Robert Heriel Mtibeli
JF-Expert Member
- Mar 24, 2018
- 21,340
- 51,891
LISU Na KICHWA CHA YOHANA MBATIZAJI KWENYE SINIA
Na, Robert Heriel
Moja ya hadithi mashuhuri duniani hasa kwa Wafuasi wa Dini za Ukristo ni Pamoja na Kisa cha Nabii Yohana Mbatizaji ambaye kwa Waislamu hufahamika kama YAHAYA. Yohana Mbatizaji(John the Baptist) aliitwa Sauti iliayo Nyikani. Alikuwa ni mtayarishaji au mtu aliyemsafishia njia Yesu wa Nazareth.
Yohana Mbatizaji alikuwa Mashuhuri kwa kipindi kile kuliko hata Yesu, licha ya kuwa alikuwa akitangaza ujio wa Masihi(Yesu Kristo) Yohana Mbatizaji alikuwa na Wafuasi wengi kuliko Yesu kwa kipindi kile bila shaka ni kutokana na uwepo wake wa muda mrefu kwenye field ya unabii. Hii ni kusema hata watawala serikalini walimfahamu akiwemo Mfalme Herode.
Yohana aliingia matatani kwa sababu ya Kusema ukweli; Mdomo wake ndio uliomponza, hata hivyo alikuwa kwenye majukumu yake ya kinabii na kiutumishi kwani moja ya kazi ya nabii ni kusema ukweli na kukemea maovu. Nabii, kuhani, Askofu au mchungaji, Sheikhe, Imamu, Mufti na wengineo wasimamao kwenye madhabahu ya Bwana moja ya kazi zao ni pamoja na Kukemea uovu na kusema ukweli bila kujali nani kaufanya na nini matokeo yake.
Ukiona unaabudu kwenye dini, kanisa, msikiti ambao viongozi wake wanashindwa kukemea uovu au kusema ukweli kwa kuwaambia watu. Au wanaubaguzi wa kukemea watu maovu yao, yaani wanauwezo wa kuwakemea waumini wa kawaida wafanyapo makosa lakini muda huo huo wanashindwa kuwakemea viongozi wakubwa wa nchi, au kukemea matajiri, basi jua unaabudu mahali pasipo sahihi. Jua kiongozi huyo wa dini hana mamlaka ya kukusalisha, hana kibali cha Mungu bali anajali maslahi yake.
Ni bora ukaabudu Msikiti au kanisa la Mashetani linalokemea maovu kuliko kuabudu katika msikiti au kanisa linalojiita la Mungu wakati linashindwa kukemea maovu.
Yohana Mbatizaji kama walivyo manabii wengine na makuhani waliowaaminifu akamchana makavu Mfalme Herode kwa kumwambia aache dhambi ta Uzinzi kwa kutoka na Mke wa Kaka yake, kwani hiyo sio halali.
Ukisoma kisa kile utagundua kuwa Mfalme Herode alikasirika mno na alitaka kumuua lakini alihofia watu kwani walishamuona Yohana Mbatizaji kuwa ni Nabii. Hivyo alichokifanya akaunda njama/ zengwe, na Hila akamsweka Yohana Mbatizaji Mahabusu. Nafikiri lengo lake ni kuondoa kero za Yohana Mbatizaji ili yeye azidi kula Uroda na Mke wa Kaka yake, yaani shemeji yake. (Na Hapa ni Mke wa Kaka yake Mfalme Herode yaani shemeji yake)
Kumbuka kusema ukweli ndio kilichomponza Yohana Mbatizaji lakini hatuwezi kusema kilimponza kwani alikuwa kwenye majukumu yake. Ni sawa na Dokta kujichoma sindano kwa bahati mbaya wakati akimchoma mgonjwa.
Kumbe yule mwanamke(Herodia mke wa Filipo anayechepuka na Mfalme Herode) naye alipenda mchezo wa kuliwa uroda, hivyo hakupendezwa na harakati za Yohana Mbatizaji. Hivyo naye alimuweka kiporo huku akimtafutia nafasi ya kumuangamiza.
