Hii habari inathibitisha kuwa ni kweli baadhi ya viongozi wa CHADEMA, CUF, Tanzania Daima na magazeti mengine wako mfukoni mwa mafisadi... Tanzania kweli safari bado ndefu kufikia uhuru kamili.
Operesheni okoa
mapacha watatu
* Ni Edward Lowassa, Rostam Aziz na Andrew Chenge
* Wapinzani, magazeti, wanavyuo wapangwa kuwatetea
* Mkakati wa siri waanza kuvuruga maamuzi ya CCM
MWANDISHI WETU
Dar es Salaam
OPERESHENI kabambe ijulikanayo kama okoa mapacha watatu sasa imeanza rasmi ikiwa na lengo la kuzuia Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa, waziri wa zamani aliyeng'oka serikalini kwa sakata ya rada, Andrew Chenge, na mfanyabiashara mwenye tuhuma lukuki, Rostam Aziz, wasifukuzwe kutoka kwenye Chama Cha Mapinduzi (CCM), KuliKoni imebaini.
Operesheni hii inakuja baada ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) kuwataka Lowassa, Rostam na Chenge, ambao wanaunda kundi la wanasiasa maarufu kama "mapacha watatu" kujiuzulu nyadhifa zao kwenye chama kutokana na tuhuma za muda mrefu za ufisadi dhidi yao.
Makada wa CCM wameiambia KuliKoni kuwa kuendelea kuwepo kwa wanasiasa hawa ndani ya chama kunaleta "hali ya hatari" kwa umoja na ustawi wa chama kuelekea kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.
Taarifa kutoka ndani ya CCM zinasema kuwa kitendo cha Sekretariat ya chama kuwapa kina Lowassa, Rostam na Chenge miezi mitatu (siku 90) kujiuzulu wao wenyewe ilikuwa ni kosa la kiufundi kwani wafuasi wa kundi hilo wamepata muda tosha wa kukivuruga chama.
"Kwa kujivua gamba, CCM ilifanya jambo la maana sana na ambalo limerejesha imani ya wananchi kwa chama hiki. Lakini kosa kubwa ni kuwapa hawa mapacha watatu siku 90 waweze kujipanga na kuzuia kufukuzwa kwao kwenye chama," Abdallah Simba, kada wa CCM anayeishi Dar es Salaam ameiambia KuliKoni.
"Hawa mapacha matatu wamekuwa ni chanzo cha CCM kupoteza haiba kwa wananchi na kutuhumiwa kuwa chama kinawakumbatia mafisadi. Ingetakiwa wavuliwe uanachama mara moja ili kuonesha kuwa kweli sasa CCM iko serious kujivua gamba."
Watu waliokaribu na wafuasi wa "mapacha watatu" wameiambia KuliKoni kuwa kuna mkakati kabambe umepangwa ili kujaribu kuwanusuru wanasiasa hawa wasifukuzwe ndani ya CCM.
Mkakati huo umelenga kuwatumia viongozi wa vyama vya upinzani, viongozi wa dini, wanafunzi wa vyuo vikuu, vyombo vya usalama na wanasiasa mahiri ndani ya chama tawala.
"Hapa CCM inatakiwa kuondokana na huu mzigo wa viongozi walioharibu sifa ya chama hiki mbele ya Watanzania. Inabidi wachukue hatua za haraka sana kuwafukuza kwenye chama. Hizo ziku 90 walizopewa watazitumia kukivuruga chama," Tumaini Masawe, mfuasi wa CCM ameiambia KuliKoni.
"Sasa hivi kuna hali ya hatari ndani ya CCM. Hawa wanasiasa ni sumu kubwa na wasiachiwe waendelee kukibomoa chama chetu. Ili kurudisha heshima ya CCM kwa Watanzania ni lazima Lowassa, Rostam na Chenge wafukuzwe kwenye chama. Hawa ndiyo wamekuwa wakitajwa na wananchi nchi nzima kuwa wanaharibu sifa ya chama."
Licha ya tuhuma za kuhusika kwenye kashfa ya Richmond/Dowans iliyomlazimisha ajiuzulu kama Waziri Mkuu mwaka 2008, Lowassa amehusishwa kwa muda mrefu kuwa amejilimbikizia mali nyingi tangu awe kiongozi wa umma.
Gazeti moja la kila wiki limewahi kuripoti kuwa familia ya Lowassa inachunguzwa na polisi ya Uingereza baada ya kununua jumba lenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 1 jijini London.
Kwa upande wake, Chenge naye alijiuzulu mwaka 2008 baada ya makachero wa Uingereza kumhusisha na kashfa ya rada na kukuta zaidi ya shilingi bilioni 1.5 zikiwa zimewekwa kwenye akaunti ya nje ya mwanasiasa huyo.
Chenge pia anahusishwa na mikataba yenye utata mkubwa wakati alipokuwa Mwanasheria Mkuu wa serikali chini ya Rais Benjamin Mkapa.
Naye Rostam Aziz ametajwa kwenye tuhuma lukuki ikiwemo Richmond/Dowans, Kagoda Agriculture Limited iliyopora shilingi bilioni 40 kutoka akaunti ya EPA ya Benki Kuu, ubadhirifu wa pesa za Mfuko wa Commodity Import Support (CIS) na mengineyo.
Lowassa, Rostam na Chenge wote wamekanusha katika wakati tofauti kuhusika na tuhuma zozote za ufisadi.
Vyanzo vyetu vya habari sasa vinasema kuwa mikakati ya kuwaokoa wanasiasa hawa wasifukuzwe CCM zinazotumia mabilioni ya shilingi ili kuleta mvurugano mkubwa ndani ya chama.
Vifuatavyo vimetajwa kuwa ni baadhi ya vipengele vikuu vya mkakati huo uliopewa jina la "okoa mapacha watatu:"
Viongozi wa upinzani
Kundi la wafuasi wa "mapacha watatu" limelenga kukitumia chama kikuu cha upinzani hapa nchini, CHADEMA, ili kujinusuru kufukuzwa kutoka CCM. Lengo ni kuibua tuhuma mpya za ufisadi za uongo dhidi ya Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Jakaya Kikwete, na viongozi wengine ili kuleta mvurugano ndani ya chama.
CHADEMA inadaiwa kubebeshwa ajenda ya "List of Shame" mpya katika siku 90 zijazo na kutoa tuhuma dhidi ya viongozi wengi wa CCM ili kina Lowassa, Rostam na Chenge wapate kujitetea.
"Kwa kutumia "List of Shame" mpya inayoendea kutangazwa na CHADEMA, mapacha watatu watasimama mbele ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) na kusema eti wao wameonewa kwa kuambiwa kujiuzulu wakati wenye tuhuma za ufisadi ni wengi akiwemo Rais Kikwete," alisema kada mmoja wa CCM.
"Hawa CHADEMA waliibuka na "List of Shame" mpya siku chache tu baada ya CCM kuwataka kina Rostam wajiuzulu. Wangekuwa kweli hawajabebeshwa ajenda hii na wanaitakia mema taifa wangesubiri hizo siku 90 zipite na mapacha watatu wang'olewe CCM ndiyo waye na orodha mpya ya mafisadi."
Pamoja na CHADEMA, viongozi wa vyama vingine vya upinzani ikiwemo CUF, NCCR-Mageuzi, TLP, UDP na DP nao wamepangwa kutumika kwenye mkakati huu.
Vyombo vya habari
Baadhi ya magazeti yanayodaiwa kuwa karibu na vyama vya upinzani na vyombo vya habari vingine navyo vimepangwa kutumika katika mkakati wa "okoa mapacha watatu."
Vyombo hivi vya habari vimepewa jukumu la kutoa umuhimu mkubwa wa tuhuma mpya za kutungwa za ufisadi dhidi ya wanasiasa kadhaa ndani ya CCM akiwemo Kikwete, mawaziri fulani na viongozi wastaafu kama Waziri Mkuu Frederick Sumaye.
"Katika siku 90 hizi tutaona magazeti yakiandika tuhuma nyingi dhidi ya viongozi wengine wa CCM. Mapacha watatu watatumia magazeti haya kama vielelezo vyao kwenye mikutano ijao ya NEC kujaribu kuzuia wasifukuzwe kwenye chama," alisema mwanachama mmoja wa CCM anayefahamu mkakati huo.
