barafu
JF-Expert Member
- Apr 28, 2013
- 6,726
- 32,818
Sijajua kama watu wengi wamefuatilia na kung'amua,kwamba kila mahali awapo,iwe ni kwenye dhifa ya kidunia au ile ya kikanisa,James huvaa rozari yake shingoni.Bila haya wala soni,James huning'iniza rozari yake popote awapo,na pindi apatapo utulivu,James hupukuchua rozari kwa mafungu ya rozari ya siku husika.
Sikutarajia kwa namna ile,ile namna niliyomuona James akiwa amechuchumaa na mwenzake "singasinga" akiwa amepiga magoti mbele ya askari wasio na vyeo vikubwa.Ni ajabu na kweli...Hakika yametimia.Nimetikisika...Nimeogopa...Nimeshangazwa!!Kama hata James kaiona Keko!!!basi wengi hatuko salama.
Kweli huyu JPM hatabiriki,leo nimethibitisha.Unapomuona mwanaparokia mwenzako amepiga magoti mbele ya amri ya sare za polisi,wakati katika jumuiya na mijumuiko ya sala hutengewa kiti sbb ya ugonjwa wa miguu,unapata picha ya haraka tupo katika zama zipi.
Zaidi ya kuwa muumini safi wa kanisa katoliki,James ni "mfuasi" hodari sana wa kusali rozari,ni mmoja kati ya waumini wachache walio walei,waliojiunga katika vyama vya kitume vinavyosisitiza rozari.Mwezi May na Octoba,ni miezi ya rozari...Usipomuona kanisani basi utamuona nyumbani akiipukuchua rozari yake
Rugemalila ni mmoja wa "waasisi" wa Parokia ya Makongo Juu,na kwa ufuasi wake mkubwa katika rozari,"ushawishi" wake ulipelekea parokia yake ya Makongo Juu kuwekwa chini ya usimamizi wa "Bikira Maria Malkia wa Rozari".Hivyo kama ilivyo Parokia ya Osterbay chini ya Mtakatifu Petro(St.Peter's Parish) au St.Joseph Cathedral kule posta,Parokia ya Makongo Juu ni Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Rozari.Ushawishi wake ulivuka kila mahali.
Rugemalila anaipenda Rozari,na Rozari inampenda Rugemalila.Mpaka Parokia anayoishi na kusali imepewa jina la Bikira Maria Malkia wa Rozari.Ushawishi kila mahali...
July 2014,James Rugemalila akisaidiana na Prof Anna Tibaijuka waliongoza harambee ya kukusanya pesa za ujenzi wa kanisa la Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Rozari-Makongo Juu.Jumla ya shilingi milioni 319 zilikusanywa katika harambee hiyo,huku wawakilishi wa Mkombozi Commercial Bank wakiongozwa na dada Edina Lupembe wakijumuika pamoja na waumini kufanikisha zoezi la harambee.Naogopa kama na hizi watazitaja.
Najua huko Keko gerezani,usiku na kwa siku zinazofuatia,Rugemalila lazima "atafungua" kanisa dogo na mjumuiko wa waumini kwa kusali rozari.Mungu huwa na makusudi yake,watakaokaa chumba kimoja na Rugemalila huko Keko,watafaidi ujuzi na uwelewa wake mkubwa juu ya sala ya rozari na baraka zitokanazo na sala hiyo.
Hili nalo litapita...Lakini sio rahisi kuwaacha watu wengi salama.Mh.Rais alipotembelea Bukoba alisali katika kanisa kuu pale Bukoba.Muhashamu Methodius Kilaini alikuwa muongoza misa,alimsisitiza Rais kupambana na ufisadi kwa nguvu zote,na yeye kama Askofu atakuwa nyuma ya Rais kuhakikisha anashinda vita hivi.
Kwa kujua au kutokujua,Askofu Kilaini alimuomba Rais "akaze kotekote" bila kuona aibu,ili wote waliokuwa wanaitafuna hii nchi,bila kujali vyeo vyao na nafasi zao katika jamii,basi wawajibishwe.
Rais alimtahadharisha Askofu Kilaini,akamwambia atakaza sana,ila na wao kanisani wajiandae kukosa sadaka au sadaka kupungua,maana atakaba mianya yote ya wizi na ufisadi,ili waliokuwa wanatoa sadaka kwa pesa za "wizi",wabanwe na wakose pa kupitia.
Yanapotokea ya Rugemalila kulala Keko,yanakumbusha mgawo wa kina Kilaini na wengine,orodha ya maaskofu na Mapadre,wanasiasana na watumishi wa uma.Kweli mtikisiko wa JPM haujawahi kumuacha mtu salama.Makongo Juu na kwaya iliyodhaminiwa kwa kiasi kikubwa,mpaka St.Joseph kwa kina Pengo patakuwa na minong'ono wakati wa chakula cha mchana na jioni meza kuu.Yalipita ya kina Papa Benedict na Bank ya Vatican,hili nalo la Rugemalila wa Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Rozari litapita.Ni lile lile,takatifu,katoliki la mitume...Juu ya mwamba huu,Mtume Petro aliambiwa litajengwa.
Si ajabu ,katika picha nyingi za dhihaka mtandaoni,zinamuonyesha James "Akisali Rozari" ili Chenge asipewe nafasi ya kukamatwa na kuletwa mahakamani kusema mengi zaidi juu ya Escrow.HAKIKA YAMETIMIA!!!
Nitarudi haraka,ninarudi kumpa pole na kumfariji....Ninarudi kusema pole ya mdomo,pole kwa muumini na mwanaporikia mwenzangu!!!Nitasema Pole James...Pole kwa yaliyokutokea na si pole kwa uliyoyatenda!
[HASHTAG]#JPMbadozaStanbic[/HASHTAG]
[HASHTAG]#JPMWamulikeSIMBATRUST[/HASHTAG]
[HASHTAG]#SIMBATRUST[/HASHTAG]
NB:Jambo hili lisichukuliwa kama dhihaka kwa waumini wa upande fulani,ustarabu ni pamoja na kujadili mambo kwa kushinda mihemko ya kiimani.
Kauli hii ya Kardinal Pengo,inatukumbusha "upande wa pili" wa Kanisa Katoliki