Halmashauri Kuu ya chama cha ACT -Tanzania kimemfukuza madarakani M/Kiti wa chama hicho Mh. Kadawi Limbu na Kumsimamisha kwa muda Naibu Katibu Mkuu ndugu Mahona.
Chanzo: Mwananchi
Dar es Salaam. Wakati Halmashauri Kuu ya Chama cha ACT-Tanzania ikikutana kujadili agenda tatu, ikiwamo ya kuazimia kumvua uongozi Mwenyekiti, Kadawi Limbu, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa leo inawakutanisha viongozi waandamizi wa chama hicho kusaka suluhu ya mgogoro wao.
Chama hicho kwa siku za hivi karibuni kimekuwa katika mvutano kati ya Limbu na viongozi wenzake, hasa Katibu Mkuu, Samson Mwigamba.
Viongozi wengine wanaosubiriwa na rungu la kikao cha halmashauri kuu ni Naibu Katibu Mkuu (Bara), Leopold Mahona na Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana, Grayson Nyakarungu.
Juzi gazeti hili lilimnukuu, Msaidizi wa Msajili wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza akisema: "Mvutano huu hata sisi tunausikia, tumeamua kuwaita Jumanne hii (leo) ili tuwasikilize wote kwa pamoja."
"Tumewaita siyo kwa lengo la kuendeleza tofauti zao, bali kuzimaliza baada ya kusikiliza kila upande."
Akifungua kikao cha halmashauri kuu jana, Makamu Mwenyekiti wa ACT-Tanzania (Bara), Shaban Mambo alisema:
"Mkutano huu ni halali kisheria, kikatiba na kikanuni, hivyo nawasihi wajumbe msiwe na hofu na mjadili kwa kujenga hoja na unapokuwa huelewi usiogope kuuliza."
Aliongeza: "Kila chama lazima kipite katika matatizo na unapopita katika matatizo kama haya ndiyo chanzo cha mafanikio na kukua kwa demokrasia, hatutaogopa kusema ukweli na kutenda haki ni jadi yetu."
Akitaja ajenda za kikao hicho, Mwigamba alisema ni kupokea na kujadili taarifa ya chama kuhusu Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu mwaka huu.
Akifafanua ajenda hizo alisema, watapitisha mapendekezo ya ratiba ya uchaguzi wa ndani iliyopendekezwa na Kamati Kuu Januari 5, mwaka huu kuanzia Januari 19 hadi Machi 28 mwaka huu.
Aidha, watajadili taarifa ya hali ya kisiasa ndani ya chama, ikiwamo taarifa ya kamati maalumu iliyoundwa kuchunguza tuhuma dhidi ya Limbu na wenzake.
Kuhusu akidi alisema kikao hicho kinapaswa kuwa na wajumbe 88 na akidi yake ni asilimia 50, ambayo ni sawa na wajumbe 44 na waliohudhuria walikuwa wajumbe 63 ambao wamevuka idadi inayotakiwa.
Katika hatua nyingine, aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Tanzania Labour Party (TLP), Hamad Tao amejiunga na ACT-Tanzania na kusema ameamua kujiunga na chama hicho kutokana na kukubali sera zake
Chanzo: Mwananchi