Great Thinkers, tuache kujadili mada juu ya mada. Mada hapa ni msimamo wa Papa Fransis juu ya kikomo cha uhuru wa kujieleza. Hii ni changamoto aliyoitoa Papa kwa dunia nzima. Tusirukie kukashifiana na kujadili dini ipi bora zaidi, hakuna majibu yatakayokubalika mpaka wewe na mimi tupotee duniani.
Binafsi naungana na Papa Fransis 100%. Kila uhuru lazima uwe na kikomo. Ameeleza kwa mfano mzuri wa kueleweka kwa kila mtu. Kwanini um-provoke mtu kwa maksudi? Akichukia unapata faida gani? Kama kuna faida inapatikana basi kuna hasara pia inaweza kutokea. Wanadamu tunatofautina sana viwango vyetu vya uvumilivu. Mifano ipo mingi hata kwa makabila yetu hapa Tanzania. Utani wanaofanyiana Wazaramo ukifika kwa Wakuria unazua majeraha au hata kifo. Unadhni Wafaransa wale hawajui hili? Mataifa ya magaharibi mara kadhaa wametumia mbinu hii ya kuwa-provoke mataifa mengine wapate kisingizio cha kuwavamia au kuwawekea vikwazo (rejea chokochoko za Marekani kwa China, Urusi na Iran).
Papa Fransis hapa anatutaka tuweke mipaka ya uhuru, kuheshimiana na kuvumiliana. Usifanye jambo ambalo litamchukiza mwenzako hata kama kwako wewe ni la kawaida. Tujifunze kuacha kila mtu aendelee na mambo yake ili mradi haingilii imani wala uhuru wa mwingine. Waislamu wanaamini kuchapisha picha achilia mbali kikaragosi cha kiongozi wao wa dini si sawa; basi tusichapishe kwani kwa kufanya hivyo tutavuruga amani yetu.
Nikirejea kwetu hapa Tanzania, nashangazwa sana na wahubiri wa dini wanaokashifu dini nyingine. Nimeona wengi. Nilichogundua wengi wao wana elimu ndogo sana (elimu ya dini zao na hata elimu ya kidunia). Ni waganga njaa 100%. Ni kama kikundi kinatumwa kwa nia fulani nyuma ya pazia. Kifupi hawajitambui. Ajabu kubwa naanza kuwaona hata hapa JamiiForum. Sidhani mtu mwenye elimu ya kutosha atakuja kuporomosha matusi ya kudhihaki dini nyingine. Sidhani mtu wa daraja la Padri wa Katoliki aandike "ubahau" kama wa wachangiaji wengi humu. Matusi na kukariri kifungu kidogo cha Biblia au Quran hakukufanyi wewe mwema duniani na naamini kwa imani yangu (mimi Muislamu 100%) hakukusaidii kuipata pepo. Elimu ya dini ni pana sana. Ni vigumu kupata umahiri katika elimu ya dini. Watu wachache walio mahiri katika dini huwezi kuwakuta wakikashifu dini nyingine.
Ndugu zangu great thinkers, sisi basi tuwe daraja la kuifanya dunia salama ambapo kila mtu ataabudu anachoamini bila kudhihakiwa wala bugudha.