Mara baada ya kuwepo taarifa za baadhi ya watu kuuza albamu ya msanii wa Bongofleva, Alikiba 'Only One King' mtaani, Serikali kupitia Chama cha Hakimiliki Tanzania (Cosota) imekemea vikali hilo na kusisitiza kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisa Mtendaji Mkuu na Msimamizi wa Hakimiliki Cosota, Doreen Anthony Sinare, watakaokamatwa kwa kufanya hivyo adhabu iliyoainishwa na sheria ni Sh20 milioni au jela miaka mitano.
"Hivi karibuni baada ya mmiliki wa rekodi lebo ya Kings Music na msanii wa muziki, Alikiba kutoa taarifa ya kupatikana kwa albamu yake ya 'Only One King' katika majukwaa mbalimbali ya mtandaoni ya kusambaza muziki 'Digital Platform' kumeibuka watu wanaodurufu na kuuza mitaani pasipo makubaliano yoyote na yeye hii ni kosa kisheria" amesema Sinare na kuongeza.
"Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki namba 7 ya mwaka 1999 imeeleza kuwa kusambaza kazi ya mbunifu yeyote bila ridhaa yake ni kosa kisheria na adhabu yake ni faini isiyopungua Sh20 milioni au kifungo cha miaka mitatu mpaka mitano au vyote kwa pamoja," imeeleza taarifa hiyo.
Utakumbuka albamu ya 'Only One King' ilitoka Oktoba 7, 2021 ikiwa na nyimbo 16 ambazo amewashirikisha wasanii zaidi ya 10 kutoka Tanzania, Kenya, Nigeria, Afrika Kusini na Ghana. Hii ni albamu ya tatu kwa mwimbaji huyo baada ya Cinderella (2007) na Ali K4Real (2009).