nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Imeandikwa tarehe 28 Desemba 2013 By Mwandishi Wetu, Mwanza
NAIBU Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba amesema Serikali haitavumilia baadhi ya askari Polisi wanaonyanyasa waendesha pikipiki za bodaboda. Akihutubia mamia ya waendesha bodaboda jana katika uwanja wa Nyamagana jijini hapa, Makamba alisema Serikali ndiye mtetezi wa madereva hao kwa hiyo iko tayari kuchukua hatua za kisheria dhidi ya askari yeyote anayewanyanyasa. Haiwezekani waendesha pikipiki kunyanyaswa kwani kazi yao inatambuliwa na Serikali na ipo kisheria, ila ninachoomba ni kuzingatia sheria za usalama barabarani, alisema Makamba.
Hata hivyo, alikiri kuwapo baadhi ya waendesha pikipiki wahalifu waliojificha katika kazi hiyo na kuendeleza vitendo viovu ikiwamo unyanganyi wa fedha kwa abiria na kadhalika.
Alitoa mwito kwa waendesha pikipiki kuepuka ajali za mara kwa mara ambazo zimepoteza maisha yao na ya abiria wao.
Makamba alisema kwa sababu maisha ni kitu muhimu, waendesha bodaboda wanapaswa kujiunga na bima ya maisha kwani vyombo wanavyoendesha tayari vina bima na kuhoji kwa nini wao wasiwe na bima ya maisha.
Kwa kuanzia alilipia bima ya maisha waendesha pikipiki 100 walioshinda bahati nasibu iliyochezeshwa papo hapo na alilipa jumla ya Sh 500,000.
Kwa kukatiwa bima hiyo, mwendesha bodaboda atakayepata kilema cha maisha kutokana na ajali atalipwa Sh milioni 10 na akipata ulemavu wa muda mfupi, kila aliyepata ajali atalipwa kulingana na kiasi alichochanga.
Aliwashauri kuanzisha vyama vya kuweka na kukopa ili waweke akiba na kujiwekea bima ya afya na akiba ya uzeeni kwani si kila siku watakuwa wanaendesha pikipiki.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Everist Ndikilo alisema suala la akiba uzeeni ni jambo muhimu kwao sawa na la kuzingatia usalama. Mwakilishi wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Dotto Mdoe alisema Polisi itafanya uchunguzi kubaini wanaojihusisha na unyanyasaji wa waendesha pikipiki na kuchukua hatua.
Hayo yalifikiwa baada ya risala ya Umoja wa Waendesha Pikipiki (UWP) Mwanza iliyosomwa na Katibu Mtendaji wake, Abubakar Juma kuwa waendesha bodaboda wananyanyaswa na Polisi.
source; Habari Leo