Fikiria mtu na akili zake timamu anatetea hilo zimwi kitengo eti kina haki ya kuwachagulia wananchi viongozi kwa sababu wananchi wanaweza kumchagua mtu hatari. Swali ni hatari kwa nani?
Kuna dai kwamba chama tawala CCM kimetekwa na wenye nguvu lakini hatujiulizi hao wenye nguvu ndio akina nani? Zipo nyakati nyingi tu viongozi wetu wa kitaifa tuliowachagua tumesikia wakilalamika, hatujiulizi wanamlalamikia nani.
Kama Raisi analalamika, Waziri Mkuu analalamika, Katibu Mkuu wa chama tawala analalamikia utendaji wa serikali iliyoundwa na chama chake...wananchi tueleweje? Katiba yetu imempa nguvu ya kimungu Raisi wetu, kwa nini alalamike?
Oh mara wasaidizi wangu wananiangusha, anawabadilisha, Haijakaa muda na hao wapya anaanza kuwalalamikia eti wanamuangusha, anawabadilisha. Muda si muda mambo bado hayaendi anaanza tena kulalamika, kulikoni wananchi wenzangu?
Tunamchagua Raisi kwa imani kubwa kwamba sasa tumempata kiongozi mzuri lakini haichukui muda mambo yanarudi kule kule. Mifano ipo tangia Mwinyi, Mkapa na sasa Kikwete...ni nani huyo anawachezesha mchakamchaka, je ni kitengo?
Hayati Mwalimu alimpigia debe Mkapa, akatembea nchi nzima akimnadi kama mtu safi lakini haikuchukua muda, tukajikuta tunatoka kapa. Mwalimu akaahidi kumpinga uchaguzi utakaofuata...je ni kitengo kilichoamua asiuone huo uchaguzi?
Cha ajabu licha ya kuwa na kitengo tumewashuhudia wezi na matapeli makubwa ya dunia yakipata hifadhi nchini na kuzidi kuneemeka kupitia rasilimali zetu.
Licha ya kuwa na kitengo tumeshuhudia matapeli wa kimataifa wakiivamia nchi yetu na kuingia mikataba mibovu ya kupora mali asili zetu kuanzia wanyama, madini hadi mimea.
Imefikia mahali ni kama nchi haina serikali, nchi haina katiba, nchi haina utawala wa sheria na vyombo vya dola viko tu kulinda maslahi ya wageni na maslahi ya wahamiaji haramu.
Ni kama vile vyombo vya usalama vipo tu kupambana na wananchi na si kuwalinda wao na mali zao. Vyombo vya kutoa haki navyo vinalalamika havina nguvu ya kupambana na wahalifu.
Ni kama vile nchi imetekwa na nchi haiko tena mikononi mwa wananchi na matakwa ya wananchi hayapewi tena uzito wala kipaumbele na serikali ni kama haiwatumikii tena wananchi.
Ni kama vile serikali haikuwekwa madarakani na wananchi bali imewekwa na hao inaowatumikia...kitengo? Kama Mtanzania hawezi kumchagua kiongozi anayemtaka kwa sababu kitengo hakikubali, je kweli tuko huru?
Kama Mzee Ngombale Mwiru, kada maarufu wa CCM aliyeitetea CCM wakati wa kiangazi na mvua, usiku na mchana leo yamemkuta na analalama kuhusu kitengo, lazima tujiulize maswali kadhaa!
Viko vifo vingi tu vya kutisha vimetokea nchini visivyo na maelezo, je ni kitengo kinanyamazisha wakosoaji?
Tumeshuhudia kila kunapotokea mtafaruku, kiongozi mkuu wa nchi anakuwa hayupo nchini, je nani huyo anaachiwa utekelezaji?
Hapana Watanzania, hii ni karne ya 21 na teknolojia inatupa fursa ya kutoka gizani. Mambo ya gizani tusiyape nafasi hivyo tujiulize. Kwa nini tuchague kiongozi tukiamini ni msafi halafu baada ya kitambo kidogo tu anaanza kucheza ngoma ya wengine?