Makapuku Forum

<br /> Ethiopia Airlines ndiyo ya kwanza Afrika kununua ndege aina ya Airbus A350 XWB<br /><br />Ethiopia imekuwa taifa la kwanza barani Afrika kununua ndege ya kisasa aina ya Airbus A350 XWB.Ndege hiyo, Airbus A350, ndiyo ya hivi karibuni kuzinduliwa na kampuni ya ndege ya Airbus ya Ufaransa.<br /><br />Ndege hiyo, iliyo na uwezo wa kubeba zaidi ya abiria 300, ilitua katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta jijini Nairobi Kenya Jumatano jioni ikitokea mjini Addis Ababa, Ethiopia.<br /> <br />"Ndege hii ya kisasa itasaidia katika utoaji wa huduma zetu, kuimarisha mtandao wetu wa usafiri, na kupunguza kwa kiasi kikubwa viwango vya hewa chafu inayotolewa wakati wa usafiri wa ndege,” Mkurugenzi mkuu wa shirika la Ethiopian Airlines Tewolde GebreMariam amesema.<br /><br />Ndege hiyo ni ya kwanza kuwasilishwa kwa kampuni hiyo, huku nyingine 13 ilizoagiza kutoka kwa kampuni ya Airbus zikisubiriwa hivi karibuni.<br /><br />Safari ya kwanza ya ndege hiyo ilifanyika tarehe 2 Julai iliposafiri kutoka Ufaransa hadi mjini Lagos, Nigeria.<br /> <br />Viwango vya juu vya teknolojia iliyotumika kuunda ndege hiyo, vinachangia katika kuinua utendakazi wake, kupunguza matumizi ya mafuta pamoja na kupunguza kwa kiasi kikubwa utoaji wa hewa chafu.<br /><br />Kampuni ya Ethiopian Airlines inaorodheshwa ya kwanza barani Afrika kwa faida na pia idadi ya maeneo inayosafirisha abiria.<br /> <br /><br />Mwaka wa 2012, shirika hilo pia lilikuwa la pili duniani na la kwanza barani afrika kununua ndege aina ya Boeing 787 Dreamliner, ya kampuni ya Boeing, yenye afisi zake kuu Chicago, Marekani.<br /> <br />Kampuni ya Airbus na Boeing zinaongoza duniani katika utengenezaji wa ndege za kisasa, japo Airbus ina umaarufu mkubwa na imeipiku Boeing kwa faida na uuzaji wa idadi kubwa ya ndege.
Chanzo: BBC
 
Baraza la mitihani Tanzania NECTA limetangaza matokeo ya kidato cha Sita mwaka huu wa 2016 na wanaume wameongoza kwa wingi katika kumi bora, katibu mtendaji wa NECTA bado anaendelea kuongea mnaweza ona matokeo kwa website yao na ya TAMISEMI,<br /><br />Ufaulu umeshuka kwa asilimia 0.93 ikilinganishwa na mwaka 2015 ambapo ufaulu ulikuwa 98.87.<br /><br /><b>Shule 10 zilizofanya vizuri: </b><br />1.Kisimiri,<br />2.Feza Boys,<br />3.Alliance Girls,<br />4. Feza Girls,<br />5. Marian Boys,<br />6.Tabora Boys,<br />7.Kibaha,<br />8.Mzumbe<br />9.Ilboru,<br />10. Tandahimba<br /><br /> <br /><br />KWA MATOKEO: <b>BOFYA HAPA
 
SEHEMU YA KWANZA
RIWAYA:ANTI EZEKIEL
MTUNZI: George Iron Mosenya


SEHEMU YA KWANZA


Marashi yaliyopuliziwa na mtu ambaye nilikuwa sijauona uso wake wala kujua yu umbali kiasi gani kutoka katika kiti nilichokuwa nimekaa kwa ajili ya kunyolewa nywele zangu yalinivutia kiuhakika, nikaamua kumshirikisha yule kinyozi aliyekuwa ametingwa katika kuninyoa nywele zangu katika mtindo niliokuwa nimeuchagua.
“Kausha….” Alinambia na sikuelewa ni kitu gani anamaanisha.
Nikahisi hakuwa akizungumza na mimi. Marashi yale yakaendelea kutawala na sasa yalisadikika kuwa karibu kabisa na pua zangu. Hapo nikajikuta nanyanyua kichwa changu, kwa lengo la kutazama ufundi ambao kinyozi aliufanya katika kichwa changu. Badala ya kutazama kichwa changu nikajikuta natazamana na tabasamu murua la kike.
Kichwa chake cha mviringo kilikuwa kimefunikwa na koti lisilokuwa maalumu kwa ajili ya kupambana na baridi bali mojawapo ya kivazi kinachoenda na wakati.
Nilipoendelea kubung’aa mara yule mmiliki wa sura ile ambaye nilikuwa natazamana naye katika kioo alinikonyeza. Hapo nikakumbwa na aibu na kisha nikajifanya kutazama pembeni.
“Ana aibu mwenyewe looh!!” ilimtoka sauti fulani yenye mchanganyiko wa besi na nyororo. Nikalazimisha tabasamu lakini sikukitazama kioo. Hakujishughulisha na mimi tena badala yake aliendelea kuzungumza na mmiliki wa ile saluni ambaye pia alikuwa kinyozi mkuu na wakati huo alikuwa katika kuzishughulikia nywele zangu. Baada ya hapo akatoweka huku nyuma akiacha harufu kali ya marashi isiyokera pua za mnusaji.
“Bwege katoka kwa wanaume” yule kinyozi akasema ili nisikie, “Nd’o wasichana wa siku hizi hao…” niliunga mkono hoja pasipo kutilia maanani.
“Wasichana!!! Bora angekuwa msichana basi….yaani mi ananikera sana ujue. Kidume kizima kabisa.” Akatokwa na kauli iliyorindima

katika mawimbi ya hasira na kupokelewa na ngoma ya
sikio langu katika hali ya mshangao na sintofahamu.
Nikaamua kuuliza. “Mwanaume? Mwanaume kivipi sasa ama umbo lake.” Niliuliza na bado sikutilia maanani mazungumzo yale kama yangeweza kunifikisha popote. Niliamini ni mazungumzo tu ya hapo saluni na yanaishia hapo hapo.
“Shoga huyu!!! Halafu yupo wazi hata aibu haoni, kuna washkaji wangu washalala naye, mimi siwezi hata kwa bunduki yaani.” Aliongea kwa kunong’ona. Nikamsikia vyema. Sasa niliishughulisha akili yangu kuelewa kile alichokuwa ananieleza. Kumbe yule dada aliyenikonyeza na kunisifia kuwa nimependeza si dada ni mwanaume anayeupenda udada? Niliduwaa hakika. Na hapo nikamuuliza maswali mengi sana yule kinyozi, naye akafurahia kuyajibu.
Haikuwa mara yangu ya kwanza kusikia kuhusu jina hilo la ‘shoga’ la!! Lakini huyu macho yake ni kama yalitangaza kitu fulani cha ziada, alikuwa kama shoga anayejilazimisha japo yule kinyozi alidai kuwa yeye mwenyewe anajitangaza waziwazi kuwa ni shoga. Macho yake ni kama yalikuwa yamebeba siri nzito sana!! Ni siri gani hiyo? Huyu hakuwa shoga wa kawaida kama kweli ni shoga!! Nilijionya.
Umewahi kumwona hata siku moja akiwa na mwanaume? Nilimtupia swali kinyozi.
“Dah mi huwa sitaki hata kumwona lakini washkaji zangu kibao wanamjua huyu”
Katika mahojiano hakuna jambo baya kama kutumia ushahidi wa wenzako katika kuliamini jambo, ndo kitu alichojaribu kutumia yule kinyozi jambo ambalo si sahihi hata kidogo!!
“Kwa hiyo wewe hujawahi kumwona, vipi sasa akisema kuwa yeye sio shoga utasema nini!! Au akuulize kwamba umthibitishie kuwa usemayo ni kweli.?”
Nilipozidi kuuliza maswali mengi na kuonekana namtetea yule shoga, kinyozi akarusha kijembe. “Vipi kaka na wewe unataka kukamatilia?” sikumjibu badala yake tukajikuta tunacheka, na hapo alikuwa anamalizia kunifuta kichwa baada ya kuninyoa.
“Vipi na ndevu niondoe..” aliniuliza nikakataa. Akaendelea kunifuta hadi alipojiridhisha
Nikafanya malipo na kisha nikajiondokea huku nikijilazimisha yale mawazo kuhusu yule kijana anayeupenda usichana yanitoke. Nilipofika nyumbani sikuwa na mawazo hayo tena na sikutaka hata kumfikiria maana kwa kashfa alizotoa yule kinyozi basi zilitosha kumaanisha kuwa kijana yule alikuwa mdhambi tena asiyestahili hata kupewa salamu. Inakuwaje mwanaume anajigeuza kuwa mwanamke??
Lakini hafananii hata kidogo na mashoga ninaowajua mimi. Ana nini huyu kwani??
Nililala nikiwa na swali hilo kichwani!!! Asubuhi hapakuwa na lile swali tena na jibu lake pia halikufanania kuwepo. Siku ikaanza nikiwa nimeyasahau ya jana.


SAFARI YA KUKUTANA ANA KWA ANA NA MUHUSIKA.

UCHAGUZI mdogo wa serikali za mitaa kata ya Makangarawe wilayani Temeke uliambatana na mechi ya kukata na shoka katika mchezo wa soka. Timu mbili pinzani zilikuwa zinaumana na mshindi angejiondokea na kitita cha shilingi laki tano. Mchezo ule ulivuta mashabiki wengi sana kutokana na upinzani wa wazi wazi baina ya timu hizo.
Nikiwa mmoja katika ya wapenzi wa mpira wa miguu niliungana na mashabiki wengine uwanjani.
Hali ya usalama ilikuwa nzuri kuanzia kipindi cha kwanza hadi ilipokuja kuchafuka kipindi cha pili majira ya saa kumi na mbili ambapo mwamuzi wa mchezo huo alipokataa goli la waziwazi. Walianza wachezaji kumzonga mwamuzi mara mashabiki nao wakaingilia kati, hapo ikazuka vita kubwa ya mashabiki wa kila upande. Kikosi cha kutuliza ghasia hakikuwa mbalki, mabomu yalipopigwa ndipo kikazuka kizaazaa cha aina yake, kila mmoja akikimbia kuelekea upande wake.
Kipigo kilitolewa haswaa na ungekuwa mwenye mikosi kama ungejikuta katika mikono ile ya maaskari. Nilichanja mbuga huku machozi yakinitoka kwa wingi baada ya kuuvuta ule moshi wa bomu. Niliruka matuta hapa na pale.
“Kakaaa…” nilisikia sauti ya kike ikiita, sauti iliyotia simanzi, sijui ilikuwaje lakini licha ya hatari ile ya kuishia kulala rumande na kipigo kupokea niligeuka kutazama kulikoni. Macho yangu yakakutana na macho yaliyonitia mashaka siku moja nikiwa mahali fulani ambapo sikupakumbuka, nilitaka kuendelea kukimbia lakini nafsi ikasita.
Nikiwa bado sijapata maamuzi mara kijana mmoja aliyekuwa katika harakati za kukimbia alipita kwa kasi na kumkanyaga mtu yule, akatokwa na kilio cha maumivu. Nikataka kuzuia huruma yangu, lakini nikakumbuka kuwa nimeajiriwa katika kampuni ya kutetea haki za wanadamu na mimi mwenyewe ni mwandishi, mara kwa mara naandika makala zinazosisitiza usawa na pia utu. Kwa maana hiyo kama ningekimbia basi ninachokiandika mara kwa mara kisingekuwa na maana.
Nisingekuwa na utu. Haraka nikakimbia mahali alipokuwa, nikamnyanyua, hakuwa mzito sana nikagundua naweza kumuhimili. Nikambeba begani! Nikajikokota hadi aliponielekeza kuwa nyumbani kwake ni jirani tu….nikafuata uelekeo aliokuwa amenielekeza. Tukaufikia mlango, nikamshusha. Akajikongoja na kuufungua mlango baada ya kujipekua na kutoka na ufunguo.
Niliaga na kutaka kuondoka, akanisihi kuwa niingie ndani hadi vurugu zipungue
Naam alikuwa amewaza jambo la maana sana, nikakubaliana naye. Nikaingia ndani. Nilipoingia ndani nikakuta picha yake, nikatazamana na ile picha nikakumbuka sasa wapi tulionana. Ni huyu kijana tulionana saluni, nikaambiwa kuwa ni shoga!! Damu ikachemka nilipofikiria kuwa nipo katika chumba cha shoga. Nilifananisha sebule ile na sebule yangu, hakika alikuwa ameniacha kwa kila kitu. Hali hii ya kuniacha kwa kila kitu ikanivuta kuendelea kukaa pale.
“Unaitwa nani kakangu.” Aliniongelesha kwa sauti ilele ya mchanganyiko.
“Sam!!” nilimjibu kwa kifupi.
“Mimi naitwa Ezekiel…asante sana kwa kuniokoa, sijui kama ningelala nyumbani kwangu leo.” Alinijibu huku akiachia tabasamu. Sikusema neno nami nikatabasamu huku nikikwepa kumtazama machoni.
“Nyumbani kwako pazuri sana!!” nilimsifia.
“Ah kawaida tu, lakini asante si unajua tena mwanamk…..si unajua tena kujipenda jambo la muhimu.” Akajibu kwa kigugumizi.
“Unaishi peke yako?” nilimuuliza pasipo na wasiwasi wowote kumtilia.
“Yah ni nyumbani kwangu naishi peke yangu……khaa! Nimejichubua jamani kucha zangu.” Alijibu kisha akalalamika akizitazama kucha zake zilizopakwa rangi. Tofauti na siku niliyomuona pale saluni, siku hii alikuwa amedhoofu sana. Alikuwa amekonda na uso wake ulikuwa umebonyea. Hali hii ilinishangaza, lakini nikalazimika kuuliza baada ya yeye kuanza kukohoa kwa fujo.
“Unaumwa…”
“Bora ningekuwa naumwa….mimi naumwa sana.” Alinijibu kwa uchungu. Sasa sauti yake haikuwa mchanganyiko sana, bali ilisikika kama ya kiume waziwazi. Sauti ilikuwa inakoroma. “ Nini tena maana siku ile tunaonana saluni haukuwa hivi, au kioo kilikuwa kinanidanganya.”
“Saluni? Saluni gani?” aliniuliza huku akistaajabu. Nikamkumbusha siku ile ambayo ilikuwa miezi miwili iliyopita. Hapo chozi likamtoka sikujua kama ni kwa furaha ama uchungu.
“Lazima nife lakini basi tu….basi tu nasema. Ipo siku yao na wenyewe” Alilalamika peke yake na sikujua kama alikuwa ananishirikisha ama la.
“Mbona unasema hivyo bro.” nilihoji. Akanyanyua kichwa akanitazama. Hakusema neno akakohoa tena kikohozi kikavu ambacho kwa kukisikia tu nilitambua kuwa kilikuwa kinamuumiza koo.
“Wewe ni nani?” aliniuliza…..kabla sijajibu akazungumza tena.
“Umesema unaitwa Sam lakini bado sijajua wewe ni nani hadi umeamua kurudi nyuma na kuniokota wakati wapo wanaharamu wengine wamejazana mitaani huko wakiunda mikakati ya kijajusi ilimradi tu kutia doa taifa letu. Kuna watu washasahau kauli mbiu ya upendo na amani. Wapo katika kuvuruga amani.” Alitamka haya huku akinikazia macho, bila shaka ni maneno ambayo yalikuwa yanamgusa sana.
Kauli yake ikanitetemesha kidogo, ni kama alikuwa ananikaripia. Sikushtuka sana nikaendelea kumtazama, kwani nilishazoea harakati hizi.
“Mimi ni Sam, mwanaharakati na pia ni mwajiriwa kwenye kampuni fulani hivi……” nilimjibu.
“Hivyo tu!” aliuliza na sikujua ana maana gani.
“Unamaanisha nini.”
“Ndo hivyo tu kuhusu wewe maana sura yako si ngeni sana kwakweli, licha ya kukuona siku ile saluni bado kuna mahali nadhani tumewahi kuonana ama nimekuona.”
“Labda gazetini, huwa naandika vihadithi hadithi.” Nilijibu bila kutarajia kuwa anaweza kuwa ananifahamu. Akasimama na kujipigia makofi, lakini kikohozi kikaondoka na cheko lake akakaza sura na kuugulia maumivu lakini bado aliweza kuzungumza.
“Nimesoma hadithi zako kadhaa, wewe si nd’o umeandika ile ya NISAMEHE KABURI…..na nyingine ile ya dada fulani hivi chuoni hana miguu wala mikono na anataka kuwa rubani….yaani napenda hadithi zako hasahasa za kipelelezi, hivi wewe ni mpelelezi eeh….” Alizungumza kwa sauti yake ya kubana pua, bila shaka alikuwa ameizoea.
Alionyesha kunifahamu vyema. Baada ya koo kukaa sawa aliendelea kuorodhesha makala na hadithi zako ambazo amewahi kuzisoma, na hatimaye tukaagana huku nikiwa sina shauku kubwa sana ya kuendelea kumsikilia Ezekiel, kwani hakuonyesha kama anajitambua vyema. Na mbaya zaidi niliamua kuondoka kwa kuhofia kujitekenezea skendo nikionekana natoka katika nyumba ya yule shoga. Mke wangu na wivu wake!!
Nilimjua mimi mwenyewe. Nikamuaga Ezekiel na kuondoka, huku nikijiapia kuwa hakuna ninalohitaji kujua zaidi kutoka kwa mwanaume aliyejigeuza mwanamke.

UTATA MKUU

Siku iliyofuata nilikuwa na safari ya kuelekea mkoani, hivyo asubuhi na mapema niliwahi kwenda Ubungo. Kiubaridi kilikuwa kinapuliza na nilikuwa nimejiegesha mahali nikipuliza hewani moshi wa sigara kupasha mwili wangu joto. Nilijitenga eneo la mbali kabisa na abiria wengine ili nisiweze kuwabughuzi.
Mawazo yangu yalikuwa yote juu ya safari yangu kuelekea Singida, niliwaza kuhusu watu wa Singida jinsi walivyo wakarimu na hapo nikajengea picha mara yangu ya mwisho mjini Singida. Nikiwa bado pale nilipojiegesha mara nilisikia naguswa begani.
Nilipogeuka nyuma nilikutana na maajabu.
Ana kwa ana na yule shoga!! Hakuwa anatabasamu ba alionekana kama anayefanya mambo kwa shinikizo. Alinikazia macho kama anayetaka nielewe kitu fulani, nilijitahidi kung’amua jambo nikasafiri na macho yake hadi katika mguu wake, akatabasamu na kisha kutoweka pale katika mguu wake wa kuume akaacha kifurushi kidogo tu cha nguo.
Nikataka kumfuata anapoelekea lakini akanionya kwa vitendo. Mwendo wake ulinishangaza sana, alitembea mithili ya ngongoti, alikuwa amenyooka na ni kama hakutaka kupinda, masikioni alikuwa ana vifaa vya kusikilizia, sijui alichokuwa anasikiliza lakini bila shaka walikuwepo watu ambao alikuwa anawasikiliza.
Ezekiel akatoweka na sikumuona tena. Nikarejea hadi pale nilipokuwa nimesimama mwanzo, nikaanza kukitafuta kile kifurushi alichokiacha pale lakini sikukiona, nilihaha sana na kujiuliza nini kimemsibu yule kijana. Na ni kitu gani alikuwa ameniachia katika fundo lile la nguo?? Lazima kilikuwa kitu cha msingi maana alionyesha kusihi sana.
Swali gumu jingine likawa, yule bwana amejuaje kama nitakuwa stendi asubuhi ile hadi aniletee ujumbe ule. Nikiwa bado katika mtihani mgumu, mara basi nililotakiwa kusafiri nalo likapiga honi kuashiria kuwa dakika yoyote ile linaondoka.
Ule utata ambao huwa naujenga kwa wahusika katika simulizi sasa ukajijenga katika nafsi yangu na sikujua nautatua vipi? Katiba basi tayari begi langu lilikuwa kule, sikukipata kifundo nilichoachiwa na mtu niliyeamini kuwa ni Anti Ezekiel.
Na ubaya mwingine sikujua hata kitu kilichokuwa kinamsibu Ezekiel. Nikayakumbuka maneno yake usiku uliopita “nitakufa …lakini….IPO SIKU YAO NA WENYEWE” Hakumalizia, na sikujua alitaka kusema nini. Kwanini afe na hao wenyewe ni kina nani??
 
