Nitakufa Mara Ya Pili

Nitakufa Mara Ya Pili

Hii hand writting ninavyoiona nahisi ni mwandiko wa chai chungu
 
19--Baada ya baba kuvuta mikupuo miwili ya sigara alinigeukia na kuniuliza swali.
“Shija vipi maendeleo yako darasani?”
Swali lile lilinishtua na kunifanya niiname chini kwa woga, nilijiuliza nitamjibu nini, kuhusiana na mwenendo wangu mbaya wa darasani.
Niliamini siri iliyokuwa moyoni mwangu ndiyo chanzo cha yote, lakini nilijiuliza nitaanza je kumueleza baba.
“Shija, nasikia siku hizi umekuwa mtukutu shuleni unagombana na wenzako, darasani husomi unasinzia muda wote tatizo nini mwanangu?”
Nilijikuta nikiwa njia panda huenda baba alikuwa amesikia habari nyingi juu yangu, pengine kanifuatilia kwa muda mrefu lakini alikaa kimya kuona kama nitamwambia.
Nilijiuliza nikimwambia itakuwaje, nilijikuta nikiamua liwalo na liwe bora nimweleze sikuwa na njia ya kumdanganya.
Kabla sijanyanyua mdomo kumueleza baba kinachonisibu, niliisikia sauti kwa mbali ya mzee Manoni akisalimiana na mtu jirani ya nyumba yetu. Woga ulinijaa na kujikuta nanyamaza kimya.

Baba baada ya kusubiri jibu langu bila mafanikio alisema.
“Shija huna jibu?”
“Baba wao ndio walionitishia kunipiga ndiyo tukapigana nao, lakini tuliyamaliza yakaisha,” ilibidi nipindishe ukweli ili nisikie ataniambia nini.
“Hivi Shija mtu niliyekuwa nakutegemea leo umekuwa hivyo , umekuwa Mung’unya kuharibikia ukubwani.
Na hii tabia ya kupigana imeanza lini tena na watoto wa kike.”
“Samahani baba, ni hasira tu.”
“Shija unakumbuka vizuri hata Father wa Kanisani alikusifia kwa akili yako, alisema kuwa wewe ndiye hazina yetu itakayotukomboa katika umaskini hivyo tukusomeshe kwa nguvu zote.
Upo darasa la sita umekuwa mgema tembo unalitia maji au sifa zimekulewesha?”
“Hapana baba, nitajitahidi siwezi kuwa nyuma tena kimasomo, nitajitajidi ili nisiwaudhi ninyi wazazi wangu.”
“Shija mwanangu kumbuka wewe ndiye kichwa cha familia, nimeapa kujinyima ili usome mpaka elimu ya juu. Unakumbuka ahadi aliyokueleza Father Thomas kuwa ukipasi darasa la saba atakupa zawadi nzuuuuri?”
“Ndiyo nakumbuka baba.”
“Sasa hiyo zawadi huitaki?”
“Naitaka.”
“Basi zingatia masomo.”
“Nakuahidi mzazi wangu nitafanya hivyo .”
“Acha utundu ambao ndio unakufanya upungue akili.”
“Sawa baba yangu, nitafanya yote uliyoniagiza.”
Baada ya mazungumzo na baba tuliagana, mimi kuingia chumbani kwangu na kumuacha baba naye akiwasha sigara yake iliyozimika wakati wa mazungumzo ili avute kabla ya kwenda kulala.
Baada ya kuingia ndani nilipanda kitandani kulala. Lakini kichwani nilikuwa na mawazo mengi sana juu ya taarifa alizozipata baba kuhusiana na matukio yaliyotokea shuleni na kumfikia baada ya muda kupita. Nilijiuliza taarifa zile alizipata zamani na kukaa kimya au baada ya kudorola katika masomo kuna mtu kamweleza habari zile.



Itaendelea...
 
20--Lakini nilimshukuru Mungu hakutaka kuyachimbua sana zaidi kunisisitizia niache utukutu na kuzingatia masomo. Bado wasiwasi wangu mkubwa ulikuwa matukio yaliyokuwa yakinitokea kila kukicha na kunifanya niwe kwenye msongo wa mawazo kiasi cha kushindwa kuyashika niliyokuwa nafundishwa. Nilipata wazo niende kwa mzee Manoni nimueleze niliyozungumza na baba juu kuporomoka kwangu kimasomo na vitisho vya usiku.
Kwenda kwake niliogopa lakini nilipanga akinitokea lazima nimwambie. Usiku wa siku ile ulikuwa mtulivu kuliko siku za nyuma nililala vizuri bila kutokewa na vitu vya kutisha.

Siku ya pili nilikwenda shuleni kama kawaida, darasani nilishangaa kuweza kutulia na kuweza kusoma kwa utulivu mkubwa hata kufanya vizuri katika masomo yangu. Baada ya kukusanya kazi na mwalimu kusahihisha kabla ya kwenda ofisini, alinisifia jinsi nilivyofanya vizuri katika somo lake.
“Leo Shija umenifurahisha sana, inaonekana umekuwa mtoto mzuri kuacha utundu na kuzingatia masomo, mpigieni makofi.”
Wanafunzi walinipigia makofi,
baada ya mwalimu kuondoka Sabina mmoja wa wale wasichana waliokuwa maadui zangu alinifuata kwenye dawati langu.
“Shija nimekuletea kiazi.”
“Asante Sabina,” nilishukuru bila kukichukua.
“Shija, si ulisema ugomvi wetu umekwisha?”
“Ni kweli.”
“Sasa mbona huchuki kiazi?” Niliona aibu kukataa japo sikumuamini moja kwa moja kwa kujua huenda katumwa ili kunimaliza. Lakini nilimtanguliza Mungu mbele na kukichukua kile kiazi.
Sabina ili kuhakikisha nakila muda ule alisema:
“Shija nikatie na mimi kidogo maana viazi hivi vilikuwa vichache nikakuchukulia wewe tu kwa mapenzi yangu kwako .
” Nilimkatia kipande tukala wote huku akinieleza nikitoka nisimuache.

Tokea siku ile nikawa na uhusiano wa karibu sana na Sabina mpaka akapelekea kuwa mpenzi wangu. Tukawa tukitoka shule tunaongozana na kwenda porini ambako hushinda mpaka jioni na kurudi nyumbani. Uhusiano wetu tuliuficha shuleni ili tusije fikiriwa vibaya , kutokana na baadhi ya wanafunzi kuadhibiwa mbele ya shule kwa kuwa na mahusiano ya mapenzi yaliyotokana na kukamatwa na barua za mapenzi.
Hata kutoka kwetu ilikuwa mimi napitia njia nyingine na Sabina naye alipitia yake na kukutana sehemu yetu tuliyoichagua kukutania. Kwa kweli uhusiano wetu japo kwa mila na desturi ni vibaya kwa vijana wadogo kama sisi kuwa na mahusiano ya kimapenzi, lakini kwa upande mwingine ilikuwa ni faida kubwa sana ambayo nilifikiri kama nisingekuwa na mahusiano ya karibu na Sabina ningebakia jina.


Itaendelea...
 
21--Nayasema haya kutokana na mambo niliyoambiwa na Sabina ambayo yaliufanya moyo wangu utetemeke kwa hofu. Niliamini kauli isemayo cheka nao lakini si wema kwako na adui yako anaweza kuwa rafiki mkubwa. Nimeamini kweli penzi hufungua moyo wa mtu na kuyatoa hata yaliyo chini ya uvungu wa moyo wake na kuwa tayari hata kufa kwa ajili ya kuyalinda mapenzi yake. Japo nilikuwa nakwenda kinyume na maadili yetu ya kujiingiza kwenye uhusiano katika umri mdogo, lakini naweza kusema ilinifungulia nisiyoyajua yaliyokuwa yakinizunguka , ambayo bila kuelezwa na Sabina binti aliyejitoa muhanga ningekufa kifo kibaya.

Siku moja baada ya kutoka shule Sabina alinieleza tusikae sehemu tuliyoizoea, nilimuuliza kwa nini, alinieleza kuna kitu anataka kunieleza ambacho kinatakiwa tuwe mbali na maeneo ya karibu na nyumbani. Tulikubaliana kama kawaida tulipita njia zetu na kukutana eneo tulilopanga kukutana kisha Sabina aliongoza kuelekea ndani zaidi ya pori.
Tulikwenda mpaka tukayaacha mashamba na kuingia kwenye pori ambalo hakukuwa na watu zaidi ya sauti za ndege. Niliamini sehemu zile kunaweza kuwa na wanyama wakali, kutokana na mwendo kuwa mrefu bila kufika nilianza kuingiwa na wasiwasi .
“Sabina unanipeleka wapi?” woga uliniingia na kuamini huenda kuonesha mapenzi kwangu ilikuwa njia ya kunikomesha. Niliona kama ni kweli alikuwa amenileta kimtego alikuwa amenipatia, kwa eneo lile sikuwa na ujanja wowote .
“Shija wasiwasi wako nini?”
”Mbona tunazidi kwenda ni habari gani za kunileta huku?”
“Shija ungejua wala usingeniuliza ungeweza kuniambia hata tupande gari tuondoke wilaya hii twende tukazungumze sehemu ya mbali zaidi.”
“Ni mazungumzo gani hayo?”
“Utayajua, japo nilionywa nisimwambie mtu yeyote , lakini nimejikuta nikizama kwenye mapenzi yako pia nakupenda sana tusingekuwa wanafunzi ningekueleza unioe,”
Sabina alisema kwa sauti ya upole.
Mmh makubwa, maneno ya Sabina yalinifanya nisihoji tena kitu na kumfuata kila alichotaka kukifanya juu yangu.
Niliridhika na maneno yake tukaendelea na safari iliyochukua nusu saa. Sabina alinieleza tukae chini ya mti wa mkalatusi, baada ya kukaa tulitulia kwa muda kila mmoja akivuta pumzi.

Baada ya kupumzika kwa muda Sabina alinitazama kwa muda usoni mpaka nikamuogopa, kilichofuatia kilikuwa machozi.
“Sabina unalia nini?” alinishtua baada ya kuongea machozi yalimtoka.
“Shija dunia hii kweli ina siri kubwa, siamini kijana mzuri kama wewe kuna watu wanautamani uhai wako?” Sabina aliniuliza huku michirizi ya machozi ikiwa mashavuni kwake .
“Uhai wangu?” Niliuliza kwa kushtuka kusikia vile.
“Ndiyo Shija.”
“Mungu wangu, kwa kosa gani?”
“Si unakumbuka kuna siku ulihudhuria ngoma ya wachawi ?”
Swali lile lilinishtua kwani kwa upande wangu nilikuwa naota, na swali lile niliogopa kulijibu kama ningelijibu basi ningekuwa nimevunja amri ya mzee Manoni ya kutomwambia mtu siri ile ya kukaa kimya kwa kila nitachokiona au kukisikia. Lakini niliamini mpaka Sabina kunileta kule basi alikuwa na siri nzito ambayo sikutakiwa kumficha ukweli wa kitu kilichokuwa ndani ya moyo wangu.
“Sabina kweli nilihudhuria ngoma ya wachawi , lakini nilikuwa ndotoni,” kwa mara ya kwanza nilitoa siri niliyokatazwa na mzee Manoni.
“Hapana Shija, kwa watu kama ninyi ambao si wachawi huhudhuria ngoma au jambo la kichawi hupitia kwa njia ya ndoto.”
“Kwa hiyo kweli nilikuwa kwenye ngoma ya wachawi ?”
“Kweli kabisa, hata sisi tulipokuona tulishangaa sana na kujua lazima siri yetu itatoka nje. Wachawi walidhamiria wakuue ili siri ile ufe nayo.”
Kauli ile ilinitisha sana na kuona kumbe kuna watu wanakufa bila makosa yoyote , sikutaka kuuliza swali nilitulia ili Sabina aendelee kunimwagia siri nzito za wachawi ambazo sikuzijua na nisingezijua. “ ...Lakini mzee Manoni,”
kusikia lile jina nilishtuka na kuficha hofu yangu,

Sabina aliendelea kuzungumza. “Lakini mzee Manoni aliwakataza wasikufanye vile kutokana na wewe kuingia bila kujua. Ila alisema atakuonya usimwambie mtu yeyote , kama utakuwa mbishi basi watachukua uamuzi huo wa kukatisha maisha yako.”
“Kwani mzee Manoni ni nani katika hao unaowaita wachawi ?” Nilimuuliza.
“Ndiye mkuu wa kanda ya wachawi .”
“Alaa kumbe, ehe.”
“Basi wachawi ambao ni wakubwa sisi ni wanafunzi ambao tumeingizwa kwa shinikizo la wazazi. Wachawi wakubwa walikubaliana kukuwekea uangalizi wa karibu pindi utakapotoa siri ile basi lazima habari wangeitapa. Wangeitana na kutoa uamuzi wa awali wa kuyachukua maisha yako.

Pale kwenu wapo watu ambao huwaoni lakini wapo kwa ajili ya kukusikiliza unazungumza nini na wazazi wako juu yetu.
“Lakini ilivyoonekana hukutoa siri nje muda wote ambao ulikuwa chini ya uchunguzi mkali. Tatizo kubwa lililowatibua wakuu wa uchawi ni siku ile uliyotuita sisi wachawi kibaya zaidi mbele ya wanafunzi.
Baada ya kuwapelekea taarifa akiwemo mama yangu ambaye na yeye yumo kwenye kamati ya wachawi wa kanda ambao wapo chini ya mzee Manoni.
“Ilitolewa amri ya wewe uuawe mara moja, lakini kabla ya hapo siku ulipohudhuria sherehe ya sadaka ya nyama ya mmoja wa wanachama, siku ile ndiyo uliyopitiwa usingizi darasani na ulipoamka watu wa kwanza kutuuliza tulikuwa sisi na kitu kibaya nasi tulikuwa kwenye sherehe hiyo.
Wasiwasi wetu ulikuwa lazima ungetoa siri kuwa ulituona kwenye ngoma ya kula nyama ya watu.”
“Sabina umeisha kula nyama ya watu?” Nilimuuliza...


Itaendelea...
 
22--“Shija huwezi kukwepa ukiingia kwenye chama kile.”
“Mmh haya, endelea”
“Lakini naomba Shija usinifikirie vibaya mimi kuwa na wewe ni mwanzo wa kuachana na kazi ile mbaya.”
“Nimekuelewa Sabina, ehe?”
“Basi siku tulipokuja shuleni tulielezwa yaliyokutokea na kitu cha ajabu hata aliyetupa habari alishangaa kwa kusema baada ya wewe kurudi darasani watu wa kwanza kuwauliza tulikuwa mimi na Helena. Kitu kile kilimshangaza hasa akizingatia siku nile hatukuwepo shule.
“Ndiyo maana tulikufuata kukuuliza sababu ya kutuuliza sisi, lakini ulitujibu kwa kiburi.

Kwa hasira baada ya kuondoka tulijigeuza fisi ili tukutie adabu, lakini mzee Manoni alitokea na kutufukuza kisha alitufuata na kutukataza tusikufanye kitu chochote. Baada ya kutukataza alitueleza tuoneshe upendo kwako . Toka siku ile bila kujieleza nilitokea kukupenda Shija hata sijui ni kwa nini, kila nilipolala nilikuota hata Helena nilimueleza. Tulikubaliana kuonesha mapenzi mazito kwako huku nafasi ya nani awe na wewe akaniachia mimi. Kumbe hata Helena naye alikuwa akikupigia mahesabu.

Hapo ndipo nilipopata kichaa cha mapenzi mtoto wa kike na kuamua kujiweka wazi mbele yako. Mpaka siku moja nilikuibia kiazi nyumbani na kukuletea, wakati nimejiweka wazi mbele yako na kunipokea na kujikuta nikiingia dunia nyingine ambayo japo kwa umri wetu ni kosa.
“Lakini bado niliamini hakuna moyo unaopenda huku unatambaa kwa vile kina mwanadamu aliyebalehe na kuvunja ungo alikuwa tayari ana matamanio ya mwili vile vile moyo wa kupenda kama mtu mzima.

Penzi langu kwako kama mama angejua basi angenifanya kitu kibaya. Nataka nikupe siri hii kumbe yale maneno ya kutuambia sisi wachawi yaliwaumiza wengi akiwemo mama yangu mzazi na baadhi ya wachawi wengine. Na kitu kikubwa alichokitaka kwako ni kukutia uchizi au akuulie mbali, na siri hii ilikuwa ya watu wachache ambao walimficha mzee Manoni ambaye siku zote alikutetea wasikudhuru.

Baada ya kumaliza tofauti zetu na kumueleza siku hizi tumekuwa marafiki mama alifurahi. Sikujua kumbe furaha yake ilikuwa ya kinafiki, siku ile nilipokuletea kiazi nilipofika nyumbani nilimueleza jinsi tunavyoelewana kiasi cha kukuletea kiazi.

Alionesha kufurahi kumbe moyoni alikuwa na dhamira mbaya sana kwako , juzi usiku mama pamoja na wanawake wenzake wa kundi la wachawi waliniita na kuniweka chini kunipa mpango mbaya wa kukumaliza. Niliwashangaa kupanga mpango ule bila kuona kosa lako, niliwauliza kosa lako nini walijibu sitakiwi kujua, nilinyamaza kimya kuwasikiliza bila kujua wewe ni mpenzi wangu.

