Simba kumalizia hasira kwa Ruvu Shooting ?
Send to a friend Tuesday, 08 March 2011 19:56
Kocha wa Simba, Patrick Phiri
Clara AlphonceBAADA ya sare ya 1-1 dhidi ya watani zao wa jadi, Yanga katika mchezo uliochezwa Jumamosi, Simba leo inashuka dimbani kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro kucheza na Ruvu Shooting mchezo wa kiporo huku ikitaka kumaliza hasira zake.
Simba ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi Kuu watakuwa na kibarua kigumu kuwakabili wanajeshi hao ambao pia nao wanajaribu kila wawezalo ili kuepuka kushuka daraja baada ya kupanda daraja mwaka jana.
Ligi hiyo ambayo ipo katika hatua za mwisho ambapo imeziacha AFC ya Arusha, Majimaji, Polisi Tanzania na Ruvu Shooting katika hatari ya kushuka ya daraja msimu huu.
Kocha wa Simba, Patrick Phiri ambaye Jumamosi alionyeshwa kadi nyekundu na hatakuwa katika benchi leo alisema mchezo huo kwao ni mgumu kwani wanacheza na timu ambayo inajitetea ili isishuke daraja huku wao wakitaka washinde mchezo huo na kupanda hadi kileleni mwa ligi hiyo na kujiwekea mazingira mazuri ya kutetea ubingwa wao.
''Sitaki kupoteza mchezo hata mmoja kuanzia sasa kwani mpaka sasa bado nina nafasi kubwa ya kuchukua ubingwa japo najua kucheza na timu ndogo mchezo unakuwa mgumu kwani huzikamia timu kubwa,'' alisema.
Hata hivyo, Phiri alisema kuwa bado ataendelea kumkosa beki wake tegemeo Joseph Owino kwa msimu mzima baada ya kusumbuliwa na goti.
Naye kocha wa Ruvu Shooting, Charles Mkwasa alisema kuwa kwa sasa anajitahidi kuhakikisha anaibakisha timu yake Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao, hivyo atahakikisha haipotezi mchezo wowote kati ya sita iliyobaki.
Alisema anajua anacheza na Simba ambayo ni ni timu ngumu, lakini watatumia vizuri nafasi ya kucheza nyumbani ili kuhakikisha wanaondoka na pointi tatu ambazo ni muhimu kwao.
Hivi sasa timu za Simba na Yanga zinashindana kuwania ubingwa huo ambapo timu itakayopteza mchezo kuanzia sasa itajiweka pabaya katika kinyang'anyiro hicho.
Simba imebakiza mechi tano ambazo ni dhidi ya Ruvu Shooting, AFC, JKT Ruvu, Kagera, Majimaji.
Huku Yanga ikiwa imebakiza mechi nne dhidi ya JKT Ruvu, Azam FC, African Lyon na Toto Africa.
Mbali na mchezo huo, leo pia kutakuwa na mchezo baina ya Kagera Sugar dhidi ya Toto African ya Mwanza kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Kocha msaidizi wa Kagera Sugar, Mlage Kabange alisema kuwa mchezo wao wa leo utakuwa mgumu kwao kwani Toto African siyo timu ya kubeza, inao wachezaji wazuri, hivyo wao wanatakiwa wajitume na kuhakikisha kuwa wanapambana ili kuibuka na ushindi kwa kuwa wanachezea nyumbani.
Alisema timu yake mpaka sasa inao majeruhi wawili ambao ni Ibrahim Mamba na George Kavila, lakini hao hawawezi kumfanya timu yake ishindwe kushinda katika mchezo huo.
Kocha wa Toto African, Choki Abeid alisema kuwa timu yake tayari imewasili Kagera kwa ajili ya kujiandaa na mchezo huo wa leo ambao amejigamba kuwa watashinda.
Alisema timu yake iko vizuri sana kuhakikisha inatoka na ushindi kwani amekwisharekebisha makosa ambayo aliyaona katika mchezo wao wa mwisho walipocheza na Mtibwa, hivyo wasitarajie mteremko japo mechi hiyo itakuwa ngumu kwa pande zote mbili.
...Lyon yachanua
Wakati huohuo Kalunde Jamal anaripoti kuwa African Lyon imeichapa Polisi Dodoma mabao 2-1 katika mechi ya Ligi Kuu iliyoendelea jana kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Bao la kwanza la African Lyon lilifungwa katika dakika ya 12 na Benedicto Yakob kwa shuti kali, ambapo mpaka mapumziko Lyon ilikuwa ikiongoza.
Kipindi cha pili katika dakika ya 59, Zahoro Pazi aliipatia timu yake bao la pili baada ya Idrissa Rashid Rashid kupiga kona na Pazi kuiunganisha.
Polisi Dodoma walipata bao la kufutia machozi katika dakika ya 81 ambalo lilifungwa na Mohamed Neto baada ya mabeki wa Lyon kujichanganya.