[h=2]Ushindani wa Kisiasa Tanzania na Siasa Tunayoitaka! (Sehemu ya II- 'AJIRA')[/h]
Wadau,
Katika sehemu ya kwanza na mada hii ya "Ushindani wa Kisiasa Tanzania na Siasa Tunayoitaka" Nilizungumzia kwa uchache suala la gesi.Sasa leo nizungumzie kidogo katika suala la ajira.
Ni wazi kwamba kwa sasa licha ya kuwa na tatizo kubwa la ajira nchini, kuna jitihada za hapa na pale ambazo zimefanywa kupunguza tatizo hilo japo tatizo bado ni kubwa.Jitihada hizo zinaweza kuwa bora au kuwa dhaifu.Katika hali ya kawaida tu, inategemewa ushindani wa kisiasa utupelekee katika kupata njia bora zaidi katika eneo hili na kama ushindani huo ukitupeleka kinyume chake, sidhani kama utakuwa na maana yeyote.
Katika serikali inayoongozwa na CCM, Tanzania kuna viwanda vidogo vidogo (Light Industries) kadhaa na hili ni jambo la wazi tu kwa sababu vinaonekana na vinatoa ajira japo kwa uchache sana.Sasa tunategemea katika ushindani wa kisiasa, tuone wanasiasa wanaopingana na jitihada mipango au mbinu zilizopo kwa sasa kwa kusema sisi tunaweza kutengeneza mazingira kwa watu binafsi/au sisi tukipewa serikali kama serikali tutajenga viwanda vizito (Heavy Industries) kama vya magari na Ndege,n.k au wataongeza kasi ya kuendeleza viwanda vidogo vidogo kama vya juice ambavyo hata sasa vipo.Hata hivyo ni lazima waoneshe dalili na nia yao kwa matendo maana kwa kusema tu, haiwezi kusaidia kitu.Kwa mfano, kama chama kitaahidi kujenga viwanda vizito ili kuwapatia watanzania ajira ,wakati huo huo kinashindwa hata kujenga ofisi yake,wala hakioneshi jitihada ya kufanya hivyo, hakiwezi kuaminika.
Kwa sasa kuna wanasiasa wamebuni mbinu mbali mbali za kuwapatia watanzania ajira.Mbinu nyingine zimebuniwa katika level ya kitaifa, na nyingine katika level za majimbo.Kwa mfano, Mtemvu wa temeke, yeye ameona kuwatafutia watanzania kazi huko uarabuni ndio njia ya kuwanusuru!, kuna wengine huko dodoma wameona kuwasaidia watanzania waweze kufuga nyuki katika maeneo yao ndio njia ya kuwanusuru, wengine wameona kuwasaidi watanzania waweze kufuga kuku ndio njia ya kuwanusuru, wengine wanadhani boda boda ndio mpango!.Ni suala la mawazo tu, mawazo haya yanaweza kuwa imara au dhaifu na ndio maana kukawa na ushindani wa siasa ili tuweze kupata mawazo bora zaidi.
Hivyo basi, katika hali ya kawaida, haitarajiwi kusikia wanasiasa wanaodhani wao ni mbadala wakilalamika na kulaumu tu bali kuja na mbinu mbadala bora zaidi na zinazotekelezeka, na nilazima wawe washaanza kuzifanyia rehearsal mbinu hizo katika majimbo wanayoshikilia.Kwa mfano, Haina maana ya CHADEMA kwa mfano,kumlaumu Mtemvu tu kwamba anawapeleka watanzania uarabuni, wakati wabunge wa CHADEMA hawajaonesha mbinu zao za kuwapatia vijana ajira katika maeneo yao ili tuweze kulinganisha. Inafaa katika majimbo ambayo yanashikiliwa na upinzani yawe mashamba darasa ili hata ahadi zikitolewa katika level ya taifa iwe ni rahisi kueleweka kwa kuangalia katika level ya majimbo.Mfano, Lema Anatakiwa kuweka wazi kwamba anawasaidia je vijana wa Arusha kwa sasa kupata ajira,Msigwa, Halima Mdee, na kadhalika wafanye hivyo hivyo ili tuweze kulinganisha na hawa wa CCM, wanaoleta mawazo mara ya kufuga, nyuki, kuku, au kuwatafutia watu kazi huko uarabuni.n.k kwa kufanya hivyo watanzania wataweza kulinganisha na kujua nani ni nani na kwa mwendo huo tutakuwa tunafanya siasa zenye manufaa.
Hizi ndizo siasa za ushindani wanazozitaka watanzania!