JESHI LA POLISI KANDA MAALUM YA DAR ES SALAAM LINAWASHIKILIA BAADA YA KUWAKAMATA WATUHUMIWA 23 KWA TUHUMA MBALIMBALI ZA KIHALIFU
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limeendelea kuisimamia oparesheni maalum kali ya mtaa kwa mtaa, Kata kwa Kata dhidi ya makundi ya wahalifu ambao wengi wao ni vijana wanaojihusisha na vitendo vya kihalifu @
Panya Road.
Kufikia tarehe 11.5.2022 tayari wamekamatwa
watuhumiwa 23 kwa tuhuma za kujihusisha na matukio ya unyang'anyi wa Kutumia silaha mapanga na visu , kuvunja nyumba usiku, kujeruhi na kuiba vitu mbalimbali hasa maeneo ya Kitunda, Mwanagati Ilala na Kinondoni maeneo ya Kunduchi Mtongani na Tegeta.
Oparesheni hii ambayo ni endelevu inafanywa usiku na mchana na ilianza
tarehe 27/04/2022 na imefanikiwa kuwakamata wahalifu hao ambao wengi wao wana umri kati ya
miaka 13-24. Katika mahojiano, Jeshi la Polisi limebaini kuwa baadhi ya watuhumiwa hao hawakumaliza shule ya Msingi kwa utoro na sababu zingine mbalimbali.
Baadhi ya watuhumiwa waliokamatwa walifanya tukio la
unyang'anyi tarehe 10/05/2022, huku wakidai kulipa kisasi kwa baadhi ya watu wa maeneo hayo baada ya mtuhumiwa mwenzao kufariki kwa kushambuliwa na Wananchi wenye hasira kali kwa kujihusisha na wizi.
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na wananchi wa eneo hilo ilifanikiwa kuvipata vitu vilivyoibwa na wahalifu hao zikiwemo TV 3 na simu 1.
Jeshi la Polisi Kanda Maalum la Dar es Salaam, limebaini pia kuwepo kwa watu wanaojenga taharuki miongoni mwa wananchi na kusambaza taarifa mbalimbali za matukio ambayo hayapo kwenye maeneo wanayoyataja kwa lengo la kujenga hofu na taharuki. Jeshi linakemea vikali tabia hiyo.
Lakini pia kuna wakati Vijana wanapotoka kucheza mpira jioni wanapokuwa wanarejea nyumbani wakiwa kwenye makundi baadhi ya watu wamekuwa wakitumiana ujumbe kuwa kuna makundi hayo ya kihalifu yamezagaa mtaani na wanatenda uhalifu. Wananchi pia watambue kuwepo na kuimarishwa kwa vikundi vya ulinzi shirikishi ambavyo navyo vinaanza kazi mapema na baadhi wakiona vikundi hivyo huvihusisha na makundi ya kihalifu.
Vikundi hivi kwa wale ambao hawavitambui wamekuwa pia wakitumiana ujumbe kuwa wamekutana na makundi ya wahalifu. Tunawaomba wananchi wanapokuwa wana taarifa yoyote katika Kanda ya Dar es Salaam au kama wanataka ufafanuzi wa jambo lolote watumie
no 0787 66 83 06 au
0735 00 99 83.
Operation inaendelea na kipindi hiki inawakumbusha wazazi au walezi wajibu wao na ambao wanashindwa kutimiza wajibu wao kisheria wa kutoa matunzo kwa watoto ikiwemo
chakula, mavazi, malazi na elimu kama inavyoelezwa katika
Sheria ya Mtoto namba 21 ya Mwaka 2009 ambayo imefanyiwa marekebisho Mwaka 2019 imeelekeza adhabu ya faini au kwenda gerezani au vyote kwa pamoja kwa atakayepatikana na hatia.
MULIRO J MULIRO– ACP
KAMANDA WA POLISI KANDA MAALUM DAR ES SALAAM