MH! MISSED CALL YA SHEMEJI!-10
Beka, licha ya kujibalaguza ilifika mahali akajua amekwisha. Akili za haraka zilimwambia kwamba katika uzoefu wa kawaida, haijawahi kutokea akatumiwa meseji usiku na mtu, kwa hiyo aliamini ni dada wa mkewe tu huyo.
"Soma basi," alirudia Aisha.
"Kaka Beka mambo? Asubuhi pitia kwa mzee Ismail uchukue ule mzigo wako. Mimi wajina."
Beka alisoma meseji ya uongo kwa kuitunga kutoka kichwani kwake, mkewe akaamini lakini akamuuliza…
"Ni mzigo gani kwani?"
"Kuna boksi la tende."
"Ooo! Halafu jana huyo wajina wako nilikutana naye pale msikitini, akasema nikupe hai."
"Okey."
Beka alipoisoma ile meseji sawasawa, iliandikwa na shemeji mtu na ilikuwa ikisema…
"Piga ua galagaza, alfajiri njoo chumbani uniamshe na joto lako tamu! Mwaaa…"
Kichwani alikasirika kidogo kwa vile aliamini shemeji yake huyo ana akili timamu kwa hiyo alijua ubaya wa kutuma meseji kama ile usiku tena akiwa kitandani na mke wake.
"Kichaa sana huyu shemeji," alisema moyoni.
***
Saa kumi na moja na nusu, Beka alitoka chumbani kwake akiwa ndani ya bukta tu hadi sebuleni. Aliangalia kulia na kushoto na kubaini hali ya utulivu na amani, akanyata kwenda kwenye mlango wa chumbani kwa shemeji yake…
"Sijui mlango uko wazi?" alijiuliza baada ya kuufikia mlango huo. Alisita kwa muda mrefu hapo mlangoni kama vile alikuwa akijua ndani kuna mwanaume mwingine sasa alikuwa akimsikilizia.
"Lakini ni kwa nini moyo unasita sana kuingia? Kuna balaa nini? Na kama kuna baya ni kutoka kwa nani sasa? Mimi nadhani nisiingie," alisemasema mwenyewe pale mlangoni lakini moyo wa kuingia ukashinda, akafungua mlango na kuzama chumbani.
Shemeji mtu alishtuka kuona mlango umefunguliwa, akainuka kutoka kitandani na kukaa kwa kunyoosha miguu."Afadhali umekuja, baridi sana," alisema shemeji mtu huyo huku akiwa hayumo ndani ya shuka wala kanga halafu eti anasema kuna baridi! Kivipi? Ilikuwa ni zaidi ya baridi.
Beka alipanda kitandani huku akisema…
"Lakini shemeji leo nimekuja huku najisikia uvivuuvivu sana, sijui kwa nini?"
"Hamna bwana, wewe unataka kuninyima joto," alisema shemeji mtu huku akimparamia mume wa mdogo wake maana alianza kuhisi anamtolea visingizio ili amwache na njaa yake.
Walilala kiubavuubavu wakiangaliana. Wakaanza kushikanashikana mwilini huku wakinong'onezana maneno ya mahaba kama vile wao ni wana ndoa tena wako wenyewe tu.
Shemeji mtu ndiye aliyetangulia kupata moto wa mahaba, akamvutia kwake kijana huyo, wakaingia uwanjani na kuianza mechi kwa kasi na standadi.
Dada wa Aisha ilikuwa kama amedhamiria kumjulisha mdogo wake nini kipo kati yao kwani aliweweseka kwa sauti hadi kufumbwa mdomo ili sauti hiyo isitoke nje.
"Sasa shemeji kama ukisikika itakuaje? Si atakuja huku na kutukuta?" Beka alisema.
"Na mimi si mimi bwana, ni munkari wa mahaba umenipanda mwenzio."
Maneno hayo pia aliyasema kwa sauti licha ya kwamba Beka alimtaka asipige kelele.
***
Aisha alishtuka kitandani na kukuta kweupe. Alishangaa!
"Huyu ameshaamka?" alijiuliza.
Alitega masikio ili kusikia kama mumewe aliingia chooni maana chumba chao kilikuwa ‘self contain'. Ukimya ulitawala hali iliyoashiria kwamba hakuwemo mle bafuni wala chooni…
"Baby…baby," alijaribu kuita kwanza ili kujiridhisha.
Akatoka kitandani na kuifuata simu yake kisha akaitupia macho…
"Mh! Saa kumi na mbili na dakika tatu. Mbona si kawaida yake saa hizi awe nje!"
***
Beka na shemeji yake walipitiwa usingizi baada ya mzunguko wa kwanza wa mechi, wakalala kabisa. Hakuna aliyekuwa na habari na dunia inakwendaje!
Baby," Aisha aliita sasa akiwa amefika sebuleni ambapo hakuona dalili yoyote kwamba mumewe alifika hapo…
"Baby," aliita kwa sauti ya juu sasa, akashtuka kutoka kwenye chumba cha shemeji yake. Kidogo aitikie ‘sema', kushtuka hivi kumbe alikuwa kwenye mchepuko.
"Mh! Shemeji tumefumwa," alisema Beka, shemeji yake naye akashtuka…
"Mungu vile tumefumwa," alisisitiza akitoka kitandani. Akavaa bukta yake na kwenda kuushika mlango. Aliposikia sauti inatokea sebuleni alirudi, akajishika kichwa na kuanza kujuta…
"Nilisema mimi, dalili zilishaonesha kwamba kuna balaa. Ndiyo hili sasa."
"Beka," Aisha aliita tena, sasa alibadili jina.
"Shemeji ingia chini ya kitanda," shemeji mtu alimwambia Beka huku akifunua godoro, akabinyua chaga za upande mmoja. Beka alizama ndani yake, ile anamalizikia tu, Aisha akagonga mlango…
"Dada," aliita kwa sauti iliyojaa utulivu.
Dada yake alirudisha chaga polepole kisha akafunika godoro vizuri na kurudishia shuka kama awali…
"Dada."
"Ee."
"Samahani, nina shida."
Dada mtu huyo alifungua mlango na kusimama katikati akijifanya hajui shida ya mdogo wake…
"Beka simwoni humu ndani dada."
"Ndani wapi?"
"Chumbani. Nimekuja sebuleni hayupo, nimekwenda bafuni, chooni kote hayupo."
"Kwa hiyo yuko kwangu siyo?"
"Sina maana hiyo dada. Kwani we huoni kuwa ni tatizo? Nimekwambia ili tusaidiane kujua alipo."
"Ohoo! Nilidhani unamaanisha yuko kwangu. Maana umesema sehemu nyingi umemwangalia hayupo. Nikasema makubwa! Kwani ametokaje?"
"Nadhani mimi nilikuwa sijaamka."
"Simaanishi hivyo, namaanisha alipotoka amevaa nini?"
"Naamini ametoka na bukta tu, maana haipo na ndiyo huwa anaivaa anapokuwa amelala. Mimi nahisi hajatoka nje ya nyumba hii."
"Unarudi palepale. Unaposema hivyo atakuwa wapi kama si kwangu sasa?"
"Dada tuyaache hayo, tumtafute."
"Simu yake?"
"Simu kaizima, ipo chumbani."
***
Kule chini ya kitanda, Beka alianza kupata maumivu kwani alijipinda sana kutokana na ufupi wa kitanda kiasi kwamba hakuweza kulala kwa kunyooka."
"Da! Ukisikia mateso ya kujitakia ndiyo haya. Sasa hapa kisa nini? Lakini kwa namna nyingine kisa ni yeye mke wangu na ugumu wake wa kunipa haki yangu."
***
Dada mtu alichukua kanga nyingine kutoka kwenye msumari nyuma ya mlango, akajifunika juu na kutoka. Lakini alipotoka tu, Aisha alinyoosha mkono akachukua funguo kwa ndani na kuufunga mlango huo kwa nje…
"Sasa tunaanzia wapi?" aliuliza dada mtu akiwa ameshafika sebuleni sasa.