Walinipa dawa ambayo walitaka nikuwekee kwenye viazi ambacho nitakuletea tukiwa shuleni, sikutaka kuwabishia lakini sikuwa tayari kufanya vile labda wakati tukiwa maadui. Basi baada ya kunipa vile vitu nilivichukua na kwenda kuvitumbukiza chooni bila wao kujua. Viazi navyo nilivitupa njiani wakati wa kuja shule, usiku nilipokutana na mama aliniuliza nilikupa nilikubali.
Waliamini usiku wa kuamkia leo usingeuona, lakini siri nilibakia nayo moyoni bila kukueleza chochote.

Siku ya pili niliporudi nyumbani niliulizwa kama umefika shule niliwajibu ndiyo umefika. Niliwaona wakichanganyikiwa kwa kuamini dawa waliyokulisha haikufanya kazi, baada ya kuona mpango wao wa awali umeshindikana walijipanga upya kwa ajili ya kukuangamiza. Nataka nikueleze kitu kimoja, usikubali kula kitu chochote utakachopewa na mtu si shuleni si njiani. Wanaweza kumtumia mtu mwingine, hata rafiki yangu Helena kwa sasa usimuamini kabisa kwa vile anaweza kushirikishwa na kukubali kukuangamiza. Nakuomba kwa hilo uwe makini sana.”

Baada ya kuzungumza kwa muda mrefu alimeza mate, wakati huo nilihisi mwili ukinitetemeka kwa hofu na jasho lilinitoka. Lakini kwa nje nilionekana nipo sawa kama mtu niliyekuwa nikifunuliwa ufunuo wa mambo yaliyojificha . Baada ya kumeza mate aliendelea. “Basi Shija upo katika wakati mgumu wa vita ya chinichini ambayo mzee Manoni hajui na kama angejua angewapa adhabu kali wote wenye njama mbaya kwako .

Shija kuna kitu kingine ambacho kilikuwa kikiniumiza sana akili yangu lakini naamini leo nikikueleza huwezi kuamini.”
“Kipi hicho tena?” nilimuuliza.
“Japo roho itakuuma lakini naomba usimwambie mtu hata wazazi wako.”

Sabina ana siri gani nzito anayotaka kumueleza Shija?

Itaendelea Baadaye.............
 
mkuu maji ukiyavulia nguo shurti uyaoge, umeamua mwenyewe kutuletea hadithi yako imwage hapa!
 
Bonge la hadithi mkuu,inasisimua kuanzia mwanzo.Wewe ni mtunzi mzuri mkuu!
 
23--“Kipi hicho tena Sabina?”
“Kuhusu kaka yako.”
“Kaka yangu yupi?”
“Kuna mwingine zaidi ya Luhemeja.”
“Luhemeja! Si ameishakufa kitambo, una habari gani zake?”
“Wewe unajua kaka yako amekufa?”
“Ndiyo.”
“Basi kaka yako hajafa.”
“Hajafa!?”
Nilishtuka kusikia vile.
”Ndiyo.”
“Utani huo Sabina hajafa vipi mtu nimemshuhudia mwenyewe akizikwa .”
“Ni kweli yote uliyashuhudia lakini ilikuwa kiini macho.”
“Mmh, mbona sikuelewi?”

“Ni vigumu kunielewa, kilichofanywa kwenu ni kiini macho kumpoteza kaka yako machoni kwenu ili aonekane amekufa.”
“Kama hajafa yupo wapi?”
“Yupo nyumbani kwao Helena.”
“Nyumbani kwao Helena?”
“Eeh, ila ni siri ambayo hakuna anayeijua zaidi ya wachawi wenyewe .”
“Mungu wangu nyumbani kwao Helena anafanya nini?” ”Amegeuzwa mwitunga (msukule) kazi yake ni kuchunga ng’ombe pembeni ya ziwa.”
“Mungu wangu, na muda aliopotea alikuwa wapi?”
“Alikuwa hukohuko, waliogopa kumchukua moja kwa moja kwa kuhofia kutafutwa na siri yao kuvuja ndiyo maana walimrudisha ili wamchukue.”
“Wampeleke wapi?”
“Kwenye kazi yake ya kuchunga ng’ombe.”
“Naweza kwenda kumuona?” “Unaweza lakini lazima tufanye kwa siri sana wakikugundua watakumaliza.”

