Mheshimiwa the Don

Mheshimiwa the Don

16
Mheshimiwa the Don
David Ngocho Samson
0629077792 WhatsApp

Maisha alimpigia simu mchumba wake Neema, ambaye alikuwa mhadhiri wa chuo kikuu cha Mzumbe na kumueleza masahibu yaliyokuwa yamempata jana ya siku hiyo. Alidai kwa hali ilivyokuwa, ni dhahiri alikuwa anakabiliwa na kesi ya mauaji, ambayo ushahidi ulimwonyesha yeye kuhusika kwa sababu aliacha kitambulisho kwenye mifuko ya koti alilokuwa ametelekeza kule shambani.
Ilikuwa habari nzito ambayo Neema aliazimia kufika Dar ili kupata uhalisia wa hayo aliyokuwa ameelezwa, ambayo yalionekana sasa kumchanganya akili. Ilikuwa imebaki miezi kadhaa kwa wawili hao kuumba mwili mmoja na kuanzisha familia, habari ile ilimshitua vibaya sana Neema.

Alijikuta anafuta machozi yaliyokuwa yameanza kumtiririka usoni, kisha akaweka chini simu na kutoka bustanini ili kuvuta pumzi na kuchukua hatua sahihi.

Kwamba mmewe mtarajiwa, mtetezi wa haki za binadamu maarufu sana sasa ibainike ni muuaji. Nini angekisema sasa kimpe unafuu na kipate kibali machoni mwa walimwengu? Na je? suala hilo lilikuwa linamweka upande gani yeye binafsi? Hakuwa tayari kuona wanafikia hapo. Kwa vyovyote vile alipaswa kuwa faraja kwa mchumba wake Maisha. Huu ulikuwa muda mwafaka wa kuonesha mshikamano kwa mwanaume aliyemtambulisha kwenye ulimwengu wa wakubwa. Ambaye hakujali umaskini wake na kumpa sapoti wakati akisoma chuo kikuu. Ndio, huyu ni mwanaume ambaye hakujali ule uvumi kwamba mchumba hasomeshwi na kufanya kile kilichompendeza kufanya.

Hakumsomesha ili baadae amuoe. Hata suala la mapenzi kipindi hicho halikuwamo akilini mwake. Ni yeye Neema mwenyewe aliyekuja kuliibua suala hilo. Na, akatumia uwezo wake wote kuhakikisha anamtunuku Maisha zawadi ya ushindi. Hakuishia hapo, bali alidhamiria kumkabidhi maisha yake yote. Alimpenda haswaa! Hivyo basi, wala kuhisi hata kidogo kuwa labda Maisha ametekeleza suala hilo la kikatili, Ni jambo ambalo halikupita kabisa kwenye fikra zake Wala kuleta maana.

Alirejea ndani na kupaki nguo mbili tatu na kuziweka sawa. Halafu aliingia kwenye gari lake ist nyekundu na kuchoma mafuta, breki ikikanyagwa chuoni Mzumbe. Alipokwisha paki gari lake eneo husika, Neema aliteremka na kupanda ngazi katika jengo la utawala kuelekea katika ofisi yenye maandishi Deputy Vice Principal - Human Resources and Education. Alizama ndani. Akafanya mazungumzo na wahusika wa ofisini hiyo. Alipotoka, alikuwa na uhakika na safari yake. Akiwa na ruhusa ya kuondoka kazini.

Hakurejea nyumbani. Tayari alikwishajiandaa kwa safari. Alichofanya ni kupita kwenye kituo cha kujaza mafuta, akajaza Lita za kutosha za petroli, ambazo zingemudu hata safari ya Dar hadi Mwanza, akaingiza gari barabarani kulitafuta jiji la Dar es salaam.

***

Ilikuwa asubuhi sana majira ya saa moja, na alihitaji sana kuonana na Elinisa baada ya kumkosa siku ile. Anastazia aliendesha gari lake kwa mwendo wa wastani tu na hatimaye akafika getini kwa Elinisa na kubisha hodi bila mafanikio. Leo asingerudi bila kuonana na Elinisa, alikuwa na maswali mengi yakimkereketa moyoni mwake na alihisi angepata majibu yake kutoka kwa Elinisa hasa sana juu ya ndugu yake Elineema Urio.

Geti lilionyesha kila dalili kwamba toka alivyoondoka siku ile basi hakuna kiichofanyika pale, kulikuwa na kila dalili ikionyesha kwamba, Elinisa hakuwepo. Hata hivyo, Ana hakurudia getini, aliusukuma mlango wa geti kwa nguvu akitegemea kupata upinzani wa kitasa kwa ndani, lakini akajikuta kidogo adondokee ndani pamoja na mlango ule uliokuwa mwepesi kulinganisha na nguvu aliokuwa ameuwekea katika kuusukuma.

Aliingia ndani na kupitiliza hadi mlangoni mwa nyumba aliyoishi Ely na kubisha hodi. Jitihada zake hazikufua dafu, akajaribu Mara nyingine, Hola! Kuugusa mlango,ukachanua kea uwazi. Ulikuwa wazi, bila shaka tokea juzi. Runinga ilikuwa inafanya kazi, lakini kulionekana kama kwa siku mbili hivi Elinisa hakuwa amerudi.
Kichwa kikazunguka, sasa alipata hofu juu ya Elinisa kwa habari ya tishio alilokuwa amepewa na Geof, tukio lile la mazungumzo kati yake na Asha, likavamia fikra zake. Mazungumzo yao yalianza kujirudia ndani ya ubongo wake.

Kulikuwa na simu ya mkononi ya Elinisa juu ya meza pale sebuleni na aliona wallet ndogo pia kwenye meza hiyo. Ana akahisi kwamba mwanaume huyo aidha alitekwa au kukumbwa na lolote bila kujiandaa, baada ya kutoka nje kwa kusudi la kurejea ndani bila kutumia muda mwingine nje, na ndio maana hakuondoka na simu Wala wallet. Akiwa angalia bado anafakari uwezekano huo, Ana akapata wazo jipya. Vipi kama labda umauti ulimkuta mwanaume huyo humo ndani? Ndio, lisingekuwa Jambo geni. Watu hufa usingizini, Kuna magonjwa Kama shinikizo la damu huondoa uhai wa mtu Kama masihara. Na pia alishasikia kesi za watu waliokufa kwa kuanguka vibaya, hali wakiwa ni wagonjwa wa pumu, kifafa na wengine kwa kujizidishia dozi ya dawa za hospitalini na hata za kulevya.

Akili yake ikamtuma kuzuga kuita jina la mwenyeji wake endapo alikuwa bafuni akioga au kitandani amelala. Hakupata mrejesho, na badala yake akajisikia sauti yake kwa mwangwi na ukimya wa kuogofya kwenye nyumba hiyo.

Akapiga hatua moja ikifuatiwa na nyingine, mkononi akiwa na bastola yake thabiti, alikusudia kufanya upembuzi yakinifu wa nini kilikuwa kinaendelea hapo. Akaufikia mlango wa chumba cha kwanza, kilikuwa kitupu zaidi ya kitanda kilichotandikwa vizuri kabisa.

Akatoka hapo na kufuata korido hiyo na kuufikia mlango wa pili, huko pia kulikuwa hakuna cha maana. Hatua zake zikamuongoza kwenda chumba alichoamini ndio master bedroom aliyotumia Ely. Alikuwa sahihi. Hata hivyo, zaidi ya kukuta kitanda ambacho kilikuwa safi na maridadi, pamoja na mali kadha wa kadha za Ely, hakukuwa na mtu yeyote na kila dalili ilionesha hakuwa amekitumia kitanda na chumba hicho kwa siku mbili hivi.

Moja kwa moja, Ana akajikuta amerejelea yale mazungumzo yake na Asha. Hisia zake zikamweleza, Geof atakuwa ama amemteka Ely au kaamua kumpoteza kama alivyomwahidi.

Akarejea sebuleni na kuichukua ile wallet ndogo na kuamua kuifungua. Mlikuwa na fedha Kiasi pamoja na vitambulisho mbalimbali vya Elinisa. Pembeni ya iliyokuwa bwallet na simu, akaona shajara ndogo ambamo Elinisa alitunza kumbukumbu zake muhimu. Ghafula simu ile ya Elinisa ilianza kuita. Haraka Sana akainyanyua akitaka kujua nani aliyekuwa anampigia Elinisa. Huenda akawa yeye mwenyewe anataka kujua kama kuna usalama nyumbani kwake. Akaona jina Asha kwenye simu hiyo. Ana aliipokea simu, jambo lililomfurahisha Asha. Alikuwa amemtafuta mwanaume huyo na sasa hatimaye ilikuwa imepokelewa. Lakini, kusikia sauti ya kike ikiijibu simu ya mpenzi wake, moyo ulimuuma kwa wivu.

“We nani na mwenye simu hiyo yu wapi!?” alihoji Asha.

“Mimi Ana, nimekuwa simpati kwa simu yake ndo maana nimeamua kuja huku ili kujua kulikoni lakini ndo hivyo, Elinisa anaonekana kupotea katika mazingira tatanishi.” Ana akamweleza.

“Nipo njiani nakuja” Asha alitamka na kukata Simu.

Kama kawaida yake, Asha alimpigia dereva teksi simu, akamfuata, akawa yuko njiani akielekea kwa Elinisa ili kujua namna ya kutatua kitendawili kile.

Alimkuta Ana amekaa kitako anakunywa juisi ya Pera kwa raha zake.

“Leo ni tarehe nne, lakini kwa mujibu wa Elinisa, alipata ujumbe wa kutishia kuuondoa uhai wake ndani ya siku mbili kama asingeliachana na wewe. Leo ni siku ya tatu toka amepata ujumbe huo, na haonekani, unadhani ni nini kina endelea hapa?” Ana alihoji akiwa anamwangalia kwa makini Sana Asha. Ukiwa mpelelezi ni shida kweli. Kila mtu unamtilia mashaka kuwa ni mtuhumiwa.

Asha akaisikia kengele ikilia kichwani mwake. Ikawa kama anayasikia mazungumzo yake na Geof kipindi kile. Sauti ya Geof ikitamka kwa uthabiti, ‘not when I'm alive and breathing darling’

Akatengeneza ubongoni mwake sura tulivu ya Geof ilivyofyonya kwa hasira na uchungu wakati akiyatamka maneno hayo. Haikuwa siri, alimjua Geof kwa muda sasa, bila shaka ilikuwa kosa pale alipoyapuuza maneno hayo, Geof alidhamiria na haikuwa na shaka kwamba Geof amehusika na tukio hilo.

Moyo ulianza kwenda mbio, kwa mara nyingi, hakufikiri angekuwa chanzo cha tukio kama hili. Aliyajua machungu ya mapenzi, alikwisha umizwa, ilikuwa vipi asahau? Angesahau vipi ilhali tabia hii ilitokana na machungu ya mapenzi, kumwacha Geof, au basi kumpenda, alichohitaji Geof ni kupendwa lakini ni nini alipata kwake?

Alianza kuhisi hisia aliyopata pindi alipoachwa na Salimu na kitendo cha kunywa sumu, sasa, yeye mwenyewe alichukua uamuzi kama huo! Labda yeye alikuwa mwoga, alishindwa kumkabili adui na kwa kihoro akataka kujimaliza, labda Geof alikuwa tofauti, alikuwa tayari kumkabili adui, adui ambaye sasa alikuwa Elinisa. Vipi hakufikiri juu ya hili. Vipi ilivyo rahisi kwa mwanadamu kusau! Vipi ilivyo ngumu mwanadamu kujifunza!

Alinyanyua macho yake kwa upole na kuyatua usoni kwa Ana aliyekuwa akimtazama kwa muda huo akijaribu kuhisi alichofikiri mchumba wa Elinisa, Asha.

“Nadhani namfahamu aliyehusika na kupotea kwa Elinisa, nadhani Geof anahusika” alivuta pumzi kwa nguvu.

“Mungu wangu nimefanya nini? Nimefanya nini mimi?” Asha alilalamika. Usoni kwake kulionekana wingu zito la huzuni mithili ya blanketi la Sufi.

Ana alimwangalia tu,

“Sasa tutafanya nini?” Asha alihoji.
Kuwepo kwa Ana pale kulitengeneza mhimili wa kuegemea, ni kama alihisi unafuu kidogo kwa uzito wa yale aliyokuwa akiyafikiri pale alipoyasema na kupata masikio ya kuyapokea.

“Labda tuwasiliane na huyo Geof ili kupata
uhakika, ingawa hata kama ni yeye anahusika sidhani kama atakiri. Tunaweza kupata kitu kwa kusikia sauti yake. Pili, tunapaswa kuripoti kwa mamlaka husika ili uchunguzi ufanyike haraka iwezekanavyo.”

Ana alimalizia kuongea huku akiukabili mlango wa kutoka ndani ya nyumba hii, nyuma akiitwa na Asha aliyekuwa anamkimbilia.

Itaendelea
FB_IMG_1591786598873.jpg
 
17
Mheshimiwa the Don
David Ngocho Samson
0629077792 WhatsApp

Mzee Hashimu aliamka alfajiri sana na kukusanya vithibitisho alivyokuta kwenye koti la Maisha Nchagwa na kuondoka haraka kuelekea kituoni. Huko kituoni alimkuta afande Masiko akiwa ameketi kwenye kiti anasoma gazeti la siku hiyo lililokuwa limefika pale kwa gari la asubuhi. Mzee Hashimu alimkabidhi vile vithibitisho.

“Maisha!?" Afande Masiko alihamaki.

"Si kweli, hapa kuna mchezo.” akamalizia. Alichukua faili na kuandika sentensi moja Kisha akanyanyua kichwa chake na kumtazama mzee Hashimu. Akamfanyia ishara kuwa aondoke, mzee akaelewa ishara hiyo, na taratibu akiwa haamini, akaondoka ofisini kwa Masiko na kupotelea uraiani.

*†*

Kwenye chumba alimowekwa Chale, zoezi la kumhoji lilikuwa linaendelea. Chale aligoma kutoa siri au taarifa yoyote ya maana, ikawalazimu polisi watumie nguvu ili kumpa maumivu kusudi atoe taarifa walizohitaji juu ya tukio lile.

Chale akachezea kipigo na mateso makali. Maumivu yalipomzidia akaahidi kusema ukweli. Hata hivyo, alikuwa akitafuta tu unafikiri kutokana na kifinyo alichokuwa anapata. Polisi wakampa nafasi aeleze ukweli. Kinyume na matarajio yao, Chale alimtaja tena Maisha kuhusika na tukio lile. Ni suala ambalo halikumwingia kabisa kichwani afande Masiko.

Alimfahamu vema Maisha, alikuwa ni mtu ambaye aliamini katika haki za binadamu. Iweje leo ahusike na uvunjifu mkubwa kiasi hiki wa haki za binadamu? Lazima kutakuwa na njama hapo. Tena kubwa ambayo ililenga kumharibia kabisa sifa kijana huyo ili yeyote yule aliyehusika basi apate nafasi ya kucheza na haki za watu.

Kwa vyovyote vile, aliyehusika na hili alikuwa ni mjanja na alijuwa mjanja kweli kweli! Afande Masiko akajipata akiwaza, 'Kama suala hili litakuwa hadharani ni dhahiri waandishi wa habari, wachunguzi wa mambo wataelekeza macho yao kwa huyo mkurugenzi ili kuacha mwanya wa mjanja huyo kufanya vitu vyake bila wasiwasi, na bila shaka hilo jambo lilikuwa kubwa.'

Sasa ingewalazimu kumtafuta Maisha, aeleze mazingira ya kupotea kwa vitu vyake vilivyokutwa eneo la tukio. Hakukuwa na namna nyingine.

***

Akiwa nyumbani kwake, Maisha alikuwa na mawazo mengi sana na kujilaumu kwingi. Yeye ni nani? Mbona akafanya upuuzi ule?. Kichwani mwake mlikuwa na mchanganyiko wa hisia na mabishano makubwa. Kwa sehemu, alijihisi mkosefu. Ni kweli hakuhusika na tukio lile lakini akiwa kama raia mwema, ilimpasa kutoa taarifa ya tukio lile kwenye mamlaka husika. Hakuwa amefanya hivyo.

Kwa sehemu, alipata moyo wa kiburi, kutotii sheria, kwamba asubiri aone hatima ya tukio lile. Hata hivyo bado kichwa kilimuuma kwa mawazo hayo.

Neema alikuwa pembeni yake akijaribu kumfariji. Mama yake alijawa na huzuni na hakujua namna gani amsaidie mwanae kipenzi. Alibaki na majonzi akijua hana cha kufanya zaidi ya kusubiri yatakayojiri huku akimwombea mwanae kwa Mungu ili hatimaye aibuke mshindi katika dimbwi hili la tope alimokuwa amezama.

Muda wa saa mbili asubuhi hivi, geti lao liligongwa. Mlinzi akajivuta kivivu na kuliendea. Akalifungua na kukutana na askari wawili waliokuwa ndani ya sare zao za kazi.

“Hapa ni kwa Maisha Nchagwa, mkurugenzi wa HRO?” alihoji askari mmoja aliyekuwa amejaa misuli mithili ya wacheza mieleka.

“Ndiyo afande” alijibu mlinzi.

“Tunahitaji kuonana nae.”

Bila ubishi, mlinzi aliongozana nao na kuelekea upenuni mwa nyumba ya Maisha.

Askari walijitambulisha. Muda mfupi baadaye Maisha alitoka ndani na kuja kukutana na askari hao baada ya kupewa taarifa na mlinzi.

“Sisi ni askari kutoka kituo kidogo cha polisi Mbande. Tuna hati ya kukuchukua kwenda kituoni mheshimiwa, tafadhali ongozana nasi.” Askari mmoja alitoa maelezo huku akionyesha hati ya kumkamata Maisha. Neema alinyanyuka na kumkumbatia Maisha huku akijaribu kumzuia asiondoke.

“Inabidi niende mpenzi, najua hii ni hujuma lakini hakuna haja ya kuhofu, ukweli utabainika na nitatoka. Jipe moyo na niombee” Maisha alitamka halafu akambusu usoni na kujitoa kwa Neema na kuongozana na askari kuelekea getini.

“Mama, niombee." Maisha alimweleza mama yake.

“Mwamini Mungu, atafanya njia pasipo na njia, na kutoa maji penye ukame na jangwa. Usihofu baba” mama yake aliongea huku akijifuta machozi.

Askari wale walimtia pingu mkononi na kuingia naye ndani ya gari la kiraia. Jambo hili lilimshangaza sana kwani alitegemea kubebwa ndani ya gari la polisi.

Hakuuliza swali japo moyoni mwake mlijaa maswali, labda kwa sababu ya ile hali ya kuhamanika. Alisahau hata taratibu za kawaida, sheria inayohusu makosa ya jinai, akiwa Ni msomi mbobezi wa sheria. Hakukumbuka hata hitaji la kuwa na wakili wa kumtetea. Akabaki anajiuliza maswali Kama raia yeyote yule wa kawaida. 'Kwa nini wamfunge pingu hata baada ya kuonesha ushirikiano? Kwa nini wazuie familia yake kuambatana naye? Hata baada ya kuwaza Hayo, Maisha alitia lijamu midomoni mwake. Kama kondoo, akakubali kuongozwa kwenda machinjioni.

Gari liliwashwa moto na kuondolewa kwa mwendo wa kasi.

*†*

Huku nyuma Neema alijaribu kuketi chini lakini hakukukalika, alitembea huku na huku na hakuelewa hasa nini afanye. Asingeweza kubaki hapa kutwa nzima kabla ya kupata wendawazimu. Aliingia ndani ya gari lake na kuliwasha moto akatoka mbio kufuatilia alikokuwa anaenda mmewe mtarajiwa.

Mbele aliliona gari liliombeba Maisha likikatiza kuelekea mwenge. Hakuelewa kwa nini waelekee huko ilhali walidai wanaenda Mbande, njia rahisi ilikuwa kupita posta na kunyoosha na Barabara ya Kilwa, moja kwa moja hadi Mbagala halafu waelekee Mbande.

Aliamua kuwafuatilia. Lakini alivyokunja kona tu alikutana na foleni ndefu ajabu, kutahamaki gari alilokuwa anafuatilia lilikuwa limepotea machoni pake. Alichanganyikiwa. Alitamani aruke hewani lakini isingewezekana. Alilaani foleni za Dar es Salaam.

Alitembea mbele kidogo baada ya foleni kuachia, na alipopata upenyo, Neema aligeuza gari kurejea nyumbani kwa Machera. Alipoingia getini tu akashuhudia gari la polisi lenye namba PT likipaki nje ya geti. Neema hakuelewa nini kinaendelea.

Wakati akitafakari nini kilikuwa kinaendelea, askari mwenye cheo cha Koplo aliteremka na kuingia ndani ya geti bila kukaribishwa. Alijongea hadi jirani kabisa na Neema na kutoa kitambulisho chake.

“Naitwa Koplo Magumashi, kituo kidogo cha polisi Mbande, nipo hapa kwa ajili ya mheshimiwa Maisha, mkurugenzi wa Shirika la Haki za Binadamu HRO.” Magumashi alijitambulisha.

Wakati huo, mama mzazi wa Maisha alikuwa kishajongea eneo lile na aliweza kumsikia Magumashi akizungumza. Uzalendo ukamshinda mama wa watu, kutanabahi mama alikuwa ananing'inia shingoni kwa Magumashi, machozi yakimtoka huku akihoji mfululizo walikompeleka mwanae kama waliotangulia hawakuwa wametoka kituoni Mbande. Ilibidi Neema kuingilia kati na kutuliza hali ya mambo.

Baada ya utulivu kushamiri, Neema alimweleza koplo kilichotokea na hisia yake juu ya kutekwa kwa Maisha. Kwa maelezo hayo, koplo Magumashi akaomba kuambatana na Neema kwa ajili ya kutoa maelezo kituoni na kufungua jalada la kutekwa Maisha ili kuruhusu upelelezi kufanyika.

Itaendelea
FB_IMG_1591786598873.jpg
 
18
Mheshimiwa the Don
David NGOCHO Samson

*†*
Maisha alishituka kuona gari linaelekezwa Mwenge.

“Mbona tunaelekea huku, nilidhani mlisema ni kituo cha polisi Mbande?” alihoji. Ni kama maneno yake yaligonga mwamba. Watu wale walimbeza kwa kila hali, badala yake wakadhihirisha kile kilichomtia jaka la moyo kuwa ni bayana.

“Ni wapi mnanipeleka?” alibwatuka kwa hasira iliyochanganyika na hofu.

“Haki za binadamu siyo? Unataka haki siyo? Kama unajua sana haki ilikuwa vipi uue?” askari mmoja alitamka halafu wote wakaangua kicheko ndani ya gari. Wasiwasi ukamvaa Maisha, bila shaka alitambua kuwa alikuwa mikononi mwa genge la Don. Genge ambalo alijua hatari yake.

“Nyinyi ni nani?” aliuliza Maisha, alijua haina maana kuwauliza maswali baradhuli wale, lakini hakuona kitu gani cha kufanya kwa wakati huo.

“Ah swali gani hilo, hata kuona sasa ni tatizo?” walicheka tena, sauti zao zilimpa kero na tayari alijua yuko kwenye hatari kubwa.

Mmoja kati ya askari wale, alitia mkono kwenye fuko la kiroba, akatoka na tambara chafu ambalo likitumika kufuta oili chafu, hakujali harufu ile mbaya, alimfunga nalo machoni tambara lile asiweze kuona mbele. Hapo Maisha akajua mambo yameharibika. Hata hivyo hakutaka kuwapa urahisi kihivyo, Alijaribu kutia ubishi, lakini haikusaidia kitu zaidi ya kuwafanya wale watu waoneshe undava wao. Akapigwa kipepsi chenye ujazo wa kilo kadhaa kwenye paji la uso wake, akaona nyota nyota. Halafu kimya kikachukua nafasi.

***

Kulikuwa na jua kali sana, watu wakiwa kwenye mahangaiko yao ya kujipatia mkate wa siku. Machera alikuwa miongoni mwa wasakatonge wa siku hiyo. Alivalia suti yake nyeusi na miwani. Na mkononi alikuwa anatazama saa, ilikuwa yapata saa nane za mchana. Alichukua gari na kulitoa mbio, alilielekeza gari lake maeneo ya uhasibu Temeke, alinyoosha kama anelekea Posta kupitia Kilwa Road na kisha akakunja kona na kuingia kwenye geti lililokuwa na maandishi The Salvation Army - Mgulani Hostel.

Alikata kona akiwa ndani ya eneo lile na kushika breki mbele ya jengo lenye maandishi, Reception (Mapokezi)
Nyuma ya meza ya mapokezi alikaa msichana mrembo mwenye asili ya kichaga na meno yaliyoungulia kidogo.

“Salama kaka, Karibu, sijui nikusaidieje?” Yule mrembo alijibu salamu ya Machera huku akinyanyuka.

“Asante dada, kuna msichana mrembo hivi, alikuwa amevalia blauzi ya pinki na sketi fupi ya kaki, na yupo hapa tangu jana. Anaitwa Anastazia. Sijui unaweza kunielekeza chumba alipo?”

“Oh ndiyo, tafadhali nipe dakika mbili hivi.”
Dada wa mapokezi alifanya mawasiliano na Anastazia na kisha akamwelekeza kuingia nyumba namba 6.

“Kwa hiyo bila wewe kusema ndiyo siruhusiwi kuonana na wewe?” Machera alimuuliza Anastazia baada ya kuwa ameishaingia chumbani hapo.

“Sio mimi, ni utaratibu wa hosteli mpenzi” alijibu Ana.

“Mh, umeniitia nini?” Machera alihoji.

“Nimekukumbuka, hivyo nilitaka nikuone”

“Ahaa! Sasa umeniona, halafu?”

“Hebu kaa kitako mwanaume. Ni juu ya yule jamaa, Elinisa Urio.” Anastazia aliongea Huku akimuonesha kiti kilichokuwa pembeni ya kitanda ambako yeye alikuwa ameketi. Machera aliketi, ikawa kwamba wamekaa wakiwa wanatazamana usoni.

“Naam, kuna nini?” Machera alihoji.

“Amepotea ghafula na haieleweki wapi aliko. Nyumbani kwake hajaondoka na kitu chochote, nyaraka zake zipo zote, hati ya kusafiria na hata leseni ya udereva. Hivyo tunahofu kwamba atakuwa ametekwa au ameuwawa.”

“Si mchezo..ha!”

“Si mchezo.”

“Tuna chochote cha kuanzia?”

“Tunahisi kwamba ni suala linalohusika na mapenzi. Yule mwanamke, Asha anadai boyfriend wake wa zamani atakuwa amehusika kwa sababu alitoa vitisho kwa huyo Elinisa na kwa kweli nimethibitisha kuwa alitoa vitisho baada ya kupitia shajara yake. Kwa hiyo, sijui unashauri nini kifanyike sasa.”

“Huyo boyfriend wa zamani anapatikana?”
“Ndiyo. Yupo Mbeya kwa mazishi ya mama yake mzazi.”

“Itabidi akamatwe ahojiwe vizuri huenda amehusika au la.”

“Vipi habari za Ken?”

“Si mwenzetu tena nasikia sasa hivi wao ndo wanatengeneza pesa, ni kusema ameukata mwenzetu.”

“Na anavyopenda anasa, mabinti watamkoma?” Machera alichombeza.

“Thubutu! Amwachie nani Martha?!” Anastazia akakanusha.

~*†*~

ILIKUWA yapata saa 11 jioni aliposhuka kwenye basi la City Express Ubungo. Geof alikokota begi lake dogo kuelekea kwenye teksi mojawapo iliyokuwa mbele yake. Ilikuwa safari ndefu na alihitaji kupumzika. Kabla ya kuingia ndani ya teksi, walisimamishwa na mtu mmoja mwanaume wa makamo hivi.

“Habari gani bwana Geof?” yule mwanaume alisalimia.

“Poa, sijui we ni nani mwenzangu, naona kumbukumbu zangu haziniletei taarifa ya mimi na wewe kufahamiana!” Geof alijibu. Uchovu wa safari ndefu toka nyanda za juu kusini Mbeya, ulimhitaji aharakishe kufika nyumbani walau ajimwagie maji akae sawa baada ya kupokelewa kwa fukuto la joto jijini Dar.

“Yeah ni kweli, lakini watu hufahamiana namna hii bwana Geof. Kama hutamaindi basi kuna gari pale linakusubiri, a free ride (usafiri wa bure) bwana Geof” Mwanaume huyo akatamka, kitendo ambacho kilimuudhi sana Geof

“A free ride?" Geof akang'aka kwa hasira, "Sasa naona tunaleteana mzaha. Tafadhali ondoka zako, usije ukaniletea balaa, au upo kwenye biashara?” Geof akatamka kwa hasira akiwa ameudhika vilivyo.

“Sikujua kwamba wewe pia ni mteja, huenda tutafanya biashara Geof, Sasa unaona lile gari pale, ninataka ubebe begi lako upande lile gari, sasa hivi!” Mtu yule alijibu akionekana kukasirishwa mno na kauli za Geof. Mshangao ukamshika zaidi Geof kuona sasa analazimishwa kupanda gari la mtu bila ridhaa yake. Geof hakuamini. Mimi nalazimishwa kupanda gari? Akajiuliza kimoyomoyo.

“Wewe ni nani?” Geof alihoji na pale pale yule jamaa akatoa kitambulisho chake. Alikuwa askari kanzu.

“Sikiliza bwana askari, hivi ndo nashuka kwenye basi...” hakupewa nafasi ya kumalizia kujieleza.

“Hata mimi nimeona bwana Geof, nachohitaji ni kuona makalio yako kwenye kiti ndani ya lile gari.” Afande alitamka kwa mamlaka!

Bila hiari, Geof aliingia ndani ya gari hilo la kiraia, lililotumiwa na polisi na kuelekea kituo cha polisi central. Tayari giza lilikuwa limeanza kuingia, lakini kwa Dar es Salaam ndiyo kwanza kulikuwa kunakucha. Taa ziliwaka mitaani huku watu wakipishana kila mtu na biashara zake.
Baada ya kufika polisi central, Geof alisindikizwa kuonana na mkuu wa kituo katika ofisi yake.

Mbele yake alikaa bwana mmoja mwenye mwili mkubwa na moustache wa wastani. Hakuwa ndani ya sare zake, alivaa tu kiraia. Ile anaingia tu, Geof alikutana na macho makali ya yule bwana. Hofu ikamwingia mwilini. Akasinyaa Kama kifaranga chenye mdondo. Kwa kuwa hakujua tatizo lililompeleka pale, Geof alijipa moyo hakutakuwa na shida kubwa. Akajaribu kutuliza nafsi, mapigo ya moyo yakarudi kwenye mstari.

Moyoni mwake, mambo yalikuwa tofauti kabisa na kile alichokuwa anajaribu kuonyesha. Alijawa na hofu kuu. Mpango wake na Mabruki bila shaka ulikuwa umevuja, 'Au yule mwanamke, Asha, baada ya kutomuona bwana yake atakuwa ameripoti polisi na kunihusisha kwa sababu nilitoa vitisho?' Alizidi kuwaza. 'Lakini bila shaka atahitaji kuthibitisha hilo.' Na vipi atajitetea, kila mtu alifahamu mahusiano yake na Asha, na kama atakiri ameachana naye kwa sababu ya Elinisa, basi ni dhahiri atakuwa mtuhumiwa. 'Nimekwisha!' Alijilaani.

“Naitwa Inspekta Marcus, nafahamu kwamba wewe ni bwana Geof!” yule bwana alijitambulisha baada ya kumuonyesha kiti kwa ishara ya kidole.

“Naam afande, Mimi ni Geof” Geof akakiri!

“Nadhani unafahamu kwa nini uko hapa bwana Geof” sauti ya Marcus ilishabihiana sawa kabisa na mwili wake. Sauti nzito iliyodai heshima, ilijawa na mamlaka kiasi ambacho Geof alihisi akiendelea kukaa pale atapata wazimu. Alijiona duni mbele ya askari huyo na hilo lilimtisha zaidi.

“La hasha inspekta, sijui chochote mimi. Kwa kweli nina mshituko sana, kuna tatizo gani hapa, hivi nimetokea mbeya Inspekta, hata kupumzika tu bado” Geof akatafuta kujitetea huku akigeuza msiba wa mama yake kama kichaka cha kujificha.

“Nafahamu, nafahamu. Kwanza nikupe pole kwa msiba” Inspekta Marcus akatamka kwa sauti ya kiungwana sana.

“Asante” alijibu Geof, safari hii sauti yake ilitoka kwa mtetemo.

Sura yake aliyokuwa ameivalisha kujiamini kwa bandia huku moyoni kukipwita kwa kipute cha taharuki nayo ilianza kumtupa mkono. Mikono yake sasa ilitota kwa jasho jembamba lililotoka sehemu mbalimbali za mwili, kwapa nazo zilikuwa tepe tepe sasa. Alijifuta kwa kitambaa na kulaani joto la Dar es Salaam.

“Naomba uondoe hofu bwana Geof. We mtu mzito sana na ndiyo maana nataka tuongee kiutu uzima kwa kuzingatia uzito wako” Marcus alisema.

Geof alijiuliza hawa watu wanafahamu mambo kiasi gani yanayomhusu. Sasa picha ilikuja kichwani. Wasingeweza kujua alikuwa msibani kama hawakuambiwa na Asha.

Ndio. Asha alikuwa amewasiliana naye akiwa bado Mbeya na yeye alimweleza alikuwa msibani. Wakati akiwa msibani Mbeya, mzee Mabruki aliwatuma vijana wake kutekeleza ombi lake. Jana tu alipata uhakika wa kifo cha Elinisa kutoka kwa Mabruki.

Elinisa sasa alikuwa historia, lakini walikuwa wamemhusisha Maisha na kifo hicho na kwa hivyo aliambiwa kutokuwa na wasi wasi kabisa. Lakini Asha, alianza kuharibu. Uhusika wake sasa bila shaka ulianza kutengenezewa dots, na muda si mrefu hizo dots zitaunganishwa na sasa Geof atabainika.

“Mwanamke malaya mkubwa yule!” Alilaani Geof akiwa anaelea katika wingu zito la mawazo. Kwa muda Inspekta alibaki anamtazama halafu akatamka

“Geof”
Geof akazinduka mithili ya atokaye usingizini, usingizi wenye ndoto za kutisha.

“Naam inspekta, nakusikiliza” Geof akatamka kwa sauti ya kinyonge zaidi. Bila shaka alikuwa kakamatika hasaa.

Itaendelea
David
FB_IMG_1591786598873.jpg
 
19
Mheshimiwa the Don
David Ngocho Samson

“Ukweli ni kwamba bwana Geof wewe ni mhusika wa kifo cha mtu ajulikanaye kwa jina la Elinisa. Ninazo habari zote juu ya kifo hicho,” inspekta aliongea halafu akanyamaza kidogo kumpa Geof nafasi ya kuyasharabu maneno yake. Geof sasa alihisi kuchanganyikiwa kabisa.

“Nimekusikia vizuri afande?” Geof aliuliza akionyesha mshituko na mshangao usio kifani.

“Vema kabisa bwana Geof, nataka tu ufahamu kuwa huna ujanja, tunavyo vielelezo vyote juu ya kuhusika kwako na kifo hicho. Na kwa taarifa tu, Mimi, inspekta Marcus ndiye nayeshughulikia jalada la upelelezi huo. Geof uko hatiani na kwa namna yoyote ile huwezi kujinasua katika hili.” Inspekta alinyamaza tena kisha akamtupia jicho la udadisi mtuhumiwa wake ambaye sasa alibaki kinywa wazi.

“Huna cha kusema bwana Geof na kusema kweli hapa uko chini ya ulinzi kisheria ila mimi nitakuruhusu uende endapo mazungumzo yetu yatakuwa mazuri” Inspekta akamtoa wasiwasi.
Geof alibaki akijiuliza kama alikuwa amepata vizuri sentensi ya mwisho ya inspekta.

Inspekta amruhusu aende kama mazungumzo yatakuwa mazuri? Mazungumzo yepi? Aliwaza Geof asipate neno la kusema. Alimwangalia inspekta akajaribu kufunua kinywa chake lakini maneno hayakutoka. Inspekta aliufahamu mtazamo ule, ulitosha kusema alichokusudia bwana Geof.

“Ndiyo bwana Geof, mazungumzo yetu yakiwa mazuri nitakuruhusu uende” Inspekta akasisitiza.
Inspekta alimtazama tena Geof kabla ya kusema.

“Unasemaje Geof” Geof alimtazama Inspekta kama bubu aliyebanwa na haja akitafuta kuelekezwa uani.

Inspekta anampa nafasi Geof kusema kitu, anataka mazungumzo mazuri. Ni huyo huyo mwenye jalada la upelelezi wa kesi yake! Kidogo alianza kuona wanapoelekea.

Aliwahi kuona, na alifahamu maisha ya askari yalivyo, wengi waliishi katika kambi ambazo kwa mtazamo wake ilikuwa mateso, vyumba vidogo sana, vyoo vya kushea vilivyojengwa miaka ya mkoloni. Kero mbalimbali za maisha yale na hapo hatujaongelea mishahara midogo isiyokidhi mahitaji ya polisi hao. Wengi waliishi maisha ya kutisha. Inspekta Marcus alikuwa kwenye umri wa ukingoni sasa, miaka 50 hadi 60 hivi. Muda si mrefu atakuwa anastaafu. Huenda hata nyumba hajajenga na sasa nafasi kama hii inajitokeza.
Nafasi muhimu ya kucheza vema, ndiyo, inspekta alikuwa amemwita mtu mzito, sasa picha ilikaa vizuri. Geof aliweza kutazama kona zote za picha iliyokuwa inaendelea hapa. Tone la tumaini lilimdondokea mithili ya tajiri na Lazaro, tone kidogo tu kwenye ulimi wa tajiri kutoka kwa maskini Lazaro.

“Inspekta, tafadhali naomba tusaidiane hili jambo, nisaidie afande. Nilitingwa na sasa naanza kuona matokeo. Tusaidiane bwana Inspekta” Geof sasa akajileta kwenye mwanga, mwenyewe bila shurti, kwa namna hiyo akathibitisha uhusika wake! Akajaa tele kwenye hila ya Inspekta Marcus. Hakujua, Inspekta alikuwa anacheza na akili yake.
Inspekta kwa mara nyingine alimtupia jicho la udadisi halafu akatikisa kichwa.

“Bwana Geof hii si kesi ya kitoto, wala ya madai kusema utalipa faini au miaka kadhaa jela, ukithibitika utafungwa maisha au utakabili kitanzi, hivyo nataka ufahamu tu kwamba hii ni suala kubwa na kama unataka nikusaidie fahamu wazi itakugharimu pakubwa, kwa maana nyingine ni kwamba mimi mwenyewe nitakuwa najiweka kikaangoni na bora iwe nimepata neno zuri toka kwako.” Alimaliza kuongea.

“Nafahamu inspekta, lakini hii ishu mpaka sasa imenigharimu pakubwa tu, aliyenitekelezea tu alichukua milioni tano. Kwa hiyo sipo vema kifedha.”

“Ndiyo na huyo kijana tumeshamtia hatiani.” Inspekta aliunguruma.

“Oh, na amemtaja bosi wake?” Geof akauliza kwa hamaki mshangao ukidhihirika usoni mwake mbashara! Paniki ilimtoa ufahamu akabaki anajianika wazi.

“Ndiyo, hakuna kilichobaki nyuma ya pazia bwana Geof,” Inspekta akaunguruma, macho makavu kwa Geof.

“Kama mzee Mabruki amekuwa kikaangoni mimi nina nafasi kweli?” Geof akajikuta ameropoka!

Inspekta alishtuka kidogo bila shaka hakuwa amefikiri suala hili lilikuwa na mtandao kiasi hiki. Hata hivyo hakuonesha mshituko wake wazi, 'Mzee Mabruki? Anahusika na kifo hiki?' Inspekta akajihoji asiamini habari hii!

“Ndiyo, nafasi unayo kwa sababu Mimi ndo nina vielelezo vyote hivyo.” Inspekta akamuondolea wasiwasi. Hata hivyo kengele ya hatari ililia maskioni mwa Inspekta. Hii bila shaka ilikuwa kesi ya aina yake!

Sasa Inspekta alitambua hatari iliyokuwepo hapo. Yule mzee alikuwa maarufu sana kwa jamii lakini vyombo mbalimbali vya usalama vilikuwa na taarifa tofauti kumhusu. Na sasa kwa mara nyingine mzee huyu alikuwa anahusishwa na mauaji. Lakini alitambua vema kwamba hatari yake ni kwamba Mabruki au The Don alikuwa na mbinu mbalimbali za kushughulikia wapinzani wake.

Maiti nyingi za wapinzani wake zilikuwa zinakusanywa kila mara, zikiwa zimetendwa ukatili na unyama wa kutisha, lakini hakuna aliyeweza kuthibitisha kuhusika kwake, zikaonekana ni tuhuma tu. Huku vyombo vyake vya habari; radio, TV na magazeti, vikimpamba kwa sifa kem kem zilizo mfanya awe mfalme kwa jamii yake. Jimboni kwake walimtambua kama mkombozi, shujaa dhidi ya udhalimu na zaidi walimtambua kama rais wao. Mabruki - The Don.

Leo kwa bahati ushahidi wa kuhusika kwake ulikuwa wazi kabisa. Mshirika wake alisema bila woga akijua anajinasua mikononi mwa kifo. Inspekta alitabasamu. Akamtazama Geof na kumpa swali

“Ofa yako ni kiasi gani?” Akauliza bila kupepesa kope.

“Afande, ninazo milioni kumi tu, ambazo nikikupa sitabakiwa na senti. Lakini ukipenda basi nitakupa kiwanja changu ambacho ni sawa na milioni hamsini.”

Inspekta alitabasamu zaidi, halafu kama mshituko hivi alipata wazo. Kiwanja cha milioni hamsini? Sina hata nyumba ya kustaafia! Halafu, nayepambana naye amethibitika kuwa mkatili wa kutisha, The Don. Huenda akapita juu na kupoteza kabisa ukweli wa ushahidi huu! Huenda akafanikiwa kunipoteza kabla sijathibitisha ushahidi wenyewe. Inspekta akajipata njia panda.

Kimya kidogo kikapita. Inspekta Marcus akiwa anatafakari dili lililokuwa mbele yake. Akatafakari uadilifu wake aliodumu nao kwa miaka yote hii, akajihoji, kipi cha maana? Kujiingiza kwenye Vita na the Don au kujiepusha naye haraka.

Ghafla Inspekta akahisi harufu ya mauti. Mwisho akapata wazo, wazo ambalo aliona ni safi litakalomwepusha na kesi hii jumla. Inspekta akatabasamu baada ya kulitafakari wazo lake.

“Nadhani ni sawa tu lakini nitahitaji na hizo milioni kumi. Najaribu kukuopoa kwenye mdomo wa tanuri la moto bwana Geof huku nikijihatarisha mwenyewe. Si suala la masihara. Wewe utanipa hizo milioni kumi na kiwanja halafu utatafuta namna nyingine ya kuishi, na nakushauri, ishi kwa mshahara wako bwana Geof.” Inspekta aliongea huku akiachia tabasamu la ushindi kwake, huku likimkejeli kwa dhihaka Geoffrey Ally Magubi Mtemvu.

~*†*~

SIKU kadhaa zilikwisha pita toka kupotea kwa Elinisa. Asha alikuwa anamtafuta lakini mafanikio yalikuwa bado kuonekana. Aliamua kutoa taarifa kituo cha polisi na sasa alikuwa anaitegemea polisi kufanya uchunguzi wa suala hilo. Sasa alishaanza kuona matokeo ya usaliti wake kwa Geof, alihisi hatia na jambo hilo lilimfanya kukosa raha kabisa.

Akiwa ndani ya gari lake aina ya Rav 4, aliendesha kukatiza Mtaa wa Msimbazi kariakoo na mbele kidogo alipaki gari lake na kuingia kwenye super market kubwa ya eneo hilo. Mchanganyiko wa mawazo na huzuni, vilimfanya Asha asiisikie salamu ya mtoto mdogo wa kiume, aliyekuwa anachukua ice cream, alipiga hatua mbele na kuinama kuchukua kopo la blue band pamoja na box la cornflakes, ile kuinua kichwa, uso wake ulitazamana na mtoto yule aliyetoa salamu hapo awali.

Kwanza alishtuka, akabaki anamwangalia yule mtoto, akili yake ikagota kwa muda, halafu baada ya jitihada kidogo ilionekana nguvu ya ubongo wake iko taratibu mno na ilikuwa inasuasua mithili ya DVD mbovu, halafu likafuatia wingu zito la mvua iliyokuwa inatoa tumanyunyu tudogo. Alipokuja kupata akili, hakumuona yule mtoto. Alizunguka haraka ndani ya ile super market akimtafuta yule mtoto lakini hakumuona. Sasa alishakata tamaa, mara akatokeza yule mtoto akiwa ameshika bidhaa zake mkononi.

“Dada, hii si kama NAKUMAT ya Nairobi haiko na pizza” yule mtoto alimwambia dada yake.

“Ah, hamjambo?” Asha aliwasalimu.

“Hatujambo” waliitika watoto wale.

“Mmependeza sana, mko na nani?”

“Sister Rosie, ametoka kidogo tu atarudi baadae kidogo. Amesema tusitoke humu hadi arejee”

“Na wewe mtoto mzuri unaitwa nani?”

“Naitwa Christian Salimu.”

Sasa mshituko wake ulileta maana. Christian alikuwa ni mtoto wa adui yake mkuu Eve na Salimu. Watu ambao walifanya maisha yake yawe ya shida mno. Hakuna kitu ambacho Christian hakuchukua kwa baba yake, alifanana mno na Salimu kiasi kwamba Asha alipomuona tu, alijua ni mtoto wa Salimu.

"Na mama ako wapi, Christian?”

“Ako Nairobi, yeye ako na big tummy,(tumbo kubwa) hawezi kuja, so wao wamebaki huko na Daddy.”

‘Ina maana Salimu ana mtoto mkubwa tu na Eve ana mimba?’ Aliwaza namna gani maisha yake yangekuwa kama asingekuwa ameharibiwa na huyo Eve, huenda yeye ndo angekuwa na mtoto wa Salimu. Ni kama alitonesha kidonda, na kuanzisha kovu jipya la maumivu yaliyokuwa moyoni kwa zaidi ya miaka saba sasa. Ipo siku, ipo siku nitaishi kwa furaha, nitazaa watoto, na nitalipa kisasi. Asha aliwaza.

Itaendelea
David Ngocho Samson
0629077792 (WhatsApp)
FB_IMG_1591786598873.jpg
 
20
Mheshimiwa the Don
David Samson Ngocho
0629077792

*†*
Kwingineko, Ken, kijana mdogo lakini mbobezi katika kazi yake ndani ya kitengo maalumu cha upelelezi katika wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, alikuwa ni sehemu ya kikosi kazi kilichoongozwa na Machera. Ikiwa ni weekend moja mujarabu sana, Ken alionekana akiwa bega kwa bega na mpenziwe Martha, mwanafunzi wa chuo kikuu Cha Dar es salaam, binti wa Waziri mkuu. Walifahamiana na hata kuanzisha uhusiano wa mapenzi wakati ambao Ken alipangiwa kazi katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Akiwa mwaka wa tatu, Martha ndio kwanza alikuwa anajiunga na chuo hicho. Mapenzi yakawakumba vijana hao. Hata Ken alipokuwa kamalizia shahada yake ya Sosholojia na falsafa, bado walibaki Chanda na Pete. Walionana kila ilipohitajika kuonana.

Pamoja na kukolea kwenye pishi la mapenzi, Martha alikuwa sehemu ya kikosi maalumu cha usalama. Ni Ken aliyehandisi mpango maalumu wa kumdahili binti huyo kwenye idara nyeti kabisa ndani ya wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Hata hivyo, licha ya kutokujua yeye alipataje kuingia, Martha hakuwa mbulula. Akili yake makini na ujanja wake wa kuzaliwa, ulimpa uwezo wa kubaini mchumba wake ni nani katika medani za usalama nchini.

Katika kikao chao hiki kama wapenzi, ndipo Ken aliamua kumfanyia usaili wa kuzugia ishara ya kumpima akili mpenziwe. Alifahamu fika misheni aliyokuwa nayo Martha. Hata hivyo, Martha aliishitukia janja yake na hakutaka kumpa nafasi ya kumgeuza zumbukuku ulimwengu uko huku. Majibu yake yakawa yapo wazi bin bayana;

“Sidhani kwamba unanipenda kwa dhati mpenzi, nina shaka. Ninaomba uelewe hilo kwamba nina shaka na sipendi hali ya mimi kuwa na mashaka juu yako. Nieleze una mahusiano gani na mtu anayeitwa Estivan Brown. Kuwa wazi. Nisingependa kuwa kama mwiba maishani mwako sababu unajua nakupenda sana.” Ken alimweleza Martha.

“Siamini kwamba una mashaka na penzi langu kwako, nakupenda sana Ken sijawahi kuota kukusaliti mpenzi na wala sitajaribu kamwe. Estivan ni mtu hatari sana kwa taifa hili na kwa kweli mimi natumika tu kama Delila. Ni hivyo tu hakuna kitu kingine zaidi” Martha akajieleza dhidi ya wasiwasi wa mpenzi wake.

“Sawa, nimekuelewa mpenzi, unajua jambo usilolijua ni kama usiku wa kiza. Lakini mpenzi unachukua tahadhari gani? Na unaweza vipi kuongea na mtu hatari kama huyo?” Ken akasaili akionesha wasiwasi wa kujali. Naam, wasiwasi uliolenga kumkoga mpenzi wake na kumjulisha kuwa alimpenda na kumjali kwa dhati.

“We mwanaume wivu utakumaliza, Mimi nachofanya huwa nampa taarifa fulani fulani ambazo ni za kweli lakini sasa tayari kunakuwa na tahadhari, kwa namna hiyo namjengea imani na yeye hunipa mipango yake kem kem.”

“Kwa hiyo wewe ni shushushu!” Ken alijifanya kushangaa.

“Vipi, wewe unaonaje?”

“Basi, tusiende mbali sana, ila tafadhali kuwa makini?”

“Usihofu juu yangu mpenzi, nambie bado una wasiwasi na mimi?”

“Wala, najivuna kwamba nina mpenzi anayetumikia taifa kwa uzalendo wa kiwango cha hali ya juu.”

"Sawa mpenzi, katika kukuondoa mashaka kabisa, labda ni vema nikakujulisha kwamba yule bwana si lolote. Kunao uvumi unaenea kuwa ni chakula cha wakubwa huko serikalini, Kama ushawahi kusikia mtu wa kuitwa Don" Martha alisimulia katika namna ya kukoleza utani. Wakaangua kicheko pamoja.

“Vipi umepata Habari za Leo? Unaweza kuamini kuwa Mr Maisha Nchagwa anatuhumiwa kuhusu mauaji ya kijana mmoja anayeitwa Elinisa? Gazeti hilo hapo.” Martha alimkabidhi Ken gazeti la Habari za Leo lililokuwa na kichwa cha habari:
MKURUGENZI WA HAKI ZA BINADAMU KUHUSIKA NA MAUAJI YA KUTISHA?
Taarifa hiyo ilivuta hisia za wengi, Ken pia akajikuta kwa namna ya pekee anavutika na habari ile.

'Na mwandishi wetu!
Kutokana na matukio ya kinyama yanayozidi kutokea hapa nchini, Habari za leo limebaini kuhusika kwa vigogo kadhaa na sasa imebainika kuhusika kwa Mkurugenzi wa Haki za Binadamu bwana Maisha Nchagwa wa HRO.
Habari za kuaminika kutoka kwa chanzo chetu zinadai bwana Nchagwa alifanya mauaji hayo mnamo siku ya Jumamosi kwenye shamba lake lililopo huko Mbande nje kidogo ya jiji la Dar. Mauaji hayo yalihusisha kutenganishwa kichwa na kiwiliwili cha marehemu Elinisa.
Inasemekana kwamba vitambulisho vya mtuhumiwa vilikutwa eneo la tukio…”

Ken aliliweka gazeti chini halafu akamtazama Martha usoni na kuhoji,
“Hii habari ina ukweli wowote?”

“Inaonekana hivyo, kwa sababu vitambulisho vya mtuhumiwa vimekutwa eneo la tukio na kama si kweli kwa nini akimbie? Taarifa hapa zinasema anatafutwa na polisi baada ya kutoweka nyumbani kwake na mmh... labda kwa sababu bado uchunguzi unaendelea hebu tuone upelelezi utafikia wapi” Martha alisema akijizuia kuongeza neno.

“Yule jamaa anaweza kuwa amehusika? Sitaki kuamini, anavyokuwa anakemea maovu!”
Ken aliongea kana kwamba hajui chochote, ukweli ni kwamba alijua ukweli kwamba Maisha ni mtu mwadilifu na walifanya kazi na yeye kama timu moja. Wabaya wao sasa ilionekana dhahiri wamedhamiria kuwaangamiza. Tayari Maisha amewekwa kikaangoni.

*†*
Geof alijaribu kutafuta usingizi bila mafanikio. Aliamka na kuketi kitandani. Aliwaza jinsi mali yake yote aliyotafuta kwa jasho sasa ilikuwa inatafunwa na watu wengine tu kirahisi kabisa bila jitihada zozote zaidi ya kutumia udhaifu wake tu, tayari kiwanja chake kilikuwa kimeenda, akiba yake benki na yenyewe imetokomea mifukoni mwa afande mwenye njaa.

Sasa alianza kuwaza kuuza nyumba yake ya kimara. Afanyeje hali amefilisika!. Yote hayo kwa sababu gani? Mwanamke malaya tu! Kwa sababu hakuwa tayari kuonekana kashindwa! Kwa sababu alidhani anaweza kumiliki binadamu! Laiti angekumbuka ule msemo wa waswahili wa akunyimae kunde…, sasa alikuwa kishachelewa.

Watu husema majuto ni mjukuu na sasa aliona maana ya methali hiyo. Alijinyanyua na kuelekea dirishani na kulifunua pazia akaangalia nje. Alitafuta majibu, majibu ya nini? Nini afanye ajiepushe na ukata uliokuwa unamkabili kwa kasi.

Alipata jibu alilokuwa anatafuta. Lilikuwa wapi muda wote? Tabasamu la kifedhuli likaenea usoni mwake. Tabasamu la hila!
Kesho ataenda kazini kwake, huko atachukua fedha nyingi awezavyo. Ndiyo, kwani yeye ni nani? Mhasibu wa TANESCO.

Atahakikisha anachota kiasi cha kutosha kukimbia na kutokomea mbali. Mbali na mkono wa sheria. Nchi za mabepari na mabeberu, ambako kuwa tajiri ni sifa muhimu. Haijalishi utajiri huo unavyopatikana, cha muhimu kodi zao wazipate. Huko ataishi kwa starehe tele. Hatakuwa na haja ya mapenzi ya mwanamke, wanawake wenye kila mbinu za mapenzi watajileta wenyewe. Hatimaye atamsahau Asha.

Alirejea kitandani na usingizi ukamvaa. Ndoto za maisha ya kufuru zikimtia kiburi cha kuthubutu kuhamisha na kutokomea na fedha za umma huko ughaibuni.

Itaendelea
David.
FB_IMG_1591786598873.jpg
 
21
Mheshimiwa the Don
David Ngocho David Samson

*†*
Chumba kilikuwa na ubaridi wa wastani, kiyoyozi kilifanya kazi vizuri na kumpa burudani mwanana. Samani zake kutoka nchi za magharibi zilipendezesha ofisi yake si haba. Meza ilisheheni vitabu na kalamu, kulikuwa na kompyuta ya kisasa na kwa pembeni kulikuwa na ashtray ya kukung'utia jivu la sigara zake za gharama! Wenyewe wakiziita cigars!

Mkononi, The Don alikuwa ameshika cigar lake kwa ufahari, Arturo Fuentes Opus X', cigar ya tatu kwa gharama duniani, watumiaji wakiisifia kwa ladha ya kipekee kokote duniani. The Don, ni miongoni mwa matajiri wachache duniani waliomudu kuvuta cigar hizo, ikimweka Mabruki katika daraja la juu la ukwasi. Kwa bongo, zilikuja kwa oda maalum, oda ya mheshimiwa Mabruki.

Mlango wa ofisi hiyo uligongwa na ndani akaingia Estivan Brown, alikuwa amevaa fulana ya kahawia iliyomkaa vema na suruali aina ya jinzi la bluu mpauko.

Kijana huyo alimwamkia The Don kwa heshima zote kuonesha utii usio dosari na kuitikiwa kwa sauti nzito ya mtetemo. The Don akavuta mtemba wake na kuachia moshi mzito ukielea hewani huku akiukodolea macho kwa husda. Ilikuwa inampa ufahari kufikiria tu tamu ya cigar yake aliyogharamia kwa karibia laki nane za kibongo, cigar moja tu!

Mezani kwa Mheshimiwa the Don, Estivan aliona gazeti la siku hiyo lenye kichwa cha habari;
‘MKURUGENZI WA HAKI ZA BINADAMU KUHUSIKA NA MAUAJI YA KUTISHA?’
Alivutiwa na habari ile. Kichwa cha habari kilichotokeza swali ambalo lilihitaji kujibiwa na kumpa hamasa msomaji kuzama kwenye habari kamili. The Don akaliona hamaniko la mshituko wa Estivani Brown baada ya kuona ile habari. Akaweka pozi la ushindi na kutamka;

“Kijana inaonekana habari imekusisimua sana". Tabasamu la zirael likasomeka usoni pake, tabasamu la ushindi likichanua na kuruhusu moshi wa cigar yake kupenya kwenye pambizo za midomo yake mipana, huku akijizungusha kwenye kiti chake usawa wa nusu duara, shati jeupe likiwa limechomekwa kwenye suruali yake nyeusi yenye suspenders zilizopishana vema kwenye tumbo lake Kubwa lisiloishiwa hamu ya kupokea mavyakula na mavinywaji ya kila namna. Ungedhani mheshimiwa Mabruki haendi chooni kwa jinsi likitambi lake lilivyokuwa kubwa!

“Kweli mzee, sasa tumebaki na Machera tu” Estivani Brown alitamka akimkazia macho bosi wake. Haikuyumkinika kama kuna wakati kijana huyo hatari Estivan Brown alipata wasaa wa kuonesha meno yake ishara ya furaha kama binadamu wa kawaida, yeye alikenua meno pale alipoondoa uhai wa mtu kikatili. Furaha yake pekee ilikuwa anapotesa na kuua au yeye mwenyewe kupitia mateso makali. Ajabu!

Estivan Brown alilitupia gazeti lile mezani halafu akatamka kwa dhati ;
“Huyo mtu ni lazima auawe la sivyo tutaumbuka mzee.” Estivani alizungumza akitoa pendekezo. Hamu ya kumwaga damu ikimkereketa moyoni. Kwa mtu wa kaliba yake, muuaji mashuhuri, kumwaga damu ilikuwa jambo la kusisimua. Sisimko la raha ambayo wachawi na wauaji wazoefu wangemudu kulielezea kinagaubaga na si mwandishi wa mkasa huu.

The Don alitikisa kichwa kama ishara ya kuafiki alichosema Estivan. Tafakari fupi iliyopita Kichwani mwake, ikampa wazo muhimu, hivyo, akiwa kama aliyezinduka usingizini, Estivan alitamka,
“Mzee, kuhusu Chale, nadhani tunahitaji kufanya kitu kabla hatujachelewa pia”

“Unashauri tufanye nini?” The Don aliunguruma, mkono wake ukiparaza kipara chake kilichoanza kuenea kwa kasi kwenye kichwa chake cha mviringo na utosi uliobonyea kiasi cha konzi moja.

“Inabidi tumuokoe au tumuue kabla hajafikia hatua ya kutoa siri juu ya kuhusika kwetu” Mabruki akaguna akitikisa kichwa kama anayetafakari jambo, halafu akatamka;
“Wazo zuri" na kuongezea amri katika kauli hiyo ya kukubaliana kimawazo na Estivan Brown.
“Fanya hivyo haraka”.

Estivani akainama kuonesha utii halafu akageuka na kutoka ofisini akiurudishia mlango taratibu.

The Don akavuta pafu nyingine ndefu na kuachia moshi uliokijaza chumba cha ofisi yake na kukung'uta pisi la cigar yake kwenye ashtray akijizungusha kama pia kwenye kiti chake huku akisikilizia stimu ya cigar lake!

*†*

Usiku wa saa tano, mvua kubwa ilikuwa inanyesha, jiji la Dar es salaam lilinururishwa na umeme wa Tanesco. Alikuwa amevaa koti refu la kuzuia mvua, akiwa ameambatana na vijana watano kutoka usalama wa taifa. Machera na wenzake waliingia kwenye Land Rover na kutoka mbio kuelekea mitaa ya Upanga.

Haikuwachukua muda mrefu kabla ya kufika eneo husika, taa kali ziliwakaribisha nyumbani kwa Mabruki. Machera alitoa ishara mbalimbali halafu kila mmoja akajipanga vema na kwa haraka sana makazi ya Mabruki yakawa yamezingirwa.

Alex ambaye pamoja na kuwa kwenye kikosi cha ‘ulipo tupo’ alikuwa ni mtaalam wa umeme.
Alizunguka nyuma kidogo ya ukuta wa fensi na kupata upenyo ambao ulimwezesha kumkabili mmoja wa walinzi wa kasri hili la Don. Akiwa tayari amekwea ukuta ule Alex aliruka na kutua juu ya mwili wa mlinzi ambaye tayari alikuwa maiti. Wenzake walikuwa wamefanikiwa kumtoa uhai mlinzi yule. Aliutelekeza mwili wa mlinzi na kusonga mbele.

Ghafula alipata hisia kali na kugeuka nyuma, kitendo hicho kilimuokoa na shambulizi la mlinzi mwingine aliyekuwa anamrushia rungu. Alichupa pembeni na kulikwepa rungu na kummiminia risasi adui yake. Alikimbia na kuingia chini ya gari moja miongoni mwa magari yaliokuwa yameegeshwa kwenye karakana ya The Don.

Kimya kikatawala, mara alisikia mlango wa gari unafunguliwa, mzee wa makamo mnene, amefuga nywele ndefu na kitambi kikubwa, ngozi kama ya watu wa mashariki ya kati, aliingia ndani akifuatiwa na vijana wawili, gari lilitiwa moto na kuondolewa kwenye makazi ya The Don.

Kitu ambacho wale watu hawakujua ni kwamba walikuwa wamepata kampani mpya ndani ya gari lao. Alex alikuwa ameingia ndani ya gari lile.

Taarifa walizopata, Machera na wenzake zilikuwa za uhakika. Walipashwa taarifa za kuwepo biashara haramu ya dawa za kulevya ambayo ilifanyika hapo nyumbani kwa Waziri Mabruki the Don. Walifika lakini huenda kwa kuchelewa kwa maana ya lile gari lililoondoka na Alex lilikuwa na wahusika muhimu. Wabia wa Don katika biashara hiyo haramu. Sehemu muhimu ya ushahidi wa operesheni hiyo.

Akiwa amesimama mlangoni, The don alilitazama gari lile kwa tabasamu pana likipotelea getini. Kukatika kwa umeme halikuwa jambo la kushangaza hasa kwa muda kama huo, na hata kama angekuwa na kazi, kulikuwa na umeme wa ziada jengoni mwake.

Alirejea ndani huku akivuta - vuta suspender za suruali yake, tabasamu likitia mgomo kuondoka midomoni mwake. Alikuwa amefunga dili la fedha nyingi sana.
Katika kasri lake hilo, The don alikuwa na ofisi kubwa ambayo kwa sehemu kubwa ilitumika kwa dili zake za kimagendo na ufisadi.

Alitembea kwa kujiamini na halafu akiwa ameifikia meza yake aliketi na kwa tabasamu akashika mouse ya kompyuta na kwa sauti kubwa kiasi akajisemea zake;

‘Kwisha kabisa habari yake, hawezi kucheza na The Don, nothing will stop me now.” (Hakuna wa kunizuia sasa). Hakujua alikuwa chumba kimoja na adui yake mkubwa.
Tayari alikuwa ameingiza habari kadhaa za kibiashara kwenye kompyuta yake na kwa mshtuko mkubwa akageuka nyuma baada ya kusikia sauti ikisema,

“Kwisha habari yake na sasa ni habari yako. Habari ya kupotea kwako The Don au siyo, mheshimiwa?” mshituko uliomvaa, Kidogo umdondoshe chini the Don. Akafanya jitihada kugeuka nyuma.

Itaendelea.
David.
FB_IMG_1591786598873.jpg
 
23
Mheshimiwa the Don
David Ngocho Samson

*†*†
Katika moja ya vyumba vya ardhini ndani ya jengo la The Don, alikutwa Maisha akiwa amefungwa kwa nyaya mithili ya nguruwe tayari kwa kupigwa shoka awe kitoweo.

Hiyo ilikuwa baada ya kutafutwa zaidi ya nusu saa hivi ndani ya jengo hilo, huku akina Machera wakijionea utajiri na ufuska wa The Don. Ilikuwa vigumu kuamini kuwa uchafu wote ule ulifanywa na mheshimiwa yule.

Jumba la The Don lilikuwa jumba la kifahari hasa, ilikuwa vigumu kuamini kuwa Tanzania nchi maskini ilikuwa na matajiri wakubwa kama The Don. Fahari ya Mabruki ilikuwa zaidi ya ikulu ikiwa na kumbi za mikutano za kisasa kabisa na fenicha kutoka mataifa makubwa ya ulaya na marekani.

Mbali na hayo, mlikuwa na casino chini ya jengo hilo ambamo ufuska aina zote ulifanyika, kulikuwa na picha za ngono kila kona ya casino hilo, kwenye jukwaa kulikuwa na eneo ambalo lilikuwa na machine bila shaka ya kukata vichwa vya adui wa mipango ya kundi la The Don. Altare ya Mauti.

Machera alihisi harufu ya mauti, ni muda mfupi uliopita alikuwa amepewa somo juu ya altare hiyo, ambayo kama The Don angefanikiwa basi angemtundika pale pamoja na Maisha kama sadaka. Baada ya hapo, bila shaka ile habari aliosimulia The Don ingefanyika, ambako matendo yote ya giza yangefanyika ikiwa ni pamoja na kulewa na kufanya zinaa kwa washirika waume kwa wake, waume kwa waume, wake kwa wake, mke kwa waume na kila aina ya zinaa huku wakijidunga madawa ya kulevya.

Maisha alishukuru msaada wa Machera na wenzake kwani bila shaka alikuwa anahesabiwa saa tu ili kufika mauti. Baada ya hapo walimchukua Maisha na kumpeleka hospitali kuchunguza afya yake kwani kwa siku tatu alikuwa gizani akipewa vyakula ambavyo hakuwa na hakika kama ni vya kiafya au huenda vilikuwa na madhara kwa afya.

Machera na wenzake walikuwa bado kumaliza kazi.


*†*

Ndani ya gari la mshirika wa Don kibiashara, yule aliyekuwa katoka kufanya biashara haramu ya dawa za kulevya, Alex alikuwa kimya masikio yakipata habari na mazungumzo ya wale jamaa. Aligundua kuwa, miongoni mwao alikuwamo mwarabu ambaye hasa alikuwa na sauti yaani boss wa kikosi hiki.

Hatimaye gari lile lilikanyaga breki, harakati za kufunguliwa kwa geti zikasikika. Gari likaingia ndani ya fensi likipokelewa na kelele kali za mbwa. Baada ya kugundua ni wamiliki wao wale mbwa walifyata mikia yao na kubaki kimya. Walishuka na kufungua buti la gari na kutoa pakiti tano za madawa ya kulevya aina ya cocaine yaliyokuwa kwenye vifuko vya glucose. Baada ya zoezi hilo waliingia ndani na kumpa fursa Alex kujitoa ndani ya gari lile na kufanya mawasiliano baada ya hapo alikata umeme ndani ya jengo hilo la waarabu.

Giza lilitanda eneo zima la Mbezi Beach, Machera na Mwita waliingia ndani kwa kuruka ukuta wa jengo la waarabu. Akiwa ndani Alex alishuhudia mwanga wa tochi ukielekea eneo alilokuwa amesimama. Kwa kuruka sarakasi Alex aliipiga teke ile tochi ikadondoka chini huku nyuma akimshushia kibano yule mwarabu. Aliinama kuokota tochi na hilo likawa limemgharimu kwani alipata kipigo kikali toka kwa mwenzie na mwarabu.

Mlangoni alikuwa anaingia Mwita na kushuhudia tukio lile na kwa haraka sana akamuwahi Alex na kumsaidia kumtoa kwenye eneo la hatari. Akiwa anatoa huduma ya kwanza Mwita alisikia gari linatoka nje kwa kasi, alitoka nje kujua kulikoni, huko alimshuhudia Machera akiwa taabani hajiwezi.

“Oh my God nini tena?” Mwita alihamaki.

“Mwita” Machera alitamka kwa sauti ya maumivu.

“Naam” akaitika Mwita.

“Steve na Andrew wako wapi?”

“Wamezunguka upande wa pili kwenye maghala”

“Hapana Mwita, wale si wenzetu ndio walionimiminia risasi hizi. Hakikisha wanapatikana na kufikishwa panapostahili, sawa?”

“Sawa, pole sana bosi” Mwita alijibu na kufanya jitihada za kumuwahisha hospitalini pamoja na Alex aliyekuwa amejeruhiwa vibaya na rungu kwenye paji la uso.

Machera alikuwa amejeruhiwa vibaya na risasi kwenye mguu wake wa kulia, hata walipofika hospitali Machera alikuwa hana fahamu ni nini kilikuwa kinaendelea. Ilibidi kulazwa kwa lengo la kufanyiwa operesheni ndogo. Ilikuwa bahati tu kwani risasi ile ya pajani ilibaki sentimita kama mbili tu iukwangue mfupa wake wa pajani. Iliishia kupenya na kujikita Jirani na ngozi ya pili ikidhamiria kutoboa upande wa pili.


***

Anastazia alikuwa sokoni kariakoo asubuhi ya saa mbili. Alinunua gazeti la NIPASHE kufuatia kichwa cha habari "Jambazi lauwawa na majambazi kituo cha polisi”

Gazeti Hilo liliandika 'Mtu anayedaiwa kuwa jambazi kwa jina la Chale Mng'umba aliyekuwa akishikiliwa na polisi wa kituo kidogo cha Mbande ameuwawa. Habari zilizotufikia zinasema marehemu ameuwawa na majambazi waliokuwa na silaha kwa lengo la kuficha ukweli ambao hata hivyo ulikuwa umebainika tayari. Ukweli wenyewe ni juu ya kifo cha raia wa Marekani aliyeuwawa hivi karibuni bwana Elinisa Urio.

'Habari za kuaminika zinadai kwamba tukio hilo linamhusisha kiongozi mmoja wa serikalini ambaye jina lake bado halijafahamika……' alilifunga gazeti na kupokea simu iliyomtaka kufika Aghakhan Hospital haraka sana.

Hakuuweka usiku, alizama kwenye gari lake na kukanyaga mafuta. Vuum!! Gari iliitika 'labeka' ikitimua vumbi la kufa mtu.

Mwendo!

Likatimua mbio likiwaacha washuhudiaji wakitokwa na mitusi ya nguoni kwa ghadhabu, huku wakijifuta vumbi nyusoni mwao!

Aliwasili hospitalini hapo na kuelekea chumba alichoambiwa kwenda. Kitandani alilala Machera patina wake wa ukweli. Mwanaume aliyekuwa anamhusudu na kuomba siku moja wawe wote kimaisha.

“Machera” alitamka kwa mshangao uliochanganyikana na hisia za majonzi. Akamsogelea na kumbusu usoni.

“Usijali mpenzi, si kitu, nitapona maadam kwa huba na makini kama kuku anavyomlinda kifaranga dhidi ya mwewe upo hapa na upo tayari kunisaidia.” Machera aliongea huku akibubujikwa na machozi. Ana alimfuta machozi kwa kitambaa chake.

“Niahidi kwamba utanisaidia mpenzi.” Machera aliongea huku akimshika mkono Ana.

“Naahidi.”

“Sawa, Steve na Andrew ndo walionifanya hivi, tafadhali hakikisha wanatiwa mbaroni.” Machera akatoa agizo macho yake ya kikamanda yakigoma kuonesha ukamanda wake. Washezi wale walidhamiria kumtoa uhai au kumtia ukilema wa kudumu. Machozi yalikuwa yakisitasita kutoka, huenda yakihofia kuonesha udhaifu wake mbele ya mwanamke huyu aliyefahamu ujasiri wake pekee! Hakuwa tayari kuonesha upande wake wa udhaifu. Hakuwa tayari kudondosha chozi mbele ya Ana.!

“Wale ni wenzetu mpenzi unadhani wanaweza kufanya hivi?” Ana akahoji kama alokumbwa na mshangao.

“Nipo timamu Ana. Nimewashuhudia wakitekeleza unyama huu, kwanza kwa Alex halafu mimi, kamuone Alex chumba kinachofuata na atakupa picha kamili ya tukio hilo kwa sababu yeye alipata nafasi ya kuwasikiliza. Unaweza ukapata wazo la jinsi gani uwapate” Machera akafafanua. Hata hivyo maumivu yake hayakumpa nafasi, uchozi ukadondoka!

“Sawa mpenzi, nitafanya hivyo. Najua utapona, sipendi mwanaume kutoa machozi, tafadhali jikaze kiume. Nakupenda sana.” Ana akatamka huku akibusu kiganja cha mkono wa kulia wa Machera.

“Nakupenda pia” Machera akatamka aibu ikimjaa hadi pomoni.

Ana alitoka na kufunga mlango nyuma yake. Kwenye korido alikutana na mwanamke aliyevaa baibui akiwa amefunikwa mwili wote isipokuwa macho tu. Mwanamke huyo alijifanya anaingia chumba fulani lakini alipohakikisha kuwa Ana amepotea aliingia chumba alimokuwa Machera.

Akiwa anashuka ngazi, Ana alihisi moyo wake unakuwa mzito. Alirudi haraka haraka kwa mwendo wa kunyata. Alifika mlangoni na kuchungulia kwenye tundu la kitasa cha mlango na kumuona Yule mwanamke mwenye baibui akiwa amenyanyua bastola. Alifungua mlango na kwa kasi ya ajabu akajitoma ndani na kumvaa yule mwanamke na kufanikiwa kumnyang'anya ile bastola.

Walimvua baibui, msichana mrembo miaka 17 hadi 20, sura yake nzuri isiyo na kovu. Alitetemeka kwa hofu na wasiwasi, uso wake ukiomba msamaha bila kutoa maneno.

“Unaitwa nani binti?” Machera alihoji.

“Jacqueline Msoffe” machozi yalimtiririka binti Huyo.

“Lengo lako nini?” Ana akahoji.

“Tafadhali nisameheni, sikuwa na lengo la kukuua ila nimelazimishwa na majambazi waliokuwa wamevalia kijeshi. Hao ndio wamenilazimisha nikuue. Nisingekuua, nilitaka nikutishe tu halafu nikueleze ukweli huu.” Machozi yalikuwa yanamchuruzika.

“Kwa nini umekubali?” aliuliza Ana

“Sikuwa na jinsi ya kukataa kwa sababu wamemchukua mtoto wangu na wametishia kumuua nisipokuua na halafu waniue na mimi.”

“Mtoto wako? Una mtoto wewe?” alihoji Machera.

“Ndiyo”binti alijibu.

“Umeolewa?”

“Hapana, nilipewa ujauzito na mwanafunzi mwenzangu”

“Anaitwa nani?” Ana aliuliza na kujikuta anaangaliwa kwa mshangao na Machera. Ukweli ni kwamba haikuwa sura ngeni sana machoni pake. Lilikuwa swali lililokusudia kuthibitisha jambo ambalo lilikuwa kichwani mwa Ana.

“Hebu muulize waliomtuma wako wapi na wanaonekana vipi” aliingilia Machera.

“Naomba jibu langu” Ana alitoa amri.

“Anaitwa David” alijibu huku akitetemeka.

“Haya toa majibu aliyouliza”

“Mmoja ni mweusi mwembamba ana kovu kwenye shavu la kushoto. Mwingine ni maji ya kunde, mzuri kwa sura na macho yanayomeremeta.” Binti yule alidadavua kinagaubaga mionekano ya watu hao waliomtaka Machera afe.

Kwa maelezo aliyokuwa ametoa hakukuwa na shaka kuwa kwa mara ya pili Steve na Andrew walikuwa wamefanya jaribio la kumuua Machera.

“Wako maeneo ya ufukweni” alimalizia Jacque.

Ana alivaa baibui lililokuwa limevaliwa na Jacque na kutoka kuelekea kwa maadui wao.


*†*

ILIKUWA yapata siku ya tatu Asha akiwa anasumbuliwa na tumbo, mara kichefuchefu, kutapika na zile tabia za kupenda malimao machachu. Alikuwa na ujauzito. Baada ya kwenda hospitali aliambiwa ana ujauzito wa wiki mbili.

Tatizo likawa kutambua ni mimba ya nani hasa, wiki mbili zilizopita aliachana na Geof na alikuwa amefanya mapenzi na Geof, na pia alifanya mapenzi na Elinisa. Moyoni mwake lakini aliomba iwe mimba ya Elinisa. Licha ya kukaa na Elinisa kwa kipindi kifupi sana Asha alipata mapenzi ambayo hakuwahi kuyapata kwa Geof. Alitamani kwa moyo wote iwe mimba ya Elinisa. Alijikokota na kujilaza kitandani usingizi ukamchukua.

Aliangalia saa yake, ilikuwa yapata saa 10 jioni, alitembea kuelekea kituo cha teksi na kusimama kumsubiria mtu aliyeonekana kumpungia mkono. Mawazoni mwake alijaribu kuvuta kumbukumbu ya nani yule aliyekuwa anamkimbilia huku akitweta. Ni dhahiri hakumjua.

Alikuwa mwanaume mwenye kifua kipana amevalia fulana na jinzi la bluu.

“Habari yako dada Asha?” Yule jamaa alisalimia. Asha alimwangalia kwa wasiwasi.

“Nikusaidie nini?” Asha akionekana kuboeka vilivyo!

“Dada kuna mtu anahitaji msaada wako na anadai ni wewe pekee unayeweza kumuokoa.”

Yule mwanaume aliongea kwa sauti nyembamba sauti ya kike kitu kilichomshangaza sana Asha. Hata hivyo hakutaka kulizingatia hilo, suala lilikuwa ni ni nani huyo aliyehitaji kuokolewa na yeye.

“Sidhani kama nakuelewa, nina haraka sana na wewe unanichelewesha” Asha aliongea na kuanza kuondoka.

“Sikiliza Asha, huna haja ya kunipuuza na sidhani kama ni jambo zuri kwa wewe kulifanya. Niko serious. Elinisa yupo kwenye hali mbaya na anakuhitaji.” Sauti ile nyembamba sasa iliambatana na mamlaka na ujasiri, ujasiri ulioonekana zaidi kwenye mwili wake uliojengeka kiume, mwili wa mazoezi. Kasoro tu sauti ile nyembamba tepetevu ambayo haikuendana na mwili ule iliyochefua kusikia.

“Sipendi kushiriki utani na mtu ambaye hata simjui hasa anapofanyia mzaha jambo la msingi linaloumiza moyo wangu.” Asha alimkaripia kijana yule.

“Dada kwa nini hutaki kuniamini?” Kijana yule alimuuliza.

“Na kwa nini nimwamini mtu nisiyemfahamu?” Asha akaghafilika.

“Ok, naitwa Asajile, Elinisa ni rafiki wa kaka yangu, tunazidi kupoteza muda tafadhali twende” kijana aliendelea kusisitiza.

Katika hali ya utatanishi na kutokuelewa Asha alijikuta anafuatana na yule jamaa. Waliipita nyumba moja kubwa na kuingia uchochoroni.

“Mbona vichochoroni?” aliuliza Asha.

“Yupo kwenye kibanda hicho.”

Asajile aliingia ndani ya kibanda kile kilichokuwa kikuukuu. Asha alimfuata. Ndani mlikuwa na vistuli viwili. Alitazama saa yake na kugundua ilkuwa saa 12.15 jioni, giza lilianza kutanda na kuifunika dunia.

Asajile alisikika akiita,

“Kakaa, kaka mkubwa!”

Sauti yake ikamchefua Asha. Kwa nini mwanaume aongee sauti ya kike? Alijiuliza asipate jibu.

Pazia kuukuu lililotenganisha kajisebule na chumba cha kibanda kile lilifunuka na nyuma yake akajitokeza mwanaume aliyekuwa anamfahamu vema. Aliduwaa kwa sekunde kadhaa akijiuliza ni nini kilimpata mwanaume huyo, alikuwa amechoka na kukonda mithili ya mgonjwa wa kifua kikuu.

“Najua unanishangaa, lakini fahamu kuwa ni kwa sababu yako. Na hapa ni mwanzo tu. Hata hivyo nafurahi kuona unazidi kunawiri na kupendeza. Lakini nyuma ya huo uzuri maisha ya watu watatu yameharibiwa, Elinisa, mimi na waziri Mabruki. Nimekuita kwa sababu nahitaji kukuaga, nataka nitokomee mbali na dunia, sijui ni akhera au ni jehanum ila nina hakika si peponi. Nilikupenda sana na haya yote ni kwa sababu nilikupenda. Sitaweza kutumia maisha yangu yote kifungoni. Heri nife” machozi yalimtoka na kwa kushindwa kujizuia Geof akaangua kilio kama mtoto mdogo.

Kwa muda wote huo Asha alijikuta anakumbuka zamani,

Alikuwa amekaa mgongoni mwa Geof, kamshikilia masikio, halafu akamnong'oneza;

“Geof wewe ni wangu wa kufa na kupona”.

Geof akajigeuza na kumwangalia usoni kama vile hamjui na kusema;

“Sio muda wa kutoa promise. Kama yanatoka moyoni hebu nibusu usoni.”

Asha akapitisha mkono wake kifuani kwa Geof na kuzipapasa nywele zilizosheni kifuani, Geof aliyekuwa ametulia, mikono yake ikazunguka kiunoni mwa Asha akapapasa maungo yake vidole vyake vikitalii pingilipingili za shanga zilizotandazwa vema pale mwinuko wa makalio yake yaliyoshiba unono unaovutia kuona hasa ukiwa ndani ya vazi tepetevu na kutia hamasa, hali akijinyonganyonga juu ya mwili wa Geof, Asha akawa anachezea midomo ya Geof, akatoa ulimi wake huku akihema na kuupitisha shingoni mwa Geof, taratibu akaupandisha hadi usoni akabusu paji la uso, hivyo hivyo ulimi wake ukaendelea kutembea usoni mwa Geof hadi kufikia kwenye pua na hatimaye mdomoni. Hapo ulimi wake ukazama kinywani mwa Geof.

Asha akawa kama amezinduka. Akamkumbatia Geof kwa nguvu na kumsihi asife.

Hali akimbembeleza asife, mlango wa kibanda ukapigwa teke na mlangoni akasimama mwanaume aliyekuwa na bastola mkononi. Bila kusema chochote mwanaume yule akamfyatulia risasi tatu kifuani. Geof akadondoka chini na kufa machoni pa Asha. Asha akapiga kelele za kuomba msaada na kudondoka chini kutoka kitandani. Akazinduka usingizini huku akihema.

“Oh God, kwa nini naota ndoto mbaya namna hii?”

Huku akijifuta jasho, akafungua mlango kuingia bafuni, ilikuwa saa12.30 asubuhi.

FB_IMG_1591786598873.jpg
 
24
Mheshimiwa the Don
David Ngocho Samson

*†*

Jackline, yule binti ambaye alitumwa kutekeleza mauaji kwa niaba ya mamluki wa Don ndani ya jeshi, yaani Steve na Andrew, alibaki hospitalini akisubiri na kuomba Mungu asaidie ili Ana arejee na mwanae salama. Machera alimwangalia kwa udadisi. Mkononi Jacque alikuwa na simu yake ndogo Aina ya tekno.

“Simu yako ina salio la kutosha?” aliuliza machera.

“Ndiyo, ina kama shilingi mia nane hivi” akatamka huku akimkabidhi Machera simu. Machera akaipokea na kubonyeza namba kadha wa kadha.

“Halo, Machera hapa, naomba vijana wanne wafike hapa hospitalini kiraia, sasa hivi” Machera akatoa agizo.

Akamkabidhi Jacque simu yake.

“Una umri gani Jacque?”

“Nina miaka kumi na nane” alijibu Jacquline.

“Oh na umesema ulipewa mimba na David, yeye ni nani na yupo wapi sasa?”

“Jina lake kamili ni David Mwita Mohere. Kwa sasa sijui aliko, baada ya kunipa mimba aliondoka, niliambiwa yuko Mbeya"

“Umesema Mwita Mohere?” Machera akauliza kwa mshangao. Jacqueline aliitikia kwa kutikisa kichwa.

“Oh, huyo dada aliyeondoka humu ndani, aliyeniokoa na risasi yako ni wifi yako” Machera akamtaarifu huku akipata jibu kwa nini Ana alisisitiza kujua aliyempa mimba. Itakuwa alifahamu uhusiano wao ingawa wenyewe bila shaka hawakujua.

“Hapana mimi sina wifi, bado sijaolewa” Jacqueline akajibu kwa msisitizo. Kila alipokumbuka kitendo Cha David, alikuwa anapatwa na hasira. Hakutaka kabisa kusikia habari zake, wala hakutaka kuhusiana na yeyote yule ambaye ni nduguye.

“Najua, lakini huyo dada ni dada yake na David ambaye alikupa mimba, kwa hiyo ni wifi yako” Machera alijibu, Jacque alikaa kimya. Hakutaka kuendeleza mjadala wa David.

“Usiwe na huzuni nina uhakika wifi yako atarudi na mwanao salama salimini.” Machera alimhakikishia!

“Kaka hujui ni jinsi gani nampenda mwanangu Davidson, siwezi kufurahi wakati mwanangu yuko mikononi mwa majambazi.”


****

“Oya anakuja.” Steve alimweleza Andrew. Walikuwa wamekaa juu ya bonnet ya gari lao ufukweni mwa bahari ya Hindi, mkabala na hospital ya Aghakhan.

“Nani?” Andrew alihoji

“Yule mwanamke" Steve alitamka akikazia macho yake pale alipoonekana mwanamke husika.

"Sasa fanya hivi, nenda kahakikishe kama amekufa kweli.” Steve alimwambia Andrew.

Anastazia alipiga hatua moja ikifuatiwa na nyingine, alikuwa ndani ya baibui alilokuwa kavaa Jack hapo awali, hivyo lilimpatia taswira ya Jackline. Katika kuwafumba wabaya wake, Anastazia alionekana akifuta machozi. Andrew alivua jaketi lake na kubaki na shati lake la mikono mifupi, halafu akaondoka na kuelekea hospitalini njiani akipishana na Anastazia.

“We mwanamke umefanya tulivyokuagiza?” alihoji Steve.

“Ameenda kuhakikisha, sasa ole wako ionekane umedanganya, haka katoto tutakatoboa macho na wewe mwenyewe tunakubaka na kukukata ulimi ili usimsimulie mtu yeyote habari yetu.” Steve akamtishia.

Hali akifikicha macho, Ana aliisogelea gari. Steve alikuwa anaangalia kule alipotokea Ana. Kwa macho yake ya kikachero, aliona gari aina ya Noah yenye vioo tinted inapaki, walishuka askari wawili aliokuwa anawafahamu vema, machale yakamcheza,

'Tumechezewa mchezo, shit!' aliwaza na kumgeukia Ana kwa lengo la kumzaba makofi. Aliduwaa kukutana na mdomo wa bastola na tabasamu mwanana la kejeli likiwa katika sura ya Anastazia.

“Mikono juu,” aliamrisha Ana.

Steve hakuwa na ujanja mdomo wa bastola ulikuwa umegusa kabisa ngozi yake ya shavuni.

“Wasaliti, kwa faida gani? Teremka na angalia usijaribu ujanja wowote, kichwa chako ni halali yangu” Ana alisonya.

