Play: Kinjeketile

Play: Kinjeketile

Lycaon pictus

JF-Expert Member
Joined
Jan 31, 2021
Posts
11,487
Reaction score
20,268
kinjekitile.jpg
 
kitabu hiki na vingine vingi vinapatikana ndani ya maktaba app(by pictuss). Inapatikana playstore.

Sehemu I



ONYESHO
I

Kijiji cha Ngarambe (Rufiji)

Njia inakwenda mtoni. Bibi Kitunda na mtoto wake, Chausiku, wanatoka kuchota maji.

CHAUSIKU: Mama tazama-nyumba ya Kinjeketile! Moshi!

BI KITUNDA: Pengine anapika. Ebu chungulia. (Mtoto anakwenda. Hajafika mbali) Ludi, Chausiku! Ludi, anakuja ntu. (Mtoto anarudi, anachukua mtungi wake).

BI KITUNDA: Habali, Bi Kinjeketile?

BI KINJEKETILE: Nzuli, nzuli. Salama?

BI ·KITUNDA: Salama tu. Leo watu hawajaludi mpaka sasa. Wamechelewa.

BIKINJEKETILE: Shamba la Bwana Kinoo limezidishwa ukubwa sasa. Kila ntu, nasikia, kapata mahali pakubwa zaidi.

BI KITUNDA: Bule tu. Hata huyo mume wangu akiludi sina cha kumpa. Nimetafuta walau muhogo, hata sikupata; na mizizi inatisha. Ntoto wa Bi Bobali amekufa—kwa hiyo hiyo mizizi.

BI KINJEKETILE: Kweli Bi Kitunda. Hata mimi naona taabu kupata chakula. Njaa.

BI KITUNDA: Isiwe njaa nanna gani, wanaume wenyewe wote wanalima shambani kwa Bwana Kinoo? Njaa itakosa wapi?

BI KINJEKETILE: Kweli unayosema.

BI KITUNDA: Mwenzangu huna hata kisamvu au kihogo unigaiye?

BI KINJEKETILE: Sina, babu.

BI KITUNDA: Basi sisi tulipoona moshi tukafikili unapika.

BI KINJEKETILE: Moshi ule ... Kinjeketile huyo anafanya kafala. Kajifungia ndani leo siku ya ngapi sijui.

BI KITUNDA: Kweli mimi simuoni. Lakini nanna gani yeye anaweza kukaa ndani bila kwenda shambani?

BI KINJEKETILE: Sijui, pengine amekwenda. Mimi sendi kuntazamatazama.

BI KITUNDA: Siku moja nikankuta ntoni peke yake. Mimi nilikwenda kalibu akuniona. Alikuwa anafata nto unakotokea. Anatazama maji kama hajayaona.

BI KINJEKETILE: Kabadilika sana. Analosema mimi silisikii. Aya kwa heli.

BI KITUNDA: Kwa heli. (Wanaachana. Kimya. Bi Kitunda na mtoto wake wamebaki peke yao. Wanatazama moshi unaotoka kwa Kinjeketile. Mama mtu anamwambia mtoto) Katazame wanapika nini. (Chausiku anakwenda nyumbani kwa Kinjeketile huku ananyema. Amefika akitaka kuchungulia-mara mbio. Mama yake anamkamata.)

BI KITUNDA: Nini?

CHAUSIKU: Nyoka! Nnafukuzwa na nyoka.

BI KITUNDA: Yuko wapi?

CHAUSIKU: Nyuma yangu.

BI KITUNDA: Wapi?

CHAUSIKU: Nyuma yangu.

BI KITUNDA: Akuna nyoka,

Akuna nyoka.

Tazama!

Yuko nyoka?

Akuna nyoka.

CHAUSIKU: Alikuwepo-nmemuona.

(Kimya. Wanatazama moshi)

BI KITUNDA: Kinjekitile.

(Kimya)

Watu wengi wanarudi kutoka shambani wamechoka, wana msaidia Kitunda. Bi Kitunda anakwenda kwa mumewe.


BI KITUNDA: Nini kimetokea?

BWANA WA KWANZA: Kitunda aliinuka kunyosha mgongo. Mnyapala akampiga viboko. Kitunda hakukubali; alikikamata kiboko. Pale pale Jumbe akaja, akaamrisha akamatwe atandikwe.

MNYAPALA: Pale akuna maongozi juu yaliyopita shambani. Itakuwa taabu.

KITUNDA: Niache nimtoe! Oho ... (Anataka kupigana. Anafungwa mdomo na bwana wapili. Anamnong'oneza.)

BWANA WA PILI: Kumbuka kuna mkutano leo, watu wamekwisha kuja. Imani. Imani. Basi, Bwana Mnyapala. Yamekwisha. Basi.

MNYAPALA: Asifanye taabu. Kesho mapema kazini. (Mnyapala anaondoka. Watu wengine wanakwenda mtoni. Kitunda na Bi Kitunda wanakwenda kwao. Chausiku angali anautazama moshi.)

KITUNDA: Unatazama nini?

BI KITUNDA: Chausiku alikwenda kalibu na nyumba ya Kinjeketile, akafukuzwa na nyoka.

KITUNDA: Nilitaka sana kuonana na Kinjeketile lakini, Ieo alipata mahali mbali na mimi.

BI KITUNDA: Alikuwa shambani?

KITUNDA: Nimemuona mtu kama yeye ... Yeye hasa, lakini kwa mbali.

BI KITUNDA: Mkewe kasema yuko ndani anafanya kafala.

KITUNDA: Mimi nimemuona leo!

BI KITUNDA: Ajabu hii. (Wanatazama moshi huku wanaondoka.)
 
ONYESHO II

Usiku. Ngulumbalyo anaingia, ameshika kizinga cha moto. Anakwenda kuelekea nyumba ya Kitunda.

NGULUMBALYO: (Anaita) Bwana Kitunda!

KITUNDA: Nakuja. (Anatokea) Je Ngulumbalyo, tayali?

NGULUMBALYO: Tayali. (Anainua mwenge wake; kwa upande mwengine tunaona mwenge. Na upande wa tatu tunaona mwenge vile vile. Baadaye kila upande anatoka mtu mmoja. Wanakuja pole pole. Wote wanne wanakutana kati kati. Watu waliochukua vizinga wanafifia gizani.)

MKICHI: Kinjeketile yuko wapi?

KITUNDA: Sifikili kama Kinjeketile atakuja leo. Siku nyingi sana hatujaongea. Namuona kwa mbali tu. Naona tuanze.

MKICHI: Toka mala ya kwanza kukutana mpaka leo akuna moja lililofanyika. Akuna moja tulilofanya.Udongo mwekundu bado yupo nchini kwetu. Bado zaidi amechukua nchi yetu. Ameichukua kwa nguvu.Sisi kama wanawake tunantazama tu. Anatulimisha kwa nguvu. Sisi tunantazama tu. Anatudai kodi. Sisi tunantazama tu. Anatudai sisi kodi? Ilikuwa sisi tundai yeye kodi, lakini apana! Sisi kama wanawake tumekaa tunantazama. Kuntazama huku mpaka lini? Tutakaa hivi hivi huku tunateswa katika nchi yetu mpaka lini?

MNGINDO: Tumuondoe—tukate shauli sasa hivi—vita. Akuna jingine.

KITUNDA: Kusema maneno unayosema ni lahisi. Sote sisi tunataka Njelumani aondoke. Lakini tutamuondoaje? Kwanza yeye ana silaha, sisi atuna. Jambo la kufanya ni kuanza kukusanyakusanya silaha—kuiba bunduki za askali, kunyang'anya, kufanya chini juu ili tupate

silaha. Hili haliwezi kufanyika mala moja. Tena basi itakua vigumu kulifanya maana hivi sasa kuna vibalaka chungu nzima. Utakachofanya, akina askali au Mnyapala kesha sikia. Tumeshikwa na njaa, na njaa hii inatufanya tuuzane. Kwa hiyo kuyapeleka mambo hayo mbio mbio haifai. Tuna maadui, na katika sisi wenyewe kuna maadui.

MNGINDO: Sasa ndio umesema nini?

KITUNDA: Tusubili, tupange. Tumengonjea muda mwingi….

MZEE: Sasa kupigana! Sasa vita tu, akuna jingine! Tufanye kafala kwa wazee na mizimu, na Hongo atatusaidia.

KITUNDA: Hongo pepo mkubwa. Lakini hana mamlaka juu ya kifo na uhai wa binadamu.

MZEE: (akisimama) Maneno unayosema ni ya hatali.

KITUNDA: Hatukuja hapa kuongea habali ya Hongo. Tumekuja hapa kukata shauli nini tufanye.

MKICHI: Na wewe unasema nini juu ya haya?

KITUNDA: Mimi nimekwisha sema—tungojee mpaka tupate silaha.

MKICHI: Hiyo ni sababu ya uoga. Lakini toka lini Mmatumbi akawa shujaa.

MZEE: Hatukuja hapa kugombana juu ya kabila.

KITUNDA: Mwache aseme tena na nitamfanya ajijutie maisha yake.

MKICHI: Wewe mwananke! Wamatumbi waogal (Kitunda anamrukia Mkichi. Wote chini.)

KITUNDA: Nitakuonyesha ... ah ... nita ... kuonye. . . sha nani mwananke. Mkichi kama . . . utanipa taabu mimi.

MKICHI: Mtumwa wa ah ... ah ... Kinoo. Mmatumbi... m ... shenzi. (Mkichi anakimbilia mkuki. Kitunda anachomoa kisu. Wanawindana. Mngindo anaingilia kati.)

MNGINDO: Tumekuja kutoka mbali kuungana, sio kupigana. Ikiwa sisi wenyewe kwa wenyewe tunataka kuuana, tutawezaje kupigana na udongo mwekundu?

(Kimya. Wanakaa kama kwanza.)

KITUNDA: Jambo la kwanza lazima tuungane, tuwe kitu kimoja.

MKICHI: Jambo la kwanza ni kupigana—vita.

MZEE: Vita bila sisi kuwa kitu kimoja kwanza, haiwezekani.

MNGINDO: Tufanye suluhu (anawanasihi).

KITUNDA: Mimi tayali kufanya suluhu na Nkichi. Lakini sisi tuliyo hapa hatutoshi kufanya vita peke yetu. Lazima tuwaambie Wazalamo.

MNGINDO: Mzalamo kasema zamani. Ikiwa kupigana atapigana peke yake. Lakini hawezi kuungana na Mngindo. Kama anajiona bora kuliko sisi, mwache.

KITUNDA: Walufiji je?

MKICHI: Walufiji wanasema wao tayali. Ikiwa tukianza vita wao watatusaidia.

KITUNDA: Hiki ni kinyume cha mambo. Atuwezi kupigana bila kwanza kuungana. Tuungane alafu tufanye vita. Watu kidogo kama sisi tutamalizwa mala moja. Nimesikia habali ya bunduki kubwa inayomwaga lisasi kama nchanga.

MKICHI: Umesikia au umeona?

KITUNDA: Sipendi unavyoniuliza.

MNGINDO: (Anamtazama Mkichi. Kitunda anawaona.) Anauliza tu.

KITUNDA: Kama munalo la kusema, semeni.

MNGINDO: Mkichi amekuuliza—je, hiyo bunduki umeiona au umeisikia?

KITUNDA: Nimeisikia.

MKICHI: Tumesikia kuwa ulikwenda Kilwa.

KITUNDA: Nilikwenda Kilwa kuntazama ndugu yangu. Alikuwa matatani selikalini.

MKICHI: Na wewe ukamsaidia.

MNGINDO: Watu wanasema kama ukienda Kilwa na maelezo fulani unapewa chochote. Udongo mwekunduanatoa pesa nyingi kupata habali.

KITUNDA: Una maana kusema mimi nitaweza kuwauzeni nyinyi nyote pamoja na watu wangu?

MKICHI: Kuna watu wanalipwa kuzuia makabila yasiungane kufanya vita.

KITUNDA: Ningalikuwa ntu wa Nzungu ningelikuwa hivi? (Anaonyesha majeraha mgongoni.)

MKICHI: Kwa nini unasita katika shauri hili la vita?

KITUNDA: Vifo vya watu—maelfu kwa maelfu ya watu.

MKICHI: Afazali kufa kuliko kukaa hivi tunatawaliwa, tunalimishwa kama wanyama. Njaa moja kwa moja kwa sababu hatuwezi kulima. Tunamulimia Bwana Kinoo tu. Afazali kufa kama Maisha haya.

KITUNDA: Afazali hayo kuliko kupigana na kupoteza maisha ya watu wote. Baadaye wale waliobaki wapate yale yale au zaidi kuliko yaliyowakuta mwanzo.

(Kimya)

MNGINDO: Tumekata shauri gani?

KITUNDA: Kuna moshi! Naona moshi! Penye moshi pana moto. Kalibu kutakuwa na moto.

MNGINDO: Moto wa mbali hauunguzi.

KITUNDA: Sijui nini la kusema. Siwezi kufikili moshi mtupu.

Mtu anakuja mbio—na kizinga cha moto.

NGULUMBALYO: Mnyapala anakuja.

MNGINDO: Sasa tunasemaje? Tukate shauri upesi.

MKICHI: Hatuwezi kusema lolote sasa. Lazima tukutane tena.

KITUNDA: Nitakuleteeni habali—upesi wanakuja.

Wanaondoka. Kitunda anakwenda kwake.
 
Back
Top Bottom