Amelie,
Ngoja nijaribu kuwa mshauri wenu kidogo...
Matatizo ya namna hii hayakuandami wewe pekee, wapo wengi wa namna yako.
Amelie, wewe ni mkristu? Mkatoliki? Mlienda semina ya ndoa kabla ya kufikia maamuzi ya kufunga ndoa kanisani? Kama si mkatoliki basi uliikosa fursa hii ya kipekee ambapo ungemsikiliza mfundishaji ungeweza kuchukua maamuzi kabla ya kuingia katika ndoa ambayo kwa mwaka mmoja tu unaanza kuhisi ni ndoano.
Ndoa ni kitu cha heri kabisa na wala usikijutie, kughafirika ni kwa kila binadamu na kubadilika inawezekana!
Kwanza:
Kuna ilani mliyojiwekea kuhusiana na masuala ya benki? Simu? Akaunti za barua pepe n.k? Kama hapana basi hili ni tatizo ila hujachelewa, mnaweza kuelewana mapema tu juu ya nini kifanyike na kivipi.
Pili:
Una kawaida ya kugawa ngawira mbele za mmeo haswa ukiwapa wadogo zako na ndugu za upande wako huku wa kwake ukiwapiga 'kibuti'? Kama ndiyo basi wewe ndiye tatizo na kama hapana basi kuna zaidi ambacho inabidi kueleweshana ili tuone pa kuanzia.
Tatu:
Una hakika ni mumeo tu au ni mume wenu? I mean, wewe ni mke wa ndoa halali ambapo una kila haki katika ndoa au mmeaminiana na kuamua kuanza kuishi pamoja? Kama hakuna ndoa baina yenu (inayotambuliwa na serikali) nitachemsha kwani huenda mwenzio ndo sasa kampata anayeona anamfaa kuwa mke... Hii inaweza kuwa habari mbaya kwako lakini bado si mwisho wa mahusiano yenu!
Nne:
Je washenga unaowaongelea ni watu wazima? Namaanisha ni watu wa makamo? Wakati anawasimulia ulitia neno? Wao walichukuliaje hali hiyo? Walitoa ushauri wa maana? Nini ulijifunza toka kwao?
Mara nyingi watu katika hali ya uchumba na wanapokaribia kuoana hukurupuka kutafuta washenga na kujikuta hawapati washenga sahihi na hivyo kubeba mamluki juu kwa juu na madhara yake mbeleni huwa makubwa. Aidha, matron na patron ni vema wawe watu wenye ndoa ili waweze kuwashauri kulingana na wao wanavyoyaishi maisha ya ndoa. Kama mlikosea na kutafuta wasela wataalam wa maneno tu hii inaweza kuwaathiri siku za usoni, washenga wakionekana si mali kitu msikimbilie kwa wazazi, kutana na matron au patron wanaweza kusaidia kabla hamjafikia pabaya.
Mwisho:
Ninaamini una mengi ya ziada na nilichoandika hakijakutosheleza, natambua wazi kuwa kuna chanzo cha yote haya, hii inawezekana kuwa imechochewa na masuala yenu binafsi (chumbani) ambayo yamepelekea hasira za mmeo naye anajikuta anakuwa mbogo. Kuwa mpole kwa mmeo, onyesha kumjali katika kipindi hiki ambacho mmetofautiana kidogo, mwambie mmeo ni jinsi gani unampenda, mweleze ni namna gani uliumizwa na kitendo cha yeye kukosa imani na wewe juu ya kitabu chako cha benki, usimwonee aibu kwani huyo ni mmeo!
Jaribu kuwa muwazi kwake, mpe 'account details' za benki na mwombe kama anaweza kukupa zake pia. Usimfiche password (neno au namba ya siri) ya akaunti yako! Penda kutumia hela yako kwa matumizi ya nyumbani na mfahamishe mmeo pindi ufanyapo hivyo, hii itamfanya aelewe mchango wako katika umoja wenu.
Nasisitiza: Ndoa si kitu kibaya, ni jambo la heshima na kusambaratika kwake ni dhahma kubwa kwa wapendanao. Kukosea ni jambo la kawaida na kuombana radhi hurejesha penzi lililoingia kiza.
Nakutakia tafakuri njema!