Katika harakati za kuteremka Steve alitoka mbio, Ana bila kufikiri akamfyatulia risasi iliyompata kwenye mguu wa kulia na kumwangusha. Alimfuata.

“Nishasema usijaribu mzaha, nitakumaliza mwanaharamu wewe.”Ana akafoka kwa hasira.


*†*

Wodini kwa Machera mlango uligongwa, Machera akahisi moyo unamuenda mbio, ni kama alihisi hatari.

“Jacque, ingia chini ya kitanda, haraka” alinong'ona kwa amri.

Haraka sana Jacque aliingia chini ya kitanda. Uzuri wa vitanda vya hospitalini, vinakuwa na uwazi wa kutosha chini, kwa maana vinakuwa vimeinuka juu. Hofu aliyokuwa nayo mwanzoni ikachanua mithili ya waridi. Alihema kwa nguvu.

“Tulia” aliamuru Machera.

Machera alijilaza kitandani sawa na maiti.

Andrew aliyekuwa mlangoni baada ya kujibiwa na kimya aliusukuma mlango na kuingia ndani. Alimkuta Machera amefunikwa na shuka gubi gubi. Alivuta shuka akiwa ameelekeza bastola yake kitandani. Alinyanyua bastola yake na kuishusha kichwani kwa Machera na kumtandika kwa kutumia kitako chake. Machera alitoa kelele za maumivu huku akiita manesi kwa ajili ya msaada, hilo lilimkera mno Andrew ambayo alitumia mkono wake wa kushoto kumziba mdomo.

“Kumbe hujafa tu, sasa sitafanya makosa” Andrew alitamka akiwa amemkazia macho.

“Tafadhali Andrew fikiri unafanya kosa gani hapa. I am your boss (Mimi ni bosi wako)” Machera akajitetea.

“Hell you are my boss,” (Bosi wangu! bosi gani?) Andrew akaongea kwa bezo na kuongezea

“….na usijifanye kunijua, maana haitakusaidia, kwa taarifa yako tu bosi wangu ni shekeli si mpuuzi kama wewe. Sasa kwa vile huu ndo mwisho wa maisha yako, nakupa fursa ya kumkumbuka Mungu wako huenda akakupokea mahali pema peponi, fanya hivyo kabla sijafikia namba tatu.”

Alianza kuhesabu moja. Akiwa chini ya kitanda Jacque alipatwa na ujasiri ghafula, maisha ya mtu yalikuwa kwenye mstari hapa, alihitajika kutoa msaada, alisikia tatu” akanyanyuka kwa kasi na kuibeba miguu ya Andrew juu na kumfanya akose balansi kabla ya kujua nini kilikuwa kinatokea, bastola ilikuwa imedondokea usawa wa Jacque na sasa ilikuwa mikononi mwa Jacque. Anapoinuka, Andrew alikutana na mdomo wa bastola yake ukiwa umemkenulia meno.

Katika harakati hizo mlangoni waliingia askari aliokuwa ameagiza Machera wafike hospitali. Machera alikuwa anatokwa na damu na kulikuwa na nundu kubwa tu eneo alikopigwa na kitako cha bastola.

Akiwa anaugulia maumivu, Machera aliagiza Andrew atandikwe virungu na halafu atiwe pingu zoezi lililofanyika mara moja.

“Namtaka mwanangu” Jacque aliongea huku akimpiga ngumi ya usoni Andrew kwa hasira huku akibubujikwa na machozi.

“Usijali Jacque utampata mtoto, nashukuru umeniokoa” aliongea Machera huku akimshika mkono kumfariji.

ITAENDELEA
David Ngocho Samson

FB_IMG_1591786598873.jpg
 
25
Mheshimiwa the Don
David Ngocho Samson

***
Akitokea kliniki, Asha alinunua gazeti lililokuwa na habari juu ya kifo cha Geof, alilisoma na halafu akaliweka chini, akili yake ikiwa kama cd inayoscratch, aliduwaa na gazeti mkononi. Alisubiri machozi yamdondoke, hayakudondoka, asingeweza kuomboleza. Alikwishaomboleza ndotoni. Ukweli ulibaki kuwa yeye alikuwa sehemu ya tatizo, yalitokea ya kutokea na hakuwa na jinsi ya kuyazuia. Isitoshe maisha mengine yalikuwa yanaanza tumboni mwake, haya yalikuwa muhimu zaidi ya yaliyopita. Aghalabu alikuwa na uwezo juu ya haya. Alifika nyumbani kwake na kujilaza kitandani. Huenda akaomboleza vizuri katka ulimwengu wa ndoto, aliwaza, na haukupita muda usingizi mzito ukamfunika mithili ya blanketi la sufi.

***
Katika ukumbi wa Dar Live Mbagala, mwanamuziki maarufu nchini Tanzania alikuwa anatumbuiza. Ukumbi ulifurika watu kutoka kila kona ya jiji la Dar es salaam wanaopenda kuburudika. Naam, kupata burudani ya kuwaondolea hofu za kodi, hasira zitokanazo na mikwaruzano ya kazini, hofu ya kesho, na ada za watoto.

Kwenye kona moja upande wa VIP kulikuwa kikao, kikao kati ya Estivani Brown yule muuaji wa kinyarwanda, Inspekta Matilda Msango, mwanamke kutoka jeshi la polisi nchini. Chirundumusi pia alikuwepo kwenye kikao hiki cha siri. Na vijana wengine kadhaa waliokuwa waasi wa jeshi la polisi. Wakimtumikia The Don, na hapa kulikuwa na taarifa. Tukio la The Don kuwa mikononi mwa polisi likitafutiwa ufumbuzi yakinifu

“Kwa hiyo Mati, unataka kusema kesho ndio uhamisho utafanyika sio?” Chirundumusi alimtupia swali Inspekta Matilda aliyekuwa kavalia nguo mithili ya changudoa au kahaba ikikupendeza zaidi. Huyu hakuwa changudoa hata hivyo. Alikuwa mtu muhimu upande wa Don, akiwa mpashaji wa habari nyeti za polisi kama ilivyokuwa kwa mamluki wake wengine kwenye idara nyeti za serikali. Naam, huyu alikuwa ni Inspekta katika jeshi tukufu la polisi la Jamhuri ya muungano. Alijuwa mtu aliyeaminiwa kutunza kiapo cha utii kwa serikali, lakini leo alikuwa hapa akitoa siri zilizohusu mtu hatari kabisa nchini na akishiriki kikamilifu katika kikao cha kupanga njama za kufanya yale ambayo yangeliaibisha jeshi hilo la polisi.

Matilda Msango, mwenyeji wa Njombe kwa kuzaliwa, mrembo mwenye maisha ya juu kulinganisha na askari wenzake wa hadhi yake. Akimiliki magari ya usafirishaji mizigo maarufu kwa jina la ‘uzalendo kwanza Exp’. Ni huyu pia ambaye siku za karibuni alikuwa kaaminiwa na raisi wa Jamhuri ya muungano na kuteuliwa awe afisa mkubwa kwenye kitengo nyeti. Hata hivyo, ikiwa vigumu kumjua msaliti, Siku tatu kabla ya kula kiapo cha utii kwa cheo kipya alichoteuliwa, tayari alikuwa anaisaliti Jamhuri kwa kuunda njama na watu dhalili.

Kikao chao kilisuka mipango, mipango ikasukika. Ambacho kingetokea baada ya kikao hiki kingeushangaza umma wa watu wa Jamhuri ya Muungano na kutikisa msingi wa nchi. Umoja wetu wa kitaifa.

*†*
Wakati Estivan Brown na wenzake wakiendelea na kikao chao cha siri kwenye eneo la wazi, katika ukumbi wa burudani, katika nyumba ya Waziri Sebastian Masebo, waziri wa mambo ya ndani, kulikuwa na tafrija ndogo ya kusherehekea ushindi wa kumtia hatiani adui wa taifa. Adui aliyemnyima mheshimiwa huyu raha hata akawa ameandika barua ya kujiuzuru wadhifa wake na kutembea nayo mfukoni. Kisa nini? kwa sababu ya mauaji ya kutisha yaliyokuwa yanaendelea nchini dhidi ya albino, watoto wadogo, watu wazima na watu maarufu katika jamii kwa sababu ambazo zilisemekana kuwa ushirikina huku watu maarufu kisiasa wakitekwa na watu wasiojulikana kila kukicha huku lawama zikitupiwa serikali iliyokuwa madarakani na kuichafua katika uga wa kimataifa.

“Asante sana Machera, kwa hakika wewe ni tegemeo la taifa hili. Ni vile tu kwa aina ya kazi yako huwezi kujulikana utendaji wako kama sisi wanasiasa. Utaona kesho magazeti yakinijaza sifa zako kwamba nimefanikiwa kuondoa chanzo cha mauaji yaliyoshamiri nchini. Nataka utakaposikia habari hizo zikihusianishwa na jina langu basi ujue kwa dhati kwamba hizo ni sifa zako.”

Masebo alitamka akiwa amemshika bega Machera.

Muziki ulikuwa unasikika na kuwaburudisha vilivyo. Anastazia pia alikuwepo. Kened na kikosi chao kwa ujumla. Nyama choma zilikuwa zinaendelea kuwiva kwenye jiko la kuhamisha ambalo jioni hii lilitolewa nje kwenye bustani nzuri uani kwa nyumba ya waziri huyu mchapakazi wa taifa linalokuwa kwa kasi kiuchumi, likiwa na daraja jipya kiuchumi, maarufu kwa wengi kama 'uchumi wa kati' kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya kitaifa na kimataifa. Mikononi, vinywaji viliendelea kulainisha koo za wageni waalikwa kwenye kikao hicho adhimu.

"Hapana mheshimiwa, siwezi kubeba sifa zako nikajitapa nimefanya kitu, hata hivyo ni mapema mno kuwaza kuwa huwenda tumemshinda adui yetu. Huyu ni mtu ambaye amekita mizizi hadi kwenye mahakama zetu, ngoja tuone kama mahakama itafanya kitu. Hata hivyo ni muhimu kukaa chonjo. Hatujui wafuasi wake wanawaza nini, lazima tujizatiti katika kuhakikisha hatuachi hata shina moja likichipua. Ni kujifunga vibwebwe na kung’oa mizizi yote. Hivyo ndo tutakuwa na hakika ya kumdhibiti huyu nduli Mabruki the Don.” Machera alitamka kisha akameza funda tatu za kinywaji chake akimpa nafasi mheshimiwa Masebo kuyasharabu maneno yake.

“Umesema kitu sahihi sana kijana wangu, hawa si watu wa mchezo, unapodhani umewadhibiti na kufurahi unaweza kujikuta matatani. Hawana sheria hawa. Muda wowote ni wa kukaa macho dhidi ya hawa mafedhuli wenye kuchukulia maisha yetu kama mchezo wa dezo.” Mazungumzo yao yalivyozidi kunoga ndivyo walivyojipata wakizidi kuwa kundi la watu wakitengeneza mduara. Machera na Masebo wakiwa kama viongozi wa kikao hiki cha watu waliokuwa wakisikilizana, wakiwa wamesimama kwenye viunga vya jengo hili la waziri wa mambo ya ndani mikononi mwao kukiwa na vinywaji mbalimbali.

"Jamaniee huku nyama choma tayari, sogeeeni” ilisikika sauti ya Ken ikitamka kwa sauti kubwa iliyofikia masikio ya kundi hili la wazalendo wa kweli wa nchi mubashara kabisa!

~~

KATIKA eneo la Ubungo mataa kulikuwa kumetokea ajali mbaya sana na ilisemekana mtu mmoja alikuwa amepoteza uhai katika ajali hiyo. Kwa mujibu wa polisi, chanzo cha ajali ilikuwa ni mwendokasi wa gari alilokuwa anatumia marehemu uliopelekea kugongana na karandinga la polisi katika eneo la mataa ya Ubungo.

Taarifa zaidi zilidai aliyegongwa alikuwa ni Geof Mtemvu mfanyakazi wa shirika la umeme la taifa - TANESCO na ambaye pia alikuwa mtuhumiwa wa mauaji ya raia wa Marekani Elinisa Urio, aliyefariki baada ya kuchinjwa mithili ya kuku, kwa sababu ambazo ilisemekana ni wivu wa mapenzi. Taarifa hiyo ilibainika baada ya jambazi lililoshiriki kwenye mauaji hayo, Chale Mwanambeti, ambaye Sasa alikuwa marehemu baada ya kuuliwa katika mtanange wa kurushiana risasi kati ya polisi wa kituo kidogo cha mbande na majambazi wenzake marehemu Chale, huku akiwa ametoa ukweli wote wa jinsi ambavyo walikuwa wameamua kumbambika kesi mkurugenzi wa HRO ndugu Maisha Nchagwa.

Itaendelea
David

FB_IMG_1591786598873.jpg
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom