Pole kwa changamoto za maisha na hongera kwa kuonesha msimamo wao bila kuficha ...lakini hiyo ndio namna ya kukua.
Katika maisha yetu ya kila siku, huwa tunakabiliwa na changamoto, tunazikabili, tunazitatua, tunakuwa wazoefu wa maisha na hatimaye tunajenga uwezo zaidi wa kupambana na changamoto zingine kwa siku zijazo.
Ningekuwa kwenye nafasi yako, ningefanya kama wewe, tena ningefanya zaidi.... ningelaani na kukemea kwa nguvu zangu zote. Nisingekubaliana kabisa na wazo hilo la shemeji na mdogo wangu kufunga ndoa. Simamia kile unachokiamini na kipiganie kwa nguvu zako mpaka mwisho, kuna siku watakuelewa hasa mdogo wako. Anaweza asikuelewe leo lakini kuna siku moja atakuja kukushukuru kwa msimamo wako huo. Usifanye mambo au usiache mambo yaharibike kwa sababu unataka kuwafurahisha wengine.. waache wakasirike kuna siku watakuelewa. Kumbuka wewe umepewa dhamana ya kuwa 'Mlezi Mama', yaani wewe ni zaidi ya dada, hivyo una jukumu la kupambana na kulinda maadili na maslahi ya mdogo wako.
Unakumbuka tulipokuwa wadogo kuna mambo mengi tulitamani kuyafanya tukiamini yangetupa furaha sana lakini wazazi wetu walituzuia na tulikasirika sana, na hata wakati mwingine tuliwachukia, lakini baadaye tulikuja kuwaelewa na kuwashukuru kwa maamuzi yao ambayo kwa wakati huo tuliyaona mabaya. Kwasababu wao walisimamia kwenye ukweli. Wewe umesimama kwenye ukweli, endelea kusimama hapohapo hata kama unapingwa na kuchukiwa na watu wako wa karibu. Inapofika mahali unatetea 'damu' yako, usimumunye maneno hatakama 'hubby' wako na shemeji hawaoneshi furaha, achana nao wataizoea hali lakini wewe endelea kusimamia kile unachoamini.
Hii ni hoja nzito na tete, inahitaji mjadala wa hoja na sio kutishana wala kununiana miongoni mwa wanafamilia, kama kweli wana nia ya dhati kwa hicho wanachotaka kufanya waambie waelete hoja yao mezani, muijadili kwa hoja. Sio kwa kutishana kwamba eti, 'unamuharibia mdogo wako', hiyo sio hoja, hata mtu anapoamua 'kutoonesha furaha yake kwako' ni aina ya udhaifu, kwani kama ana hoja ya kweli anapaswa aiweke mezani. Waneleta na kufanya yote hayo ili wewe ushindwe hoja yako, ili wao waendelee.
Hata kama huko mbeleni watafanya ujanjaujanja na labda wakafanikiwa nia yao ovu, ni muhimu sana wewe uoneshe msimamo wako sasa kwamba hukubaliani na hilo, ili hata yakitokea ya kutokea huko mbeleni utabaki na heshima kwamba msimamo wako haukutetereka.