Wadau, amani iwe kwenu.
Katiba na sheria za nchi zinampa Rais mamlaka ya kutoa msamaha kwa wafungwa. Hata hivyo, taratibu za kuwapa misamaha wafungwa hao ni lazima ziendane na sheria nyingine. Kwa maana nyingine ni kwamba Rais hana mamlaka ya kutoa msamaha kwa kila mfungwa bali kwa wale tu walioainishwa kwenye sheria husika. Hii ni kwa sababu, wafungwa wengine wamewekewa katazo la kupewa msamaha kutokana na uzito wa makosa waliyotenda.
Miongoni mwa wafungwa ambao hawapaswi kupata msamaha wa Rais ni pamoja na;
1. wafungwa waliohukumiwa kunyongwa,
2. wanaotumikia kifungo cha maisha gerezani,
3. wafungwa wa kupokea na kutoa rushwa,
4. unyang'anyi na unyang'anyi wa kutumia silaha,
5. wafungwa waliopatikana na silaha au risasi.
6. wafungwa wanaotumikia vifungo kwa kulawiti,kunajisi na kubaka.
7. Wafungwa wanaotumikia kifungo kutokana na makosa ya ugaidi
8. waliofungwa kwa makosa ya kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya
9. waliofungwa kwa makosa ya wizi wa magari kwa kutumia silaha,
10. waliotoroka au waliojaribu kutoroka wakiwa chini ya ulinzi halali ambao wanatumikia kifungo hicho gerezani
11. waliopatikana na hatia kwa kutumia madaraka yao vibaya.
12. wafungwa wanaotumikia kifungo kwa kosa la kufanya biashara haramu ya binadamu,
13. Wafungwa wanaotumia kifungo kutokana na kosa la kukutwa na nyara za Serikali
14. waliofungwa kutokana na makosa ya ubadhirifu wa fedha za Serikali.
Kwa nyakati tofauti, Mgombea Urais kwa tiketi ya UKAWA, EDWARD LOWASA amejikuta akiwa kituko kwa kutamka mambo ambayo ni kinyume cha sheria za nchi. Kwanza alisema kuwa akiwa Rais, atamtoa kifungoni Babu Seya ambaye anatumikia kifungo cha maisha kwa kesi ya kubaka na kunajisi.
Jana akiwa Zanzibar amesikika akisema kuwa atawafutia mashtaka watuhumiwa wa Ugaidi wa kikundi cha UAMSHO cha Zanzibar.
Ikumbukwe kuwa sheria zinazomkataza Rais kutoa msamaha wa wafungwa hao hazikutungwa na Chama cha Mapinduzi bali zimetumgwa na Bunge ambalo linajumuisha wabunge wa vyama vyote akiwemo Lowasa. Kwa hali hiyo, ni kituko kilioje kwa mtu ambaye anasaka madaraka kujifanya upofu kutoona uzito wa sheria ambazo yeye ameshiriki kuzitunga.
Yapo masuala tunaweza kuingiza siasa na masuala mengine ni lazima tuziweke siasa pembeni. Sijui kama Lowasa angekuwa ni mwana familia ya wale watoto waliolawitiwa na Babu Seya angekuwa na jeuri ya kutamka hayo. Mahakama zote nchini zimethibitisha pasi na shaka kuwa Babu Seya alifanya kosa hilo na ndo maana hata alipokata rufaa alishindwa.
Nina hakika pia kuwa kama Lowasa angekuwa ni mwana familia ya wale waliouawa kule Zanzibar na Magaidi huku kikundi cha UAMSHO kikihusishwa asingekuwa na kiburi cha kutamka maneno hayo.
Nimalizie kwa kusema kuwa kutafuta Urais si kazi bali kazi ni kuitendea haki kazi ya Urais.