“Mbona alirudi bila kuzungumza na mtu na kuingia chumbani kwake ?”
“Wakati ule anarudi kwenu hakuwa Luhemeja bali kivuli chake ndiyo maana hakuzungumza na watu. Aliingia chumbani ili mjue amerudi waliamini hamtamuuliza hadi asubuhi ambapo mngemkuta ameishakufa.”
“Mmh, inatisha.”
“Pia kuna siri moja ambayo familia yenu hamkuijua mapema, kuitwa kwako mchawi kulitokana na mpango wa chinichini uliopangwa bila ninyi kujua ili watu wafiche madhambi yao.
Lakini walikuwa na lao jambo, na kuharibika kwa akili kwa kwa kaka yako si bangi bali mchezo wa wachawi walimfanya vile ili waweze kumchukua kwa urahisi.

“Chanzo cha yote ni tatizo ni ugomvi wa shamba kati ya wazazi wako na wazazi wa Helena, baada ya baba yako kushinda kesi ya shamba walilokuwa wakigombea. Mama Helena aliapa kulipa kisasi nacho ni kumchukua mtoto mmoja kumgeuza mfanyakazi katika mashamba yake.
Si kaka yako tu kuna vijana wengi waliofariki kijijini na kujulikana wamekufa , lakini ukweli wote wapo pamoja na watu wengine ambao wametoka sehemu mbalimbali za wilaya yetu wapo kwao na Helena kazi yao kubwa ni kufanya kazi mbalimbali kama kulima na kuchunga ng’ombe. Hujiulizi ng’ombe wote wale nani mchungaji wao?
Au shamba lile lote nani anayelima?
Basi ni kaka yako na wenzake, lakini nakuomba suala hili usimwambie baba au mama yako itakuwa vita ambayo nina wasiwasi pengine wanaweza kumuua kabisa.

Ila nakuahidi kukusaidia kumrudisha.”
Mmh, nilishusha pumzi na kuzipandisha, nilihisi kuchoka, nilimuangalia Sabina na kuamini kweli ananipenda nami lazima nioneshe upendo kwake .
Siri aliyoniambia ilikuwa nzito sana ambayo mzee Manoni ndiyo aliyoiogopa mimi kuitoa kwa watu.

Baada ya Sabina kutulia alinitazama kama ananishangaa, nilimuuliza.
“Nini chaanzo cha wewe na Helena kuingia katika uchawi wakati bado ni wasichana wadogo?”
“Shija siyo mapenzi yetu bali shinikizo la wazazi huku tukitishiwa kama tungekataa basi tutatolewa kafara na nyama yetu kuliwa katika kikao cha wachawi .

Tuliogopa na kukubali, mwanzo kweli tulifanya kwa kulazimishwa lakini siku zilivyozidi kwenda tulijikuta tukizoea na kuifurahia kazi hiyo.
“Hata siku ya kuja kumchukua kaka yako nilikuwa na Helena.”
“Na mwalimu Veneranda naye mchawi?”
“Kwani kwenye ngoma hukumuona?”
“Nilimuona.”
”Basi naye ni mwanachama mkubwa sana.
” “Mbona hafanani?”
“Kwani mimi ukiambiwa mchawi utakubali?”
“Siwezi kukubali.”

“Basi huwezi kumjua mchawi kwa kumtazama tu labda uwe mganga au mchawi kwa vile wachawi tuna alama zetu. Ukimuona tu utajua huyu mwanachama.”
“Na wote niliowaona kwenye ngoma ni wachawi?”
“Shija mbona hukumuona baba au mama yako, kila aliyekuwepo ni mchawi.”
“Sasa kwa nini nilipelekwa kwenye mkutano wa wachawi .”
“Hizo ni dalili siku moja utakuwa mwanachama.”
“Mungu wangu, sikubali.”
“Lazima utakubali, utaulizwa uchague kifo au kuwa mwanachana.”


Inaendelea....
 
Kumbe uko huku! Poa cjakuona toka asubhi!
23--“Kipi hicho tena Sabina?”
“Kuhusu kaka yako.”
“
“Mbona alirudi bila kuzungumza na mpango wa chinichini uliopangwa bila ninyi kujua ili watu wafiche madhambi yao.

ma nioneshe upendo k mwanachana.”
[color/]

Inaendelea....
 
Back
Top Bottom