SEHEMU YA PILI
SEHEMU YA PILI


Nikarejea hadi pale nilipokuwa nimesimama mwanzo, nikaanza kukitafuta kile kifurushi alichokiacha pale lakini sikukiona, nilihaha sana na kujiuliza nini kimemsibu yule kijana.
Na ni kitu gani alikuwa ameniachia katika fundo lile la nguo??
Lazima kilikuwa kitu cha msingi maana alionyesha kusihi sana.
Swali gumu jingine likawa, yule bwana amejuaje kama nitakuwa stendi asubuhi ile hadi aniletee ujumbe ule.
Nikiwa bado katika mtihani mgumu, mara basi nililotakiwa kusafiri nalo likapiga honi kuashiria kuwa dakika yoyote ile linaondoka.
Ule utata ambao huwa naujenga kwa wahusika katika simulizi sasa ukajijenga katika nafsi yangu na sikujua nautatua vipi?
Katiba basi tayari begi langu lilikuwa kule, sikukipata kifundo nilichoachiwa na mtu niliyeamini kuwa ni Anti Ezekiel.
Na ubaya mwingine sikujua hata kitu kilichokuwa kinamsibu Ezekiel.
Nikayakumbuka maneno yake usiku uliopita “nitakufa …lakini….IPO SIKU YAO NA WENYEWE”
Hakumalizia, na sikujua alitaka kusema nini.
Kwanini afe na hao wenyewe ni kina nani??
Nafsi yangu haikubariki wazo lolote kati ya hayo matatu yaliyokuwa yakinihangaisha kwa wakati ule. Ni kama nilikuwa mbumbumbu wa sekunde kadhaa.
Ufahamu ulinirejea baada ya kumuona mtoto mdogo akiwa na mfanowe kile kifundo mikononi mwake akirandaranda maeneo ya pale stendi, nilimwendea mbio mara akageuka na aliponiona akaanza kutimua mbio, sijui ni kipi alikiona kwangu hadi akaanza kutimua mbio kiasi kile, nilitamani sana atambue kuwa sikuwa na ubaya wowote bali nilihitaji kile kifundo, lakini angeanza vipi kunielewa iwapo watoto wadogo wasiokuwa na makazi maalumu maisha yao ni kama kivuli tu hawaishi kukimbia siku zote, na ningejuaje huenda alinifananisha na mgambo wa jiji ambaye husafisha mazingira hadi watoto wasiokuwa na makazi.
Niliendelea kutimua mbio hadi akafikia lile geti la kutokea nje ambalo magari huytumikia kupita pale, kwa sababu yeye alikuwa mbele alifanikiwa kupenya lakini mimi nikiwa mtu mzima nilizuiliwa, hakuna mtu aliyeruhusiwa kupita pale pasipo na sababu za msingi, nilijitahidi kumweleza yule bwana kuwa nina haja sana na mtoto yule lakini hakuonekana kukaribia kunielewa, akaniomba nimpe tiketi yangu ambayo itaonyesha kuwa nilikuwa ni abiria kweli lakini hata ile tiketi sikuwa nayo kwani niliiacha katika begi langu lililokuwa ndani ya gari.
Kitendo cha kurejea ndani ya basi kufuata tiketi kingekuwa cha kizembe tena kisichostahimilika na kile kifundo nisichokijua kingepotea hivihivi mbele ya macho yangu na kila kukicha ningeendelea kuteseka pasi na kujua ni ujumbe gani ulikuwa katika kifundo.
“Naomba nipite yule mtoto ameniibia!!!!” nilidanganya ili yule jamaa aweze kunielewa lakini aliendelea kuweka ngumu. Hasira zikanipanda na kuamua kufanya maamuzi, nikamsukuma kando kwa nguvu, akajikwaa na kupiga mweleka huko. Hapo sasa nikapenya kwa kasi, nyuma nikasikia filimbi ikipigwa, sikujali nilichohitaji ni kile kifundo, kwani kwa kukipata kile basi ningeweza kuituliza nafsi yangu.
Niliangaza huku na kule pasi na mafanikio ya kumwona yule mtoto, nilijaribu kuwaulizia watu juu ya mtoto yule lakini hakuna aliyejishughulisha nami, nd’o kwanza kulikuwa kunakucha na kila mtu alikuwa akijipanga kuikabili siku ile.
Sikukata tamaa, niliendelea kuangaza huku na kule, nilijitahidi sana kukumbuka kuwa mtoto yule hakuwa na nywele kichwani na alikuwa na kaptula iliyopasuka pajani, sikuwa nikiijua sura yake.
Nikajificha mahali na kuendelea kufuatilia nyendop za watu mbalimbali, baada ya dakika zipatazo kumi nikafanikiwa kumuona mtoto yule, mkononi hakuwa na kile kifundo lakini alikuwa ni yeye.
Nikamnyemelea na kufanikiwa kumkamata, nilimuuliza maswali kadhaa, akakiri kukiokota kifundo kile na alikitupa mahali, niliongozana naye hadi mahali alipodhani amekitupa.
Tukafanikiwa kukipata, nikampataia pesa ambayo angeweza kunywa chai na kula chakula cha mchana siku hiyo, nikakishindilia mfukoni, na hapo nikachukua pikipiki na hima nikamuamuru dereva alifukuzie gari ambalo lilikuwa na begi langu na tayari lilitoka stendi.
Wakati tunakubaliana bei na dereva mara niliguswa bega, ni kama alivyonigusa Ezekiel. Nikageuka upesi nikidhani ni Ezekiel tena, lakini sasa sikukutana na sura ya mtu bali ngumi kali katika shavu langu.
“We mpumbavu umejifanya mjuaji kunikimbia sivyo.” Alikoroma kipande cha mtu ambaye nilimsukuma kule getini ili niweze kukimbilia kile kifundo alichokuwanacho yule mtoto.
Wakati nataka kujitetea nikamuona yule jamaa akijiandaa kunirushia ngumi nyingine, nikajihami na kuruka kando.
Mwendesha pikipiki akaona isiwe tabu, akawasha pikipiki yake na kutoweka mbali.
Akaniachia kizaazaa kinikumbe peke yangu.
Amakweli mchuma janga hula na wa kwao!!
Kipande cha mtu kikiwa na hasira, kikanikaba mkono wangu kwa uimara wa hali ya juu. Akaanza kunivuta kuelekea anapotaka yeye.
Nikatambua kuwa nikifanya uzembe tu hata lile begi katika gari litapotea, huyu kipande cha mtu lazima angenifikisha katika chombo cha dola na hapo ndipo mlolongo ungeanza, mbaya zaidi hata kitambulisho changu cha kazi sikuwa nacho tena. Vyote vilikuwa katika begi langu.
Akili yangu ikanituma kufanya tukio la mwisho ambalo litaniweka huru, yule kipande akiwa ameridhika jinsi alivyonikwida nami nilijilainisha na kisha ghafla nikamfyatua mtama, mguu wake wa kushoto ukakutana na ule wa kuume, akaniachia kisha akayumba na kuanguka chini tena.
Nikatimua na kufanikiwa kuvuka upande wa pili wa barabara, nikakuta pikipiki nyingine, nikakwea na kutoa maelekezo kama yale niliyotoa awali kwa yule aliyenikimbia baada ya kupata msala.
Tukatoweka!!
Baada ya dakika thelathini nilikuwa nahema juu juu nikiwa ndani ya basi siti ileile, yaliyotokea yote yalikuwa kama ndoto.
Sikuamini kama nimefanikisha mambo yote kwa wakati na sasa nilikuwa katika safari yangu kana kwamba hakuna kilichotokea.
Bahati nzuri nilikuwa siti ya dirishani hivyo upepo ulipunga vyema na kunirejeshea amani pamoja na usawa katika akili yangu ambayo kidogo ilikuwa imeanza kuvurugika.
Hapo sasa nilijipekua mahali ambapo nilihifadhi kile kifundo, nilipanga nikifungue mwisho wa safari lakini kihoro kikanisukuma kukifungua kabla hata safari ya kuikaribia
Morogoro haijakaribia.
Nilifungua kwa makini na tahadhari ya hali ya juu huku nikijitahidi nisiiingie katika taharuki kwa kitu ambacho nilikuwa sijakiona bado.
Kifundo kikawa wazi hatimaye na ndanmi yake kulikuwa na funguo moja ambayo ilikuwa na kutu sana. Haikuonekana kama ilifungua mahali fulani katika siku za karibuni na wala haikuonyesha kama hata siku za usoni itakuwa na manufaa kwa kufungua mahali. Ama la hapo pa kufunguliwa na penyewe pana kutu na pamechakaa kwa kiasi kikubwa.
Funguo ya nini hii? Nilijiuliza huku nikifadhaika na kujiona kuwa nilihangaika na kukaribia kuiokosa safari yangu kwa sababu ya kitu kisichokuwa na mantiki.
Nikakifunga kile kifundo na kisha nikakiweka katika mfuko wa suruali yangu!!
Na hapo nikamkumbuka Ezekiel, hali niliyomshuhudia akiwa nayo maeneo ya Ubungo na hali niliyomshuhudia usiku mmoja kabla baada ya vurugu kumkumba nami nikamwokoa.
Alikuwa katika muonekano wa tofauti sana hasahasa asubuhi hiyo, alikuwa muoga na alitembea kikakamavu na ni kama alikuwa akiongozwa na watu!! Kisha akatoweka.
Akatoweka na asionekane tena!! Ufunguo ule mmoja ni wa nini? Na kwanini alinipa mimi?
Maswali haya yalinisumbua sana.
Simu yangu iliita na mlio wake ukayakatisha mawazo yangu yasiyokuwa na dalili ya kufika kikomo.
Ni namba kutoka ofisini kwetu, nikaipokea na kupewa taarifa kuwa semina iliyotakiwa kufanyika mjini Singida imesogezwa mbele kwa siku mbili kutokana na sababu ambazo nitaelezwa baada ya kufika Singida. Aliyenipigia simu akanieleza kuwa nitapewa posho ya kutosha kuniweka mjini pale hadi siku ya semina.
Simu hii ikanipa mwongozo mwingine, kama Singida hakuna semina kwa siku hiyo basi ningeweza kurejea jijini Dar na kama kuna lolote kuhusiana na Ezekiel na ule ufunguo basi nitaling’amua.
Katika maisha yangu hakuna kitu nilikuwa sipendi kama kubaki na majibu nusunusu!!!
Nilishuka Chalinze na kuchukua usafiri wa kurejea jijini Dar. Bahati nzuri nikapata basi linaloenda Kariakoo moja kwa moja.
Nikakwea, na baadaye tulikuwa tunapita Ubungo, nikatabasamu na kukumbuka balaa nililozusha asubuhi ile.


****


Niliujua ukorofi wa mama Eva ambaye ni mke wangu japo si wa ndoa. Hivyo nilimjulisha kuwa narejea jijini Dar baada ya dharula hiyo.
Nilifika nyumbani na kulitua begi langu kisha nikiwa na ule ufunguo uliochakaa nilienda nyumbani kwa Ezekiel ili kama kuna lolote niweze kutambua na nijue maana ya ufunguo ule uliochakaa tena wenye kutu. Nilishukuru kuwa muda ule nafika nyumbani mama Eva alikuwa ametoka kwenda sokoni maana sikuliona kapu ambalo huwa anabebea mazagazaga mbalimbali.
Upesi nikatoweka, safari hii sikumpa taarifa kuwa nimefika na kuondoka kwani nilitarajia kurejea upesi.
Katika safari yangu kwa Ezekiel nilitarajia kukuta lolote lile ambalo lingeweza kunipa mwanga iwapo kuna tukio limemsibu Ezekiel, lakini hapakuwa na lolote la kushangaza kila mmoja alikuwa katika harakati zake.
Chumba cha Ezekiel kilikuwa kimefungwa, nilijaribu kugonga hodi japo kwa ushahidi tu lakini hapakuwa na majibu.
Ili kuingia ndani ya nyumba ile nilihitaji kuwa na funguo!!
Kutaja neno ufunguo nikakumbuka kitu!
Ni hapo nikaukumbuka ule ufunguo wenye kutu. Nikajipekua na kuibuka na kile kifundo nikakifungua upesi na kuibuka na funguo wenye kutu. Japo sikuwa naamini sana kama yaweza kuwa kweli nililazimika kujiaminisha. Nikatazama kushoto na kulia hakuna hata mtu mmoja aliyejishughulisha na mimi, nikajikoholesha kama yupo ambaye atasema nami bado hakujitokeza mtu yeyote.
Naam!! Ufunguo ukakifungua kitasa, nikaingia ndani.
Sasa mbona una kutu huu funguo?? Nilijiuliza huku roho ya kipekuzi ikiniandama, na ni hii roho ilinituma mara kwa mara kufanya upekuzi mara kwa mara. Hata katika ofisi niliyoajiriwa walinitambua kwa tabia hii isiyokera bali kuwashangaza.
Mara nikakizoea kile chumba, nikaangaza huku na kule sikuona mabadiliko yoyote yale, nikajiuliza kama niliota kuonana na Ezekiel ama tulionana kweli.
Kama hatukuonana ule funguo ningeutoa wapi? Macho yangu yakavutika na karatasi iliyokuwa mezani, ilikuwa imeandikwa kwa wino mweusi mwandiko wa kuyumbayumba, bila shaka mwandishi aliandika huku akiwa na haraka sana.
“CHUMBANI USIACHE…PEKUA HATARI OKOA” maandishi yalisomeka vile, mapigo yangu ya moyo yakaenda mbiombio, nikaukumbuka mdomo wa Ezekiel kule Ubungo ulikuwa unachezacheza ukisema maneno haya kwa kurudia na sikuweza kutambua lolote lile.
Roho ya kidadisi ikazidi kunitawala, nikajiingiza kwa tahadhari kubwa katika chumba cha Ezekiel. Nilipoufikia mlango na wenyewe ulikuwa na tatizo lilelile, haukufunguka hadi ule ufunguo wenye kutu ulipoutekenya!
“Vitasa vinafanana ama…..” nilijiuliza huku nikiufungua vyema mlango.
Chumba kilikuwa kikubwa lakini hakikusheheni vitu vingi sana, kabati la nguo na meza ya kujirembea ya wanawake.
Meza ile ya kisasa ilikuwa na mtoto wa meza, na juu ulikuwa na vipodozi tele, haraka nikauendea mtoto wa meza, nikauvuta na hapo nikakutana na makaratasi mengi yakiwa yameandikwa mambo ambayo sikuyaelewa, nikayatwaa yote na kuyajaza katika mfuko mmoja mweusi, nikapapasa huku na kule sikukutana na kitu kingine ambacho niliona kina maana kwangu.
Katika hayo makaratasi kuna yaliyokuwa yameandikwa na mengine hayakuandikwa chochote.
Nikabeba, wakati nataka kutoka nje nikakumbuka karatasi ile ilinisihi kupekua zaidi tena ilisema nisiache.
Nikaishughulisha akili yangu, nikapekua zaidi na zaidi, mwisho kabisa nikatoa mashuka kitandani.
Hapa ndipo nilipokutana na jambo la kushangaza na kushtua kuliko yote ambayo hadi kipindi hicho cha utu uzima wangu macho yangu yaliwahi kushuhudia.
Sura haikuwa ngeni na ilifanana kabisa na ile niliyoonana nayo asubuhi ya siku hiyohiyo maeneo ya Ubungo!!
Sura ya Ezekiel!!
Alikuwa ametulia tuli kitandani, bora angekuwa anasema neno lolote ama anatabasamu.
Haukuhitaji utaalamu wa kidaktari kutambua kuwa mwanadamu yule alikwishapoteza uhai siku nyingi sana, na alikuwa ameanza kuharibika. Ezekiel hakuwa mweupe tena, ngozi yake ilikuwa nyeusi, alikuwa uchi mnyama.
Kifurushi cha makaratasi kikanitoka mkononi, lakini nilikumbuka kuuzuia mkojo uliotaka kunitoka. Miguu ilikuwa inatetemeka na jasho jembamba lilinitoka.
Ezekiel aliyenipa funguo, Ezekiel sasa ameozea kitandani!!!
Tofauti ya masaa matatu tu!!
Hapana!!
Nikaanza kurudi kinyumenyume na hapo nikajikwaa kwenye kile kifurushi na nikakumbuka kukiokota, ujasiri ukakaa kando, nikashindwa hata kumfunika Ezekiel pale kitandani.
Mara mlango wa Ezekiel ukagongwa!!!
Sikujibu chochote kile!! Mara sauti ya kike ikaita jina lake.
Hofu ikazidi kutanda, yule ni nani anayemtafuta Ezekiel, na je anamtafuta Ezekiel aliye hai ama huyu anayeozea kitandani!!
Maswali yakawa lukuki huku nikiwa sina majibu, na sauti kutoka nje ikazidi kuita.
 
SEHEMU YA TATU
SEHEMU YA TATU

Upesi nikatoka kule chumbani na kujichanganya sebuleni nikiwa na kifuko changu mkononi nikijiandaa kukabiliana na huyo ambaye alikuwa anabisha hodi.
Mapigo ya moyo yalikuwa juu sana na sikuweza kujizuia kuitangaza hofu yangu waziwazi.
Nilipofika sebuleni na Yule mgongaji alikuwa anaingia.
Haikuwa mara ya kwanza kuonana na yule mwaamke, lakini haikumaanisha kuwa nilikuwa naye karibu sana. Mara kwa mara tulikutana asubuhi katika kituo cha mabasi kila mmoja akienda anapojua mwenyewe.
“Mambo….mambo kaka” alinisalimia huku akionekana kuusoma uso wangu katika namna ya wasiwasi.
Labda alidhani najihusisha kimapenzi na yule mwanaume anayesadikika kuwa ni shoga.
Yule dada lazima alihisia kuwa nina uhusiano na Anti Ezekiel. Nilijilazimisha kutabasamu ili kumwopndoa wasuiwasi na hapo akanishambulia kwa swali moja zito ambalo sikujiandaa kulijibu. Wakati nadhani ataniuliza Ezekiel kama yupo ama la, aliniuliza kama Ezekiel bado amelala.
Hapo nikajaribu kuzungumza lakini nikashindwa kusema neno lolote. Ina maana Ezekiel alikuwa amelala na kuna baadhi ya watu walikuwa wanafahamu ama. Sasa akama alikuwa amelala na yule aliyenipa funguo kule Ubungo ni nani?
“Aaah…hayupo Ezekiel hayupo…kwani nani alikwambia alikuwa amelala.”
Nilimweleza bila kujipanga. Na hapo nikausoma wasiwasi wake moja kwa moja usoni.
“Acha utani basi kaka….” Alilaumu huku akionyesha fadhaa waziwazi.
“Hayupo dadangu…” nilisisitiza.
Yule dada akaamini kuwa nilijaribu kufanya naye utani wakati hakuwa na utani hata kidogo, na hapo nikatambua kuwa alikuwa na ufahamu mkubwa na uzoefupia katika nyumba ile. Akanipita na kuelekea chumbani kwa Ezekiel huku akiita jina la Ezekiel kwa mikogo.
Akili ikaniambia kuwa kama ni mtego tayari ulikuwa umefyatuka na ni lazima ningejikuta nimenasika.
Upesi nikapepea na mfuko wangu mfukoni.
Nilipotoka nje nikaamua kutimua mbio kabisa, nikiwa na kile kifurushi kuelekea nyumbani, nilijikwaa mara kwa mara lakini sikusimama baada ya dakika tano tayari nilikuwa katika mlango, na nilitanabai kuwa mke wangu naye alikuwa amefika muda si mrefu kutokea sokoni.
“Na wewe…nini kimekusibu.” Aliniuliza huku akinishangaa, alikuwa ameshika kiuno.
Macho yake aliyakazia miguuni mwangu na nilipojitazama nikagundua kuwa sikuwa na viatu mguuni bali nilikuwa nimevaa soksi pekee.
“Viatu vipo wapi?” alinitupia swali jingine. Bado sikuweza kujibu na niklibaki kubung’aa kama zezeta tu. Mama Eva akanikaribia na kunitikisa na hapo kidogo nikatanmbua kuwa kuna kitu nilitakiwa kufanya, nikaingia ndani huku nikitweta, nikautua ule mfuko kitandani. Mama Eva akanifuata huku akisisitiza kuwa kuna jambo natakiwa kumweleza, sikumjibu kitu chochote kile.
“Niwekee maji ya kuoga…ama acha nitaweka mwenyewe maji ya kuoga…hivi yanatoka bombani ama…” nilizungumza bila kituo nikijitahidi kujizuia bila mafanikio.
“Umekuwaje baba Eva…” alihoji sasa alimaanisha zaidi.
Sikumjibu na badala yake nikachukua ndoo, nikaenda bombani na kuchota maji, nikamwahidi kuwa nikitoka kuoga nitamsimlia kilichojiri huko nilipotoka, akanikubalia kwa shingo upande.
Wakati naoga nilizidi kuilazimisha akili yangu ikae sawa. Nilimuwaza yule mwanamke niliyeonana naye wakati natoka katika chumba cha Ezekiel. Swali kubwa lilikuwa ni iwapo yule dada anatambua nyumbani kwangu ni wapi, na swali jingine lilikuwa juu ya maongezi yake. Alidai kuwa Ezekiel alikuwa amelala chumbani wakati mimi nimemuona tena akiwa anaelekea kuoza.
Haikuwa mara yangu ya kwanza kuona maiti!! Sikuwa na shaka kwa nilichokiona.
Nilijimwagia maji nisipate walau hisia kama ni ya baridi ama ya moto, manukato yaliyotoka katika ile sabuni hayakuniingia katika hisia hata kidogo. Nilikuwa niponipo tu, nilijua kuwa ninaogopa lakinbi sikujua nafanya nini ili kujitoa katika hali hii.
Mara katika mawazo yangu ikaniajia sauti ya yule mwanamke, ni kama alikuwa anapiga kelele, anapiga kelele akinitaja, nikajigongagonga kichwa mara sauti zile zikakatika, lakini tena zikarejea kama mauzauza sasa nilimsikia akiongea na watu, sauti ileile. Baada ya yeye kuzungumza nikasikia sauti ya kiume, baada ya sauti ya kiume nikasikia sauti ya kike. Sauti hii sasa ilikuwa ya mke wangu,mama Eva.
Bafu letu la nje halikuwa refu sana, nikanyanyua miguu juu nikisimamia kucha ili niweze kuona kama hizo sauti ni kweli ama ni mawazo yangu tu!! Wakati huohuo nikajiapiza kuwa kama nikimaliza kuoga, nitammweleza mke wangu kila kilichotokea naye atanishauri nini cha kufanya, lakini nitaenda na wazo langu kuwa sitakiwi kuwa kimya!! Na kubwa zaiodi sitakiwi kuwa mtaa huo.
Nilitambua kuwa itakuwa ngumu kwa m,ke wangu kunielewa kutokana na wivu wake, lakini ilikuwa lazima anielewe ili niwe huru na mwenye amani.
Kichwa kilifanikiwa kutoka nje na hapo nikamuona mke wangu, na wanaume wawili na mwanamke mmoja ambaye sikuhangaika kumtambua kuwa alikuwa ni yule ambaye tulikutana katika nyumba ya Ezekiel na kisha nikatoroka nikimwacha akakabiliane na kimbembe chumbani.
Kimbembe cha maiti ya Ezekiel.
Mapigo ya moyo yakaongeza kasi yake na hapo nikasikia joto kwa mbali miguuni. Nilikuwa najikojolea.
Maaskari!! Niliwaza kitu kile, nikataka kujipa moyo kuwa sasa ningeweza kutoka na kuzungumza nao lakini nilipowatazama kwa makini walikuwa na nywele ndefu.
Si kwamba hakuna askari mwenye nywele ndefu lakini mmoja alikuwa ni mzungu.
Wametoka wapi upesi kiasi kile.
Hatari!! Kengele zikapiga katika kichwa changu.
Kuendelea kushangaa isingeweza kusaidia, upesi nikakwapua kaptula yangu na kuivaa, nikaachana na taulo, nikapanda juu na kupitia katika dirisha nikaangukia kwa nyuma, sikuishia hapo nikazunguka upesi upande wa pili wa nyumba nikiwa vilevile na bukta yangu, nikawaona wale watui wakiendelea kuhojiana na mke wangu na yule mwaamke akiwahakikishia kitu ambacho sikiweza kukisikia. Mikono ya mama Eva ilielekezea kule bafuni, nikajua anawaambia kuwa nitatoka muda wowote. Nao wakaendelea kusubiria, hadi yule mzungu alipomwambia mwenzake akatazame, yule mtu mweusi akajipapaasa kiunoni na hapo nikaona bastola.
Wanataka kuniua???
Kuna nini? Nilijiuliza huku nikitetemeka. Sikuwahi kuingia katika mlolongo mzito kama huu hapo kabla, nilizoea kupambana kwa maneno lakini sasa kuna mtu ananitafuta akiwa na bunduki, nina hatari gani mimi?
Yule mtu mweusi alirejea akiwa ametaharuki, aliangaza huku na kule kama anayetafuta kitu.
Mzungu akampokea kwa mfadhaiko, na baada ya chochote walichoweza kuongea nilimwona mzungu akijipekua, akatoka na kitu mfanowe pingu, akamfunga mama Eva na kumuunganisha na yule dada.
Nilichanganyikiwa, nikataka kujitokeza na kupambana, nafsi ikakubali lakini mwili ukasita, yule mzungu akaingia ndani mwangu na kutoka baada ya muda, hakuwa amebeba chochote. Nikamshuhudia kitoa maneno makali nisiyoweza kuyasikia, kisha wakaongozana wote na kutoka eneo lile. Nikabaki kuwasindikiza kwa macho.
Punde baada ya wao kutoweka nilitaka kurejea nyumbani lakini nikahisi kuwa patakuwa na mtego wameweka, na kuninasa mimi ingemaanisha kuwa kama ni taarifa kufia hapo basi ni mimi chanzo.
Nilidumu katika fumbo hilo hadi alipopita Selemani, mtoto mtukutu aliyejulikana mtaa mzima, nilimwita huku nikijifanya kuwa niliamua tu kuwa katika vazi lile la kaptula. Selemani alinishangaa lakini mkubwa mkubwa tu hakuniuliza.
“Sele, nenda pale ndani kwangu, angaza pale katika kochi kuna mfuko mweusi una makaratasi niletee, nenda sasa hivi.” Nilimsisitiza naye akatoweka huku akiruka huku na kule na kuimba nyimbo za wasanii anaowajua yeye.
Alipoondoka nilimsindikiza kwa macho hadi alipoingia pale ndani, nil;iangaza kwa makini kama kuna mtu atamvamia lakini hakutokea.
Hatimaye akatoka na mfuko mkononi, hakika nilikuwa nimecheza pata potea.
Maana kama wale watu walihitaji mfuko ule basi ulikuwa umepatikana kirahisi. Mapigo ya moyo yalienda mbio wakati nangojea kukabidhiwa mfuko ule.
Hakuna lolote lililotokea Selemani akanifikishia mfuko ule wenye makaratasi kama ulivyokuwa. Nikastaajabu kuwa kivipi watu wale hawakuuona mfuko ule pale sebuleni hadi waamue kumchukua mke wangu??
Ama hawatafuti mfuko?? Nilijiuliza tena.
Nikamuita Selemani tena, safari hii nikamuagiza suruali yangu na shati.
“Nikuletee na karatasi lile?”
“Karatasi gani tena.” nilihoji.
“Utamfuata mkeo.” Alinambia huku akicheka, yeye alichekeshwa nay ale maandishi lakini mimi yalinistaajabisha.
“Leta tuone..” nilimwambia naye akatoweka mimi nikabaki na ule mfuko wenye makaratasi ambayo sasa niliamini kuwa hayakuwa na maana tena.
Safari hii niliamini kuwa hapakuwa na uangalizi wowote wa nyumba yangu, sikuwa katika uoga. Nikamsindikiza kwa macho huku nikiamini atarudi salama.
Lakini haikuwa hivyo, wakati Selemani anaingia chumbani mwangu, niliwaona anaume wawili. Sio wale wa awali lakini, wakamvamia na kumvuta nje, wakamuuliza kitu nikaona ananyoosha mkono kuelekea upande niliokuwa.
Na mara wale watu wakaanza kutimua mbio kufuata uelekeo huo huku wakiwasiliana kwa simu zao.
Sikungoja kuambiwa, nikaanza kutimua mbio na kaptula yangu mfuko mkononi, miiba ilinichoma lakini sikukumbuka kupunguza mwendo. Hali ya hatari ilikuwa nyuma yangu. Nilikaza mwendo zaidi na hatimaye nikaanza kusikia vishindo vikijongea nyuma yangu kwa kasi kubwa!!
Nimekwisha!!! Nilijisemea!!
 

Similar Discussions

Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…