Mkasa Wa Kweli: Ombaomba Aliyeuza Wanae

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,446
Image may contain: one or more people and text
 
OMBAOMBA
ALIYEUZA
WANAE

Bagamoyo, PWANI.

ILIKUWA ni jioni yenye mawingu angani na tulivu sana, upepo ulivuma kutoka upande wa kasikazini ukielekea kusini. Jua halikuwa likiangaza na si kwamba lilikuwa limekwisha potelea machweo, lilimezwa na mawingu yaliyokuwa yametanda! Kila dalili zilionyesha kwamba kama si jioni hiyo, basi usiku wa siku hiyo mvua ingenyesha.
Katika anga la kituo cha kusaidia wathirika wa dawa za kulevya na vilevi cha Tumaini, mwewe walionekana kwa mbali wakielea na kuifurahia jioni hiyo tulivu. Sauti za ndege mbalimbali waliokuwa kwenye miti iliyoota jirani zilikuwa zikisikika pia ndani ya kituo hicho.
Ni katika wakati huo huo, mwanamme mmoja, mweusi, mwenye makovu usoni, alikuwa amekaa kwa kuuegemeza mgongo wake kwenye kiti cha plastiki alichokiegesha ukutani nje ya jengo la ofisi za kituo hicho.
Mwanamme huyo alikuwa amevaa pullover nyeusi, iliyoandikwa kifuani kwa maandishi madogo meupe yaliyosomeka; We Care For Cervical Cancer Patients. Yakimaanisha; Tunawajali Wagonjwa wa Kansa ya Shingo ya Kizazi!
Kiunoni, alivaa suruari ya jeans ya blue, aliyoibana kwa mkanda mweusi, na miguuni alikuwa na sandozi nyeusi zenye mikanda ya moja kwa moja.
Jirani na alipokaa mwanamme huyo kulikuwa na kiti kingine cha plastiki ambacho hakikukaliwa na mtu, bali kilibeba kitabu. Kitabu kilicho andikwa kwenye kava; BECOME A BETTER YOU na kilionyesha kimeandikwa na mwandishi Joel Osten.
Mwanamme yule alionekana amezama kwenye mawazo fulani. Kwa namna alivyokuwa amekaa kwa kujiegemeza na kuikunjia mikono yake kifuani, kule alikokuwa ameyatoa macho yake kutazama hakuwa anaona lolote, macho na akili yake ni dhahiri vilikuwa sehemu nyingine kabisa.
Alikuwa amekaa kwenye hali hiyo kwa muda unaotosha kuitwa mrefu!
Na punde utulivu huo uliokuwa umemtawala uliondolewa na mtu aliyesota kwa baiskeli ya magurudumu, maalumu kwa ajili ya walemavu wa miguu mpaka mbele yake. Huyo mwanamme aliyepotelea mawazoni, alizirudisha fahamu zake mahali pale na kumtazama huyo mtu aliyekuwa mbele yake.
Kisha akakaa sawa!
Alikuwa ni mwanamama wa rangi ya maji ya kunde, mwenye umri wa kati ya miaka hamsini na tano mpaka sitini na aliyejifunga kilemba cheupe kichwani. Shingoni alikuwa amevaa rozali, machoni alivaa miwani nyembamba ya macho na mwilini mwake alitupia gauni lenye maua na rangi zaidi ya moja zilizo lipendezesha.
Huyo mwanamama alikuwa anatabasamu.
“Mwanangu…” alizungumza kwa bashasha.
“Mama…” yule mwanamme aliitika.
“Nilikwambiaje juu ya kukaa namna hii?” Alimhoji.
“Aaah,” yule mwanamme alitoa sauti ya kujilaani juu ya hilo. “Imetokea tu mama.” Alimwambia.
“Unajua ni kwa nini inatokea?”
“Hapana…”
“Unapenda kukaa mpweke.”
Yule mwanamme alipepesa macho.
Yule mama akaongeza upana wa tabasamu lake.
“Hata hivyo ninakufurahia,” akasema.
Mwanamme yule akaongeza umakini wa kumtazama.
“Kwa lipi mama?” Alimuuliza.
“Maendeleo yako,” alimjibu haraka. “Si’ kama ulivyo kuja. Ulikuwa hueleweki, mtu si mtu,mnyama si mnyama, lakini kwa sasa…angalau…haya makovu usoni yakiondoka utarudia kwenye ubinadamu!”
Wote walitabasamu.
“Najifurahia pia mama,” Hatimaye yule mwanamme alisema. “Kuna muda ninahisi nipo kwenye kisima ninakunywa maji yenye uhai wa kuishi kwa mara nyingine tena.”
Yule mama alitikisa kichwa kukubaliana na hiyo kauli huku akimuangalia huyo mwanamme kwa tabasamu la matumaini.
“Ulifanya uamuzi wa busara kuachana na pombe!”
“Hili unaniambia kila siku mama.”
“Na sitachoka kukwambia.”
“Kwa nini?”
“Unahitaji pongezi.”
“Ndio za kila siku?!”
“Ndio.”
“Mh!”
“Yes,… hivi unaf’kiri ni watu wangapi wapo kwenye janga kama hili ulilokuwepo na wameshindwa kutoka?”
Mwanamme huyo alipiga kimya.
“Si ni wengi?!” Yule mama alijijibu mwenyewe kwa swali.
Yule mwanamme akaafikiana naye kwa kupandisha na kushusha kichwa.
“Sasa kwa nini nichoke kukupongeza mwanangu…,” mama huyo alimwambia huku anatabasamu.
Huyo mwanamme naye aliachia tabasamu la mbali.
“Ila…” akasema kwa kusita. “Nayajutia sana maisha hayo ya ulevi!”
“Hakuna makosa maishani…ni mafunzo ya kutuonyesha njia…acha kujuta,” yule mama alimwambia.
Mwanamme akatulia kidogo.
“Na mama…” alimvuta usikivu yule mwanamke, “unaf’kiri ni kwa nini watu wanashindwa kutoka kwenye matatizo kama haya?” alimuuliza.
“Kwa sababu wapo kwenye janga…halafu hawakubaliani na ukweli huo, kwamba wapo jangani. Kila kinachoendelea kwenye maisha yao wanakiona ni sawa tu. Kwamba ndio maisha waliyo nayo na yanatakiwa yaendelee kuwa hivyo,” yule mama alijibu kirahisi.
Yule bwana akamakinika naye.
Huyo mama akatabasamu.
“Vipi?” Akamuuliza. “Umemaliza kusoma kitabu nilichokupa?” Huyo mama aliuliza akichukua kitabu kwenye kiti kilichokuwa mbele yake. “Naona umekiweka kushoto.”
“Nimemaliza mama.”
“Kwa hiyo nichukue kitabu changu?”
Yule mwanamme alitabasamu.
“Unaweza ukaniachia nikazidi kupitia kwa mara nyingine.”
Lilifuata tabasamu hafifu kutoka kwa yule mama mbele ya maneno hayo.
“Usijali…” alimwambia. “Lakini umepata ya kuambulia ambulia?” Alimuuliza.
“Mengi tu.”
“Basi yatumie kuyajenga upya maisha yako. Hii ni nafasi ya kuishi kwa mara ya pili ambayo umeipata. Nafasi ya kurekebisha pale ambapo ulijikwaa na kudondoka. Kwa kuwa ipo mikononi mwako unaweza kuitumia uwezavyo ama kuichezea na ikapotea kama awali.
“Lakini kumbuka, nafasi hii ni adimu na adhimu. Huja kama upepo na hupotea mfano wa moshi angani. Itumie vyema,” mama huyo alimaliza.
Huyo mwanamme ni kama alikuwa anasikiliza shairi kwa namna alivyokuwa amemakinika.
“Mama, samahani lakini….”
“Bila samahani.”
“Ni kweli hii niliyo nayo ni nafasi ya pili. Lakini…kwenye maisha mtu anayedondoka hupata nasafi moja tu… hiyo ya pili?...akidondoka tena na tena inawezekana hatimaye asiinuke?”
Yule mama alitabasamu.
“Nafasi ya pili kwa lugha rahisi ni nafasi nyingine!” Alimjibu. “Unaweza ukadondoka na kuamka…ukadondoka tena na kuamka…ukadondoka, hadi mara mia moja. Lakini nafasi ya muhimu ni ile unayoamka.”
Yule bwana hakuonyesha ishara yoyote usoni.
Mama yule mbele yake alimtazama kwa macho ya kusaili jambo. Akamuuliza kwa upole;
“Unajua kwa nini nafasi ya muhimu ni hiyo unayoinuka?”
Yule mwanamme alishikwa kigugumizi.
“Sina uhakika kama ninachoelewa ndio sawa.” Alijibu.
“Unaelewa nini?”
Akameza mate.
Kisha akajibu; “Ni muhimu kwa sababu ukidondoka, pale unapoamka unakuwa umejifunza mengi.”
“Ni kweli!” Yule mama alidakia kwa msisitizo. “Na nikwambie mwanangu; Hakuna anayedondoka kwenye maisha kwa bahati mbaya. Kwa kufahamu au kutokufahamu, tunadondoshwa na makosa. Yanaweza kuwa makubwa au madogo. Jambo la kusikitisha ni kwamba watu wengi tunapodondoka huwa tunakuwa na visingizio vingi. Visingizio vya kuwabebesha lawama watu, hali zetu za kimaisha na mambo mengi yanayoendana na hayo.
“Hiyo ni mbaya sana. Ili uamke unapaswa kuelewa ni kwa namna gani umedondoka. Lawama haziwezi kukuinua. Na pale tu unapofahamu sababu zilizo kudondosha na ukapania kuamka, hiyo ndio nafasi ninayoizungumzia. Nafasi ya pili!”
Yule bwana alishusha pumzi fupi.
Mama yule akacheka.
“Nikuache Masika The Best…” alimwambia akikiweka kitabu kile cha BECOME A BETTER YOU, kwenye mapaja ya Masika.
“Natamani tuendelea kuzungumza mama.”
“Hata mimi natamani iwe hivyo…lakini majukumu mengine yananingoja. Tupo wote, tutazidi kuzungumza zaidi!”
Masika alibakia kwenye tabasamu wakati mama yule akiiongoza baiskeli yake ya magurudumu kuelekea upande mwingine wa pale alipokuwa amekaa.

JIONI hiyo ambayo Masika alifanya mazungumzo na mama yule mlemavu wa miguu, aliyetambulishwa kwake kwa jina la Bi Modester siku ya kwanza tu anafika mahali hapo, ilikuwa ni ya kumi na nne tangu ajiunge kituoni hapo Tumaini.
Kwa hiyo alikuwa amefikisha wiki mbili!
Muonekano wa siku yake ya kwanza anafika, ulikuwa ni wa tofauti sana na huo aliokuwa nao wakati huo. Wakati anafika kituoni hapo afya yake ilikuwa imedhoofika mno kutokana na unywaji uliokithili wa pombe kali bila kula chakula cha kutosha.
Mbali na hivyo, midomo ilikuwa imebabuka na ngeu zilimjaa usoni. Lakini baada ya kupitia kwenye huduma za kitaalamu zilizotolewa mahali hapo, chakula bora na mazoezi yaliyofanywa kila asubuhi, Masika alikuwa ameanza kupata ahueni kubwa.
Lakini pia kutokana na kuhudhuria mafundisho ya kila siku yaliyotolewa kwenye ukumbi wa kituo hicho, juu ya madhara ya pombe, dawa za kulevya na vilevi, pamoja na namna ya kufufua maisha mtu unapodondoka kwenye majanga ya maisha na namna ya kuanza kuota upya, ufahamu wa Masika ulianza kurudi kuwa kama awali kabla hajaanza matumizi ya pombe kali.
Ufahamu wake uliimarika zaidi baada ya kuwa karibu na Bi Modester. Aliyekuwa kituoni hapo kwa ajili ya ushauri wa masuala mbalimbali kwa watu waliojiunga kwa ajili ya kupata msaada.
Ukaribu wao ulianza siku moja, mwanzoni mwa wiki ya pili ambapo Masika alikwenda kuzungumza na Bi Modester kwa ajili ya masuala fulani…
Wakiwa kwenye mazungumzo yale, Bi Modester alimuuliza Masika ni nini alikuwa anafanya huko nyuma.
Masika alimueleza juu ya taaluma yake ya habari.
Bi Modester aliomba aelezwe zaidi.
Masika akamueleza namna alivyojiingiza kwenye taaluma hiyo, alivyoitumikia kwa juhudi na upendo, lakini mbali na sifa za kubatizwa jina la Masika The Best, ilimuachia maumivu!
Masika akaendelea kumweleza pia Bi Modester namna alivyojiingiza kwenye masuala ya biashara, kabla ya ulevi kumzamisha. Hakusita kumsimulia pia mkasa wa kusikitisha uliompeleka jela mkewe.
“Kila kitu kwenye maisha hutokea kwa sababu…” Bi Modester alimwambia baada ya Masika kumaliza kumsimulia, “na wakati mwingine sababu zinaweza kujificha juu ya fikra zetu za kawaida!”
Masika alihamanika kana kwamba hakuelewa.
“Unamaanisha nini?” Alimuuliza.
“Umewahi kuona kitu kisichokuwa na chanzo?” Bi Modester naye alimuuliza.
Masika akainua macho akitafakari.
Msamiati juu ya msamiati!
“Mfano; huu uhai tulionao si unachanzo chake…?” Bi Modster aliendelea kwa kuuliza tena akimtazama Masika kwa macho yenye mkazo. “Mimea, miti, mawe, mabonde, kila kitu kina chanzo chake…si ndio?”
“Ndio!” Masika alimjibu.
“Na chenye chanzo kina mwisho…unakubaliana na mimi?”
“Ndio.”
“Sasa kama kitu kilianza…” Bi Modester alizungumza akimuonyesha Masika kwa ishara ya kupeleka kidole kutoka sehemu moja kwenda nyingine; “halafu kikaja kufika mwisho… hapa katikati kuna sababu iliyokifanya kiwepo!” Aliongeza.
Masika alibaki amemakinika na kidole kile cha Bi Modester.
“Mmmh…ni kweli,” kisha alijibu baada ya ukimya wa bibi yule, lakini kama asiye na uhakika.
Bi Modester alitabasamu.
“Ipo hivyo Masika!” Alimwambia. “Kinachoanza na kufika mwisho kina sababu ya kuwepo. Ni kama sisi binadamu, kwa sababu mwanzo wetu ni kuzaliwa na mwisho wetu ni kifo, tunasababu ya kuwepo duniani.
“Na hata matatizo yanayotutokea. Hua na sababu ya kutokea kwenye maisha yetu!”
“Kwa hiyo unataka kumaanisha yote yaliyonitokea mimi yanasababu ya kunitokea?” Masika alimuuliza kwa wahka.
“Ndio!”
“Sababu ipi sasa?”
“Pengine ufike hapa tulipo!”
Baada ya kauli hiyo Bi Modester aliachia kicheko kifupi.
Masika alibaki kimya.
“Nisikilize mwanangu,” akamwambia. “Hayo yoote yaliyokutokea bila shaka yamekuacha na mafunzo mengi kwenye maisha yako. Hayo mafunzo ndio sababu yenyewe ya kila kitu kutokea. Ni wakati wako wa kuchukua njia nyingine…elekea unapotaka kuwa kwenye maisha!”
Kwa hiyo, baada ya mazungumzo yao ya siku hiyo wawili hao walijikuta wanakuwa karibu sana. Mara kwa mara walipopata nafasi walikaa na kuzungumza mambo mbalimbali kuhusu maisha. Na siku moja Bi Modester, alimuazimisha Masika kitabu kiitwacho Become A Better You, ambacho Masika alijifunza mambo mengi kwenye kitabu hicho.
Ukaribu wao haukuishia hapo.
Ilifikia hatua Bi Modester akamsimulia Masika historia ya maisha yake. Alimueleza wazi kwamba hakuzaliwa akisota kwenye kiti kile cha magurudumu. Alifika pale kutokana na masaibu ya dunia, ambayo yaliendelea kufumuka mpaka akajikuta akiwa ombaomba mtaani. Hako nako alikutana na mengi yenye kuumiza yaliyomfanya akate tamaa ya kuishi, akafika hatua ya kuwauza wanae wa kuwazaa na ndipo jina la Ombaomba Aliyeuza Wanae, lilipoibukia.
Masika alimsikiliza kwa makini bibi huyo na baadaye akajitoa muhanga, kwenda kuwatafuta watoto hao waliouzwa. Safari hiyo haikuwa ya mchezo, ndio safari iliyotengeneza historia nyingine ya mkasa wa kuvutia na kusisimua kwenye maisha ya James Masika.
Masika The Best!

ITAENDELEA….
 
OMBA OMBA ALIYEUZA WANAE- 2

NILIPOZALIWA nami nilikuwa na miguu yangu,” Bi Modester alianza kumsimulia Masika. “Najikumbuka enzi hizo nikiwa msichana…” akaufyatua ulimi wake kwa kite cha kulaumu ama kusikitika akiwa kwenye tabasamu hafifu. “Nilivutia sana!”
Masika alitabasamu.
“Lakini ni safari ya maisha ndio imenifikisha hapa!” Masika alizidi kukaa kwenye hali ya utulivu akimsikiliza.
“Ningekuwa siamini kuwa, kuna sababu ya kila kitu kuwepo…ningesema nilizaliwa kwa bahati mbaya na ninaishi kwa bahati mbaya!” alisema na kutulia.
“Kwa nini?” Masika alimuuliza kwa sauti ya chini.
“Nkhm!” Bi Modester aliguna.
Kisha akasema; “Hata baba yangu sijawahi kumtambua!”
Masika alivutika zaidi.
Akaweka mkono shavuni na kumakinika na bibi huyo.
“Alikufa ukiwa hujazaliwa…?” Alimuuliza. “Au ukiwa mtoto mdogo?”
“Na bora ingekuwa hivyo…lakini hata mama yangu tu hamjui!”
Eeeh!
Hali ya udadisi ilimuongezeka zaidi Masika.
“Mama yako hamjui?!” Aliuliza kwa hamaniko. “Hamjui vipi mtu aliyempa ujauzito?” Akauliza kwa mgandamizo wenye msisitizo.
Bi Modester aliachia tabasamu la kujificha, akapepesa macho pembeni. Kisha alianza kumsimulia Masika kwamba;

ALIZALIWA mjini Dodoma, na mama yake aliitwa Jema Teu. Akaendelea kuwa; akiwa binti mwenye akili za kujitambua, aliwahi kusimuliwa na bibi yake mzaa mama kwamba, ujauzito wake mama yake aliubeba wakati akiwa shuleni sekondari.
Alikuwa akisoma shule ya bweni huko jijini Mwanza,iitwayoBwiru Girls. Akiwa kidato cha nne, wikendi moja Jema aliondoka shuleni na rafiki zake na kwenda kujirusha kwenye klabu ya usiku. Akiwa huko akajikuta akipendana na kijana ambaye walikutana siku hiyo hiyo.
Kutokana na kubanwa shuleni, na tamaa ya ngono aliyokuwa nayo kwa muda mrefu, aliishia kulala na kijana yule kwenye nyumba ya kulala wageni.
Wakafanya mapenzi.
Lakini baada ya usiku huo hawakuonana tena kwa sababu hakuna kati yao aliyekuwa na simu na baada ya yeye kurudi shuleni hakupata nafasi ya kutoka. Baada ya mwezi mmoja Jema alijigundua kuwa ni mjamzito. Alihisi kuchanganyikiwa.
Akajiuliza atampata wapi kijana yule aliyempa ujauzito huo?
Hakupata majibu!
Alichokumbuka yule kijana alimuelekeza kuwa anaishi mitaa ya Ghana na jina lake ni Stanley. Lakini hata ujauzito ulipogundulika shuleni na kufukuzwa, alipo kwenda mitaa ya Ghana kumtafuta kijana huyo akiliulizia jina lake, aliishia ‘kumanga manga’ tu!
Ghana ilikuwa kubwa. Kila aliyemuuliza kuhusu kumfahamu Stanley anayeishi Ghana, swali la kwanza alilomuuliza, lilikuwa ni; anaishi Ghana ipi?
Ghana Kotazi? Ghana ya juu? Ghana ya chini?...Ghana ipi?
Hakuwa na jibu.
Jema akaamua kurudi nyumbani kwao Dodoma na ujauzito ule. Mama yake alifadhaika mno, mpaka alilia mbele ya mwanae!
“Jema umeniweza akia Mungu!” Alilalama kwenye kilio. “Kwa namna ambavyo nimekuwa nikijivunia kwa kinamama wenzangu juu ya jitihada zako za masomo, umeamua kunilipa kwa hili? Kubeba ujauzito usio na baba...!! Umeniweza siyo siri!...nilikuwa nina kutegemea siku moja utanifuta machozi baada ya kifo cha baba yako, kumbe nilikuwa najidanganya…aisee!”
Hakuna kilichobadilika, Hatimaye Jema alijifungua mtoto wa kike, wakamuita Modester!

MODESTER akiwa na miaka sita, Jema alifariki dunia ghafla. Kifo chake kilihusishwa na mambo mengi ikiwemo masuala ya kishirikina. Lakini ni kifo hicho kilichobadilisha taswira nzima ya maisha ya Modester wakati huo, kwani baada ya mama yake kufariki alichukuliwa na mjomba wake Saimoni aliyekuwa anaishi Singida.
Nyumbani kwa mjomba wake huyo, aliishi kwa kuteswa sana na mkewe.
Alifanyishwa kazi za nyumbani kama msukule, alikatishwa masomo na mengine mengi ya kuumiza. Hata alipolalamika kwa mjomba wake, hakuna mabadiliko yoyote yale aliyoyaona, alipodai kurudishwa kwa bibi yake, aliishia kuambiwa bibi huyo hana uwezo wa kumlea.
Ndipo siku moja akiwa mwenye umri wa miaka kumi na moja, Modester akaamua kuiba pesa nyumbani hapo na kutoroka.
Akaenda mpaka stendi ya mabasi ya Singida, madhumuni yake akate tiketi ya kuelekea Dodoma kwa bibi yake.
Lakini akiwa stendi hapo alijikuta anabadili mawazo ghafla- ni baada ya kufikiria kuwa akienda kwa bibi yake, kuna uwezekano mkubwa wa kurudishwa kwa mjomba wake, kwa sababu bibi huyo hakuwa na uwezo wa kumlea na kumhudumia mahitaji yake. Yeye mweyewe alitegemea msaada kutoka kwa wanae, hasa huyo huyo Saimoni, aliyekuwa anaishi naye.
Modester alifahamu pia kuwa, asingeweza kukataa kurudishwa kwa Saimon kama ingehitajika hivyo, maana hata angeleta ubishi ingewezekana kuchukuliwa kwa nguvu.
Aliutambua vyema ‘utemi’ wa mjomba wake!
Kwa hiyo, Modester alijifikiria mahala pengine pa’ kwenda. Akawaza kwa muda juu ya hilo, lakini hakupata majibu kwa sababu hakuwa na ndugu aliyemfahamu kwamba anaweza kukimbilia na akapata hifadhi. Akizidi kuwaza sasa achukue uamuzi gani, ndipo kuna mawazo yakamwambia aende Dar es Salaam!
Alipata mawazo hayo, kwa sababu amekuwa akiwaona vijana wengi katika maeneo hayo aliyoishi Singida, wakimaliza shule au kukatisha masomo wanakimbilia Dar es Salaam, wakidai kuwa wanakwenda kutafuta maisha.
Naye akajua huko, pengine angeweza kujitafutia maisha yaliyotafutwa na wengine akiwa mbali na macho ya ndugu zake.
Akakata tiketi ya basi liendalo Dar es Salaam!
Wala hakujua huko angefikia wapi, na wakati huo hakutaka kujali juu ya hilo, alimuachia kila kitu Jalali, na akajiapiza moyoni kwamba yatakayo jitokeza mbele ya safari atakabiliana nayo.
Akiwa basini alikaa upande wa dirishani, kimya! Jirani yake alikuwa amekaa mwanamke mmoja mnene wa makamo, ambaye umri wake ulikuwa kwenye miaka arobaini mpaka hamsini.
Safari iliendelea, lakini walipofika Chalinze yule mama alimzungumzisha Modester;
“Wewe binti, toka tunaanza safari sijakuona unakula…umekaa tu unaonekana mawazo yako yapo mbali, vipi?” Alimuuliza.
Modester akabakia kimya.
Mara machozi yakaanza kumbubujika.
Ama!
Yule mama alishangazwa na hilo.
“Huna pesa ya chakula?” Alimuuliza.
Modester akapandisha kichwa kukubali.
Yule mama hakujifikiria mara mbili, akamuita kijana aliyekuwa na kapu lenye soda, na vitu vya kula kula garini mle, akamnunulie mkate na soda Modester.
Modester akaanza kula.
Wakati anaendelea kula yule mama ikabidi amdadisi.
“Unaenda sehemu gani?”
“Dar!” Alimjibu.
“Najua ni Dar…lakini namaanisha Dar mtaa gani?”
Alikaa kimya.
Yule mama akamtazama kwa makini.
“Mbona kimya binti?” Alimuuliza kwa mkazo.
Binti yule akamtupia macho ya huruma.
“Sina pa’ kufikia!”
Yule mama alifinya macho ghafla, mdomo ukiachama kwa mshangao. Alimsikia yule binti alichokizungumza, lakini ni kama alikuwa hajamuelewa vile! Au hakikumuingia akilini!
Au hana akili timamu?
Alijikuta anajiuliza.
Anawezaje kusafiri pasipo kuwa na mahali pa’kufikia?
Aliendelea kujiuliza.
Akamtazama kwa kumsaili umri wake akamuona ni mwenye umri wa msichana kuweza kujitambua. Ikabidi amuulize vizuri;
“Sasa… umewezaje kufunga safari ukiwa huna mahali pa’kufikia…?? Na ukisha shuka kwenye basi…itakuwaje…? Utabaki hapo hapo Ubungo? Na wazazi wako wamekuruhusu ufunge safari ya hivi?”
“Sina wazazi…” Yule binti alijibu kwa sauti ya chini.
Mama yule akashusha pumzi na kuzungusha kichwa kwa masikitiko.
Ndipo alipomuuliza juu ya alikotoka na nini kilimsibu mpaka akaamua kufunga safari ile,isiyokuwa na mahali pa’ kufikia.
Modester alimsimulia kila kitu. Juu ya mama yake kufariki dunia, kutomfahamu baba yake na mateso makubwa aliyokuwa akiyapata nyumbani kwa mjomba wake.
Mama yule alimuonea huruma mno. Roho ya kumsaidia ikamuingia.
“Ninatamani kukusaidia…” alimwambia. “Lakini sijajua juu ya ndugu zako kama hawatakutafuta…wasije kukukuta nami wakaniwajibisha!”
“Hapana mama…kama unaweza kunisaidia naomba unisaidie tafadhali!” Modester alimsihi kwa unyenyekevu mwanamama yule.
Naye aliingiwa na roho ya huruma. Binti huyo alikuwa na umri sawa na binti yake wa kumzaa. Akawaza vipi kama hali hiyo ndio ingekuwa inamkuta binti yake, alihisi mpaka tumbo la uzazi likimkata. Machozi yakabisha hodi machoni kutoka.
Akaamua kumsaidia!
Akaenda naye mpaka nyumbani kwake. Alipozungumza na mumewe naye hakuwa na shida, wakakubaliana waishi na binti huyo, ikitokea ndugu zake wakimtafuta, watawapa.
Alimtambulisha kwenye familia yake kwa wanae wawili. Emiliana, aliyekuwa akiendana naye kwa umri na kwa Jackson, huyu aliwazidi kwa umri na Modester akamueshimu kama kaka yake.

ITAENDELEA JIONI..
 
OMBAOMBA ALIYEUZA WANAE- 3

NYUMBANI kwa mama Emiliana, Modester aliishi vizuri sana, yaani utadhani alikuwa ni mtoto wa pale. Hakunyanyaswa wala kusemwa tofauti, zaidi alipewa mahitaji yote muhimu kama walivyopata kina Emiliana na Jackson.
“Tumuandikishe shule?” Siku moja mzee Lauliani, baba wa familia ile alimwambia mkewe.
“Mh!” Mama Emiliana aliguna. “Na umri huo, atakubali kweli?”
“Zungumza naye, anapaswa tu kukubali…akafute ujinga!”
Mama Emiliana alizungumza na Modester juu ya jambo hilo la kuandikishwa tena shule ya msingi baada ya kukatisha masomo Singida akiwa darasa la pili, jambo ambalo hakulitegemea, Modester alilipokea kwa furaha sana jambo hilo.
Akaandikishwa shule.
Akiwa shuleni alikuwa anafanya vizuri sana. Zaidi akawa anawafundisha wanafunzi wenzake ubaoni pale ambapo mwalimu hakuwa darasani. Walimu wakamuona ni kichwa, wakamrukisha madarasa.
Darasa la kwanza alilisoma muhula mmoja, muhula mwingine akausoma akiwa darasa la pili. Ikawa hivyo katika miaka iliyofuata, katika mwaka wa tatu Bi Modester akawa amefika darasa la sita. Mwaka wa nne alipoingia darasa la saba, aliingia pamoja na Emiliana!
Kwenye mtihani wa kumaliza shule ya msingi wawili hao walifaulu pamoja, tena walipangwa shule moja.
Kutokana na kusoma shule moja na kuishi pamoja nyumbani Modester na Emiliana walitokea kuwa marafiki wakubwa sana, walioshirikiana kwenye mambo mengi, na pia walidokezana juu ya siri zao.
Kwa upande wa Jackson, kina Modester wakiwa kidato cha pili, yeye alimaliza kidato cha nne, na matokeo yalipotoka alikuwa amefaulu kujiunga kidato cha tano nje ya jiji, kwa hiyo baada ya kwenda shuleni muda mwingi wakawa mbali naye, walikutana kipindi cha likizo.
Miaka ikasonga mbele, Modester na Emiliana wakamaliza kidato cha nne, wakati Jackson yeye akimaliza cha sita. Bahati mbaya hakufaulu kwenda chuo kikuu. Baba yake mzee Lauliani alimtafutia nafasi jeshini alikokuwa na jamaa zake wanaofahamiana.
Akaenda huko.
Kina Emiliana na Modester walipomaliza kidato cha sita, walifanikiwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mlimani. Modester akisomea masuala ya saikolojia na mwenzie akisota na sheria!
Wakati huo, Jackson alikuwa mwajiriwa jeshini, kwa muda wa miaka miwili, na alifanyia kazi katika kituo cha Lugalo!

***
WAKIWA chuoni mwaka wa kwanza, Emiliana tayari alikuwa amekwisha jihusisha kwenye masuala ya mapenzi, na kila kitu alikuwa akimueleza Modester, lakini jambo la kushangaza mpaka wakati huo hakuwahi kusikia hata siku moja mwenzie huyo akimueleza juu ya kuwa na mpenzi ama kuvutiwa na kijana yeyote!
Ilibidi amuulize.
Ilikuwa ni katika jioni moja, siku moja kabla ya Sikukuu ya Pasaka, wakiwa chumbani kwao, Modester akiwa amejilaza kitandani akipitia pitia baadhi ya mambo aliyokuwa ameyaandika kwenye diary yake, na Emiliana akiwa anakunja nguo.
“Inamaana,” aliaanza kwa kuvuta usikivu. Modester akamtupia macho. “Mpaka sasa hujawahi kukutana na kijana akakupenda, nawe ukampenda?”
Nt’see!
Modester alicheua kite cha kutolitegemea swali lile.
“Nilifikiri unataka kuongea kitu cha maana…kumbe huo upuuzi!” alimjibu.
“Kwa hiyo uhusiano wa mapenzi kwako ni upuuzi?” Emiliana alimuuliza kwa sauti ya kushushua akisimama kuendelea kufanya kile alichokuwa anakifanya.
“Kwa sasa…ni upuuzi, na sitaki kujihusisha nao.”
Emiliana alitabasamu.
“Na sisi tunaojihusisha nao ni wapuuzi?”
“No…sijamaanisha hivyo, kwangu ndio upuuzi, kwa wengine unaweza kuwa jambo la msingi…ntajuaje!”
“Na, je?” Emiliana aliendelea akizungumza kwa pozi; “Akitokea kijana mzuuri ambaye hujawahi kumuona duniani, mrefu, aliyejazia, mwenye kifua kipana, anayezungumza kwa besi na kila sifa unazozipenda…bado utamkatalia, kisa kwa sasa mapenzi ni upuuzi kwako?”
Modester alifunga diary yake ile iliyokuwa mikononi.
“Emmy!” Akaita akisajili tabasamu hafifu. “Unanjaa eeeh?” Alimuuliza, “na kijana wa namna hiyo utampata wapi?”
“Wapo…” Emmy alizungumza akiyazungusha macho yake kwa maringo.
“As long as kwa sasa mapenzi ni upuuzi kwangu…hata aje nani, sitaweza kumkubalia mpaka pale nitakapokuwa tayari…baada ya kumaliza masomo na kupata kazi!”
Emmy aliguna.
“Haya…nitakuona!” Akamwambia akiweka nguo ile aliyokuwa ameishika kabatini.
“Utajijua mwenyewe!”
Modester alisema akimpuuzia kwa kuchukua simu yake na kubofya.
Baada ya nusu saa toka wafanye mazungumzo hayo, ndipo walipokaa mezani kwa ajili ya chakula cha usiku. Walikuwepo wawili hao, mzee Laulian, mkewe na mfanyakazi wa ndani waliyezoea kumuita kwa jina la Dada!
Wakiendelea kula huku wakifanya mazungumzo, Emiliana aliropoka;
“Pasaka ya mwaka huu mbaya kweli…!”
Watu wale waliokaa pamoja naye wakamtazama.
“Ubaya wake?” Mama yake alimuuliza.
“Hakuna ahadi yoyote ya kutolewa out…kutoka kwa baba,” alisema kwa sauti ya chini kwa mtindo wa utani.
Wote mezani pale wakacheka wakimtazama mzee Laulian.
Mzee Laulian alitafuna chakula kilichokuwa mdomoni na kumeza, kisha akajitetea;
“Si’ kwa sababu kaka yenu ndiye atawatoa!”
“Mh!” Emilliana aliguna. “Kaka mwenyewe huyo, tangu awe mwanajeshi anaonekana mwaka hadi mwaka…tutamuonea wapi sie?”
“Kesho anakuja…” Mama yake alimpasha.
“Kaka Jackson kesho anakuja?” Modester alijikuta akivutika kwenye mazungumzo yale na kuuliza.
“Ndio…alisema atakuja kula sikukuu nasi, na atawatoa out!”
“Eeeh! Bora…nilikuwa nimemkumbuka kweli,” Modester alisema.
“Kwa hiyo kutakuwa na out, usijali juu ya hilo Emmy…” Mzee Laulian alizungumza kwa kusisistiza akimtaza binti yake yule machepele.
“Sasa hapo Pasaka itanoga…eeeh?” mama yake naye alimuuliza.
Mezani pale wote walimtazama, Emiliana akainamisha kichwa chini akitabasamu.
Wote wakacheka!

“KAKA Jackson ameamua kutufanyia surprise…maana sio kawaida yake kupanga kuja bila kutujulisha.” Emiliana alimwambia Modester walipoingia chumbani kwao baada ya chakula.
“Si’kajua kesho sikukuu ni lazima tu atatukuta nyumbani!”
“Ahaaa! Na kweli!”
Kilijengeka kimya kifupi. Kisha Emiliana akakivunja kimya hicho.
“Kuhusu kesho sijui itakuwaje…?” Alisema akionyesha hali ya kuchanganyikiwa.
“Kuhusu nini?” Modester alimuuliza.
“Sidhani kama nitatoka na kaka Jack…”
Modester alimakinika naye.
“Kwa nini hudhani…wewe sindiye uliyekuwa unazungumzia habari za out, pale mezani?!”
“Nilikuwa nafurahisha genge…baada ya kuona baba hana mpango wa kututoa…lakini nina mtoko na Chris!” Alisema akimtaja mpenzi wake aitwae Christopher ambaye Modester alimfahamu.
Modester aliguna.
“Sasa utafanyaje ili kaka Jack akuelewe. Kuja kwake ni kwa ajili yetu. Halafu wewe umwambie kwamba hutoki…atakuelewa kweli?”
“Mh!... Sijui nifanyeje! Na kumkacha Chris siwezi…hili amenisisitiza kweli yaani, nami nilimpa uhakika kuwa nitakuwa naye…”
“Aaah!…utajua mwenyewe utakavyo handle!”
Modester alionyesha kumpuuzia.
“Ona…” Emiliana akamvuta usikivu tena. “Tutatoka wote kama kawaida, halafu tukiwa njiani nitamuomba kaka Jackson kwa kumdanganya kuwa kuna rafiki yangu anashughuli muhimu na alinisisitiza niwepo…wewe utoke naye…halafu nitajitahidi kabla nyie hamjarudi nyumbani tuonane na kurudi wote!”
Modester alipandisha mabega na kuyashusha.
“Utaongea naye!” Alimwambia mwenzie yule.

***
SIKU hiyo ya Pasaka ilikuwa ni yenye heka heka sana. Modester na mama Emiliana, ndio waliokwenda kanisani, Emiliana alipoamka alidai hajisikii vizuri, na akataka abaki nyumbani, kukichangamka amsaidie dada wa kazi nyumbani pale kuandaa chakula.
Majira ya saa sita za mchana ndipo kina Modester walipotoka kanisani. Wakaungana na Emiliana na dada wa kazi jikoni kuandaa chakula.
Hadi saa nane wakati Jackson anafika chakula kilikuwa kipo tayari, familia ile kwa pamoja na jamaa kadhaa ambao walikuwa wamealikwa kujumuika kwenye sikukuu hiyo inayosherehekewa na baadhi ya Wakristo, kila mwaka baada ya mfungo wa Kwarezima walikaa mezani pamoja kwa ajili ya chakula.
Wakiwa mezani hapo, wakiendelea kupata chakula waliendelea pia na mazungumzo mbalimbali.
“Ila kaka Jack na we’ uoe sasa!” Mama wa kuropoka Emiliana, aliropoka.
Watu mezani pale walicheka wengine wakitabasamu.
“Emmy…wewe hunaga staha?!” Mosdester alimuuliza mwenzie kwa kumshangaa.
“No… sisi ni dada zake inabidi tumwambia, sikukuu kama hizi, hatupaswi kuhangaika majikoni peke yetu, inabidi tuwe na wifi anayekuja tunakomaa naye…”
Watu waliendelea kutabasamu, Modester naye alitikisa kichwa huku anatabasamu.
“Nitaoa tu mdogo wangu…very soon!” Jackson alisema.
“Ila hakikisha wifi yetu awe mzuri kuliko sisi!”
“Jamani!” Modester aling’aka kwa mshangao kutokana na kauli ile ya Emiliana.
“Ndio,” Emiliana alidakia kwa msisitizo. “Akituletea kibwengu bwengu tunakitimulia mbali!”
Wakazidi kucheka.
Na mazungumzo yakaendelea yaliyotawaliwa na utani mwingi.
Baada ya chakula na kupumzika sebureni, mida ya saa kumi Jackson aliwaambia Emiliana na Modester wajiandae ili awatoe out!
Wawili hao walielekea chumbani kwao mbio mbio kwa furaha.
Wakaoga na kujiandaa.
Walivaa mavazi yao mahususii waliyoyatenga kwa ajili ya mitoko ya mara moja moja. Kama huo!
Modester aliyekuwa mrefu wa wastani, alipigilia gauni la kitenge cha Makenzi, alilolishona kwa mtindo wa nguva ya chini. Mtindo huo wa ushonaji ulilifanya gauni hilo liushika vyema mwili wake uliojazia na kutengeneza muinuko mahususii chini ya mgongo wake. Liliishia maeneo ya mapajani, likaacha sehemu kubwa ya miguu yake iliyoshiba, wazi. Rangi ya gauni hilo ilimkaa vyema kutokana na rangi yake ya mwili na ilishabihiana na rangi ya pochi ndogo aliyoishika mkoni. Kichwani hakuwa amesuka, alikuwa na nywele fupi, alizozilisha vyema mafuta yaliyozipendezesha.
Modester alivutia.
Miwani ya jua aliyoitupia machoni ilimpendezesha zaidi. Ikamfanya aonekana mfano wa staa wa filamu. Viatu vya chini alivyoweka miguuni navyo vikampa chati, akaonekana mwanamke asiye na mambo mengi, lakini mzuri halafu simple!
Kwa upande wa machepele Emiliana, naye alivaa gauni la kitenge, lakini cha Java, alichokishonesha kwa mtindo wa mwanamke nyonga. Lilimkaa vyema kutokana na umbo lake jembamba. Kichwani, alikuwa amesuka nywele zake kwa mtindo wa serfe, alibeba mkoba wa rangi nyeusi, na miguuni alivaa viatu vyeusi vya mchuchumio.
Wote kwa pamoja walijipulizia manukato, ila yenye harufu zinazotofautiana.
Wakatoka chumbani Na kuelekea sebureni, alikokuwa amekaa Jackson peke yake.
Jackson kuwaona, alipigwa na butwaa.
Hasa akimakinika na Modester.
Alivutia mno.
Moyo wake ukamdunda.
Ukamjuza pia msichana huyo alikuwa ni mzuri aliyejaaliwa umbo na sura. Lakini upande mmoja wa nafsi yake ukamhoji; mbona uzuri huo alikuwa hajawahi kuuona kwa namna ya kipekee kama siku hiyo?
Upande mwengine wa nafsi hiyo ukajibu; pengine ni kwa sababu nina muda sijamtia machoni…lakini ni mzuri!
“Mmependeza sana…” Hatimaye alijikuta akizungumza akishindwa kulificha hilo moyoni.
Wasichana wale walitabasamu.
“Asante,” Modester alijibu.
“Sasa kwa kupendeza huku…usije ukatwambia unatupeleka Coco Beach, sisi siyo watoto!” Emiliana asiyekaukiwa kauli za masishara alimwambia kaka yake yule.
Jackson alibasamu.
“Yani huyu…!” Modester alisema akitikisa kichwa!
“Ghafla nimepata shida ya kujiuliza wapi niwapeleke…” Jackson naye alisema kwa masihara.
“Kwani mwanzo ulipanga utupeleke wapi?” Modester alimuuliza.
“Nilipanga tupitie Mlimani City, tununue Ice Cream, kisha twende Slipway!”
“Unaona sasa…!” Emiliana alisema kwa masihara.
“Unaona nini…mbona haina shida!” Modester alisema kwa uhakika.
“Twendeni bwana, nilikuwa natania.”
Jackson alisimama.
“Na mama yupo wapi?” Emiliana alimuuliza kakaye.
“Atakuwa huko uani na Dada.”
“Ngoja nikamuage.”
“Niagie na mimi Emmy!” Modester alimwambia.
“Twende tu akuone ulivyopendeza.”
“We’naye…” Modester alizungumza akicheka. Kisha akamfuata Emiliana nyuma. Wakaenda kumuaga mwanamke huyo na kisha wakaelekea kwenye safari hiyo ya mtoka wa jioni.
Ni katika mtoko huo ndipo vita kali ilipoanzia baina ya Modester na Jackson. Ni vita iliyoihusisha baadaye familia ya mzee Laulian, iliyomlea Modester tangu akiwa na umri wa miaka kumi na moja.
Ikasababisha maafa makubwa sana yaliyodumu kwenye maisha ya wahusika hao na familia zao!
Ukaribu uliojengwa katika kipindi chote hicho, ukafa!

ITAENDELEA
 
OMBAOMBA ALIYEUZA WANAE- 4

WALIPOTOKA nyumbani kwao maeneo ya Aroma, Tabata na kuishika barabara ya Mandela, walielekea mpaka Ubungo. Wakazivuka taa za barabarani za maeneo hayo na kuishika barabara ya Sam Nujoma na baada ya mwendo wa dakika takribani saba, wakaingia kwenye majengo ya biashara ya Mliman City, walimo nunua ice cream!
Walipotoka ndani ya majengo hayo, wakiwa maeneo ya maegesho ndipo Emiliana alipomwambia kaka yake kwamba alikuwa na safari nyingine.
Jackson alibaki akimshangaa.
“…kaka tafadhali naomba uniruhusu…ni siku muhimu sana kwa rafiki yangu huyu anayenihitaji niwepo, pleeease…nakuomba…” Emiliana aliongea kwa kubembeleza akivikusanya viganja vya mikono yake pamoja na kuviinua juu.
Jackson alishusha pumzi fupi.
“Anyways…” alimwambia kama aliyekubali yaishe. “Ukichelewa kurudi nyumbani, utajua utawajibu nini wazazi wako.”
“Tutarudi wote…” Emiliana aliongea haraka na kwa msisitizo. “Nyie mkiwa mnatoka huko Msasani nijulisheni kwenye simu, nitawasubiri hapa hapa!”
“Haya poa…”
Waliagana huku Emiliana akimkonyeza Modester.
Modester alitupia tabasamu la mbali wakati akiingia ndani ya gari lile, Mark X, la Jackson, kwenye siti ya mbele iliyokaliwa mwanzoni na Emiliana.
Wakaondoka katika eneo hilo na Emiliana alishika hamsini zake.

WAKIWA ndani ya gari, Jackson na Modester waliisherehesha safari yao kwa mazungumzo yaliyohusu mambo tofauti tofauti. Jackson alianza kumuuliza Modester mambo yaliyohusiana na masomo, baadaye Modester naye akamuuliza juu ya maisha ya wanajeshi yalivyo!
Walipo hama kwenye mazungumzo hayo, Jackson alimuuliza Modester kama alikuwa na mpango wa siku moja kwenda kumtembelea bibi yake Dodoma.
“Ndio…huo mpango ninao!” Modester alimjibu. “Lakini sio sasa.”
“Kwa nini isiwe sasa?”
“Aaah...! Wakati huu hata nikienda sina cha kumsaidia…angalau nikimaliza masomo na kupata kazi…hapo naweza kwenda, nitakuwa na chochote. Siunajua mkono mtupu haulambwi!”
Jackson aliishia kutabasamu.
Akajibu kwa ufupi; “Ila ni kweli!”

WALIFIKA Msasani baada ya dakika arobaini na tano hivi toka watoke Mlimani City. Baada ya Jackson kuliegesha gari lake eneo la maegesho ya hoteli inayopendwa na watalii ya Slipway, alishuka pamoja na Modester wakawa wanatembea taratibu.
Wakapitia kwenye eneo ambapo ziliuzwa picha za michoro mbalimbali ya asili, zenye kuvutia, wakashangaa kidogo hapo, halafu wakaelekea kwenye eneo jingine ambalo lilikuwa na maduka yanayouza vitu mbalimbali vya kiasili.
Zikiwemo nguo, bangili, cheni, mikebe ya kuhifadhia ufunguo, mikoba, mabegi, viatu na vingine vingi. Wakiwa hapo Modester alipenda hereni fulani hivi ambazo zilining’inizwa kisanamu kidogo cha mwanamke aliyevaa mavazi ya kimasai, ambaye amebeba mtoto mikononi.
Jackson alimnunulia.
Baada ya hapo walielekea eneo la mbele, kwenye view ya bahari ambapo kulikuwa na siti za kukaa zikielekezwa baharini, huku kwenye eneo lingine la jirani na hapo kukiwa na sehemu maalumu iliyoandaliwa kwa ajili ya bar!
Katika wakati huo wote, jambo moja ambalo lilimfurahisha Jackson ni namna watu walivyokuwa wakiwatolea macho. Ilikuwa ni tofauti kabisa na watu wengine alio waona wakifika hotelini hapo wakiwa wawili katika jinsi tofauti kama vile yeye na Modester walivyokuwa.
Wao walionekana kuwa kivutio na ni wazi watu wengi walifahamu Modester ni mpenzi wa Jackson, na kwa uzuri wa msichana huyo na namna alivyopendeza, Jackosn akajua moja kwa moja alizoa medali nyingi mioyoni mwa watu wale, za kumiliki msichana bomba!
Ni mawazo hayo yaliyozaa kitu kipya.
Kumuhitaji Modester kuwa naye kwenye uhusiano wa mapenzi, ikiwezekana siku moja amuoe. Suala hilo ingawa hakuwahi kuliwaza kabisa huko nyuma, kutokana na kumchukulia Modester kama dada yake, lakini siku hiyo lilimuingia moyoni asilani.
Walisogea na kwenda kusimama kwenye ukingo wa hoteli hiyo, ulio itengenisha na bahari kwa msingi wa zege zito uliochomekwa miti mikavu juu yake, iliyopangwa kwa namna ya kumzuia mtu asipitilize na kudondokea upande ule wa baharini.
Wakawa wanatazama baharini.
“Bahari ni kitu cha kipekee sana,” Modester alimwambia Jackson kwa utulivu.
“Kwa nini?” Jackson alimuuliza.
“Tazama inavyovutia.”
Jackson akamakinika baharini huko akitazama yaliyoendeleako.
Baada ya kama dakika moja, akamgeukia Modester;
“Utapenda kutalii baharini?” Alimuuliza.
“Unamaanisha nini?” Modester alimjibu kwa swali. “Kuogelea?” Aliongeza swali jingine.
Jackson akajenga tabasamu lisilo hafifu wala pana . “Hapana.” Akamwambia. “Namaanisha…”akaongeza tena kwa pozi. “Tukodi boti ituzungushe kidogo.”
“Waoh!” Modester alilipuka kwa furaha, “sawa!” Akasema kwa bashasha zenye mapozi ya kike.
Hilo ndilo likafanyika.
Wakaelekea kwenye kibanda zinapouzwa tripu za majini, baada ya dakika kumi wakawa ndani ya boti wanazungushwa wakiwa wamelipia muda wa nusu saa.
Wakiwa wameliacha kwa mbali eneo la hoteli ile, Modester alisimama na kunyoosha mikono, akatengeneza umbo kama la msalaba kisha akafumba macho yake. Upepo wa baridi uliovuma baharini humo ukawa unampuliza.
“Kusema na ukweli ninahisi raha isiyo na kifani…” alisema akiwa amefunga macho.
“Kweli!” Jackson alimuuliza.
“Hakika.” Modester alijibu. “Ni kama nipo kwenye Titanic, God!” alimalizia kulitaja neno lile kwa mbwembwe zenye msisitizo.
Na hapo wimbi likapiga, boti ile ikayumba kidogo.
“Aaah!” Modester aliachia ukulele wakati anashuka bila kutegemea.
Jackson alimdaka kiuno, akamuweka taratibu mpaka kwenye siti.
Kitendo hicho cha kumdaka Modester kiuno kilimsisimua sana Jackson. Kwa namna alivyomshika aliyahisi vyema maungo ya msichana yule yalivyo laini. Akili yake ikachanganyikiwa vibaya mno.
“Ona…” Modester alimtoa kwenye mawazo hayo aliyokuwa anawaza akimuonyesha view, ya mji wa Dar es Salaam ilivyokuwa inaonekana kutokea eneo lile walipokuwa.
Ulikuwa unapendeza sana.
Waliendelea kutalii wakiufaidi pia muonekano wa maandhari yenye kuvutia ya Kisiwa cha Bongoyo kilichopo jirani na Hotel ya Slipway na baada ya muda waliolipia kumalizika walirudi hotelini pale na kukaa eneo tulivu, wakaagiza vinywaji.
Wote waliagiza kinywaji kilichofanana, juisi ya embe!
“Asante sana kaka Jackson…” Modester alimwambia Jackson.
“Asante ya nini tena?”
“Nimefurahia mno tripu ya baharini.”
“Aaah!..ni kuhusu hilo?”
“Ndio, katika maisha yangu yote nilikuwa sijawahi kupanda chombo chochote cha majini, kwa hiyo leo ni siku yangu ya kipekee sana!”
“Haya mama hongera.”
Kimya kidogo kilijengeneka.
Jackson akameza mate ya baridi yaliyomjaa kutokana na kile alichotaka kukizungumza. Akainua uso na kumtazama Modester aliyekuwa amekaa mbele yake.
“Mo’,” alimuita akilifupisha jina lake.
Modester aliinua macho kutoka kwenye juisi yake aliyokuwa anaikoroga kwa kutumia mrija na kumtazama.
“Nambie…”
“Kuna kitu kinanichanganya sana!”
“Kitu gani?”
Jackson alisitia kidogo.
“Juu ya kuoa.” Alisema kwa unyonge.
“Mh!” Modester akaguna. “Ni kwa sababu Emiliana amekwambia wakati ule tunakula?” Akamuuliza.
“Hapana ni kwa sababu wakati wangu umefika.”
“Na ndio uoe sasa!” Akamwambia kwa msisitizo wa masihara.
Jackson aliguna kwa namna ya kujuta au kukata tamaa.
“Wa kumuoa je?” akauliza kibwege.
“Huna?” Modester alimuuliza bila kuweka usiriasi kwenye uongeaji wake.
“Nahisi hivyo.”
“Muombe Mungu…mke mwema hutoka kwa Mungu!”
Jackson alipiga kimya kifupi. Ni kimya hicho ambacho Modester alikitumia kuiinua glasi ya juisi mezani pale, na kuinywa kwa kuinyonya kupitia kwenye mrija.
“Kama ni Mungu nimekwisha muomba sana…” Jackson alisema wakati Modester anarudisha glasi ile mezani.
“Na hajakujibu tu?”
“Nahisi amekwisha nijibu.”
“Kwamba…? I mean, amekuonyesha huyo mke?”
“Ndio.”
“Sasa kaka’ngu…mara huna…mara amekwisha kuonyesha…mbona sikuelewi…
hebu tuletee siye wifi!”
Neno lile ‘kaka’angu’ lilimkata maini Jackson.
Ikambidi tu ajikaze kisabuni.
Akajilipua;
“Na je,…nikikwambia mke niliye onyeshwa ni wewe?!” Kisha akamtupia Modester macho yenye msisitizo kwa kauli ile.
Modester akabaki ametulia akiyaacha maneno yale yasambaye akilini mwake.
“You can’t be Sereous?!” Modester akasema kwa kimombo.
“No...”
“Stop kidding bhana!” Modester alimkatisha Jackson kwa sauti yenye mkalipio wa chini.
Jackson akatulia akimtazama msichana yule machoni kwa macho yenye hisia za wazi za kumhitaji.
“I am not kidding Mo’…nipo siriasi!” Alisema kwa utulivu.
“Jackson…!!” Modester alijikuta akimuita kwa mkazo Jackson, kwa jina lake kavu kavu bila kutanguliza neno ‘kaka’ jambo ambalo hakuwahi kulifanya kabisa huko kabla!
Jackson alielewa wazi amemvuruga msichana huyo!
“Wewe ni sawa na kaka yangu…na sasa unaleta habari gani tena?” Alimuuliza kwa kishindo cha kukereka.
“Ni kweli imekaa hivyo,” Jackson alizungumza taratibu lakini kwa mkito wa kujiamini na kumaanisha kile alichokuwa anakisema, “lakini huo si ukweli halisi. Sisi ni watu ambao tumekuwa tu pamoja ila hatuna vinasaba vya undugu!”
Akili ya Modester ilihisi kuvurugika vibaya mno.
Mwanzoni alifikiri kijana yule alikuwa anatania, lakini akagundua alikuwa anamaanisha kile ambacho alikizungumzia.
Akabaki kimya akiuzungusha mrija kwenye glasi ya juisi.
“Suala hili haliwezekani Jackson…!” Modester alizungumza bila haraka.
“Usilipe daraja la kutowezekana…jipe nafasi ya kulifikiria.”
Modester alizungusha kichwa kukataa.
“Siwezi hata kulifikiria,” alisema tena pole pole lakini kwa mkazo.
Jackson akabaki kimya akimtazama.
“Please, take me home…!” Modester alimwambia kwa unyonge akimaanisha Jackson amrudishe nyumbani.
Jackson alitanua macho kwa mshangao.
“Nakuomba tuondoke…” Modester alimsisitiza.
“Nimekuudhi?” Jackson alimuuliza.
“Hapana…nimetosha tu kuwa mahali hapa. Asante kwa ofa zako zote!” Alisema na kusimama.
Jackson hakuwa na ujanja, alikwapua mkebe alioutumia kuhifadhia ufunguo zake muhimu mezani pale, kisha akasimama na kuongoza njia kuelekea kule alikoliegesha gari lake.
 
OMBAOMBA ALIYEUZA WANAE- 5


“Please, take me home…!” Modester alimwambia kwa unyonge akimaanisha Jackson amrudishe nyumbani.
Jackson alitanua macho kwa mshangao.
“Nakuomba tuondoke…” Modester alimsisitiza.
“Nimekuudhi?” Jackson alimuuliza.
“Hapana…nimetosha tu kuwa mahali hapa. Asante kwa ofa zako zote!” Alisema na kusimama.
Jackson hakuwa na ujanja, alikwapua mkebe alioutumia kuhifadhia ufunguo zake muhimu mezani pale, kisha akasimama na kuongoza njia kuelekea kule alikoliegesha gari lake.
Wakaingia garini.
Modester alikaa siti ya nyuma.
Jackson akaliondoa gari. Safari ikatawaliwa na ukimya mkuu. Kila Jackson alipojaribu kuanzisha mada fulani, Modester aliijibu kwa mkato. Akikaa kimya naye Modester aliuchuna zaidi. Mpaka wanafika Mlimani City, kumpitia Emiliana ambaye walikuwa wamekwisha wasiliana naye, hakuna cha maana walicho kuwa wameongea.
Baada ya Emiliana kupanda garini alishangazwa na hali aliyoikuta. Modester alikuwa amekaa kwenye siti za nyuma tena kwa unyonge sana, jambo ambalo hakulitegemea. Wapo wawili garini anakaaje nyuma?
Aliwaza kwa kujiuliliza.
Ikabidi aulize kulikoni kuuondoa mkanganyiko ule wa mawazo aliokuwa nao!
“Vipi…?” Emiliana alimuuliza Modester wakiendelea na safari.
“Safi tu!” Modester alijibu.
“Mbona nimekukuta umekaa nyuma na kinyonge?”
“Nimejisikia tu!”
Emiliana alipepesa macho akiwatazama Modester na Jackson kwa zamu, akijaribu kuangalia kama kuna jambo angelibaini, akamuona kaka yake anatabasamu.
“Kuna tatizo bro?”alimuuliza.
“Tatizo lipi?” Jackson naye alimuuliza haraka. “Hebu acha maswali maswali bhana…kila kitu kipo sawa!”
Kaka yake aliongea kwa mkalipio wa kumtoa kwenye jambo hilo alilokuwa analichimba. Emiliana akaamua kulipuuzia jambo lile, safari ya kurudi nyumbani kwao ikaendelea.

***
SUALA la Jackson kumtaka kimapenzi lilimpa wakati mgumu mno Modester. Mwanzoni aliapa kutolipa uzito wa kulifikiria, lakini siku hadi siku alijikuta akigundua jambo hilo linamtafuna.
Lilimtafuna kwa sababu lilimuweka kwenye mkanganyiko mkubwa wa mawazo. Alikuwa akiwaza nisipomkubalia ikiwa hivi…maisha yangu yatakuwaje? Na nikimkubalia ikawa vile…nitakuwa mgeni wa nani?!
Ukweli ni kwamba, alijikuta kwenye wakati mgumu sana!
Hata hivyo, mbali na sababu zote ambazo Modester alikuwa nazo za kumkataa Jackson, ikiwemo ya kufadhiliwa na familia ya kijana huyo toka akiwa na umri wa miaka kumi na moja, akilelewa kama mmoja wa watoto wa nyumbani pale, hakuwa anampenda kabisa kijana huyo.
Hilo ndilo zaidi lilisababisha asihitaji kuwa naye!
Lakini kwa uzoefu wake na wanaume waliowahi kumtaka kimapenzi, Modester alifahamu kwamba Jackson angeendelea kumsumbua tu, akilenga nia yake ikubaliwe. Asingekubali kuachana naye kirahisi.
Kwa hiyo alijihadhari kuwa, kwa kuwa hamtaki ni lazima ajipange kukabiliana naye. Lakini swali likawa;atakabiliana naye vipi?
Akapata wazo la kumweleza suala lile Emiliana.
Kwa mantiki kwamba msichana yule ni roporopo, na kwa kumweleza kwake akimsisitiza kuwa alimhesabu Jackson kuwa ni kaka yake na hakuhitaji kuuvunja ‘undugu’ huo kwa uhusiano wa mapenzi, pengine Emiliana angelivalia njuga kwa kumtaka kaka yake asiendelee kumsumbua.
Lakini akiwaza hivyo, alipata hadhari nyingine. Akawaza; vipi kama Emiliana akiamua kulishadadia jambo hilo kwa kusimama upande wa kaka yake?
Na hapo ndipo alipoanza kuiona dosari ambayo ingetokea kwenye uhusiano baina yake na msichana huyo.
Alifahamu kama Emiliana angemsihi akubali kuwa na kaka yake, naye kukataa ingefika hatua wangekwazana, jambo ambalo hakuhitaji litokee.
Mawazo yalimpeleka Modester mpaka kufikiria kuwaeleza wazazi wa Jackson. Lakini hata uamuzi huo alioufukiria aliuona una pande mbili ambazo zote zina uzito wake!
Upande wa kwanza ndio huo aliokuwa anautamani yeye. Kwamba uhusiano wake na familia hiyo ubakie kuwa wa ‘binti na wazaziwe’ na Jackson akanywe juu ya ombi lake lile.
Lakini upande wa pili ndio uliomuogofya zaidi. Ndio ule aliouwazia pia kwa Emiliana, kwamba vipi ikiwa wazazi hao watasimama upande wa kijana wao!
Kwa yote waliyomfanyia, Modester alijiuliza angekuwa na msuli wa kuwakatalia juu ya hilo?
Hakika aliona ni jambo lisilo wezekana. Kwa mtu yeyote mwenye moyo wa shukurani, asingethubutu kukataa juu ya hilo ukizingatia naye katendewa mengi.
Sasa kama angemkubalia, angewezaje kuishi na mtu asiye mpenda?
Kuna wakati Modester aliwaza kuwa, pengine ingekuwa Jackson anahitaji uhusiano wa mapenzi wa kawaida, angethubutu kulifikiria hilo, kwa matumaini kuwa baadaye angeachana naye na kufunga ndoa na mtu ambaye anampenda.
Lakini Jackson alihitaji ndoa, na wao walikuwa ni Wakristo, na ndoa kwao ilimaanisha kuishi pamoja kwa namna yoyote ile katika kipindi cha maisha yao yote!
Hapo ndipo alipochoka zaidi.
Modester akaliona giza nene likitanda mbele kwenye maisha yake ambayo yalikuwa yamekwisha pata nuru.
Hata hivyo msichana huyo hakuchoka kuendelea kuusugua ubongo wake. Bado akili yake ilimwambia kuna jambo alipaswa kufanya ili kujiepusha na Jackson bila kuuharibu uhusiano baina yake na familia ile.
Baada ya kuwaza sana, alipata uamuzi wa nini afanye.
Akauona uamuzi ule upo sahihi.
Kumbe alijidanganya.
Mambo akazidi kuyakoroga!

ITAENDELEA....
 
SEHEMU YA 6

JACKSON alikuwa kwenye wakati mgumu kutokana na penzi la Modester. Hali aliyokuwa nayo haikuwahi kabisa kumtokea huko nyuma, ni kama kirusi kilikuwa kimeingia kwenye maisha yake na kuitafuna furaha aliyokuwa nayo. Ni katika kipindi hicho Jackson alipojifunza kuwa, mapenzi yanatesa!
Kwa nini Modester hataki kuwa na mimi?
Alijiuliza kila mara.
Ukiachana na siku ambayo aliiwasilisha nia yake kwa Modester ya kuwa naye, wakiwa Msasani jioni ile ya Pasaka, Jackson alikwisha kutana takribani mara tano na msichana huyo, kwenye mikutano ya kumsishi amkubalie, lakini bado alitolewa nje!
Mpaka hapo, ilimtosha kumfahamisha kuwa mwendo alikuwa akienda nao usingemsaidia kumpata msichana huyo. Akili yake ikamwambia analazimika kubadili mbinu. Baada ya kuwaza hilo, ndipo mawazo ya kumueleza suala hilo Emiliana alipo yapata.
Jackson aliona Emiliana ni mtu sahihi wa kumsaidia katika hilo. Kwamba kama angemweleza nia yake na Emiliana kuzungumza na Modester, pengine msichana huyo angelegea na kumkubalia.
Aliupitisha uamuzi huo.

***

KWA upande wa Modester, wazo alilolipata la kumuepusha na Jackson, lilikuwa ni kujiingiza kwenye uhusiano na mtu mwingine, halafu kumtambulisha mtu huyo kwenye familia ile kuwa ni mchumba wake.
Modester aliamini hiyo ndio ingekuwa kinga njema. Ambapo, pale Jackson angefikia uamuzi wa kuieleza familia yake juu ya kumpenda na kuhitaji kumuoa, angekutana na kizingiti hicho, kwamba mwenzie amekwisha tambulisha mchumba wake kwenye familia.
Hapo aliona Jackson asingekuwa na la kufanya.
Angekuwa amemuweza!
Kwa hiyo, alichoamua kukifanya Modester, ilikuwa ni kujiingiza kwenye uhusiano na kijana mmoja aitwaye Daud Moyo, ambaye alikuwa amekwisha mfuatilia kwa muda mrefu. Alimkubalia kijana huyo, kwa sababu pia alikuwa anamvutia, mwanzoni hakuhitaji kuwa naye kutokana na malengo yake ya kujihusisha kwenye uhusiano baada ya kumaliza chuo na kupata kazi!
Baada ya kujiingiza kwenye uhusiano na Daud, Modester hakutaka kuchelewa kumpasha habari hiyo Emiliana, na aliifanya kazi hiyo siku moja usiku wakiwa chumbani kwao kitandani, baada ya chakula cha jioni.
“Emmy…” Modester aliita wakati mwenzie huyo akiwa busy, anachati kupitia simu yake.
Kitandani hapo, Emiliana alikuwa amelala chali, miguu yake akiwa ameiegemeza ukutani huku Modester akiwa amelala kifudifudi, akiwa amejiinua kwa namna iliyosaidiwa na mikono yake, na mkononi alikuwa ameshika simu pamoja na diary yake.
“Nambie…” Emiliana aliitikia bila kutoa umakini wake kwenye kile alichokuwa anakifanya.
“Angalia huku sasa…” Modester alimwambia.
“Nini bwana…!!!” Emiliana aliongea kwa kukereka kuondolewa kwenye kile alichokuwa anakifanya, lakini alizungusha shingo na kutazama upande ule aliokuwepo Modester.
Alikuwa anaonyeshwa picha.
“Ndiye nani?” Aliuliza akiitazama kwa makini picha ile.
“Shika…umuangalie vizuri.”
Emiliana alishika picha hiyo na kuitazama vizuri, lakini kumbukumbu zake hazikumweleza kama alikuwa akifahamiana na ile sura.
“Ni handsome,” Emiliana alisema akiirudisha. “Mkaka wa wapi huyu?” Aliuliza.
Modester akatabasamu.
“Inamaana humjui?” Alimuuliza.
“Kama ningekuwa namjua ningekuuliza?” Emiliana naye alirusha swali.
“We’ nawe…huyu si Daud, humkumbuki tuliwahi kuonana naye kwenye lile duka la simu maeneo ya Mliman City, pale karibu na car wash!”
“Tulipokwenda kununua betri ya simu yako?”
“Ndio…”
“Hebu…”
Emiliana aliongea akinyoosha mkono kuichukua tena ile picha aliyokuwa ameshika Modester, akaishika na kuitazama vyema.
“Ni bonge la mkaka,” alimmwagia sifa. “Na mmeshapeana hadi picha?!” alihoji kwa mshangao.
“Kuna tatizo?”
“Mh!”
“Mbona unaguna?”
“Ndiye umenasa hapo nini?”
Modester akacheka.
Emiliana alimtupia macho na kusoma jambo, akakurupuka kitandani kwa kiherehere na kukaa kwa mtindo wa kukunja magoti na kuikalia miguu yake.
“Usiniambie…” alisema kwa bashasha. “Unatoka na huyu mkaka?” Aliuliza kwa namna ile ile aliyosema nayo.
“Nimeamua nikuridhishe mwaya…maana maswali ya kila siku, ya bado hujakutana na mkaka, yalikuwa yamekwisha nichosha!”
“Heee!” Emiliana alisema kwa mshangao wa bashasha. “Mkh!” Akaguna. “Eti uniridhishe…nyooo!…Sema umenasa tu…na ile nadharia ya mapenzi ni upuuzi uliyokuwa nayo, kwa huyo ndio Kigoma mwisho wa reli…”
Wakacheka!
Hivyo ndivyo Emiliana alivyotambulishwa kwa Daud. Na ndani ya wiki hiyo hiyo Modester alifanya mpango akawakutanisha wawili hao. Mkutano ambao ulifanyikia Samaki Samaki, Mlimani City!
“Ni mkarimu kweli huyo mkaka,” Emiliana alimwambia Modester walipoachana na Daud.
“Ananifaa eeh?”
“Sana tena…halafu mnaendana ile mbaya!”
Modester alitabasamu kwa furaha.
“Nashukuru Emmy…” Akasema. “Kwa ninavyo mpenda, ninamuomba Mungu tusiishie njiani!” Aliongeza.
“Nami nawaombea muwe na mwisho mzuri!” Emmy alimwambia kwa upendo.

***

HUKU Modester akijiona amefanikiwa katika hatua yake ya kwanza ya kujiepusha na Jackson, baada ya kumtambulisha mpenzi wake Daud kwa Emiliana, Jackson alikuwa kwenye mpango wake wa kuzungumza na Emiliana juu ya nia yake ya kumuoa Modester na kumuomba mdogo wake huyo amsaidie kuzungumza na Modester.
Tena Jackson hakutaka jambo hilo lichukue muda mrefu kukamilika.
Katika wikendi moja ambayo alifahamu wasichana hao hawakuwa busy na chuo, Jackson alimpigia simu Emiliana na kumuomba wakutane nje ya nyumbani kwao, lakini akimuhadhari asimuhusishe Modester katika hilo.
Emiliana alishangaa!
Akajiuliza maswali mengi yasiyo na majibu juu ya mkutano huo asiotakiwa kufahamishwa Modester! Alichoamua kufanya ilikuwa ni kumsikiliza kaka yake, kwenda kuonana naye bila kumweleza Modester.
Walikutania maeneo ya Ubungo, kwenye mgahawa mmoja uliopo kwenye majengo yaliyojengwa pembeni ya sheli, iliyopo pembezoni mwa barabara ya Sam Nujoma, kwa uelekeo wa Mwenge na barabara ya Morogoro katika uelekeo ilipo stendi ya mkoa!
Jackson ndiye aliyekuwa wa kwanza kufika. Akaagiza soda baridi na kukaa akimsubiri Emiliana, mdogo wake huyo alifika mahali hapo robo saa baadaye. Walijuliana hali na kufanya mazungumzo ya hapa na pale, ndipo Jackson akaamua kumweleza kile hasa kilichowakutanisha pale.
“Mkh!” Emiliana aliguna baada ya kumsikiliza kaka yake.
“Mbona unaguna?” Jackson alimuuliza.
“Sijui hata niseme nini…kwanza, katika hili baba na mama unaf’kiri wataungana na wewe? Modester ni kama ndugu yetu kwa namna tulivyo lelewa, leo ije ibadilike awe mkeo! Unaona hilo watakubaliana nalo?” Alimuuliza kwa wahka.
“Emmy…niamini mimi, kuhusu baba na mama wala sio shida…kikubwa ni Modester kukubali. Huu undugu wa kulelewa ni undugu wa aina gani? Si bora nikimuoa ndio tutakuwa tumeunganisha undugu wa kweli!” Jackson alizungumza kwa msisitizo.
Emiliana alibaki kimya akimkodolea macho.
“Emiliana nakuomba mdogo wangu…nisaidie kwenye hili,” Jackson mara hii alizungumza kwa kubembeleza. “Kiukweli ninampenda Modester…na nipo tayari kufanya lolote lile ilimradi tu nimuoe!”
Bado Emiliana alikuwa kimya pamoja na kaka yake kumueleza hayo. Msichana huyo alimung’unya midomo na kuinywa soda iliyokuwa mbele yake. Kisha akakwangua sauti kwa namna ya kujiandaa kuzungumza.
Akauliza; “Amekwambia pia kama ana mchumba?”
Jackson alifinya macho kwa mbali. Kisha akazungusha kichwa kukataa.
“Ndio maana na kwambia kaka Jack hili jambo ni gumu kuwezekana…Mo’ anamchumba wake..halafu anampenda kweli huyo mkaka…sidhani kama atakubali kuachana naye!”
Huo ukawa ni mkuki mwingine moyoni kwa Jackson.
Wawili wale wakabaki wanatazamana.
Jackson akajikakamua.
“Ni mwanafunzi pia?” Aliuliza kwa upole.
“Hapana…ni mtu tu mwenye maisha yake.”
“Anafanya kazi wapi?”
“Ni mfanyabiashara…anamiliki maduka ya simu!”
Jackson alipiga kimya kingine.
“Mbona wanawake tena wazuri wapo wengi kaka…mpaka Modester tu…kwa nini usiache huu undugu uliopo uendelee…muhesabu tu kama ni dada yako na uachane naye!” Emiliana alizidi kusisitiza.
“Huwezi kuelewa Emmy kwa ninavyo mpenda…sikia nikwambia…we’ ninakuomba ongea naye tu!”
“Eeeh!” Emiliana alilipuka kwa mshangao.
“Ndio, we’ jaribu kuongea naye na umsikilize atasemaje!”
“Kwa kulazimisha mambo wewe…!!”

ITAENDELEA….
 
SEHEMU YA 7

EMILIANA alirudi nyumbani kwao mida ya saa moja za jioni na alimkuta Modester akiwa amekaa sebuleni akiwa na mama yake, na msaidizi wa kazi za ndani Dada, wakifuatilia mchezo kwenye televisheni.

Baada ya kumsabahi mama yake na wenzake wale, Emiliana alimwambia Modester amfuate chumbani.

Modester alikataa akisisitiza hawezi kuinuka kabla mchezo ule aliokuwa anafuatilia haujaisha.

Emiliana akamsisitiza kuwa anazawadi yake.

Modester akainuka na kumfuata.

Walikwenda mpaka chumbani.

Emiliana akatoa kwenye mkoba mfuko mweusi na kumkabidhi Modester. Msichana huyo akaushika mfuko huo na kumtazama mwenzie.

Kisha akamuuliza;

“Ni nini?”

“Fungua!”

Modester akakaa kitandani na kuufungua.

Akapokelewa na harufu nzuri wakati akiikunjua karatasi maalumu inayo fungwa kwenye chakula cha take away, na baada ya kuikunjua vyema akakutana na chakula akipendacho cha makange ya kuku!

“Waoh!” Modester akalipuka kwa furaha mate yakimjaa mdomoni.

Emiliana akatabasamu kwa namna mwenzie yule alivyo kifurahia chakula hicho.

“Nilikuwa nimeyamisi kweli makange,” alimwambia akiwa bado kwenye tabasamu. “Ni Chris ndiye kaninunulia?” Akauliza.

Emiliana alitingisha kichwa kukataa.

“Nani basi, ni wewe?” Aliuliza.

“We’ siule jamani…mbona maswali mengi!”

“Mh! Lazima kujua maana ofa zingine si kawaida…unaweza kukuta zinaambatana na malipo baadaye!”

“Huna akili kweli wewe…”

Wakacheka.

Modester alibeba chakula kile na kuelekea nacho sebuleni, alikokwenda kukidonoa donoa na wenzake, mama Emiliana na Dada huku wakiusindikiza muda kwa kutazama mchezo waliokuwa wanaufuatilia.

Siku hiyo ikapita.

Siku iliyofuata ilikuwa ni Jumatatu.

Modester na Emiliana walikwenda chuoni siku hiyo. Wakati wanatoka Modester alimwambia Emiliana wapite dukani kwa Daud kumsalimia. Lakini baada ya kauli hiyo ya kumuomba amsindikize, Emiliana aliguna. Modester alimshangaa! Alipomuuliza kulikoni, mwenzie yule akamkatalia kuwa hakuna lolote. Modester alipuuzia. Wakapita kwa Daud na baadaye wakarudi nyumbani.

Wakiwa nyumbani kitandani baada ya kumaliza shughuli zao na kupata chakula cha usiku, wakisogoa stori zao za hapa na pale, kuna jambo Modester alimwambia Emiliana lililomhusu yeye na Daud, msichana yule akaguna.

Modester akashangazwa tena na tendo lile.

“Kwani wewe vipi?” Alimuuliza akimtolea macho yenye mshangao. “Leo, kila nikikwambia kuhusu Daud unaguna! Kuna nini?”

Emiliana aliguna tena. Kisha akakaa kitandani.

“Mo’ hebu kaa ninamaongezi na wewe kidogo!”

Modeser alikaa ili amsikilize, kile kinacho mgunisha gunisha!

“Hata sijui nianzie wapi…!!” Emiliana alisema kwa kubabaika.

Modester akazidi kumtazama kwa macho ya kumsaili.

“Unakumbuka jana wakati natoka nilikwambia nakwenda wapi?” Emiliana alimuuliza Modester.

“Si’ kwa Chris!” Modester alimjibu kwa msisitizo.

“Haikuwa hivyo!”

“Kumbe…?”

“Aliyeniita alikuwa ni kaka Jackson…”

Baada ya kauli ile Modester alishusha pumzi fupi. Akahisi nguvu zikimuishia kwenye maungo yake yote. Akajivuta nyuma kwa makalio akisapotiwa na mikono yake akaegemea ukutani.

Tayari alikwisha elewa nini angeelezwa na Emiliana baada ya hapo.

“Kaka Jack aliniita lakini alinitaka nisikwambie…” Emiliana aliendelea.

Akamtazama Modester aliyekua amejiegemeza ukutani akimtazama kwa macho ya pembeni.

“Akanieleza nia aliyonayo ya kukuoa…na akaomba nizungumze na wewe!” Emiliana alisema kwa sauti iliyokaribiana na ya kulalamika.

Modester alimeza mate ya baridi yaliyojaa mdomoni mwake.

Kisha akaikunja pamoja mikono yake na kuichopeka katikati ya mapaja kwenye miguu aliyokuwa ameinyoosha.

“Sasa…”Emiliana aliendelea. “Sijui…wewe unasemaje?” Alisema kama mtu anayehofia jambo.

Modester aligeuza uso wake mzima na kumtazama Emiliana.

Akamuuliza;

“Na hii ndio sababu ya kuguna kila nilivyokuwa ninakweleza leo kuhusu D?”

“Ndio Mo’…” Emiliana alijibu kwa kusisitiza. “Unaf’kiri ni nini kilikuwa kinaendelea akilini mwangu kwa uliyokuwa unanieleza na kazi niliyopewa na kaka Jackson?” Naye alimuuliza.

Modester akaguna. Akautoa uso wake kwa Emiliana na kutazama mbele yake.

“Siwezi kuwa naye Emmy…” Modester alisema kwa sauti kavu. “Angalieni namna wazazi wenu wametulea. Wametutengenezea mazingira ya sisi kuwa ndugu. Mtu na kaka yake na mwingine na dada yake. Leo nije niwalipe malipo haya…kwa kutoka na mtoto wao…unafikiri watanichukuliaje Emiliana?” Modester aliuliza kwa kulalamika.

Emiliana akapepesa macho.

“Hata mimi nimemwambia!” Kisha alisema. “Lakini amesema kukuoa ni namna ya kuufanya undugu huu uwe na uhalisia zaidi!”

Modester alipiga kimya kifupi.

“Hakuna sababu ambayo anaweza akapewa duniani na kuielewa hata akaamua kuachana na mawazo yake hayo…ninawafahamu vyema wanaume…wakiamua kung’ang’ania lao, hakuna wanae kuwa tayari kumsikiliza…”

Baada ya maneno hayo Modester alimalizia na kuguna kwa tafakari. Akaendelea tena kusema wakati Emiliana akiwa bado kimya.

“Jackson alicholenga tu ni kunitafutia matatizo…lakini pia, Emmy…unafahamu kabisa nipo na Daud…ninampenda na tunamalengo yetu…!”

Kimya kikawatawala watu wale.

Takribani dakika moja ilikatika bila mtu yeyote yule kati yao kuzungumza.

“Niachie hili Emmy nitajua nitadili nalo vipi!” Modester alisema huku akijilaza kitandani hapo.

Msichana huyo alikuwa ameondoka kabisa kwenye hali ya kawaida aliyoshinda nayo siku hiyo. Raha ilipeperuka. Akajikuta ni mwenye mawazo. Alivuta shuka pembeni yake na kujifunika. Emiliana akiwa kimya naye akilala upande mwingine.

Usiku huo ukaendelea...

***

JACKSON alikutana tena na Emiliana kuzungumzia suala lake alilo muagiza. Baada ya kukutana kwao, mdogo wake huyo alimweleza kila kitu juu ya mazungumzo aliyoyafanya na Modester.

“Ila Modester hana shukurani!” Jackson alisema.

“Kwa nini?” aliulizwa.

“Kwa yote ambayo wazazi wetu wamemfanyia, hakupaswa kufanya hivi?”

“Aaah!” Emiliana alihamanika. “Sasa…walimfanyia ili aje awe mkeo?” Akamuuliza kaka yake kwa kushushua.

“Pengine hawakuijua dhamira kama hiyo ingetokea, lakini imetokea…naye anapaswa kufikiria kuwa ni wakati wa kuzilipa fadhira alizofanyiwa.”

Emiliana aliishia kuguna.

“Sasa utafanyaje?” Alimuuliza.

“Nafikiria kuongea na mama!”

“Mama!”

“Ndio.”

“Unaf’kiri kwa kuongea na mama ndio nini…? Kwamba nd’o atakubali?”

“Pengine anaweza kumuonea aibu ama kumuogopa… kwa sababu, yeye ndiye chanzo haswaa cha msaada uliomfikisha alipo leo.”

“Mkh!...haya mambo wewe unataka tu kuyakuza.”

JACKSON hakuwa anatania. Alikuwa amepania. Kama alivyomwambia Emiliana, kweli alitafuta wasaa akakutana na mama yake na kumweleza nia yake ya kumuoa Modester.

“Umezungumza naye?” Mama yake alimuuliza.

“Ndio.”

“Amesemaje?”

Alimsimulia kila kitu.

Mama huyo akabaki anaitafuna ubongoni taarifa ile aliyoelezwa na mwanae. Kisha akamwambia;

“Suala la undugu…sidhani kama lina uzito zaidi…tena ukimuoa ndio kutakuwa kuna uhalisia kwenye undugu huo. Lakini pia ni msichana ambaye amekua tunamuona na tunajua tabia zake. Sio mbaya. Niachie hili…nitazungumza naye, halafu nitazungumza na baba yako…nitakupa mrejesho!”

Jackson alimuachia mama yake suala hilo.

***

MZEE Laulian naye alielezwa juu ya mwanae Jackson kuhitaji kumuoa Modester. Mzee huyo alishangazwa nalo. Lakini alipoeleweshwa alilipokea kama ambavyo mkewe alikuwa amelipokea.

“Wamekwisha zungumza?” Aliuza.

“Ndio,” mkewe alimjibu.

“Na wamekubaliana nini?”

“Bado hawajakubaliana…Modester atakuwa anatuhofia sisi.”

“Kwa nini atuhofie?”

“Pengine kutokana na nadharia ya undugu aliyo kuwa nayo…anaona akimkubalia mwenzie, na kwa namna tulivyo walea, ataonekana ametukosea.”

“Na we’ unasemaje?”

“Binafsi ninaliona ni jambo jema tu!”

Mzee Laulian alipiga kimya akilitafakari jambo hilo. Kisha akamwambia mkewe; “Hebu zungumza naye umsikilize!”

Mama Emiliana akazungumza na Modester.

Lakini bado msichana huyo alishikiria msimamo aliokuwa nao, wakati huu akiweka kisingizio kwamba akili yake haikuwa kabisa kwenye masuala ya uhusiano na alihitaji amalize kwanza shule ndio angefikiria kuhusu kuolewa.

Mama huyo akamwambia kama ni hivyo amkubalie Jackson wawe wachumba na wauhalalishe uchumba huo, huku wakisubiri mpaka pale atakapomaliza masomo.

Bado Modester alikataa akiomba apewe muda wa kulifikiria suala hilo zaidi. Ukizingatia wakati huo walikuwa wanakaribia mitihani chuoni.

Akapewa muda.

ITAENDELEA….
 
SEHEMU YA 8

HATA hivyo, ukweli ulikuwa, si kwamba Modester alihitaji muda wa kujifikiria juu ya kuolewa na Jackson, alihitaji muda wa kufikiria nini afanye kulipangua suala hilo lililokuwa limekwisha mfika shingoni.
Kwa namna lilipofikia, lilimfanya apaone hata nyumbani hapo alipoishi tangu akiwa na umri wa miaka kumi na moja mpaka wakati huo akiwa na miaka ishirini na mbili, kuzimu. Na hakika alijihisi mgeni mahali hapo!
Muda mwingi Modester akajikuta akikaa chumbani kwao na Emiliana akilia. Hasa alipojifikiria kuwa jambo hilo limembakizia pande mbili tu, kumkubali Jackson aendelee kuwa ndugu katika familia hiyo au kumkataa aonekane adui.
Suala la kumkubali kwake ni jambo ambalo lilikuwa haliwezekani.
Wazi aliliona suala hilo ni la kuusaliti moyo wake. Na kwa nini ausaliti? Hakuiona sababu yoyote asilani.
Kila sababu alikwisha ipima kwenye ubongo wake na majibu aliyo yapata ni kwamba, yote aliyofanyiwa na familia ile hayakuwa ni kwa ajili ya kumuandaa awe mke wa mtoto wao huyo mwanajeshi.
Suala la kuolewa, iwe na Jackson ama na mtu yeyote yule alifahamu ni suala la kuhiyari mwenyewe, na si kulazimishwa ama kusongwa songwa kama hivyo ilivyokuwa inatokea.
Hata hivyo katika waza waza yake ya muda mwingi ya uamuzi gani achukue, kuna jambo Modester aliona wazi kuwa alilikosea. Wakati anaanzisha uhusiano na Daud nia yake ilikuwa ni kwamba, amtambulishe kwenye familia hiyo ili kuepusha hilo ambalo lilikuwa linatokea wakati huo.
Lakini hakufanya hivyo.
Aliishia kumtambulisha Daud kwa Emiliana, hapo akaliona kosa kubwa alilofanya. Modester aliliona suala hilo ni kosa kwa sababu, akisema wakati huo ndio amtambulishe Daud, alifahamu wazi angeonekana anafanya hivyo makusudi kumuepuka Jackson. Na hata kama angemruhusu Daud na familia yake wafike nyumbani hapo kwa ajili ya kumtolea posa, bado Modester aliona asingeonekana vizuri.
Sasa afanyeje?
Alizidi kujiuliza.
Ndipo akapata wazo.
Wazo la kumbebea Jackson ujauzito.
Modester aliliona hilo ni wazo jema ambalo lingesahihisha kosa alilokwisha lifanya. Pale ambapo angeitwa kwa ajili ya mazungumzo na mama yake Emiliana basi angempasulia kuwa ni mjamzito. Alifahamu lingekuwa ni suala la aibu kubebea ujauzito nyumbani lakini mwisho wa siku lingemuweka mbali Jackson.
Kwa hiyo alichoamua kukifanya Modester, ni kuwa makini na kalenda yake, akaenda kukutana na Daud wakati akiwa kwenye siku zake za hatari.
Akabeba ujauzito.

ALIYEKUWA mtu wa kwanza kumweleza juu ya ujauzito huo alikuwa ni Daud mwenyewe, na kilichomfariji Modester, Daud alilipokea kwa furaha sana suala hilo.
“Kweli…?!” aliuliza kwa bashasha.
“Kweli D!”
“Siamini.”
“Amini unakwenda kuitwa baba!” Daud alimvutia kwake Modester na kumkumbatia kwa furaha.
Lakini mara ghafla wakielea kwenye hali hiyo ubaridi ukamuingia moyoni. Akamtoa msichana huyo kifuani kwake kwa kumuinua. Wakatazamana. Kisha akamuuliza;
“Nyumbani watalipokeaje hili jambo?”
Modester aliinamisha macho.
“Sijui…” akajibu kwa unyonge. Kisha akainua macho yake taratibu na kumtazama Daud aliyekuwa ametahayari.
“Daud…” aliita kwa sauti yake laini. Daud alibakia akimtazama. “Hivi ni kweli unanipenda kwa dhati?” Alimuuliza.
Daudi alifinya macho kwa mbali katika hali ambayo Modester hakuigundua. Akilini mwake tayari alikuwa amekwisha fahamu Modester alilenga nini kumuuliza swali la namna ile.
“Napenda chapati,” alimjibu. “Kwani we’ ni chapati?” Kisha Daud alimuuliza Modester.
Modester alitanua macho yake kwa wahka. Akamshuhudia Daud akichanua uso wake kwa tabasamu hafifu, kisha kijana huyo akamwambia;
“Nisikilize Mo’!!” alisema kwa mkazo. Modester akamtazama sawasawa. “Ninakupenda kwa dhati na hilo unalijua vilivyo…nipo tayari kushikamana nawe kwenye hili na kuulea ujauzito huu, hata kama kwenu wakitaka nikuoe…nipo tayari!”
Modester alifurahishwa sana na maneno hayo ya Daud, hakika yalimpenya na kwenda kutuama katikati ya moyo wake, akaachia tabasamu mwanana!
“Sasa…” alisema kwa mapozi ya kike, “ unanipenda kwa dhati, je…nimekuwa chapati?” aliuliza kwa mapozi hayo yaliyomletea msisimko wa kipekee Daud.
Daudi akatabasamu na kumrudisha kifuani kwake msichana huyo.
Modester naye akamkumbatia mpenzi wake huku akijihisi faraja isiyo na kifani moyoni mwake. Naye akamwambia yupo tayari kuolewa naye, ili wautunze ujauzito huo wakiwa pamoja. Akamtaka ampe muda azungumze na walezi wake kabla ya ujauzito huo haujawa mkubwa, ili aone mapokeo yao.

***

MTU wa pili kuelezwa kuhusu suala hilo la ujauzito alikuwa Emiliana. Modester alimwambia siku moja walipokuwa wakifanya mazungumzo na wote wakiwa kwenye mood nzuri!
“Usiniambie…?!!” Emiliana aliuliza kwa mshangao mkubwa.
“Mungu moja tena.” Modester aliapa.
“Ni wa muda gani?”
“Mwezi sasa.”
“Na Daud anasemaje?”
“Atasemaje…! Yupo tayari nizae!”
“Na chuo?”
“Kwani tupo sekondari…? Wangapi wanasoma chuo ni wajawazito?!”
Emiliana alipiga makofi ya mkupuo mmoja ya kutoamini jambo hilo au kuonyesha bado halimuingii akilini. Wakabaki kimya Modester akimtazama msichana huyo amepokeaje taarifa hiyo, na Emiliana akawa anaitafakari zaidi.
“Kwa hiyo…” alianza kusema Emiliana. “Habari za kaka Jackson ndio zinaishia hapa?!” Aliuliza kama mtu asiye na uhakika na alichokuwa anakizungumza.
Modester akafinya macho kana kwamba hakuelewa Emiliana alimaanisha nini.
“Unamaanisha nini?” Hatimaye alimuuliza.
“Uliomba muda wa kulifikiria suala lake…na sasa umekuja na habari hii ya ujauzito…unafikiri ni nani atakuelewa humu ndani?”
Modester alikaa vizuri kitandani pale.
“Emmy…” akaita kwa msisitizo. “Ni kweli niliomba muda wa kulifikiria. Na lilikuwa limekwisha anza kuniingia akilini…lakini hili lingine limeibuka, unaf’kiri nitafanyaje?”
Emiliana aliguna.
Modester akawa kimya akimtazama.
“Sasa mama utamwambiaje?” Emiliana aliuliza huku sauti akiwa ameishusha.
Modester akaonekana kubabaika.
“Sijui hata nitamwambiaje? Na hata nikimwambia sidhani kama atanielewa.” Modester alizungumza kwa sauti iliyoonyesha kutekwa na mfadhaiko.
“Haya mambo haya…mkh…ngoja tuone tamati yake…” Emiliana alibwabwaja akiinuka kitandani na kutoka chumbani humo!
Akamuacha Modester akimsindikiza kwa macho huku akishindwa kubashiri juu ya mapokeo ya msichana huyo katika suala hilo alilomueleza.

EMILIANA hakupenda kukaa na habari ile moyoni. Wakati ambao Modester akijipanga namna ya kulifikisha suala hilo la kubeba ujauzito kwa walezi wake na kuwaeleza juu ya mpango wa Daud wa kumuoa, yeye alikwenda kulibwaga mbele ya kaka yake Jackson.
Jackson alihisi kuchanganyikiwa. Tena kule kuchanganyikiwa kwa kuvurugikiwa kabisa. Matumaini yote ambayo alikuwa ameanza kuyapata juu ya kuifanikisha azma ya kumuoa Modester yakayeyuka.
Baada ya kuachana na Emiliana walipokutania na kulizungumzia suala hilo, Jackson alikwenda na kujifungia chumbani kwake na kulia sana.
Bado ilikuwa ngumu kumuingia akilini kuwa alikuwa anakwenda kumkosa mwanamke anayempenda katika maisha yake, Modester.
Hata hivyo, pamoja na mamivu aliyokuwa nayo moyoni Jackson, bado aliamini Modester alimfanyia makusudi juu ya hilo ili tu kujiepusha naye.
Kwa nini ujauzito abebe sasa hivi?
Alijiuliza.
Akajikuta ghafla anamchukia Modester. Chuki ikatambaa mpaka kwa aliyembebesha ujauzito. Huyo ndiye aliyemchukia zaidi na akaona ni mtu anayemkosesha furaha aliyoihitaji maishani.
Jackson alijiuliza; huyo mtu anafananaje? Analinganaje? Anatembeaje? na anatoka familia gani? Akaendelea kumuwazia. Kwamba; anavaa nguo za aina gani? Saa ya brand gani na hata gari analo endesha ni la aina ipi?
Aliwaza mambo mengi juu ya huyo mtu. Swali kuu likiwa kwa nini amnyime furaha?
“Yeye anatabasamu la aina gani ambalo mimi sina?” Alitamka kwa hasira. “Ana maneno matamu ya namna gani ambayo siwezi kusema?”
Akatamani kumuona.
Jackson akashika simu, akaibofya, ikaitia kiganjani mwa Emiliana.
“Emmy…” aliongea kwa msisitizo baada ya simu yake kupokelewa.
“Kaka!”
“Kuna kitu nataka unisaidie.”
“Kitu gani?”
“Nataka kumfahamu huyo Daud.”
“Kaka Jackson…!!”
“Emmy naomba unisaidie kwenye hili.”
Emiliana aliishiwa maneno ghafla. Akabaki kimya.
“Hallo…!” Jackosn aliita akiwa hana uhakika kama simu imekatika au la!
“Bee…!”
“Umenielewa.”
“Nimekuelewa laki…”
“Lakini ya nini kama umenielewa?!”
“Unataka umfahamu ili iweje?”
“Emmy unanisaidia…au hunisaidii?”
Emmy alipiga kimya tena kifupi bila kukata simu.
“Emmy…” Jackson aliita.
“Bee…”
“Nijibu…na kama hunisaidii nambie.”
“Na unataka kumfahamu vipi…yani nikusaidie nini, sijaelewa!”
“Nielekeze wapi naweza kumpata na muonekano wake upo vipi.”
“Ili ukamfanyie fujo?”
“Sijasema hilo.”
Emiliana hakuwa na namna. Alifanya kama kaka yake alivyotaka.
Jioni hiyo hiyo Jackson aliwasha gari na kuliendesha mpaka jirani na yalipo majengo ya biashara ya Mlimani City! Akaingia kwenye duka aliloelekezwa kuwa ndimo angemuona Daud.

JE, NINI KITAENDELEA? USIKOSE SEHEMU INAYOFUATA….

ITAENDELEA….
 
SEHEMU YA 9

Ndani ya duka hilo, Jackson alikuta watu watatu. Mtu mmoja, alikuwa ni mwanamme aliyekuwa amesimama upande aliopo yeye. Akiangaza kwenye meza kubwa ya vioo iliyokuwa mbele yao iliyohifadhi simu mbalimbali. Dhahiri alionekana kuwa ni mteja.
Mtu wa pili, alikuwa ni mdada. Rika la kina Emiliana. Mweupe na mwenye meno yaliyoungua mfano wa baadhi ya watu kutoka Bariadi, Singida ama Arusha. Alimpokea kwa tabasamu na kumkaribisha.
Mtu wa tatu alikuwa ni mwanamme wa rika lake. Mweupe na asiye mrefu sana. Hawakupishana kwa kimo. Kichwani mtu huyo alikuwa amenyoa staili ya zungu la unga, na alikuwa amevaa shati jeupe la mikono mifupi lenye drafti nyekundu, na mkononi alivaa saa ya chuma kutoka brand ya Diesel. Huyo ndiye aliyempeleka mahali hapo kwani hakutofautiana kabisa na maelezo aliyopewa na Emiliana.
“Asante…” Aliitikia karibu ya yule dada.
Kisha akazuga kwa kuangaza simu kwenye ile meza ya vioo wakati yule mteja aliyemkuta akilipia simu aliyokuwa ameichagua. Alipoondoka, Jackson aliinua kichwa kutoka kwenye meza ya vioo na kumtazama yule jamaa ambaye alikuwa akiandika mauzo yale waliyofanya kwenye daftari.
“Brother…!” Aliita kwa mkazo.
Yule kaka aliinua uso na kumtazama.
“Bila shaka wewe ndiye Daud…sio?” Alimuuliza.
“Ndiye.” Alijibu yule kaka kwa mashaka.
“Na bila shaka unamfahamu Modester?”
Daud hakujibu zaidi ya kufinya macho na kumtazama huyo mgeni wa ajabu kwa makini.
“Nakuuliza?” Jackson aliuliza kwa kishindo kilichoonyesha hakwenda pale kwa wema.
“Sema shida yako ndugu… maana naona umekuja kwa shari…hakuna salamu…maswali kwa hali ya kutishia amani…vipi bwana?” Daud alijikakamua na kufoka.
Hakujua alikuwa anacheza na mtu aliyekwisha jiandaa na jambo hilo.
Bila kutegemea Jackson alichomoa bastola yake ya kazini. Akamnyooshea Daud. Daud alitoa macho akiinua mikono juu akijibinya mgongo kwa woga. Yule msaidizi wake wa kazi naye alitoa macho na kufanya kama ambavyo bosi wake alifanya.
“Usije ukathubutu tena kunifokea…?” Jackson alifoka akiwa ametoa macho yake. “Na nisikilize kwa makini. Kufikia kesho, huo uchafu wako tumboni kwa Modester nahitaji uwe haumo, ikizidi kesho…ukiona nimerudi tena hapa, ni ama zangu…ama zako?”
Baada ya maneno hayo, Jackson hakupoteza muda, alitoka mbio mbio na kwenda mpaka alipoegesha gari lake, kisha akatoweka kwa kasi katika eneo hilo!
Aliwaacha wale watu wawili mule dukani wamehamanika vibaya mno.

SIMU ya mkononi ya Modester iliita, lakini msichana huyo hakuisikia. Ikaita tena na tena, mpaka mara kumi ilipigwa bila kuisikia ingawa ilikuwa pembeni yake mgongoni kitandani hapo alipokuwa amejilaza. Hakuisikia kwa sababu alikuwa ameitolea sauti ya muito.
Ilikuwa silent!
Wakati simu hiyo inapigwa Modester alikuwa amezama kwenye dimbwi zito la mawazo, akiwaza mustakabali wa maisha yake katika yote hayo yaliyokuwa yanayendelea. Modester aliona dhahiri mambo yalikuwa mengi na muda ulikuwa mchache!
Akiwa amezama kwenye dimbwi hilo la mawazo, Modester alijikuta akiwaza kuwa pengine kuna sehemu alikuwa anakosea na ni yeye aliyekuwa sababu ya hali hiyo iliyokuwepo upande wake wakati huo.
Akajikuta akijiuliza; kwa nini nisingemkubalia tu Jackson na kuepukana na yote haya? Kwani naye si ni mwanaume kama Daud au wanaume wengine?
Lakini nafsi yake nyingine ilimwambia amekwisha chelewa kuwaza hilo, anaujauzito wa mtu tumboni na kwa vyovyote huyo ndiye mtu wa kushikamana naye ambaye angeweza kumtoa kwenye wakati huo mgumu aliokuwepo.
Nafsi hiyo ikitua kumjuza hilo, ile nyingine ya mwanzo ikamwambia anakuwa mjinga!
Ikamuuliza; unawezaje kumkabidhi mwanamme maisha yako? Leo na kesho mkikosana na Daud utakimbilia wapi na kwa walezi wako ukiwa umekwisha haribu?
Nafsi hiyo ikamfunulia pia kuwa, kama akiolewa na Jackson hata kama wakitofautiana alikuwa na mahala pa’ kukimbilia. Angerudi nyumbani hapo na angepokelewa kama mkamwana au mtoto vile vile.
Nafsi hiyo ikamwambia ameyakoroga mambo mwenyewe.
Modster akazidi kuchanganyikiwa.
Jahazi kwenye maisha yake akaona wazi linazidi kuzama. Kila anachojaribu kufanya ili kujiweka katika namna ya kupata furaha, anakuta kinazidi kumfukia shimoni.
Akiwa katika mkanganyiko huo wa mawazo, Emiliana aliingia mbio mbio chumbani humo.
Alimshitua kweli kwa namna alivyoingia na kuubamiza mlango!
“Simu yako iko wapi?” Alimuuliza kwa sauti yenye msisitizo wa ukali.
Modester alizungusha mkono na kupapasa mgongoni kwake, akaichukua.
“Kuna nini?” Aliuliza kabla hajaitazama.
“Daud anasema amekupigia sana hupokei…na kumbe simu upo nayo hapo hapo…!!”
“Niliitolea muito,” Modester alisema kwa utulivu akiitazama simu hiyo. “Hee! Kapiga mara kumi…na meseji juu!”
Emiliana hakuzungumza, alibakia amesimama akimtazama.
Modester akaipigia namba ya Daud.
Simu ikapokelewa baada ya kuita mara kadhaa.
“Mbona hupokei simu wewe…mpaka nakutafuta kwa Emiliana?!” Daud alimuuliza kwa ukali.
“Nilikuwa nimeitolea muito…” Modester alijibu taratibu.
“Kwa nini?’
“Aaah…nina mengi kichwani Daud…nilikuwa sihitaji kuzungumza na simu!”
“Mkh…!” Daud aliongea kwa mtindo wa kuguna. “Upo wapi?” Alimuuliza.
“Nyumbani…” Modester alijibu na kuuliza; “Kwani vipi mbona haupo kwenye hali ya kawaida?”
“Upo na nani?” Alijibiwa kwa swali.
Kha!
Modester alijikuta akihamanika na kumtupia macho Emiliana.
“Nipo na Emmy…vipi?…kuna nini?” alijibu na kufurumusha maswali.
“Nisikilize…” Daud alimsimulia tukio zima la kuvamiwa dukani pale na mgeni wa ajabu pamoja na vitisho alivyompa.
Modester alibaki mdomo wazi akishindwa aseme nini. Kwa namna Daud alivyomuelezea juu ya haiba ya huyo mtu, alifahamu kuwa ni Jackson. Akabaki kimya katika mshangao usio elezeka.
“Halloo…” Daud aliita simuni.
“Nakusikia Daud…” Modester alijibu kwa unyonge mno.
“Umemuelewa huyo mtu…?”
“Ndio nimemuelewa.” Machozi yalianza kumbubujika Modester.
Kikafuata kilio na akashindwa kabisa kuendelea kuzungumza na hiyo simu. Akaitupa kitandani na kuzama kwenye kilio cha kwikwi.
Emiliana haraka akasogea na kukaa karibu yake.
“Kuna nini?” Aliuliza.
Modester alizidi kulia.
“Mo’ ni nini jamani…?!”
Lakini hakumjibu aliendelea kulia.
Mawazo aliyoyapata Emiliana ilikuwa ni kumpigia simu Daud na kumueleza juu ya hali aliyonayo Modester baada ya kuzungumza naye ikiwa ni pamoja na kuhoji nini kimetokea.
Msichana huyo alipoelezwa kilichotokea alipigwa na mshangao wa mwezi!
“Kaka Jackson…!” Emiliana alibwata baada ya kukata simu. “Aaah!...kafika mbali ni lazima nimwambie baba…”
“No…” Modester alidakia haraka akivuta mafua yaliyomvagaa ghafla akimnyooshea mkono Emiliana utadhani alikuwa akimzuia asiondoke. “No…no…no…big no Emmy…usikurupuke…!”
Baada ya maneno hayo ya Modester Emmy alijiinamia akizitafakari taarifa zile. Zilikichanganya kweli kichwa chake. Akajikuta pia akijilaumu kumueleza habari za ujauzito kaka yake na kumuelekeza mahali ambapo Daud anapatikana.
“Sasa utafanyaje Mo’?” Baada ya muda Emiliana alimuuliza Modester.
“Sijui…” Modester alimjibu kwa sauti ya chini yenye kishindo cha kuchanganyikiwa.
Emiliana aliguna na kuzungusha kichwa kwa masikitiko.
“Nilikuwa upande wake…” Alisema. “Ni kaka yangu nisingeweza kumtupa…lakini huku alipofika… hapana…!!” Ilikuwa ni kama Emiliana anazungumza peke yake.
“Mo’” akaita.
Modester alimtazama.
“Wacha nimwambie baba…” Emiliana alimwambia kwa msisitizo.
“Emmy huwezi jua wazazi wako watazipokeaje taarifa hizi…sitaki kuwa sehemu ya kupoteza maelewano kwenye familia yenu Emmy…aaah…nafikiria niondoke tu mimi…nipotee…niende mbali na ujauzito wangu….Jackson afurahi na roho yake…” Modester alianza kuangua kilio tena.
Emiliana naye machozi yaligonga kwenye mboni za macho yake. Akauzungusha mkono wake mmoja mabegani mwa Modester.
“Usiseme hivyo mpenzi…” alimwambia. “Familia yetu ni familia yako. Sote tumelelewa kwa upendo na tukiwa kitu kimoja toka tupo wadogo…leo hatuwezi kutengana kisa hili…”
“Sasa…” Modester aliongea na kusita. “Kama mama hakunielewa wakati nakataa kuwa na Jackson, unafikiri hapa ataelewa kitu?…Tuna ushahidi gani juu ya kilicho tokea…siataona tunatengeneza sinema ili tu nisiwe na mwanae?!”
“Ndio maana nimekwambia niruhusu niongee na baba au mama mimi mwenyewe!”
“Emmy…nipe muda nilifikirie hili…” Modester alimwambia na kujiinamia.
Emiliana hakujibu, alibakia akimfariji kwa kumpapasa mgongoni.

***

BAADA ya kufika nyumbani kwake alikoishi, kwenye makazi maalumu wanayoishi wanajeshi kwenye kambi ya Lugalo, Jackson alijibwaga sofani na kushusha pumzi ndefu.
Jambo alilotoka kulifanya lilimuogofya hata yeye mwenyewe.
Kumnyooshea mtu bastola kisa mwanamke!
Lilikuwa ni jambo ambalo hakuwahi kufikiria kulifanya katika maisha yake yote. Lakini ni tukio hilo lililomfanya azidi kutambua kuwa moyo wake ulikuwa taabani kwa Modester. Na alikuwa tayari kufanya lolote lile kwa ajili yake.
Akiwa sofani hapo akizidi kulikumbuka tukio hilo alilotoka kufanya, simu yake iliita.
Akaichukua haraka haraka kutoka mfukoni. Akaona mpigaji ni aliyemhifadhi kwa jina la; sisiter Emmy!
Akaipokea simu ile.
“Ndio umefanyaje…?” Aliulizwa.
“Unamaanisha nini?” Akajifanya kuhoji.
“Hujui eeh…sasa kwa taarifa yako namwmabia baba!”
Jackson alibaki kimya bila kuzungumza akitafuta neno la kusema, simu ikakatika. Akaipiga haraka lakini haikupokelewa.
Akabwaga kite cha hasira akishindwa aendelee na uamuzi gani.

ITAENDELEA….
 
SEHEMU YA 10

DAUD naye hakuwa kwenye hali ya kawaida. Kilichomtokea kilimtisha mno na aliiona hatari kubwa kwenye maisha yake. Baada ya mgeni huyo wa ajabu kuondoka, hakutaka kuendelea na biashara tena.
Tayari siku hiyo ilikuwa imekwisha kuwa siku mbaya, alifunga duka kisha yeye na msaidizi wake wakaelekea majumbani kwao. Yeye akienda Mtaa wa Makongo Juu ambako ndiko alikuwa anaishi.
Akiwa nyumbani kwake ndipo alipompigia simu Modester na baada ya simu kuita sana bila kupokelewa, baadaye Modester alipompigia na kumueleza tukio lililotokea, alifahamishwa kuwa mgeni huyo wa ajabu kwake alikuwa ni kaka yake na Emiliana aitwae Jackson.
Jina hilo halikuwa geni.
Daud alikuwa anafahamu kuwa Emiliana alikuwa na kaka yake anayeitwa Jackson, ambapo hata Modester alimuita kaka na alimuheshimu kama ambavyo Emiliana alikuwa akimuheshimu.
Suala la Jackson kutaka kumuoa Modester hakulifahamu!
Sasa akabaki anajiuliza; Hasira alizozionyesha Jackson, za hadi kumtolea bastola ni kwa sababu ya ujauzito aliompa ‘dada’ yake huyo Modester?
Jambo hilo likawa ni vigumu kumuingia akilini. Daud aliona hasira alizozionyesha Jackson ni za kiwango cha juu mno. Suala la ujauzito tu, tena kwa dada ambaye sie wa tumbo moja naye ndilo limfanye afanye vile?
Aliona haiwezekani.
Ni lazima kuna kitu cha zaidi.
Lakini ni kitu gani?
Hilo ndilo likaonekana ni swali gumu zaidi kulipatia jibu. Lakini akili yake ilimwambia jibu la swali hilo ni lazima analo Modester. Hapo hapo alishika simu na kumtumia meseji Modester ya kumuomba wakutane siku iliyofua.
Mkutano wao siku hiyo, ndio ukawa kiama chao!

“HUWA sipendi kuikumbuka kabisa hiyo siku Masika…” Bi Modester alimwambia James Masika huku akivua miwani na kupangusa machozi kwenye pembe za macho yake. Akaendelea kuzungumza kwa sauti ya kizee iliyokauka kwa simanzi akivikunja vishikio vya miwani ile ya macho;
“Ni katika siku hiyo, picha ya maisha yangu ilipobadilika. Zaidi nikawa mlemavu hivi nilivyo leo…” Aliongeza kwa utulivu.
Masika akashusha pumzi fupi akimtazama mwanamke yule kwa huruma.
“Pole sana mama,” alimwambia.
“Aaah! Ndilo fungu la maisha nililopewa …” Bi Modester alisema kwa msisitizo wa chini. Akaendela hapo hapo; “Angalau mimi pamoja na kuwa mlemavu niliweza kusaliwa na uhai na leo nipo nasaidia watu kituoni hapa…lakini yule handsome wangu, Daud ambaye ndio kwanza maisha yake yalikuwa yanaanza kuchanua… alikufa…!”
“Daud alikufa?!” Masika aliuliza kwa hamaniko lenye simanzi, “Na Jackson Je?” Aliongeza swali.
Bi Modester aliguna akizungusha kichwa kwa huzuni.
“Ni siku mbaya sana kukumbuka mwanangu…” alisema tena kwa utulivu bibi yule.
Masika akamtazama naye kwa utulivu uso wake ukitahayari.
Kisha akamwamba; “hebu endelea kunisimulia!”
Bi Modester aliokota chupa ya maji iliyokuwa chini pembeni ya baiskeli yake ile ya magurudumu, kisha akaifungua na kulowanisha koo lake kwa mafunda kadhaa ya maji. Akakifunga kifuniko cha chupa ile.
Kisha aliendelea kumsimulia James Masika ‘Masika The Best’, ilivyokuwa.

***

JIONI ile, kama Emiliana alivyokuwa amepania, baada ya baba yake kufika nyumbani na kumaliza kupata chakula, alimuomba pamoja na mama yake wakae pamoja sebuleni akiwaambia alikuwa na kikao nao.
Walimkubalia na kukaa.
Akawaeleza mkasa uliotendwa na Jackson na wote walilipuka kwa mshangao kwa habari hiyo.
“Jackson ndiye kafanya hivyo?!” Baba yake aliuliza kwa hamaniko. “Muite Modester!” Akaongeza upesi.
Modester aliitwa.
Alipofika na kukaa aliulizwa na mzee Laulian;
“Hizi habari kumhusu Jackson ni za kweli?”
Alijibu kwa kuinua kichwa na kukipandisha.
Kimya kifupi kikatawala sebuleni hapo.
“Na ni kweli we’ ni mjamzito?” Hatimaye mama Emiliana aliuliza kwa kishindo cha ukali wa chini.
Hilo Modester hakulijibu mara moja, alibaki akitazama chini kwenye sakafu wakati watu wale watatu wakimtazama.
“Ninakuuliza…!” Mama Emiliana aliongeza msisitizo kwenye swali lake.
Modester alipandisha kichwa na kushusha.
“Hilo suala ni la kujihusisha nalo muda mwingine…kubwa ni hili la huyu anayeshikia watu bastola…hili ndilo la kuanza nalo…” Alisema mzee Laulian akichukua simu yake kisha akaipigia namba ya Jackson.
Baada ya Jackson kupokea, baba huyo alimtaka siku iliyofuata afike nyumbani hapo bila kukosa kwani alikuwa na mazungumzo naye ya muhimu.
Baada ya kukata simu, mzee Laulian alishusha pumzi ndefu na kumalizia kwa kutoa kite cha kuchoshwa na jambo lile. Kisha aliwaambia Emiliana na mwenzie waende zao chumbani wamuache na mkewe!

“EMMY kwa nini umesema?” Modester alimuuliza Emiliana kwa kulaumu walipofika chumbani kwao.
“Jackson hajafanya jambo zuri Mo’ wacha ashughulikiwe,” Emiliana alimjibu.
“Na kuhusu ujauzito?!”
“Imekwisha tokea, utaficha mpaka lini?”
“Yanakwenda kuwa makubwa haya!” Modester aliongeza kwa msisitizo wenye simanzi.
“Wacha yawe lakini we’ ubaki huru.” Emiliana alimjibu.
Modester alitoa kite cha kukata tamaa.

***

SIKU iliyofuata, Jackson alifika nyumbani kwao majira ya saa sita za mchana wakati kukiwa na maandalizi ya chakula jikoni. Alienda mapema ile kwa sababu jioni alitakiwa kwenda kazini.
Kwa hiyo, alishiriki chakula cha mchana mezani na familia hiyo. Na tofauti na siku zote ambazo familia ile imewahi kukaa pamoja kwa ajili ya chakula, siku hiyo ukimya usio wa kawaida ulitawala mezani pale.
Kila aliyejaribu kuanzisha jambo la kuzungumziwa, lilikosa wa kushadadia.
Modester ndiye alikuwa wa kwanza kusitisha zoezi la kula, akainuka mezani kimya na kuondoka kila mmoja akimsindikiza kwa macho ya pembeni. Alifuata Emiliana ambaye baada ya kuosha mikono, alielekea chumbani kwao alikokuwa ameenda Modester.
Baada ya chakula na kupumzika, ndipo mzee Laulian alipowakalisha watu wale sebuleni. Mkewe, Jackson, Modester na Emiliana.
Mzee Laulian alianza kwa kuuzungusha uso wake akizitalii nyuso za watu wale waliokuwa wamekaa kimya, kisha alijikohoza kuvuta usikivu kwamba alikuwa anakwenda kuanza kuzungumza;
“Kikao hiki ni kwa ajili yako Jackson, bila shaka unafahamu hilo?” Jackson alimung’unya lipsi za mdomo wake akikwepesha macho kutazamana na baba yake.
“Mama yako aliniambia juu ya uhitaji wako wa kumuoa Modester,” Aliendelea mzee Laulian. “Sina haja ya kukuuliza ni kweli au la, kwa sababu ninaamini kile ambacho alinieleza. Je, umefikia wapi katika mpango wako huo?” Alimuuliza swali la mtego.
Jackson hakujibu, aliinamisha kichwa chini!
“Hakuna jibu?” Mzee Laulian aliuliza tena.
Hakuna aliezungumza.
“Jackson mambo hayaendi kama ambavyo unataka yaende mwanangu, ni aghalabu kusikia mtu kachumbia kwa panga au mtutu na ndoa ikawezekana. Inakuwaje unafikia hatua ya kumshikia mtu bastola kwa ajili ya mwanamke ambaye hujafanya naye makubaliano? Na hata kama ungekuwa umefanya naye makubaliano…unamshikiaje mtu bastola? Kwamba ndio jambo lako litawezekana?...Unajidanganya…!”
Mzee Laulian alimtazama kijana wake kusaili aliyozungumza kama yalikuwa yanamwingia, kisha aliendelea;
“Kwanza, hili suala umelikosea toka awali. Halikuwa jambo baya wewe kuhitaji kumuoa Modester, ni kweli hamna undugu wa damu. Lakini kwa namna tulivyo walea, pale tu ulipoipata hiyo tamaa ya moyo, ulipaswa kunieleza mimi kama baba yako na nikakwambia jambo la kufanya. Kirahisi tu ungempata mke unaye mtaka…lakini we’ umekurupuka…unaf’kiri kila kitu kinatumia nguvu kama mfanyavyo huko jeshini!”
Mzee Laulian alitulia tena. Akataka kuendelea lakini akajikuta akigonganisha maneno na Jackson ambaye alihitaji kujibu jambo. Ikabidi amruhusu aseme alichotaka kusema.
“Nakubali nimekosea…” Alianza Jackson akimtazama baba yake. “Lakini mengine yanayoendelea kwa sasa ninafanyiwa makusudi ili nionekane mbaya!”
“Unamaanisha nini?” Baba yake alimuuliza kwa utulivu.
“Kwa nini suala la ujauzito lije sasa?” Aliuliza. “Namaanisha kwa nini hakuupata huko awali kabla sijamtangazia nia ya kumuoa?…Sasa hivi ndio amekuja na habari hii…haya si makusudi, hata mimi ni binadamu na ninamoyo baba…” Jackson alizungumza akionekana kupandisha hasira.
“Come down son!” Baba yake aliongea kwa kimombo akimtuliza kwamba arudi chini. “Na ndio imekwisha tokea…sasa wewe kwa mawazo yako unatakaje?” alimuuliza.
“Mimi nipo tayari kumuoa na ujauzito huo…au autoe!”
Maneno yale yalimshangaza kila mmoja aliyekuwa sebuleni pale. Hakuna alietegemea kama Jackson angeweza kuzungumza ‘utumbo’ ule.
“Ebo! Unasemaje?” Mama yake alilipuka. “Hivi unaakili wewe?” Aliongeza kwa mkazo wa hasira. “Ni kwa sababu wanawake wameisha duniani…au huyu mtoto wa kike tu ndiye ulizaliwa umuoe?!” mama huyo alizidi kuporomoka kwa ghadhabu.
Jackson naye alimjibu.
“Mama…kila mtu duniani ana chaguo lake…Mo’ mimi ndiye chaguo langu!”
Kijana yule alizidi kuwahamanisha watu wale.
“Hee! Jackson…unatumia siku izi bange eeeh!”
“Mama Emilian hebu tulia…” Mzee Laulian alimtuliza mkewe aliyekuwa amekwisha pandwa na mhemko. “Modester unamsikiliza mwenzio…” mzee huyo akasema kwa utulivu.
Modester ambaye alikuwa ameinamisha kichwa chini alikubali kwa ishara ya kutumia kichwa.
“Una lipi la kusema?” Mzee Laulian alimuuliza.
“Atakuwa na lipi la kusema baba Emmy?” mkewe aliingilia. “Mmeshaambiwa ni mjamzito…atakuwa na lipi la kusema…?!” aling’aka mwanamke huyo.
“Hapana muache aseme kwa mdomo wake…” Mzee Laulian alisisitiza.
Kimya kidogo kikajikita.
“Mode tunakusikiliza….” Alirudia kusisitiza mzee Laulian.
Modester aliinua kichwa kwa unyonge.
“Sijui niseme nini baba…ila siwezi kuwa na Jackson… ni kaka yangu…naomba ibaki kuwa hivyo tu!” Alisema binti huyo kwa unyonge.
“Mi’ si kaka yako…!!” Jackson alilipuka kwa hasira.
Akatupiwa macho ya mshangao na kila mmoja.
Mama yake akazidi kuhamanika vibaya mno.
Mzee Laulian yeye aliachia kicheko kifupi cha masikitiko. Kisha aliwaambia Emiliana na Modester wawapishe sebuleni pale waende chumbani kwao, huku akimtaka Jackson kubaki.
Binti wale waliondoka na kuelekea chumbani.
Hata walipofika chumbani wawili hao walikuwa bado wakizungumzia kilichokuwa kimetokea. Emiliana ndiye alikuwa msemaji zaidi akishangazwa na tabia aliyoionyesha kaka yake.
Wakiendelea na mazungumzo Modester alishika simu yake aliyokuwa ameiacha chumbani humo hapo awali, alikutana na meseji kutoka kwa Daud!

Daud: Mambo! Utakuja saa ngapi?
Modester aliijibu.
Modester: Kwa hali ilivyo nyumbani nitashidwa D, we’ fanya kuja maeneo ya huku.
Punde ilijibiwa.
Daud: Kuna kingine zaidi kimetokea?
Modester: Nitakwambia tukionana.
Daud: Na huko tutaonania wapi?
Modester: Hata maeneo ya Aroma pale kituoni, au kwenye ile lodge ya upande wa pili wa kituo, kuna sehemu ndani tunaweza kuzungumzia, au mazingira yoyote, hatuwezi kukosa sehemu ya we’ kuegesha hata gari lako na tukazungumza. Najua nikija Makongo na mafoleni haya, nitachelewa kurudi nyumbani…”
Daud: Basi poa, nakuja muda si mrefu. Nikifika Mwananchi nitakwambia uanze kusogea.
Modester: Poa mpenzi.
Daud: Nakupenda Mo’
Modester: Nakupenda pia D!
Modester aliiweka simu pembeni.

ITAENDELEA TENA….
 
SEHEMU YA 11

AMBACHO hakikufahamika katika familia ya mzee Laulian ni kwamba, baada ya kwenda depo, kwa ajili ya mafunzo ya kijeshi, kuna makundi ambayo Jackson alijiingiza ili kuonekana mwamba.
Alifanya hivyo kutokana na mazingira aliyo yakuta mafunzoni huko. Ilikuwa ni uwe mbabe uonee au uwe mnyonge uonewe, kama si hivyo basi uwe na kundi la kusimama mbele yako pale unapotaka kugeuzwa dagaa na ma’samaki yaliyokuwepo huko.
Hapo ndipo Jackson alipojiunga na kikundi kimoja kilichokuwa kinajihusisha na matumizi ya bangi. Suala hilo la kutumia bangi akaendelea nalo kwa siri hata pale alipotoka mafunzoni huko.
Na tabia moja ambayo alikuwa nayo, baada ya kuvuta mihadarati hiyo alijikuta anakua mtu mwenye hasira mno na angeweza kufanya jambo lolote lile au kuzungumza lolote lile, alipohitaji jambo lake liende.
Kwa hiyo, baba yake alipompigia simu na kumueleza juu ya kuhitaji kikao naye, alijua ni kwa ajili ya masuala ya Modester. Jackson aliwafahamu wazazi wake kuwa ni watu siriasi wasio penda kupindisha maneno hasa pale wanapokuwa tofauti na mtu. Kwa mambo yalivyokuwa Jackson alijua siku hiyo ya kikao angechapwa kwa maneno vibaya mno tena kwa zamu, kwahiyo alijipanga kukabiliana nao.
Ndipo alipovuta bangi zake. Akaenda kwenye kikao kile akiwa amewaka. Akayadabanganya mambo kweli kweli.
Hata wazazi wake walipombakiza sebureni kwamba wazungumze naye jambo lile kwa ustaarabu ikiwezekana aachane nalo, yaliwashinda. Aliwajibu ovyo ovyo mpaka wakashangaa.
Ikabidi wamuache, na kumtaka aondoke zake.
Akatoka…

DAUD alipofika Mwananchi alimjulisha Modester kwamba anakaribia kufika. Modester akatoka kwa ajili ya kwenda kukutana naye maeneo ya kabla ya kituo cha Aroma, kama walivyokuwa wamekubaliana. Wakati Modester anakwenda kukutana na Daud, ndipo wakati ambao Jackson alikuwa anatoka.
Sasa Jackson alipofika kwenye kituo cha Aroma alimuona msichana huyo akitembea barabarani. Akajiuliza anakwenda wapi? Kuna nafsi ikamwambia; hebu mfuatilie. Akamfuatilia. Akamuona baada ya kukipita kituo cha Aroma, alielekea jirani na saluni moja ya kiume, akasimama kwenye gari moja nyeupe ambayo hakuitambua mara moja ni aina gani.
Jackson ikambidi asimamishe gari yake pembezoni mwa barabara. Akazidi kumfuatilia msichana yule kwa macho. Baada ya kama dakika tatu za Modester kusimama mbele ya lile gari, aliona mlango wa dereva hapo alipokuwa amesimamia ukifunguka na akashuka kijana mweupe.
Jackson alifinya macho zaidi kumtazama jamaa huyo kwa umakini, akamtambua. Kuwa ndiye Daud aliyemfuata jana yake pale jirani na Mlimani City. Kijana huyo akahisi kuchefukwa ghafla. Hasira zisizo na kifani zikafumuka kifuani kwake. Akajihisi mpaka kutetemeka.
Akazidi kuwafuatilia watu wale akiwa katika hali hiyo.
Akamuona huyo mgomvi wake akimshika mkono Modester. Moyo ukamlipuka. Akawafuatilia kwa macho moyo ukimwenda mbio, akawaona wawili wale wakitembea wameshikana mikono kuelekea barabarani, akafahamu wazi walihitaji kuvuka kuelekea upande wa pili kulipokuwa na lodge!
“Haiwezekani!” alijikuta akisema kama aliyechanganyikiwa.
Wakati wawili wale wakiivuka barabara, bila kuelewa akili ile ya kinyama ilifumuka kutoka wapi, aliliwasha gari na kulifyatua kwa kasi.
Daudi na Modester wakaliona gari hilo lililofyatuka. Wakapigwa na butwaa isiyo ya kawaida. Wakabaki wameshikana mikono barabarani huku wametoa macho wasijue cha kufanya. Wakati huo huo kelele zikasikika pande zote za barabara kwa watu waliokuwa wanashuhudia kile kilichokuwa kinakwenda kutokea.
Bila huruma Jackson alikwenda na kuwakumba wawili wale kama tsunami, akawabeba na kwenda kuwatupa mtaroni huku gari likifika na kumpondea zaidi mtaroni humo Daud.
Ukweli ni kwamba lilikuwa ni tukio la aina yake na kila aliyeliona alishika kichwa kwa kutoamini. Punde tu baada ya kutokea kwa tukio hilo watu walijaa eneo lile ambapo watu wale watatu wote walikuwepo.
Daud alikuwa amebanwa na gari, Jackson aliyechomoka kupitia kwenye kioo cha mbele alikwenda na kujipiga kwenye ukuta wa mtaro ule wa zege akasambaratikia mtaroni humo na Modester alikuwa hatua kadhaa kutoka pale alipodondokea Jackson.
Mashuhuda wa tukio hilo walifanya jitihada za kuliinua gari, wakamtoa Daud, lakini walikuta amekwisha poteza maisha. Wakamtazama Jackson, naye ubongo ulikuwa umemwagikia pale pale. Modester pia alikuwa kimya. Ila kwa mbali alikuwa na uhai. Miguu yake tu ndio ilikuwa imesagika vibaya kutokana na kuburuzwa na gari pale lilipowakumba kwenye rami. Yeye alichukuliwa haraka na msamalia mwema mmoja aliyekuwa na usafiri, akakimbizwa kwenye Hospitali ya Amana na watu wawili wengine walioambatana naye, kuona kama wangeokoa maisha yake.
Walipomfikisha Amana alikataliwa kutokana na hali aliyokuwanayo, wakamkimbiza Muhimbili.
Hapo, mara moja Modester aliingizwa kwenye chumba cha uangalizi maalumu, na jopo la madaktari bingwa wa huduma ya kwanza lilianza kumshughulikia.
Huku akishughulikiwa na madaktari hao, wasamalia wema wale walirudi mpaka Tabata hapo maeneo ilipotokea ajali, wakapeleleza mpaka nyumbani kwao Modester kwa kuwaulizia dereva bodaboda waliofanyia kazi kwenye mazingira yale, wakaelekezwa, ndipo walipokwenda kuwapa taarifa ya ajali aliyoipata Modester na tukio lililosababisha ajali ile.
Taarifa hizo zilimshitua kila mmoja!
Mzee Laulian, mkewe, Emiliana na Dada wakainuka mbio mbio wakiambatana na watu wale mpaka eneo la tukio. Waliwakuta askari wa usalama barabarani wakiendelea na taratibu zao, pia waliwakuta watu wakiwa wamekusanyika kulizunguka eneo la karibu na lilipokuwa gari la Jackson, ndani ya mtaro likiwa limebondeka vibaya mno. Lakini si mwili wa kijana wao huyo wala Daud waliukuta, walikuwa wamekwisha kwenda kuhifadhiwa kwenye hospitali ya Amana.
“Naombeni mnieleze ukweli…” mama Emiliana aliongea kwa kuchanganyikiwa, “mwanangu amekufa au la?” Aliwauliza wale wasamalia wema kwa simanzi.
“Mtoto wa kike ni mzima…” aliambiwa.
“Na wa kiume?” Aliuliza haraka.
“Hatufahamu…alichukuliwa na watu wengine kwenda hospitali, sie tulimbeba wa kike. Ila bila shaka, atakuwa yu mahututi tu, kama walivyo wenzie.” Alijibiwa.
Hata hivyo katika hali halisi mwanamke huyo alifahamu Jackson alifariki kwenye ajali ile jambo ambalo alilisoma kutokana na jibu alilopewa. Alijua ni wazi alikuwa anajalibu tu kutulizwa lakini mwanae hakuwepo tena duniani.
Kwa nini naye asingepelekwa Muhimbili kama mwenzake, na aambiwe kuwa alichukuliwa na watu wengine? Inamaana usafiri ulikuwa mdogo? Suala hilo halikumuingia akilini katu!
Uchungu wa mzazi ulimkumba mama Jackson! Bila kuelewa alijikuta akihisi kuishiwa nguvu akakaa chini. Akaanza kulia taratibu, kila jambo hilo lilivyozidi kumuingia moyoni ndivyo na kilio alivyozidi kuongeza, ikafika wakati akawa anaangua kilio kikubwa akipokezana na Emiliana.
Ukweli ni kwamba hali ya simanzi ilienea mahali hapo. Kila aliyemtazama mwanamke huyo na mwanae kwa namna walivyokuwa wanalia, alijikuta akifuta machozi kwa simanzi!
Mzee Laulian akawaomba wanawake waliokusanyika mahali pale wamsaidie kuwarudisha nyumbani wawili wale waliokuwa hawajiwezi kwa hali, kisha baada ya kufanikiwa hilo, alielekea katika Hospitali ya Amana pamoja na ndugu na jamaa ambao walifika mara moja baada ya kuwapasha juu ya tukio hilo, huko ndiko walikothibitisha kwamba Jackson na Daud walikuwa wamekufa!

MASIKA alishusha pumzi za msisimko baada ya kusimuliwa na Bi Modester juu ya tukio hilo lililoondoka na uhai wa Jackson na Daud. Akajiegemeza kwenye kiti kile alichokuwa amekalia hohehahe akimtazama kwa simanzi bibi yule ambaye hali ya majonzi ilikuwa imekwisha mteka na machozi yalikuwa yakimbubujika.
“Usilie,” alimsihi akijiinua pale kitini na kukaa kawaida.
“Hapana silii,” Bi Modester alimjibu Masika, akifuta machozi kwa viganja vya mikono yake huku akijenga tabasamu la bandia.
“Machozi yanakububujika…!” Masika alimwambia.
“Siyo siri, kila nikikumbuka juu ya hiyo siku huwa naumia sana!” Bi Modester alisema kwa utulivu na akashusha pumzi fupi.
“Ni mapito ya maisha mama…”
Bi Modester aliachia mguno mfupi. “Nafahamu mwanangu,” alimjibu Masika. “Lakini mapito kama haya huwa ni mzigo mzito moyoni...na ni kisima cha majonzi kwa mtu aliyepitia!”
Masika alimeza mate ya baridi yaliyotokana na simanzi iliyoanza kumtwaa pia.
“Mungu anamakusudi kwenye kila alilokupitisha …” alimwambia.
“Ni kweli…nimekuwa nikikweleza mara kwa mara, nimaamini kupitia sababu kwenye kila kitu kinachomtokea binadamu duniani.”
Ukimya mfupi ukajikita.
“Kwa hiyo…?” Masika alikivunja kimya hicho akiongea kwa mvuto wa kuuliza. “Baada ya wewe kupelekwa hospitali ndio ulikatwa miguu?”
“Ndio,” Bi Modester alijibu. “Ilionekana mifupa imesagika vibaya mno na hakukuwa na uwezekano wa kuungwa. Kilichotakiwa kufanyika…ilikuwa ni kuikata!”
“Daah…!”
“Mkh!”
“Pole sana mama.”
“Nilisha poa.”
“Na misiba ile ilipokelewaje kwenye familia za wahusika?”
“Aaah…ilikuwa shida sana…”
“Kwa nini?”
“Kwanza kwa upande wa nyumbani kwetu pale…nasikia msibani mama yake Jackson, alikuwa akilia huku analaumu kwa kunitaja jina kwamba mimi ndiye niliyesababisha kifo cha mwanae. Jambo ambalo lilisababisha niishi kwa shida sana hata baada ya kutoka hospitali.
“Lakini kwa upande wa Daud, ilifika hatua hawakuwa na namna, walikubaliana na matokeo wakaamua jambo lile kuliacha lipite tu…maana kama ni mtu wao alikuwa amekwisha kwenda, hata wangefanya nini asingeweza kurudi!”
“Utanisimulia kuhusu namna ulivyo ishi na familia ya kina Emiliana baada ya kifo cha Jackson…lakini hebu niambie kuhusu ujauzito, haukutoka?”
Bi Modester aliachia tabasamu la mbali. Kisha akatikisa kichwa akimaanisha haukutoka.
“Ndiyo niliwazaa wanangu hao mapacha!” Akasema.
“Na uliitaarifa familia ya Daud kwamba una watoto wao?”
“Baada ya kujifungua niliwatumia ujumbe…lakini, yule naye alikuwa ni yatima kama mimi, hata taarifa ile walipoipata walezi wake, walionyesha kujali siku za mwanzoni tu baadaye wakapotea, na toka hapo hakukuwa na ufuatiliaji ule wa watu kutambua kwamba wanamtoto wao sehemu!”
“Aisee…” Masika alisema kama aliyechoka. Akashusha pumzi fupi na kumtazama Bi Modester, akifyatua ulimi na kutoa kite kama cha kulaumu.
“Haya…nisimulie sasa, maisha yalikuwaje baada ya kutoka hospitali!” Alimwambia.
Bi Modester alianza tena kumsimulia James Masika ilivyokuwa!

Alimsimulia kwamba…

ALIKAA hospitali pale Muhimbili kwa muda wa miezi mitano. Baada ya afya yake kuimarika ndipo aliporudishwa nyumbani akiwa kwenye kiti cha magurudumu. Hali hiyo ilikuwa inamuumiza mno Modester. Kila wakati alikuwa akikaa mpweke na mnyonge huku analia.
Kilichomfanya alie zaidi ni pale alipokuwa akizitazama picha alizopiga wakati akiwa mzima na miguu yake akifurahia maisha na watu wengine!
“Modester…” Emiliana aliongea kwa kuita. “Hupaswi kuwa unalia kila muda dada’angu!” Alimwambia.
“Emmy… inaniuma…sikuzaliwa hivi!”
“Imekwisha tokea…huna budi kukubaliana na hali halisi.”
“Nashindwa kuukubali ukweli…kuna muda najifikiria kuhusu chuo…nitasomaje?”
“Mbona kuna walemavu tunaona wanasoma!”
“Lakini kwa shida! Haitakuwa kama nilivyokuwa na miguu yangu. Ila pia ninafikiria kuhusu wanangu nitakapo wazaa…nitaishi nao vipi nami nikiwa kwenye hali hii?!”
“Mo’ sisi tupo…”
“Hamuwezi kuwepo kwenye maisha yangu yote Emmy…kuna muda mtatakiwa kuangalia ya kwenu…”
Emiliana alikosa la kusema.
Modester akaendelea huku machozi yakimbubujika;
“Kiukweli Emmy inaniuma sana…inafika wakati najiuliza kwa nini mimi tu kila kitu kwenye maisha yangu kinakuwa mtihani?…Sina furaha ya kudumu…simjui baba…mama yangu alikufa nikiwa mdogo…na leo nimekuwa mlemavu!…Inaniuma…inaniuma sana Emmy…” Modester alianza kuangua kilio cha uchungu.
Emiliana naye machozi yalimbubujika kutokana na huruma aliyokuwa akimuonea Modester. Akamsogelea kwenye kiti chake kile cha magurudumu na kumkumbatia akimgawia kipande cha faraja.
Akamwambia;
“Baada ya mlima mkali, mbele kuna mteremko Mo’, huwezi jua…pengine kesho yako itakuwa ni yenye kukufuta machozi…muachie Mungu kila kitu!”
Modester alizidi tu kulia Emiliana akimbembeleza bila kuchoka.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 12

Siku zilizidi kusonga mbele na ujauzito wake ulizidi kukua. Na huo ndio ulio geuka kuwa faraja yake kubwa, Modester aliamini kwamba atakapo jifungua wanae mapacha alioambiwa kuwa amewabeba baada ya kufanya kipimo cha utlasound, wangemfariji pale ambapo angekuwa akiwaona. Akapanga kuwapenda wanae hao kuliko kitu chochote kile duniani.
Lakini akiwa katika mategemeo hayo, mambo yakaanza kubadilika kwenye familia ile. Ule upendo ambao alikuwa akiuona mwanzoni baada ya kuwa kwenye hali hiyo ya ulemavu aliyokuwa nayo, ukaanza kuyeyuka taratibu.
Na suala hilo alianza kuliona kwa mama yake Emiliana. Huyo ndiye alianza visa. Kumsema kwa vijembe, na kijembe kilichomuuma zaidi ni pale mwanamke huyo alipomwambia mbele ya uso wake kwamba kwa sababu mwanae Jackson alikuwa amekufa, naye ilikuwa ni haki yake asote kwenye kiti kile cha magurudumu.
Hilo lilimuuma sana Modester. Akaona anageuziwa kibao kwenye jambo ambalo yeye ndiye angepaswa kulaumu kwamba mwanae huyo marehemu ndiye kamsababishia matatizo hayo aliyokuwa akiyaishimo. Lakini anageuziwa kibao yeye? Aliumia mno! Ila hakuwa na budi ya kujivika roho ya paka, na kuwa mvumilivu.
Hatimaye miezi tisa ikafika na msichana huyo akajifungua watoto mapacha wa kike. Akawaita Magdalena na Mariam Daud!
“Hongera sana…” Emiliana alimwambia.
“Asante Emmy!” Alijibu.
“Umefanana kweli na wanao!”
Modester alitabasamu.
“Mbona mi’ naiona sura ya Daud!”
“Mh! Mi’ naona wamemchukua tu pua!”
“Ha! Ha! Haa!” Modester alicheka. “We’ kweli hujui kufananisha.” Alimwambia.
“Ila ni wazuri!”
“Nashukuru mpenzi hawa ndio faraja yangu…”
Akimaliza kuyasema hayo Modester, mara mama Emiliana aliyekuwa kimya pembeni yao akiwasikiliza, alikwangua koo lake kama mtu aliyetaka kuzungumza. Modester na Emiliana wakaendelea kubaki kimya…
“Na tutaona hao nyau wako utawalelea wapi…!” Alibwata.
“Mama!” Emiliana aling’aka kwa mshangao.
Modester naye alihamanika kuliko kawaida.
“Si’ wanakwao?” Mama Emiliana alisema kwa kiulizo akimtazama mwanae. “Awapeleke kwao.” Aliongeza na kuondoka kitandani pale alipokuwa amelala Modester na wanae, hospitalini Amana huku Emiliana akiwa amekaa pembeni yake.
Modester alimeza mate ya uchungu akijaribu kuzuia machozi yasimbubujike.
Emiliana alibaki kimya akimtazama akishindwa aseme nini! Maneno ya mama yake hata yeye yalimvuruga, ni wazi yalikosa staha, utu na hata huruma. Ukimya wa muda ukajikita. Wakiwa katika ukimya ule Emiliana bila kutegemea alimsikia Modester akiimba…

“Hakuna kitu kibaya sana humu duniani kama shida....

Emiliana alimakinika naye. Akamsikia Modester akiendelea;

Shida haichagui mtu, siku wala mwaka, hohoo...
Haina katu taarifa, shida huingia shida bila hodi...
Si mtoto wala mkubwa, wote shida, ohooo...
Kila siku shida shida haiishi mpaka siku ya mwisho....

Machozi mengi yalikuwa yakimbubujika Modester wakati akiimba kipande hicho cha ubeti kutoka kwenye wimbo uitwao Shida wa Mbaraka Mwishee! Emiliana pia lilianza wingu la machozi kumfumba macho yake, kisha yakaanza kumbubujika kwa wingi. Donge la uchungu likawakaba moyoni wawili hao wakaanza kulia pamoja.
Walilia pasipo mfano!

***

AKIWA mnyonge katika hali hiyo ya kutoelewa nini ilikuwa inakwenda kuwa hatima ya maisha yake, Modester alirudishwa nyumbani, baada ya wiki moja tu za kujifungua. Aliporudi nyumbani jambo la kwanza alilofanya ilikuwa ni kumuomba Emiliana, amsaidie kwenda nyumbani kwao Daud, kwa walezi wake kuwaeleza juu ya taarifa zile za yeye kujifungua.
Emiliana alikwenda.
Baada ya siku tatu za kuwapa taarifa, alifika mjomba wake Daud na mkewe kwa ajili ya kuwaona watoto na kutoa vijizawadi vingine. Wakaongea mengi na Modester. Msichana huyo hakuwaficha pia juu ya hali halisi ya mazingira aliyokuwa anapitia. Akawaomba uwezeshwaji, wa kupangishiwa chumba na wanae ikibidi pia afunguliwe kibiashara kidogo awe anafanya cha kumsaidia yeye na watoto wake.
Wawili wale walimuahidi mambo mengi, lakini baada ya kuondoka siku hiyo hawakurudi tena. Hata alipo wafuatilia kwenye simu, hawakuonyesha kuwa ni watu ambao wangemsaidia.
Hakuwa na namna aliachana nao!
Mambo yakazidi kuwa magumu kwa upande wa Modester. Maisha ya nyumbani hapo kwao Emiliana yakazidi kuwa machungu siku hadi siku. Visa vikawa havikatiki. Wakati mwingine akiwa anapika uji wa wanae bila sababu yoyote, mama Emiliana akawa anaumwaga. Ilimradi visa tu. Akikuta kitu hakipo sawa na Modester kuonekana ndiye kasababisha, bila hata kujali ulemavu wake alimuosha matusi ya kumlowesha chapachapa na akafikia hatua ya kuvunja chupa za wanae za kuwekea uji. Ulifika wakati Modester alikata shauri. Akakata na tamaa kabisa ya kuendelea kuishi, akawaza awaue wanae na kisha ajiue yeye kuliko kuendelea kuishi kwenye mateso yale.
Lakini akiwaza hayo na kuwatazama wanae, alijikuta akipatwa na huruma ya ajabu mno.
“Kwa nini niwaua malaika hawa?” Alijiuliza. “Sijui ni nini makusudi ya Mungu kuwaleta duniani, kwa nini niwaue?”
Akaiona hiyo ni roho chafu iliyo muingia. Akayatupilia mbali mawazo yale! Akapata mawazo mengine, kuondoka nyumbani hapo kwa kina Emiliana na kuelekea mitaani.
“Hapana usifanye hivyo…” Emiliana alimsihi baada ya kumkuta akikusanya vinguo nguo vyake na kumweleza juu ya azma yake ya kuondoka!
“Acha tu Emmy…ngoja niende huko nikahangaike, ni yale yale hata hapa sina furaha!”
“Utaishije na watoto mtaani…ndio kwanza wana miezi saba?”
“Mungu atatulinda.”
“Mo’!!”
“Emmy nashukuru kwa upendo unao nionyesha sitakusahau kwenye maisha yangu…Mungu akubariki usije kuwa na roho kama hii ya mama yako kwa kizazi chako…ila mimi yamenishinda…wacha tu niende…”
“Ngoja nimweleze baba…pengine atatafuta namna ya kukusaidia…!!”
“Hapana usifanye hivyo…kumbuka yaliyotokea baada ya kumweleza juu ya ujauzito na masuala yangu na Jackson…siunakumbuka yaliyo tokea….leo hatuna Jackson na mimi ni mlemavu…hatuwezi jua nini kinatokea baada ya hili la sasa…acha tu Emmy!”
“Jamani…roho inaniuma sana Mo’!”
“Najua…hata mimi naumia! Lakini nitawezaje kuendelea kuishi katika hali kama hii?”
“Basi vumilia vumilia hata watoto wajiweze!”
“Usijali…nipo nao. Hakuna kitakacho haribika.”
“Mo’ usiondoke…!”
Emmy alilia sana.
Msichana huyo pamoja na yote yaliyotokea kikiwemo kifo cha kaka yake, alikuwa akimuonea huruma mno Modester kwenye hali aliyokuwa anapitia na hakupenda kutengana naye. Alimsihi mno asiondoke, lakini Modester hakubadilisha uamuzi huo. Alikuwa amekwisha fikia hatua ya kukubali kwamba liwalo na liwe, litakalo mtokea na limtokee lakini si kuendelea kuishi kwa mateso ya namna ile pamoja na watoto wake nyumbani hapo kwa kina Emiliana.
Akatokomea mtaani!

ITAENDELEA…
 
SEHEMU YA 13

MAISHA ya mtaani kwa Modester yalikuwa ni magumu mno, hasa ukizingatia hali ya ulemavu aliyokuwa nayo. Ilikuwa inamuwea vigumu hata kumudu kuwalea watoto wake wale wawili.
Ili ajisukume kwa baiskeli yake ile ya magurudumu ilikuwa ni lazima awafunge watoto wake mmoja mgongoni, mwingine kifuani na ndipo aanze kujisukuma kukatiza mitaani.
Magari na vyombo vya usafiri vikawa vinamkosa kosa kumpitia pale alipotaka kuvuka barabara, akajikuta akiishi maisha ya roho mkononi kweli. Jua likawa ni la Modester na mvua ikawa ni yake.
Kila asubuhi alikuwa akienda kuombaomba kwenye mitaa ya Kariakoo na kituo chake kikawa nje ya Kituo cha Polisi Msimbazi, jioni alijisukuma kwa baiskeli yake ile ya magurudumu na kwenda kulala mitaa ya jangwani, karibu na kilabu ya Yanga ndani ya magofu yaliyokuwepo enzi hizo pamoja na ombaomba wengine wasio na makazi na vijana wengine wa mtaani.
Taratibu akaanza kuyazoea maisha hayo. Lakini moyoni mwake hakuamini kwamba hayo ndiyo maisha ambayo angeishi siku zote za uhai wake. Modester aliamini ipo siku muujiza utatokea na ataweza kutoka mtaani na kuwa na maisha mengine!
Akaanza pia kuzoeana na ombaomba wenzake na wakawa wanazungumza juu ya simulizi zao za kuumiza zilizowakuta maishani mpaka zikawafikisha pale.Kila simulizi aliyosikiliza ilikuwa na uzito wake.
Kuna simulizi nyingine zilimgusa kiasi kwamba akaona aliyopitia yeye yalikuwa na nafuu!
Maisha yakaendelea, miongoni mwa vijana ambao Modester alizoeana nao, alikuwa ni Musa, kijana chokoraa ambaye alikuwa anaokota makopo mtaani na mtumia dawa za kulevya. Kijana huyo kuna muda akili zake ni kama zilikuwa zinafyatuka na muda mwingine alikuwa akionekana sawa!
Kilichofanya Modester azoeane na Musa, ni baada ya kijana huyo kumsaidia siku moja ambapo vijana wahuni walitaka kumuibia kwa nguvu vijisenti alivyopata kutokana na kuombaomba.
Kutokana na hilo alilolifanya, wakazoeana. Mazoea yao yakakuwa na wakawa wanaitana kaka na dada!
Kabla ya mazoea hayo Musa alikuwa analala eneo la mbali kidogo na alipolala Modester, lakini kutokana na mazoea yaliyojengeka kati yao, akahama alikokuwa analala akawa analala naye karibu kwa ajili ya kumsaidia pia kuwalea watoto wake.
Lakini pia Musa ndiye akawa mpishi, pale Modester anapoombaomba na kurudi na chochote, kama Musa hakurudi na kitu, basi alitoa alichopata na kumpa, naye akaandaa chochote wakala!
Siku zikasonga mbele…

SIKU moja, majira ya katikati ya mwaka mawingu yalitanda kweli kwenye anga la Jiji la Dar es Salaam. Jambo lililowafanya ombaomba na vijana waliokuwa wanaishi kwenye yale magofu ya karibu na klabu ya Yanga warudi mapema kwenye makazi yao kuangalia usalama na vitu vyao ili mvua itakapo anza kunyesha isiviharibu.
Modester alipofika katika eneo hilo alimkuta Musa akiwa amekwisharudi lakini alikuwa anatetemeka vibaya mno. Modester alipomuangalia, akajua moja kwa moja ‘kaka’ yake huyo hajapata unga, au kuvuta bangi alizokuwa anatumia ndio maana alikuwa katika hali ile. Modester alitikisa kichwa kwa masikitiko. Akakumbuka namna ambavyo huwa anamsihi Musa aachane na matumizi hayo ya dawa za uraibu, lakini kijana huyo hakuwa anamsikiliza. Moyoni akamlaumu kwa kitendo hicho cha kutomsikiliza kinachopelekea mpaka anakuwa kwenye hali hiyo aliyokuwepo wakati huo.
Lakini mwisho wa siku alimuonea huruma hasa akikumbuka wema ambao alimtendea na namna ambavyo amekuwa akimsaidia kuwalea wanae na kupika. Kwa hiyo Modester akaamua kuchukua pesa kidogo kati ya alizokuwa nazo akampa Musa ili akajitibu ugonjwa wake ule.
Musa akapotea. Modester naye akaendelea na utaratibu mwingine. Baada ya muda wa takribani nusu saa, tangu Musa aondoke, mvua ilianza kunyesha. Kukawa na mtafutano kwenye eneo lile maana halikuwa na paa. Ombaomba na watu wengine waliolitumia wakaanza kuelekea kwenye maeneo ambayo wangeweza kujikinga.
Kwa upande wa Modester alipata wakati mgumu kweli kusota na wanae kwenye baiskeli yake ile ya magurudumu. Mvua ilikuwa inapiga ya upepo, watoto nao wanalia, sehemu aliyotakiwa kupita na baisikeli yake maji yakawa yanapita, ikawa ni shida juu ya shida.
Akizidi kuhangaika ni wapi aelekee kuna kijana mmoja alimuona ambaye hua anakua na Musa mara nyingi hasa wanapozunguka mitaani kuokota makopo. Akamuita.
“Wewe…” hakuwa anamjua jina.
Ile sauti ilikwenda ikakita kwenye ngoma za masikio za yule kijana akageuka.
“Naomba msaada wako…” alimsihi,
“Oh!” Yule kijana alihamanika. “Kumbe sister!” Akasema na kurudi mbio kisha akawachukua watoto wa Modester.
Akawakimbiza kuwaepusha na mvua na kuwaficha kwenye ‘chimbo’ alilojua yeye kisha akamrudia Modester, kijana huyo akambeba mgongoni na kumpeleka kule aliko wachimbia wanae.
Hali aliyoikuta huko ilitisha!
Ilikuwa ni kwenye korido ya wavuta bangi na watumiaji wa dawa za kulevya wakiendelea na mambo yao. Modester alitoa macho kwa mshangao akiwatazama watu wale.
“Sister hapa safi…hamna gozi wala nini…we’ chuna tu!” Yule kijana aliongea kwa maneno ya kihuni.
Modester alimeza mate ya woga akimwemwesa macho. Na kutokana na hali halisi ya mvua, hakuwa na namna, ikabidi ajikunyate na wanae kwenye kigunia walichokuwa wametandikiwa mahali hapo. Akajilaza.
Mvua iliendelea kuongezeka kunyesha ikiambatana na ngurumo za radi na upepo. Ilizidi kuwa kubwa kadiri muda ulivyokuwa unasonga mbele. Modester akiwa kimya mahali hapo baada ya watoto wake kulala, hatimaye naye usingizi ulimpitia.
Akiwa amelala ikamtokea hali ya kama ndoto. Akaota ameshikwa na watu watatu kwa nguvu, na wako wanalazimisha kumbaka huku watoto wake wale mapacha wakiachia kilio kikali. Modester katika hali ile ya kufurukuta akipambana na watu wale, akaona anachaniwa nguo ya ndani baada ya zile za nje kuraruliwa vibaya na mmoja kati yao akaanza kumuingilia.
Akaanza kupiga kelele za uchungu na kuomba msaada wakati jamaa yule akishughulika. Wakati jamaa huyo akizidi kumshughulikia akionekana kufikia hatua ya kulifurahia tendo lile la kikatili alilokuwa anafanya Modester akakurupuka pale alipokuwa amelala.
Haa!
Kumbe haikuwa ndoto na alikuwa kweli anabakwa na yale mavuta bangi. Mschana huyo baada ya kugundua haoti alizidi kupambana kwa nguvu ili kujaribu kujinasua mikononi mwa watu wale, lakini walimzidia nguvu, wakambaka watakavyo mpaka walipotosheka tena wakishirikiana na kijana aliyemsaidia kumpeleka kwenye ‘chimbo’ hilo. Modester alipata maumivu makali mno, na alilia kwa uchungu sana mbele ya watoto wake waliokuwa wanapiga kelele!
Baada ya kumaliza kutenda tukio hilo wahuni wale walitokomea kusiko julikana!

“SISTER,” ilikuwa ni sauti ya Musa akiongea kwa mshituko baada ya kumuona Modester akigaragara chini pamoja na watoto asubuhi ya siku iliyofuata baada ya kunyesha mvua kubwa!
Hapo, Musa alikuwa amemuona baada ya kumtafuta sana usiku uliopita bila mafanikio baada ya kurudi kutoka kwenye ‘chimbo’ lake la kutumia dawa za uraibu.
Musa alisogea mpaka alipokuwa Modester.
“Nini kimekupata sister?” aliuliza akiwa kwenye hali ya hamaniko. Modester alikuwa analia kwa sauti iliyokauka.
Musa alipomtazama vizuri akagundua michirizi ya damu iliyoganda katika mwa mapaja ya msichana yule.
“Dah!” Alisema kwa kutoamini. “Wamekubaka…” akabwaga tusi la nguoni.
Kisha akamuinua Modester na kwa shida akamrudisha kule kwenye makazi yao akiwa amewabeba pia watoto wale wa Modester, Magdalena na Mariam, mmoja akijifunga mgongoni kwa kanga iliyochoka, mwingine akimbeba mkononi. Akatafuta maji na kumsafisha. Kijana yule akaenda kwenye duka la dawa baridi akanunua vidonge vya maumivu akamletea Modester.
Modester akanywa.
Alipomuona anapata nafuu kidogo ndipo alipoandaa chakula wakala.
“Ni kina nani wamekufanyia hivi?” Musa alimuuliza.
Modester alimsimulia.
Musa alibwaga tusi kubwa la nguoni baada ya simulizi ile.
“Lazima niwatafute,” alisema kwa ghadhabu.
“Musa…achana nao,” Modester alimwambia akizungumza kwa shida na kwa sauti kavu kutokana na sauti yake kukauka kwa kilio.
“Hawawezi kukufanyia hivi sister nikawaacha…haiwezekani!”
“Ndiyo wamekwishafanya achana nao tu…”
Musa alishika kichwa na kujilaani kwa nini aliondoka mahali hapo, na kumuacha ‘dada’ yake huyo mpaka masaibu yakamkuta!
Hilo nalo likapita kama mengine yalivyopita kwenye maisha ya Modester…

ITAENDELEA…
 
SEHEMU YA 14

WATOTO wake nao walizidi kukua japo kwa shida. Hatimaye wakafikisha mwaka mmoja na nusu akiwa nao hapo hapo mtaani.
Ingawa alikuwa anakula nao msoto wa hatari, wakikutana na masaibu ya kuumiza ya kila aina mitaani, lakini kuwa nao karibu na kuwatazama wanae, ndio ilikuwa furaha ya Modester, na alikuwa anawapenda kuliko kitu chochote.
Sasa, wakati wanatimiza umri huo, ilikuwa imepita kipindi cha miezi miwili tangu Modester afanyiwe ule unyama wa kubakwa.
Ingawa taratibu alikuwa ameanza kulisahau tukui hilo, lakini kuna jambo lilianza kumtia hofu. Nalo lilikuwa ni ujauzito!
Mwezi wa kwanza baada ya kubakwa, hakuingia kwenye mzunguko wake. Kutokana na majira kubadilika, mvua za hapa na pale kunyesha, Modester alifikiri pengine majira yalibadilika na mzunguko huo, lakini mwezi wa pili nao ukapita kavu bila kuingia kwenye mzunguko, jambo hilo likamuweka roho juu.
Ikabidi amuagize Musa, amnunulie kipimo cha mimba kwa njia ya mkojo. Musa alifanya hivyo na alipomletea Modester alifanya kipimo hicho kwa sababu alijua kukisoma.
La haula!
Alijikuta ni mjamzito!
Macho yalimtoka. Akili nayo ikamzunguka. Moyo ukampasuka na akaiona shida kubwa mbele yake.
Mtoto wa tatu tena asie na baba?
Alijiuliza akahisi na nguvu zikimuisha. Alipofikiria mateso makali aliyokuwa anapitia na watoto wake hao mapacha, roho ikazidi kumuuma zaidi, akajikuta machozi yanambubujika na akaanza kulia. Modester alilia sana akiwalaani vijana wale waliombaka.
Hao ndio aliona wamezidi kumsababishia masaibu kwenye maisha yake. Mbaya zaidi kati yao hawezi kujua ni yupi alie mpa ujauzito. Na kwanza ulikuwa ni usiku wenye giza alipotendewa tukio lile, kwa hiyo hata kama huwa anawaona vijana hao hakuna anayemkumbuka. Kwa mara nyingine kwenye maisha yake Modester, alizielekeza lawama kwa muumba wake. Akimhoji kwa nini alikuwa anaruhusu kila gumu limfike yeye tu!
Katika suala hilo, Musa ndiye aliyekuwepo kumtuliza baada ya kumshirikisha.
“Sister watoto ni baraka…” Musa alimwambia.
“Sio kwa hali yangu Musa, unafikiri nitaishi nao vipi?”
“Tutasaidiana tu…usijali!”
“Mzigo unazidi kuwa mkubwa!”
“Aah! Sasa utafanyaje, utaitoa?”
“Siwezi kuitoa.”
“Basi komaa nayo kibigwa!”
Kweli Modester akakomaa na ujauzito huo kibingwa. Lakini ulimuweka kwenye wakati mgumu sana wa mawazo. Kila nukta alipojifikiria kwamba ni mjamzito wa miezi miwili alijikuta akihisi kupagawa na machozi yakambubujika.

“HABARI za leo dada,” mtu mmoja alimsalimia Modester, siku moja akiwa nje ya uzio wa Kituo cha Polisi cha Msimbazi, akiwa amejianika kwa ajili ya kuombaomba. Pia alikuwa ameshika tama kutokana na mawazo aliyokuwa nayo juu ya ujauzito aliobeba.
Modester alitoa mkono shavuni na kuinua uso taratibu kumtazama mtu huyo alie msalimia. Alikutana na sura ngeni machoni kwake, ya kijana alie vaa kitanashati.
“Nzuri…” Modester aliitikia kwa sauti iliyosikikia chini, bado alikuwa akijiuliza maswali mengi dhidi ya huyo kijana.
“Samahani…” huyo kijana alisema; “Naitwa Amos…” akajitambulisha.
Modester alitanua macho kwa ishara kwamba anamsikiliza.
“Natokea kwenye taasisi inayojihusisha na kusaidia watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu kwa kuwatafutia wafadhiri, inaitwa Compassion ipo chini ya Kanisa Anglican, sijui kama umewahi kuisikia?” Alimuuliza.
Modester akafinya macho.
Compassion…Anglican…!
Vitu hivyo vilipita akilini mwake.
“Ndiyo,” alijibu kwa upole kimoyo kikimdunda.
“Sawa…sasa kuna kitu napenda nikushirikishe,” Kijana huyo aliongea huku akichutama pembeni yake, jambo lililomaanisha hilo alilohitaji kumshirikisha hakutaka lisikiwe na wengine. Hali ya butwaa ikawa inaendelea kumchukua Modester.
“Kitu gani?” Aliuliza.
“Kabla sijakushirikisha naomba nitoe angalizo…” huyo kijana alisema kwa sauti ndogo lakini iliyosikika. “Kama hutakuwa tayari…tafadhali nijibu tu sipo tayari…yasiwe mambo mengi…siunajua hapa ni mjini…kikitokea kitu kidogo watu hawachelewi kujaa!”
Modester alijikuta akiguna moyoni kutokana na angalizo hilo.
Akajiuliza ni jambo gani anaenda kuelezwa mpaka liwe na angalizo la namna ile?
“Na jambo lenyewe linahusu nini?” alijikuta akiuliza.
“Nafanya kazi kwenye hii kampuni ya Compassion kama meneja…,” Amos alitoa kitambulisho na kumuonyesha.
“Mkh…” Modester akamruhusu aendelee kwa hali ya mguno baada ya kutazama kile kitambulisho.
“Kutokana na nafasi niliyo nayo…nimejikuta nikitengeneza wigo mkubwa wa marafiki katika nchi mbalimbali. Nina rafiki zangu wapo Holland, ni mtu na mkewe na ni watu wazima wa kuitwa wazee.
“Hawa watu, hawajabahatika kupata watoto katika maisha yao, na walikuwa wanahitaji watoto wa kuasili kutoka Afrika. Ndio wakawa wameniomba mimi msaada wa kuwatafutia. Lakini wakiwa na kigezo kwamba wanataka watoto mapacha.
“Wapo tayari kutoa pesa yoyote ile mtu atakayo ihitaji ilimradi iwe ndani ya uwezo wao. Sasa, nilikumbuka huwa nikipita hapa ninakuona, ndiyo maana nikaamua kuja kuzungumza na wewe!”
Modester alibaki ameganda akimtazama huyo kijana mbele yake. Wakawa wanatoleana macho wakati maneno yale yakigonga kichwani kwake.
“Kwa hiyo…wewe huko kwenye taasisi yenu hakuna watoto wa kumpa?” Akauliza kama mtu anayetengeneza hali ya ushari.
“Sio kwamba hakuna, lakini nielewe…taasisi yetu inajihusisha na kuwatafutia watoto wafadhiri…hawa watu wanatafuta watoto wa kuasili…hiyo ndio tofauti iliyopo. Ingekuwa wanatafuta watoto wa kuwafadhiri lingekuwa ni jambo ambalo linamalizikia ndani ya taasisi pale pale!”
Modester alishusha pumzi. Akabaki kimya kwa muda.
“Dada’angu nikwambie kitu…” yule kaka alimwambia Modester.
Modester akamtazama.
“Sio suala la kufikiria hapa kwa hapa na ukatoa jibu…unaweza ukaniambia muda ambao unataka nikuachie ufikirie juu ya hili…kisha nikaja kuchukua jibu,” alimwambia.
Lakini Modester alitikisa kichwa.
“Hapana…siwezi kuwauza wanangu…” alimjibu yule kaka.
“Imekaa hivyo…lakini fikiria kuhusu kuwasaidia hawa watoto kutoka hapa walipo. Ni kweli unafurahi kuwa nao…lakini nini kitakuwa mwisho wa maisha yao hapa mtaani? Unataka wanao wawe ombaomba kama wewe? Wawe machokoraa au waishie kubakwa na wavuta bangi na kuzalishwa? Fikiria haya pia,” Amos alisema kwa msisitizo.
Modester akahisi moyo wake ukipoa.
“Anyways…” Amos alisema. “Nitapita muda mwingine, nitafurahi kupata jibu lolote, ikiwa sio, basi…ikiwa ndio, ni kheri pia!”
Baada ya kusema hayo kijana huyo alisimama, akachomoa waleti yake na kutoa noti za shilingi elfu kumi tano, akampa Modester.
Modester alizipokea huku mikono ikimtetemeka. Kisha akamsindikiza kwa macho kijana huyo aliyepiga hatua akiondoka zake!

“DAAH!” Masika aliguna. Akasajili tabasamu hafifu usoni kwake. “Alikuachia mtihani mgumu sana,” alimwambia Bi Modester.
“Sana…” Bi Modester alimjibu.
“Kwa hiyo ukaamua nini sasa?” Masika akauliza.
“Kiukweli jambo hilo lilinivuruga sana. Kuna upande wa moyo wangu uliniambia pengine Mungu amewatuma kwenye maisha yangu na wanangu watu wale kuja kutuondoa mtaani kwa namna hiyo. Lakini upande mwingine nikawa nawaza kwamba nitakuwa na uhakika gani juu ya hilo.
“Je, kama watu hao si wema. Pengine wanahitaji watoto wa kuwatoa kafara na mambo mengine ya kidunia, maana yake si watoto wangu watakuwa wamekwenda hivyo! Nilihisi kukanganyikiwa,” Alieleza Bi Modester.
Akaendelea;
“Sikutaka kukaa tena pale Msimbazi…nilirudi kule kwenye magofu tulipokuwa tunalala. Nikiwa huko nilijifikiria sana kuhusu suala hilo. Nikapiga magoti na kumuomba Mungu anifunulie uamuzi wa kuchukua, kwa sababu nilikuwa katikati ya maamuzi.
“Kama alivyosema yule kaka, pia sikuhitaji maisha ya wanangu yaishie mtaani. Mambo niliyokuwa nakutana nayo yalikuwa ni makubwa sana. Kutukanwa, kubakwa, kukoswa koswa kuuawa na mengine mengi ya kuumiza sikutaka yawapate.
“Sasa kama ningewauza na huko wanakokwenda wakaishi vyema, wakikua wangekuwa na maisha yao na kizazi chao kingeishi vizuri. Jambo lingine nilifikiria kuhusu mtoto ambaye nilikuwa naye tumboni.
“Nikawaza, hizo pesa ambazo ninawauzia dada’zake si zingemfanya yeye azaliwe kwenye mazingira mazuri! Pengine hata maisha yake yangekuwa tofauti kabisa, angepata msingi mzuri wa elimu na baadaye akaweza kujisaidia kwenye maisha yake na kizazi chake!
“Lakini yale mawazo ya kwamba huenda wale si watu wazuri yakawa yananirudisha nyuma kufanya maamuzi,” alieleza Bi Modester.
Masika akabaki kimya akimtazama wakati bibi huyo akiokota kwa mara nyingine chupa ya maji na kulowanisha koo lake.
“Hukumshirikisha Musa?” Masika alimuuliza.
Bi Modester alijibu kwa kuzungusha kichwa akikataa huku akisukutua mdomo kwa maji na kuyameza kisha akaufunga mfuniko wa chupa ile ya maji.
“Sikutaka kumshirikisha Musa kwa sababu…nilipokuwa namshaurisha jambo lolote, halafu nikamjengea hoja ambayo hakuifikiria…alikuwa ananiambia maliza kibingwa…sasa wakati huu nilitaka nimalize kibingwa mwenyewe!”
Ha! Ha! Haaa! Masika alicheka.
Bi Modester naye akacheka, na mikunjo ya kizee ikasambaa usoni kwake.
“Kwa hiyo ukamalizaje sasa hiyo kibigwa?”
 
Duhhh.....
Sijawahi kuona Uzi mrefu kama huu.
Ebu atakae usoma wote alete summary tafadhali.
 
Back
Top Bottom