Ndoa Yangu

Ndoa Yangu

Madame S

JF-Expert Member
Joined
Mar 4, 2015
Posts
17,177
Reaction score
34,444
NDOA YANGU (01)
‘Chozi langu litalipwa’
By; KING T CONTROL

Nilipokuwa mdogo kipindi bado nasoma, nakumbuka maneno aliyokuwa anapenda kunambia marehemu baba. Maneno ambayo awali niliyachukulia mepesi sana kwa kuyanukuu pasipo kuujua uzito uliokuwa ndani yake. Endapo ningeyabeba na kumakinika nayo…. Huenda hadithi hii isingekuwepo kwenye maisha yangu.
Baba alisema....
"Utapokuwa mkubwa usije kuoa mwanamke eti kwa sababu unampenda naye anakupenda…! hapana. Bali oa mwanamke ambaye unamuhitaji na ukahakikisha naye anakuhitaji. Hapo mtaishi vizuri na kujenga familia bora. Kua ukikumbuka haya mwanangu ili usije kukosea kuoa kwani utakuwa umeyakosea kabisa maisha."
Maneno haya ya baba yaliishia kuwa ya baba akilini mwangu wala sijawahi kufikiria kama ipo siku yanaweza kuzitesa hisia zangu na kuuchoma moyo wangu kila nikumbukapo puuzio langu.
Hakika hii ni hadithi ya kweli katika maisha yangu. Hadithi ya NDOA YANGU...... Ingawa yanaweza kuwa ni makosa yangu lakini sikustahili malipo haya. Maumivu makali ya moyo yalizishawishi akili zangu zilipe kisasi lakini imani yangu ndiyo iliyonizua ikinikumbusha kuwa yupo mkuu baba mwenye kutoa hukumu siku ya malipo. Siku ambayo sote tutakuwa wadogo zaidi ya chembe ya punje ya haradali. Kama tunaamini kweli Mungu yupo na ndiye mwenye kuhukumu basi naamini kwa ubaya niliotendwa…….. chozi langu litalipwa.
Karibu kwenye mkasa wangu naamini nawe utajifunza mengi.
*******
Naitwa Onesmo, ni mtoto wa mwisho na pekee wa kiume kati ya watoto watano kwenye uzawa wetu. Nilipokuwa mkubwa baada ya kumaliza kidato cha nne baba alifariki kwa ajali ya gari na kutuachia ukiwa. Maisha yalibadilika siku baada ya siku na kuwa magumu. Dada yangu mmoja tu alibahatika kuolewa huku wengine wakizalishwa wakiwa nyumbani. Hali hii iliniumiza sana. Ndoto yangu ilikuwa kuona siku moja tunaishi maisha mazuri na ya fahari. Mama aliniusia mara nyingi sana kuwa nina mzigo mkubwa kwenye familia yetu, hivyo yanipasa niwe na upeo mkubwa kuweza kuwaongoza dada zangu nikiwa ndiye kaka yao wa pekee.
Hali hii ilinifanya niishi kwa kujituma sana kwenye kazi ingawa nilifeli kuendelea na masomo ya elimu ya juu. Siku zote niliamini kufeli shule sio kufeli maisha.
Nilijituma na kujichanganya kwenye kazi mbalimbali. Sikuchagua kazi ilimradi tu iwe ya halali isiyovunja maadili na utu. Na hapo ndipo nilipojijengea marafiki wengi wanaopenda kujishughulisha. Ni kweli kabisa ukiwa mvivu basi utatengeneza marafiki wengi wavivu. Ukiwa tapeli utawapata marafiki wengi matapeli. Halikadharika ukiwa mwizi vivyohivyo kama ukiwa mpenda kukaa vijiweni basi rafikizo watakuwa wa vijiweni tu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwangu kupenda kujituma na kufanya kazi ilinijengea kutengeneza marafiki wa tabia zangu. Na ndipo baada ya miaka kadhaa nilijiunga na kampuni moja ya umeme kama kibarua kipindi cha kujenga miradi ya umeme vijijini iliyosimamiwa na REA. Jitihada zangu kwenye kazi ngumu za umeme zilinifanikishia kuujua ujuzi wa kazi yenyewe mara baada ya kudumu kwenye miradi zaidi ya miwili mwishowe nikawa najua kila kitu kuhusu ufundi wa kujenga umeme mkubwa. Tabia yangu ya ucheshi na heshima ikawa kivutio cha kupendwa na kila mtu. Na ndipo viongozi wengi wa ‘site’ waliponizoea na kuniita kwenye miradi mbalimbali hadi pale nilipoajiriwa kwenye kampuni moja iliyoitwa Intercity Builders ltd. Sikuamini punde nilipoletewa barua ya kuajiliwa na kampuni hiyo kama fundi daraja la pili tulipomaliza mradi wa Dodoma.
Taratibu hadithi ya maisha yangu ikaanza kuwa nzuri mara baada ya kufika ofisini na kupewa maelekezo yote. Niliiona nyota njema ya ndoto yangu ikiangaza mbele yangu. Mkataba wangu ulikuwa wa miaka miwili sambamba na mshahara wa laki saba. Haikuwa pesa nyingi kwa wenye nazo, lakini kwa mwenzangu na mimi ilikuwa ni zaidi ya tunu ya ndoto. Kiwango cha mshahara ambao sijategemea kama nitakipata nikiwa na umri ule. Miaka ishirini na nne tu! Hakika ilikuwa furaha si kwangu tu bali kwa familia nzima.
“Mwanangu nakupa baraka zote, kafanye kazi utukumbuke baba kuwa makini sana na matumizi ya pesa unaona hali yetu baba. Nakuombea kila la heri baba uende salama.”
Hayo yalikuwa maneno ya mama siku moja kabla ya safari. Usiku ambao tulikesha kuzungumza mambo mengi sana ya kimaisha. Ilikuwa ndio ajira yangu rasmi ya kwanza na kazi ilikuwa jijini Mbeya.
“Usijali mama, nawaahidi sasa ugumu wa maisha tuliyopitia unaenda kuwa kikomo.”
Nilizingatia moyoni na kumuahidi mama huku nikimtoa hofu.
Alfajiri saa kumi na moja mama na dadaangu walinisindikiza hadi Ubungo nilipokutana na mafundi wenzangu wawili tayari kuelekea kazini mkoani Mbeya. Tuliagana na kujumuika na wenzangu huku moyoni nikiwa mwingi wa matumaini. Nilijua fika sitoweza ufanyia mchezo mshahara wa laki saba kwa mwezi. Kila nilipofumba macho niliziona picha za utajiri wangu baada ya miaka miwili ya mkataba. Daaah! Laiti ningelijua juu ya safari ile ndio itakuwa chanzo cha matukio ya kuumiza maisha yangu? Basi nisingelithubutu kukubali kwenda huko wala kusaini mkataba na kampuni ile. Hakika wao ndio walionifanya nipajua Mbeya kwa mara ya kwanza na kunikutanisha na hasidi wa maisha yangu…………
Oooooh! ! NDOA YANGU
Hakika Chozi langu Litalipwa
IMG_20181019_222759.jpg
 
NDOA YANGU (02)
‘Chozi langu litalipwa’
By; KING T CONTROL

Tulisafiri salama hadi Mbeya. Ilikuwa ndio mara yangu ya kwanza kufika mkoa huo ulio nyanda za juu kusini mwa Tanzania. Tulilala Kyela mjini kabla ya gari ya kampuni yetu kutufata kesho yake na kutupeleka ilipo kambi yetu ya kazi Kyela vijijini katika kijiji cha Ipinda.
Huko ndipo maisha mapya yalianza. Tulipokewa vizuri na uongozi wa ‘site’ ambao walitangulia mapema na kujenga ‘yard’ yetu. Wanakijiji pia walitupokea kwa heshima na tulifanya kazi kwa ushirikiano mzuri wa vibalua wa huko ambao ndio walikuwa wenyeji wetu nambari moja.
Kipindi chote nikiwa kazini, jambo kuu nililozingatia ni matumizi ya pesa. Kila siku sikuacha kutafakari jinsi ya kuuchambua mshahara wangu wa mwezi na kujiwekea bajeti ya walau kila mwezi niweke laki tano. Lakini kwa kuwa ujaji wa mshahara nusunusu ulianza kuyumbisha lengo langu la laki tano hadi kufikia laki mbili ama tatu. Mara kwa mara niliwasiliana na mama sababu ndiye alikuwa mtu wangu wa karibu. Kila ilipokuja pesa niliigawanya nusu na kuwatumia huku robo nikiweka na robo nyengine nilifanya matumizi yangu binafsi.
Mtindo wa maisha yangu ya bajeti ukanifanya niwe tofauti na maisha ya mafundi wote. Kwanza sikuwa najichanganya bar kunywa pombe kama ilivyokuwa desturi ya wenzangu mwishoni mwa wiki. Pia hata kama ningeenda huko basi pombe sikugusa kabisa. Vilevile sikuwa ‘kicheche’ wa kutongoza wanawake pale kijijini kama ilivyokuwa kwa mafundi wengi ambao walishobokewa na wasichana mbalimbali. Muda mwingi niliutumia kukaa nyumbani siku za wiki nikibadilishana mawazo na vijana wa lika langu na jioni tulijumuika pamoja mpirani. Mtindo huu wa maisha yangu ukazidi kuwa kivutio na kuonekana kijana wa pekee sana. Miezi ilisonga mbele na msimamo wangu ukawa palepale.
Ingawa kiumli na muonekano mimi ndie nilikuwa fundi mtoto kuliko lakini ndiye nilionesha kuwa na akili kuliko. Simaanishi wengine hawakuwa na akili, hapana ila kwa upande wa matumizi ya pesa wengi walitumia ovyo na ukata ulipowashika walinifata kuwakopesha ihali tulipokea mshahara siku moja na pengine walinizidi kiasi cha malipo. Pesa nilizokuwa natuma kwa mama zilimuwezesha kununua kiwanja maeneo ya Mbezi Marambamawili. Ndoto ya Imani yangu ilikinaisha nafsi yangu. Moyo wa tamaa niliuweka kando na kuupa kipaumbele moyo wa utafutaji. Siku zote nilijiona mimi ni tajiri mtarajiwa.
Siku zilienda huku nami nikijipanga zaidi kule Mbeya kwa kununua vitu vya ndani kuanzia vyombo na majiko ya kupikia, kitanda, godoro, kabati la nguo, tv flati, deki na king’amuzi, sabufa, meza na vitu kadha wa kadha vilivyopendezesha chumba nilichopanga pale Ipinda. Chumba kilishiba machoni mwa kila aliyeingia hata mafundi wenzangu walinishangaa sana.
“Mwanangu ndo umeamua kuyafanya maisha hukuhuku nini utapoisha mradi?” Hilo lilikuwa swali la fundi mwenzangu tuliyezoeana sana. Aliitwa Sultani ama Sulu. Aliniuliza hivyo siku moja tukiwa chumbani kwangu tunatazama tv.
“Hapana Sulu, ila kujiandaa kidogokidogo ni bora kuliko kusubiri cha mkupuo.”
Ndivyo nilivyomjibu na ndivyo nilivyoamini.
Ulipofika mwisho wa mwaka tulipata likizo ya wiki mbili kupisha msimu wa sikukuu za krismasi na mwaka mpya. Safari hii kampuni ilituletea mshahara wa mwezi mzima kwa mpigo sambamba na pesa ya likizo ya mwezi ambayo ilifanana na mshahara.
Kila fundi alituna. Mifuko ilinona. Kwa upande wangu nilikuwa na zaidi ya milioni mfukoni. Kipindi mafundi wenzangu wote na madereva wa ‘site’ wakiwa kwenye mishe za kusafiri kwa upande wangu ilikuwa tofauti. Sikusafiri kwenda popote zaidi nilituma pesa nyumbani za nsikukuu na kumtumia mama nauli aje tule sikukuu pamoja Ipinda jijini Mbeya.
Na kweli sikukuu hiyo mama alijumuika nami. Alifurahi sana kuyaona maendeleo yangu ambayo nilimsuprise sana. Baada ya kupita sikukuu siku moja kabla ya safari ya mama kurudi Dar, aliniweka kitako na kunambia.
“Mwanangu, wewe ndiye tumaini letu nazidi kukuombea siku baada ya siku. Ila kwa hapa ulipofikia ukitaka usonge mbele zaidi na akili yako ipate kivuli, basi unahitaji kuwa na mwenzio. Mtayeendana katika maisha.”
“Nakusikia mama, ila bado sijaelewa unamaanisha nini?” Nilimuuliza ihali nilishahisi lengo la mama.
“Nina maana sasa uoe. Tafuta mke ama nikutafutie mie, mwaka huu kabla haujesha uwe una mke wako. Hapo sasa nitaona kweli mwanangu umekua.”
Maneno ya mama yalinifanya nicheke kwanza nikichukulia anafanya mzaha.
Lakini hata alipoondoka hakuisha kunisisitiza suala hilo la kuoa. Na niliona yuko ‘serious’ zaidi mara baada ya siku moja kunambia kuna binti amemuona ananifaa sana na kama bado sijapata basi atatuma mshenga apeleke posa.
“Hapana mama! Mi nishapata binti wa kumuoa na utapoisha mradi nitakuja nae mumtathmini kabla hatujafanya shughuli nyenginezo za ndoa.” Nilimwambia siku moja mama kwa njia ya simu.
Na hapo sasa kwa mara ya kwanza ndipo wazo la mke likanijia. Maneno ya mama yalizidi kupalia moto kichwa changu juu ya kuoa. Lakini bado ukweli sikuwa na demu wa aina yoyote tokea nikanyage ardhi ya Mbeya. Mwaka ulikatika bila hata kungonoka. Uchovu wa kazi za porini, mawazo juu ya maisha na kutojichanganya vishawishini vilinifanya niliweze hilo. Ingawa nilikuwa rijali niliyekamilika lakini nilijikuta najipa kifungo huru.
Kitu ambacho sikukijua ni kwamba mabinti wengi wa pale Ipinda waliniongelea sana na kunitamani. Na yote yalichochewa na Tuswege. Binti wa Kinyakyusa aliyekuwa anatembea na Sulu. Yeye ndiye alikuwa na mzoea ya kufika chumbani kwangu na bwanake kutazama cd na hata ninapowaachia uhuru walifanya yao. Sikuwa najali sana lakini kumbe alipiga picha nyingi sana za ndani kwangu na kurekodi video kwa simu yake kubwa aliyohongwa na Sulu.
Video na picha alizowaonesha mabinti wenzake na kuwateka hisia na mazingira ya chumba changu yaliyowapagawisha na utulivu wangu uliwamaliza. Walitamani wawe wangu lakini walihofia msimamo wangu.
Ucheshi wangu ulizidi kuwaroga lakini machoni mwangu bado hawakunivutia kuwa karibu nao kimapenzi. Ndoto yangu kuhusu mke niliwazia kuwa na mke msomi, mwenye uzuri wa sura mpaka umbo. Awe na mvuto usiochosha kumtazama. Niliamini mke wa namna hiyo ndie atanifaa maishani kwa kuwa na mawazo chanya ya kimaisha.
Hizo zilikuwa akili zangu ambazo sikuwahi kumshirikisha mtu. Niliamini mawazo yangu nikisahau kabisa maneno ya baba aliyoniusia mara kwa mara kabla ya kifo chake.
Kazi ziliendelea huku mradi ukiwa unaendea mwishoni baada ya kukatika mwaka na miezi kadhaa. Upande wangu na Sulu tulipangiwa kupima maeneo ya kuchimba nguzo za majumbani (lv). Kazi yetu kubwa ilikuwa kunyoosha line na kuhamisha ‘page’ zilizotoka nje ya line ya umeme. Sasa tukiwa katikati ya kazi katika kijiji cha Ndorobo, mbele ya nyumba moja ya nyasi macho yangu yalistushwaq na kitu nilichokiona hata kupelekea mapigo ya moyo kwenda kasi.
Alikuwa ni binti mmoja mzuri sana aliyenivutia asilimia zote machoni mwangu.
Ameketi kwenye kibao akiosha vyombo. Nilisimama na kushangaa uumbaji wa Mungu kana kwamba sikuwahi kuwaona wanawake hapo kabla.
Ingawa macho yenye kupenda hutawaliwa na upofu! Lakini kwa huyu binti nina imani akitupiwa jicho la mwanaume yeyote hata awe mgumu vipi lazima akubaliane nami kuwa ni mzuri. Lakini msemo wa wahenga kuwa ‘si kila king’aacho ni dhahabu’ una maana kubwa sana ambayo wengi huipuuzia.
Oooooh! Atuganile, laiti ningejua kama uzuri wako wa nje ni kiini macho cha ubaya wako wa ndani. Basi ningefumba macho yangu hata nisingekusogelea kabisa……..
Hakika Chozi langu Litalipwa
 
SEHEMU YA 03
Moyo wangu ulijikuta unakubaliana na macho yangu hata kuzipeleka mbali fahamu zangu kila nilivyomtazama binti ambae mpaka muda huo hakujua kama kuna mtu jirani yake.
“Mambo!” Nilijongea karibu na kumsalimu. Kwa sauti ya kumtoa nyoka pangoni alijibu huku akisimama na kunionesha heshima. Hakika hapo alizidi kuniroga kabisa. Niliushuhudia uzuri wake wa mwili timilifu pindi aliposimama. Kifuani matiti yake madogo ya mviringo yenye chuchu mchongoko yalisimama vizuri ndani ya fulana ya jezi aliyokuwa amevaa muda huo. Ingawa chini alijifunga kitenge lakini haikuficha uzuri wa umbo alilokuwa nalo. Namba nane yani ile namba yenyewe hasa.
Nakumbuka nilimuuliza swali ambalo halikuwa kwenye mawazo yangu kabisa.
“Eti mjumbe wa mtaa huu ni nani?”
“Anhaa! Mna shida na mjumbe.. mjumbe ni mamaangu ila sasa hivi yuko shamba!” alijibu huku nikizidi mchunguza uzuri wake. Sauti yake ilinikosha kila alipoongea niliuona uwema Sepetu mdomoni mwake.
“Oooh! Kumbe wewe mtoto wa mjumbe? Unaitwa nani mrembo?” Nilileta uchakaramu kuutuliza mtima wangu uliobadili mapigo huku nikitazama nyumba yao ya nyasi ambayo juu kulikuwa na bendera ya chama cha mapinduzi.
Alitabasamu na kunitazama kabla hajajibu, tulikutanisha macho.
“Naitwa Atuganile.” Alijibu kwa haiba ya kike huku akiinamisha macho chini. Sijajua haraka ni aibu au yalikuwa mapozi yake. Nilizidi kumuuliza maswali kana kwamba yeye ndie alikuwa mjumbe.
“Hivi wewe ni mwenyeji kweli wa huku?” Nilimuuliza swali kutoka moyoni kabisa maana kwa jinsi nilivyomazama Atuganile hakufanana kabisa na mazingira yale. Nathubutu kusema hakustahili kuwa mtoto wa mkulima kwa jinsi alivyo kimuonekano. Alitakiwa aishi kama mtoto wa malkia. Lakini bila kupepesa Atu alinijibu ukweli.
“Ndio, mimi ni mwenyeji sana ila tu nilikuwa shule Kyela.”
“Oohooo! Kwa hiyo sasa umemaliza?”
“Hapana tupo likizo. Mwakani ndio naingia form 4.” Alinijibu na kunifanya nipunguze kasi ya maswali baada ya kubaini kumbe nazungumza na wakusoma.
Lakini moyo mwengine bado ulinisisitiza kuwa huyo ndiye mke wa kuoa. Nilijikuta natumia zaidi ya robo saa kuzungumza na Atuganile pasipo kufanya kazi. Sulu nae kumbe hakuwa mbali. Aliniona muda wote nikizungumza na mtoto pasipo kutema sumu zozote zaidi ya kumuuliza maswali. Ukweli sikumtongoza siku hiyo zaidi ya kumuacha na kumuahidi tutakuja jioni kuzungumza na mjumbe ambae ni mamaake juu ya mipango yetu ya umeme kijijini kwao.
Huo ndio ukawa mwanzo wa kumfahamu Atuganile Mwakyusa. Binti mrembo wa Kinyakyusa. Binti aliyejawa haiba ya kike machoni ukimtazama. Sauti yake ya laini ya upole utapenda pindi aongeapo. Umbo lake mashruti akitembea hutochoka kumuangalia. Yaani hata akikupita lazima ugeuke. Hakika Atuganile alikuwa kifaa haswa. Hata Sultani Rwambo rafikiyangu tuliyekuwa pamoja siku hiyo alikiri kuwa kama nitafanikiwa kumng’oa Atuganile basi nitakuwa nimeokota dodo chini ya msufi.
Jioni ya siku hiyo ya kwanza kumuona nilirudi kama nilivyomuahidi Atuganile. Safari hii nikiwa nimevaa nguo za kiraia tofauti na awali nilipokuwa na maovaloli ya kazi.
Nilikodi pikipiki pale Ipinda nikamchukua mshkaji wangu Sulu na kuelekea tena kule kijijini. Ilikuwa yapata saa moja kama sio mbili za usiku. Tulifika na kupokewa vizuri sana. Kiukweli hata mwenyewe nilishangaa, mama Atuganile alikuwa mcheshi mno.
“Karibuni kina baba! Karibuni sana.” Alitukarimu na kutuwekea vigoda. Tulikaa huku mie nikiwa ndiye msemaji mkubwa nilizungumza na mama Atu kuhusu taratibu zetu za umeme kijijini kwao.
“Mama ukiwa kama mjumbe, tunakuomba uwaambie wakazi wako kuna vimti tumevichimbia maeneo mengi jirani na makazi yao vikiwa na rangi nyekundu, wasiving’oe. Maana hizo ndizo nguzo za umeme zenyewe! Eneo lenye kimti ndipo kutachimbwa shimo la nguzo hivyo waelewe hatujavieka kimakosa.” Nilimwaga swaga ya ujio wangu kwa mjumbe huku nikisikilizwa kwa umakini mkubwa na mama Atuganile. Alinielewa na kunitoa wasi.
Kutokana na ucheshi wa mama Atu ulinifanya nijisikie huru moyoni na kuchomekea uchakaramu wangu.
“Sasa mama mkwe sisi tunaenda ila kesho itabidi na mke wangu aende shamba na yeye asizoee kushika kalamu tu ajue na kushika jembe.”
“ha ha ha! Nani Atuganile.”
“Eeeh! Au una warembo wengine mama!”
“Enhee kuna mdogoake yuko chekechea huyo ndie mlimaji haswa kama unataka mkeo alime.”
“ha ha ha ! mama bwana!basi msalimie mzee mwambie tukishawawashia umeme nitaoa wote.” Niliendelea kutania lakini safari hii kidogo mama Atuganile aliongea kwa upole na si kwa sauti ya utani.
“Mimi ndie baba mimi ndie mama! Wenzako hawa yatima ndio maana namsisitiza sana Atu mwanangu asoime kwa bidii elimu ndio ulithi wake pekee. Hawana baba namie mama yao sina mbele wala nyuma.”
“Daah! Pole sana mama ila usiseme hivyo unaniumiza. Mungu ni mwema na anawapa mitihani wale awapendao ili wazidi kuwa jirani nae kwa kumtaja mara kwa mara. Tusichoke kumuomba na kumtumaini mama.”
Nilinena maneno kama mchungaji wa kanisa na kumfurahisha sana mama Atuganile ambapo alinionesha tabasamu la dhahiri shahiri kutoka moyoni.
“Basi msubiri kula, Atu mkeo yuko anakarangiza jikoni. Au hampendi chakula cha kunukia moshi? Mshazoea majiko ya ueme huko kwenu?”
“Hamna mama, tunapenda sana ila tutakula siku nyengine mama etu.”
Tulimjibu pamoja na Sulu ambae muda mwingi a;likaa kimya.
Niliwasha pikipiki, Sulu akapanda tukawaaga na kuondoka huku moyo wangu ukiwa umesimama dede kwa furaha na kuiona njia ya kumpata Atuganile ikizidi kuwa nyeupe.
Ingawa mama Atuganile alichukulia kama utani lakini moyoni mwangu nilichukulia ndivyo ilivyo kwa asilimia mia.
Atuganile ndie mke wangu wa maisha. Mwanamke aliyeishi kwenye ndoto zangu muda wote sasa nilijua nimeshampata.
Hata Sulu alinipongeza sana na kunihakikishia kuwa yule mama nyota zetu zinaiva sana.
“Yaani One, muda mfupi tu mmezoeana hata kufikia utani wa namna ile? Hakika nakuhakikishia yule demu ushindwe mwenyewe tu lakini ni wako asilimia mia.”
Maneno ya Sulu yalizidi kunichagiza ushindi. Tabasamu moyoni halikukauka. Muda wote niliiona picha ya Atuganile kichwani mwangu.
Hakika nilimuandalia pumziko kubwa sana la faraja. Lakini looooool! Kweli neno ‘laiti ngejua’ huja baada ya tendo.
Ooooooooph! NDOA YANGU….. Hakika ni zaidi ya msiba
 
SEHEMU YA 04

“Yaani One, muda mfupi tu mmezoeana hata kufikia utani wa namna ile? Hakika nakuhakikishia yule demu ushindwe mwenyewe tu lakini ni wako asilimia mia.”
Maneno ya Sulu yalizidi kunichagiza ushindi. Tabasamu moyoni halikukauka. Muda wote niliiona picha ya Atuganile kichwani mwangu.
Hakika nilimuandalia pumziko kubwa sana la faraja.
Mazoea baina yangu na mama Atuganile yalipozidi ndipo yalinipa nafasi zaidi ya kumtania Atu. Nilifanya utani wenye ukweli ndani yake. Bado nilikuwa navutia pumzi jinsi ya kumtobolea Atu undani wa utani wangu ili naye asichukulie utani kabisa.
Nakumbuka huo ulikuwa mwezi wa saba mwanzoni. Wiki moja tu tokea nimuone Atuganile. Kabla hata sijamfaidi vizuri wala kumtobolea ya moyoni ndipo siku hiyo jioni nilipopitia kwao nilishangaa kuambiwa na mamaake kuwa ameshasafiri amerudi shule. Hakika katika siku niliyonyong’onyea basi ilikuwa hiyo. Ingawa nilijibalaguza mbele ya mama Atu na kujifanya kawaida huku nikimuombea asome kwa amani, lakini moyoni niliumia sana.
“Daaah! Inakuaje ameondoka kabla sijamwambia juu ya ukweli wa utani wangu?” Nilisema na moyo wangu lakini sikuwa na budi kunyamaza. Nilijilaumu sana na kujiona ni mjinga nisiye na bahati. Nilijua mradi unaelekea mwishoni na huenda tukamaliza kabla ya Atuganile kurejea tena pale kijijini. Nilitamani kumuuliza mamaake kama Atu anayo simu basi anipe namba zake. Lakini moyo ulinisuta na kunikumbusha heshima mbele ya mama mwenye ndoto za kuona bintie anasoma. Na hapo sasa ndipo nilipozidi kudata na kuanza upelelezi wa kujua rafiki wa karibu na Atuganile ili ikiwezekana nipae mawasiliano yake au hata nipajue shule anayosoma huko Kyela.
Moyo wa kupenda ulikuwa tayari hata kumtembelea shuleni kwao muda wowote pasipo hofu wala mashaka.
“Oii! Ambokile eti vipi kuhusu yule demu wako mtoto wa mjumbe pale kitaani kwenu? Mbona simuoni siku hizi..?” Nilianza upekenyu wangu kwa dogo mmoja ambae alikuwa miongoni mwa vibalua wetu aliyeishi mitaa ileile ya kina Atu.
“Demu wangu mtoto wa mjumbe? Sio kweli kaka Onesmo unamaanisha Atuganile?”
“Ndie bwana usinifiche mbona mkanda wako ninao.”
“ha ha ha haaa! Duh sio kweli kabisaaa. Hata mazoea nae sinaga.” Alijibu Ambokile na kuzidi nipa nafasi ya kumpekua ili niweze kujua mengi zaidi kuhusu Atuganile.
“Hivi Ambokile mtaani kwenu nani anakula yule mtoto.”
“Mh! Sio siri bro Onesmo uongo dhambi yule mtoto kichwa sana. Hapa kijijini yeye tu ndie alifaulu kwenda sekondari huko Kyela na ametulia balaa. Sijui labda huko shuleni kwao. Lakini kwa hapa Mtakuja hata Ipinda nzima nina hakika hakuna kidume anayemmiliki yule mtoto. Kwanza akija kutwa yupo kwao.. akitoka ameenda kanisani ama kwa kina Siwa.”
Maneno ya Ambokile yalizidi kunipa mwanga juu ya Atuganile. Moyo wangu ulizidi kufurahi na kujipongeza kuwa nimependa sehemu sahihi kabisa.
“Siwa..siwaaaa! okey yule mtoto wa mchungaji eeh!”
“Ndio huyo.”
“Sasa Ambokile naomba unisaidie kitu. Fanya kila uwezavyo muingie Siwa tupate namba ya Atuganile.”
Mwishowe ilibidi nimtobolee Ambokile ili anisaidie kupata namba ya simu ya Atuganile. Hilo aliliitikia Ambo lakini baada ya jitihada zake zote mwishowe ilishindikana. Jibu nililopata ni kwamba Atuganile hana simu.
Nilichoka kwa kweli. Nilianza staa aliyeanza mpambano vizuri akielekea kushindwa dakika za mwisho. Kichwa kiliuma moyo wa matumaini ulianza kufifia mwangaza.
Lakini nakumbuka siku hiyo nikiwa sina lile wala hili tuko site mara simu yangu iliita. Ilikuwa kipindi hiko tunasimamisha nguzo za mitaani (lv). Iliita mpaka ilikata yenyewe na kuanza kuita tena, lakini umakini wangu kazini niliuweka kipaumbele kuliko simu. Ingawa nilisikia mtetemo wa muito wake pindi ikiwa mfukoni lakini sikuwa na haraka kuipokea hadi tukio muhimu lililokuwa linaendelea muda huo limalizike.
Ndipo baadae muda wa mapumziko na kula chakula cha mchana niliitoa simu kuangalia nani alinipigia masaa kadhaa yaliyopita. Niliitoa simu na kukuta namba ngeni na kuamua kupiga. Baada ya kuita na kupokelewa upande wa pili nilisikia sauti ngeni ya kike.
“Hallow! Samahani ulinipigia ila nilikuwa bize sikupokea. Ningependa kujua nani mwenzangu?” Niliuliza baada ya mpokeaji nae kuniuliza.
“Mh! Hapana, ujue simu hii kuna wanafunzi tofauti hapa wakija kula huitumia kupiga kwa ndugu zao. Inawezekana kuna mwanafunzi alikupigia…”
Ilinijibu sauti ya huyo mdada na kunichanganya huku nikifikiria mwanafunzi anipigie mimi? Mwanafunzi gani huyo.
“Kwani hapo wapi?” niliuliza.
“Hapa Kyela kaka shule ya sekondari.” Jibu la dada wa kwenye simu lilinifanya ninyanyuke pale nilipokaa na wenzangu na kusogea pembeni zaidi huku mapigo ya moyo wangu yakizidisha kasi. Nilikumbuka mtu pekee aliyewahi kunambia anasoma Kyela ni Atuganile. Mwanamke wa ndoto zangu. Ina maana leo amenitafuta ama kuna mwanafunzi mwengine alikosea namba?
Nilijiuliza maswali mengi ndani ya sekunde chache.
“aahaa! Au Atuganile?” niliuliza kwa shauku kubwa moyoni mwangu huku viungo vyote vya mwili wangu vikizizima kwa sekunde chache kuyaachia masikio utulivu mkubwa wa kusikia jibu la dada wa kwenye simu juu ya huyo mwanafunzi wa Kyela aliyenipigia.
“Enhee nimekumbuka. Ni Atuganile ndio.. Atuganile alinipa maagizo kama ukipiga nikwambie.”
Jibu lake lilinitoa chozi la furaha sijui niliite chozi la huba...? Njaa yote iliniisha. Shibe ya kusikia nimetafutwa na Atuganile ilinijaa mwilini.
"Dada naomba Atuganile akija hapo anipigie tafadhali?"
Nilisisitiza sana. Ama kwa hakika siku hiyo sikula kabisa na wala sikuchoka kazini. Mwili wangu ulikuwa na nguvu vilevile. Akili zangu zilikuwa safi kama nimezaliwa upya. Moyo wa matumaini ulinivaa tena. Shauku ya kuongea na Atuganile haikukatika mtimani mwangu.
Kuanzia hapo sikuisha kuwa msumbufu kwa yule dada mwenye simu ambaye alinielekeza kuwa ni mpishi pale shuleni. Mara kwa mara nilimpigia kumuulizia Atu ambae kila nikipiga nilimkosa wala nae hakunitafuta siku hiyo tena.
Wiki ilikatika hadi mwisho wa wiki tena ndipo ile namba ilinipigia. Tena nakumbuka siku hiyo nilikuwa juu ya nguzo. Almanusura nipuluchuke baada ya kutazama namba ya mpigaji na kuona ni ile ya mpishi wa shule.
"Hallow! hallow Atuganile wangu?" Niliita baada ya kupokea.
Sauti upande wa pili ilisikika. Haikunipa tabu hata kidogo kuuliza kwa utamu wa sauti husika. Nilijua fika ni Atuganile tu. Binti mwenye sauti ya kinanda cha kumtoa nyoka mafichoni.
"Hallow mambo!" Alinisalimu huku nikiwa siamini kama kweli ni mimi leo hii naongea na binti mchoma mtima wangu.
"Atuganile siamini kwa kweli kama naongea na wewe mke wangu."
"Acha utani bwana. Nasikia uliniulizia kwa mama ndio akanipa namba yako." Alinambia na kuanza kupata wazo kuwa namba yangu aliipata kwa mamaake ambae alikuwa nayo siku za nyuma baada ya kuwa na mazoea naye.
Siku hiyo ndiyo niliyotoboa ukweli wa moyo wangu juu ya Atuganile. Nilimwambia kitu ambacho sikuamini alivyonijibu.
"Atu, ukweli wa Mungu nakupenda sana na wala sikwiti mke kama utani hapana, bali nia yangu ukimaliza shule nikuoe uwe wangu wa maisha. Niko tayari kukuendeleza hata kielimu mamy naomba uelewe nisemacho si utani kabisa."
Nilipumua kidume nikisikilizia jibu la Atuganile na alichokijibu nilichoka kwa kweli............
 
SEHEMU YA 05

"Onesmo usinichekeshe bwana. Ukweli naomba uelewe kuwa katika kitu ambacho hakijawahi kuwa akilini mwangu wala sina mpango wa kukifikiria basi ni mapenzi sijui mchumba au mume! sijawahi kujihusisha wala sitarajii kwasasa nawaza kusoma tu. Elimu ije kutukomboa. Ila nashukuru kwa kumsaidia mamaangu lakini usitumie hiyo kuwa sababu ya kukupenda ama kukubali ushawishi wako. Hapana! kama nia ya msaada wako kwetu ndiyo hiyo basi naomba kuanzia leo usipeleke chochote kwa mama wala usinitafute tena. Kwaheri." Alikata simu Atuganile na kuniacha kinywa wazi.
Nilimpiga lakini simu ilikatwa. Nilipiga tena nikaambiwa kashaondoka. Nilichoka!
Nilijilaumu kwa haraka zangu za kumwambia yale kwa njia ya simu. Lakini pia sikuwa na budi sababu nilijua mradi unaelekea mwishoni na huenda tukaondoka kabla ya kuonana tena na Atu wangu.
Niliumia lakini sikukoma kumpigia simu kwa ile namba lakini jitihada zangu za kuongea nae ziligonga mwamba kila nipigapo. Ikafika hatua hata nilikuwa namboa yule dada mwenye simu.
"Kakaangu ni vyema tukaheshimiana! unanigombanisha na mpenzi wangu kwa simu zako za mara kwa mara. sasa hadi usiku unapiga simu ikiwa unajua kuwa kina Atuganile nakutana nao mchana. Pia kama atahitaji kuzungumza nawe yeye ndie atapiga. Naomba usinipigie tena mpenzi wangu hanielewi sababu yako."
Aliniwakia siku moja yule dada baada ya kumpigia usiku walau kujua kama kina Atu alionana nao siku hiyo na alimpa ujumbe wangu. Sikuwa na budi zaidi ya kuomba radhi na kuwa mpole. Niliacha kumpigia tena yule dada ingawa moyo wangu ulitamani kujua habari za Atuganile. Muda wote masikio yangu yalikuwa makini pindi simu iitapo niliwahi kuangalia namba ya mpigaji nikihisi Atu amenitafuta tena, lakini haikuwa hivyo.
Huo naweza kuthubutu kusema ndio ulikuwa mwanzo na mwisho wa kuzungumza na Atuganile kwa njia ya simu pindi akiwa shule anasoma.
Siku zikaenda, nikajifunza kumsahau Atuganile kama alivyohitaji mwenyewe.
"Mwanamke mzuri si Atu pekeake ndugu yangu kuna wazuri wengi kuliko yeye. Ni ujinga unavyojikondesha kumfikiria mtu ambae hata mwaka haujafika tokea umemjua. Huyo si riziki yako One achana nae utakufa bure na mawazo ya kupenda ujinga."
Hayo yalikuwa maneno ya Sulu yaliyonichochea ujasiri wa kumsahau Atuganile. Kuna muda nilijiuliza inakuwaje nilimpenda kiasi kile? ilikuwa ajabu kwa kweli.
Miezi ikasonga hatimaye ulibaki mwezi mmoja tu wa mradi kumalizika. Nakumbuka ilikuwa mwanzoni mwa mwezi wa kumi na mbili.
Siku hiyo nikiwa tunamalizia kuunga nyaya. Nikiwa nimeamka mwenye afya kabisa na kujumuika na wenzangu kazini kama kawaida. Nakumbuka vizuri ilikuwa katika kijiji kilekile cha Mtakuja ndani ya Ipinda wilaya ya Kyela mkoani Mbeya. Ilikuwa majira ya saa tatu za asubuhi, Ndio kwanza tulikuwa tumefika 'site'.
Tukiwa tunatembea kuelekea tulipofunga transfoma, ndipo nilishangaa kuona kitu cha ajabu kikitokea mbele yangu. Kitu ambacho kilikuwa kama ndoto ayotayo mtu aliye macho.Ndoto ya ajabu na ya kutisha isiyostahili kuitwa ndoto. Ilikuwa ni hali halisi kabisa kwa maono yangu lakini sivyo ndivyo ilivyokuwa inatokea kwa maono ya wenzangu tuliokuwa pamoja.
Nakumbuka kitu cha kwanza chaajabu nilichokiona eneo tulilokuwa tunapita ambapo kulikuwa na shamba dogo la mahindi yaliyostawi ukijani, niliona ghafla mahindi yote yakipoteza hali ya ustawi wake na kuanza kunyauka kana kwamba yamepigwa na jua kali kupita maelezo. Nikiwa natembea tena huku nazungumza na wenzangu nilishangaa na kujaribu kuipotezea hali ile akilini mwangu nikihisi labda mawenge yangu tu. Lakini ajabu kadri nilivyopiga hatua ndivyo yale mahindi yalivyozidi kunyauka na hatimaye yakaanza kutoweka kabisa mithili ya nailoni iyayukayo kwenye moto.
Nilijikuta nasimama kwa staajabiko la mwaka. Wenzangu waliendelea kusonga mbele wakiwa hawana shaka nami. Bumbuwazi lilinipiga zaidi baada ya kuona hata wenzangu nao wakipotea katika uso wa ulimwengu na kujiona nikiwa mwenyewe ndani ya ulimwengi wa ajabu usiokuwa na kitu chochote chenye uhai wala jani bichi. Ilikuwa sehemu ya jangwajangwa. Sehemu iliyoshiba ukame. Sehemu isiyofaa kuwa makazi ya kiumbe yoyote hai.
Nikiwa naanza kuchanganyikiwa kwa kile kinachotokea kwenye mboni zangu, ghafla sekunde zilezile kwa mbali nilishuhudia ardhi ikipasuka na kuibuka kiumbe wa ajabu sana. Kiumbe wa kutisha akija kwa kasi kule niliko mara tu alipoibuka. Alikimbia mwendo wa kishari. Uso wake mbovu wa umafia ulionesha wazi alikuwa amenilenga kuja nifanyia unyambizi. Lilikuwa ni jitu moja kubwa sana kama jitu la kale. Nywele nyingi timutimu zilishona kichwani mwake huku akiwa kavaa manguo makubwa yaliyofanana na ukame wa eneo zima. Ngozi yake ilishiba mpauko wa jangwa kuonesha yeye si kiumbe wa kawaida. Sikujua kama ni shetani ama jitu la kuzimu.
"SUUULUUUUU"
Niliita kwa sauti kuu nikijaribu kuomba msaada kama kuna mtu ananisikia katika ulimwengu wa kawaida lakini sikusikia majibu yoyote wala kuona dalili za kusaidiwa zaidi ya kushuhudi jitu likizidi kunikaribia.
"Nikizubaa nitakufa kizembe!" Nafsi ilitoa sauti iliyoungwa mkono na viungo vyote vyaq mwili. Kwa ujasiri wa hali ya juu punde yule kiumbe aliponikaribia na kunirukia kwa nguvu nilijikuta namkamata shingo juuu kwa juu huku naye akinikamata shingo na tukaanguka chini kama mafurushi.
Alinikaba kooni nami nikamkaba kooni kisawasawa. Kwa nguvu zangu zote. Niligumia maumivu na kuzidisha kumkaba na yeye.
Kumbe kipindi nadondoka kina Sulu waliniona wakiwa kwenye ulimwengu wa kawaida. Wote walishangaa na kunikimbilia. Walikuta nikitetema mwili mzima mithili ya mtetemo wa simu. mtetemoi ulioweza kuusukuma mwili sehemu moja kwenda nyengine. Wao walinishika na kuniita huku kila mmoja akiwa katika hali ya kuchanganyikiwa sana.
Lakini kwa ulimwengu nilokuwepo mambo yalikuwa mengine. Nilikuwa katika vita nzito na kile kiumbe chaajabu kilichodhamiria kuinyofoa nafsi yangu.
Tumaini la imani ya kushinda halikuniisha nafsini ingawa maumivu ya kukabwa yalikuwa hayavumiliki. Sikumbuki ilikuwaje baadae kwani nilihisi kupoteza fahamu nikiwa kwenye ulimwengu ule wa ajabu. Lakini kwa hali halisi upande wa kina Sulu walichanganyikiwa na kuwaita viongozi waliokuwa eneo la pili la kijiji wakiendelea kukagua kazi ya mradi. Fomeni wetu akiwa na Injinia aliyekuja siku mbili tu za nyuma walifika haraka sambamba na dereva. Wote walishangaa kwa hali waliyoikuta. Nilikuwa bado kwenye mtetemo wa ajabu mithili ya jenereta.
"Mvueni viatu na mkanda! Chinga leta gari haraka daaah! wee Sulu imekuwajeee?"
Alichanganyikiwa fomeni na kuuliza huku akiwa haelewi wala haamini kile akionacho. Ingawa hayo yote nilikuja kuyajua baadae sana kwa kilichokuwa kinatokea, lakini ukweli ulikuwa kwa muda huo sikuwa nasikia wala kuhisi chochote kwenye ulimwengu. Nilikuwa sehemu tofauti kabisa. Hata walivyonihangaikia hata kuniweka kwenye gari ya kazi na kunikimbiza hospitali sikuwa najua wala kuhisi chochote. Nilikuwa nusu mfu nusu mtu.
Kila aliyesikia juu ya tukio lililotokea asubuhi ile kwa fundi umeme alishangaa sana na aliumia zaidi aliposikia kuwa mpatwa tukio lenyewe ni mimi. Kijana niliyesifika utulivu na heshima. Kila mtu aliyenijua na hata asiyenijua alizijua sifa zangu. Hii iliwatoa machozi wengi na kushika tama pindi nikikimbizwa hospitalini ihali bado sijafa.
Nilifikishwa hospitali ya Ipinda ambapo baada ya daktari kunifanyia uchunguzi alionesha wasiwasi mkubwa. Ingawa nilitundikiwa dripu lakini hali yangu ilizidi kukatisha tamaa. Mwishowe niliacha kutetema na macho yakaanza kubadilika kwa kuingia ndani. Hapo ndipo vilio vilipoanza hospitalini palepale. Hata daktari aliyenipokea alionesha dariri zote za kukata tamaa na kumwambia fomeni kuwa hospitali yake ni ndogo, hivyo ni vyema nipelekwe hospitali ya wilaya Kyela kwa kuwa pale hata mochwali haikuwepo.
Kauli ya daktari kuitaja mochwali ndiyo ilipelekea fomeni atoe machozi na kulia kama mtoto. Daaaah! mafundi wenzangu na vibarua nao kila mmoja alijitenga upande wake akilia kivyake. Walinililia na kushangazwa kwanini nakufa ghafla vile! Nini kinaniua? Yaani tena nakufa katika hatua za mwisho kabisa za kula matunda ya mradi? Hii iliwachoma wengi hasa pale ilipofika gari ya wagonjwa na kubebwa nikiwa nimetulia tuli sitingishiki. Pumzi zangu zilikuwa zinatoka kwa mbali sana tena kwa shida. Hospitali nzima na Ipinda yote ilizizima kwa huzuni huku habari ya tukio langu ikisambaa kwa kasi kama umeme hata kufika shuleni kwa kina Atuganile.
Aaaaaagh! ama kweli mtu ujuae anakupenda kwa dhati na asiyechoka kukusaidia kwenye heri! utamringia kipindi akiwa mzima anasema..lakini ukisikia yu mahututi ama amekata kauli...Lazima nafsi itakusuta kwa upande mmoja utahuzunika na kuyakumbuka mazuri yake yatayokuchoma moyo kwa kutomlipa hisani yake hata kumwambia asante hadi ameondoka. Aaaaaaah Atuganile! hakika mshtuko wako ulikuwa na maana kubwa.
 
SHEMU YA 06

Taarifa za kuanguka kwangu na kukimbizwa hospitali hatimaye zilifika jijini Dar kwa mama na ndugu zangu. Wote walichanganyikiwa hususani mama alilia na kuomba kwa Mungu nipate uponyo kutoka kwenye hali hiyo. Siku hiyo hiyo walipopata habari walitamani wapae wanione. Lakini ikashindikina zaidi ya kukata tiketi ya basi ya kwanza kesho yake. Siku nzima mama alishindwa kula zaidi ya kunifikiria. Ama kweli kifo cha mtoto humrejeshea mama uchungu wa uzazi.
Nilifikishwa Kyela nikiwa vilevile mahututi na moja kwa moja kukimbizwa chumba cha daktari. Madaktari walifanya kile walichokijua huku nikichukuliwa vipimo vyote muhimu mpaka vya moyo. Lakibni kitu kilichoiwashangaza madaktari ni kwamba sikuonesha tatizo lolote mwilini mwangu. Yaani chaajabu hata bp sikuwa nayo.! Hii iiwashangaza na kuwapa maswali inakuaji pumzi zangu kuwa chini halafu presha kuwa kawaida tu?
Lakini kwa kuwa sayansi ni pana na hawawezi kuniruhusu ihali niko mahututi! ilibidi nipelekwe kwenye chumba maalum cha wagonjwa. Huko niliwekewa dripu lengine sijajua lilikuwa la maji ama dawa gani. Masaa yakasogea hadi jua likazama pasipo kufumbua macho wala kutingisha kiungo chochote cha mwili. Fomeni wetu alikaa na mimi pale nilipolazwa muda wote akisali na kuomba nafsini mwake nisife moja kwa moja. Naweza thubutu kusema kwa hali niliyokuwa nayo kilichokuwa kinasubiriwa ni vipumzi vichache nilivokuwa navyo vikatike.
Wakati huo katika ulimwengu ule wa ajabu uiliogubika fahamu zangu matukio yaliendelea. Nilistuka baada ya kuzima. Nilijiona kwenye chumba kimoja kizuri huku pembeni yangu akiwa amekaa mwanamke nimpendae sana. Mwanamke huyo alikuwa Atuganile. Akiwa ananikanda kanda kwa kitambaa cha maji vuguvugu sehemu za kichwani huku akinisindikiza kwa sauti yake tamu ya kinanda.
"Oooh! umeamka! pole mume wangu!" Alinifariji huku akiniuliza ninavyojisikia.
Nilizidi kushangaa na kujiuliza imekuwaje tena niwe na Atuganile tena sehemu nzuri kama ile ihali nilikuwa nimepambana na jitu la ajabu? Tena ajabu zaidi sijajua nililishindaje hata kuniachia na kuwa na Atuganile muda ule! tena si Atuganile mtoto wa mjumbe! bali Atuganile mke wangu.
"Nimekuandalia juice ya parachichi uipendayo mume wangu." Aliongea Atu.
"Hivi ulimuona na wewe?" Nilimuuliza nikimaanisha kile kiumbe cha kutisha kilichonivamia.
"Ndio mume wangu nimeliona limaiti lake...ila hakika wewe shujaa, kweli nimepata mume bora."
"Atu ni kweli sasa umekubali kuolewa nami?"
"Jamani One wangu! au amekukaba sana hadi umepoteza kumbukumbu? sasa niolewe nawe mara ngapi baby? pumzika basi kwanza naona bado hauko sawa." Kauli za Atuganile zilizidi kunishangaza na kuniumiza kichwa huku nikifikiria tukio la kumuoa likiwa halipo kabisa kwenye kumbukumbu zangu. Nikitazama uzuri wa chumba na ukutani niliiona picha kubwa ya harusi tukiwa mimi nimevaa suti huku Atu amevaa shela.
"Haa!" nilishangaa nafsini huku upande mmoja nikikumbuka kuwa mbona nilikuwa kazini asubuhi tena bado nilikuwa Mbeya?
Atuganile akiwa ametabasamu aliniinamia na kunibusu kwa huba huku akinisisitiza nipumzike kwanza nilale.
"Pumzika mume wangu bado hujakaa sawa! ukiamka utaelewa kila kitu baby!" Nilijilazimisha kufumba macho huku nikiwa nimechanganyikiwa ndani ya ulimwengu ule uliokuwa unanilazimisha kuuamini na kuusahau ulimwengu wa kawaida ambao bado kiuhalisia nilikuwa hospitalini sina fahamu.
Saa zilizogea hatimae ilitimia saa saba usiku. Fomeni akiwa hana hata lepe la usingizi. Macho kodo akinitazama kwa umakini nilivyotulia huku pumzi zangu zikiwa haziongezeki wala hazipundui nzaidi ya pale. Madaktari kila baada ya dakika kadhaa walifika kunikagua. Fomeni alishakata tamaa juu ya uzima wangu huku wengine wakiwa wanapeana taarifa za chinichini kuwa tayari nimeshakata roho ila uongozi unasita kutangaza haraka haraka hali halisi na kilichobaki wanaweka mipango sawa na taratibu za kuusafirisha mwili wangu kwa mazishi. Hivyo kila mtu hususani mafundi walikaa tayari kwa safari wakisubiria asubuhi ifike wapate habari za uhakika juu ya kifo changu cha ghafla na ajabu.
Lakini hali haikuwa kama walivyodhani. Mwenyezi Mungu ndiye mpangaji wa kila kitu. Tunapata matatizo kwa rehma zake na tunapata neema kwa rehma zake pia. Yeye ndiye muamuzi mkuu na wa mwisho. Na hilo lilithibitika majira hayo ya saa saba za usiku. Zaidi ya masaa kumi na sita tokea nipatwe na zohari ile saa tatu asubuhi.
Katika fahamu zangu sasa nilifumbua macho kuamka ili nijue vizuri ukweli wote wa picha lilivyokuwa kama alivyonambia Atuganile! lakini ajabu nilikuta nafumbua macho na kuona mazingira tofauti kabisa na nilipozinduka mara ya kwanza. Hakuna Atuganile wala sio kwenye chumba kile kizuri cha kuvutia. Nilizidi kudata fikrani mwangu bila kujua sasa ndio nilikuwa nazinduka kikwelikweli katika ulimwengu halisi wa dunia. Kila nilivyopepesa macho niliona neti neti nyingi, vitanda vingi, na zaidi kilichonishangaza kumuona kukutanisha macho na fomeni aliyeonesha mshtuko wa waziwazi na kumuita daktari kwa sauti ya juu.
"DOKTAAA..DOKTAA!"
Hapo ndipo fahamu zangu zikabaini kuwa kumbe pale ni hospitali. Lakini yu wapi Atuganile? mbona naziona picha mbili tofauti katika tukio moja? Daktari alifika akiwa ameongozana na muuguzi mmoja.
"Onesmo..Onesmo! unanisikia vizuri?" aliniita daktari na kuniuliza.
Lakini nilipojaribu kusema nilijikuta nashindwa kabisa. midomo ilishindwa kunyanyuka ingawa fahamu ilikuwa sahihi kile nilichodhamiria kusema. Nilipotaka kumeza mate nilijikuta yanarudi kabisa kwa maumivu makali niliyoyahisi kooni. Nikataka kunyanyuka lakini loooooooool ndio kabisa hata mkono kuunyanyua ilikuwa shida. Mwili mzima ulikosa nguvu na mawasiliano.Niliuhisi kama mwili wangu umepondwapondwa. Kitu pekee nilichoweza ni kupepesa macho kwani hata shingo nilishindwa kuigeuza. Sauti pia haikutoka mbali ya kushindwa kusema. Kitu pekee kilichoweza kutoka yalikuwa ni machozi. Machozi yaliyotabanaisha maumivu makuu niyapatayo. Machozi ya hamaniko na sikitiko la nafsi kwa mateso yaajabu yaliyonikumba ghafla.
Yaani asubuhi tu nilikuwa nina nguvu zangu, nafanya kazi zangu mwenyewe, tena naongea na kucheka vizuri tu? lakini llol ama kweli binaadamu sisi si kitu kabisa. Uhai ni kitu kidogo mno kitudanganyacho kama kitadumu nasi milele kumbe kinaweza kuponyoka muda wowote. Nilijiuliza au huenda nimepooza?
"Hee! ndio mama, amezinduka muda si mrefu hapahapa hospitali ya wilaya Kyela. Eee usiku huu kama saa saba hiviiii nane kasoro... eeeh! madaktari wako nae..Asante mama naomba tuzidi kumuombea kuwa na nguvu mamaangu tena ule kabisa...haya mama"
Hiyo ilikuwa sauti ya fomeni akiongea na simu huku akitoka eneo la wodi kuongelea nje kidogo. Lakini masikio yangu yalifanya kazi vizuri na nilimsikia hata kubaini aliyekuwa anaongea naye si mwengine bali mamaangu.
"Tuko Kyela! Saa saba?" Nilijiuliza nafsini na kupata picha kuwa kama nilianguka kweli asubuhi ile basi ndio kusema napata fahamu saa hizi usiku mkubwa? tena tukiwa hospitali ya wilaya Kyela? aaaah nilizidi kuchoka na machozi yalizidi kunibubujika wakati daktari akiandika andika kwenye faili langu baada ya kunipimapima.
Fomeni alirudi kukaa tena jirani yangu pale nilipolala kitandani huku akijaribu kunisemesha lakini niliiishia kumtazama. Alijitahidi kunifuta machozi yaliyokuwa yakitiririka pasi kukoma. Nilitamani kumjibu.....Nilitamani kumuuliza mengi... Hakika nilitamani sana lakini nilishindwa. Kadri nilivyojilazimisha kusema ndivyo nilivyozidisha kasi ya machozi kutokana na maumivu makali ya koo na nyama za midomo.
muuguzi alifika na kunichoma sindano niliyofungwa kwenye mishipa ya mkono mmoja.
Ajabu sindano hii sikuyasikia maumivu pale mkononi, bali niliisikia ikiwa inapita ndani kabisa na kuhisi kunikaba pumzi hata kunikereketa nafsini. Nilitamani nimwambie asichome lakini nilishindwa. Niliendelea kulia huku fomeni wangu akiendelea kunifuta machozi.
Saa zilisogea siku ya pili ikawadia. Mimi na fomeni wangu tukiwa tunaendelea kutazamana huku kibarua chake kikiwa kunifuta machozi nami nikishindwa kuyazuia hadi kunakucha.
Muda wa kuona wagonjwa ulipofika inaweza kuwa nilivunja rekodi ya watu waliokuja kuniona. Kial mmoja aliposikia kuwa nimefumbua macho kwa mara nyengne hakuamini kabisa. Wengi walionijua walisafiri mpaka hospitalini kuja kuniona asubuhi hiyo. Niliwasikia kila walichonambia na dua walizoniombea lakini nilishindwa kuwajibu zaidi ya kuwatazama. Kweli mwili wangu ulishindwa kufanya kazi kwa zaidi ya asilimia tisini, lakini fahamu zangu zilikuwa timamu kwa asilimia mia. Nilimtambua kila aliyefika. Nilikumbuka matukio yote. Namaanisha kumbukumbu zangu zilikuwa timamu kabisa.
Na hapo ndipo katika watu waliofika kuniona na kunifariji hakika wote walinigusa sana moyoni na kumshukuru Mungu kwa kunifanya niwe mkarimu na kumuheshimu kila mtu hata kusababisha upendo mkubwa ulioonesha na watu waliokuja kuniona ambao wengine sikuwatambua kabisa. Hawakuwa mafundi tu, wla vibarua wa kazini, bali hadi wanakijiji na wafanya biashara wa Ipinda walionifahamu waliacha kufungua biashara zao na kudamkia hospitali kuniona.
Na katika ingia toka ingia toka za watu waliokuja kuniona... Ndipo moyo wangu ulipiga kifuani na kupata mshtuko wa mwili mzima baada ya macho yangu kumuona mtu mmoja. Mtu aliyeishi ndani ya akili zangu siku zote nikiamini ndiye chaguo sahihi la maisha yangu. Binti mrembo wa Kinyakyusa mwenye kila vigezo vya kuitwa mzuri.
Naye si mwengine bali Atuganile. Msichana wa ndoto yangu niliyemfungulia mlango wa moyo wangu kabla hajabisha hodi....
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom