Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,316
- 33,125
Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, akisisitiza jambo wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, amesema hakutofautiana na msimamo wa Rais Jakaya Kikwete kuhusiana na suala la uchaguzi mkuu wa visiwa vya Comoro unaotarajiwa kufanyika mwakani.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Membe alisema msimamo wa Rais Kikwete ni kwamba uamuzi uliochukuliwa na Bunge la Comoro kuwa uchaguzi mkuu ufanyike Novemba mwakani uheshimiwe.
Huo ndio msimamo wa Rais Kikwete na ndivyo nilivyosema mimi, inawezekana watu walioandika tumetofautiana na Rais walimsikia vibaya wakati ule alipokwenda Comoro, lakini sisi tunaheshimu chombo cha kidemokrasia ambacho ni Bunge, alisisitiza Membe.
Alisema kamwe serikali ya Tanzania haiwezi kupinga maamuzi yaliyofanywa na chombo cha kidemokrasia kama Bunge na kwamba kufanya hivyo ni kuleta chokochoko ndani ya visiwa hivyo.
Wapinzani wa Comoro wakiongozwa na Ali Houmadi Msaidie, wanapinga uamuzi huo wa Bunge wakisema kufanya hivyo ni sawa na mapinduzi ya Katiba na kwamba yatakayomwezesha Rais wa Visiwa hivyo Abdalah Mohamed Sambi kuendelea kuwa madarakani kwa miezi18 zaidi badala ya Mei mwaka huu.
Walisema alipotembelea visiwa vya Anjuan, Moheli na Grande miaka miwili iliyopita, Rais Kikwete alisema si vyema kubadili Katiba ili kumwezesha mtu kuendelea kuwa madarakani.
Wanapinga kauli ya Waziri Membe aliyoitoa juzi alipotembelea visiwa hivyo ya kuunga mkono uamuzi wa Bunge kupanga uchaguzi huo ufanyike Novemba mwakani kwamba inapingana na ile ya Rais Kikwete.
Alieleza kuwa wapinzani wa visiwa hivyo wamekuwa wakipita katika balozi mbalimbali hapa Tanzania kupinga uamuzi huo wa Bunge kusogeza uchaguzi huo hadi mwezi Novemba mwakani.
Rais Kikwete alisema Bunge la Comoro lisikilizwe na lipewe heshima yake na mimi nimesema hivyo hivyo, tunaunga mkono uchaguzi wa magavana wote na Rais ufanyike kama Bunge la Comoro lilivyoamua, alisema Membe.
Alisema wakati wa kikao hicho cha Bunge lenye wabunge 83, wabunge 21 wa upinzani walitoka nje wakipinga wazo hilo, lakini wengine 63 waliobaki walipiga kura ya kuunga mkono wazo hilo.
Alisema viongozi hao wa upinzani walikwenda hadi kamisheni ya AU kulalamikia uamuzi huo wa Bunge lao na viongozi wa kamisheni hiyo walimpigia simu (Membe) kumwomba ushauri wa serikali ya Tanzania kuhusu mgogoro huo.
Alisema kabla ya kutoa ushauri alikwenda Comoro kuangalia hali halisi na alifanya hivyo baada ya kuagizwa na Rais Kikwete.
Alisema alipokuwa Comoro aliuliza iwapo wapinzani hao wamepinga uamuzi wa Bunge katika mahakama ya Katiba lakini aliambiwa kuwa hawakuwahi kufanya hivyo.
Nilikwenda Comoro nikaonana na Rais wao na baada ya hapo nikatoa tamko kwa vyombo vya habari kuwa msimamo wa Tanzania tunaheshimu maamuzi ya Bunge la Comoro kwamba uchaguzi ufanyike Novemba mwakani, alisema.
Alisema kwa hali tete ilivyo Comoro lazima serikali ya Tanzania iheshimu maamuzi yanayofanywa na Bunge na aliwataka wapinzani waheshimu maamuzi ya vyombo vya kidemokrasia kama Bunge.
Alisema kama wapinzani wanataka kufanya maamuzi yao wajitahidi wawe wengi ndani ya Bunge ili wafanikishe malengo yao badala ya kupinga wakiwa nje.
Comoro imepitia mapinduzi 21 hadi sasa na kwa kweli Tanzania imechagia sana kuleta amani ya Comoro hivyo lazima tuheshimu mamlaka zilizopo ili kuepuka choko choko, alisema.
CHANZO: NIPASHE