Hebu tujikumbushe:
Kikwete chupuchupu
na Juma Kasesa (Tanzania Daima)
RAIS Jakaya Kikwete amenusurika kupata ajali baada ya gari alilokuwa amepanda kulegea gurudumu na kisha kung'oka muda mfupi baada ya yeye mwenyewe kuteremka katika gari hilo kwa dharura wakati akiwa ziarani jijini Dar es Salaam.
Tukio hilo lilitokea jana majira ya saa 9:15 katika Barabara ya Kilwa maeneo ya karibu na zilipo ofisi za makao makuu ya kampuni ya mafuta ya BP.
Kabla ya tukio hilo, msafara wa Rais Kikwete ulisimama ghafla na rais akahamishwa kutoka katika gari hilo aina ya Land Cruiser VX na kwenda katika gari jingine.
Watu walioshuhudia tukio hilo walilieleza Tanzania Daima kuwa, muda mfupi baada ya msafara wa rais kuendelea na safari, dereva wa gari alilohama rais alijaribu kulisogeza pembeni ya barabara, hatua iliyosababisha gurudumu la gari hilo kung'oka na kusababisha ligote chini upande wa mbele kulia.
Tukio hilo liliwashtua watu waliokuwa katika eneo hilo, ambao walianza kujadili ni nini kingetokea iwapo gurudumu hilo lingeng'oka wakati rais akiwa ndani ya gari hilo.
Tukio hilo la rais kulazimika kuhama kutoka katika gari alilokuwa amepanda lilikuwa ni la pili baada ya kufanya hivyo kwa mara ya kwanza akiwa katika maeneo ya Kimara Mavurunza.
Kikwete alikuwa katika ziara yake ya siku moja ya kutembelea miradi ya maji jijini Dar es Salaam.
Msafara huo ukiwa unaondoka Kimara ulisimama ghafla na kuzua taharuki kwa maofisa usalama na wananchi baada ya kuona Rais Kikwete akishushwa ndani ya gari alilokuwa amepanda na kuingia katika gari jingine baada kupata hitilafu huku mvua kubwa ikinyesha.
"Ni kweli matukio hayo yalitokea, katika tukio la kwanza gari alilopanda lilipata hitilafu baada ya gea kugoma kubadilika wakati katika tukio la pili, gari alilopanda lilipata pancha," alisema Rweyemamu.
Alipoulizwa kuhusu taarifa za gari la pili kung'oka gurudumu hata kusababisha kuitwa kwa gari la kubeba magari mabovu, Rweyemamu alikanusha habari hizo na akasema hazikuwa sahihi.
"Ndugu yangu yaani ninyi mnaona taarifa za matatizo ya kawaida ya magari aliyopata rais ni muhimu kuliko adha za maji ambazo alikuwa akikagua katika Jiji la Dar es Salaam?" alihoji Rweyemamu.
Mwandishi wa habari hizi alimweleza Rweyemamu kuwa, gazeti hili liliona umuhimu wa suala hili kwa kuwa lilikuwa likigusa usalama wa kiongozi mkuu wa nchi moja kwa moja.
Jibu hilo lilisababisha Rweyemamu amuombe mwandishi afuatilie kuhusu ukweli wa taarifa hizo na ndipo baada ya muda usiozidi dakika 30 alipiga simu chumba cha habari na kulihakikishia Tanzania Daima kuwa hitilifu za magari alizokabiliana nazo Rais Kikwete zilikuwa ni za kawaida.
MY TAKE: Gari kuzimika kwa kuwa na mafuta machafu, ni jambo la kawaida.