SEHEMU YA 107
Haikuwa kawaida kwenye hoteli kubwa kama hiyo, akachungulia chini kupitia dirishani, alichoweza kuona ni kundi la polisi waliokuwa na bunduki wakiwa wamefika hotelini hapo na walikuwa wakiwasisitizia wafanyakazi waruhusiwe kuingia ndani ya vyumba vya hoteli hiyo.
“Mungu wangu! Wamejuaje kama nipo humu?” alijiuliza, hakupata jibu. Hakujua ni kwa jinsi gani angeondoka ndani ya hoteli hiyo, alibaki akitetemeka kwa hofu kubwa kwani kule chini ambapo ndiyo kulionekana kuwa rahisi kwake, pia kulikuwa na polisi.
“Nifanye nini? Mungu nisaidie,” alisema huku akiwa hajui ni kitu gani alitakiwa kufanya.
**** Maria alioga haraka sana, mwili wake uliwehuka, Fareed alimchanganya kupita kawaida, hakukuwa na kitu kingine alichokifikiria mahali hapo zaidi ya ngono tu. Alijisugua hasa, kuanzia chini, kati mpaka juu kuhakikisha mtoto wa kike anakuwa msafi.
Alipomaliza, akachukua taulo lake na kuanza kujifuta, tena huku akihakikisha anakausha maji ya kila sehemu. Alipohakikisha kila kitu kipo sawa, akaufungua mlango wa bafu na kutoka.
Chumbani hakukuwa na mtu, alijaribu kumwangalia Fareed huku na kule lakini hakuweza kumuona sehemu yoyote ile.
Hakujua mwanaume huyo alikwenda wapi, mara ya kwanza alihisi kwamba inawezekana aliamua kufuata chakula chini, hakutaka kumsumbua mhudumu lakini kitu cha ajabu kabisa, hata kibegi chake kidogo hakikuwepo chumbani humo.
“Mmmh!” aliguna.
Akaanza kumuita mwanaume huyo chumba humo, hakusikia kitu chochote, hakumuona, akaufungua mlango na kutoka ndani ya chumba kile. Akaanza kuwa na hofu, akahisi kulikuwa na mtu aliingia ndani ya chumba hicho na kumteka mpenzi wake huyo.
Akarudi chumbani na kuanza kuvaa nguo zake harakaharaka lakini hata kabla hajamaliza, akasikia mlango ukianza kugongwa kifujofujo hali iliyomfanya kuwa na hofu.
“Nani?” aliuliza kwa sauti.
“Fungua mlango!” alisikika mwanaume aliyekuwa nje ya chumba kile.