SEHEMU YA 29
Tuliona vespa, bajaji na magari yanayokokotwa na punda yakipita chini yetu. Nikawa natabasamu peke yangu.
“Yasmin unakuona kwetu?” nikamwambia Yasmin.
“Ahaa ndio hapa!” Yasmin akaniuliza.
“Hapa ni Zanzibar. Kisiwa hiki kinaitwa Unguja”
“Uliniambia wewe unatoka Pemba”
“Pemba ni kwetu na Unguja pia kwetu. Yote ni Zanzibar moja”
Yasmin akatabasamu.
“Nimefurahi kufika kwenu. Nitawaona wazazi wako na ndugu
zako”
SASA ENDELEA...
Wakati nazungumza na yasmin helikopta ilikuwa inatua kwenye kiwanja cha ndege. Tukaacha mazungumzo na kuchungulia kwenye madirisha. Tuliona jingo la kiwanja cha ndege kwa mbele. Pia tuliona ndege kadhaa zikiwa zimeegeshwa huku wafanyakazi wakienda huku na huko.
Helikopta ilipotua tulishuka
Kwa vile rubani alikuwa akifanya mawasiliano tangu tukiwa juu. Tulikuta maofisa wanne wa polisi wakitusubiri. Polisi tuliyekuwa naye aliwapa maelezo ya zoezi lililofanyika. Akawaeleza pia tulivyopatikana katika kile kisiwa.
Polisi hao walituchukua katika chumba kimoja wakaanza kuwahoji wale wazungu pamoja na mwendesha boti waliyekuwa naye. Baada ya wao kutoa maelezo lilikuja gari likawachukua. Tukaanza kuhojiwa mimi na Yasmin. Maelezo yetu ndio yaliyowaacha hoi maofisa hao.
“Unasema wewe ni bini wa rais wa Comoro na ulikumbwa na jinni aliyekupeleka katika hicho kisiwa mwaka mmoja uliopita?” Afisa mmoja akamuuliza Yasmin.
“Ndiyo”
Niliposema “ndiyo” maofisa hao walitazamana kwa mshangao.
“Hebu tueleze ulivyofikishwa katika kisiwa hicho kutoka Comoro?” Afisa huyo akaendelea kumuuliza.
“Sijui. Ninachokumbuka ni kwamba nilikuwa kwenye sherehe ya harusi yangu nikaanguka na kupoteza fahamu. Nilipozinduka nikajikuta niko katika kile kisiwa ndani ya lile jumba nililokuwa ninaishi” Yasmin aliendelea kueleza.
“Ulijuaje kuwa ulikumbwa na jinni?’
“Wakati nazinduka nilimuona jinni mwenyewe. Aliniambia anaitwa Harishi na kwamba yeye ndiye aliyenikumba na kunileta pale”
“Alikuwa anataka nini kwako?”
“Alikuwa anataka niishi naye kama mke wake”
“Na ukawa unaishi naye?”
“Sikuwa na la kufanya zaidi ya kukubali”
“Ulikuwa unapata wapi chakula na mahitaji mengine?”
“Alikuwa ananiletea yeye chakula na nguo”
“Anavipata wapi?”
“Aliniambia kuwa anaiba kwenye maduka”
“Wapi?”
“Alikuwa anazunguka sehemu nyingi za Afrika Mashariki pamoja na Comoro”
Tumeambiwa kwamba kisiwa ulichokuwa unaishi wewe hakina watu isipokuwa nyumba tupu, ni kwanini?”
“Harishi alinieleza kuwa watu waliokuwa wakiishi katika kisiwa kile aliwaua yeye kwa kuwafyonza damu na kula bongo zao. chakula chake kilikuwa damu na ubongo”
Maafisa hao wakatazamana tena kwa mshangao.
“Chakula chake kilikuwa damu na ubongo wa binaadamu?” Afisa huyo akamuuliza tena Yasmin.
“Ndiyo” Yasmin alimjibu.
“Kwanini wewe hakukula?”
“Mimi alinichukulia kama mke wake”
“Na tuliambiwa kwamba kuna watu saba ambao chombo chao kiliharibika baharini na walifikakatika kile kisiwa, ni kina nani?”
“Mmojawapo ni huyu hapa” Yasmin alinionesha mimi na kuongeza.
“Walifikapale wakiwa watu saba wakauawa na Harishi akabaki yeye peke yake”
“Kwanini yeye hakuuawa?”
“Kuna kisa kirefu kimepita”
“Tunataka tukisikie”
Yasmin akawaeleza yaliyotokea hadi tukaweza kumzamisha Harishi chini ya bahari akiwa ndani ya chupa.
Baada ya Yasmin kuhojiwa nilihojiwa mimi. Nilijieleza kuwa nilikuwa Mzanzibari na kazi yangu ilikuwa uvuvi. Nikaeleza jinsi nilivyofika katika kisiwa kile na kumkuta Yasmin ndani ya lile jumba.
Nilipomaliza maelezo yangu simu zilipigwa sehemu mbalimbali. Haukupita muda mrefu maofisa usalama wa ikulu pamoja na waziri wa nchi ofisi ya raisi walifika kiwanja cha ndege.
Baada ya kupata maelezo yetu, waziri wan chi alimuuliza Yasmin kama kweli alikuwa binti wa rais wa Comoro.
Yasmin akasisitiza kuwa alikuwa binti wa rais huyo na akaomba aunganishwe naye kwenye simu.
Taarifa za Yasmin zilipofika ikulu, Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi iliwasiliana na Wizara ya mambo ya nje ya Comoro.
Mpaka inafika saa kumi na moja jioni ndege ya serikali iliyotoka Comoro ikiwa imempakia kaka wa Yasmin ambaye alikuwa kanali wa jeshi pamoja na maofisa usalama wa ikulu ya Comoro ilitua kiwanja cha ndege cha Unguja.
Watu hao walipokewa na mkurugenzi wa usalama na kupelekwa kukutanishwa na Yasmin ambaye mpaka wakati huo nilikuwa pamoja naye.
Kaka wa Yasmin Kanali Umar Sharif Abdilatif alipomuona Yasmin alishituka. Na Yasmin naye alishituka. Walitazamana kwa sekunde kadhaa kabla ya kukimbiliana na kukumbatiana kwa furaha na majonzi.
Maofisa usalama waliotoka ikulu ya Comoro ambao walikuwa wakimfahamu Yasmin nao walishangaa walipomuona kwani taarifa zilizokuwa nchini mwao zilionesha kuwa Yasmin alipotea katika mazingira ya kutatanisha wakati wa harusi yake zaidi ya mwaka mmoja uliopita.
Baada ya maofisa hao kumsalimia Yasmin walithibitisha kwamba alikuwa binti wa Rais Sharif Abdulatif aliyepotea nchini mwao katika mazingira ya kutatanisha.
Wakati huo Yasmin alikuwa akitiriikwa na machozi kwa kumuona kaka yake.
Yasmin aliwaeleza masahibu yaliyokuwa yamemtokea, maelezo ambayo yalimshitua kaka yake pamoja na maofisa hao.
Baada ya kuthibitishwa kwamba Yasmin alikuwa binti wa Rais wa Comoro aliitwa ikulu pamoja na kaka yake. Yasmin aliomba na mimi niwemo kwenye msafara huo. Ombi lake lilikubaliwa. Nilipatiwa mavazi mengine tukapakiwa kwenye gari kupelekwa ikulu ambako tulikutana na rais wa Zanzibar.
Rais wa Zanzibar alimsikiliza Yasmin na kushangazwa na maelezo ya binti huyo wakati akimsimulia masahibu aliyokutana nayo.
“Hata hivyo wewe ni shujaa kwa sababu hukukata tama” Rais alimwambia Yasmin. Pia alinipongeza mimi kwa kunusurika kufa.
“Mkasa uliowakuta ni historia kubwa ya visiwa vyetu” Rais aliendelea kutuambia.
ITAENDELEA