Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF), Mzee Joseph Butiku, amesema matukio ya vurugu, uharibifu wa mali na vifo vilivyoripotiwa wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, yameitumbukiza Tanzania katika hofu na kupoteza misingi ya amani ambayo taifa limeijenga kwa zaidi ya miaka 60.
Akizungumza na wanahabari kando ya kongamano la wazee lililoandaliwa na Taasisi hiyo jijini Dodoma tarehe 2 Desemba, 2025 likizungumzia Haki na Amani ya Tanzania kuelekea tarehe 9 Desemba 2025, Mzee Butiku amesema tangu Disemba 1961 hadi kabla ya siku ya uchaguzi wa 2025, Tanzania imekuwa ikijivunia misingi ya usawa, haki, heshima, upendo, kutobaguana na kazi kwa faida ya wote, ambayo imewezesha taifa kuishi kwa umoja na amani.
Hata hivyo, amesema uchaguzi wa mwaka huu umeibua changamoto mpya baada ya maandamano ya vijana na baadhi ya watu wazima ‘kubadilika kutoka kuwasilisha hoja hadi kuwa ghasia’, na kusababisha vifo, uharibifu wa mali na kusambaratika kwa utulivu wa umma.
Amesema vyombo vya ulinzi na usalama ‘vilijaribu kulinda amani’, lakini mazingira yaligeuka kuwa ya mapambano yaliyosababisha madhara makubwa kwa wananchi, ikiwemo watu kufungiwa majumbani bila chakula na maji, huku wengine wakijeruhiwa au kuuawa.
“Vyombo vyetu vya ulinzi na usalama katika kujaribu kuyazuia na kulinda kwamba amani tuliyokuwa nayo zamani inaendelea, ni kama walitoka wakaenda kupambana na wale waandamanaji, kwahiyo kukatokea vifo, kukatokea uharibifu wa mali nyingi- zingine kwa ajali zingine kwa makusudi”, ameeleza Butiku na kuongeza,
Amesema wazee kupitia Taasisi ya Mwalimu Nyerere wameamua kuzungumza hadharani ili kuelekeza tahadhari kwa vijana wanaoendelea kuandaa maandamano mengine, ikiwemo yale yanayosadikika kutarajiwa Desemba 9. Amesema wazee wanaamini bado kuna uwezo mkubwa wa taifa kukaa pamoja, kujadiliana na kupata maridhiano bila fujo, vurugu au uharibifu wa mali.
“Tumepoteza ndugu zetu, wamefariki hatujajua wako wapi, wengine walitekwa, hatujajua kumetokea nini, na yako mazungumzo kutokana na makundi yaleyale ya vijana kwamba tarehe tisa Desemba maandamano yapo, tutake tusitake”, ameeleza Mzee Butiku
Chanzo: Jambo TV