Mbunge wa Jimbo la Hai, Saashisha Mafuwe, ameionya Serikali kuwa idadi kubwa ya vijana wanaohitimu vyuo vikuu kila mwaka inaweza kugeuka kuwa ‘bomu la kijamii’ ikiwa hakutakuwa na mpango madhubuti wa kuwaingiza kwenye sekta za uzalishaji.
Akichangia Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu (2026/27–2050/51), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/27, Mafuwe amebainisha kuwa takwimu za sasa zinaonesha vijana wengi zaidi wanatarajiwa kuhitimu lakini mpango wa kuwapokea mtaani bado haujajitosheleza.
Mafuwe ameshauri kuwa sekta ya kilimo ndiyo yenye uwezo wa haraka wa kutoa ajira kwa vijana hao, mradi tu ionekane kama fursa ya kibiashara na si adhabu. Ameitaka Serikali kutumia mifano ya vijana waliofanikiwa kuwahamasisha wasomi hao kurejea shambani kwa kutumia teknolojia na sayansi.