"Kuna baadhi ya wajumbe wa NEC wamepangwa kusimama kwenye vikao na kuwatetea mapacha watatu na kutumia List of Shame mpya ya CHADEMA na taarifa za magazeti yaliyopangwa kama vielelezo vyao."
Viongozi wa dini
Viongozi wa dini hawa nao wamejumuishwa kwenye mpango wa kuivuruga CCM. Taarifa za uhakika zinasema kuwa baadhi ya viongozi wa dini wamepangwa kujitokeza hadharani kukosoa maamuzi ya CCM na kuwatetea "mapacha watatu."
"Kuna baadhi ya viongozi wa dini tayari wameanza kusambazwa nchi nzima kutoa matamshi hadharani kupinga maamuzi ya kihistoria ya CCM. Ni aibu sana kuona viongozi hawa wanakubali kutumika," alisema mwananchama mmoja wa CCM.
Vyombo vya usalama
Imedaiwa kuwa kundi la wafuasi wa wanasiasa waliojeruhiwa na uamuzi wa CCM kujivua gamba limepanga kutumia ushawishi wake kwenye vyombo vya usalama hapa nchini ili kuleta hofu potofu ndani ya chama na nchi kwa ujumla.
"KUna ripoti za kupikwa zinaandaliwa kupelekwa kwa Rais Kikwete na kudai eti kufukuzwa kwa mapacha watatu kutaleta mpasuko mkubwa zaidi CCM na kukifanya kisambaratike," alisema ofisa mmoja aliye karibu na serikali.
"Taarifa hizi za uongo za kiintelijensia zimepengwa kuleta hofu kubwa ndani ya CCM ili waogope kuendelea na hatua za kujisafisha."
Wanavyuo
Hivi sasa kuna jitihada za kuwapa pesa baadhi ya viongozi wa wanafunzi kwenye vyuo vya elimu ya juu nchini ili kujaribu kuwaunga mkono wanasiasa wasiotakiwa CCM kutokana na tuhuma za ufisadi.
"Ni kweli baadhi yetu tumepewa pesa na kuitwa kwenda kwenye vikao vya kujadili nini cha kufanya. Tunatarajiwa kupewa maelekezo ya nini cha kufanya," alisema mwanafunzi mmoja wa chuo cha elimu ya juu kilichopo Dodoma bila kufafanua zaidi.
Wajumbe wa NEC
Karata ya mwisho ya wafuasi wa "mapacha watatu" ni kujaribu kuibomoa CCM na kupindisha maamuzi ya NEC. Mbinu hii inalenga kupata kuungwa mkono na wajumbe kadhaa wa NEC ambao watasimama kidete kwenye vikao vijavyo vya chama kupinga wanasiasa hao wafukuzwe uanachama wa CCM au wanyang'anywe nafasi zao za uongozi.
"Wenyeviti wa CCM wa mikoa, wenyeviti wa wilaya, baadhi ya waasisi wa CCM na viongozi wakongwe wanaoheshimika, pamoja na wajumbe wa NEC wameendaliwa fungu kubwa la pesa wapindishe maamuzi ya CCM ya kujivua gamba," amesema kada mmoja wa CCM.
"Wamepangwa kuja na hoja kwenye vikao vijavyo kuwa NEC haijaagiza Lowassa, Rostam na Chenge wapewe siku 90 kujiuzulu na kuwa eti hakuna azimio lolote la NEC kuhusu hilo. Hizi ni mbinu za kukibomoa chama tu ili waweze kujiokoa."
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Taifa, Nape Nnauye, amekaririwa na baadhi ya vyombo vya habari wiki hii akisema kuwa chama hicho kimedhamiria kujisafisha na kuondokana na viongozi wote wenye tuhuma kubwa za ufisadi.
Tumewapa miezi mitatu watuhumiwa wote wa ufisadi katika chama chetu wajiondoe wenyewe. Baadhi wanajaribu kupinga na kujibu mapigo kwa kutumia magazeti, vyama vya siasa na taasisi za dini...tunajua tutashinda na wao lazima waondoke, alisema Nape.
Tumeandaa mkakati wa kusafisha chama kutoka ngazi za chini mpaka katika ngazi ya taifa. Tumechunguza na tunajua wanaotakiwa kuondoka ndani ya chama chetu."
<Source: KULIKONI, Aprili 22-28, 2011>