Naomba niwajibu wote kwa pamoja mnaofikiri kwamba mimi nimeajiriwa ...
Nikiwa mdogo (chini ya miaka 14) nilikuwa na uwezo wa kutengeneza vikapu - entukuru na kupeleka minadani. Haikutosha, nikawa nafuga kuku wa kienyeji, nauza mayai na kuku pia. Shughuli hiyo niliendelea nayo hadi nilipomaliza elimu ya msingi na kulazimika kwenda sekondari - bweni.
Wakati nikiwa sekondari, likizo zangu zote nilirudi kijijini kuendelea na mchakato huo huo. Hivyo kwenye kukua kwangu nilizoea mzingira ya kujitafutia pesa za kwangu binafsi kwa ajili ya matumizi yangu. Wazazi waliwajibika kulipa karo (japo ilikuwa kidogo) pamoja na matumizi mengine ya lazima pindi niwapo shuleni.
Baada ya kumaliza kidato cha nne, nilijiunga moja kwa moja DarTech (kwa sasa inaitwa DIT); nikiwa hapo nilikuwa nachukua bidhaa toka mipakani Tunduma na Mtukura na kuwauzia wamachinga kwa bei ya jumla; wao wanaingiza mtaani na kupata faida. Baadaye nikapata mchongo wa kwamba chuma chakavu kina soko nchini Kenya - mnunuzi mzuri alikuwa anaitwa Mkole (sijui kama bado yupo). Niliporudi nyumani nilinunua mzani kwa ajili ya kupima chuma - hivyo vijana wa pale mtaani walikusanya masufuria mabovu, nyaya n.k na kuleta kupima; nilimwajiri kijana ambaye kazi yake ilikuwa ni kupima na kutunza kumbukumbu. Akifikisha mzigo unaozidi kilo 100 nilisafiri toka Dar kurudi home ili nisafirishe mzigo kupeleka Kenya. Huko nilirudi na bidhaa za urembo ambazo niliendelea kuwauzia wamachinga.
Baada ya kumaliza chuo; sikuwa na wazo la kuajiriwa kwa kuwa tayari nilishakuwa mzoefu wa kutosa hela kwenye biashara na kupata faida. Kwa kuwa nilikuwa huru, nilifanikiwa kupata watu wenye mali ambazo zina spidi ndogo (hazitoki sana) hivyo walinipatia ili niwe na mlango wa biashara hapa Tanzania. NIliendelea na shughuli hizo na baadaye niliona kuwa shughuli za matumizi ya computer zinalipa; hivyo nilijiandikisha kufanya mitihani kwa kuwa ujuzi wa kutumia computer nilikuwa nao tayari (Nilisoma computer DarTech kama somo la ziada ambalo tulikuwa hatufanyi mtihani - miaka ya 90 hiyo).
Hadi sasa ninapoandika hivi; huwa nafanya kazi za muda; nalipwa kilicho changu naendelea na shughuli zangu. Ajira inafunga ufahamu; sio kwamba nawadanganya - hii ndiyo kweli yangu. Kwa sasa ni muelimishaji wa vikundi vya wajasiriamali; nafuga, nafanya kazi na NGO ambayo mimi ni mwanzilishi - MAISHA YANAENDA.
Ukipata ajira fanya ila usikae tu nyumbani eti unasubiri ajira wakati benk una pesa kama laki 500,000/= inaendelea kupungua kila iitwayo leo.