g) Wakuu wa Mikoa
Wakuu wa Mikoa
118.-(1) Kutakuwa na Mkuu wa Mkoa kwa kila mkoa katika Jamhuri ya
Muungano ambaye, bila kuathiri ibara ndogo ya (3), atakuwa ni kiongozi katika
Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Wakuu wa Mikoa katika Tanzania Bara watateuliwa na Rais baada ya
kushauriana na Waziri Mkuu.
(3) Wakuu wa Mikoa katika Zanzibar watateuliwa na Rais wa Zanzibar.
(4) Bila kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (5), kila Mkuu wa Mkoa,
atakuwa na wajibu wa kusimamia utekelezaji wa kazi na shughuli zote za Serikali
ya Jamhuri ya Muungano katika Mkoa aliokabidhiwa; na kwa ajili hiyo,
atatekeleza kazi na shughuli zote zilizotajwa na sheria, au kwa mujibu wa sheria
kama ni kazi au shughuli za Mkuu wa Mkoa na atakuwa na madaraka yote
yatakayotajwa na Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge.
(5) Pamoja na wajibu na madaraka yake yaliyotajwa kwenye masharti
yaliyotangulia ya Ibara hii, Mkuu wa Mkoa wa mkoa wowote katika Zanzibar
atatekeleza kazi na shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
atakazokabidhiwa na Rais wa Zanzibar, na kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya
1984 au sheria yoyote iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi.