Mshindi Kisura kuzawadiwa Sh mil. 5
Imeandikwa na Mwandishi Wetu; Tarehe: 11th March 2011 @ 23:30 Imesomwa na watu: 42; Jumla ya maoni: 0
MSHINDI wa kwanza wa shindano la Kisura wa Tanzania ambalo fainali zake zitafanyika Machi 18, jijini Dar es Salaam atajinyakulia Sh milioni 5.
Kampuni ya Beautiful Tanzanie Agency (BTA), waandaaji wa shindano la uanamitindo la Kisura wa Tanzania, walitangaza zawadi hizo Machi 11 ambapo shindano hilo litafanyika katika Hoteli ya Kilimanjaro Kempinski.
Licha ya kupata Sh milioni 5, atakayeibuka Kisura katika kinyang'anyiro hicho pia atatunukiwa kuwa Balozi wa FHI kwa mwaka mmoja, ambapo atakuwa akilipwa katika kila kazi atakayofanya ya shirika hilo.
Zawadi nyingine itakayotolewa katika shindano hilo ni ofa ya kusomeshwa bure kwa mmoja wa visura hao katika chuo cha mmoja wa wadhamini wa shindano kiitwacho Pure Academy.
Pia wafadhili wakuu FHI watatoa zawadi nyingine tatu za fedha taslimu kwa vikundi vitatu vilivyofanya vizuri katika mpango wa kutoa ujumbe mzuri juu ya elimu ya unyanyasaji wa kijinsia kwa wananchi, zaidi ikiwa ni janga la Ukimwi kwa wakati wote visura hao walipokuwa kambini.
Zawadi hizo ni Sh 1,400,000 kwa kikundi cha kwanza, wakati kikundi cha pili watapata Sh 1,050,000, huku kikundi cha tatu kitajizolea Sh 700,000.
Visura 10 wamefanikiwa kutinga fainali ya shindano hilo, ikiwa ni baada ya mchujo uliofanyika kwa awamu tano, wakiwa kambini.
Visura waliofanikiwa kutinga fainali na mikoa wanayotoka katika mabano ni Glory Msangi, Neema Kilango na Neema Seley (Arusha), Lilian Busa(Mara), Susan Manoko, Letina Christopher, Joyce Joseph na Grace David (Dar es Salaam), Flaviana Makungwa (Dodoma) na Silipa Swai (Mwanza).