Kwa maelezo yako na uwelewa wangu nianze na jinsi ninavyo kuona:
- Mosi, unaelekeakuwa una wivu wa kupindukia kiasi kuwa hupendi mkeo atoke nyumbani hata kwa kwenda kanisani.
- Pili una udikiteta fulani, ndani mwako ni amri tu hakuna mjadala (negotiation), Unalotaka ndilo linakuwa.
- Una mapenzi ya kizamani ya kikurya ambayo yanahusisha kupigana pigana.
Ulipaswa kabla ya kuoa, uchunguze kwanza: Unataka mke wa kushinda kwenye baa au saloon ama kitchen party, maana hawa nao wapo ni wewe tu na upendeleo wako. Si rahisi kumbadilisha mtu mlevi akawa mlokole na mlokole akawa mlevi hivyo ulipaswa upate ready made kuliko kutransform. Mkeo, licha ya mapenzi yako ya kizamani ya kupigana pigana, amekusamehe, anataka mrudiane wewe hutaki. Maana yake huna roho ya msamaha. Waswahili husema 'Asiye samehe haliwezi penzi.' Kumbe wewe huwezi penzi ingawa unaweza kupanda.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa uhuru wa kila mtu kuabudu imani aitakayo, lakini wewe unataka mkeo aabudu namna unavyotaka wewe, hivyo bila kujua, unataka kuwa juu ya Katiba ambayo ndiyo sheria mama ya sheria zote nchini. Masikini nduyu yangu hata hujui kuwa kuvunja Katiba ni kosa. Unaishi katika jamii ya watu wasiostarabika, wastaarabu huheshimu sheria zilizowekwa. Ni wanyama wa porini ndiyo wanaoishi kama unavyotaka wewe na mkeo muishi.
Sijazungumzia upande wa mkeo wala wazazi wake kwa sababu sijawasikia, lakini kubwa ni wewe uliyeomba ushauri na wao hawajaomba chochote. Ndoa ni taasisi inapaswa iheshimiwe na watu wote ukiwemo wewe mwenye ndoa. Mtu yeyote aliyemo kwenye ndoa hushawishiwa wakati wote na mtu mmoja mmoja vikundi vya watu marafiki mbalimbali wakike kwa wakiume, lakini wewe mwenye ndoa unapaswa kuwa na ushawishi mkubwa kushinda makundi yote. Tunapomshawishi mke hatumshawishi kwa mabavu, tunamshawishi kwa hoja huku ukinyunyiza juu yake UPENDO usiopatikana mahala pengine popote isipokuwa kwako tu