SEHEMU YA 109
Hakujua sababu iliyomfanya Fareed kufanya mauaji hayo, alishangaa, hakuona kama Bilionea Keith aliwahi kuzozana na mwanaume yeyote yule, kwa nini Fareed alimuua? Je, Fareed alijua kwamba polisi walikuwa njiani kufika hotelini hapo mpaka kuamua kumtoroka?
Na kwa nini hakumwambia ili watoroke wote? Kila alichokuwa akijiuliza, alikosa majibu.
**** Kila mtu aliyesikia taarifa juu ya kifo cha Bilionea Keith hakuamini, wengi walijua ni tetesi ambazo ziliandikwa kwenye mitandao ya nchini Misri ili kuishtua dunia, kwao, bilionea kama huyo kuuawa kizembe namna hiyo lilionekana kuwa jambo gumu mno.
Watu waliokuwa na ndugu zao nchini Misri waliwapigia simu, walitaka kufahamu kilichokuwa kimetokea, walitaka kujua ukweli juu ya jambo hilo. Waandishi wa habari wa CNN, BBC na wengineo wakawatuma waandishi wao nchini Misri kufuatilia kile kilichokuwa kikiendelea.
Walipofika katika Hospitali ya Sheikh Mazrui iliyokuwa pembezoni kidogo mwa Jiji la Cairo, wakakutana na madaktari ambao waliwathibitishia kwamba mtu aliyekuwa ameuawa alikuwa Bilionea keith.
CNN walipotoa taarifa hiyo ndiyo kila mtu akaamini kwamba kweli mtu huyo alikuwa ameuawa. Lilikuwa pigo kubwa, watu wengi walihuzunika kwani miongoni mwa mabilionea walipokuwa na roho nzuri duniani alikuwa mwanaume huyo, hakukuwa mtu aliyejua ubaya wake kwani kila alipokuwa katika umati wa watu, alijivisha roho ya kondoo na wakati alikuwa mbwa mwitu.
Kila mtu alitaka kujua kuhusu mtu aliyefanya mauaji, kila mmoja masikio yake yalikuwa kwa polisi wa nchini humo wakitaka kujua ni nani hasa alikuwa amehusika katika mauaji hayo na wakati huo muuaji huyo alikuwa wapi.
Polisi wa nchini Marekani, kupitia kitengo cha Interpool walikuwa wakiwasiliana kwa ajili ya kuufahamu ukweli na kujua mahali muuaji huyo alipokuwa. Kulikuwa na kazi kubwa, walipewa picha zake zilizopigwa kwa kutumia kamera za CCTV ambazo hizohizo ndizo walizokuwa wakizitumia.