Siku moja ya ya karamu katika Jumba la Mfalme Herode kulikuwa na muziki ambapo binti mmoja alicheza kupitiliza (binti huyu mamaye ni Herodia) mpaka Mfalme Herode akafurahi na kumpa nafasi ya kutaka lolote naye akiahidi kumpa. Binti Herodia kusikia hivyo akaenda kwa Mamaye(ndiye Herodia) kumuuliza, hii ikawa nafasi ya herodia kummaliza Yohana Mbatizaji. Hivyo akaagiza aletewe kichwa cha Yohana Mbatizaji kwenye Sinia.
Binti akarudi akamuambia Mfalme Herode kuwa anahitaji kichwa cha Yohana Mbatizaji kiletwe pale muda ule ule kikiwa kwenye sinia. Bila shaka Mfalme akajua kuwa hizo ni hila za mchepuko wake(Herodia) Pengine ingekuwa filamu basi angegeuza shingo taratibu na kumuangalia mchepuko wake, kisha mchepuko wake(Herodia angetabasamu kwa kuona ameshinda.
Mfalme Herode aliumia sema hakuwa na jinsi kwani tayari alishaahidi tena mbele za watu. Hatimaye kichwa cha Yohana Mbatizaji kilikatwa huko Gerezani na kuletwa kwenye sinia. Loooh!
Kichwa cha Nabii leo juu ya sinia, mbele za watu mziki wa starehe ukipigwa watu wakishangilia wachache wakisononeka.
Lisu ni kama Yohana Mbatizaji, anasema ukweli lakini ukweli wake hauna maana yeyote kwa watu wapumbavu na waovu. Lisu yupo kwenye majukumu yake, hata ajali aliyoipata ni ajali kazini.
Lisu anaeleweka zaidi kwa watu wapenda haki, watu wa Mungu, na anaeleweka zaidi na Mungu.
Lisu hawezi na kamwe hataeleweka kwa watu waovu, wenye tabia ya umungu mtu, mashetani, pengine na wale wajinga ambao sio kosa lao kwani wamepotoshwa na waovu.
Hakukuwa na sababu ya Kumkata Kichwa Yohana Mbatizaji, haikuwepo. Pengine ilikuwepo sababu moja tuu! nayo ni uovu, yaani kumuua msema kweli, mkemea maovu kusudi waovu waendelee kutanua.
Ukweli ni huwezi kumuua ateteaye uovu ukaacha kuua. Lazima uendelee kuua na kuua na kuua mpaka nawe utakapokufa. Walipomuua Yohana Mbatizaji, walidhani wamemaliza kazi lakini kumbe mambo hayaendi hivyo. Punde Yesu naye anaingia kwenye Field, naye wakamuua, wakadhani wamemaliza, lakini haikuwa hivyo, wakaanza kuwaua wanafunzi wake, wakadhani wamemaliza, Looh! haikuwa hivyo wakazaliwa wengine mpaka wakina Martin Luther, Kina Wyclif, William Miler, mpaka hivi leo tupo bado watetezi wa haki huuawa.
Wauaji hawajui jambo moja, huwezi ukamaliza watetezi wa haki kwa kuwaua. Kama ilivyo kwa watetezi wa haki, huwezi kumaliza uovu kwa kuwaua waovu. Uovu haumalizwi kwa kuua watu. Au haki au wema haumalizwi kwa kuua watu wema. Bali mambo hayo humalizwa kwa elimu ya kiroho, na kuchanganya damu.
Lisu ni kama kichwa cha Yohana Mbatizaji kwenye Sinia. Kumkata kichwa haimaanishi ndio kumaliza harakati zake.
Nafikiri waliompiga Lisu Risasi wataungana na Mimi kuwa Risasi au kumuua mtu sio njia sahihi ya kuondoa utetezi wa haki, au kuondoa uovu kama waliona uovu kwa Lisu.
Nimalize kwa kusema; Mungu ni Upendo, nao wenye upendo hao ndio watoto wake.
Hatuwezi nyamazishwa na wanadamu ikiwa tunajua tunatetea haki. Lakini pia hatuwezi kukaa kimya kisa watendao uovu ni watu wetu wakaribu tuwapendao.
Robert Heriel
Taikon wa Fasihi
0693322300
Kwa sasa Unguja.