Michezo magazetini leo...

Michezo magazetini leo...

Status
Not open for further replies.
Afrika ya Kati yaja kamili kuivaa Stars

Imeandikwa na Mwandishi Wetu; Tarehe: 11th March 2011 @ 23:55 Imesomwa na watu: 132; Jumla ya maoni: 0








WAZIRI wa Michezo wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Aurelien Zingas, ataongoza msafara wa timu ya Taifa ya nchi hiyo itakayokuwa na watu 32 kwa ajili ya mchezo dhidi ya Taifa Stars.

Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura amesema kuwa wamepata taarifa kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu Jamhuri ya Afrika ya Kati (FCF) msafara huo utakuwa na wachezaji 23 watakaotokea Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad, Gabon, Ufaransa, Morocco, Congo Brazzaville na Singapore.

"Wachezaji hao ni Prince Samola, Delphin Gbazinon, Audin Boutou, Nicaise Ozingoni, Mamadi Saoudi, Hilaire Momi, Geoffroy Lembet, Euloges Enza, Manasse Enza, Foxi Kette-Vouama, David Manga, Habib Habibou.

"Wengine ni Josue Balamandji, Fernander Kassai, Salif Keita, Freddy Lignanzi, Amores Dertin, Eudes Dagoulou, Vianney Mabide, Charly Dopekoulouyen, Emmanuel Yezzouat, Onassis Kemo na Franklin Anzite," alisema Wambura. Mchezo utafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam Aprili 27 mwaka huu.

Wakati huohuo, Wambura alisema mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Mohamed Adolf ameteuliwa kuwa Meneja wa timu ya Taifa ya wachezaji wenye umri chini ya umri wa miaka 23 inayoshiriki michuano ya mtoano ya Michezo ya Olimpiki itakayofanyika mwakani jijini London, Uingereza.

Pia Adolf kitaaluma ni mwalimu wa mpira wa miguu. Timu hiyo ambayo inafundishwa na Jamhuri Kihwelo akisaidiwa na Mohamed Ayoub itacheza mechi ya mchujo ya michuano hiyo dhidi ya Cameroon.

Mechi hiyo ya kwanza itachezwa Machi 27 mwaka huu jijini Yaounde. Timu hizo zitarudiana jijini Dar es Salaam wiki mbili baadaye.
 
Tamasha la wanahabari sasa kufanyika Cine Club

Imeandikwa na Mwandishi Wetu; Tarehe: 11th March 2011 @ 23:50 Imesomwa na watu: 30; Jumla ya maoni: 0








BONANZA la vyombo mbalimbali vya habari litafanyika leo ukumbi wa Cine Club, Mikocheni Dar es Salaam badala ya Coco Beach.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Katibu Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (Taswa), Amir Mhando imeeleza kuwa uamuzi wa kuhamishia Cine Club unalenga kufanya bonanza liwe zuri zaidi.

"Tamasha litafanyika kama ilivyopangwa Jumamosi Machi 12, 2011, lakini tumeamua kuhamisha kutoka Coco Beach hadi Cine Club kwa nia ya kulifanya liwe zuri zaidi.

"Licha ya kuwa malipo yalishafanyika Coco Beach na hata taratibu nyingine za maandalizi zilianza, lakini kumejitokeza jambo lingine kwamba kuna watu wa Tigo wana tamasha lao la mambo ya promosheni siku hiyo.

"Hivyo kwa kuhofia muingiliano na watu wengine, Taswa pamoja na wadhamini wa bonanza Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), leo tulifanya kikao cha dharura na kufikia uamuzi wa kubadili ukumbi.

"Ingawa Tigo shughuli yao inaanza mchana na ni eneo lile la kuegeshea magari, lakini Taswa na TBL inaona wageni wake watashindwa kujinafasi na kukosa ule uhuru wa kuwa wenyewe kama dhamira ya bonanza ilivyo.

"Pia tumezingatia maoni ya wadau mbalimbali wa bonanza hili waliotaka tutafute mahali ambapo wataweza kujinafasi zaidi, hivyo Taswa na TBL wanaamini Cine Club ni mahali mwanana," alisema Mhando.

Alieleza kuwa dhamira yao ni kuhakikisha kwamba waandishi 1,000 watakaohudhuria wanakuwa huru bila kuwepo na watu wengine na kuomba radhi kwa usumbufu ambao utajitokeza huku akisisitiza kuwa mabadiliko waliyoyafanya yana dhamira ya dhati ya kujenga.

Tamasha hili mgeni rasmi atakuwa Waziri wa Habari, Vijana Utamaduni na Michezo, Dk. Emmanuel Nchimbi, hivyo mambo mengine ikiwemo ratiba inabaki kama ilivyo," alisema.

Alieleza kuwa leo pamoja na mambo mengine kutakuwa na mashindano ya mbio za meta 100 kwa ajili ya wahariri na mshindi wa kwanza atapewa medali ya dhahabu, wa pili fedha na wa tatu shaba.

Alisema michezo mingine itakayoshindaniwa ni soka ya ufukweni (wanaume), netiboli (wanawake), wavu (jinsia zote watachanganyika), mbio za magunia (wanawake na wanaume), mbio meta 100, kuruka kichura (wanawake na wanaume) na kuvuta kamba (jinsia zote watachanganyika) na kucheza muziki (wanawake na wanaume).
 
Status
Not open for further replies.
Back
Top Bottom