Muuaji Mwenye Barakoa

Muuaji Mwenye Barakoa

MUUAJI MWENYE BARAKOA - 14
Sultan Uwezo
+255

Walitoka na kuingia kwenye gari aina ya Nissan Patrol 'box board' lililokuwa likiwasubiri nje. Catherine aliendelea kupata woga kwani ndani ya gari pia kulikuwa na vijana wengine wawili pamoja na wale waliopanda idadi yao ikiwa ni tano ukiongeza mzee Malick na Catherine jumla wakawa watu saba huku mmoja kati yao akiwa dereva.

Hapa ndipo alipoamini kuwa usalama wake ni mdogo sana alimtazama mjomba wake mzee Malick Bolenge katika ya mbele alikuwa bize akichati na simu tu kitu ambacho kilimfanya ashushe pumzi ndefu, alipotuliza akili kidogo akapata wazo la kuwatumia ujumbe wakina Adoyee akaingiza mkono kwenye kipochi chake aitoe.

"Sista mbona tunaminyana bila utaratibu?" Mmoja wa wale vijana aliyekuwa amekaa karibu na Catherine alimuuliza huku akivua miwani yake.

"Braza tuheshimiane basi maneno gani hayo unaongea? Tumeminyana vipi hapa wakati hapa niko kutoa simu?" Catherine alimuuliza kijana huyo akiwa kamkazia macho usoni kama vile kamfumania hivi.

"Unajua nini? Mimi huwa sibishani na watu wa jinsi yako ebooo!!!" Kijana alimjibu huku akimsindikiza kwa kibao kikali cha shavuni kilichopelekea Catherine kumuangukia miguuni kijana wa upande wa pili.

"Aaaghh...! Kaka nimekukosea nini mpaka unipige kibao kikali kiasi hiki?" Catherine alimuuliza akiinuka huku mkono ukilishika lile shavu kuona kama liko sawa.

"Unataka kuijua sababu siyo?" Yule kijana aliyekuwa kajazia kuliko wengine wote mle garini alimuuliza.

"Ndiyo nataka wewe unaona ulichokifanya kiko sahihi? Mjomba mbona huyu kijana wako ni korofi kiasi hiki?" Catherine alimjibu kisha akaona amtupie swali Mjomba wake ambaye muda wote huo alikuwa bize na simu kama vile hakuona wala kusikia kilichokuwa kikiendelea nyuma yake.

" Majura hujui kama huyo ni Mjomba wangu? Kwanini unakosa adabu hivyo?" Mzee Malick alimjibu kijana huyo aliyemwita kwa jina la Majura, lakini kitu cha ajabu kijana huyo ambaye ni kama alizamilia jambo kwa Catherine ni kama vile aliambiwa ongeza tena kwani kilichotokea alimvuta na kumpiga kichwa cha usoni na kumpasua eneo la juu ya jicho hali iliyopelekea kuanza kuvuja damu nyingi.

"Mjomba mbona kijana wako anataka kuniua? Nimemkosea ni......" Kabla hajamalizia kuongea alipoteza fahamu na kumuangukia kijana wa upande wa pili. Hapo hapo Majura alitoa kitambaa cheupe kwenye kibegi chake kisha akachukua kichupa kidogo mfuko wa pembeni wa kibegi hicho na kukifungua, dawa iliyokuwa nyeusi hivi ya maji maji aliimwagia kwenye kile kitambaa na kumfunga usoni mpaka puani Catherine kisha akamuegesha kitini.

" 'Well done ma boy' kazi nzuri sana msimuache hivyo hivyo mfungeni kamba za mikono na miguu." Mzee Malick alimpongeza Majura kwa kitendo alichokifanya kwa Catherine.

"Lakini bosi huyu si mtoto wako, kwa ninavyojua mimi mtoto wa dada yako ni mtoto wako pia kulikoni kwako?" Kijana mwingine aliyekuwa kiti cha nyuma kabisa alimuuliza mzee Malick.

"Wayaki tulia kijana wangu kwenye hili halikuhusu hata kidogo nimelianza mwenyewe nitalimaliza mwenyewe au tayari rangi ya mtoto imekuingia kwenye mishipa ya damu? Maana ninyi vijana msione vichaka tu tayari." Mzee Malick alimjibu Wayaki.

"Aaahh bosi maneno gani hayo tena mimi sikuwa na maana hiyo hata kidogo nilitaka kujua tu." Wayaki alimjibu bosi wake baada ya kuona anaingiza maneno ya utani lakini yakiwa na maana fulani. Wakiwa wamekolea kwenye mazungumzo gari lilikuwa likiacha barabara kuu na kuingia barabara ya vumbi ambayo ilikuwa ni chakavu na ikionesha hakuna magari ambayo huingia kule mara kwa mara. Na baada ya mwendo kama wa kilometa saba hivi waliwasili kwenye eneo lililokuwa na mashamba lakini yakiwa ni kama vile ya mtu mmoja kwa sababu hakukuwa na mashamba mengine jirani zaidi ya lile lililokuwa limeizunguka nyumba ambayo bati lake lilikuwa limechoka kiasi. Mpaka wakati huo Catherine hakuwa akijua chochote kilichokuwa kikiendelea kwani alikuwa bado kazimia.

"Mshusheni huyo mwanaharamu na mpelekeni waliko wenzake." Mzee Malick aliongea akishuka garini na kuelekea ndani. Catherine alishushwa na Majura alimbeba peke yake na kumpeleka kwenye chumba cha giza kilicho ndani ya ile nyumba kama mzee Malick Bolenge alivyoagiza.

Lakini wakati hayo yakiendelea pale, nje kidogo ya lile shamba kulikuwa na watu waliokuwa wakifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Na hakuna hata mmoja miongoni mwa watu wa mzee Malick aliyeweza kushtukia hilo na watu hao hawakuwa wengine zaidi ya Seynabou mtoto wa marehemu mzee Alioune aliyekuwa mganga wa Mchungaji Rodney akiwa sambamba na kijana wa Kichad ambaye historia yake kidogo siyo nzuri kutokana na maisha aliyoishi huko nyuma kabla ya kukutana na Mchungaji Rodney pamoja na mke wake Bi Catherine ambapo baada ya kumfanyia darasa maalum la Saikolojia ambalo lilimsaidia kwa kiasi kikubwa na hapo ndipo alipopewa kazi ya ulinzi nyumbani kwa Mchungaji Rodney.

Hawakuwa peke yao bali walikuwa na kijana mmoja mwenye asili ya Kiarabu aitwaye Awadh na huyu ndiye aliyekuwa akilifukuzia gari la wakina Majura na hii ni baada ya kupewa ujumbe na Catherine walitafuta msaada wa haraka kuhakikisha wanamuokoa bosi wao na hapo ndipo walipokutanishwa na kijana huyo ambaye ni fundi Bajaj na Pikipiki, baada ya kuwafukuzia na kuhakikisha sehemu walipoingia waliamua kutafuta njia ya kuwafikisha pale bila kuonekana. Ndani ya nyumba ile mzee Malick Bolenge na kundi lake walikuwa kwenye mazungumzo huku Jumbe na wenzake wakiwa hawaamini macho yao kumuona bosi wao kwenye hali ile ya kutojitambua.

"Hivi kaka Jumbe tutatoka salama hapa kweli ikiwa tuliyekuwa tunamtegemea kaletwa akiwa hajitambui kiasi hiki sijui kafa au mzima?....." Kabla hajamaliza kuongea kauli yake Jumbe alimtandika kibao yule kijana.

"Unaongea nini wewe? Hivi unafikiri ni muda wa kuongelea hayo?" Jumbe alimuuliza.

"Nisamehe kaka nimetokwa tu na maneno haya." Kijana huyo alimjibu.

"Okay nimekuelewa, kitu cha msingi hapa ni kuangalia tunajinasuaje kwenye mtego huu tulioingia bila kutarajia." Jumbe aliwaambia wenzake huku akimuangalia Catherine aliyekuwa chini hajitambui.

"Mhh mmhh mhhh...." Catherine alizinduka lakini akili haikuwa sawa ni kama alikuwa akiota hivi.

"Haa haa kaka Jumbe bosi Catherine kazinduka!!" Aliongea kijana mwingine aliyekuwa kimya muda wote wakati Jumbe akifokeana na mwenzake.

"Mathew na Soud nisikilizeni vizuri wadogo zangu, sisi ndiyo tuliosalia hapa ngomeni si mnamkumbuka yule mzee aliyetekwa pamoja nasi namna alivyouawa bila huruma? Na sasa tegemeo letu liko hapa pamoja nasi hivyo tukilaza akili tumekwisha." Jumbe aliwaambia wenzake.

" Mjomba, mjomba mbona unamuangalia tu huyu kijana? Au umeridhika na ninavyofanyi.... " Kabla hajamaliza alishtuka na kuanza kuangalia huku na kule mle ndani.

" Nimefikaje hapa na ninyi ni wakina nani?" Catherine aliwauliza wakina Jumbe.

"Sisi ni wakina nani?" Jumbe alimuuliza.

"Mhh wewe ni...."

"Mimi ni Jumbe au umenisahau?" Alimuuliza.

"Ndiyo kusema nimetekwa? Jumbe hebu niambie hapa nimefikaje?" Catherine aliuliza baada ya akili yake kuanza kukaa sawa na kuwatambua vijana wake.

"Tusipochukua tahadhari mapema bosi wetu hawa watu wanakwenda kutuulia mbali." Matthew aliongea akijivuta mbali na Jumbe.

"Nisikilizeni vijana wangu, mtengeneza hii filamu nimemfahamu tayari lakini msiwe na mashaka tunatoka salama kikubwa mimi nitaendelea kujifanya bado sijazinduka ili kuvuta muda mnanielewa?" Catherine aliwaambia wakina Jumbe na wakati huo huo mlango ulianza kufunguliwa, Catherine alijilaza vile vile kama awali.

" Toka nje ninyi, fanya haraka!!" Mmoja wa vijana wa mzee Malick aliwaambia wakina Jumbe ambao bila kubisha waliinuka na kuongoza nje na kumuacha Catherine pale chini huku yule kijana akiinama kumuangalia Catherine kama kuna dalili zozote za matumaini na baada ya kubaini hakuna aliinuka na kutoka nje na kuufunga mlango ambapo alikwenda mpaka walipokuwa wakina Jumbe na kuanza kuwasurubisha kwa mijeredi.

"Hapa mtaongea tu hata mjidai ni mabubu kiasi gani, najua mnaelewa ni wapi ulikotunzwa mzigo." Mzee Malick aliwaka kama Mbogo huku akiwatandika yeye mwenyewe.

"Kwanza kwanini nitoe mijasho ilhali vijana wangu mpo hebu walainisheni mbwa koko hawa mpaka waongee walikohifadhi mzigo."

Mzee Malick aliwaamrisha wakina Wayaki kuwashughulikia vilivyo wakina Jumbe ambao walikuwa wamefungwa kwenye mti.
"Sawa bosi." Walijibu.

"Mkuu nakuhakikishia sisi hatujui huo mzigo uko wapi na wala hatuujui hata ulivyo." Jumbe alijitetea mbele ya sura ya mzee Malick iliyokuwa imefura kwa hasira.

"Unasemaje weweeee? Unathubutuje kuongea na mimi maneno ya kichawi kiasi hicho? Na kwanza eleweni kuwa mimi siyo bosi wenu au mnanifananisha na huyo Pimbi wenu?" Mzee Malick alimwambia Jumbe kisha alimtemea mate usoni na kuondoka zake.

"Wewe mshenzi umeona ulivyomuudhi bosi? Sasa leo mtatutambua vizuri." Kijana mmoja aliongea hayo na kuanza kuwatandika mijeledi bila mpangilio hakuangalia ni wapi awapige au wapi awaache yeye alikuwa akiwashushia mijeledi tu.

"Hivi ninyi mnacheza na akili yangu? Mmempeleka wapi huyu Nyambuda? Nawauliza ninyi hapo mbona mmenitumbulia mimacho, nataka majibu haraka." Mzee Malick alitoka macho yakiwa yamemtoka pima kama vile kapewa taarifa ya kurejea kwa duniani kwa mtu ambaye alifariki kitambo na hii ni baada ya kuingia kwenye chumba ambacho alihifadhiwa Catherine na kutomkuta zaidi ya dirisha kuvunjwa. Maneno yale ya mzee Malick yaliwatoa pale vijana wake na kuelekea mle ndani kuhakikisha kama kweli hakuwepo ndani.

"Buushiiiiit...... Kavunja dirisha na kutokomea, Haraka poteeni mkamtafute huyu Mbagdad kabla hajavuka msitu huu." Wayaki aliwaamrisha wenzake huku yeye akirejea kwa bosi wake ambaye muda huo alikuwa akienda mbele mara nyuma mara akae mara akune kichwa kwani ni tukio ambalo hakulitarajia ukizingatia mtu mwenyewe alikuwa kazimia hivyo hawakumtilia maanani sana zaidi ya wakina Jumbe.

"Enhh mmempata?" Alimuuliza Wayaki.

"Hapana bosi ndiyo wamekwenda kumsaka." Wayaki alimjibu.

"Unasemaje wewe? Eti wamekwenda kumchaka kumchakaaaa na wewe unafanya nini hapa?" Aliyarudia maneno ya Wayaki akiwa kaibana pua yake.

"Nakwenda bosi." Wayaki alimjibu na kuondoka.

"Mnanijua vizuri sana na ole wenu mrudi mikono mitupu mtanitambua." Mzee Malick aliongea akiwageukia wakina Jumbe waliokuwa wamepigika vilivyo pale mtini.

JE NI NINI KITATOKEA HUKO PORINI KATI YA CATHERINE NA MJOMBA WAKE?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 15
Sultan Uwezo
+255

"Sijawahi kushindwa 'game' zote nilizocheza kwenye biashara zangu ninyi ni wakina nani mpaka mnikwamishe? Nawaapia kwa jina la wale walionileta duniani na kisha kulala hapa chini nitawachinja kwa kisu changu butu ambacho chenyewe huwa hakitaki kunolewa, haiwezekani muwe kikwazo." Mzee Malick aliendelea kulalama macho yakiwa kwa Jumbe mtu aliyeamini ndiye mkwamisha mpango wake.

" Mzee wangu na...na..najua una hasira na sisi lakini hatujui kilicho nyuma ya pazia kati yako na bosi Catherine ungekuwa wazi kwe..kwe...kwetu tunaweza kuwa msaada." Jumbe aliona aongee kitu ambacho kinaweza kumfanya mzee Malick kushusha presha kidogo ili waweze kumlaghai.

" Unasemaje wewe... Halafu ungejua nina hasira na ninyi kama huyo bosi wenu wala usingejaribu kuuliza ujinga wako. Narudia tena kifo chenu kinakaribia labda apatikane huyo asiye na wazazi." Jumbe aliwatazama wenzake ambao muda huo walikuwa wamekata tamaa ya kupona kutokana na vile walivyochapika halafu ukijumlisha na maneno ya mzee huyo walichoka kabisa.

" Kaka kuna kupona kweli hapa?" Aliuliza Soud kwa sauti ya chini huku damu zikiendelea kumtiririka kichwani na kumfanya jicho moja kushindwa kuona vizuri.

" Nawahakikishia hapa tutatoka hata kama itakuwa kwa kuchelewa naombeni mniamini kiongozi wenu." Jumbe alimjibu. Akiwa anawajibu wenzake mara alirudi Wayaki akiwa ametapakaa damu mwili mzima huku akitembea kwa taabu sana hali ile ilimfanya mzee Malick kumfuata na kumkunja.

" Usiniambie kile ambacho tayari nahisi ndicho kilichokupateni huko." Mzee Malick alimwambia Wayaki.

"Bo...bo...bosi ha..hali si shwari huko porini wenzangu wameuawa baada ya kuotewa tukiwa tunawatafuta." Wayaki alimjibu.

"Ng'ombe mmoja wewe iweje mtoto wa kike ambaye hata taaluma ya mapigano hana uwashambulie huo si ujinga?" Mzee Malick aliongea kwa hasira kiasi cha kumsukuma chini Wayaki ambaye alikwenda kuangukia dimbwi la maji lakini mzee Malick yeye hakujali kitu alichokifanya ni kurudi ndani.

Baada ya kuondoka tu, huku nyuma Jumbe alifanikiwa kuzikata zile kamba ambazo muda wote alikuwa akizisugua kwenye mti mpaka zikajibu. Hakutaka kupoteza muda alichokifanya ni kumuwahi Wayaki pale chini na kumfunga kamba na kumvutia pembeni kisha akaufuata mlango na kuufunga kwa nje ili mzee Malick asiweze kufanya chochote alipohakikisha kila kitu kiko sawa alirudi na kuwafungua kamba wenzake na kutokomea zao porini huku mkononi Jumbe akiwa kashika bastola aliyokuwa nayo Wayaki.

"Oyaa ee acheni umama jikazeni wakitukuta safari hii hatuwezi kupona hata kidogo."Jumbe alimwambia wenzake ambao hawakuwa sawa.

" Tunajitahidi kaka sema ndiyo hivyo jointi hazina kazi wale watu hawana utu hata kidogo." Mathew alijibu akiachia tabasamu la kimaumivu.

" Jamani mimi nina wazo mnaonaje turudi tukaiwashe moto nyumba yule mzee naye aipatepate." Soud alitoa wazo lake ambalo hakuna aliyelikubali kati yao.

" Jamani hebu twendeni huyo mzee tuachane naye si mnajua kuwa ni ndugu yake na bosi wetu?" Jumbe aliwaambia akipangua majani kuiweka sawa njia ili wenzake wapite kwa urahisi zaidi. Walipita pori kwa pori mpaka walipofika barabarani lakini hawakutokeza walichokifanya ni kutembea kando yake ili wasionwe na maadui zao. Walipofika kwenye kitongoji fulani ambacho hakina makazi mengi ya watu Jumbe aliona waingie hapo kutafuta mawasiliano.

"Naombeni mnisubiri hapa mimi nikatafute mawasiliano kwenye zile nyumba kama itawezekana."

"Kaka si unakumbuka ilivyokuwa mpaka tukatekwa na yule mzee wa viazi? Na huko yasijetokea hayo." Matthew hakukubaliana naye kutokana na kile kilichowatokea siku ambayo walitekwa.

"Nitakuwa makini ndugu yangu wala usijali, lakini nilikuwa nina wazo pia iwapo tutapata mawasiliano itabidi tuelekee lile eneo ambalo tulifukia silaha zetu." Jumbe alimwambia wenzake ambao walikubaliana naye kisha akawaacha pale kichakani.

Baada ya kama mwendo wa dakika saba kuweza kuyakaribia makazi ya kijiji kile alisikia mlio wa kitu kikigongwa kutoka upande wa pili wa kichaka kilichokuwa mbele yake ikabidi asogee karibu na hicho kichaka ili aweze kuangalia ni nani huyo na anafanya nini pale. Kumbe alikuwa ni mama mmoja akiwa na mtoto mgongoni akisenya kuni taratibu.

"Nyamaza mwanangu namaliza sasa hivi, tunakwenda kumuona baba sawa mwanangu?" Mama huyu alikuwa akimbembeleza mtoto wake aliyekuwa akimsumbua mgongoni.

"Habari dada!" Jumbe alimsalimu.

"Habari? Wewe ni nani na umefuata nini huku?" Mama huyo alimuuliza badala ya kuitikia salamu yake.

"Uungwana ni kutakiana hali dada yangu kwani ni vibaya kufanya hivyo?" Jumbe alimuuliza.

"Siyo vibaya lakini sikufahamu na sura yako ni ngeni kabisa hapa." Mama huyo alimjibu.

"Okay iko hivi mimi ni msafiri tu dada yangu gari langu limepata tatizo hapo barabarani na simu yangu imeishiwa chaji hivyo nikiwa najisaidia nikakusikia ukiongea na mwanao nikaona nije niombe msaada wa simu niweze kufanya mawasiliano." Jumbe alimweleza mama huyo ambaye kwa muonekano wa haraka alianza kumuamini.

" Kumbeee! Pole sana kaka ulikuwa unaelekea wapi?" Alimpa pole baada ya kusikia kilichomtokea huku akiitoa simu yake iliyokuwa kwenye kimfuko cha nailoni kilichokuwa kwenye mfuko wa sketi yake iliyochoka na kufanana na udongo wa eneo hilo.
"Hii hapa ila sijui kama salio kutosha, iwashe niliizima baada ya kuona imebakiza kajiwe kamoja." Alimkabidhi.

"Nashukuru dada yangu." Jumbe aliipokea na kuiwasha.

"Imewaka?" Alimuuliza wakati akiwa kapiga magoti akifunga mzigo wake wa kuni.

"Imewaka tayari wacha niingize namba kwanza." Jumbe alimjibu dada huyo.

Baada ya kuipiga namba ya Catherine ambayo iliita kwa muda mrefu bila kupokewa hatimaye ilibonyezwa kitufe cha kijana na kumfanya Jumbe kuita.

"Bosi! Jumbe hapa uko poa?" Lakini upande wa pili haukuongea chochote kitu kilichompa hofu Jumbe.

"Mhh au ni mtandao!" Alijisemesha akiiangalia simu ambayo ilikuwa 'full network' kitu kilichomshangaza, na hapo ikabidi aikate kisha aipige tena.

"Kama mtandao unasumbua sogea karibu na mti huo mbele yako." Yule mama alimwambia Jumbe akiwa kaushikilia mzigo wa kuni uliokuwa tayari kuwekwa kichwani alichokuwa akikisubiri ilikuwa ni simu.

"Unafikiri ni mtandao! La hasha nadhani kuna tatizo kwa ninayempigia." Jumbe alimjibu akiisikilizia tena kuona kama itapokelewa.
"Halo halooo." Jumbe aliita.

"Ulijua ni huyo nyang'au wako siyo? Sasa nisikilize vizuri kijana mkosa sura mimi ni sawa na kivuli chako hivyo kukikimbia kivuli chako sidhani kama inawezekana jiandae." Mzee Malick alimjibu na hapo ndipo alipogundua kuwa simu ya Catherine ilibaki mikononi mwa mzee Malick Bolenge hivyo haraka sana aliikata kisha akatafakari kwa muda kabla ya kuirejesha simu kwa mwenyewe.
" Samahani kwa kukuchelewesha dada yangu." Jumbe aliomba radhi.

"Usijali vipi lakini umempata?" Alimuuliza.

"Hapana inavyoonekana simu yake imekamatwa na mtu mwingine na siyo yeye maana naona hatujaelewana sijui anaongea vitu gani." Jumbe alimjibu.

"Pole kaka yangu utafanyaje sasa?"

"Itanibidi nivizie gari lolote linalokwenda mjini St.Louis, naomba nikutwike tafadhali."

"Asante nashukuru." Alikubali na kumfanya Jumbe kuuinua mzigo ule mpaka kichwani kwa dada huyo.

"Mungu akubariki kaka yangu na ufike salama uendako."

"Asante na wewe uendelee kuwa moyo huo huo uliouonesha kwangu." Jumbe alimjibu akianza kuondoka. Alirejea mpaka walikokuwa wenzake ambako aliwakuta wakiwa wamejilaza pale alipowaacha.

"Ninyi hivi mna wazimu kweli? Mnawezaje kulala kwenye mazingira kama haya?" Jumbe aliwauliza wakina Mathew.

"Kaka tulipitiwa tu si unajua tena mchoko." Mathew alimjibu.

"Mbona umechelewa hivyo?" Soud aliuliza.

"Ndugu zangu inukeni hapa hakuna usalama tena yule Dubu tuliyemkimbia kule ndiye anayeishikilia simu ya bosi hivyo anaweza kumtraki yule dada aliyeniazima akamsurubisha vya kutosha na yeye akashindwa kustahimili maumivu na kuamua kutaja eneo alilokutana nami na hivyo wakaanza kututafuta kwa udi na uvumba."

" Kwa kichapo kile mwenzenu nahisi kupona kabisa hebu tuwahini kuchukua silaha zetu halafu hao makarambwanda watusogelee wauone moto unavyowaka." Soud aliongea akiwa mbele japo alikuwa akichechemea lakini hatua zilikuwa ndefu kuliko wenzake.

***

"Jamani hivi tutawaokoa vipi wenzetu?" Seynabou aliwauliza wenzake wakiwa nyumbani kwa Awadh wakiendelea kumkanda Catherine maeneo yenye vidonda.

"Tunatakiwa tufanye kila tunaloweza ili kuwaokoa maana kitendo cha kunikosa mimi sijui watawafanya nini wakina Jumbe." Catherine alijibu akiwa kakunja sura wakati Seynabou akiendelea kufanya huduma ya kwanza.

"Adoyee hebu jiandae tuelekee porini." Awadh alimwambia Adoyee huku akichukua jaketi lake ambalo hulivaa anapoendesha pikipiki.
"Kuweni makini yule mzee ni sawa na Nyati aliyejeruhiwa." Catherine aliwasihi wakitoka.

"Usijali bosi." Adoyee alimjibu akitoka kumfuata Awadh alipokuwa.

MOTO UMEWAKA KIASI CHA KUIFANYA PLETI NAMBA YENYE MAANDISHI 'MUUAJI MWENYE BARAKOA' KUSOMEKA VIZURI BILA CHENGA.

UNAJUA NINI MDAU? KAA TAYARI KWA SEHEMU YA KUMI NA SITA, LAKINI WAKATI HUO HUO ANZA MAZOEZI YA KOPE MAANA MOTO HUU SI WA KITOTO.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 16
Sultan Uwezo
+255

Walipanda pikipiki na kutokomea kule walikokuwa safari hii ikiwa ni kuwafuata vijana watatu ambao ni muhimu kwa mustakabali mzima wa mwanamama Catherine na hao vijana si wengine bali ni Jumbe, Matthew na Soud wakiamini wako mikononi mwa mzee Malick Bolenge mtu tunayemjua kama Mjomba wa Catherine japo majibu tunaanza kuyapata.

Awadh alicheza na usukani wa pikipiki mpaka katikati ya msitu wa Kaludenge unaojulikana zaidi kwa uzalishaji wa viazi mviringo pamoja zao la chai. Barabara ilikuwa imeharibika sana kutokana na mvua kubwa ambayo ilinyesha.

"Mwamba jishikilie barabara imeharibika sana." Awadh alimwambia Adoyee.

"Usijali kaka nimejishikilia mpaka najiogopa mwenyewe." Adoyee alimjibu Awadh akikaa vizuri baada ya pikipiki kuruka juu na kutua chini kulikotaka kuwabwaga chini.

"Kaka wacha tuegeshe hapa kwanza kwa hili tope hatuwezi kutoboa tunakokwenda." Awadh alimwambia Adoyee akiipaki pikipiki pembeni.

"Tutakaa wapi sasa?" Adoyee alimuuliza.

"Wacha tuiingize kwenye lile chaka kisha tutembee kwa miguu si unajua tumekaribia kufika." Awadh alimjibu akifunga kamba za buti lake ambalo lilikuwa limekula tope la kutosha hivyo alihisi kama mguu unachomoka.

"Tufanye fasta basi ulianzaje kuvaa mibuti kama hiyo? Cheki mwenzako niko ndani ya raba hata ikila mitope nasonga mbele." Adoyee alimwambia Awadh.

"Ni siku nayo kaka hata mimi sikutarajia kukutana na hali hii imetokea tu. Lakini yote kwa yote lazima tufike kwenye lile shamba kabla mzee Malick hajawafanyia kitu kibaya jamaa zetu." Awadh alimjibu. Waliificha pikipiki kwenye kichaka kisha Awadh alilichukua begi alilokuwa kalifunga kiti cha nyuma kisha akalibeba wakaondoka. Hawakufika mbali sana kutoka ilipoachwa pikipiki wakasikia mlio gari ambao uliwapa wasiwasi.

" Watakuwa wenyewe nini hao?" Adoyee aliuliza.

"Nahisi hivyo sijui watakuwa wanakwenda wapi? Itakuwa poa sana kama tutakutana na walinzi kama ilivyokuwa mwanzo tukiwa tunamuokoa bosi Catherine." Awadh alijibu huku akiwa anaangalia sehemu ya kupita.

"Kwa sasa watakuwa makini sana kikubwa hapo tusiende kifalafala." Adoyee alitoa tahadhari.

"Usijali hapa uko Komandoo aliyewaasi Wanajeshi wa Kijapani." Awadh alimjibu. Walitembea mpaka walipolikaribia shamba ambalo hatujajua kama liko chini ya mzee Malick.

"Kamata silaha yako vizuri tumeshafika eneo la mapambano." Awadh alimwambia Adoyee.

"Niko tayari kaka."

"Okay, sasa wewe kamata hili begi wacha mimi nikaangalie usalama wa mazingira na namna ya kutimba pale." Awadh alimwambia Adoyee akimkabidhi begi.

"Poa lakini kuwa makini."

"Nipe dakika tatu nitakuwa nimekamilisha kila kitu huko." Alimjibu na kuondoka. Adoyee aliuegemea mti uliokuwa nyuma yake na kushusha pumzi kwa nguvu kubwa kama vile kuna zigo kubwa kalitua.

"Ugenini shida sana tumejificha kwenye eneo ambalo hatujui kama ni salama au ndiyo tumejileta wenyewe." Adoyee alijisemesha mwenyewe. Wakati huo Awadh alishajipenyeza mpaka nyuma ya nyumba ambayo hutumiwa na mzee Malick kuwahifadhia mateka wake na baada ya kufika alijiinua mpaka usawa wa lile dirisha ambalo walilivunja na kuchungulia ndani, ukimya wa ile nyumba ulimtisha kidogo kwa kuwa walipokuja mwanzo hukukuwa kama kulivyo sasa.

"Mbona kimya sana au ni mtego nini?" Alijiuliza akiangalia kushoto na kulia kuulinda usalama wake. Na alipojiridhisha kuwa hakuna pingamizi alilishika dirisha lile na kujivuta mpaka juu kisha akajitupa ndani kwa staili ya kuviringika kama tairi bastola ikiwa mkononi, alijiinua na kukifuata chumba kilichokuwa kushoto kwake kisha alirudi na kuingia cha kulia ambako nako hakukaa sana alirudi sebuleni na kukaa chini huku akikipiga kichwa ukutani na meno kayauma kwa hasira.

"Watakuwa wapi hawa mashetani?" Alijiuliza Awadh, lakini hapo hapo akapata wazo jingine la kuufungua mlango wa nje ili akalikague eneo la mbele ambako kulikuwa na mabanda mengine huko alihisi anaweza kupata kitu chochote.

Aliushika mlango na kujaribu kuufungua lakini haukufunguka hivyo akaona ni bora apitie tena dirishani, alipotoka mle ndani aliizunguka ile nyumba mpaka mbele ambako bado kulikuwa kimya kitu kilichomfanya azidi kuwa makini kiasi cha hata unyasi ukianguka tu bastola imeshanyooshwa kwenye huo uelekeo.

Lakini bado hakuambulia chochote kwenye vile vibanda zaidi ya michirizi ya damu kwenye nyasi zilizokuwa karibu na kibanda kilichokuwa na kinyesi cha kuku lakini hao kuku hawakuwepo. Aliinama na kuzigusa zile damu ambazo zilianza kuganda.

"Mmh ina maana hawa wajomba watakuwa wameuawa na huyu chizi? Na kama siyo hizi damu ni za nini?" Awadh aliendelea kujiuliza maswali ambayo hakuyapatia majibu.

Baada ya kutoona mtu yeyote pale zaidi ya makanyagio ya tairi za gari ambalo linaonekana liliondoka masaa kadhaa yaliyopita kabla ya yeye kufika.

" Mzee huyu ni pasua kichwa sana atakuwa kawapeleka wapi? Yaani pamoja na kukimbia kote huku tumeambulia patupu?" Na wakati akiendelea kujiuliza maswali hayo mara alimsikia mtu akipiga mluzi wa wimbo fulani aujuaye mwenyewe na ilionesha hana hata chembe ya wasiwasi hii ilimfanya Awadh kujificha nyuma ya mti ili apate nafasi ya kumuangalia huyo mtu ni nani, haikuchukua muda alitokea mzee mmoja wa makamo akiwa na magogo mawili begani huku mkononi akiwa kashika shoka.

Alitua chini magogo yake na kuvua makubazi yaliyokuwa yamebeba tope la kutosha hivyo kwa kutua shoka aliyatoa matope yote kisha kuyavaa tena.

"Tulia hivyo hivyo mzee usivute hata hatua moja mbele wala nyuma ukijaribu tu nitaumwaga ubongo wako." Awadh alishamsogelea mzee huyo na kumuwekea bastola kisogoni. Mzee wa watu hakuwa na pingamizi lolote zaidi ya kutii amri iliyotolewa.

"Rudisha mikono yako nyuma haraka." Alimwamrisha mzee huyo ailete mikono nyuma ambapo aliifunga kwa kamba iliyokuwa pale chini kisha alimtaka aketi chini.

"Nafikiri mpaka ushajua nahitaji nini mzee wangu, ukweli wako utakuweka hai lakini tofauti na hapo ubongo wako utamwagika sasa hivi." Awadh alimtisha mzee wa watu aliyekuwa akitetemeka pale chini.

"U..u...una...taka nikusaidie nini kijana?" Mzee huyo aliuliza.

"Unauliza tena? Yaani unataka kuniambia hujaelewa chochote?"

"Ninge...ninge..ningekuwa najua wala nisingekuuliza mwanangu." Mzee alimjibu kitu kilichomfanya Awadh aidhibiti hasira yake na kumwambia kilichomleta pale.

"Nawahitaji watu wetu mliowateka."

"Kijana wangu! Wale vijana hawapo hapa kwa sasa walishatoroka zamani."

"Unasemaje mzee? Hebu acha kucheza na akili zangu hivi unafikiri mimi ni mwepesi kiasi cha kunidanganya hivyo? Umekosea mzee niambie kabla sijachukua hatua za hatari kwako." Awadh aliendelea kumtisha mzee huyo ambaye hata jina lake halijafahamika.

"Kwanini nikudanganye kijana wangu na nifanye hivyo ili iwe nini?" Mzee alimjibu.

"Unataka kusema nini?" Awadh alimuuliza akiwa kamkazia macho ili kuona kama kuna ukweli wowote au anadanganya.

"Si unayaona hayo matairi ya gari?" Alimuuliza Awadh.

"Kuna uhusiano gani na swali langu?"

" Mzee Malick amechanganyikiwa kiasi cha kuongea peke yake na hii ni baada ya hao wenzenu kutoroka na kutokomea kusikojulikana hivyo mzee kaamua kwenda kuwasaka." Mzee alimjibu.

"Wametoroka lini?" Awadh alimuuliza swali jingine.

"Kama masaa matano yaliyopita hivi." Alimjibu.

"Okay sawa mzee mimi ninaondoka lakini nitarudi pale nitakapobaini kuwa ulinidanganya." Awadh aliondoka bila kumfungulia hata kamba kitu kilichomfanya mzee wa watu kumtolea macho Awadh ambaye wakati huo hakuwa anafikiria chochote zaidi ya kumuwahi Adoyee aliyekuwa kamuacha vichakani.

Alitimua mbio kutoka eneo lile na moja kwa moja akamfuata Adoyee alikokuwa kamuacha, lakini alipofika hakumkuta Adoyee zaidi ya pikipiki iliyokuwa pale pale alipokuwa kaiweka. Akaangaza huku na kule lakini hakuweza kuona mtu hivyo akafuata alama za viatu alimopita ili kubaini alikokwenda, baada ya kutembea kwa muda aliamua kurudi.

"Watu wengine bwana ni wa ajabu sana unakwendaje kujisaidia kwenye vichaka vya mbali wakati hivi vyote ni vichaka au alifikiri kuwa hapa tutalala ndiyo maana akaona aipeleke mbali harufu yake."

Awadh alijiuliza akiwa anaikagua pikipiki, alipoona iko sawa aliiweka silaha mahali pake kisha akaanza kuisukuma pikipiki ili kuiondoa pale ilipokuwa na baada ya kufanikiwa kuitoa pale kichakani alianza kuikokota kijiti mkononi kwa ajili ya kutolea tope ambalo lilikuwa kikwazo kwenye pikipiki. Alipoona kuwa shughuli inazidi kuwa tete kwenye usukumaji wa pikipiki akaona dawa pekee ni kuiwasha tu.

"Ni bora nipambane nayo nikiwa juu kuliko kuisukuma nisije shitua nyonga bure yakawa mengine hapa." Alijisemesha mwenyewe akiwa anaiwasha. Aliiwasha kwa muda mrefu kidogo lakini haikukubali hata kidogo kitendo hicho kilimkwaza Awadh na ukizingatia mpaka muda huo Adoyee hakuwa karejea toka alikokuwa kaenda.

" Pikipiki igome jingine halijarudi mpaka sasa sijui huko liliko linashusha mnyororo, watu wengine bwana kulikuwa na sababu gani ya kwenda kote huko ilhali vichaka vimejazana eneo lote hili." Awadh aliongea kwa sauti akiwa anashuka kwenye pikipiki baada ya kugoma kuwaka.

" Na ushukuru imegoma kuwaka ungetembea kwa miguu." Alisema hivyo baada ya kusikia kishindo cha mtu akija pale alipokuwa kasimama.

" Mimi siyo? Na vipi kuhusu wewe utafanya nini?" Ilikuwa ni sauti yenye mikwaruzo iliyounguruma kutoka nyuma yake na kumfanya kugeuka kabla ya kujibu kwani ilikuwa ni ngeni masikioni mwake.

"Haaa wewe ni nani na umefuata nini kwangu?" Awadh aliuliza baada ya kukutana na sura ya kazi iliyokuwa ikitokwa jasho huku mdomo wa bunduki ukiwa kichwani kwake Awadh.

"Labda mimi ndiyo nikuulize unatafuta nini huku mtoto mrembo kama wewe au ninyi ndiyo kundi la mzee mtekaji?" Mtu huyo aliuliza.
"Hapana wala siyo sisi kaka, tuko huku porini kuwafuata wenzetu ambao wametekwa na mzee Malick Bolenge lakini mpaka sasa hatujafanikiwa kuwapata kwani Kambi yao ni tupu zaidi ya mzee mmoja ambaye kaniambia wametoroka." Awadh alijibu akijivuta nyuma kidogo kidogo.

" Unaleta janja janja unajivuta kuelekea wapi unafikiri utafanikiwa katika hilo? Kitu muhimu hapa ni wewe kuongea ukweli wako tu na siyo kuleta longolongo hapa nitausambaza ubongo wako mara moja." Mtu huyo alimtisha Awadh.

Wakiwa wanaendelea na maongezi ya nani ni nani mara pikipiki ilianguka chini kwa kuwa hakuitega stendi vizuri na hivyo Awadh akataka kwenda kuiinua kutokana na sababu kuwa tenki lake ni kidumu cha lita tano ambacho juu ya kifuniko kuna paipu inayopitisha mafuta na hivyo kuhofia mafuta kuishia pale chini.

"Unanyanyua miguu kwenda wapi? Hebu utulize mshono wako kabla hujawa chakula cha wanyama sasa hivi." Mtu huyo alimzuia Awadh.

"Mafuta yataishia chini kaka." Awadh alimjibu.

"Kwa hiyo nilie mimi ambaye sina pikipiki?" Aliulizwa.

"Siyo hivyo kaka, nili...." Kabla hajamalizia kuongea alipigwa teke la tumbo lilimpeleka chini huku mkono wa kulia ukiwa umelishikilia.
"Mnafahamiana?" Awadh aliulizwa baada ya Adoyee naye kuletwa pale kutoka alikuwa kashikiliwa.

"Ndi..ndi..ndiy...o tuko pa..pa..pamoja." Awadh alijibu kwa tabu huku mkono ukiwa bado tumboni.

"Ulisema kuwa mmekuja kuwatafuta ndugu zenu ambao wametekwa na mzee Malick je ni wakina nani hao?" Mathew aliwauliza.

"Kwa sura hatuwajui kwa kuwa hatujawahi kuonana lakini majina yao kwa mujibu wa bosi ni Jumbe, Matthew na Soud." Alijibu Adoyee.

"Unasemaje weweeee? Unaleta utani siyo?" Aliuliza huku kakunja sura yake Jumbe baada ya kusikia majina yao.

"Hapana siyo utani ndivyo ilivyo jamani kwanini tudanganye?" Awadh alijibu.

"Na huyo bosi wenu anaitwa nani?" Soud ambaye aliwasogelea karibu baada ya kuanza kuwaamini hivi aliuliza.

"Anaitwa Madam Catherine naye alitekwa lakini tulifanikiwa kumtorosha kutoka kwenye chumba ambacho walimfungia na baada ya kufanikiwa hilo ndipo tuliporudi kuwaokoa vijana wake hao ambao tulijua wanaweza....."

"Kimyaaa." Jumbe alimkatisha Adoyee aliyekuwa akiendelea kueleza kisha akamwita Mathew pembeni huku Soud akibaki nao.

"Unasemaje juu ya maelezo yao tunaweza kuwaamini kweli siyo vijana wa mzee Malick hawa?" Mathew alimuuliza Jumbe.

"Kwa asilimia fulani naanza kuwaamini na asilimia nyingine itakamilika baada ya kumpigia simu bosi Catherine na sisi kuongea naye." Jumbe alimjibu.

"Tusipoteze muda tuwaambie wampigie simu haraka." Matthew aliongea huku akiwa kamshika mkono Jumbe wakirudi pale walipo wakina Adoyee.

"Ili tuweze kuwaamini mpigieni simu huyo Catherine tujue kweli yenu au janja janja." Jumbe aliwaambia wakina Awadh.

JE NI KWELI WAKINA JUMBE WANAKWENDA KUWAAMINI WAKINA AWADH NA KUUNGANA NAO?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA TUJUE MBIVU NA MBICHI.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 17
Sultan Uwezo
+255

Kauli ya Jumbe ilileta ahueni kwa Awadh na Adoyee ambao walitazamana kwa muda kisha wakakonyezana kuashiria kuwa kifo kimewapitia mbali hivyo Awadh aliingiza mkono mfukoni akatoa simu na kutafuta namba ambayo baada ya kuipata aliipiga na kuweka simu sikioni.

"Lakini dada mkubwa hajanunua simu nyingine bado ile ya awali aliipotezea kule porini alikokuwa kashikiliwa na watekaji."
"Kama hana simu huyo unayempigia ni nani au unataka kutuuza siyo?" Jumbe alimuuliza swali ambalo liliambatana na teke moja matata sana ambalo lilimpeleka chini Awadh na kupelekea simu kuanguka mita kadhaa pembeni.

"Bro mbona hatuaminiani? Yaani niwauze? Kwa bei gani hasa, sikia ndugu yangu michezo kama hiyo huwa sifanyi kabisa na huyo niliyekuwa nikimpigia ni mfanyakazi wake anaitwa Seynabou." Awadh alimjibu Jumbe akiupukuta mdomo uliokuwa umejaa vumbi. Bahati nzuri simu haikupata mushkheri iliendelea kuita hivyo Soud aliichukua na kuiweka sikioni.

" Unasikika ongea." Ulisikika upande wa pili baada ya kupokelewa. Soud akaona haina haja ya kuanza kujieleza akamkabidhi Jumbe ambaye aliiangalia tu kisha akamkabidhi Awadh.

"Naomba mkabidhi dada mkubwa simu." Aliongea Awadh na baada ya muda alianza kusimulia kilichowakuta huko porini.
"Kuna watu wametukamata na hawaamini kama sisi ni watu wako hivyo wamesema tukupigie ili waweze kuamini." Wakati Awadh akiendelea kuongea na Catherine, Jumbe alimnyang'anya simu na kuiweka sikioni.

"Unaongea na Jumbe hapa Mwamba usiokata tamaa kirahisi, nihakikishie juu ya hawa watu wasijekuwa ni wale wale." Jumbe aliongea kwa sauti ambayo ilimtisha kidogo Catherine.

"Ni Jumbe? Mbona sauti imebadilika?" Ilibidi aulize kwanza.

"Wala haijabadilika bosi wangu sema tu baridi la huku porini limetuathiri sana." Jumbe alifafanua.

"Poleni sana Chama langu vipi mko salama wote?" Catherine aliuliza.

"Si Soud wala Mathew ambaye anatatizo wote tu wazima wa afya kama utujuavyo vijana wako." Jumbe alimjibu.

"Nafurahi kusikia hivyo, kuhusu hao wakina Adoyee ni timu moja na ninyi ila wao ni kambi nyingine. Wako wawili ambao ni Adoyee na Seynabou na huyo Awadh ni 'new member' ambaye tumeungana naye kwenye harakati za kuwaokoa ninyi hivyo naomba muanze safari kabla Maadui wetu hawajawatia mikononi mwao."

"Sawa bosi lakini nikuhakikishie kuwa hawawezi kufanya hivyo tena walifanikiwa kututeka kwa kuwa silaha zetu tuliziacha kona fulani hivi kwa sasa tuko 'full' Nondo tunahamu nao mpaka basi." Jumbe alimjibu Bosi wake Catherine huku akimpa mkono Awadh ili amsaidie kuinuka.

" Sawa Jumbe lakini kwa sasa njooni kwanza ili tujipange kwani mpaka hapa tuna maadui wengi hivyo tukiingia kichwa kichwa tutaangukia pua." Catherine alikazia pointi yake baada ya kuona Jumbe ana hasira na mzee Malick.
"Nimekupata tuko njiani." Alimjibu na kukata simu.

"Nisikilizeni watu wangu, kwanza naomba tusameheane kwa kilichotokea hapa bila shaka kila mmoja anajua tuliyopitia hivyo isingekuwa rahisi kuwaamini lakini yote kwa yote yamepita tuianze safari moja tukiwa timu moja." Jumbe aliongea akiwa katikati ya vijana wenye sura za kazi ambao ni Adoyee, Awadh, Mathew na Soud.

" Kwa niaba ya mwenzangu Adoyee tumeshasamehe kwani tuko kwenye uwanja wa mpira ambao muamuzi alikuwa ni dada mkubwa Catherine. Hivyo kwa kuwa ninyi ni wageni itabidi tuwaongoze njia na sijui tufanyaje kuhusu pikipiki?" Awadh alikubaliana na yaliyozungumzwa na Jumbe kisha wote wakakumbatiana kuashiria mwanzo mpya, kundi jipya ambalo linakwenda kuyaanza maisha mapya. Na kuhusu pikipiki Adoyee alishauri kuwa Awadh arudi nyumbani akachukue gari huku wao wakiendelea kujivuta taratibu kuipunguza safari.

" Wazo hilo nakubaliana nalo ila itabidi hii simu mbaki nayo ili tusipoteze mawasiliano mimi nitachukua nyingine nyumbani kikubwa msiizime." Awadh aliwasihi katika hilo ambalo walikubaliana kwa pamoja kisha yeye aliwasha pikipiki na kuondoka.

***

Baada ya kuhitimisha siku zao za kuwepo mjini Morogoro ambazo walizitumia kwa mapumziko ili kuweza kumuonesha mazingira ya huduma ya Kanisa lao mgeni wao Mchungaji Rodney, waliianza safari yao ya kuelekea jijini Mbeya ambako Mchungaji Rodney hakujua atakuwa huko kwa muda gani kutokana na machafuko yaliyoibuka Kanisani kwake nchini Senegal.

"Kampuni hii haina muda mrefu katika kutoa huduma zake za usafirishaji abiria kati ya jiji la Mbeya na jiji la Dar es Salaam lakini cha kushangaza imekuwa maarufu sana utadhani ina miaka ishirini huko." Daktari Sylvester Kitesa alimwambia Mchungaji Rodney wakiwa wameianza safari ndani ya basi la Kampuni ya Sauli.

" Mmiliki wa mabasi haya ni Mtanzania au ni 'investor' kutoka nje ya nchi?" Mchungaji Rodney aliuliza akilitazama vizuri basi hilo ambalo ni miongoni mwa mabasi yanayoingia jijini Mbeya mapema zaidi ya mengine.

"Hakuna cha 'Investor' hii ni Kampuni ya mzawa kabisa tena kutoka nje ya miji ambayo imewekeza zaidi kwenye usafirishaji wa abiria, inaweza kuwa ndiyo Kampuni ya kwanza kutoka eneo hilo." Daktari Sylvester Kitesa alimjibu.

"Ni kutoka mji gani?" Mchungaji Rodney aliuliza tena.
"Kampuni hii yenye makazi yake jijini Dar Es Salaam lakini Tawi likiwa jijini Mbeya mmiliki wa kampuni hii anaishi wilayani Chunya, wilaya ambayo ni miongoni mwa zile zinazotoa dhahabu kwa wingi."

"Aisee kwa hiyo huko madini ni ya kuchota tu." Mchungaji alitania.

"Hapana si kawaida watu wanapambana sana huko mitaji inatumika na wengi wao wanaendelea kutaabika huku wachache ndiyo wananufaika na hayo madini ya dhahabu. Hivyo uvumilivu unahitajika huko Mchungaji." Daktari Sylvester Kitesa alizidi kumjibu Mchungaji na muda huo walikuwa wakiiacha Hifadhi ya Taifa ya Mikumi ambayo inachukua zaidi ya kilometa arobaini.

" Aisee Tanzania ni nchi nzuri sana katika maisha yangu sikuwahi kuwaza hata siku moja kama Tanzania ina uzuri huu. Na hapa tulipo sasa ni 'zoo' au?" Mchungaji Rodney alizidi kuchanganyikiwa.

"Hapana kijana wangu hii siyo 'zoo' bali ni Hifadhi ya Taifa ya Mikumi hapa unakutana na Wanyama wa aina mbalimbali na siyo hii tu tunazo nyingi sana tuna Serengeti, Ruaha, Ngorongoro na nyingine nyingi ambazo ukizitembelea hutotatamani kuondoka ndani yake."

Daktari Sylvester Kitesa alimjibu na kuendelea kumtamanisha Mchungaji Rodney ambaye muda huo alikuwa bize kuwapiga picha Twiga waliokuwa umbali kama mita thelathini hivi lakini kwa ubora wa simu yake ilikuwa rahisi kwake.

" Itabidi unifanyie mpango niishi Tanzania ili nizidi kuufaidi uzuri wa ardhi hii iliyobarikiwa haiwezekani Mbuga za Wanyama na Hifadhi nzuri kama hizi ziko kwenu tu, Madini adimu ya Tanzanite yako kwenu tu, Nchi isiyo na Corona ni yenu tu hapana mzee si kwa upendeleo huu ninahisi hapa kuna mibaraka mingi ambayo bado hamjaijua kama ipo." Mchungaji Rodney alimjibu Daktari Sylvester Kitesa ambaye alikuwa akitabasamu tu.

" Karibuni kwa huduma abiria wetu." Aliongea mhudumu.

" Tunashukuru sana mimi niletee maji ya baridi." Daktari Sylvester Kitesa alimjibu.

" Hata mimi niletee hayo hayo." Mchungaji Rodney naye aliagiza maji kama alivyofanya mzee Kitesa.

"Kwanini usiagize kitu kingine?" Mzee Kitesa alimuuliza Mchungaji.

"Ukiwa mgeni unatakiwa kuangalia mwenyeji wako anafanya nini usijidai mjuaji utaumbuka oohhooo." Majibu ya Mchungaji yalimfanya Daktari Sylvester Kitesa kucheka huku mkono ukiwa umeziba mdomo.

"Achana na mawazo ya watu wa mataifa kumbuka wewe ni mtumishi wa bwana au mambo yako yamekuchanganya?" Mzee Kitesa alimuuliza.

"Hapana mzee tunacheka tu umenisahau kijana wako?"

"Nikusahau wewe tena siwezi hata kidogo hasa nikikumbuka miaka ile tukiwa ziarani Israel namna ambavyo ulitaka kupotea." Mzee Kitesa alimjibu.

"Karibuni." Mhudumu alifika na kuwakabidhi maji kama ambavyo waliagiza.

"Asante dada yangu." Mchungaji alishukuru. Kwa hakika safari hii ilikuwa nzuri kwa upande wa Mchungaji Rodney ambaye alifurahi sana hasa kwa yale aliyoyaona njiani. Ikiwa ni saa kumi ya jioni basi lilikuwa likiingia ndani ya 'Mbeya Bus Terminal' maeneo ya Uhindini.

" Karibu sana jijini Mbeya Mchungaji." Daktari Sylvester Kitesa alimwambia Mchungaji wakati Basi likiwa linasimama.

"Asante sana mzee wangu nafurahi sana kuikanyaga ardhi hii ya Mbeya kwa mara kwanza." Mchungaji Rodney alimjibu huku akiigusa ardhi kwa kiganja chake cha mkono wa kulia.

"Bwana Yesu asifiwe." Kijana mmoja alifika walipokuwa na kuwasalimu.

"Amina Joseph, pole kwa kusubiri." Daktari Sylvester Kitesa alimjibu.

"Asante mzee wangu lakini nimefika muda si mrefu sana." Joseph alimjibu.

"Anaitwa Mchungaji Rodney kutoka nchini Senegal." Daktari Sylvester Kitesa alimtambulisha Mchungaji Rodney kwa Joseph ambaye ni dereva wa mzee Kitesa.

"Nashukuru kumfahamu karibu sana baba Mchungaji nchini kwetu Tanzania nchi ya asali na maziwa." Joseph alimkaribisha Mchungaji Rodney ambaye alitabasamu kwa maneno ya Joseph.

"Nashukuru sana Joseph nimeshafika nitafurahi sana katika kipindi hiki ambacho nitakuwa hapa ikiwa nitapata hiyo asali na maziwa." Mchungaji Rodney alimjibu Joseph akimpiga mgongoni.

"Joseph chukua hii mizigo iweke kwenye gari tuondoke mgeni wetu hajazoea baridi huyu asije tugandia hapa bure."

"Mzee bwana kwamba afya yangu ni ya kubusti kweli?" Mchungaji alimuuliza wakiingia kwenye gari.

"Sijasema hivyo, lakini unalionaje hili baridi?" Daktari Sylvester Kitesa alimjibu kwa swali.

"Mmhh linapuliza tofauti na Dar es Salaam pamoja na Morogoro huku ni nchi nyingine kabisa." Alimjibu. Gari liliondoka stendi hapo na kuelekea yaliko Makao Makuu ya Kanisa la 'JESUS OUR KING' ambalo liko chini ya Daktari Sylvester Kitesa ambaye ni Askofu na Kiongozi mkuu wa Kanisa hilo.

***

Awadh alifika nyumbani kwake ambako aliwakuta wakina Catherine wakiwa mezani wakiendelea kuchora ramani ambazo Awadh alizitazama lakini hakuelewa kitu. Baada ya kuwasalimu aliingia chumbani kwake na baada ya kurejea aliketi kuungana na wakina Catherine.

"Poleni na kilichowakuta huko porini." Catherine alimpa pole Awadh.

"Asante dada lakini tunashukuru Mungu kila kitu kimekaa sawa huko na sasa tu kitu kimoja." Awadh alimjibu.

"Nilipatwa na wasiwasi nikahisi tayari mmekutana na yule mzee asiye na haya." Seynabou naye aliongeza.

"Usijali Seynabou tuko salama na sasa Jeshi linarejea nyumbani tayari kwa vita mpya." Awadh alimjibu Seynabou kisha aliinuka na kuingia chumbani ambako hakukaa sana alitoka na kuwaelekeza kuwa anawafuata wenzake ambao wako porini wanamsubiri yeye.

"Basi sawa Awadh wewe wahi mkirudi tuanze mikakati mipya ya kumkabili kwanza mzee wangu Malick mpaka aeleze kwanini alifanya alichokifanya kuna kitu gani ambacho mimi sikifahamu." Catherine aliongea machozi yakimtoka.

"Madam wacha niende nikirudi kila kitu kitakuwa sawa." Awadh alimwambia Catherine baada ya kuona ameanza kulowanisha sakafu hivyo akaona arudi porini kuwafuata wenzake kabla hayajatokea mengine.

JE NINI KITAENDELEA BAADA YA TIMU HIZI MBILI KUUNGANA PAMOJA?

USIKAE MBALI NAMI TAFADHALI, WEKA BANDO LA KUTOSHA TAYARI KWA MTANANGE UNAOFUATA.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 18
Sultan Uwezo
+255

Aliwasili kule porini na kwa kuwa ilikuwa ni mida ya saa mbili usiku giza likiwa limelikamata anga vilivyo alikutana nao barabarani wakiwa taratibu huku kimvua kikinyesha. Kila walipokuwa wakiona gari lolote waliingia msituni na kujificha na ndivyo ilivyokuwa hata kwa Awadh, baada ya kuliona gari walifichama likapita.

"Huyu ni Awadh kapita." Adoyee aliongea baada ya kuliona gari likipita karibu na pale walipofichama.

"Umejuaje Mwamba kama ni yeye?" Mathew alimuuliza.

"Mataa yale ya juu ndiyo yamenitambulisha kuwa ni yeye lakini tusubiri mpaka atutafute tusije jiingiza motoni bure hapa." Adoyee alimjibu.

"Hayo ndiyo maneno asipotukuta atatutafuta mwenyewe." Jumbe aliongeza. Na haikuchukua muda simu iliita Jumbe aliitoa na kuipokea.

"Kapiga, haloo!" Jumbe aliongea.

"Mko wapi ninyi? Nimekaribia." Awadh alimuuliza.

"Si uko na gari lenye mataa ya juu?" Jumbe alimuuliza Awadh.

"Umejuaje kaka au nimewapita sehemu nini?" Awadh alimuuliza.

"Wingu la mvua lilitufanya tuanze mdogo mdogo hivyo geuza utatukuta hapa kwenye hili daraja."

"Okay kaka dakika sifuri niko hapo." Alikata simu. Jumbe akiwageukia wenzake na kuwaambia kuwa jamaa ni yeye.

"Ulikuwa sahihi ni yeye kasema dakika sifuri hivyo turudi barabarani." Jumbe aliwaambia wenzake akiinuka alipokuwa kakaa. Kama alivyoahidi haikuchukua muda mrefu gari lilifunga breki na kusimama.

"Kumbe waoga hivyo? Mmefichama mpaka sijawaona nilipopita." Awadh aliwatania wakati akishuka.

"Ni kawaida tu Awadh kumbuka huu ni usiku hivyo hatuwezi kumulikwa na kila gari tukidakwa tena?" Mathew alimjibu akisogea karibu.
"Jamani acheni maneno mvua inazidi tusije lala porini bure." Jumbe alimwambia Awadh baada ya kuona stori zinazidi.

"Sawa kaka mkubwa nimekupata ingieni tuondoke maana dada mkubwa ana hamu ya kuwaona huyo! Inaonekana ni muda mrefu hamjaonana naye." Awadh aliwaambia akifunga mkanda. Kisha safari ilianza mara moja na wakati huo mvua ilichanganya lakini kwa kuwa Awadh ni mwenyeji wa barabara ile haikuwa tabu kwako kuukabili usukani japo barabara haikuwa nzuri sana.

" Awadh naweza kukuuliza swali?" Jumbe alimuuliza.

"Uliza tu kaka mkubwa." Awadh alimruhusu.

"Umejuana vipi na Madam Catherine?"

"Mmh nilikutana naye kupitia hawa wakina Adoyee na Seynabou ambao walinisimamisha na kuniomba msaada wa kulifukuzia gari ambalo lilimchukua Madam. Ilikuwa ngumu kufanya maamuzi lakini baada ya kunisimulia kilichotokea niliingiwa na huruma kiasi cha kuamua kuwasaidia na ukizingatia huyo mzee aliyemteka Madam namfahamu vizuri sana kadhulumu nafsi za watu wengi sana kwa michezo yake ya kuteka na kuhitaji kiasi kikubwa cha fedha, ukishindwa kutoa kiasi hicho huwa haoni shida kuichukua roho yako."

Awadh alimjibu Jumbe swali lake kwa urefu kidogo.

" Okay, sasa serikali kwanini imemfumbia macho wakati shughuli zake ziko wazi?"Soud aliuliza tena.

" Unazungumzia serikali? Bro kuna serikali mbele ya noti kweli? Na kingine usichokijua kumhusu mzee Malick anashirikiana na baadhi ya viongozi wa vyombo vya Dora hivyo hata mumpeleke leo hachukui hata saa moja lazima atoke. Na ili kuwafumba midomo watu kaanzisha huduma ya kutoa tiba za asili tena ndani ya jengo la serikali lenye historia kubwa tu sijui wamemuuzia au kapanga hakuna ajuaye." Awadh aliendelea kufunguka juu mzee Malick Bolenge.

" Kwa hiyo unataka kusema kuwa utajiri alionao ni matunda ya utekaji watu? Na kwanini aliamua kumfanyia hivi Madam Catherine wakati ni Mjomba wake?" Mathew aliongeza swali jingine.

" Unajua nini ndugu yangu? Kwenye haya maisha kuna siri nyingi ambazo hatuzijui inawezekana kuna jambo lililo nyuma ya pazia wanalolijua wenyewe mpaka kufikia hatua hiyo ya kuchezeana rafu kama hizi." Awadh alijibu akikata kona kuingia nyumbani kwake na wakati huo mvua ilikuwa imekata ila radi ziliendelea kumulika na ngurumo za kutisha hazikukoma kuashiria kuwa muda si mrefu itashuka mvua ambayo ni kubwa zaidi ya iliyokata.

"Karibuni sana nyumbani kwangu na jisikieni mko maskani kwenu." Awadh aliwakaribisha wageni.

"Asante sana Awadh." Jumbe aliitikia.

"Waooo majembe yangu hayoo yamewasili kwa umoja wao, karibuni sana." Catherine aliwakaribisha vijana wake kwa furaha kubwa sana.

"Tumefika salama madam, pamoja na magumu yote tuliyokutana nayo lakini mwisho wa siku tumekutana tena." Jumbe alimwambia Catherine akiwa kakumbatiana naye.

"Mungu ni mkubwa Jumbe." Catherine alimjibu huku akiwaonesha ishara ya kuingia ndani. Waliingia ndani na kukutana meza iliyochafuka kwa vyakula vya kila aina. Soud na Mathew walichanganyikiwa baada ya kuviona vile vyakula na ukizingatia wana muda mrefu hawajapata chakula cha maana kama kile, hivyo walikaa tayari kuanza kula.

"Jamani ndiyo nini sasa muanze kula katika hali hiyo? Hii meza ni kwa ajili yenu wala haiondoki ogeni kwanza badilini mavazi kisha mketi kwa chakula au mnasemaje?" Catherine aliwazuia.

"Tumekuelewa bosi sema njaa ndiyo ilitusogeza hapa lakini wacha tukaoge kwanza kisha tufanye maangamizi mezani." Mathew alimjibu akimpa msaada wa kuinuka Soud.

"Awadh kama utuonavyo hatuna nguo za kubadili kama una za ziada tusaidie ili hizi zetu tuzifue." Jumbe alimvuta pembeni Awadh na kuomba nguo.

"Usijali kaka kwenye kile chumba pale kuna kabati la nguo mtachagua zinazowatosha." Awadh alimwelekeza Jumbe ambaye hakutaka kusubiri alienda kuangalia.

Na wakati huo Awadh alitoka nje na kuingia kwenye gari na kuondoka akiwaacha wageni wake.

"Awadh anakwenda wapi tena?" Seynabou alimuuliza Catherine.

"Mimi tena? Nitajulia wapi kaondoka tukiwa wote hapa hivyo kuniuliza swali kama hilo ni kunionea tu mdogo wangu. Vipi umeanza kumuelewa nini?" Catherine alimjibu Seynabou.

"Nani? Huyu Awadh? Walaaa nilikuwa nauliza tu maana katoka kimya kimya."

"Sema kama tayari umeanza kuoza sehemu ya moyo wako, usijifiche ukatuletea majanga mengine hapa." Catherine aliendelea kusisitiza.

"Ningekuambia dada." Seynabou alimjibu.

"Haya bwana utakavyoona." Catherine aliongea akiwa kamkazia macho Seynabou. Na wakati huo huo wakina Jumbe walikuja na kuungana nao pale mezani walipokuwa wamekaa.

"Niliwakumbuka mpaka basi watu wangu." Catherine aliwaambia.

"Kuna mbu kule porini acha tu mpaka nilihisi kuugua." Soud alianza utani wake.

"Huna lolote mbona porini ulikuwa kama umepigwa 'super glue' hapa unajidai muongeaji mwenyewe." Mathew alimwambia Soud tayari alishaanza kujipakulia chakula hakutaka kusubiri karibu wakati anakiona.

Wakiwa wanaendelea kupata chakula mara Awadh aliingia akiwa na boksi mkononi ambalo lilikuwa limefungwa kwa 'ribbon' maalum. Seynabou aliinuka na kwenda kumpokea boksi hilo.

"Awadh mbona na maboksi?" Catherine alimuuliza.

"Timu imekamilika na kila mtu ana furaha ya ajabu kukutana na mwenzake lakini kwangu imekuwa ni tofauti sana Madam. Unajua nini? Miaka kadhaa huko nyuma niliwahi kuwa ndani ya kundi moja ambalo lilijihusisha na burudani hapa St. Louis. Lilikuwa ni kundi maarufu sana hakuna ambaye hakulijua, tulikimbiza zaidi kwenye maonyesho ya majukwaani.

Lakini kama wasemavyo watu kutoka Afrika Mashariki kuwa 'Kizuri huwa hakidumu' ndivyo ilivyokuwa kwetu kwani tukiwa tumetimiza miaka mitatu ya Umaarufu kundi letu la 'THE MAGICIAN' lilipata ajali mbaya sana ya majini...." Alishindwa kuendelea alianza kulia kitu kilichomfanya Jumbe kuinuka alipokuwa kaketi akila na kumfuata Awadh.

" Pole sana Awadh inaonekana siyo kumbukumbu nzuri kwako."

"Kaka acha tu nikiwakumbuka rafiki zangu Hemedy, Smith, Gadsden, Paul na msichana pekee kwenye kundi Teresa 'Black Angel' inaniuma sana." Awadh alimjibu.

"Ndiyo nini kuleta kumbukumbu za kuhuzunisha? Hebu acheni basi." Catherine aliona awakatishe.

"Iko hivi ndugu zangu tarehe kama ya leo miaka minne iliyopita nilitenganishwa na rafiki zangu ambao walikuwa ni zaidi ya marafiki.

Nakumbuka siku hiyo ilikuwa Jumamosi tulipanga tukapumzishe vichwa ufukweni, kuna ufukwe mmoja uitwao 'Maucha Beach' ni maarufu sana huu Ufukwe. Basi tulipofika huko tulijiachia wenyewe kwa raha zetu ikiwa ni bata juu ya bata.

Jamaa yetu Smith alitoa wazo kuwa tukodi boti itupeleke umbali wa kilometa kama kumi kuingia ndani zaidi ya bahari ili tukirudi nyumbani tuwe na 'story' mpya. Na kwa kuwa kila mmoja alikuwa pombe hakuna ambaye alibisha isipokuwa mimi nilikuwa kinyume nao kwa kuwa mimi na maji mengi ni sawa na mbingu na ardhi hivyo niliwaambia gharama nitachangia ila siyo kwenda.

Walinicheka sana na kuniita Jogoo la shamba na hawakuwa tayari kuchukua hata kumi yangu walidai hawawezi kuchukua hela ya jogoo poyoyo hivyo waliingia ndani ya moja ya boti ambazo zilipaki pale ufukweni wakiwa na mzuka sana makelele kwa wingi kumbe ile ilikuwa kama kuagana vile kwani ndani ya dakika ishirini hivi nikiwa na napasha kuna boti ilikuja na kutoa taarifa kuwa kuna boti imezama baada ya kukumbwa na dhoruba, nilipouliza ni boti gani hiyo nikajikuta naangusha kilio baada ya kubaini ni ile waliyokuwa wamepanda rafiki zangu.

Boti za Msalaba mwekundu zilifanya kazi yake ya kujaribu kuokoa maisha ya rafiki zangu lakini waliambulia miili tu iliyokuwa kuwa imeshaharibika kwani ilipatikana baada ya siku tano.

Kilikuwa ni kipindi kigumu sana kwangu kuyapoteza majembe yangu ambayo tulikuwa marafiki toka shule. Toka hapo nilibadili gia na kuamua kuishi maisha mengine kabisa ambayo nitawasimulia siku nyingine." Awadh alihitimisha akilia kwa kwikwi.

" Kama simulizi yenyewe itakuwa kama hii ni bora ubaki tu haiwezekani badala ya kufurahi tunalialia tu." Seynabou aliongea wakati Awadh akiwaacha na kuelekea chumbani kwake.

" Kumbe Awadh kapitia magumu huyu? Na watu wa hivi ni wazuri sana kushirikiana kwenye kazi." Catherine alijikuta akiongea wakati macho yake yakimuangalia kila mmoja kwa zamu.

"Hebu fungueni hilo boksi tujue kaleta nini kwa ajili ya kumbukizi hii." Jumbe aliagiza boksi lifunguliwe.

"Hapana hatutakuwa sahihi kwa kuwa Awadh ndiye mwenye tukio hili na pia kumbukeni kuwa katufanyia kama 'surprise' hivi hivyo wacha tumsubiri mwenye shughuli yake tuache viherehere." Mathew alipingana na kauli ya Jumbe.

"Tukio ni letu sote ndugu zangu hivyo hatuna budi kushiriki wote humo kwenye boksi kuna 'WINE' maalum ambayo rafiki zangu waliipenda hivyo nikaona niinunue ili usiku wetu uwe mfupi sana." Awadh alitokea nyuma yao na kumjibu Mathew.

"Kwa hiyo ni mwendo wa kuvunja glasi?" Soud aliuliza.

"Yes brother" Awadh alimjibu. Wakati wanaendelea na kujadili nini kifanyike kwenye usiku wa kumbukumbu ya rafiki zake Awadh, Seynabou alikuwa kainamia laptop akifuatilia kitu ambacho aliagizwa na Catherine.

"Dada njoo uone." Seynabou alimwita Catherine.

"Umefanikiwa mdogo wangu?" Catherine alimuuliza akimfuata pale mezani.

"Naweza kusema hivyo dada yangu si unakijua kichwa changu dakika mbili kinakuwa kimenasa maelezo." Alimjibu.

"Mmhh okay nimekupata, kwa hiyo huyu kiumbe hayupo nchini? Hebu ifuatilie hiyo 'code number' ni ya nchi gani." Catherine alimuagiza Seynabou.

"Hebu lete niifanye mimi hiyo kazi." Awadh aliongea akinyoosha mkono kuitaka laptop. Seynabou alimkabidhi na hapo hapo aliinamia na kuanza kufuatilia ile 'code number' kujua ni ya nchi gani.

"Yes, nimemnasa tayari Madam huyu mzee yuko nchini Mali." Awadh alimjibu.

"Mjomba umeondoka saa ngapi nchini? Unafikiri umepona? Labda siyo mimi Mjomba wangu." Catherine aliongea mkono ukiipiga meza.

JE NINI KITAENDELEA?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.
1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 19
Sultan Uwezo
+255

Baada ya kuburudika usiku ule kwa kumbukizi ya rafiki zake Awadh waliofia baharini kwa ajali ya boti miaka kadhaa iliyopita kila mmoja aliingia kulala kwa ajili ya kupumzisha mwili kwa sababu ni siku nyingi walikuwa hawajapata usingizi wa kutosha zaidi ya purukushani tu zisizokwisha.

"Mbona mwili umetapakaa matope asubuhi yote hii?" Seynabou alimuuliza Awadh aliyemkuta katika hali hiyo mara tu baada ya kuamka.

"Ndiyo maisha yangu haya Seynabou, kuna jamaa yangu alinifuata asubuhi kunitaka msaada baada ya gari lake kumgomea huko porini wakati akienda shambani. Sasa eneo lenyewe lilikuwa na tope hilo acha tu ila kwa kuwa ndiyo kazi yangu niliingia mzigoni.

" Pole sana kaka yangu kumbe oga maji niliyokuwa nimemchemshia madam kwa kuwa yeye bado unaufidia usingizi wewe kayaoge kisha nimtengee mengine." Seynabou alimwambia Awadh.

"Nashukuru sana Seynabou lakini maji ya moto mimi ni msamiati sijawahi nishazoea ya baridi." Awadh alimjibu Seynabou.
"Mmh hebu oga ya moto baridi hili ni kali sana ujue." Seynabou alisisitiza.

"Nikwambie kitu dada yangu?" Awadh alimuuliza swali.
"Kitu gani hicho?"
"Uko tayari nikwambie? Jibu moja."
"Okay niambie." Seynabou alimjibu.

"Nitaoga wakati mwingine kwa ajili yako lakini leo wacha nioge tu ya baridi kwa kuwa nishaloa kwa mvua." Awadh alimwambia.
"Utajua mwenyewe bwana mimi nilifanya hivyo kwa kukuonea huruma tu sasa kama wewe mwenyewe hujionei huruma mimi ni nani mpaka nikulazimishe?" Seynabou ni kama hakufurahishwa na majibu ya Awadh aliongea akiingia ndani. Awadh aliishia kumtazama tu kisha akatingisha kichwa na kuendelea kuliosha gari lake lililokuwa tope tupu.

" Mbona makelele asubuhi asubuhi jamani?" Catherine aliuliza baada ya kumuona Seynabou akiongea peke yake sebuleni.
"Si Awadh huyo, mwili mzima umetapakaa matope sijui alikuwa wapi huko kwenye ufundi wake namwambia aoge maji ya moto ili kuupa mwili joto lakini yeye kashikiria historia tu eti hajawahi oga ya moto." Majibu ya Seynabou yalimfanya Catherine kuanza kucheka.

"Sasa mdogo wangu kuna ubaya gani hapo sasa? Kakueleza ukweli kuwa hajawahi kuoga maji ya moto kazoea ya baridi, na wewe unataka kumlazimisha je huwa yanamletea tatizo?" Catherine alimjibu.

"Nilijua na wewe utakuwa upande wake tu, haya mmeshinda basi." Seynabou alimjibu Catherine akielekea chumbani huku Catherine yeye akitoka nje akiwa na kikombe mkononi pamoja na mswaki. Lakini baada ya kufika nje alishangaa kumuona Awadh akiwa kachafuka sana sambamba na gari ambalo alilitumia.

" Mhh kweli wewe ni mtu wa kazi yaani asubuhi yote, baridi lote hili lakini wewe umelivaa tope kiasi hicho?"
"Unajua nini dada yangu ukiachana na kila kitu ninachokifanya lakini ufundi magari pamoja na mitambo mingine ndiyo shughuli inayoniweka hapa mjini." Awadh alimjibu.
"Hongera sana."

"Nashukuru." Awadh alimjibu akifunga mlango wa gari.
"Halafu kabla sijasahau tunafanyaje kuhusu kile tulichokibaini jana?" Catherine alimuuliza.
"Muda ule nilitamani tuimalize pale pale sema ninyi shangwe liliwazidi kiasi cha kunizuia nisiendelee. Ngoja nioge kisha tutulie kufuatilia kuona kama bado yuko Mali au kaondoka si unajua ni bilionea yule anaweza kufanya lolote na wakati wowote ule." Awadh alimjibu.

" Ni kweli kabisa hebu jiandae waamshe na hao jamaa zako tuanze michakato asubuhi hii hii mikono yangu inawasha sana ina hamu ya kumkamata Mjomba wangu mzee Malick Bolenge."

" Nipe dakika kama kumi tu hivi." Awadh aliongea akimpita Catherine kuingia ndani.
" Poa." Catherine alimjibu na kuendelea kunawa uso. Wakati akiendelea kuuweka sawa uso wake kuna wazo lilipita kichwani kwake kama umeme.

" Mjomba alijuaje kama wakina Jumbe wako kule porini na kwanini aliwateka?" Na hapa ndipo alipopata wazo la kumpigia simu ili aone atasema nini, alirudi ndani na kuichukua simu ya Seynabou na kumpigia.

"Mhh mbona hapatikani? Ndiyo kusema kabadilisha tayari namba yake au?" Alijiuliza baada ya kumkosa hewani. Akaona isiwe shida akamwita Adoyee aliyekuwa koridoni akipiga miayo tu.
"Naam Bosi." Aliitika.

"Njoo na laptop ya Awadh mara moja."
"Sawa, hivi vitu vyetu tutavichukua lini kule kwa mzee Malick? Si unajua vitu kama Laptop yako viko kule na ile ni muhimu sana kwa shughuli yetu iliyo mbele." Adoyee alimuuliza.

" Ni kweli lakini si rahisi kihivyo tunatakiwa kupanga mikakati imara kabla ya kuelekea huko si unajua yule ni adui yetu kwa sasa?" Catherine alimuuliza.
" Najua hilo Madam." Alimjibu

"Lete kwanza laptop kuna jambo nina wasiwasi nalo." Alimsisitiza Adoyee akalete laptop. Adoyee aliingia mpaka chumbani kwa Awadh na kuichukua laptop ambayo ilikuwa kitandani ikiwa imeshawashwa na kutoka nayo, alipitia chumbani kwao na kuwaamsha wakina Jumbe ambao walikuwa wamejiachia kwenye magodoro yaliyokuwa yamewekwa chini na hili lilikuwa ni wazo la Mathew ambaye alishauri kuwa waachane na vitanda waweke magodoro chini ili waufaidi vizuri usingizi usio na bughudha.

"Wanangu ee amkeni tayari kumekucha Madam ana mzuka kama wote." Adoyee aliwaambia wakina Jumbe ambao walikuwa bado wanajigeuza geuza kwenye malalo yao.

"Oyaa mwamba ee wewe si tayari umeshamaliza kiasi cha usingizi ulicholipia wenzako tulilipia bando kubwa hivyo bado kabisa, unaweza kuondoka wivu wa nini?" Mathew alimjibu akigeukia ukutani.

"Poa lakini ujumbe umewafikia tayari." Alimjibu na kutoka.
"Lakini nimeikuta imewashwa kabisa sijui alitaka kufanya nini?" Adoyee alimwambia Catherine akimkabidhi laptop.

"Hakuna tatizo kama kuna programu aliifungua ambayo hainihusu nitaachana nayo." Catherine alimjibu akianza kugusa batani za laptop huku Adoyee akiondoka na kumuacha peke yake.

"Msirudi kulala tena jiandaeni tuanze zoezi mapema maana kazi ya leo naiona ngumu kwa kiasi fulani hivi." Catherine alimwambia Adoyee aliyekuwa akielekea chumbani kwao.

"Nakwenda kuchukua mswaki na kuwaamsha wakina Jumbe." Alimjibu.
"Fanyeni haraka bwana."
"Sawa bosi." Adoyee alimjibu.

"Mhh sasa mbona simu yake haipatikani wakati kwenye 'signal' inaonekana iko 'active'?" Catherine alijiuliza akichukua simu kuijaribu tena namba ya mzee Malick.

"Dada mbona unaongea peke yako na wewe? Kuna usalama?" Seynabou alikuja na kumuuliza Catherine.
"Kuna kitu kinanichanganya hapa huyu mzee anaonekana bado yuko nchini Mali lakini cha ajabu nikiipiga simu yake haipatikani." Catherine alimjibu.

"Mzee Malick anaweza kutuchezea mchezo namfahamu vizuri sana si mwepesi kama ambavyo ulimdhania." Awadh alijibu akiketi karibu yao.
"Anaweza kufanya nini Awadh?" Catherine alimuuliza.

"Kuna kitu kinanizunguka kichwani sitaki kukiamini mpaka tukifanyie kazi kwanza." Awadh alimjibu.
"Kitu gani hicho Awadh?" Seynabou alimuuliza.

"Cha kufanya kwa sasa ni sisi kufungua kinywa kwanza kisha tugawanyike makundi mawili, moja liende nyumbani kwake na jingine hotelini kwake huko tunaweza kupata majibu ya maswali yetu." Awadh aliwajibu.

"Kwa hiyo unahisi anaweza kuwa bado yuko nchini?" Catherine alimuuliza.
"Kitu kama hicho japo sina uhakika." Awadh alimjibu akibonyeza batani za rimoti ya televisheni.

"Habari za hivi punde zinasema kuwa baada ya kutafutwa kila kona ya nchi hatimaye Mchungaji Rodney wa Kanisa la 'JESUS OUR KING' kaonekana nchini Tanzania yaliko makao makuu ya Kanisa hilo. Hiyo ni kwa mujibu wa mtoa taarifa aliyeomba kutotajwa kwa jina lake kuhofia kusimamishwa kazi kanisani hapo.... Nikuombe uendelee kuwa nasi kwa Habari zaidi. Nikutakie asubuhi njema. Niite Gladness Pittsburgh wa 'National Television'." Taarifa hii iliwafanya wakina Catherine kutazamana kwa muda kabla ya kuongea chochote.

" Anajisumbua tu yeye anatakiwa arejee nyumbani kwani kufia ugenini hakuna ladha yoyote." Catherine aliongea huku uso wake ukiwa umejaa tabasamu kuashiria nguvu ya ushindi.
"Maskini ya Mungu huyo ndiyo...." Kabla hajamalizia kuongea Awadh Catherine alimkatisha.

"Yes, ndiyo mume wangu huyo mwanaume ambaye aliyachukua maisha ya mama yangu kipenzi kwa maslahi yake na kanisa lake kisa tu alimwambia amechoka kudanganya mbele ya Madhabahu ya Bwana." Catherine alimjibu Awadh.
"Kivipi madam?" Awadh alivutiwa na hii simulizi.

"Mama yangu katokea katika familia ya kimaskini sana hivyo miaka kadhaa huko nyuma alitoka kijijini na kuja mjini kutafuta kazi na baada ya kuhangaika sana kwa muda mrefu bila kupata kazi alikata tamaa mpaka alitamani kurejea kijijini kuishi maisha ambayo aliyazoea japo hakuyapenda. Ndipo siku moja akiwa anakatisha maeneo ya 'shopping center' moja ambayo haina haja ya kuitaja jina lake alikutana na mama mmoja ambaye alijitambulisha kwa jina la Oliver Lunyatoga ambaye alijitolea kumsaidia baada ya kumueleza hitaji lake.

Na kweli kama alivyomuahidi kesho yake alimpeleka mpaka kanisani kwao huko ndiko walikutana na Mchungaji Rodney ambaye alifurahi kumuona mama yangu na baada ya kuelezwa shida ya mama yangu Mchungaji alimuahidi kumfurahisha. Kwanza kabisa walimshawishi mama yangu kuokoka na kwa kuwa shida yake ilikuwa ni kufanikiwa maishani na alishaahidiwa hivyo hakuona shida kukataa alikubali kuokoka.

Baada ya kuokoka mama na wenzake kumi hivi walipelekwa nchini Nigeria kwa ajili ya Mafunzo maalum ambayo yalikuwa ni ya kimbinu. Mafunzo hayo yaliwachukua miaka mitatu na baada ya kuhitimu walirejea mjini ambapo Kanisa lilianza kufanya Mikutano mbalimbali ya injili ambayo iliambatana na uponyaji wa magonjwa mbalimbali huku Vilema 'fake' ambao ni wakina mama walikuwa wakiponywa hadharani kitendo ambacho kililifanya Kanisa kukua na kujipatia Umaarufu sana." Catherine aliendelea kuwasimulia mkasa wa mama yake na Mchungaji Rodney.

" Ni hadithi ya kuvutia sana hii inahitaji umakini zaidi." Jumbe aliongea akikaa vizuri.
" Madam samahani umesema kuwa mama alikuwa anafanya vitu vya ku'fake' kivipi?" Soud aliuliza.

"Mama yangu na wenzake walikuwa wanauwezo wa kufanya chochote watakachoagizwa na viongozi wa Kanisa kulingana na eneo ambalo watakuwa wamekwenda Kuhubiri na mkumbuke alisomea taaluma hiyo kwani walikuwa wana uwezo wa kuigiza Utahila, ulemavu wa Viungo vya miguu na mikono na huwezi kuwashtukia hata kidogo pia hata ububu."

" Mhh hiyo ilikuwa ni hatari sana eehh nini kiliwatokea?" Seynabou alimuuliza kwani hata yeye pamoja na kuongea vitu vingi vya maisha ya nyuma lakini hakuwahi kuambiwa hadithi hii.

" Kuna wakati ulifika mama yangu alichoshwa na maisha ya maigizo hivyo akawashauri wenzake wagome. Na kweli walikubaliana lakini mwisho wa siku kuna mwanamke mmoja aliwasaliti na kwenda kupeleka taarifa kwa Mchungaji Rodney ambaye aliwafanyia kitu mbaya sana yeye na rafiki yake ambaye ndiye alimpokea mama kama mnakumbuka wakati naanza aitwaye Oliver, aliwachukua na kuwaua kwa kuwapiga risasi kwenye msitu wa Casamance ambapo maiti zao zilikuja kuonekana baada ya siku wiki moja zikiwa zimeharibika sana kilichotambuliwa ni nguo zao." Kufikia alianza kulia kitu kilichowafanya waanze kumnyamazisha. Alitulia kidogo kisha aliendelea na simulizi.

" Najua mtakuwa na shauku ya kutaka kujua mimi nilizaliwa kipindi gani na baba yangu yuko wapi na ni nani alinipa hizi taarifa. Kifupi mama yangu wakati anakuja mjini kutafuta unafuu wa maisha mimi nilikuwa nimeshazaliwa na nilikuwa na umri wa miaka kumi na tatu na nilikuwa nikiishi na bibi yangu mzaa mama kwani sikuwahi kumjua baba yangu, taarifa hizi nilizipata kwa bibi yangu ambaye alikwenda kujiuliza kwa wataalam wa jadi kujua mwanaye aliuawa na nani.

Na hakwenda kwa mmoja la hasha aliwatembelea zaidi ya watatu lakini wote jibu lilikuwa ni moja tu kama haitoshi hata baada ya mimi kuja mjini na kukutana na mtu huyo huyo ambaye nilimtageti na yeye kuingia kwenye kumi na nane zangu na kunioa nilibaini vitu vingi sana kuhusiana na kifo cha mama yangu kwani alikuwa akiongea wazi kabisa baada ya kuona mimi mwenyewe nashabikia mambo yake ya kuwaua wale wote wanaokwenda kinyume naye." Alihitimisha baada ya kukatishwa na Jumbe ambaye muda wote alikuwa akifuta machozi kutokana na simulizi hiyo kumgusa.

" Jamani ee hebu tuachane na simulizi hiyo kwanza chai inapoa na mkumbuke kuwa baada ya hapa tunaelekea wapi?"
" Ni kweli kabisa Madam hebu tuiweke 'pending' hii simulizi tuianze ratiba yetu ya leo japo ni inavutia na kuumiza." Seynabou aliunga mkono.

"Pamoja na yote mimi niko tayari kuungana nanyi katika hii vita ya kuhakikisha waliohusika wote wanalipa kwa ubaya wao." Awadh aliongea kitu ambacho kiliwafanya wote kumtazama kwani baada ya kusema hivyo aliichomoa bastola yake na kuilamba.

JE KUILAMBA BASTOLA KUNAAMAANISHA NINI?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA TUPATE KUJUA KITAKACHOTOKEA KWA KUNDI HILI AMBALO NAWEZA KUSEMA NI KAMA NDIYO LIMEZALIWA UPYA.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 20
Sultan Uwezo
+255

"Madam tunaomba muongozo maana naona tukiendelea kukaa hapa mezani hatutaifanya ya leo ambayo kwangu naiona ni ngumu sana." Jumbe aliongea baada ya kuona kila mmoja hajafanya maandalizi.

"Jamaniii si tumalizie kifungua kinywa kwanza?" Seynabou aliona aulize.

"Toka tumeanza, mimi ninaona tujiandae kwa 'lunch' tu na si kingine hapa tunaendelea kupoteza muda jamani vipi?" Jumbe alikuwa mkali kidogo, kwa sauti aliyoitoa kila mmoja mle ndani alitulia.

"Naombeni mnisikilize Wanajeshi wangu, tutakuwa na maeneo mawili ya kazi kama tulivyoelekezana mnajua. Wafuatao watakwenda nyumbani kwa mzee Malick Bolenge nao ni Adoyee, Soud na Awadh waliobaki yaani Jumbe, Seynabou na Mathew ninyi mtaelekea hotelini kwake pale TRAVIS MARK HOTEL na kwenye maeneo hayo yote kazi itakuwa ni moja tu kupata majibu ya wapi alipo mzee Malick na kama kutakuwa na ugumu tumieni hata nguvu ikihitajika kufanya hivyo kwa mnaokwenda nyumbani kwake mlifanikiwa kuingia ndani msisahau kuchukua mizigo yetu yote. Kama kuna swali niulizeni mara moja." Catherine alihitimisha kugawa majukumu.

" Ndiyo Seynabou nakusikiliza." Alimpa nafasi Seynabou aweze kuuliza swali lake.

" Wewe utakuwa wapi maana kote haujatokea?"

" Fanyeni nilichowaagiza mkirudi mtanikuta mimi nitabaki kurekebisha masuala fulani hivi si mnajua kwa sasa hatuna zana za kutosha? Hivyo natakiwa nifanye michakato ya kuhakikisha hilo linakuwa siyo tatizo kwetu hata kidogo." Alijibu.

Baada ya kupata majibu hayo kila mmoja aliingia kuchukua silaha ambayo alihisi inaweza kumsaidia mbele ya safari na kisha walitoka na kuondoka kama walivyoelekezwa.

" Msifanye makosa huko." Catherine aliwasisitiza wakipanda kwenye magari ambayo yaliandaliwa na Awadh kwa shughuli hiyo. Kisha alirudi ndani kuwaacha waianze safari kama walivyopanga na baada ya kuingia ndani alipitiliza chumbani moja kwa moja huko alijiandaa na kutoka, na kwa kuwa pale ndani hakukuwa na magari mengine ya maana zaidi ya yale yanayohitaji akili na nguvu sana kwenye uendeshaji wake hivyo alitoka na kuelekea barabarani ambako alipanda Bajaj ambayo haikuwa na abiria wengine zaidi yake kwa hilo tu alimshukuru Mungu.

"Samahani kaka naomba unifikishe TRAVIS MARK HOTEL mara moja, sijui utanitoza kiasi gani?" Catherine alimwambia dereva Bajaj.
"Kwa kule ukinipa shilingi elfu tatu siyo mbaya dada yangu." Alimjibu.

"Okay kanyaga mafuta tuwahi kuna jambo la muhimu sana pale."

"Sawa dada." Dereva Bajaj alimjibu na kuikoleza Bajaj yake kutimiza matakwa ya abiria wake. Muda wote Bajaj ilipokuwa ikikata mitaa Catherine alikuwa kimya sana na muda mwingine alikuwa alikuwa akibonyeza vidole vyake vya mkononi huku macho yake yakiangaza nje mara kwa mara kama vile kuna kitu alikihitaji kwa wakati huo kutoka nje. Walipofika eneo moja hivi ambalo siyo mbali sana kutoka Hotelini kuna kitu alikiona hivyo hivyo kumtaka dereva asimamishe Bajaj.

"Hatujafika bado dada."

"Ni kweli lakini nishushe tu hapa kaka yangu." Catherine alimjibu dereva Bajaj huyo.

"Okay sawa." Alisimamisha Bajaj pembeni na kumgeukia mteja wake.

"Si panatosha hapa?" Alimuuliza.

"Wala usijali panatosha sana hapa, naomba unipe baki yangu tafadhali." Catherine alimjibu akimpa hela yake.

"Okay, hii hapa dada vipi naweza kukusubiri?" Alimuuliza akimpa chenji yake.

"Noo, unaweza kuendelea na pilika zako tu kaka." Alimjibu na kuondoka. Aliingia kwenye duka moja hivi ambalo lilikuwa limeandikwa SHOOTERZ humo kulikuwa na kila aina ya silaha.

"Kwema kaka!" Alimsalimu kijana aliyemkuta mle ndani.

"Kwema karibu tukuhudumie." Alimjibu.

"Mbona bango haliko wazi kiasi hicho kaka yangu?" Catherine alimuuliza kijana huyo.

"Dada unakuwa kama mgeni na wenye dola yao? Japo kuna muda inatuletea ugumu kwenye biashara lakini ndiyo hivyo tunafanyaje sasa." Alimjibu.

"Okay sawa nahitaji bastola aina ya MAC-10 ya mwaka 1970 'original' kutoka USA? Naweza kuipata?"

"Hiyo inapatikana wenyewe tumezoea kuiita kishingo." Alimjibu akielekea zilikokuwa zimepangwa.

"Enhh inakwendaje hiyo?" Catherine alimuuliza.

"Haina bei sana dada yangu ni dola 2450 lakini hatutoi risiti." Alimjibu.

"Unamaanisha nini kusema sipati risiti?" Catherine alishtuka kusikia hivyo.

"Hizi ni za dili hivyo huwa tunagawana hasara na wakubwa." Kijana huyo alimjibu akiwa kwenye kabati la silaha.

"Okay sawa haina shida." Catherine alimjibu huku akiangalia nje kama kuna watu wanaokuja pale dukani. Na baada ya kuona ni salama kabisa alimsogelea yule aliyekuwa bize kuitafuta hiyo bastola.

"Nifungie nne zikiwa 'full' nikitoka hapa ni mwendo wa kuzitumia tu." Catherine aliongeza.

"Sawa dada." Kijana huyo alimjibu. Alizipata na kuziweka kwenye boksi zake na wakati akikagua ni kipi kakisahau alishtukia tu kitu cha baridi kinagusa shingo yake.

"Upole wako ndiyo uhai wako tofauti na hapo natenganisha shingo na kiwiliwili, sawa?" Catherine aliongea kwa sauti ya kunong'ona masikioni mwa kijana huyo.

"Sa..sa..sawa da...da yangu mbona mimi sina tatizo kabisa hata kama kuna vingine unahitaji nitakupa." Kijana huyo aliongea huku akitetemeka.

"Huwa sipendi maneno mengi kamilisha mzigo niondoke na pia niwekee boksi mbili za visu kisha zifunge kwenye boksi moja tu ili nisipate tabu wakati natoka." Catherine aliendelea kumtia hofu kijana wa watu kwani wakati anaongea hayo kisu kilikuwa kinasuguasugua ngozi ya shingo.

" Nimekuelewa dada." Alimjibu.

Na baada ya kila kitu kuwa sawa Catherine alimtaka kijana huyo ambebee hilo boksi mpaka zilipopaki Taxi.

"Sasa utalibeba hilo boksi mpaka zilipo Taxi na kitu muhimu cha kuzingatia ni kuwa mpole kama hujafanyiwa kitu kibaya, nataka sura yako yenye tabasamu iwe hivyo hivyo mpaka nitakapoondoka ukifanya tofauti sijui nitakufanya nini?" Catherine alimpa maagizo.

" Nayapenda maisha yangu siwezi kufanya tofauti na maagizo yako." Kijana huyo alimjibu akiliinua boksi tayari kwa kutoka.

" Simama kwanza wewe mbona haraka kiasi hicho." Catherine alimzuia kijana huyo kwa mbele kisha akatoa kila kilichokuwa mifukoni mwa kijana huyo kuanzia simu pamoja na hela kisha akaongozana naye kutoka nje huku akimsemesha semesha.

"Ninapoongea unatakiwa uwe unatabasamu siyo kulikaza sura lako, sawa?" Catherine alikazia maneno yake.

"Sawa dada." Alimjibu wakitoka. Kutokana na kisu kilichokuwa shingoni lakini kikiwa hakionekani kutokana na staili ambayo alikikamata. Na kama zali pale nje hakukuwa na mtu yeyote hivyo ilikuwa ni rahisi kwao.

"Jamani hapo hapo msiiondoe riziki yangu nilikuwa nashtua tumbo mara moja." Dereva wa Taxi ambayo walifikia aliongea akija kasi huku mikono yake ikitambaa tumboni kwake kujifuta.

"Unakaaje mbali na ofisi bwana Chuma, fungua mlango basi." Kijana yule aliongea huku akilazimisha tabasamu.

"Kila kitu kiko sawa Murchison mwambie mteja wako aingie tu."

"Dada unaweza kuingia sasa huyu ni dereva mzuri sana atakufikisha uendako." Murchison alimwambia Catherine akiwa kaushikilia mlango.

"Tanguliza boksi kisha fuata wewe." Catherine alimbadilikia Murchison aliyefikiria zoezi limekwisha kumbe alifikiria tofauti.
"Da....(alimkatisha)"

"Shiiiiii... ingia garini sihitaji maneno." Kijana wa watu akiwa kamtolea macho Catherine aliingia garini pamoja na boksi Catherine naye akafuata na kufunga mlango.

"Na wewe......" Kabla hajamalizia sentensi yake Catherine alimuwekea kisu shingoni.

"Acha udadisi usiokuhusu ondoa gari haraka."

"Sawa Madam." Chuma alimjibu na kuondoa gari. Walipotoka nje ya mji na kuufikia msitu wenye miti mirefu na iliyofunga na wenye kutisha alimuamuru dereva aiache barabara hiyo inayokwenda mpaka wa Mali na kuingia porini.

"Katisha hapo mbele fuata hiyo njia kulia kwako." Catherine alitoa maelekezo.

"Sawa dada." Chuma aliitikia na kufuata maelekezo.

Mwendo kidogo mbele alimtaka dereva asimame wakati huo tayari kijana yule muuza duka la silaha alishalala nusu kaputi kwani sumu ilishamtafuna. Kumbe kile kisu kilikuwa na sumu kitendo cha kuikata ngozi ya shingo kidogo tu sumu ilishapenya na vivyo hivyo kwa dereva naye alianza kuona kizunguzungu.

"Umenifanya nini dada mbona sioni mbele vizuri?" Chuma aliuliza mikono ikifikicha macho. Catherine alishuka haraka na kumvutia chini dereva ambaye aliendelea kufikicha macho yake kisha alimvuta Murchison chini akaingia garini akaifunga milango na kuondoa gari kwa kasi.

" Sijawahi kosea hata siku moja kwenye kazi zangu kituo kinachofuata ni ndani ya mji wa Dakar huko wataujua muziki wangu si wanajua nimekufa." Alianza kucheka Catherine huku mikono ikipigapiga usukani.

Gari liliendelea kupasua misitu na mabonde kuutafuta mji wa Dakar

ambao anaufahamu vizuri sana kwa kuwa kauishi kwa muda mrefu na hivyo hakuna hata kona moja ya mji huo asiyoifahamu, lakini wakati mwingine alipofikiria zaidi alianza kulia na bila shaka hayakuwa machozi ya furaha kutokana na kisasi kilicho moyoni mwake.

"NIMETOKA KIDOGO WANAJESHI WANGU HIVYO KAMA MMEKAMILISHA ZOEZI NILILOWAPA NISUBIRINI MPAKA NIRUDI LAKINI KUWENI MAKINI NA WATU WA MJOMBA WANGU." Ulikuwa ni ujumbe ambao uliingia kwenye simu ya Awadh. Na baada ya kuusoma ujumbe ule aliwageukia wenzake.

"Jamani eehh Madam sijui kaelekea wapi?"

"Kwa ninavyomjua Bosi wetu anaweza akawa kaelekea Mali kumfuata mzee Malick." Adoyee alijibu.

"Jamani ee achaneni na hizo habari hebu kaeni sawa kwa kuingia ndani." Soud aliwaambia baada ya kuona wenzake wamejisahau wapo eneo gani.

"Okay sawa kumbe wewe kaka Awadh na Adoyee pitieni lango la nyuma la jumba hili na mimi nitasalia hapa kufanya doria." Soud aliwaambia Wenzake ambao walikuwa wakiweka sawa silaha zao.

"Kuwa makini kaka wacha tuzame ndani." Adoyee alimsihi Soud kisha wao wakaondoka.

Waliingia ndani kupitia mlango wa nyuma na moja kwa moja wakaelekea mpaka vyumbani ambako walihifadhi vitu vyao.

"Mmh mbona nyumba imepoa kiasi hiki kuna usalama kweli?" Adoyee alimuuliza Awadh.

"Achana na mawazo hayo kikubwa tuwe makini tu." Awadh alimjibu. Walikagua vitu vyao wakakuta viko salama wakatoka na kuingia chumba ambacho kilitumiwa na Catherine pamoja na Seynabou nako kama kawaida walikuta kila kitu sawa baada ya kukagua. Walibeba yale mabegi haraka na kuanza kutoka.

" Hamtakiwi kurusha hata hatua moja kutoka mlipo." Ilisikika sauti nzito nyuma yao na kuwafanya kutii.

MOTO UNAENDELEA KUWAKA, JE NINI KITAWATOKEA WALE WATU KULE MSITUNI, VIPI KUHUSU CATHERINE ANAFUATA NINI DAKAR? NA WAKINA AWADH WAMEKUTANA NA KISIKI GANI?

MAJIBU YOTE NI KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 21
Sultan Uwezo
+255

Adoyee alimtazama Awadh ambaye alimpa ishara ya kutii amri, hivyo waliweka chini bastola zao chini mabegi yakiwa migongoni.

Mmoja wa wale watu alisogea na kuinama kuzichukua zile bastola alianzia ya Adoyee na kisha akaigeukia ya Awadh, alifanya kosa alipompa mgongo Adoyee akiinama kuiokota bastola ya Awadh kwani Adoyee alimtazama kwanza yule aliyekuwa kasimama kawanyooshea bastola akagundua kuwa kajisahau hivyo haraka sana aliingia katikati ya miguu ya mtu yule ambaye bila shaka ni mmoja wa vijana wa mzee Malick Bolenge aliyekuwa kainama kuiokota bastola ya Awadh na kumfanya kijana yule kuanguka chini kama gunia la pamba na bila kuchelewa Adoyee alimfuata na kumpiga kichwa cha utosi kilichomfanya ashindwe kujimudu, yule mwenzake alipigwa na butwaa asijue afyatue risasi au afanye nini kwani lilikuwa ni tukio ambalo hakulitarajia na wakati akitaka kufanya maamuzi alishachelewa kwani Awadh aliviringika kwa kasi ya ajabu kuelekea alikokuwa bastola mkononi akimfyatulia risasi zisizo na idadi.

"Hamuwezi kuucheza mchezo huu ninyi vikaragosi." Awadh aliongea akiinuka baada ya kujiridhisha kuwa mpinzani wake alishakufa huku damu ikiendelea kuukataa mwili wake. Kwa upande wa Adoyee yeye alikuwa kambananisha vilivyo huyu mwingine baada ya akili kukaa sawa kutokana na kichwa alichogongwa.

" Sasa tunaweza kuongea kirafiki kabisa kwa kuwa sisi si kama ninyi mnaovizia wanaume wakiwa kazini haya niambie nani kawatuma kwetu?" Adoyee alimuuliza kijana huyo ambaye macho yalikuwa yamemtoka isivyo kawaida kutokana na kutazamana na mdomo wa bastola.

"Mimi hata sijui lolote niliambiwa na mwenzangu Keita kuwa kuna bosi kamwambia tumlindie nyumba yake mpaka atakaporudi na kwa kuwa nilikuwa sina kazi nilikubali." Alimjibu.

"Keita ndiyo nani?" Adoyee alimuuliza.

"Yule kule aliyelala."

"Aliyelala? Sema aliyekufa humu umebakia wewe tu na ukileta jeuri ya kutudanganya unamfuata." Awadh alidakia.

"Bila shaka umesikia hivyo hatutegemei brabra hapa, sawa?" Adoyee alimwambia akimgonga uso kwa mdomo wa bastola.

"Ndiyo kama nilivyokujibu kaka wala sijakudanganya." Kijana huyo aliongea.

"Wewe ni mwenyeji hapa?" Awadh alimuuliza.

"Ndiyo kaka." Alijibu.

"Mmh kwa hiyo unacheza na akili yangu siyo? Si umetoka kuniambia kuwa Keita alikupa dili kutoka kwa bosi mmoja ukimaanisha humjui." Adoyee alimsogelea karibu zaidi na safari hii alimkusanya shati kwa mbele huku sura yake ikiwa sambamba na ya huyo kijana.

"Ni kweli kabisa mimi simfahamu bosi wetu na wala sijawahi kuonana naye mawasiliano yote yalikuwa yakifanywa na Keita." Alimjibu.

"Una roho ngumu sana kwa ninavyokuona, hii nyumba ni ya nani?" Adoyee aliendelea kumbananisha huku Awadh akimkagua mifukoni.
"Mwenye hii nyumba?" Alirudia kuuliza kama vile hakusikia vizuri.

"Usitucheleweshe kaka tuma shughuli nyingi za kufanya tupe jibu haraka,, unafikiri haya ni matangazo ya vifo?" Mara hii Adoyee alimtolea utafikiri ndiyo alikuwa akimtazama kwa mara ya mwisho.

"Unamchelewesha tu huyo si unajua wa hivyo hata uwafanye nini hawaongeagi ukweli malizana naye fasta tutoke humu ndani." Awadh alimwambia Adoyee akiurekebisha mkanda wa begi lake.

"Naombeni msiniue nitawaambia kila kitu nimekumbuka."

"Una dakika moja tu ya kuvuta hewa safi ongea haraka." Adoyee alivurugwa.

"Bosi wetu ni mzee Malick Bolenge na ndiye mwenye hii nyumba." Aliona aongee ukweli tu maana kauli ya Awadh haikuwa salama kwake.

"Kwa sasa yuko wapi?" Awadh alimuuliza.

"Yuko Hotelini kwake."

"Hotelini kwake? Kivipi?" Adoyee alishangaa.

"Siwezi kuwadanganya yuko huko kaka." Alijitetea.

"Unauhakika na unachokiongea? Hajasafiri?" Adoyee alimuuliza.

"Hajasafiri yuko kule." Majibu yale yalimfanya Awadh atoe moja ya simu aliyoikuta kwenye mifuko ya Keita akaiwasha.

"Mpigie simu bosi wako huyo mwambie Keita hali yake ni mbaya sana."

"Sawa, sawa." Aliitika akiipokea simu. Na baada ya kuipiga haikupatikana namba ya mzee Malick.

"Hapatikani."

"Unasemaje?"Awadh alimsogelea na kumkita kisu cha tumbo kisha akamsindikiza kwa risasi ya kichwa.

" Hauwezi kutupotezea muda wetu kiasi hiki."Aliongea Awadh wakati kijana huyo akitapatapa pale chini.

" Chukua simu hiyo tuondoke zetu." Alimwambia Adoyee wakati yeye akianza kuondoka.

" Oya vipi kwema humu? Nimeona hamtoki nikajua mmekumbana na misukule maana mjumba wenyewe haueleweki huu." Alitokea Soud na kuwauliza.

"Acha maswali kaka okota zile silaha pale zinaweza kutusaidia mbele ya safari." Adoyee alimjibu.

"Okay sawa, lakini mnauhakika kama walikuwa ni hawa hawa jumba zima?" Soud aliuliza tena.

"Endelea kuuliza hapo hapo ukitosheka na maswali yako utatufuata." Adoyee alimjibu akitoka anakimbia. Soud hakuwa na la kufanya zaidi ya kuzihesabu hatua zake kutoka nje. Walifika nje moja kwa moja wakaingia kwenye gari, Awadh akaliwasha na kuondoka zao.

"Kuna kitu sijakielewa hapa mjue?" Awadh aliongea.

"Kipi hicho?" Soud aliuliza.

"Kama ni kuhusu mzee Malick mimi ndiyo nimechoka kabisa." Adoyee aliongeza.

"Ikoje kwani?" Soud ilibidi aulize baada ya kuona wenzake kuna jambo wanalijua.

"Kama ambavyo tulihisi ndivyo ilivyo mzee baba hayuko Mali tunaye mjini hapa hapa, sijui wakina Jumbe watakuwa wamefanikiwa?" Awadh alimjibu Soud na kuuliza swali.

"Sasa kama yupo hapa hapa na vipi kuhusu ile signo kuonekana nchini Mali?" Soud alitaka kujua.

"Soud unapouliza unatakiwa uwe unafikiria kwanza huu ni wakati gani?" Awadh alimjibu kwa swali.

"Basi bwana yaishe, unanikazia sauti utafikiri mimi ndiyo mzee wenu Malick." Soud hakutaka makuu.

"Acha hizo kaka kwa hiyo umeshachukia?" Adoyee alimuuliza.

"Niacheni bwana." Soud alijibu akigeukia mlangoni.

"Yaani hili jamaa sijui Madam aliitoa wapi maana mambo yake yamejaa utoto tu sasa hapa kipi kimemnunisha." Awadh aliongea akishuka baada ya kulipaki gari sehemu yake walikuwa wameshawasili nyumbani kwao.

"Unakwenda wapi hebu simama hapo." Soud aliongea akishuka na kumfuata Awadh aliyekuwa akielekea ndani.

"Unataka kufanya nini?" Awadh aliuliza baada ya kuona Soud anamfuata kwa kasi.

"Soud una nini wewe?" Adoyee alimuuliza.

"Unataka kujua?" Soud aliuliza akiiweka sawa bastola yake.

"Muache afanye anachotaka kufa si amedhamiria hilo huwezi kujua mzuka wake unamuongoza nini kwa wakati huu.

" Nakuona mrembo sana Awadh huwezi kucheza na mimi hata mara moja usione ni mpole hivi ukajua ni moto wa makaratasi, huu ni moto wa pumba za mpunga ambazo huwaka taratibu bila papara hivyo tuheshimiane sana." Soud alimwambia Awadh maneno hayo kisha akaishusha bastola yake ambayo alishamuwekea kichwani.

" Nimekuelewa Mwamba, lakini haikuwa kwa ubaya nilikuwa natania tu si unajua tena kazi yetu hii muda mwingine tunatakiwa tufurahi sasa kama tutakuwa tunanyanyuliana vyuma itakuwaje? Lakini usijali nimekuelewa katika hilo sitakukwaza tena." Awadh aliona ajishushe baada ya kuona Soud kapaniki isivyo kawaida.

" Ndiyo nishamaliza hivyo huwa sipendi kudharaulika hata kidogo." Alikazia akikaa chini pale pale nje akionekana kachukia kutokana na kauli za Awadh. Adoyee alimuangalia kwa muda kisha alimfuata pale alipokaa.

"Msamehe tu mshikaji alikuwa anatania, si unajua sisi ni timu au umesahau?"

"Najua hilo." Alimjibu.

"Kama ndiyo hivyo basi tusiruhusu pepo la hasira kupita katikati yetu badala yake tumruhusu utani awe sehemu ya maisha yetu.

Tukiruhusu hasira tutakuwa na mwisho mbaya hebu angalia kama pale umemnyooshea bastola unafikiri nini kingetokea? Sijapenda hata kidogo." Adoyee aliongea maneno yaliyoonekana kumuingia vilivyo Soud ambaye aliinuka na kuingia ndani ambako alimfuata Awadh na kumtaka radhi. Walisameheana na kisha walitoka nje na kumkuta Adoyee akiwa bado kaketi pale chini akiwa mwenye mawazo mengi.

"Mbaba usiwaze sana tumezika mgogoro wetu ni ukurasa mpya sasa." Awadh aliongea akimshika bega Adoyee ambaye aliinua kichwa na kuwaona wako pamoja.

"Mambo si hayo sasa washikaji zangu." Adoyee aliinuka na kuwakumbatia kwa furaha huku kila mmoja akionekana mwenye furaha sana.

"Woyo woyo woooyoooo piga keleleeee!!" Awadh alipiga kelele.

"Oya tuingieni ndani tupange mipango tuna kazi ya kufanya mbele yetu." Adoyee aliongea baada ya kuona furaha inazidi katikati yao wakati wako kwenye uwanja wa vita.

Wakiwa bado katikati ya furaha mara simu ya Awadh iliita.

"Simu inaita hiyo." Soud alimwambia Awadh ambaye alionekana kutojali.

"Sijui ni nani huyu?" Aliongea akiitoa mfukoni na kuangalia mpigaji ni nani.

"Ni Seynabou huyu sijui kuna nini huko?" Aliongea akiiweka sikioni simu.

"Unasemaje Seynabou?" Awadh aliuliza.

"Aaagh kakata, oya ee hali ni tete kule wakina Jumbe yamewakuta."

"Yamewakuta? Kuna nini?" Adoyee aliuliza.

"Seynabou kapiga simu akiongea kwa sauti ya chini sana inavyoonekana ni kama kajificha hivi." Awadh alimjibu.

"Tunasubiri nini sasa?" Adoyee aliuliza akiingia ndani kasi.

"Sikilizeni ndugu zangu tusikurupuke huko huwezi jua inawezekana wametekwa na kuwashinikiza na sisi twende huko tukadakwe hivyo basi lazima tujiandae." Soud aliwaambia wenzake walioonekana kuwa na moto.

"Unasema nini Soud?" Awadh alimuuliza.

"Hebu twende ndani kwanza tukaichore ramani ya eneo hilo na namna tutakavyoingia." Soud alimjibu akimshika mkono. Waliingia ndani na kumwita Adoyee aliyekuwa chumbani akijiandaa.

"Fanya haraka basi." Soud aliita.

"Ninyi tayari?" Aliuliza akiwa anatoka.

"Mbona siwaelewi washikaji mnapata wapi nguvu ya kutulia wakati wenzetu wamebananishwa huko." Aliuliza baada ya kuwakuta wenzake wamekaa.

"Labda sisi ndiyo tukuulize wewe unakwenda kufanya nini?" Awadh alimuuliza Adoyee aliyekuwa akihema juu juu viatu mkononi. Swali hilo lilimfanya atulie kidogo kwani hakujua alijibu vipi.

JE NI NINI KITATOKEA?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 23
Sultan Uwezo
+255

Alipoingia kwenye kile chumbani alimfuata Mchungaji Rodney Hauser na kumkagua mifukoni mwake na kufanikiwa kutoa waleti pamoja na simu nyingine aina ya 'Motorola smartphone T45' kisha akaviweka mfukoni mwake.

"Mchungaji Simon endeleeni na maombi ngoja mimi nifanye kazi moja hivi." Daktari Sylvester Kitesa alimwambia.

"Sawa baba, mlango wa ofisi uko wazi haukufungwa." Mchungaji Simon Mwaiduko alimwambia kiongozi wake.

"Okay basi endeleeni na maombi akizinduka na kila kitu kuwa sawa mtaniita."

"Sawa baba." Mchungaji Simon Mwaiduko alimjibu. Kisha Daktari Sylvester Kitesa alitoka na kuelekea iliko ofisi ya Kanisa hilo na baada ya kuingia alirudisha mlango, akatoa vitu alivyovitoa kwa Mchungaji Rodney na kuviweka mezani kisha alivua koti lake na kuliweka nyuma ya kiti. Alisogea mbele kidogo akavuta pumuzi kwa nguvu kisha alifumba macho na kuanza kuomba kwa Mungu.

"Ee Mungu baba nakushukuru kwa Upendo wako na Baraka zinazoendelea kumiminika ndani ya jengo hili. Nasema asante sana na sisi tukiwa kama daraja na waonyesha njia hatutachoka kuwaongoza wapendwa wako malangoni mwako, imani yetu ikaimarike kila iitwapo leo ili majaribu ya wakala wa Shetani walio kila kona chini ya jua wakashindwe. Ni katika wewe unitiaye Nguvu, nikiomba na kushukuru. AMEEN!" Kisha alirejea kitini akaketi na kuanza kuikagua ile waleti ya Mchungaji Rodney.

" Ooh my God! Nini hiki? " Daktari Sylvester Kitesa alijiuliza mara baada ya kukikuta kibahasha cha kaki kilichokuwa na vifuko vidogo viwili vya nailoni kimoja kikiwa na unga mweupe na kingine kikiwa na unga mweusi. Hii ikamfanya azidi kuikagua ile waleti vizuri, alijikuta mwili ukitokwa na kijasho chembamba kilichotiririka kwenye uti wa mgongo wake na hii ni mara baada ya kukutana na shanga nyeupe iliyotungwa kwenye kiuzi cheusi.

"Mhhh Mchungaji Rodney ni Mungu gani unayemuamini wewe?" Daktari Sylvester Kitesa alijiuliza akivirudisha vile vitu vilimokuwa kwenye waleti.

"Ee Mungu tupe jicho la tatu lenye nguvu tuweze kuyaona ya sirini." Alishukuru akiitoa simu ya awali ambayo ilipotea ujumbe uliomfanya Mchungaji Rodney kupoteza fahamu kisha akaichukua namba ile na kuipiga.

"Haloo!"

"Haloo, naitwa Daktari Brown Lutasya naongea na nani tafadhali?" Alijitambulisha baada ya kuipokea simu.

"Daktari Sylvester Kitesa hapa, bila shaka wewe ni miongoni mwa wazee wa Baraza la Wadhamini wa Kanisa la JESUS OUR KING nchini Senegal sijui niko sahihi?" Aliuliza.

"Hujakosea ni kweli kabisa na wewe je?" Aliuliza baada ya kukubali.

"Mimi ndiye Mkurugenzi mkuu wa Makanisa haya nchini Tanzania lakini pia nahudumu mara moja moja Makao makuu jijini Mbeya." Alimfafanulia.

"Ooh Bwana Yesu asifiwe Kiongozi!" Utambulisho huo ulimshtua kidogo Daktari Brown kwani hakutarajia kuongea na kiongozi kama huyu.

"Amina Daktari mwenzangu, nafurahi sana kuona Kanisa letu lina Madaktari wa kutosha. Wanasemaje Senegal?"

"Haswaa baba kiongozi, huku si kwema kabisa kwani Mchungaji wetu Rodney hajapatikana mpaka leo..."

"Kwani alipotea?" Daktari Sylvester Kitesa aliuliza kama vile hajui kinachoendelea.

"Ni muda mrefu sana na hii ilikuja mara baada ya mke wake na mlinzi kupotea na kuuawa lakini mama Mchungaji kaonekana jana usiku nyumbani kwao aliingia na kisha kutoka akitumia moja ya magari yao." Daktari Brown alieleza.

"Una uhakika ni yeye? Na mlifuatilia kujua anaelekea wapi?" Aliuliza Daktari Sylvester Kitesa.

"Kiukweli hatuna uhakika wa moja kwa moja kwani taarifa hizi tuliambiwa na jirani yao aliyenipigia simu na tukapata uhakika kidogo kuwa inawezekana baada ya kufika pale na kutolikuta gari moja ambalo alipenda kulitumia yeye mama Mchungaji."

"Polisi mlikwenda kutoa taarifa hizi?"

"Hapana baba Kiongozi." Alijibu Daktari Brown.

"Okay hebu fanyeni uchunguzi wa chini chini kujua yuko wapi ikiwa ni pamoja na kutafuta mawasiliano yake."

"Sawa baba."

"Basi fanyeni hivyo na sisi huku tukiendelea kumtafuta Daktari Rodney." Daktari Sylvester Kitesa aliongea.

"Kuna tetesi zinasambaa kuwa yuko huko Tanzania sijui ni za kweli?" Aliuliza.

"Hizo ni tetesi tu kiongozi na kama ni za kweli basi tutamuona wala msihofu."

"Sawa baba."

"Tujuzane kila hatua ambayo mtaifikia."

" Bila shaka kabisa Kiongozi." Daktari Sylvester Kitesa alikata simu baada ya mlango kugongwa aliuangalia kisha akatoa vitu pale mezani akainuka na kwenda kuufungua.

" Mchungaji kuna Habari gani huko?" Alikuwa ni Mchungaji Simon Mwaiduko ndiye aliyekuwa akibisha hodi.

" Mungu mkubwa baba Kiongozi mgeni wetu ameshazinduka tayari."

"Asante Mungu wangu, asante sana kamleteni sasa." Alifurahi sana kupata taarifa hii ya kuzinduka Mchungaji Rodney.

"Sawa baba Kiongozi." Mchungaji Simon Mwaiduko alijibu na kutoka. Na kumuacha Daktari Sylvester Kitesa akiendelea kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa muujiza alioufanya.

"Ni muda muafaka wa kupata machache kutoka kwake yanayomhusu mke wake." Aliwaza Daktari Sylvester akiwa kaiinamia meza.

***

Awadh alibana kwenye ukuta wa nyumba ya jirani na Hotel ya mzee Malick ambapo kuna mtu alikuwa akija kasi huku risasi zikimfuata nyuma.

" Mamaaaaa........ " Ulikuwa ni mlio wa maumivu makali baada ya kukutana teke kifua kutoka kwa Awadh aliyekuwa kajiandaa. Na kabla hajamsogelea mtu huyo alishafika Jumbe akiwa kachakaa huku sura yake imetapakaa damu.

"Awadh? Mlikuwa wapi?" Jumbe aliuliza akimrukia kwa furaha.

"Tutaongea lakini huu si muda muafaka." Awadh alimjibu akimsukuma pembeni Jumbe kumuepusha na risasi ambayo mtu yule alikuwa anajiandaa kuifyatua kisha yeye Awadh akamshindilia za kutosha kichwani na kifuani.

"Asante brother." Jumbe alimshukuru akimuangalia mtu huyo.

"Usijali, umemtambua?" Awadh alimuuliza.

"Huyu ni miongoni mwa vijana wa IT wa mzee Malick Bolenge ndiyo waliotufanyia shambulizi la kushtukiza kiasi cha kummaliza Mathew." Alimjibu.

"Kwa hiyo ni kweli Mathew hatuko naye?" Awadh aliuliza kwani hakuamini ambacho alichoambiwa na Seynabou.

"Ni kweli tupu wala si utani kaka hawa jamaa si watu wazuri hata kidogo huko ndani kulikuwa kudogo acha tu." Jumbe alimjibu akitema mate yaliyochanganyika na damu.

"Poleni sana, na vipi kuhusu Seynabou?"

"Yule mwanamke nilimdharau duu ni moto wa kuotea mbali kawasambaratisha huko wee acha tu kwanza hebu twende alikuwa akifukuzana na dada mmoja mle ndani." Jumbe alimjibu wakiondoka mbio. Waliupanda ukuta na kutinga ndani ya Hotel kwa kutumia mlango wa 'Emergency' ambao waliutumia wakati wanatoka na kijana aliyesambaratishwa na Awadh. Walishachelewa kwani waliwakuta wakina Adoyee wakiwa na Seynabou wanakikagua kile chumba chenye kompyuta ambazo baadhi yake zilikuwa zimechakazwa na risasi.

"Wanajeshiiii....!" Awadh alipiga kelele baada ya kuiona timu yake.

"Hapana chezea hili 'crew' ni moto mwingine kabisa omba usikutane nao." Seynabou alijibu akikumbatiana na Awadh.

"Kwanza poleni kwa yaliyowakuta." Awadh aliwapa pole.

"We acha tu Awadh yaani ile namaliza kukutumia ujumbe wa mwisho jinga moja hili hapa likiwa limevurugwa, si likamvaa Jumbe ambaye hakuwa na silaha yoyote muda huo na kuanza kupimana ubavu. Jumbe alimsambaza chizi yule we acha tu lakini bado nikaona anamchelewesha si nikamfyatulia risasi iliyozua tafrani mle ndani kwani waliokuwa nje wakajua tuko kwenye kile chumba." Seynabou aliwasimulia.

" Kilichoendelea baada ya hapo?" Soud aliuliza.

" Unauliza kilichofuata Soud? Muulize Jumbe nilichowafanya pale mlangoni." Seynabou alimjibu.

" Kila aliyekuwa akiingia ndani alikutana na risasi ya kichwa kutoka kwa Seynabou mpaka yule mmoja aliyekuja dirishani na kuachia risasi ambayo hata hivyo haikuwa na madhara lakini ndiye aliyesaidia wanne kuingia wakati sisi akili ikiwa dirishani wao ndiyo wakatuvaa na kuanza kutudunda. Lakini tuliwaonesha ni kwanini sisi ni timu ya ushindi." Jumbe alimaliza.

" Poleni sana ndugu zetu, lakini kuna mtu mmoja haonekani hapa?" Adoyee aliuliza.

" Nani mzee Malick?" Seynabou alimuuliza.

" Huyo huyo."

"Lile dingi ni chawi wala si hivi hivi kwani wakati kimechanganya alitoroshwa na mmoja wa wafanyakazi wake ila kuna yule mpishi niliyepiga na kumfungia kule uliko mwili wa Mathew ndiye ataeleza kila kitu ikiwa ni pamoja na kuchimba kaburi." Seynabou alimjibu akiwaongoza wenzake kwenye hicho chumba.

" Vipi kuhusu hiki chumba?" Soud aliuliza.

"Mfumo umeharibiwa hapo hakuna jipya." Awadh alimjibu wakitoka lakini Soud kwa hasira alirudi na kuzisambaza zile zilizosalia na baada ya kuridhika alitoka zake.

"Oyaa tokeni haraka shoti imeanza kwenye kile chumba."

"Nini wewe?" Seynabou aliuliza.

"Acha maswali jengo linashika moto muda si mrefu." Soud alijibu akiushika mkono wa Seynabou na kuanza kumvuta.

"Ndiyo umefanya nini sasa?" Seynabou alimuuliza Soud ambaye hakujibu zaidi ya kuongeza hatua kuelekea nje.

"Ongeza spidi ninyiii....!!!" Awadh aliwaambia baada ya kuona limeanza kuwaka moto. Kama bahati hivi ile wanafika tu nje jengo liliwaka moto.

"Soud utatuua wenzako bwana ndiyo nini sasa?" Adoyee alimuuliza.

"Sikutarajia hili kutokea mimi nilikuwa nahesabu nyingine kabisa."

"Hesabu gani hizo bwana angalia sasa tumeshindwa kuuzika mwili wa mwenzetu Mathew." Seynabou alimuuliza.

"Tuangalie tunatoaje taarifa kwa dada mkubwa hili lilishatokea tayari hakuna haja ya kutupiana lawama, ama vipi?" Jumbe aliwaondoa kwenye malumbano na kuwataka kuangalia Catherine anapataje ujumbe. Wakiwa wanajadiliana hilo mara simu ya Seynabou iliita ikabidi aipokee.

" Uko wapi dada? " Seynabou alimuuliza.

" Kuna sehemu niko nipe habari ya huko." Catherine aliuliza.

"Huku mambo ni magumu dada mzee Malick hatujafanikiwa kumtia mikononi badala yake tumempoteza Mathew inauma sana." Seynabou alimjibu.

"Unasemaje?" Catherine alimuuliza.

"Ndiyo hivyo na hapa bado tuko nje Hotel tukiishuhudia inavyoteketea." Seynabou alimjibu lakini Catherine hakuongeza neno zaidi ya kukata simu.

"Anasemaje dada mkubwa?" Awadh aliuliza.

"Amepaniki si unamjua mambo yake? Kakata simu." Seynabou alimjibu.

"Tuondokeni mahali hapa najua muda si mrefu tutapokea simu ya dada kiongozi ya maelekezo hivyo tunatakiwa kufanya maandalizi." Jumbe aliwaambia wenzake waliokuwa wamekaa macho yakiwa kwenye Hotel ya TRAVIS MARK iliyokuwa ikiishia lakini kilichoanza kuwatisha zaidi ni kitendo cha moto kuhamia nyumba ya jirani ambayo haikuwa ya biashara bali ya mtu binafsi ya kuishi.

" Janga jingine hili?" Seynabou aliongea baada ya kuuona moto unavyohama.

"Hili giza kwetu ni msaada hebu tuondokeni haraka kabla chochote hakijatokea hapa." Awadh aliongea huku akiwapa ishara wakina Seynabou kuingia kwenye gari.

"Tunapitia mtaa wa nyuma ambako tulilificha gari letu." Awadh aliwaambia wenzake.

"Washa gari kaka." Jumbe alimwambia Awadh akihisi kama vile anachelewesha muda, waliondoka eneo hilo huku kwa mbali wakisikia mlio wa king'ora.

JE NI NINI KITATOKEA?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA TUPATE KUJUA MBIVU NA MBICHI KWENYE KIGONGO HIKI.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 24
Sultan Uwezo
+255

Hali haikuwa shwari muda huo hasa baada ya kukisikia king'ora kikiendelea kupiga kelele nyuma yao, kila mmoja alikuwa akimtazama mwenzake pasipo kuongea chochote lakini macho yaliongea kila kitu.

"Jumbe izime hiyo taa tafadhali naona kama inatuchora tu." Seynabou alimwambia Jumbe aliyekuwa pembeni yake.

"Mbona hata mkono wako unaifikia swichi? Si uizime mwenyewe." Jumbe alimgomea.

"Kaka si uizime? Mwenzako hapa naona tumbo linanivuruga balaa."

"Haya bwana furahi basi nimeizima." Jumbe aliizima.

Lakini Awadh alikuwa bize kwenye usukani kuhakikisha kuwa gari iliyo nyuma yao haiwasogelei hata kidogo na katika hilo alifanikiwa kwani walianza kuliona kwa mbali hii ilileta faraja ndani ya gari.

"Kaka Awadh gari letu tunaliacha?" Adoyee alimuuliza Awadh.

"Kikubwa liko kwenye mikono salama ya mzee Jeremiah sina wasiwasi wacha tupambane kuukwepa mkono wa sheria kwanza." Awadh alimjibu. Na walipofika kwenye mtaa mmoja uitwao 'Makoto Street' alipunguza mwendo na kisha alikunja kuelekea kulia iliko barabara ya kuelekea jijini Dakar na kwa mbele kidogo alisimama na kuzima taa zote.

" Ndugu zangu tunatakiwa tuzuge kwa muda hapa kuwapoteza maboya kisha tutaianza safari ya kuelekea Dakar." Awadh aliwaambia wenzake akiufungua mlango.

"Dakar tena? Haturudi nyumbani kwanza?" Jumbe aliuliza.

"Kama nilivyowaambia hawa jamaa wanatufuatilia hivyo si vizuri kuendelea kuzagaa mjini hapa. Cha msingi hapa ni kuzama chimbo kwanza kusikilizia upepo unavumaje kisha tutajua cha kufanya." Awadh alimjibu. Kisha walishuka wote na kuingia kwenye mtaa huo uliokuwa kimya na kuwafanya kutulia bila hofu yoyote.

" Hatuwezi kupata chakula mitaa hii mwenzenu sijala kitu kutwa nzima naweza kupata vidonda vya tumbo." Soud aliuliza baada ya kuona hakuna mpango wowote wa kushughulikia hilo.

"Kaka Soud jitahidi kujikaza basi unafikiri hilo linawezekana kweli?" Seynabou alimuuliza badala ya kumjibu.

"Hivi hili kundi lina nini? Mbona kila ninachokiongea mimi kinapuuzwa?" Soud alisimama na kuuliza kwa sauti huku akirusha mikono yake kuonesha kukerwa na Seynabou.

"Soud ndiyo nini sasa kupayuka kiasi hicho kuna haja gani ya kujificha hapa si tuendelee na safari tu." Jumbe alimwambia Soud.

"Kaka Jumbe unanijua vizuri sana lakini hawa wengine wananidharau sana mimi sijui kwa sababu nina kamwili kadogo kanakomfanya kila mmoja kutaka kufanyia mazoezi?" Soud alimjibu.

"Shida yako wewe si ni chakula tu?" Jumbe alimuuliza.

"Ndiyo, sihitaji kingine zaidi." Soud alijibu. Jumbe alitoka pale alipokuwa kasimama na kuondoka kuelekea eneo ambalo lilionekana kwa mbali likiwa na mpishano wa watu.

"Jumbe usiende huko ni hatari, pale pale unapokwenda wanaweza kuwepo jamaa na ukumbuke kuwa wewe ni mgeni hivyo kufika pale ni rahisi kwao kukuhisia vibaya." Awadh alimwambia Jumbe ambaye tayari alishaanza kuelekea huko. Maneno ya Awadh yalimfanya asite kidogo kisha alirudi.

" Tunafanyaje sasa maana madai ya Soud ni ya muhimu na si yeye tu wote tuna njaa hapa." Jumbe alimuuliza Awadh.

" Nalijua hilo kaka nafikiri tuingie garini tuanze safari tutapita barabara moja hivi ambayo hutumiwa na wavunaji wa maliasili hiyo itatupeleka mpaka kwenye kijiji kimoja kiitwacho Sakai hapo tutapata chakula na kunywa na kwa kuwa utakuwa ni usiku mkubwa tutatembea kwa kujiachia mpaka tunaingia Dakar bila kuingia barabara kuu ambayo nahisi mpaka sasa watakuwa wameweka vizuizi vya kutosha." Awadh alimpa majibu ambayo yalimuingia kiasi Jumbe kiasi cha kutikisa kichwa.

" Basi tusipoteze muda kumbe ulikuwa unalijua hilo kwanini usingeunga toka muda ule, tungekuwa tunakula msosi sasa." Jumbe alimwambia Awadh akimpiga mgongoni. Waliwapa taarifa wenzao ambao walikubaliana na wazo hilo kisha wakaingia kwenye gari na kuianza safari. Lakini walipokatisha barabara kuu kwenda upande wa pili kuna gari nyingine nayo ilikunja na kuanza kuwafuata. Awadh aliliona hilo gari akaongeza mwendo kwani japo halikuwa na king'ora lakini lilimpa mashaka.

"Jamaa walikuwa wamebana sehemu nini?" Jumbe aliuliza baada ya kuiona kwenye 'site mirror' ya upande wake.

"Hawa tunatakiwa tukacheze nao tukifika mbele huku wacha waendelee kutufuata tu." Awadh alimjibu macho yake yakiwa yanacheza kama kinyonga dakika sifuri mbele dakika sifuri kulia na kushoto kwenye 'site mirror' na kwa kuwa zile barabara za pembezoni anazijua vizuri hakusumbuka alikuwa anatembea mwendo wowote maana alijua ni wapi kubaya na wapi kuzuri.

Walipoanza kuuacha mji Awadh alizima taa kubwa na kuanza kutembelea za chini na akaongeza mwendo zaidi lengo likiwa ni kuwatimulia vumbi la kutosha waliokuwa nyuma yao. Lakini kila alipokuwa akiangalia pembeni ile gari aliiona nyuma yake, alitumia kila ujuzi wa kuwaacha lakini wapi jamaa walikuwa vizuri sana hilo likaanza kumchanganya akili yake.

"Mpaka huku wanatufuatilia watakuwa ni askari kweli hawa au ni vija wa mzee Malick?" Awadh alijiuliza akikata kona na kuingia porini ambako alisimamisha gari ghafla na kuwaambia wenzake washuke na kujificha. Kisha yeye akaendelea na kuendesha huko huko porini lile gari nalo likafuata huko huko alikokwenda Awadh, alipoliona alicheka kuashiria kuwa mtihani wake ameufaulu kwa alama za juu alijiandaa vizuri silaha yake mkononi kisha akafungua mlango.

"Endeleeni kulifuata si mnashida nalo wacha niwaoneshe mimi ni nani nikiwa maeneo kama haya." Alijisemesha akiruka na kuliacha gari liendelee kisha yeye aliviringika haraka na kwenda kujificha kwenye mti mmoja ambao haukuwa mbali na ile taxi aina ya Toyota GX100 ilipita karibu yake kuendelea kulifuata gari lake ambalo halikufika mbali liligonga mti.

Kitendo hicho kilimfanya yeye kurudi nyuma mpaka walipokuwa wenzake na kusikilizia wanafanya nini baada ya hapo na ni wakina nani hao.

"Haitakiwi tuwaachie hawa kaeni sawa." Jumbe aliwaambia wenzake wakati alipoona wamesimamisha gari na kushuka kuelekea lilipo gari lao.

"Hakuna mtu ndani ya gari aise." Ilisikika sauti.

"Mulika pembeni huko tuone."

"Tumulike vipi kaka wakati unaona kabisa milango ya nyuma imefungwa ila wa upande wa dereva ndiyo uko wazi." Mmoja alipinga.

"Unataka kusema gari lilikuwa na mtu mmoja tu ambaye ameruka siyo?"
"Ndiyo hivyo." Alijibiwa.

"Si tuko wanne hapa, kila mmoja upande wake tumsake huyu hayawani yeye ndiyo atasema wenzake kawacha wapi." Maagizo yalitolewa na wote wakatawanyika.

"Nisikilizeni wanangu, nitatoka mbio na baada ya kufika mbali kidogo nitapiga risasi kuwapa ishara niliko najua watakuja kichwa kichwa ninyi mtaingia kwenye gari lao Awadh utafanya yako mimi nitawazuga wakizugika mtanisubiri mbele wakiwa makini nitapiga risasi ya pili juu hapo itabidi mje kwa shambulizi. Tumesomana."Jumbe aliwauliza.

" Tumekupata kaka." Awadh alijibu kisha Jumbe alianza kukimbia.

" Huyu huku." Alisikika mmoja wao mara baada ya kusikia mlio wa risasi.

Walipoanza kumfuatilia tu wakina Seynabou nao wakaanza kulivizia gari lao kwa tahadhari bila kushtukiwa. Wakiwa wanaruka kwenye gogo lililokuwa limelala chini Seynabou aliruka vibaya na kuangukia kimti kilichokuwa kimechongoka na kujikuta akitoa mlio mkali.
"Paja languuu......" Moja kwa moja zoezi la kusonga mbele likakwama ilibidi warudi tayari kwa kujihami.

"Wako wengi hawa chukueni tahadhari." Mmoja ambaye alionekana kuwa kiongozi wao aliwaambia wenzake baada ya kusikia kelele za Seynabou. Jumbe alichomoa kisu chake na kukishika vizuri mkononi baada ya kugundua alipokuwa yeye hapakuwa mbali sana na alipokuwa mtoa tahadhari hivyo alianza kumvizia. Na upande wa wakina Awadh nao walichokifanya ilikuwa ni kumsogelea Seynabou lakini wakamuacha kwanza na kujificha ili awe kama chambo cha kuwadaka Maadui.

"Mamaaaa nafwaaa....... Gregory ki...ki...kimbieni mna...mna...manak...." Hakumalizia neno lake alikata kauli kutokana na kisu alichokuwa kachomwa ubavuni wa kushoto.

"Nyambaaafu......" Jumbe aliongea akichomoa kisu na kuondoka zake kuelekea waliko wenzake.

"Kaka kamsaidie Seynabou wacha tule sahani moja na hawa." Soud alimwambia Jumbe wakati wakipishana. Jumbe hakujibu chochote zaidi ya kuongeza spidi kumfuata Seynabou aliyekuwa akilalamika kwa maumivu.

"Pole Seynabou hebu geuka nikusaidie." Jumbe alimwambia akimsaidia kumgeuza. Alichomoa kipande cha mti kilichokuwa kimebakia kisha alivua shati lake na kisha kuvua 'vesti' ambayo aliitumia kumfungia sehemu yenye kidonda na kisha alivaa shati lake na kumbeba Seynabou mpaka lilikokuwa gari.

" Mungu wangu naumia mimi kaka Jumbe." Seynabou alilalama.

"Jikaze utapata matibabu vizuri tu kisha utapona kikubwa kuwa jasiri." Alimtuliza wakati akimlaza chini. Alilifuata gari lao ambalo lilikuwa bado linaunguruma. Lakini baada ya kulifikia akitikisa tu kichwa na kujaribu kuufungua mlango ambao ulikuwa umebonyea sana huku sehemu ya mbele ikiwa imebonyea zaidi. Na baada ya kupambana nao sana hatimaye ulifunguka na alichokifanya aliingiza tu mkono na kuizima kisha kuitoa funguo na kuliendea gari la maadui zao ambao walikuwa bado hawajajulikana na askari au watu wa mzee Malick Bolenge.

"Mungu mkubwa." Jumbe alishukuru baada ya kuikuta funguo haijatolewa, aliingia akaliwasha na kurudi nyuma mpaka alipokuwa Seynabou na kusimama. Alishuka akamchukua na kumpakia kwenye gari akaurudisha mlango na kuingia mbele tayari kwa kuondoka kuelekea barabarani.

" Usirushe hatua hata moja kijana kwa kufanya hivyo nitausambaratisha ubongo wako." Sauti ilisikika kutoka mbele yake, Jumbe aliishiwa nguvu kwani hakuweza kuhisi kitu kama hicho hivyo alinyoosha mikono juu kusalimu amri. Mtu huyo alisogea mpaka karibu yake na kumtaka asilete jeuri yoyote ile. Jumbe alibakia kamkodolea macho mtu huyo akiamini mwisho wa safari yake umewadia aliendelea kuwa mpole.

"Wewe ndiyo kiongozi wa hao wajinga wenzako siyo?" Mtu huyo alimuuliza alipomfikia karibu.

"Si ninakuuliza au hujasikia swali langu?" Alimuuliza tena baada ya kuona hajibiwi, lakini kabla Jumbe hajamjibu swali lake akishtukia mtu akienda chini. Akiwa hajui nini kimetokea mpaka mtu huyo kwenda chini na ukizingatia kulikuwa na giza mara alisogea Seynabou akijivuta kutoka upande wa pili wa gari.

"Ni wewe?" Jumbe alimuuliza.

"Sikuwa na jinsi ilibidi nitokee mlango wa pili na kumtandika risasi maana nilijua nikifanya mchezo tunaishia huku huku porini."

Seynabou alimpa jibu lililomfanya Jumbe amfuate na kumkokota mpaka kwenye gari tena.

"Wewe ni shujaa wangu nashukuru sana umeniokoa." Alimwambia akimuweka sawa kwenye kiti.

"Usijali ingia tuondoke." Seynabou alimjibu. Jumbe aliangaza huku na kule hakuona chochote hivyo akaingia kwenye gari na kuliondoa, alipoikaribia barabara tu alitokea Adoyee akijikongoja mkono ukiwa eneo la tumbo. Jumbe hakuamini macho yake mpaka alipolielekeza gari vizuri upande wake ndipo alipomuona vizuri.

"Adoyee umepatwa na nini huko?" Jumbe alipiga kelele akisimamisha gari na kushuka.

"Kapatwa na nini tena?" Seynabou aliuliza baada ya kuinua kichwa na kumshuhudia Adoyee akienda chini kwa kukosa nguvu.

NI WAKINA NANI HAO TENA WALIOZUIA SAFARI YA WAKINA JUMBE? NA VIPI KUHUSU AWADH NA SOUD WAKO SALAMA?

FUATILIA SEHEMU IJAYO UPATE JIBU LA FUMBO HILI.

1607534661335.jpg
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 25
Sultan Uwezo
+255

Alimkimbilia na kumshika mabega akimkagua lakini Adoyee hakuongea kitu zaidi ya kumtazama tu Jumbe usoni hali hii ilimuogopesha sana akazungusha macho yake huku na kule kisha akamkongoja mpaka kwenye gari.
"Seynabou naomba nifungulie mlango." Jumbe alimwambia Seynabou akiwa kamshikilia Adoyee ambaye alikuwa hajiwezi. Mlango ulifunguliwa kisha akampa sapoti kupanda kisha akaurudisha mlango alitembea kama hatua kadhaa kisha alirudi na kuufungua tena mlango.
"Nakuja sasa hivi wacha niwafuatilie Awadh na Soud huko waliko."
"Tungeongozana Jumbe lakini ndiyo hivi nilivyo." Seynabou alimjibu akimuonesha jeraha lake.
"Usijali." Alimjibu na kuubamiza mlango kisha aliondoka akiiweka sawa silaha yake. Alizunguka huku na kule kuwasaka wenzake bila mafanikio alikata tamaa akataka kurudi kwenye gari lakini hapo hapo wazo likamuijia asonge mbele kidogo mpaka kwenye chaka moja lililokuwa mbele akaangaza bila mafanikio ndipo alipoona aanze kuita kwani giza lilikuwa limetanda vilivyo.
"Awadh mko wapiiiiiii.....???" Akatulia na kusikilizia kama anaweza kupata mrejesho wa muito wake lakini kimya kilitawala akaita tena na tena lakini hakuna jibu lolote ambalo alilipata mpaka hapo alichoka alijivuta mpaka kwenye kigogo kilichokuwa pembeni yake akaketi na kutoa simu yake akaitafuta namba ya Catherine na kuipiga.
"Bosi naye kapatwa na nini? Mbona hapatikani hewani?" Jumbe aliirudisha mfukoni na kujishika kichwa chake akiwaza itakuwaje.
"iiiiiisyaaaaaaaa....." Ulisikika mlio wa chafya kutoka nyuma ya kile kichaka.
"Mhh kuna mtu hapa?" Jumbe aliuliza akiinuka na kuelekea alikosikia hiyo chafya.
"Awadh kulikoni?" Jumbe alimuuliza baada ya kumkuta hatamaniki mwili mzima uko vumbi tu huku akiwa kafungwa mikono kwa nyuma, alimuona vizuri baada ya kummulika kwa tochi ya simu baada ya kushindwa kumuona vizuri.
"Na..na..nao..naomba nifungue kamba kwa..kwanza (akikohoa)" Awadh aliongea kwa shida kidogo akigeuka na kulala kifudifudi kumpa urahisi Jumbe amfungue kamba alizokuwa kafungwa.
"Pole sana kaka imekuwaje mpaka kufanywa hivi?" Jumbe alimuuliza akimfungua kamba.
"Kwa kweli sifahamu chochote zaidi ya kukumbuka tukio la mwisho ambalo lilikuwa ni kupigwa na kitu kizito kichwani." Awadh alimjibu.
"Ina maana baada ya hapo ulikata moto na jamaa wakapata nafasi ya kukushughulikia ukiwa hujitambui."
"Kitu kama hicho, vipi mko salama?" Awadh aliuliza.
"Salama wapi kwenye gari Seynabou na Adoyee hali zao ni tete na wewe ndiyo kama hivi." Jumbe alimjibu akimshika mkono kumpa sapoti kuinuka.
"Na Soud je hamkuwa naye?" Jumbe hakuchoka kuuliza maswali.
"Mmh tulikuwa pamoja lakini tuliachana baada ya kukisogelea hiki kichaka, hebu tumcheki upande wa pili tunaweza muona huko." Awadh alimjibu akijikagua mifukoni kisha akampa ishara waondoke hapo na kuendelea kumtafuta Soud. Walimtafuta kwa muda mrefu lakini hawakubahatika kumuona.
" Brother twenzetu tukasikilizie kwanza kupambazuke kisha tuendelee kumsaka." Jumbe aliona muda unakwenda lakini hawaoni hata kivuli chake hivyo akaona warudi kwenye gari kuvuta muda kupambazuke.
"Poa kaka tuondoke." Awadh alimjibu huku akionekana kuendelea kuimarika kwani alianza kutembea vizuri.
"Unajisikiaje kwa sasa?" Jumbe alimuuliza.
"Ni maumivu ya kichwa tu ndiyo yamebaki maeneo mengine naimarika." Awadh alimjibu. Walifika kwenye gari na kuwakuta wakina Seynabou wamelala hivyo hawakutaka kuwaamsha walichofanya walilifuata gari lao lililokuwa halitamaniki ili wakaangalie kama wanaweza kujibana humo mpaka asubuhi. Wakati Jumbe anashusha haja ndogo Awadh alikwenda na kuufungua mlango wa gari. Hakuamini alichokutana nacho humo ndani ya gari.
"Jumbe njoo uone maajabu."
"Maajabu! Maajabu gani tena?" Jumbe aliuliza akifunga mkanda wa suruali.
"Njoo uone mwenyewe usijesema mimi muongo." Awadh alimjibu. Alimfuata na kuchungulia ndani ya gari kuona kulikoni.
"Hee Soud! Kafikaje hapa?" Jumbe aliuliza akimgusa.
"Yaani huyu jamaa ni pasua kichwa aisee cheki anavyokoroma utadhani magari ya zamani yale mafiati." Awadh aliongea akiwa kashika mkono mmoja kiuno na mwingine kwenye gari.
"Nini jamani? Mbona tunaharibiana pozi?" Soud alilalamika akijivuta wasimuamshe.
"Ndiyo nini sasa umefanya Soud?" Jumbe alimuuliza.
"Hebu niacheni kwanza tutaongea kukicha bwana." Soud alimjibu.
"Unasemaje wewee hivi unajisikia kweli? Yaani tuendelee kusubiri giza liondoke wakati wenzetu wana hali mbaya?" Jumbe alimuuliza.
"Wana hali mbaya?" Soud aliposikia hivyo aliuliza akishuka na hakukuwa na la kujadili wakaondoka kuelekea waliko wakina Seynabou.

***

Akiwa ndani ya Hotel moja pale mjini Dakar iitwayo THREE DAYS, Catherine alikuwa bize kwenye simu yake huku earphones zikiwa masikioni mkono kwenye biki aliyokuwa akiandika vitu kwenye 'diary' inavyoonekana alikuwa akifuatilia taarifa fulani pale na baada ya kumaliza alitoa zile earphones na kuondoka kwenye ile 'program' akaiweka simu pembeni na kuelekea bafuni.
"Daktari Brown Lutasya na mzee Butazalage Lukosa jiandaeni." Catherine aliongea akiwa mbele ya kioo kilichokuwa mle bafuni.
"Yaani sitakubali katika hili mtajuta kunijua." Aliongeza na kuanza kulia pale mbele ya kioo na baada ya hasira kuisha alioga na kurejea chumbani kwake ambako alijiandaa na kutoa mavazi yake ya kazi akaweka mwilini kichwani alitupia 'cap' kofia ambayo ilimfanya aonekane mrembo fulani ambaye kila aliyepishana naye koridoni alitamani kumsimamisha. Alitembea kwa kujiachia mpaka mapokezi na kuacha maagizo.
"Kama kuna mgeni atakuja kuniulizia utamwambia nimetoka nitarejea baada ya saa moja hivi."
"Bila shaka dada." Dada huyo wa mapokezi alimjibu kisha akaondoka mpaka kwenye pikipiki ambayo aliichukua kwa kijana mmoja ambaye anamiliki kampuni ya kukodisha magari na vyombo mbalimbali vya usafiri huku akiwa kayaacha magari yake pale lile alilopora St.Louis pamoja na la kwake akimpa kazi ya kuyabadili rangi.
"Niambie Martin!" Aliongea Catherine baada ya kupokea simu akiwa juu ya pikipiki.
"Kila kitu kiko sawa yaani ukiyaona wewe mwenyewe utayapotea."
"Kweli?"
"Haswaa."
"Vizuri sasa wewe endelea kuyapendezesha wacha mimi nifanye yangu kesho jioni nitakuja hapo kuyaangalia." Alimjibu na kukata simu kisha akaliwasha pikipiki na kutokomea gizani. Alikwenda mpaka sehemu moja kulikokuwa na kikao cha siri kwa baadhi ya viongozi wa kanisa kujadili masuala muhimu ambayo watakwenda kuyabadili kwenye kikao kitakachofanyika Kanisani juu ya hatma ya Mchungaji Rodney na mambo yake. Aliingia mpaka uchochoroni ambako alisimama na kushuka akafungua begi lake lililokuwa nyuma ya pikipiki akatoa koti refu na jeusi akalivaa na kichwani akavua ile kofia na kuvaa mzura wa kuficha sura bastola kiunoni na kisu mkononi kisha lile begi akalihifadhi vizuri pale kwenye pikipiki kisha akaangaza huku na kule na alipoona kuna usalama alitoka pale uchochoroni na kuupanda ukuta. Alitua ndani ya lile jengo lililokuwa na ulinzi kiasi chake, alimvizia mlinzi wa kwanza aliyekuwa akiangalia video zilizokuwa kwenye simu yake na kwa usiku ule bila shaka zilikuwa ni za ngono kutokana na milio iliyokuwa ikisikika. Akiwa bize Catherine alimpita na kuingia ndani bila kuonwa na yeyote pale nje.
"Jamani bila shaka tumeelewana katika hili haiwezekani mtu mmoja aliingize Kanisa letu kwenye matatizo." Daktari Brown Lutasya alisikika katika kikao hicho.
"Na hapo bado sijawaambia maovu yake mengine aliyokuwa akiwafanyia wake zetu kwa kisingizio cha Kikundi cha Faragha." Mzee Lukosa aliongea katika kutia chachandu.
"Kwa hilo napingana na wewe mzee wangu mbona na mimi ni miongoni mwa wana Faragha lakini hakuna baya lolote lile." Mama mmoja aliinuka na kupinga neno la mzee Lukosa.
"Haya mama yangu lakini elewa kuwa usilolijua ni sawa na usiku wa giza nene." Mzee Lukosa aliongea hayo kisha akainuka na kuelekea maliwatoni akiwaacha wenzake wanaendelea na majadiliano katika kumaliziamalizia mazungumzo.

Aliingia chooni na kurudisha mlango, lakini kabla hajafanya chochote mara mlango uligongwa.
"Mhh nani tena jamani si nakuja huko huko?" Mzee Lukosa alikwazika kwa tendo hilo alirudi na kuufungua mlango.
"Shiiii... Usipanue kinywa chako mzee Lukosa." Catherine alimwambia huku akiutoa mzura wake kumpa nafasi mzee Lukosa kuiona sura yake.
"Ni macho yangu au naota?" Mzee Lukosa aliuliza akipitisha mkono wake usoni kwake akihisi macho yake kumdanganya.
"Unaonaje wewe yanakudanganya au?"Catherine alimuuliza akiwa ameuegemea mlango.
" Mama Mchungaji ni wewe?" Mzee Lukosa aliuliza akiwa kamtolea macho Catherine.
" Wala hujakosea mzee wangu ndiyo mimi mwenyewe, unahisi nini kuniona mahali hapa?" Catherine alimuuliza.
" Tuko hapa tunajadili masuala ya kiutawala tu mama Mchungaji."
"Hayanihusu hayo mimi mzee Lukosa kilichonileta kwako ni kitu kimoja tu."
"Kipi hicho mama?" Mzee Lukosa alimuuliza.
"Najua wewe ni msiri mkubwa wa Mchungaji Rodney na kuna mengi mliyofanya pamoja ila sitaki kuchimba zaidi hilo hebu niambie ni wapi alipo Mchungaji pamoja na mtoto wake Jennifer aliyezaa na marehemu mke wa Otago Mathew?"
"Kusema ule ukweli alipo Mchungaji sifahamu lakini Jennifer Otago yupo masomoni nchini Nigeria." Mzee Lukosa alimjibu akiwa kaanza kutokwa na jasho.
"Yuko chuo gani na ni nani anayemlipia ada?" Catherine alimuuliza akimsogelea huku akiwa kachomoa kisu.
"Anasoma 'Lagos International University na mlipaji wa ada ni Kanisa kupitia mfuko wetu JUHUDI." Mzee Lukosa alijibu akirudi nyuma.
"Mzee mzima mbona muda mrefu humo au unafikiri uko kwako tupishe na wengine bwana." Sauti ya Daktari Brown ilisikika nje huku akiugonga mlango.
"Vizuri sana kajileta mwenyewe." Catherine alijisemea kimoyoni akimpa ishara mzee Lukosa ya kumjibu.
"Tumbo bwana limenitinga sana." Mzee Lukosa alimjibu.
"Basi fanya haraka tunakusubiri huku nje upate posho yako." Sauti ilisikika ikiondoka.
"Buu... shiiiiiit!!!" Catherine alipiga kelele akigonga ukuta kwa kisu alipogeuka mzee Lukosa alikuwa anataka kumpita pale mlangoni.
"Umechelewa mzee wangu unakwenda wapi?" Catherine alimwambia akimvuta kwa nyuma na kumfanya kuteleza na kuanguka chini.
"Naomba unisamehe mama yangu mimi sina kosa lolote."
"Ni kweli kabisa lakini una damu za mama yangu mikononi mwako ninauhakika akikuona siku ya leo atafurahi saaaaaana." Catherine alimjibu akimkita kisu cha kifuani kisha aliichomoa bastola yake yenye kiwambo cha kuzuia sauti akampiga risasi ya kichwani. Alitoa kikaratasi kidogo na kukivisha kikamba chake kwenye mpini wa kisu kilichokuwa na ujumbe uliosomeka ; " JIANDAE DAKTARI BROWN KUPOKEA ZAWADI HII." Kisha aliufungua mlango na kulifungua dirisha lililo koridoni na kuruka nje lakini wakati akifanya hivyo mmoja wa wajumbe waliokuwa wamehudhuria kikao kile cha usiku mnene aliona mtu akipotelea dirishani hivyo alikimbia kuelekea chooni. Catherine baada ya kufika chini alichungulia na kushuhudia kila kitu kilichotokea kisha aliruka ukuta na kukimbia mpaka kwenye egesho la pikipiki na kuwasha akatokomea zake na kuwaachia majonzi. Alifika na kuiacha pikipiki nje ya Hotel akaingia na kumkuta mhudumu mapokezi akisinzia pale mezani akampita na kuelekea chumbani kwake ambako alichukua kila kilicho chake na kutoka tena.
"Dada mbona umeingia sasa hivi halafu unatoka na mizigo haraka kwema?" Mlinzi alimuuliza baada ya kumuona Catherine akiwa kasi.
"Hebu nishikie kwanza hili begi." Badala ya kumjibu Catherine alimpa begi ambebee.
"Mbona hujibu unanipa begi je ni madawa?" Mlinzi huyo aliendelea kumuuliza akimfuata nyuma. Lakini Catherine hakujali kitu alizidi kusonga mbele mpaka alipoifikia pikipiki yake na kuweka boksi kisha akalipokea lile begi kwa mlinzi na kuanza kulifunga.
"Usiondoke nikupe zawadi yangu Afande."
"Zawadi eee, afadhali maana siku ya leo iliisha vibaya." Mlinzi huyo alijibu akichekacheka. Lakini hakujua kinachofuata juu yake.
"Hiyo ndiyo zawadi yako Bosi." Catherine alimwambia akimchapa risasi na kuondoka zake.

CATHERINE ANAELEKEA WAPI BAADA YA MAAFA HAYO ALIYOYATEKELEZA? NA VIPI KUHUSU VIJANA WAKE KULE PORINI WATATOKA SALAMA?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.
1607534661335.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 26
Sultan Uwezo
+255

Pikipiki ilitia nanga ofisini kwa Martin, Kijana wa Kinigeria ambaye shughuli zake nchini Senegal ni wizi wa magari kutoka kila kona ya nchi na kuyauza nje ya nchi lakini pia hujishughulisha na kazi ya kukodisha magari na vifaa vingine vya moto kwa makundi mbalimbali ya kiharifu. Martin Onukwwo alikuwa kijana mtanashati na Tajiri sana akiwa anaiendesha Kampuni yake ya Kuuza magari aliyokuwa akiimiliki kihalali kabisa lakini nyuma ya pazia alikuwa ni mtu mwenye roho mbaya sana kuwahi kutokea nchini humo na sifa hii ndiyo iliyomkutanisha na Catherine ambaye alimweleza azma yake ya kuwaangamiza wale wote waliohusika na kuukatisha uhai wa mama yake.
"Mwanamke wewe ni hatari sana aisee lete habari." Martin alimuuliza Catherine wakati akishuka kwenye pikipiki.
"Huwa nikidhamiria kitu lazima kiwe hivyo huna haja ya kuuliza kilichotokea wewe pigia mstari tu." Alimjibu akivua glovu huku Martin naye akisaidia kufungua lile begi.
"Nakuvisha manyota yote mama Mchungaji, naanza kukuogopa ujue!" Martin alimtania.
"Hauwezi kuniogopa ukiwa huna tatizo lolote na mimi ila ukitaka kunijua nikoje ingia kwenye anga zangu." Catherine alimjibu. Waliingia mpaka ndani ambako waliongoza mpaka kwenye chumba ambacho Catherine alihifadhi vitu vyake kabla ya kuondoka.
"Sasa ukiwa tayari utanijulisha wacha mimi nifanye michakato fulani hivi huku nje." Martin alimwambia Catherine akimkabidhi begi lake baada ya kuufikia mlango wa kuingia chumbani.
"Poa poa." Catherine alimjibu. Baada ya kuingia chumbani humo moja kwa moja alielekea liliko dirisha na kufunua pazia kidogo kuangalia kitu ambacho alikihisi mapema.
"Leteni habari vijana wangu." Alimsikia Martin akiongea na vijana ambao Catherine hakuwaona vizuri kutokana na eneo ambalo walikuwa wamesimama ila sauti ilisikika vizuri.
"Tumefanikisha bosi mzigo huu hapa." Mmoja wa vijana wale alimjibu akimkabidhi begi.
"Vipi hamjaua mtu yeyote kwenye tukio?" Martin aliuliza akipokea begi.
"Kiukweli hali ilikuwa tete tusingefanya hivyo tungetiwa mikononi."
"Kwa hiyo mmemwaga damu?" Martin aliuliza kwa sauti ya juu kidogo.
"Ndiyo mkuu." Alimjibu kijana huyo. Catherine kusikia hivyo akajua huko nje si salama hivyo akaweka sawa zana zake kisha akaingia kuoga. Akiwa anaoga mara akasikia mabishano yakiendelea nje sauti aliyoisikia ilikuwa ni ya Martin na watu ambao Catherine alitaka kuwafahamu hivyo alifanya haraka akatoka mle bafuni na kujifunga tu taulo na kutoka mpaka kwenye korido na kujibana kusikiliza mabishano yalihusu nini.
"Kwa hiyo unataka kutuambia hakuna pikipiki yoyote iliyoingia hapa kwako Martin?" Mtu huyo aliuliza.
"Kiukweli hakuna aliyeingia hapa muda huu."
"Na kwanini hujalala mpaka muda huu kuna kazi ulikuwa unafanya?" Mtu huyu aliyeonekana kama Afisa wa jeshi la Polisi aliendelea kumbana kwa maswali.
"Naomba nisubiri kwanza bosi wangu najua unachokihitaji." Martin alimwambia na kutoka kuelekea chumbani kwake.
"Unafanya nini hapa Catherine?" Alimuuliza baada ya kumkuta kabana koridoni akimfuatilia.
"Ni nani huyo?" Catherine alimuuliza.
"Niache nimalizane naye huyo wala usijali." Martin alimjibu akiingia kwenye chumba kingine.
Catherine aliachana naye na kurudi chumbani kwake ambako aliendelea na maandalizi yake kwa kuweka kila kitu sawa tayari kwa safari na baada ya kumaliza alitoka na kumkuta Martin akiifuatilia Habari kwenye Televisheni, Catherine naye aliketi na kuiangalia Habari hiyo.
"Katika tukio jingine watu wanaodhaniwa kuwa ni Majambazi wamevamia gari lililokuwa limebeba Watalii likiwa limepaki ndani ya Hifadhi ya Wanyama ya Kadino na kupora vitu mbalimbali vya Watalii hao ikiwa ni pamoja na fedha zinazokadiriwa kufikia Dola laki tatu, Majambazi hao hawakuishia hapo walimuua dereva wa gari hilo ambaye alitaka kupambana nao. Jeshi la Polisi linaendelea kufuatilia waliohusika na tukio hilo. Nasi tutaendelea kuwajuza kila linaloendelea... " Martin aliizima TV na kumgeukia Catherine.
" Vijana wangu wamefanya kosa sana kuua aisee kila siku nawaambia waepuke kumwaga damu lakini hawaelewi."
" Kwa hiyo wewe ndiyo umefanya tukio hilo?" Catherine alimuuliza akiketi vizuri.
" Ni vijana wangu sister." Martin alimjibu.
"Ndiyo ni wewe hao si vijana wako unafikiri wakikamatwa hawawezi kukutaja?" Catherine alimrekebisha.
"Ni kweli lakini pia na tukio lako la kimafia limelipotiwa hapa."
" Unasemaje Martin?" Catherine alimuuliza kwa mshangao.
"Ndiyo hivyo, mzee aliyekuwa akisimulia kanifanya nicheke badala ya kusikitika aisee." Martin alimjibu akicheka.
"Hebu acha utani bwana niambie kasemaje hawajanitambua?" Catherine alimuuliza akimtingisha mabega Martin.
"Kasema kuwa aliona tu mtu aliyeficha sura yake akipotelea dirishani ndipo alipowaambia wenzake wakakimbia kuingia kule chooni na ndipo walipokutana na mwili wa mzee Lukosa ukiwa umeshambuliwa huku kukiwa na ujumbe unaomtaja Daktari Brown." Martin alimwambia.
" Ooh vizuri sana Martin kwa hiyo yule Afisa wa Polisi umemalizana naye vipi?" Catherine alimuuliza.
" Hakuna kitu kitamu kama Chapaa, pesa ndiyo kila kitu unaulizaje hivyo?"Martin alimjibu.
" Okay sawa, kama unavyoona kumepambazuka natakiwa kuondoka zangu si gari liko tayari?"
" Kila kitu kiko tayari ni wewe tu kuamua unaondoka na lipi kati ya yale mawili." Martin alimjibu.
" Hapana ningependa niondoke na gari lako lile lenye sura mbaya naona litanifaa sana." Catherine alimjibu akitaka kutumia gari la Martin lenye muonekano kama magari ya tata tairi kubwa lakini lenyewe ni NYUMBU TZ 0010 ambalo alilinunua kutoka Tanzania na ni gari ambalo limetengenezwa nchini humo chini ya Kampuni iliyo chini ya Jeshi la Kujenga Taifa.
"Utaliweza lile weweee?" Alimuuliza wakitoka.
"Hakuna chombo cha moto kinachonishinda mimi weweee nikabidhi funguo nianze safari." Catherine alimjibu.
"Hii hapa kikubwa kuwa makini barabarani maana linakimbia sana hili." Alimpa tahadhari.
"Usijali kwenye hilo ila ninachokuomba Martin vijana wangu watakuja kwako naomba uwape hifadhi mpaka pale nitakaporejea mimi ila kuna kuna mtu mwingine watakuja naye mchunge asitoroke mapema." Catherine alimuomba jambo hili ambalo halikuwa tatizo kwa Martin.
" Ni mtu gani huyo?" Martin alimuuliza.
" Kuna Daktari mmoja nakwenda kumteka ambaye atawashughulikia majeruhi wangu"
"Kuhusu hilo ondoa shaka Daktari yupo ambaye huwa anaishughulikia timu yangu kikubwa wewe nielekeze waliko na wao waelekeze kuhusu mimi nitakutana nao na mipango mingine itaendelea wewe ianze ratiba yako." Jibu la Martin lilimfanya Catherine atoe tabasamu na kuingia kwenye gari.
" Ndiyo maana huwa napenda kufanya kazi na wewe una akili sana Martin." Alimsifia akiliondoa gari. Safari ya Catherine ilikuwa ni kumfuatilia mzee Malick Bolenge ambaye ni Mjomba wake na safari hii akiwa kadhamiria kumkabili yeye mwenyewe bila kundi lake ambalo lilimkosa.

***

Ilikuwa ni siku ya shamrashamra nyingi ndani ya mji wa Lagos nchini Nigeria huku hali ya hewa ikiwa inaruhusu shughuli mbalimbali kufanyika bila tatizo lolote. Ndani ya Uwanja wa michezo wa Lagos International University kulikuwa na Michezo mbalimbali ikifanyika chini ya Chuo hicho ukiwa ni msimu wa tisa toka kuanza kwake na safari hii kulikuwa na Michezo zaidi ya sita tofauti na misimu iliyopita. Michezo ambayo iliongezeka ni pamoja na Mashindano ya Baiskeli, Pikipiki na ya kuwatafuta Walimbwende Chuoni onesho ambalo huko nyuma lilifungiwa kutokana na Utekaji ambao ulitokea miaka kama kumi nyuma kutokana na kuvamiwa na kundi la Waasi ambalo liliwateka Visura wote dakika kadhaa kuelekea kuanza kwa shindano hilo na hivyo Serikali kuamua kulifungia Shindano hilo. Lakini safari hii liliruhusiwa mara baada ya Serikali kujiridhisha na hali ya Usalama ndani na nje ya Chuo hicho. Wageni waliendelea kuwasili ndani ya Viwanja vya Chuo hiki huku wahusika nao wakiendelea kujifua. Ufunguzi wa Michezo hii ulifunguliwa na shindano la waendesha pikipiki ambalo lilikuwa likianzia ndani ya Uwanja na kutoka mpaka nje ya mji na kisha kurudi tena ndani ya Uwanja ambako ndiko mshindi angepatikana na kutangazwa. Wakiwa wamejipanga kwenye eneo la kuanzia huku muongozaji akipita kuwakagua wahusika wa mashindano akipitia kitabu chake na kufananisha na vitambulisho vya washiriki. Lakini alipofika kwenye pikipiki aina ya MAC TONG 10 - 007 iliyotengenezwa nchini India muongozaji alipata shaka kidogo na kuamua kumshusha dereva.
"Sorry, mbona aina hii ya pikipiki hatunayo kwenye orodha yetu?" Alimuuliza mshiriki ambaye alionekana hana hata chembe ya wasiwasi.
"Baada ya pikipiki ya awali ambayo ndiyo ipo kwenye orodha kupata hitilafu nikaona nije na hii ili kuendana na muda kwani haifai kwenye mashindano?" Mshiriki aliyekuwa ndani ya kofia ngumu alimuuliza muongozaji.
"Hapana nilitaka kujua tu maana iliyosajiliwa sikuiona na badala yake nikaiona hii ambayo haiko kwenye orodha yetu lakini nairuhusu iende uwanjani." Alimruhusu kuendelea na mashindano na baada ya kuambiwa anaruhusiwa mshiriki aliingia ndani ya gari tayari kwa mtanange huo. Baada ya kila kitu kwenda sawa muongozaji aliinua Bendera juu kisha akaishusha chini kuruhusu shindano kuanza. Kelele zilianza pale ndani ya Uwanja kila kundi la watu wakimshangilia mshiriki wao kwani kabla ya kutoka nje ya uwanja ilikuwa ni lazima kuuzunguka Uwanja mara sita. Chuo cha Lagos kilikuwa na Mshiriki mmoja kwenye Mashindano hayo ambaye alikuwa akishangiliwa kila wakati kutokana na mbwembwe zake kwenye pikipiki kwani ukiachilia mbali kuwa mbele lakini alikuwa akifanya vimbwanga mbalimbali ikiwa ni pamoja na kupanda juu ya pikipiki mara kuachia mikono mara kulala kwa nyuma akiwa kaachia mikono naye hakuwa mwingine bali ni Jennifer Otago Mathew.
"Haka kabinti nakapenda sana aisee kanapenda michezo, tabasamu muda wote darasani kako vizuri angalia hapa kanachofanya yaani ni full burudani." Yalikuwa ni maneno yake mama mmoja ambaye ni Lecture ndani ya Chuo hicho na akiwa ni mlezi wa wanachuo wote wa kike wenye Vipaji.
" Natamani kama kijana wangu Paul angemuoa huyu binti." Mume wa mwanamama huyo alimwambia mke wake.
" Mabangi ya mwanetu unafikiri itawezekana kweli?" Mke wake alimuuliza.
"Hilo ndio tatizo lake sasa, Hee angalia kule mke wangu." Alimwambia mke wake aangalie namna pikipiki iliyokuwa nyuma ya Jennifer ilivyokuwa ikitembea mpaka usawa wa Jennifer na kurudi nyuma kisha kumpita na kurudi tena nyuma kitendo hicho kiliufanya Uwanja wote kulipuka kwa Shangwe na Nderemo.
" Wachaa weee huyu mshiriki kiboko yaani anampita Jennifer kisha anarudi tena nyuma au yeye hataki kushinda nini?" Aliuliza mtazamaji mwingine alikuwa kavalia miwani ya jua huku kichwani katupia kofia iliyotengenezwa kwa 'materials' zinazotumika kutengenezea mikeka huku wengine huita kofia za mikeka hivyo hivyo na muda wote akiwa bize kula karanga.
" Vipi umefanya mawasiliano na vijana wako kujua Catherine yuko wapi?" Alimuuliza aliyekuwa pembeni yake akipiga picha pale ndani ya uwanja.
"Bado lakini ni masaa zaidi ya kumi toka jana usiku siwapati hewani." Alimjibu.
"Unasemaje wewe? Hivi kichwa kinafanya kazi kweli? Yaani umekaa ukiwa bize na simu kupiga piga mipicha yako isiyo na maana wakati kule mambo hayaendi." Huyu mtu mwenye kofia hilo alimlalamikia kijana wake kiasi cha kumkunja koti lake na kupelekea simu yake kwenda chini na kupasua kioo. Kijana huyo hakujibu kitu zaidi ya kuinama chini kuiokota simu yake ambayo ilishaweka ramani ya mipasuko kwenye skrini na kuanza kuikagua.
"Unashangaa nini hapa nahitaji ripoti inayoeleweka ndani ya saa moja tofauti na hapo nitakufanya kitu mbaya." Aliendelea kumtisha kijana wake huyo ambaye aliona hakuna haja ya kuendelea kuwepo pale ambapo watu walikuwa wanawashangaa akainuka na kuondoka zake kuelekea yaliko maegesho ya magari. Aliingia kwenye gari na kuondoka huku akiikagua simu yake nyingine ilikuwa ndani ya gari na baada ya kuzipitia namba kadhaa aliipiga mojawapo. Hii iliita hivyo akaliweka gari pembeni na kuisubiri ipokelewe.
"Mwamba si upokee simu bwana." Alijisemesha akiwa amejishika kichwa.
Lakini haikupokelewa hivyo akaamua kumuandikia ujumbe mtu huyo.
"Naomba uwafuatilie vijana wangu siwapati kabisa hewani na mara ya mwisho jana walielekea barabara ya Dakar kuna washenzi walikuwa wanawavizia hivyo jitahidi kisha utanijuza." Akaiweka simu juu ya 'dashboard' akawasha gari na kuondoka lakini kabla hajafika mbali aliona kundi kubwa la watu mbele yake wakiwa pembeni kidogo ya barabara.

Alisogea pembeni kidogo akapaki gari lake na kushuka ili akaangalie kuna nini kwenye kundi lile la watu. Alipofika pale hakuamini macho yake baada ya kukutana na zile pikipiki mbili zilizokuwa mbele kwenye mchuano zikiwa hazitamaniki huku waliokuwa wakiendesha hawapo.
"Kuna nini tena jamani?" Kijana huyo alimuuliza mmoja wa vijana waliokuwa wamesimama wakishangaa.
"Hata mimi ndiyo nafika sifahamu chochote japo nasikia hizi pikipiki zilikuwa kwenye mwendo mkali zikagongana na kuwa kwenye hali hii." Alimjibu.
"Na vipi kuhusu madereva wa hizi pikipiki?" Alimpiga swali jingine ambalo hakupata jibu kwani kijana huyo alimuangalia kwa muda kisha akaondoka eneo hilo.

JE UNAHISI AJALI HIYO IMESABABISHWA NA NANI NA KWANINI NA MAJERUHI WAKO WAPI? MZEE WA KOFIA LA MKEKA NI NANI?

UNGANA NAMI TENA KATIKA SEHEMU YA 27 TUPATE KUJUA AMBACHO KILITOKEA IKIWA NI PAMOJA NA KUJUA HALI ZA WAKINA SEYNABOU.
1607534661335.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 27
Sultan Uwezo
+255

Kuulizwa maswali mengi kulimfanya kijana huyu kuondoka sehemu hii akiamini kuwa kuelezea tukio hili kwa mtu asiyemfahamu ni kujitengenezea ushahidi mbele ya vyombo vya sheria. Lilifika gari maalum ambalo lilizichukua pikipiki zile na kuondoka nazo huku maafisa wa Jeshi la Polisi wakiendelea kukusanya taarifa za ajali ile kutoka kwa mashuhuda wa tukio.
"Nikiwa nimesimama naongea na simu nilisikia mlio nyuma yangu ambao ulinifanya nikatishe kuongea na simu nikakimbia kuja lakini cha ajabu nilimshuhudia mmoja wa watu ambao bila shaka alikuwa ni dereva wa moja ya pikipiki akiifuata pikipiki ile ya rangi nyeusi na kumuinua dereva wake akaondoka naye na hawakufika hatua hata tatu ilitokea taxi iliyowabeba na kuondoka kasi." Shuhuda huyu alielezea.
" Hukuweza kumtambua mmoja wao kati yao wawili?"
" Ningewafahamu vipi wakati nilikuwa nafanya yangu ndipo niliposikia kishindo cha ajali hii lakini Taxi iliyowachukua ilielekea upande huu." Shuhuda huyu alionesha upande wa kulia wa barabara. Maafisa hawa waliendelea kukusanya taarifa za ajali hiyo ambayo iliwachanganya sana kutokana na waliokuwa wakiendesha kutopatikana eneo la tukio.
" Vipi umeambulia chochote ulikopita wewe? Maana mimi bado naona chenga chenga tu sioni picha halisi." Afisa mmoja alimuuliza mwenzake wakiwa wameegemea gari lao wakipitia taarifa zao.
"Inaonekana hii ajali iliandaliwa na mmoja wao na ndiyo maana hata baada ya kutokea aliinuka haraka akamfuata mlengwa na kuondoka naye kwa usafiri ambao aliuandaa." Mwenzake naye alitoa ufafanuzi wake kutokana na kile alichokipata kwa mashuhuda.
"Inspector Oso naanza kuipata picha hapa, inavyoonekana mtekaji alishaandaa mazingira ya kufanikisha zoezi lake na ndiyo maana gari lililowabeba lilikuwa linasubiri hapa."
"Naanza kukuelewa hebu twende eneo la tukio tukauchore mchoro pale pale." Inspector Oso alimwambia mwenzake na kuelekea katikati ya barabara.
Baada ya kufika pale katikati waliuchora mchoro wao wa namna ajali ilivyotokea na mpaka kupelekea mtekaji kufanikisha zoezi lake bila kutambulika.
" Hapa mtekaji alitumia akili kubwa sana kitu kinachovutia zaidi ni namna gani aliweza kupenya katikati ya wanashiriki wa shindano bila kushtukiwa? Hivyo ninachokiona hapa ni kwenda kuwahoji waandaaji wa mashindano haya wanaweza kuwa na majibu ya maswali yetu." Mmoja wa Maafisa ambaye alikuwa ndiye kiongozi wa zoezi hilo alitoa wazo ambalo waliona lina mashiko hivyo walirudi kwenye gari na kuondoka kuelekea chuoni.

***

Alifungua macho yake na kujikuta akiwa kafungwa kamba kwenye vyuma vilivyo ndani ya chumba chenye giza na alipojaribu kujitingisha mikono yake akajikuta akichomwa na vitu vyenye ncha kali.
"Niko wapi hapa?" Jennifer aliuliza swali ambalo lilimfikia moja kwa moja Catherine ambaye alikuwa akiongea na simu nje ya chumba hicho na kumfanya kurudi ndani.
"Ooh Malkia umezinduka? Karibu sana kwenye dunia ya giza." Sauti ile ilimfanya Jennifer kugeuza kichwa na kujaribu kuangalia kama atayathibitisha masikio yake ambayo yalimpa taarifa ya sauti hiyo.
"Usihangaike kutaka kunijua mimi ni nani." Catherine aliwasha taa iliyokuwa karibu na kiti ambacho alikalia ambayo ilimfanya kuonekana vizuri.
"Haaa wewe si mama Mchungaji?" Jennifer alimuuliza baada ya kuiona sura yake vizuri.
"Yes wala hujakosea mwanangu mimi ndiye na hutakosea ukiniita Catherine." Alimjibu akiinuka kitini kumfuata.
"Kwanini umeniteka mama yangu?" Jennifer alimuuliza.
"Unaka kujua sababu ya kukuteka Jennifer?" Catherine alimuuliza.
"Ndiyo maana nikifikiria sijawahi kukukosea hata siku moja mama yangu." Jennifer alimjibu.
"Nisikilize binti yangu nimefanya hivi baada ya marehemu mama yako kushirikiana na mume wangu kufanya ambayo walifanya huku wakijua kufanya hivyo ni kinyume na taratibu za kanisa."
"Una maana gani kusema hayo?" Jennifer alimuuliza.
"Labda nikuulize swali dogo tu Jennifer, hivi wewe ni mtoto wa nani?" Catherine alimuuliza akiwa nyuma yake akiishikashika kamba iliyokuwa ikining'inia.
"Mimi?" Jennifer alimuuliza.
"Ndiyo wewe kwani tuko wangapi hapa ndani?" Catherine alimuuliza.
"Mimi si ni mtoto wa Otago Mathew?" Jennifer alimjibu.
"Uko sahihi Jennifer lakini na mimi nikikuambia kuwa wewe si zao la Otago utaamini?" Catherine alimuuliza.
" Kivipi mama Mchungaji?" Jennifer alimuuliza.
" Sina jibu la moja kwa moja lakini kuna simu nakwenda kuipiga hapa na hii ndiyo itakupa ukweli Jennifer." Catherine aliipiga simu ya Mchungaji Rodney Hauser huku akirudi kwenye kiti.
" Naongea na nani tafadhali?" Mchungaji Rodney Hauser alimuuliza baada ya kupokea simu kwa sababu Catherine alitumia simu yenye usajili mwingine ambayo Mchungaji hakuwa nayo.
"Ongea naye huyu mtu anza kwa kujitambulisha." Catherine alimwambia Jennifer akimkabidhi simu ambayo ilikuwa loudspeaker.
"Haloo!!" Jennifer aliita.
"Haloo , haloo ya nini nimeuliza naongea na nani?" Mchungaji aliuliza kwa hasira.
"Naitwa Jennifer na wewe ni nani?" Jennifer alimuuliza.
"Jennifer? Jennifer gani?"
"Jennifer Otago." Jennifer alimjibu.
Lakini kabla hajaongea kingine chochote Catherine alimnyang'anya simu Jennifer na kutoka nayo nje ya kile chumba na kwenda kumkabidhi kijana wake aliyeshirikiana naye kwenye utekaji huo.
"Jennifer, Jennifer!!" Mchungaji Rodney aliendelea kuita.
"Unaonekana unampenda huyu binti yako au nakosea?" Kijana huyo aliuliza akiwa anaingia ndani alimo Jennifer.
"Binti yangu? Kwani wewe ni nani?" Mchungaji Rodney alimuuliza mtu huyo.
"Mimi ni mfanyabiashara wa watu kama Jennifer." Alimjibu akimgeukia Catherine kuona kama anakwenda sawa na Catherine akamuonesha dole kuashiria kuwa yuko sawa.
"Mfanyabiashara kivipi?" Mchungaji Rodney alimuuliza.
"Naomba unisikilize vizuri wewe Mchungaji Uchwara mikononi ninaye mwanao Jennifer najua unampenda vizuri sana hivyo basi ili usikutane na jina jingine la huyu mtoto fuata maelekezo yetu."
"Isiwe umemteka binti wa watu wewe?" Mchungaji aliuliza lakini kabla hajafanya chochote kile simu ilikatwa.
Kisha alimkabidhi simu Catherine ambaye alikuwa kamtolea macho Jennifer.
"Mbona siwaelewi? Mimi sina kosa lolote ambalo nimelifanya kwenu naomba mniachie tafadhali." Jennifer aliomba msaada akiwa anatokwa machozi.
"Nakufungua kamba lakini utaendelea kuwa chini ya uangalizi wetu ndani ya hili pango. Umeelewa?" Catherine alimwambia Jennifer.
"Mama yangu naomba uniachie nikaungane na wenzangu chuoni."
"Chuoni? Chuo gani hicho? Kuhusu chuo kwa sasa hesabu ziro mpaka zoezi langu likamilike." Alimjibu huku kijana wake akimfungua kamba.
Akiwa amesimama akimuangalia kijana wake anavyomfungua kamba Jennifer mara simu yake iliita na baada ya kuiangalia ilikuwa namba ngeni hivyo aliipokea na kuweka sauti ya juu (loudspeaker) kisha akamkabidhi Jennifer hebu ongea na hii simu.
"Halo, ha...halooo...." Jennifer alipokea.
"Naombeni msimfanye chochote mwanangu na kama kuna mnachohitaji tafadhali niambieni mimi lakini msimtese mwanangu."
"Ba..ba...baba ni wewe?" Jennifer aliuliza baada ya kuijua sauti ya Otago.
"Mwanangu Jennifer ni wewe? Vipi hawajakufanya chochote hao watekaji?" Otago Mathew alimuuliza binti yake.
"Ha...ha...hapana huyu ni....." Lakini kabla hajaongea chochote alikutana na kofi ambalo lilimpeleka chini.
"Unataka kumwambia nini baba yako? Jiangalie wewe." Catherine alimwambia akimkabidhi simu kijana wake.
"Kuna nini tena mwanangu?" Otago aliuliza baada ya kusikia mzozo upande wa pili wa simu.
"Jiangalie wewe kiumbe acha kufuatilia mambo yasiyo kuhusu na kama unamhitaji binti yako akiwa salama funga domo lako na subiri simu yetu kinyume chake utapokea taarifa mbaya za mwanao" Alikata simu na kumkabidhi Catherine ambaye aliipokea na kuiweka mfukoni kisha alimfuata Jennifer pale chini alipokuwa kalala akilia.
"Jennifer ukijitia kujuajua utaishia kuyaonja mauti ambayo hayata kuwa na mliaji."
"Naomba unisamehe mama sirudii tena." Akiendelea kulia pale chini.
"Unatakiwa kuwa mpole tofauti na hapo utajuta si umeona simu ya pili imekuja wakati sisi tulipiga kwa mwingine? Hivi ndivyo watu wanavyokuwa hawana subira Jennifer hivyo unatakiwa kuwa mpole." Catherine alimwambia Jennifer aliyekuwa akijikongoja kuinuka.

***

"Niambie Daktari wangu, Wanaendeleaje wagonjwa wangu?" Martin alimuuliza Daktari anayewashughulikia wakina Seynabou.
"Wanaendelea vizuri sema huyu wa kuitwa Adoyee itamchukua muda kupona majeraha yake kutokana na namna ambavyo alishambuliwa lakini huyu Seynabou muda wowote atakuwa sawa." Alimjibu.
"Hawa wengine?" Martin aliuliza akionesha waliko wakina Awadh waliko.
"Wale hawana tatizo wako vizuri tu sema niliyekuwa nina wasiwasi naye alikuwa yule Soud lakini vipimo vimeniridhisha yuko vizuri." Daktari alimjibu Martin.
"Vizuri kumbe wewe endelea kuwashughulikia wakina Adoyee wacha mimi nikafanye yangu." Martin alimwambia akielekea ndani kwake.
"Sasa wacha mimi nirudi kituoni nikaendelee na shughuli nitarudi baadaye kuwaangalia." Daktari alimuaga Martin ambaye alimpa tu ishara akiingia ndani.
"Nipe taarifa Martin." Ulikuwa ujumbe ambao uliingia kwenye simu ya Martin akiketi ofisini kwake. Aliusoma kisha akaona aujibu. "Makamanda wanaendelea kuimarika kila dakika." Lakini akakumbuka kitu hivyo akaona wacha amuulize Catherine.
"Kuna tukio la kutekwa kwa mmoja wa wanamichezo kutoka Chuo kikuu cha Lagos, vipi umeipata hiyo?" Alimaliza na kuutuma.
"Nimeipata hiyo sijui ni nani atakuwa amefanya hilo tukio kwa kweli na kwa anavyoonekana alijiandaa iweje asikamatwe?" Catherine alimjibu.
"Du mimi nilijua ni wewe, sasa iweje unashangaa?" Martin alimuuliza.
"Hivi huyu mwanamke hausiki kweli?" Martin alijiuliza swali akilifungua kabati kuchukua nyaraka zake.
"Hivi kaka Martin sisi si tunaruhusiwa kuanza mazoezi kama ulivyosema jana?" Jumbe alimuuliza Martin.
"Tunaweza kuanza lakini wacha kwanza tupate taarifa ya mwisho ya Daktari ili ikiwezekana tuanze pamoja na wakina Seynabou." Alimjibu.
"Sawa kaka lakini vipi kuhusu ile taarifa ya Lagos umewasiliana na Madam?"
"Yeye mwenyewe anashangaa kama sisi sijui mhusika ni nani?" Martin alimjibu akipitia nyaraka moja baada ya nyingine.
"Naomba Jumbe na Awadh waanze safari kesho kuja Nigeria kuna kazi nataka ikamilike ndani ya siku nne zijazo." Ni ujumbe uliotumwa kwa Martin na Catherine.
"Kesho? Na huko kuna kazi gani?" Alijiuliza swali baada ya kuusoma ujumbe huo. Akaona wacha ampigie moja kwa moja.
"Madam sijauelewa ujumbe wako." Martin alimwambia baada ya simu kupokelewa.
"Ni hivi, huku nimefanya tukio la kwanza mliloliona kwenye vyombo vya habari lakini katika pitapita yangu kwenye 'app' nimeiotea namba ya mzee Malick ikiwa kama kilometa hamsini tu kutoka nilipo hivyo ninataka kuifanya hiyo kazi kabla hajashtuka." Catherine alimjibu.
" Kwa hilo ondoa shaka wataanza safari alfajiri." Martin alimjibu.
" Na iwe hivyo aisee." Catherine alisisitiza na kukata simu. Martin alitoka na kuwaita wakina Awadh na kuwaeleza kila kitu kama alivyoambiwa na Catherine hivyo akawataka wafanye maandalizi ya safari.

JE NI NINI KITATOKEA KATIKA KITIMUTIMU HIKI?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.

1607534661335.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
MUUAJI MWENYE BARAKOA - 28
Sultan Uwezo
+255

Jiji la Lagos lilikuwa limekumbwa na Taharuki iliyopelekea kila mtu kupatwa na hofu, hii ilikuja baada ya tukio la kutekwa kwa mmoja wa wanamichezo kutoka Lagos International University ambaye ni mtoto wa Otago Mathew aitwaye Jennifer. Tukio hili liliwachanganya mpaka wamiliki na waandaaji wa michezo hiyo kutokana na umakini wao katika zoezi la kuwasajili washiriki. Kutokana na kutokea kwa tukio hili Chuo kiliiahirisha michezo hiyo ili kutoa nafasi kwa vyombo vya Usalama kufanya kazi yake kuhakikisha wanampata Mtekwaji pamoja na Mtekaji. Kikosi kazi kilichopewa Jukumu hilo kilifika chuoni hapo kuongea na Viongozi wa chuo pamoja na Wanachuo kwa ujumla hasa wale ambao walikuwa karibu na Jennifer.
"Karibu sana Inspector, naitwa Prof. Oneke Kauzeni ndiyo mkuu wa chuo hiki." Alimkaribisha.
"Asante mkuu kama kitambulisho kinavyojieleza mimi ndiye niliyepewa jukumu la kufuatilia tukio lililotokea hapa chuoni kwako kwa leo nitakuwa nina maswali machache kwako."
"Karibu tu Inspector niko tayari kutoa ushirikiano kwa kadri nitakavyoweza." Mkuu wa Chuo alimjibu.
"Prof. Oneke Kauzeni unaweza kuniambia Chuo chako kina Wanachuo wangapi jumla?"
"Kina Wanachuo wapatao Elfu Kumi na Sita mia mbili." Alimjibu.
"Vizuri kati ya hao ni wangapi wanaishi Bweni na wangapi wanaishi nje ya Chuo pia kama hutojali nipate idadi yao kwa jinsi." Insp. Jonathan alimuuliza swali jingine ambalo lilimfanya mkuu wa Chuo kuinuka na kuelekea lilipokuwa kabati akalifungua na kutoa faili kubwa la bluu na kurudi nalo mezani.
" Mmh wanaoishi hapa chuoni wapo Elfu nane mia tano na kati ya hao wa kike wako elfu tano na waliobaki ni wa kiume ambao wako elfu tatu mia tano. Na wanaoishi nje ya Chuo wako elfu saba mia saba huku wa kike wako elfu mbili mia sita na wa kiume wako elfu tano mia moja." Alihitimisha kwa kufunika faili huku akitoa miwani yake machoni.
" Oo kumbe, inaonekana idadi kubwa ya Wanachuo wanaoishi nje ya Chuo ni wanaume siyo?" Insp. Jonathan aliuliza.
" Iko hivyo Inspector unajua Chuo chetu kilitoa nafasi kubwa kwa wanawake kukaa hapa huku nafasi chache zikibaki kwa wanaume." Prof. Oneke Kauzeni alimjibu.
" Na kwa picha hiyo Chuo chako kina kundi kubwa la Vijana wanaotumia madawa ya kulevya ikiwa ni pamoja na Uhalifu. Unalizungumziaje hili Profesa?" Alimuuliza.
" Kwa upande huo sina jibu la moja kwa moja kama unavyojua hawa ni watu wazima na wana mambo yao ambayo mengine yako wazi na mengine wameyaminya kwapani." Alimjibu.
" Sawa hebu tuache hayo turudi kwa Jennifer Otago ni mtu wa aina gani?" Inspector Jonathan aligeukia kwa Jennifer.
" Ni msichana anayejitambua sana kuanzia kiakili na kitaaluma." Alimjibu.
" Hakuna mtu aliyekuwa kwenye mahusiano naye au aliyekuwa na ugomvi naye kwa siku za hivi karibuni?"
" Kiukweli hapana ila toka atoke kwenye msiba wa mama yake Jennifer amekuwa mkimya sana hata idadi ya marafiki zake amepunguza. Na kuhusu mahusiano kuna kijana mmoja hivi alikuwa naye karibu mpaka walipokuja kuingia kwenye mgogoro ambao sikujua uliishia wapi." Mkuu wa Chuo alimjibu.
" Unaweza kunitajia jina la huyo kijana tuanze naye."
" Anaitwa Taddeo Makoko ni mwanachuo wa mwaka wa tatu akichukua Shahada ya Mahusiano ya Umma." Alimjibu.
" Nitampataje kijana huyu?"
" Namba yake ya simu ni hii hapa pamoja na picha yake." Alimjibu akimuonesha picha ya passport iliyokuwa ukutani sambamba na mawasiliano yaliyokuwa chini yake. Inspector Jonathan aliinuka akaitoa ile passport kisha akaandika namba ya simu nyuma ya picha ile kisha aliaga na kuondoka. Akiwa nje ya jengo la utawala wa Chuo hicho alipokea taarifa kupitia simu yake.
"Inspector kuna tukio jingine limetokea ndani ya Hoteli ya Virgo iliyo mtaa wa Mandela jirani na kituo cha mafuta cha 'Sahara Petroleum' kwa Maelezo ya Wahudumu ni kwamba tukio limetokea dakika kumi sita zilizopita." Aliusoma ujumbe ule kisha akacheka, aliangaza huku na kule kuona kama kuna mtu aliyemuona akicheka.
" Kazi tunayo haki ya Mungu." Alijisemesha akiipiga ile namba.
" Umeuona ujumbe mkuu?" Upande wa pili uliuliza baada ya simu kupokelewa.
" Nimeuona ujumbe Koplo Dorine mpaka nimecheka maana naona akili zetu zimekamatwa na kikundi fulani cha watu. Kwa hiyo mko wapi ninyi?" Inspector Jonathan aliuliza.
" Sisi tuko njiani kuelekea eneo la tukio mkuu." Koplo Dorine alimjibu.
" Wanasemaje kuna mauaji yaliyotokea?"
" Hakuna mauaji yoyote ila Mhanga hali yake ni mbaya sana." Alimjibu.
" Tunakutana huko muda si mrefu." Inspector Jonathan alimjibu akikata simu na kuingia kwenye gari. Baada ya kuingia kwenye gari aliwasha redio akifunga mkanda tayari kwa safari.
" Zilizotufikia hivi punde ni kwamba watu wasiojulikana wameingia ndani ya Hotel ya Virgo na kumshambulia mmoja wa wateja wa Hotel hiyo huku mwenzake akifanikiwa kuwakimbia watu hao. Kwa mujibu wa wafanyakazi wa Hotel hiyo wamesema wameshindwa kumtambua mshambuliaji ambaye aliificha sura yake kabla ya kufanikisha shambulio hilo. Kwa sasa wanaosubiriwa ni watu wa Usalama na sisi tutakuwa bega kwa bega kuwaletea kila linaloendelea... Kwa Habari zaidi endelea kusikiliza '100.7 Oceanic FM radio' Burudani bila Karaha." Habari hii ilimfanya Inspector Jonathan kukuna kichwa akimuangalia aliyekuwa mbele yake akikatisha.
" Mji wetu umekumbwa na nini mbona matukio ya ajabu ajabu kama haya hayakuwepo?" Aliendelea kujiuliza. Aliondoka kasi eneo lile kiasi cha kuwafanya waliokuwa eneo lile kugeuza vichwa kuliangalia. Na ndani ya dakika kama kumi alikuwa eneo la tukio alishuka na kuingia ndani ambako aliwakuta wenzake wakiwa wameanza kufanya uchunguzi.
" Mgonjwa yuko wapi?" Aliuliza Inspekta.
"Bado yuko kwenye kile chumba pale." Mhudumu alimjibu akimuonesha. Aliongoza mpaka kwenye hicho chumba akaingia na kukutana na wakina Dorine wakimfanyia uchunguzi.
"Mmegundua nini?" Aliuliza akimuangalia kwenye macho.
"Amedungwa sindano ya sumu eneo hili la shingo."Koplo Dorine alimjibu akiandika vitu fulani kwenye kijitabu chake.
" Mmemtambua utambulisho wake?" Alimuuliza tena Dorine ambaye badala ya kumjibu alitoa kitambulisho na kumkabidhi baada ya kukipokea alikiangalia kitambulisho hicho kwa umakini mkubwa kisha aliinuka na kumuaga Koplo Dorine.
"Ukimaliza akimbizwe Hospitali ripoti nitaikuta mezani kwangu."
"Sawa Mkuu." Koplo Dorine alimjibu. Inspekta Jonathan alitoka na kuelekea kilikokuwa chumba cha ulinzi kinachoongoza kamera zote mle Hotelini.
"Namuomba mhusika wa hiki chumba tafadhali." Alimwambia kijana aliyemkuta koridoni.
"Ni mimi Afande."
"Okay vizuri kifungue mara moja." Alimwamuru akifungue. Kilifunguliwa na moja kwa moja alielekea zilikuwa Kompyuta na kumwita yule kijana.
"Hebu niwashie hizi Kompyuta zote haraka." Ziliwashwa kama alivyoagiza kisha akampisha Inspekta Jonathan ambaye aliketi na kuanza kufuatilia picha mjongeo zote za siku hiyo. Akiwa anaangalia picha moja baada ya nyingine macho yake yalitua kwenye picha ya watu wawili waliokuwa wakiingia chumba namba 99 aliichunguza vizuri na kugundua walikuwa na wanaume wawili.
"Hawa watu waliingia kufanya nini kwenye hiki chumba." Alijiuliza swali akiziangalia picha za kwenye kile chumba.
"Mmh mbona siwaelewi hawa watu." Aliendelea kujiuliza akiziangalia zile picha.
"Hebu niitie mhusika wa vyumba mara moja." Alimuagiza kijana yule. Na wakati akiendelea kuziangalia mara alimuona mmoja wa wale watu akitoka nje na hapo aliigandisha ile picha na kuikuza.
"Ni nani huyu?" Alijiuliza akimfuatilia huyu mmoja ambaye aliingia chooni cha ajabu alipotoka alikuwa ni jinsi nyingine ya kike lakini akiwa kaificha sura yake kwa kofia maalum kisha akatoka na kutokomea kupitia dirishani.
"Whaaaaat! Ni mwanamke?" Alitoka haraka na wakati akiwa koridoni alikutana na mtu wa mapokezi aliyekuwa kaongozana na yule kijana aliyemuagiza.
"Ndiyo wewe?" Alimuuliza.
"Ni mimi mkuu."
"Chumba namba 99 kilichukuliwa na mgonjwa aliyeshambuliwa?"
"Hapana kilichukuliwa na rafiki yake ambaye alijitambulisha kwa jina la Karij."
"Yule hakuwa na lengo zuri." Aliwaambia na kuondoka akiwaacha wanamshangaa na moja kwa moja akaongoza kwenye gari lake.

***

"Nipe ripoti ya hapo Awadh." Catherine alimwambia Awadh akiwa kwenye kilima kilicho nje kidogo ya mji akiiweka simu ambayo alikuwa akiitumia awali.
"Bado tuko naye hapa mwanao kwa sasa kapunguza kulia." Awadh alimjibu.
"Na vipi kuhusu chakula amekula?"
"Hilo ndiyo tatizo kakataa kabisa kula na sisi tumeona tusimlazimishe njaa itamuita tu."
"Kuna mtego nautega wa hawa vinyago ambao wanajiandaa kuja kuifuatilia simu ya jana hivyo nimeona nije niiweke huku niliko na kuhusu Mjomba ashukuru nilikikosea chumba chake akanitoroka lakini mpambe wake Gidion anapumulia mashine na bila shaka muda si mrefu watapata majibu kwani kwa sumu ile sidhani kama atatoboa kesho." Catherine alimjulisha Awadh kilichotokea.
" Ila kuwa makini sana si unamjua Mjomba wako hawezi kukubali kirahisi." Jumbe alimtahadharisha Catherine.
" Wala msiwe na wasiwasi na mimi mkitaka kujua ilikuwaje tegeni masikio yenu." Alimaliza na kukata simu kisha akarudi kwenye gari na kuondoka eneo lile kabla hajashtukiwa.
" Hivi Mchungaji Rodney Hauser kukimbilia sijui Tanzania unafikiri nakuacha huu moto mwingine hauzimwi kwa maji wala zimamoto." Alijiwazia akiwa nyuma ya usukani wa gari akishuka kutoka kule kilimani alikokuwa. Aliichukua simu akampigia Martin kutaka kujua hali ya wagonjwa wake.
" Martin unaendeleaje kaka yangu?"
" Tunashukuru mambo yanakwenda na hawa vijana wako wanazidi kutengamaa kila wakati nafikiri ndani ya siku kadhaa watakuwa sawa." Martin alimjibu.
"Yaani sijui nikushukuru vipi kaka yangu maana ningekuwa peke yangu sidhani kama ningeweza." "Wala usijali dada yangu ni mambo ya kawaida haya." Martin alimjibu.
"Nashukuru sana kaka naomba uniunganishe na Seynabou niongee naye."
"Wala usijali huyu hapa ongea naye katoa macho hapa utafikiri anakamuliwa majipu." Martin alitania akimkabidhi simu Seynabou.
"Dada huyu achana naye maneno mengi kama nini?" Seynabou alianza.
"Niambie mdogo wangu, unaendeleaje?" Catherine alimuuliza.
"Kwa sasa nisiwe muongo, naendelea vizuri kwa kweli naona hata Adoyee kaanza mazoezi mdogo mdogo." Alinijibu.
"Nashukuru kusikia hivyo wacha niwaache kuna kazi naifanya hapa nitawacheki."
"Sawa dada." Seynabou alimjibu kisha simu ilikatwa na Catherine akaendelea na safari kurudi Pangoni.
"Kwanini hutaki kula chakula au una undugu na kifo?" Catherine alimuuliza baada ya kufika.
"Naombeni mniachie nirudi shuleni mimi chakula cha nini?" Jennifer alimjibu.
"Naomba tumieni nguvu zenu kuhakikisha anakula huyu." Alitoa maagizo akienda kwenye fuko lake la nguo. Baada ya kukaa aliiwasha 'app' na kuingia kwa lengo la kumfuatilia mzee Malick alikoelekea.
"Kumbe, nakufuata leo leo na majibu utayapata mimi ndiyo Catherine." Alijisemea akiiangalia signo kwenye simu yake.
"Ukitaka kupata salama ya moyo wako nakuomba ujisalimishe kabla sijakufikia si unajua mimi huwa sikimbiwi na mtu yoyote yaani ni kama kivuli hivi." Catherine aliutuma ujumbe huo kupitia kwenye 'app' ile kwa lengo la kumpoteza boya mzee Malick Bolenge. Kisha aliondoka kwenye 'app' na kuiweka simu yake pembeni na kuanza kula chakula ambacho alikuwa kakiweka pembeni yake.
" Najua muda huu utakuwa unahangaika kumjua aliyekutumia ujumbe." Alijisemesha akinawa.
"Hivi ninyi mmekula kweli?" Catherine aliwauliza wakina Jumbe.
"Yaani mpaka muda huu tuwe bado si tunaweza kufa, kitambo tulishatupia na matumbo yako sawia kwa sasa." Jumbe alimjibu.
"Madam hivi unauhakika hapa hawawezi kutukuta kweli?" Awadh alimuuliza.
"Labda tuamue sisi kuondoka lakini siyo kuogopa kitu chochote kumbuka kabla ya kuja hapa nilipafanyia utafiti." Catherine alimjibu.
"Ila tunatakiwa kuhama hapa kwanza hili eneo lina mbu sana tunaweza kuugua malaria." Awadh alimwambia Catherine.
"Hilo tutalifanyia kazi kesho wala msijali kwa leo waache mbu wapate faida ya mwisho." Aliwaambia huku akicheka. Lakini mara simu yake iliita aliiangalia kisha aliipokea.

JE NI NINI KITATOKEA?

TUKUTANE KATIKA SEHEMU INAYOFUATA.

1607534661335.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Poti tupo tunaendelea kukata kona mitaa ya Nigeria
 
Back
Top Bottom