Na Anna Mrosso
21st May 2011
Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema
Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema, amewaweka wafiwa katika kambi ya pamoja hadi mtafaruku wa kutozika watu waliokufa katika mapambano na polisi.
Lema alisema jana kuwa yeye kwa kushirikiana na viongozi wa Chadema wilaya ya Tarime wamechukua uamuzi huo kwasababu baadhi ya viongozi wa serikali wamekuwa wakiwafuata wafiwa hao na kuwashawishi kwa fedha ili wakubali kuzika ndugu zao.
Alisema baadhi ya wafiwa walimweleza kuwa viongozi wa serikali wamekuwa wakiwaeleza kuwa endapo watakubali kuzika watawasaidia kugharamia mazishi ikiwa ni pamoja na usafiri na chakula,pamoja na hayo waliahidiwa kupewa kiasi cha zaidi ya Sh. milioni tatu kama pole kwa kila familia iliyofiwa.
Waziri huyo alisema baada ya kupata taarifa hizo, aliwakataza wafiwa kupokea fedha wala kukubali serikali kugharamia mazishi kwa kile alichosema kuwa wakifanya hivyo vitendo holela vya mauaji kwa watu wanaoishi jirani na mgodi wa dhahabu wa North Mara(Nyamongo) vitakuwa kawaida.
Katika hatua nyingine, Lema alisema kuwa Jeshi la Polisi nchini linatakiwa kuwa makini la sivyo wataendelea kutumiwa vibaya na serikali hali itakayofanya Jeshi hilo kudharaulika kwa jamii japo wao wanapokea maelekezo kutoka kwa viongozi wa serikali.
Alisema kufuatia mauaji yanayotokea mara kwa mara katika mgodi huo si kwamba wawekezaji wanafurahia bali wao pia wanasikitika kwavile wanaona ni vigumu sana kukaa katika eneo ambalo jamii inayowazunguka hawawakubali.
Vitendo vinavyofanywa na Jeshi la Polisi vinaweza kuhatarisha hata wawekezaji kukimbia,serikali inatakiwa kuwa makini na hilo,alisema Lema. Naye Mbunge wa Viti Maalumu wa Chadema, Ester Matiko alitaka serikali ikae chini itafakari ni kwanini mauaji ya mara kwa mara yanatokea katika maeneo yaliyo na wawekezaji.
Matiko alisema mauaji hayo hutokea kwa sababu jamii inayoishi jirani na wawekezaji wanakuwa na hali ngumu ya kimaisha ambpo serikali haijafikiria ifanye nini ili jamii inayoishi katika maeneo kama hayo zijione nazo ni sehemu ya malighafi zinazozalishwa katika eneo husika.
CHANZO: NIPASHE