“Haloo JM, njoo ‘faster’ tukutane pale bar ya Y2K Buguruni ili tufanye mpango wa kuondoka leo hii hii, kabla ya kesho!”
Jm akamuuliza kwa makini Dokta Masawe.
“Nije ‘faster’, au nisije?!”
Dokta Masawe akasisitiza.
“Njoo faster bwana, fanya faster!”
Na Jeradi Mwaipopo au kwa kifupi JM, alijibu kwa maneno yasiyozidi matatu kisha akakata simu, alijibu;
“Itabidi iwe hivyo!”
Jeradi Mwaipopo baada ya kukata simu, alitingisha kichwa kwa masikitiko kisha akachomoa Bastola yake na kuibusu, na alipofanya kitendo kile macho yake yalikuwa yamemuiva kwa huzuni, na sekunde chache baadae machozi yalianza kumlengalenga!
Ama ukiona mtu mzima analia, basi ujue kuna jambo ni kweli.
Jeradi Mwaipopo ingawa aliambiwa maneno yale na alietokea kuwa Swahiba wake mpenzi, kwa siku za hivi karibuni Dokta Masawe, alipatwa na simanzi siyo kwa maneno yale laa hasha!
Bali kwa wito wa Dokta Masawe anapomtaka aende faster!
“Ama kwa yakini mimi sipajui, anapokaa Mwaipopo, ila kama mnataka apatikane, nipeni simu yangu ili nimpigie, kwangu yule kama pipa na mfuniko vile, atakuja tu kama Ng’ombe na zizi lake vile kisha nanyi mtamkamata!”
Wale askari wawili wakaona lile ni wazo lililokwenda shule, na bila ajizi Inspekta Jamila akawasha simu ya Dokta Masawe aliyokuwa nayo katika droo za ofisi yake, kisha akaitafuta namba ya Mwaipopo na kuipiga na baada ya sekunde chache simu ile ikawa inaita akaiweka katika ‘Loud speker’, ndipo alipompa Dokta Masawe ili amvute Jerdi Mwaipopo.
Na Dokta Masawe hakufanya makosa, akaenda hewani na kumtaka JM aende pale Y2K Bar Buguruni.
Hiyo ikiwa ni saa nne asubuhi siku ya Ijumaa.
Wingu zito jeusi lilitanda angani, kuashiria mvua inaweza kunyesha muda si mrefu.
Maafande wale walishauriana namna ya mtego wao jinsi utakavyokuwa, wakajipanga nani ake wapi, na afanye nini.
kisha akapakiwa Dokta Masawe, ndani ya gari ya polisi yenye namba za kiraia, isiyoonyesha vioo vyake kwa mtu alie nje kumuona wa ndani, bali wa ndani anaweza kumsanifu mtu wa nje kwa namna anavyotaka!
Safari ya kwenda Buguruni Y2K, ikaanza bila kuchelewa, kwani chelewa chelewa, utamkuta mwana si wako!
Inspekta Jamila, Afande Kubuta na Dokta Masawe, walikuwa ndani ya gari moja, na nyuma ya gari yao, kama gari ya tatu hivi kutoka katika gari yao, kulikuwa kuna gari nyingine ikiwafata!
Walitoka katika jengo la Wizara ya mambo ya ndani, wakachukua mtaa wa Azikiwe hadi Sokoine Drive wakapinda kulia, na kuendelea hadi yalipokutana maungio ya Mtaa wa Sokoine Drive na Barabara ya Uhuru, wakakata kulia kushika njia ya Barabara ya Uhuru waliyonyoosha nayo moja kwa moja hadi Buguruni, na kabla ya kituo cha mafuta cha Buguruni wakapinda kulia, na baada ya mwendo kidogo, wakawa katika Baa ya Y2K Buguruni, na kila mmoja akachukua nafasi yake, kama walivyokubaliana.
Katika kiti cha peke yake pale nje, Dokta Masawe aliletewa Bia aina ya Ndovu akapewa ajiburudishe nayo.
jamaa watatu waliokuwa wanaifatilia kwa nyuma gari aliyopandiswa Dokta Masawe, walishuka pale pia na moja kwa moja wakaenda katika meza ya mchezo wa Pool, wakawa wanajiburudisha kwa mchezo ule, wakiwa hawapo mbali sana na meza aliyokaa Dokta Masawe!
Afande Kubuta alikaa upande wa kaskazini, akiangalia upande wa kusini, walipotokea na gari yao.
Inspekta Jamila hakuwepo kabisa katika Baa ile ingawa alikuja pamoja wakiwa katika gari moja na Dokta masawe na Afande Kubuta, kwani kukaa pale kungeweza kuharibu mtego wao, kwa kuwa Jeradi Mwaipopo, alishamuona na anamfahamu!
*******
Jeradi Mwaipopo baada kuongea na simu ya Dokta Masawe, aliingia chumbani kwake huku bastola yake akiwa sasa ameichomeka kiunoni kwakwe, alitumia kiasi ya dakika ishirini hivi mle ndani, kisha akatoka huku akiwa anatabasamu!
Aliziendea Taxi zinazoegesha pale kiwandani kwa Fida Hussein akapanda katika gari moja iliyo makini, na kumwambia Dereva wa Taxi.
“Nipeleke Buguruni Sheli haraka iwezekanavyo”.
Yule dereva wa taxi, hakutaka kupatana, aliwasha gari na safari ya Buguruni ikaanza.
Na walipofika Pale Buguruni Sheli, JM akamlipa pesa zake dereva yule na wakaagana.
Akaanza kupiga hatua kuelekea katika Baa ya Y2K pale Buguruni.
Watu wachache waliokuwa katika Baa ile kulipafanya eneo lile kuwe na utulivu wa namna yake, Afande Kubuta akiwa na chupa yake ya soda ya Coca Cola, alikuwa ametulia kimya akinywa funda mojamoja, huku akiwa hana raha hata kidogo.
kwani muda unakwenda na Mwaipopo hakuwa na dalili kama angetokea!
Huku akiwa makini na kila anaeingia na kutoka katika Baa ile. Mara alimuona mzee mmoja mwenye kibyongo alievaa kanzu iliyochakaa na kofia chakavu miguuni mwake akiwa amevaa viatu vya kubazi,akiwa anaombaomba pesa.
Afande Kubuta akakumbuka kumbe leo ni siku ya Ijumaa, hivyo akayaondosha macho na mawazo yake kwa yule mzee masikini wa kutupwa. Nakuendelea kuangalia watu ambao anaweza kumuona mtu anaemuhitaji.
Muda ukawa unakatika dalili za kumuona Mwaipopo zilikuwa finyu sana.
Yule mzee ombaomba alikuwa katika meza ya Dokta Masawe, akiendelea kuombaomba kwa watu waliokuwa katika eneo lile.
Dokta Masawe alitazamana na yule mzee uso kwa uso na kisha yule mzee akaelekea uani kwenye Baa ile, akashika njia inayokwenda msalani.
Dokta Masawe kwa ishara maalum aliyoelekezwa na Afande Kubuta akaifanya, na mara moja Afande Kubuta akang’amua kwamba Dokta Masawe anataka kwenda chooni, akanyanyuka pale alipo kisha akakaa!
Hiyo ilikuwa ni ishara kwamba imetolewa ruhusa ya Dokta Masawe aende msalani.
Dokta Masawe akainuka,
na kuelekea katika vyoo vya wanaume.
Huku nyuma yake akiwa na mtu aliekuwa anamsubiri nje ya mlango wa vyoo vile, akiwa anaongea na simu yake!
Nyuma nje ya choo kile, pia alikuwapo mtu mmoja akiwa na sigara yake mdomoni akichukua doria!
Kiasi eneo lile lilikuwa na ulinzi wa kutosha.
Kiasi cha kama dakika mbili hivi yule mzee ombaomba alitoka chooni mle akatoka nje ya Baa ile na kuondoka zake.
Zikapita kiasi ya Dakika tano Dokta Masawe alikuwa bado hajatoka chooni, yule askari aliekuwa akiongea na simu, akamgongea mlango atoke kwani muda umekwenda sana na wao hawakwenda kwenye Baa ile kwaajili ya kustarehe, bali walikuwa na kazi maalum,
Lakini hata alipoendelea kugonga na kugonga, hakupata jibu lolote kutoka kule chooni alikokuwa Dokta Masawe!
Akaamua kuusukuma ule mlango wa choo ili amtoe Dokta Masawe chooni mle akaendelee kuwa chambo kule nje, katika mtego wao wa kumnasa Jeradi Mwaipopo.
Yule askari aliusukuma mlango kwa nguvu na kuingia mle chooni, Hamadi?!
Hakuyaamini macho yake kwani alimkuta Dokta Masawe alikuwa amelala mle ndani chooni akiwa hana dalili za uhai, macho yamemtoka pima, huku damu zikiwa zinamvuja pembeni ya sikio lake!
“Shit” Yule askari alisema maneno hayo kisha akasonya na kutoka nje mbio huku akiwa hakuugusa popote mwili wa marehemu Dokta Masawe!
Afande Kubuta alipomuona yule askari ametoka mbio kule uani huku akiangaza huku na kule kwa fadhaa, yeye akakimbilia kule uani,akapitiliza hadi chooni nakumshuhudia Dokta Masawe akiwa sasa ameshabadilika jina kwa kuongezewa jina la Marehemu Dokta Masawe!
Afande Kubuta alipatwa na mshangao usiosemeka, kwani wamezidiwa maarifa ingawa hakuelewa ni nani aliefanya vile!
Dokta Masawe hakuwa na silaha hivyo isingekuwa rahisi kujiuwa! Kwa kuwa shimo lililokuwa linaonekana chini ya sikio la Dokta Masawe, au Marehemu Dokta Masawe, lilikuwa ni tundu la risasi!
Kitu kilichomuumiza kichwa zaidi ni kuwa, silaha iliyotumika katika mauaji yale haikusikika mlio, kwa hiyo ilikuwa imewekwa kiwambo chakuzuia sauti isitoke!
Jasho likamtoka Afande Kubuta nae akatoka nje kwa haraka na kumfata askari ambae alipewa jukumu la kumlinda Dokta Masawe akiwa chooni, nakutaka maelezo ya kina ya nani aliefanya mauaji yale, na namna yalivyotokea!
“Mimi kama mpango ulivyokuwa, nilimsindikiza hadi chooni huku nikiwa sionyeshi kama nipo nae, alipoingia chooni mimi nilibaki nje ya choo kile nikijifanya naongea na simu, huku macho na masikio yangu nikiyaelekeza katika kazi iliyonileta.
mara akatoka mzee mmoja ombaomba mle chooni, mimi nikaendelea kumsubiri Dokta Masawe nikaona muda unakwenda nikaanza kumuhimiza Dokta Masawe atoke ili tuendelee na zoezi letu, lakini hakunipatiliza kwa chochote, nikaamua kuusukuma mlango ambao kumbe ulikuwa haujafungwa.
Ndipo nilipomkuta Dokta Masawe katika hali ile, na mle chooni zaidi ya yule babu ombaomba, hakuwemo mtu mwingine!”
Yule askari aliekuwa na jukumu la kumlinda Dokta Masawe alikuwa anaeleza vile ilivyotokea.
Wale jamaa waliokuwa wanacheza Pool, mara moja wakaungana na Afande Kubuta, na wakapewa maelezo ya kumtafuta yule ombaomba maeneo yale haraka iwezekanavyo!
Na mara moja kazi ikaanza huku yeye na yule askari wakirudi tena kule chooni kufanya upekuzi, na katika kutafuta tafuta mle chooni wakiwa wamevaa “gloves” mikononi mwao, Afande Kubuta akaokota ganda la risasi iliyotumika kumuua Dokta Masawe.
Na alipoliangalia vyema lile ganda, Afande Kubuta akatingisha kichwa kwa masikitiko.
Afande Kubuta, alibaini kuwa silaha iliyotumika kumuua Dokta Masawe, kwa mujibu wa ganda lake la risasi, ndiyo silaha ileile iliyotumika siku moja nyuma kule maeneo ya Tabata Baracuda!


ITAENDELEA…….


Jagarld Jullie Z Sangomwile Khantwe Mr Rocky Gunda66 Himidini VAN HEIST BPM ABUBAKAR SHEKAUNYIROmamsapkhan born again pagan princetx Ennie mcubic jonnie_vincy slim5 MAVUNO mp anold amoneyazan
 
Da, Jerad Mwaipopo ananikumbusha mbinu za Joram Kiango
^^
 
Jamila Ndie stering wa mchezo Jm kubwa la maadui picha ndo limeanza. Safi sana casuits
 
Mwaipopo ni Nouma...Hii ndo inatakiwa sio kamtego kadogo tu wewe unauvaa..inabidi wakukamatie mbali.
Big up Casuist
 
RIWAYA: BARUA KUTOKA JELA
MTUNZI: GAMA Ibrahim


SEHEMU YA KUMI NA NANE

Yule askari aliekuwa na jukumu la kumlinda Dokta Masawe alikuwa anaeleza vile ilivyotokea.
Wale jamaa waliokuwa wanacheza Pool, mara moja wakaungana na Afande Kubuta, na wakapewa maelezo ya kumtafuta yule ombaomba maeneo yale haraka iwezekanavyo!
Na mara moja kazi ikaanza huku yeye na yule askari wakirudi tena kule chooni kufanya upekuzi, na katika kutafuta tafuta mle chooni wakiwa wamevaa "gloves" mikononi mwao, Afande Kubuta akaokota ganda la risasi iliyotumika kumuua Dokta Masawe.
Na alipoliangalia vyema lile ganda, Afande Kubuta akatingisha kichwa kwa masikitiko.
Afande Kubuta, alibaini kuwa silaha iliyotumika kumuua Dokta Masawe, kwa mujibu wa ganda lake la risasi, ndiyo silaha ileile iliyotumika siku moja nyuma kule maeneo ya Tabata Baracuda!
Mara moja akang"amua kwamba Jeradi Mwaipopo alikuwa pale muda si mrefu, huku akijibadilisha na kujifanya ni ombaomba!
Afande Kubuta, akakumbuka jinsi Yule mtu, aliemdhania kuwa ni ombaomba, alivyokwenda katika meza ya Dokta Masawe akijifanya kuomba hela, kumbe ilikuwa ni geresha kwani alipotoka tu na kwenda chooni, haikupita hata dakika mbili, na Dokta Masawe akainua mikono yake juu huku akivifunganisha vidole vyake kule juu, ikiwa ni ishara aliyopewa na yeye mwenyewe Afande Kubuta, ikiwa kama atabanwa na mkojo.
kufikia hapo akaamini kwamba kweli Geradi Mwaipopo au JM alikuwa ni askari mwenye mbinu za kujihami[MK]na mbinu za medani[MM].
Watu waliokuwa wanataka kwenda chooni kwa wakati ule, walizuiliwa kuingia chooni mle huku wakielezwa kuna mtu amekufa chooni mle!
Mara muda si mrefu Afande Kubuta alitoka nje na kumuacha askari mwenzake kushika doria ili kuhakikisha haingii mtu yeyote chooni mle.
Afande Kubuta haraka alikwenda pale walipoiegesha gari yao na Inspekta Jamila, alipofika pale sehemu walipokuwa wameegesha gari yao, akakuta papo peupe!
Siyo gari wala Inspekta Jamila aliekuwa katika eneo lile, na Afande Kubuta akashika kiuno kwa kuchoka na mambo yaliyokuwa yanamuumiza kichwa kwa siku ile.
Akatoa simu yake ya mkononi, na kumpigia Inspekta Jamila ili ajue alipo,lakini pia ampe kilichojiri.
kitendo kilichozidi kumchosha kwani simu yake ilimwambia;
"Namba unayoipigia haipatikani kwa sasa, tafadhali jaribu tena baadae."
Afande Kubuta sasa akawa kama mtu aliepagawa vile, akaangalia maeneo yote ya jirani na Baa ile lakini mambo yalikuwa kama anavyoyaona, hakuna gari ya Inspekta Jamila, wala yeye mwenyewe! ikambidi akate shauri.
Mara akaona kundi la watu wanawake kwa wanaume, wakikimbia katika barabara ya Uhuru kuelekea upande wa kulia kule kwenye taa za kuongozea magari pale Buguruni sheli.
Afande Kubuta akiwa anatafakari, ukasikika mlio wa Risasi! Na sasa akaona watu wengi zaidi wakikimbilia kule kulikosikika mlio wa Risasi.


******
Inspekta Jamila akiwa ametulia ndani ya gari pale nje kwenye Baa ile ya Y2K pale Buguruni, alivutiwa sana na yule Ombaomba!
Kwani alipokwenda kwenye meza iliyokuwa na kinywaji cha Dokta Masawe, hakuonyesha mkono kama ishara ya kuomba pesa, aliyokuwa anaifanya katika meza za watu wengine!
Inspekta Jamila alimuona yule Ombaomba akimtazama kwa makini Dokta Masawe, na kisha kichwa cha yule Ombaomba kililazwa upande kidogo sana, kikielekeza upande wa uwani wa Baa ile!
Baada ya kufanya vile, yule Ombaomba akaelekea uwani mwa Baa ile, na katika muda usiozidi dakika mbili Dokta Masawe alifanya ishara iliyoashiria kwamba anataka kwenda chooni.
Inspekta Jamila moyo ulimripuka Ripu na damu yake ikaanza kuchemka! Huku mapigo ya moyo yakiongeza kasi katika mapigo yake!
Inspekta Jamila akiwa mle ndani ya gari alimshuhudia Afande Kubuta, akimruhusu Dokta Masawe aende chooni. Na Dokta Masawe akaelekea uwani mwa Baa ile ambapo vyoo vyake ndipo vilipokuwa.
Inspekta Jamila akaongeza umakini mara dufu, na hapo akamuona Afande Michael Chazza aliekuwa ameshika mti maalum wa kuchezea mchezo wa pool Table, akiuweka ule mti pale juu ya meza na kuelekea uwani sanjari na Dokta Masawe.
Na baada ya kama dakika nne hivi, Inspekta Jamila alimuona yule Ombaomba akitoka na kuondoka zake eneo lile akiifata ile barabara ya Uhuru kwa mwendo wa haraka kidogo.
Inspekta Jamila alimshuhudia yule Ombaomba akiipita gari aliyokuwemo yeye mle ndani, na aliporudisha macho yake kule kwenye Baa ya Y2K Dokta Masawe alikuwa bado hajarudi katika meza yake!
Kitendo bila kuchelewa, Inspekta Jamila aliwasha gari nakumfatilia yule Ombaomba kwa mwendo wa taratibu.
yule Ombaomba alikuwa ameshachanganya mwendo, na sasa alikuwa ameshaikaribia ile barabara ya Uhuru, akageuka nyuma kutazama kule kwenye Baa ya Y2K, huku akiwa anatembea kwa mwendo wa haraka, akaiona gari ndogo yenye vioo vya kiza ikija taratibu.
Hamadi! Yule ombaomba akagongana na Dada mmoja hivi aliekuwa anaelekea kule wenye bar ya Y2K.
Yule Ombaomba akakutanisha viganja vyake vya mikono kifuani kwake, na kuinama kidogo kama ishara yakumtaka radhi yule dada aliegongana nae. Lakini yule dada badala yakupokea samahani ile, alitoa msonyo mrefu kisha akashika Hamsini zake.
yule Ombaomba akapinda kulia kuelekea Buguruni Sheli.
Inspekta Jamila alipofika pale kwenye barabara ya Uhuru alisimama na kumfatilia kwa macho yule Ombaomba aliekuwa anazidisha hatua.
Inspekta Jamila akaiingiza gari katika barabara ya Uhuru akapinda kulia katika ile barabara inayoelekea Buguruni Sheli, huku macho yake yakiwa hayampotezi yule Ombaomba.
Yule Ombaomba alikuwa nae akiitazama ile gari ya Inspekta Jamila kwa makini na kituo, ambayo sasa alikuwa nayo sanjari yeye akiwa upande wa kulia katika njia ya watembea kwa miguu, na ile gari ikiwa upande wa kushoto katika njia ya gari kwenye ile barabara ya Uhuru.
Yule Ombaomba mara akasimama ghafla na kuingia katika duka moja la kuuza Vipuri vya magari, lakini pia akitaka kuthibitisha kwamba ile gari ilikuwa inamfata yeye au ilikuwa na safari zake!
Akiwa pale dukani aliishuhudia ile gari ikiegeshwa pembeni, na hata baada ya kuegeshwa kulikuwa hakuna mtu alietelemka kutoka katika gari ile, wala aliepanda!
Yule Ombaomba akiwa anabawabu muelekeo, mara akaja Bwana mmoja akiwa na pikipiki aina ya Honda 750 GL, akashuka na kutaka kuingia dukani mle.
kilifanywa kitendo ambacho hata Inspekta Jamila hakukitarajia kama kingeweza kufanyika, tena kwa wepesi wa ajabu namna ile!
Yule Ombaomba aliingiza mikono mifukoni mwake, alipoitoa mikono ile ilikuwa imekamata bastola iliyofungwa kiwambo cha kuzuia sauti, na kuifanya bastola ile ionekane ndefu kiasi!
Akamnyooshea bastola ile yule bwana aliekuja na pikipiki, huku akimtaka ampe funguo za pikipiki ile bila ya kuchelewa, na yule bwana aliekuja na pikipiki huku akigwaya kwa kitendo cha kuonyeshewa silaha ya moto namna ile, alimrushia zile funguo yule Ombaomba ambae kwake yule bwana mwenye ile pikipiki alimuona kama mtu mzima aliechanganyikiwa, Lakini pia dhalili na masikini wa kutupwa!
Yule Ombaomba alizidaka zile funguo na kuirukia ile pikipiki iliyokuwa inaangalia mjini, akaipiga stati na ile pikipiki bila hiyana, ikawaka ikisubiri safari!
Yule Ombaomba bila kufanya ajizi, kitendo bila kuchelewa akaigeuza kwa kupiga msele pikipiki ile. ikawa inatazama Buguruni Sheli!
Kila mtu ambae ameiona ile pikipiki ilipogeuzwa angeamini kuwa ni pikipiki yake yule mzee namna alivyoimiliki.
Aliingiza barabarani kiufundi katika barabara ile ya Uhuru akawa anatembelea barabara inayoruhusu kupita magari yanayotoka buguruni kwenda mjini! yaani alikuwa anatembelea barabara "NO ENTRY"
Bahati njema kwake ni kwamba, kulikuwa hakuna magari yanayokuja upande ule kwani taa za pale katika makutano ya barabara ya Uhuru na Mandela ilikuwa imeziruhusu gari kutoka Ilala kwenda Tabata, na usawa wa Tazara na hakukuwa na gari ilyokuwa inakata kuelekea Ilala.
Inspekta Jamila alipoona kitendo kile nae akaiingiza gari barabarani katika mwendo uliowaacha hoi watu wote walioiona namna gari ile ikichimba huku ikitoa mlio wa tairi zilizokuwa zikisuguana na barabara, na kusababisha vumbi kubwa sana sehemu ile.
Ikawa sasa upande wa kulia kulikuwa na pikipiki aina ya Honda 750 GL, na upande wa kushoto kulikuwa na gari aina ya Toyota Soluna XL zote kwa pamoja zikiiwahi sehemu ya maungio ya barabara ile pale kwenye kituo cha mafuta pale Buguruni.
Pikipiki iliongwezwa mwendo kwa mkono, na gari iliongezwa mwendo kwa mguu!
Kiasi kulikuwa hapatoshi eneo lile la Buguruni, kwani watu waliokuwa wanatokea Buguruni upande wa sokoni, na wale waliokuwa wanatokea upande wa Buguruni chama na kwa Mnyamani na kule upande wa sheli wote walikuwa wanakimbilia upande ule kulipotokea kizazaa cha pikipiki kelele zake lilipogeuzwa uelekeo, na kule kulipotokea kelele za gari alilokuwa anaendesha Inspekta Jamila.
Kwa kweli ilikuwa ni hatari tupu kukimbilia jambo kama lile.
Pikipiki ndiyo iliyowahi kufika katika maungio yale ikaingia, huku Inspekta Jamila akiwa amezuiliwa na gari iliyokuwa ikisuasua mbele yake, akaipita gari ile mkweche aina ya Datsun Nissan Old Model yakubebea mizigo, na sasa akawa yeye nyuma ya Pikipiki iliyokuwa imeibiwa na yule Ombaomba wa ajabu!
Mara Inspekta Jamila akamshuhudia yule Ombaomba akigeuza uso wake kumtazama, huku mkono wake wa kushoto ukiwa na bastola iliyofungwa kiwambo cha kuzuia sauti isisikike {Silence} akimnyooshea pale upande wake usawa wa dereva.
Mara akaona kidole kikigusa kile kifyatulio cha risasi {Trigger}

***HATARI…..Jamila mdomoni mwa kifoo!!!

NINI KITAJIRI…..OMBAOMBA WA ajabu huyu!!


ITAENDELEA!!!

Jagarld Jullie Z Sangomwile Khantwe Mr Rocky Gunda66 Himidini VAN HEIST BPM ABUBAKAR SHEKAUNYIROmamsapkhan born again pagan princetx Ennie mcubic jonnie_vincy slim5 MAVUNO mp anold amoneyazan
 
Casuist bora ungeishia pale mwanzo hii ya pili moyo mi unanidunda aisee tuwekee nyingine tafadhali (I beg u)
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom