Niko mwenyewe kitandani

Dotto C. Rangimoto

JF-Expert Member
Nov 22, 2012
1,985
1,282
NIKO MWENYEWE KITANDANI.
1462354756920.jpg


Barua hino sichane, tena situpe jaani,
Kila siku uione, uipime kwa mzani,
Saahu vitu vingine, si mahaba yetu hani,
Japo mithili ya tone, yakukae mtimani,
Nataraji nikushike, ewe wangu wa moyoni.

Ewe wangu wa imani, leo nataka ninene,
Niko mwenyewe chumbani, na kiza hiki kinene,
Nawaza yangu thamani, ilo yazidi mapene,
Yenyewe nambari wani, wa kununa na anune,
Nataraji nikushike, ewe wangu wa moyoni.

Ningeomba nikuone, tuwe wote kitandani,
Taratibu tushikane, sote twende mlimani
Laazizi tunong'one, tunapokuwa njiani,
Kwa matao tubebane, tukaketi kileleni.
Nataraji nikushike, ewe wangu wa moyoni.

Nashikwa na Subiani, uchomapo manemane,
Sautiyo ya puani, tulichezapo sebene,
Yanikita mtimani, kiasi moyo unene,
Siniwate maishani, miye nawe tuoane,
Nataraji nikushike, ewe wangu wa moyoni.

Mpenzi karne na karne, tuwe sote furahani,
Duniani tunatane, kama ngeda natamani,
Firdaus tukutane, kwa uwezo wa Manani,
Wabaya waulizane, wanipa nini mwandani,
Nataraji nikushike, ewe wangu wa moyoni.

Kupika ni yako fani, si mahando si vinane,
Nakumbuka biriani, ulo nipa na chatine
Hebu nitoe shakani, 'tanipa siku nyingine?
Nipe tena si utani, siniwache nisonone,
Nataraji nikushike, ewe wangu wa moyoni.

Dotto Rangimoto Chamchua.(Njano5)
whatsapp/call 0622845394 Morogoro
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom