Moyo Ulioonja Maumivu

Moyo Ulioonja Maumivu

SEHEMU YA 52

Penzi jipya likamteka na kumsahaulisha na kila kitu. Siku zikaendelea kwenda mbele ndipo alipogundua kwamba Watanzania walijua kilichokuwa kimetokea na mbaya zaidi tayari waliweka kwenye mitandao picha zake mbalimbali ambazo alipigwa akiwa na mwanamke huyo.
“Violeth...” hilo ndilo jina lililomjia kichwani mwake.

Akahisi moyo wake ukishtuliwa na kitu kama shoti ya umeme, kama watu walipiga picha kwa siri na kuziweka kwenye mitandao ilimaanisha kwamba hata mke wake huyo aliziona picha hizo.
Hilo likamkosesha amani kabisa.

Alikumbuka kwamba kwa siku mbili mfululizo alizokuwa akila raha na Iyanya alisahau kumpigia simu mwanamke huyo, alitekwa na penzi hilo jipya kitu kilichompa hofu kwamba inawezekana huo ukawa mwisho wa ndoa yake.

Akaichukua simu yake na kutaka kumpigia. Aliliangalia jina la mke wake huyo, alisita, alisikia maumivu makali mno. Violeth alikuwa mwanamke aliyetulia, aliyempenda na kumjali, kitendo cha kutembea na mwanamke mwingine kilionekana kuwa usaliti mkubwa mno.

“Mungu naomba unisamehe!” alisema Theo na kumpigia simu mke wake.
Simu ikaanza kuita, akaichukua na kuipeleka sikioni. Iliita na kuita lakini haikupokelewa. Hilo likampa majibu kwamba kile alichokihisi kilikuwa kweli kabisa, mke wake alifahamu kila kitu na kwa hasira hakutaka kabisa kupokea simu yake.

Simu iliita mpaka ikakatika. Hakutaka kuacha, akapiga tena zaidi na zaidi lakini matokeo yalikuwa yaleyale, hofu ikazidi kumuingia na alipoangalia kwenye mitandao ya kijamii, kila Mtanzania alikuwa akimlaumu kwa kile alichokuwa amekifanya.

Baada ya kupiga nusu saa, simu yake ikaanza kuita, haraka sana akaangalia kioo cha simu ile, jina la mke wake alilolisevu kwa B.A.E likaonekana, haraka sana akaipokea.

“Halo mpenzi...” aliita Theo.
“Theo! Kwa nini unanifanyia hivi?” lilikuwa swali la kwanza kutoka kwa Violeth, aliuliza huku akisikika kama mtu aliyeanza kulia.

“Kuna nini mke wangu?” aliuliza Theo kana kwamba hakujua kilichokuwa kikiendelea.

“Unanisaliti! Yaani umefikia hatua ya kunisaliti?” aliuliza Violeth huku akisikika akianza kulia.
 
SEHEMU YA 53

Theo akaanza kumbembeleza, alichomwambia ni kwamba hakuwa akimsaliti, asingeweza kufanya hivyo maishani mwake, alimpenda kuliko mtu yeyote yule katika dunia hii, asingeweza kufanya kitu cha kipumbavu kama kile.

“Kumbe yule ni nani?” aliuliza Violeth.
“Ni video mpya! Nitaachia video mbili hivi karibuni mpenzi! Picha nimeziruhusu ziwekwe kama kiki ila hiyo ni video mpya,” alisema Theo.

“Yaani picha hizo ni kiki?”
“Ndiyo mpenzi! Siwezi kukusaliti, na kama nimekukosea naomba unisamehe!” alisema Theo huku akitoa sauti ya kutia huruma mno.

Kwa jinsi alivyokuwa akimpenda mume wake, Violeth akaamua kukubaliana naye, alihitaji kuona mwisho wa kila kitu ungekuwa nini.

Alichokifanya Theo ni kuangalia picha zile, akatunga wimbo harakaharaka, akamuomba Iyanya warekodi video kwenye maeneo yaleyale tena huku akiwa amevaa nguo zilezile.
Hiyo haikuwa kazi, wimbo ulikamilika na hatimaye video kushutiwa na kisha kuanza kupandishwa vipande vichache.

Kila mtu aliyeziona picha zile, akashtuka, wengi wakaanza kujilaumu kwa kumtukana Theo na wakati picha zile zilikuwa ni za kwenye video yake mpya.
Watu wengi wakaanza kuwalaumu watu waliokuwa wamsambaza picha zile kwa lengo la kumchafua Theo ambaye alionekana kupendana na mke wake kupita kawaida.

Na ili kuongezea, kwenye akaunti yake akaandika maneno mengi ya kuwalaumu watu kusambaza picha zile pasipo kuuliza kilichokuwa kikiendelea kwani ndoa yake ilitetemeshwa kutokana na picha zile zilizokuwa zimesambazwa.

Mpaka kufikia hapo, kichwa chake kikawa na akili zaidi, aligundua kwamba alikuwa akifuatilia hivyo kufanya mambo yake kwa siri kubwa kabisa.

Penzi likazidi kukua mpaka ilipofika siku ya kurudi nchini Tanzania. Aliporudi na kuonana na mke wake, akamfuata na kumkumbatia, alimng’ang’ania kwa nguvu kiasi kwamba hakuwa amefanya jambo lolote lile.

Alimwambia jinsi alivyokuwa akimpenda, hakukuwa na mwanamke mwingine zaidi yake katika maisha yake. Violeth aliridhika maneno ya mume wake na kuamini kwamba hakukuwa na jambo baya lolote lile ambalo lilitokea huko Afrika Kusini.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom