Nusu Siku Ndani ya Jeneza-23-
ILIPOISHIA WIKI ILIYOPITA:
Alipomaliza kusema hayo, alituamuru kila mmoja apite mbele yake ili amuwekee mikono kama kiapo chake.
Hali ilikuwa sivyo kwangu sikutaka kabisa kukubaliana na tukio lile.
Sikuwa tayari kupita kwake na kuniwekea mikono kwani hilo nililiona kama ni kumsaliti Mungu wangu ambaye niliamini hata wao viumbe pia hawamuwezi.
ENDELEA SASA
NIKAANZA kuangaza huku na kule, moyo ukawa unaenda kwa kasi ya ajabu sana. Moyoni nikajawa na wasiwasi mkubwa ambao sikujua ulitoka wapi.
Nataka kila mmoja akae kwenye mstari kwa ajili ya kupita kwangu, ni kitendo cha haraka sana.
Akazidi kutuamuru yule kiumbe, lakini safari hii alikuwa makini na siriaz sana, kwani alikunja sura kwa kumaanisha alichokizungumza.
Wenzangu wote walijipanga mstari kwa ishara ya kukubaliana na amri ile, mimi na wenzangu wawili tulikuwa bado tukijikokota.
Basi, yule kiumbe akaamka na kuja hadi mahali tulipokuwa tumekaa.
Akatutaka sote tujipange mstarini kama alivyokuwa akielekeza.
Kwa shingo upande, tukajipanga kwenye mstari na kuanza kumsogelea yule kiumbe ili tukiri kuwa tutafuatisha maagizo yake.
Sasa baada ya zoezi hili, kuna nguvu kubwa na ya ajabu mno itakayoingia ndani yenu, na mtakuwa viumbe wapya kabisa na kuyafurahia maisha haya kwani mtakuwa mkifanya mambo yenu kwa uhuru mkubwa bila kipingamizi chochote kutoka kwa viumbe dhaifu kama bibadamu, alisema.
Akawa anasisitiza, lakini safari hii sauti yake ilitoka kwa juu sana huku ikiwa na kitetemeshi ndani yake, hali iliyomshitua kila mmoja wetu na kuanza kuingiwa na hofu kubwa ndani yetu.
Zoezi likaendelea hadi ilipofika zamu yangu. Hakika sikuwa tayari kabisa kukiri mbele ya huyo kiumbe kuwa nitafuata amri zake. Nilijiona kuwa na hatia kubwa mno kufanya jambo hilo kwani lilidhihirisha kuwa Mungu wangu wa Mbinguni alikuwa ameshindwa mbele ya viumbe wale.
Wewe, sogea hapa muda umekwisha nataka tupangiane majukumu.
Aliniamuru yule kiumbe baada ya kuona nasitasita kusogea karibu yake.
Hapa naomba niseme jambo moja. Hakuna kitu ambacho viumbe wa aina hiyo huwakasirisha kama kuona binadamu wa kawaida anaonesha kiburi mbele yao.
Basi, akawa ananiita nami niliendelea kusimama bila hata kujisogeza. Nikageuka kuwaangalia wenzangu ambao walikuwa wamekwisha tawazwa, nikakuta wakinishangaa. Lakini walikuwa tofauti kidogo. Macho yao yalikuwa makubwa na maangavu sana. Hata maumbo yao yalikuwa yamebadilika na kuwa makubwa kuliko yale ya awali.
Nikiwa naendelea kujiuliza, ghafla nikaanza kuona giza nene mbele yangu, kizunguzungu kikali kikanizingira na kuishiwa nguvu kabisa.
Kwa jina la Yesu Kristo aliye hai, kwa jina la Yesu, shetani tokaaa.
Nilijikuta nikikemea kwa nguvu kubwa sana, sikuelewa ni wapi nilipata ujasiri huo, lakini nikazidi kukemea tena na tena.
Nilipokemea kwa mara ya mwisho, nilijikuta niko ndani ya jeneza!
Jeneza lililokuwa limefunguliwa upande wa kichwa. Watu wengi walikuwa wakizunguka na wengine wakilia huku walikitaja jina langu, hali ilitisha.
Wakati naangaza huku na kule, nilishangaa kuona watu wote wakikimbia huku wakipiga mayowe na kusema marehemu amefufuka. Watu wote walikimbia na kuniacha peke yangu pamoja na mzee ambaye kwa kumuangalia kwa haraka, alikuwa ni mchungaji kutokana na aina ya mavazi aliyokuwa amevalia.
Mkononi alikuwa ameshika biblia. Akanitazama usoni na kukutanisha macho.
Bila hata kumsalimia nikamuuliza mahali nilipokuwa.
Hapa ni kijijini kwenu Kilosa, tumekuja kukuzika, alisema yule mzee huku akinisogelea kwa ujasiri mkubwa sana.
Akapiga magoti na kujiegemeza kwenye jeneza na kuuunyosha ule mkono uliokuwa na biblia kwa upande wangu.
Kunizika.
Ndiyo, akanijibu yule mzee huku akianza kukemea kwa sauti ya chini mno.
Sasa hivi ni saa ngapi, nilimuuliza.
Ni saa kumi na mbili jioni, tulikusafirisha kutoka huko ulikokuwa ukiishi tangu saa moja asubuhi, sasa kutokana na ubovu wa barabara, tumefika huku saa kumi na moja, kutokana na shughuli za kuweka mwili wako hapa na kukuaga, hatimaye imetimu saa kumi na mbili, akazidi kunifafanulia yule mzee.
Tulikuwa tumeamua kukuzika jioni hii kutokana na maamuzi ya kifamilia yaliyofikiwa na baadhi ya ndugu zako.
Nilikufa lini?
Ulikufa alifajiri, ilipotimu saa moja tukakuweka kwenye jeneza tayari kwa kukusafirisha, akanijibu yule mzee ambaye alijawa na ujasiri wa ajabu mno.
Hapa naomba niseme kitu kimoja. Watu wa Mungu huwa na ujasiri wa hali ya juu mno, hata kama watakumbana na maajabu kama yangu ya kufufuka.
Ina maana nimekaa nusu siku ndani ya jeneza?, nikamhoji kwa huku nikiwa nimemkazia macho yule mzee.
Ndiyo kijana wangu, umekaa nusu siku ndani ya jeneza, hebu nieleze ulikuwa wapi?, aliniuliza yule mzee na kunifanya nishtuke kwani sikutegemea kama angeniuliza swali kama lile.
Itaendelea wiki ijayo... siku ya Jumamosi.......