Michirizi ya Damu

Michirizi ya Damu

SEHEMU YA 124

Mzee Al Fakh alipokuwa akizungumza naye, aliongea kiupole mno kiasi kwamba wakati mwingine Fareed alihisi kwamba mzee huyo alikuwa malaika aliyejivisha mwili wa binadamu.

Akalala na siku iliyofuatia, Mustapha akafika nyumbani hapo ambapo akatambulishwa kwa Fareed na hivyo kumchukua tayari kwa kuondoka naye kuelekea sehemu na kupanga safari hiyo.

Nyumbani kwa Mustapha akakutana na wanaume wengine wawili ambao hao nao walitakiwa kuondoka nao kuelekea nchini Marekani, vijana hao walikuwa weusi kama yeye, walikuwa wametoka nchini Senegal na wao walitamani kuingia nchini Marekani na kufanya mambo yao.

Siku hiyo wakasalimiana, wakazoeana na kulala pamoja. Usiku walizungumza mambo mengi, kila mmoja alimwambia mwenzake jinsi alivyosumbuka mpaka kufika nchini Uturuki. Kila mmoja alipitia msoto mkali mpaka kufika hapo.

Kila walipoongea, waliwashukuru Waarabu hao, walionekana kuwa watu wazuri waliokuwa na lengo la kuwasaidia kufika nchini humo.

Walikaa pamoja kwa siku mbili tu kisha wakachukuliwa na kupelekwa sehemu iliyokuwa na makontena mengi.

Wakaambia kwa sababu walitaka kuzamia nchini humo ilikuwa ni lazima waingie kupitia makontena hayo ambayo kwa ndani kulikuwa na kiyoyozi ambacho kingewafanya kuwa salama kipindi chote hicho.

Humo ndani, waliwekewa mabegi madogo ya mgongoni ambayo yalikuwa na vitu ndani, hawakujua kulikuwa na nini ila waliambiwa kwamba ile ilikuwa ni mizigo ambayo walitakiwa kuipeleka sehemu fulani ambapo huko wangekutana na mtu ambaye angewaambia ni nini cha kufanya.

Kwa New York ambapo walitakiwa kwenda, waliambiwa kabisa kwamba safari yao ingekwenda mpaka katika kituo cha treni cha Pennsylvania kilichokuwa jijini New York, watakapofika hapo, kuna mtu angewafuata na kuzungumza nao kisha kuondoka zake.

Hilo halikuwa tatizo, walichokuwa wakikihitaji ni kufika nchini Marekani tu. Hawakupoteza muda safari ikaanza kuondoka hapo Uturuki kwenda nchini Marekani. Kwa usafiri wa meli hiyo, wangetumia mwezi mmoja njiani mpaka kufika huko.

“Mwezi mmoja?” aliuliza Fareed.
“Ndiyo!” alijibu Mustapha.
“Ni kipindi kirefu mno, kweli hatuwezi kutumia hata wiki moja au chini ya hapo?” aliuliza Fareed.
 
SEHEMU YA 125

“Ila ni mbali sana.”
“Ndiyo! Ila mwezi mzima nao ni mwingi mno,” alisema Fareed.
Hawakuwa na jinsi, hakukuwa na uwezekano wa kuwahi huko, ilikuwa ni lazima watumie mwezi mzima mpaka kufika nchini humo. Hawakuwa na hofu, walichojua ni kwamba walikuwa katika mikono salama na kusingekuwa na tatizo lolote lile.

Hawakutaka kujiuliza sana kuhusu mabegi madogo ambayo waliambiwa kwamba ni lazima waingie nayo nchini Marekani na kukutana na mtu ambaye aliwaambia kwamba wangekutana naye. Walimwamini Mustapha, kila mtu ambaye walikutanishwa naye, walimwamini kwa asilimia mia moja.

Safari ikaanza, ilikuwa ni ndefu na yenye kuchosha mno lakini hawakujali. Wiki ya kwanza ikakatika wakiwa majini, ya pili, ya tatu mpaka ya nne bado walikuwa njiani kuelekea nchini Marekani kwa kupitia katika Bahari ya Atlantiki.

Baada ya kupita siku ishirini na nane, wakaingia katika Visiwa vya Puerto Rico ambapo walipokelewa kinyemela na Waarabu wengine na kupelekwa katika nyumba moja kubwa na kutulia huko.

Bado waliendelea kuwaona Waarabu kuwa watu wema, hawakujua mpango mzito waliokuwa nao watu hao, hawakujua kama walikuwa wakienda kutolewa mhanga pasipo wao kujua.

Hapo Puerto Rico walikaa kwa siku mbili kisha kuondoka na kuelekea nchin Cuba ambapo hapo wakakutana na Waarabu wengine waliowaunganisha kwa baadhi ya wanajeshi na kuambiwa lengo la watu hao kufika hapo.

Kutokana na uadui mkubwa baina ya Marekani na Cuba, mipango ikaanza kusukwa upya, ilikuwa ni lazima Marekani ilipuliwe kwa mara nyingine tena na watu hao ndiyo waliowafanyia mpango Fareed na wenzake kuingia nchini Marekani kinyemela kabisa, njia walizokuwa wakitumia Wacuba hasa wauza unga na kutulia jijini New York.

“Kesho mtaelekea katika Kituo cha Pennslyvania, hapo kuna treni itakuja, kuna mtu atawaletea tiketi na nyie kuondoka, popote mtakapokwenda mtajua kivyenuvyenu, cha msingi tumekwishawaleta Marekani, sasa kutafuta maisha ni juu yenu,” alisema Mustapha huku akiwaangalia.

“Tunashukuru sana!” waliitikia huku wakiwa na furaha.
“Kesho ndiyo mtakwenda. Jiandaeni!”
“Sawa.”
 
SEHEMU YA 126

Mustapha aliwapanga vijana wake ambao walitakiwa kuwapokea wakina Fareed ambao ndiyo wangekwenda katika kituo cha treni cha Pennslyvania kwa ajili ya kulipua kituo hicho.

Siku ambayo ndiyo ingekuwa siku ya tukio, vijana wa Mustapha ambao ndiyo wangeyaseti mabomu hayo tayari walifika katika kituo hicho kwa ajili ya kuwasubiri vijana waliokuwa na mabomu kwa ajili ya kuyalipua pasipo wao wenyewe kugundua kitu chochote kile.

Wakati hayo yote yakiendelea, Fareed alikuwa katika chumba kimoja na vijana wenzake, walikuwa wamejiandaa kwa ajili ya kwenda kulipua kituo hicho cha treni pasipo kujua kama ndani ya mabegi hayo kuliwa na mabomu.

Baada ya kupewa kiasi fulani kama kuwalaghai kwamba sasa wangekwenda huko na kuanza maisha yao, wakaelekea nje ambapo wakapanda gari na Mustapha na kwenda katika kituo hicho. Hakukuwa mbali sana, hawakutumia muda mrefu wakafika ambapo moja kwa moja wakaingia ndani.

Hakukuwa na mtu aliyejua kitu chochote kile, kila aliyekuwa akiwaangalia, alijua kwamba watu hao walikuwa abiria kama wengine. Walijichanganya na watu wengine na wao kusubiri treni ambayo ingefika mahali hapo muda si mrefu.

Bango kubwa lililokuwa mahali hapo lilikuwa likionyesha dakika zilizokuwa zimebaki kabla ya treni hiyo kufika katika kituo hicho.

Watu walijikusanya, bango hilo lilionyesha kwamba ziliokuwa zimebaki dakika tano tu kabla ya treni hiyo kuchukua abiria kwenye kituo hicho na kuondoka.

Kila mmoja macho yake yalikuwa yakiangalia saa yake, kwa Fareed, alikosa amani, wenzake walikuwa wakifurahi kwamba hatimaye maisha yao yangeanza nchini Marekani lakini kwake, kila dakika zilipokuwa zikienda mbele ndivyo alivyokuwa na hofu zaidi.

“Humu ndani ya mabegi kuna nini? Kwa nini hawakuturuhusu tufungue ili tuangalie? Kama kuna kitu kizuri, hivi kweli wasingependa tujue?” alijiuliza Fareed huku akijaribu kujiuliza juu ya kile kilichokuwa ndani ya begi.
 
Back
Top Bottom