Rare Sapphire
JF-Expert Member
- Jul 24, 2021
- 576
- 1,626
Dar es Salaam. Ujio wa mabehewa mapya 22 yanayotumika reli ya kati na kaskazini umeleta matumaini ya uhakika wa usafiri kwa abiria wanaosafiri kupitia njia hizo.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Desemba 15, 2022 asubuhi Balilusa Kitunda akiwa stesheni ya Kamata tayari kuanza safari kuelekea Kigoma amesema huenda mabehewa hayo yatapunguza adha kubwa ya usafiri kwa watumiaji wa reli ya kati.
“Nasema huenda yakasaidia kwa sababu hatuna uhakika kama hili litaendelea au kutakuwa na kusuasua, ikiendelea hivi basi tutaachana na usafiri wa mabasi turudi kwenye treni usafiri tuliouzoea.
“Leo nimepanda kwenye, behewa jipya najisikia vizuri ikiwezekana ratiba ya safari kwa wiki iongezwe isiwe mara mbili ikiwezekana wafanye kila siku maana kuna uhitaji mkubwa wa usafiri njia ya bara hususani Kigoma isiwe nguvu ya soda,” amesema Kitunda.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa amesema hiyo ni safari ya kwanza kwa mabehewa hayo mapya kubeba abiria ikiwa ni baada ya kufanyiwa majaribio na kuthibitishwa kuwa yako tayari kwa kazi.
Amesema katika safari hiyo ya kwanza mabehewa yamepelekwa safari ya Kigoma na yatakaporejea baadhi yatakwenda reli ya kaskazini kwa ajili kupunguza adha ya usafiri kwa abiria wanaoeleka mikoa ya kaskazini kueleka sikukuu za mwisho wa mwaka.
“Inawezekana tusimalize matatizo yote ya usafiri lakini uwepo wa mabehewa mapya unapunguza presha hasa katika kipindi hiki ambacho watu wengi wanasafiri. Tulikuwa na mabehewa 22 tumepata mapya 22 tunaendelea kuboresha.
“Safari ya leo itahusisha mabehewa mapya yote ndani yake kuna abiria zaidi ya 1,500 kila behewa lina uwezo wa kubeba abiria 80 na yapo katika makundi mbalimbali kuna ya kulala na kukaa,” amesema Kadogosa.
Mkurugenzi huyo amewahikikishia wananchi wanaotumia usafiri wa reli kwamba hakutakuwa na changamoto ya usafiri katika kipindi hiki cha mwisho wa mwaka kwani TRC imejipanga kuhakikisha usafiri huo unakuwepo kwa nauli zilizopangwa na si vinginevyo.
Mwananchi