"Humuhumu ndani dada."
"Uani ulikwenda?"
"Sijaenda."
"Sasa kwa nini usiende. Kule si ndiyo anaweza kuwepo maana ya Mungu mengi."
Aisha alikuwa kama hamuelewielewi dada yake kwa kauli zake. Mara aseme ‘kwa hiyo yupo humu kwangu?' mara ‘ya Mungu mengi.'
"Dada unaposema ya Mungu mengi una maana gani?"
"Nina maana labda yuko uani."
"Sasa atakwenda kwa njia gani wakati mlango umefungwa? Kama alitoka uani nani alifunga mlango kwa ndani baada ya yeye kutoka na humu ndani niko mimi, wewe na yeye tu?"
"Kwa hiyo bado una maana ni mimi nilifunga mlango baada ya yeye kutoka si ndiyo?"
"Ha! Dada bwana! Sina maana hiyo mimi."
"Sasa maana yako ni nini we Aisha?"
"Mbona una hasira dada?"
"Hata ungekuwa wewe ungepata hasira."
***
Kule chumbani, Beka alijua kwamba shemejiye na mkewe wametoka kwenda kumtafuta, akasukuma chaga kisha akatoka, akazirudisha vilevile. Alisimama chumbani humo na kuangaza huku na kule. Alijua akitoka atakutana nao. "Huyu mwanamke hajui kama niliwahi kupitia mafunzo ya kijeshi, sasa tangu lini askari anaweza kufumaniwa kirahisirahisi, mimi ndiyo Beka bwana nimezaliwa mjini na kukulia mjini!" Beka alizungumza moyoni kisha akapanda kwenye dari.
Alipozama, akarudishia mfuniko, akatambaa kwa upole akikumbuka kwamba, kuna mfuniko mwingine kwenye bafu chumbani kwake. Alifanikiwa kushukia huko bafuni ambapo alisimama kwa muda akihema kwa sana. Alivua bukta na kujimwagia maji.
Mlio wa maji bafuni ulimshtua Aisha, akaenda mbio chumbani na kumkuta mumewe anaoga…
"Beka," aliita Aisha kisha akatoka mbio kwenda chumbani kwa dada yake akijiuliza ataukuta mlango ukiwaje? Alishangaa kuukuta umefungwa kwa funguo nje lakini pia bado alijua kama mumewe angekuwa humo, asingeweza kutoka mpaka afunguliwe kwa nje na ndiyo maana yeye alifunga.
Alirudi tena hadi chumbani. Wakati huo dada yake alikuwa sebuleni akimshangaa. Alipokwenda chumbani kwake, dada mtu huyo alishangaa kukuta mlango umefungwa kwa nje na funguo ikining'inia. Akazama ndani na kuinua godoro hakumwona Beka!
"Mh! Huyu vipi? Yaani ametoka akaamua kuufunga mlango kwa nje? Mbona balaa, mkewe atajua," alisema moyoni.
Hakujua kama mlango huo ulifungwa na mdogo wake.
***
"
Ulikuwa wapi Beka?" aliuliza Aisha kwa sauti iliyopandwa na midadi…
"Chooni."
"Una uhakika?"
"Ningekuwa sina uhakika ningekwambia sijui nilikokuwa."
"Mimi nimeita sana hukuitika. Bafuni nimekuja sijakuona."
"Ulitaka niitike nikiwa chooni?"
Aisha alikosa jibu la moja kwa moja. Alitoka mpaka sebuleni na kumjulisha dada yake, alipomkosa akaenda chumbani na kumwambia kwamba, mumewe kumbe alikuwa chooni na sasa ametoka yupo bafuni anaoga.
"Kwa hiyo hakupotea kama ulivyokuwa unaamini?" aliuliza dada mtu huyo.
"Inawezekana."
***
Kulikucha, dada mtu huyo akawa na dukuduku la kutaka kujua shemeji yake alitokaje ndani ya chumba hicho mpaka mkewe akaamini? Akawa anamtafuta aongee naye kabla hajaenda kazini.