ya takrima: Tendwa amtetea Kikwete
• Asema rais alikuwa akitania
na Hellen Ngoromera
MSAJILI wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa amesema kauli aliyoitoa Rais Jakaya Kikwete kuhusu takrima ilikuwa ni ya utani na wala hakuwa na lengo la kupingana na uamuzi wa Mahakama Kuu kuhusu suala hilo.
Tendwa alitoa kauli hiyo ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari katika mkutano aliouitisha ili kuzungumza nao kuhusu sheria ya gharama za uchaguzi.
Msajili huyo alisema wakati rais anazungumza suala hilo katika mkutano uliowajumuisha viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini uliofanyika Ijumaa iliyopita jijini Dar es Salaam, alikuwa akifanya utani na kwamba yeye binafsi (Tendwa) hakuona kama kuna utata.
"Rais alitoa joke, mimi sikuona kama kuna utata na wala si kubariki takrima, haiwezekani hata kidogo, na rais hawezi kufanya hivyo, alichosema ni kuwa kuna ugumu na wala hakuhalalisha, sasa utani ni utani na sheria ni sheria… hivi kweli nanyi mnaichukulia hiyo kama kuhalalisha suala hilo wakati lilifutwa?" alisema Tendwa.
Ijumaa iliyopita, Rais Kikwete alisema mbele ya viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini kwamba, suala la kudhibiti takrima hasa wakati wa uchaguzi ni gumu.
Kikwete ambaye alitoa kauli hiyo muda mfupi kabla ya kufunga mkutano wa siku mbili ulioandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, lengo likiwa kujadili masuala ya uchaguzi na sheria zake kwa viongozi hao wa dini, alisema kwenye baadhi ya mikoa yapo mazingira maalumu ambayo kabla ya kuzungumza jambo lazima walengwa wawe na kitu (alitoa mfano wa pombe) vinginevyo hautaeleweka.
Akizungumzia kuhusu sheria ya gharama za uchaguzi, Tendwa alisema ofisi yake imeanza utaratibu wa kuelimisha wananchi ili kuelewa na wameshatoa elimu hiyo katika Kanda ya Mashariki inayojumuisha mikoa ya Pwani, Dar es Salaam na Morogoro, pia ya Kaskazini inayojumuisha mikoa ya Kaskazini, Arusha Tanga, Kilimanjaro na Manyara.
Alisema madhumuni ya kutoa elimu kuhusu sheria hiyo ambayo alisema ni nzuri lakini ngumu kutekelezwa, ni kuwawezesha wananchi kuielewa kwani inagusa jamii nzima wakiwemo wagombea, vyama vya siasa, wapiga kura na kwamba lengo lake ni kuondoa rushwa katika uchaguzi.
"Sheria hii ni nzuri, lakini ngumu kutekelezwa, kama tutakumbuka chaguzi nyingi zilizopita zilitawaliwa na rushwa na kuharibu maadili ya taifa, hata hivyo sheria hii inatoa mamlaka kwa vyombo vya dola kuwashughulikia wanaohusika na rushwa, mfano TAKUKURU," alisema Tendwa.
Kwa mujibu wa Tendwa, kwenye vyama vya siasa ndiko kwenye makosa mengi ya rushwa, akatolea mfano katika uchaguzi wa mwaka 2005 kuwa wagombea wengi walituhumiwa kwa rushwa, lakini hakukuwa na ushahidi wa kisheria uliowabana kutokana na ushahidi wa mazingira kutowabana na kwamba sheria ya sasa itawafanya watakaothibitika kukosa hata ubunge.
Msajili alisema sheria hiyo itawawabana pia wananchi, hivyo alitoa onyo kwa wanaotumia mwanya katika kipindi cha uchaguzi kuwa ni cha mavuno au neema kwa kujipatia fedha au kujenga nyumba na kusema tabia hiyo sasa basi na atakayebainika kufanya hivyo atashtakiwa.
Alibainisha pia kuwa sambamba na kuwabana wananchi, sheria hiyo pia itakifungia chama chochote kitakachojihusisha na rushwa kushiriki katika uchaguzi utakaofuata.
Alipoulizwa ikiwa mgombea wa Chama Cha Mapinduzi ambaye ndiye rais anayemteua yeye (Tendwa) kushika wadhifa huo akipatikana na hatia ya kuhonga wapiga kura itakuwaje, alijibu kuwa; "hata kama rais yuko mstari wa mbele kutoa kitu kidogo hakuna jinsi, tutashughulika na sheria."
Aliyataja maeneo mengine yaliyokatazwa katika sheria hiyo kuwa ni mgombea kuahidi cheo, wadhifa kwa mpiga kura, zawadi, malipo ya chakula, vinywaji, kusafirisha wapiga kura kuwapeleka katika vituo vya kupigia kura na nyingine kwani serikali ndiyo itakuwa na wajibu wa kuwashughulikia wapiga kura wakati wa uchaguzi.
Alipoulizwa kuhusu marekebisho ya kanuni za sheria ya gharama za uchaguzi zilizolalamikiwa na wabunge, ikiwemo kiwango kidogo cha fedha kwa wagombea urais na wabunge, alisema kanuni ziko tayari na leo yatapelekwa katika kikao cha Kamati ya Katiba ya Baraza la Mawaziri kwa hatua zaidi.
Alisema pamoja na mambo mengine, jana alikutana na watendaji wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili kujua wajibu wao kuhusu sheria hiyo, pia alishakutana na wabunge na kwamba kwa sasa ofisi yake inaandaa utaratibu wa kukutana wa waandishi wa habari ili kuwapa elimu kuhusu sheria hiyo. Alibainisha pia kuwa ofisi yake na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) hazina haja kushirikiana kwani wao ni wadau wamoja katika sheria hiyo na kwamba kipindi hiki si cha kuleta migongano.
Source:
Hoja ya takrima: Tendwa amtetea Kikwete