SIKU moja baada ya serikali kuamua kupitisha waya za umeme wa kilovoti 132 karibu na Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF), Askofu Mkuu wa Kanisa hilo, Zachary Kakobe, amesema anaamini umeme hautawaka kwa nguvu ya Mungu kwa vile hakuna nguvu zitakazopita hapo. Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana, Askofu Kakobe alisema ameshangazwa na kauli ya Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, kuutangazia umma kuwa ameridhia umeme huo kupitishwa kwenye kanisa hilo.
Nakwambia hata wakipitisha umeme huu hapa
hautawaka kwa vile nguvu ya Mungu itashinda nguvu ya umeme lakini kibaya nimesikitishwa na Waziri Ngeleja kuutangazia umma eti nimekubali umeme upitishwe hapa, nasema siyo kweli jamani, alisema Askofu Kakobe.
Alisema yeye mwenyewe hana uwezo wa kukataa maamuzi yaliyofikiwa na serikali ndiyo maana hadi jana hakukuwa na muumini hata mmoja ambaye alikuwa akililinda eneo hilo.
Huu ni uonevu wa hali ya juu, sijakubaliana na maamuzi hayo kwa kuwa vipimo vyote vilivyotolewa havikuwa vya kweli na kama ningekuwa nimeafiki basi ile siku Waziri Ngeleja alivyotoa taarifa yake ningeshiriki katika hicho kikao, alisema Askofu Kakobe.
Alisema hivi sasa amegundua hawatakiwi kupinga upitishaji wa umeme huo kimwili kama walivyokuwa wamefanya huko siku za nyuma bali ni kutakiwa kukaa katika maombi.
Alisema ni hatari kukatalia utawala ambao hauna hofu ya Mungu kwa kuwa hauwezi kudumu na mara nyingi unakosa kutenda haki, hivyo jamii nzima inatakiwa kuondoa tofauti zao na kuwa na sauti moja ili kukemea unyanyasaji unaofanywa na utawala.
Alisema hivi sasa amepata taarifa za uhakika kuwa baadhi ya watu wamepewa taarifa kuwa wanatakiwa kuhama katika eneo hilo kupisha upitishaji wa nguvu hiyo ya umeme kitendo ambacho kinampa ishara kuwa kuna mpango wa kanisa lake kuvunjwa.
Kwa sasa jamii haiwezi kunielewa, lakini ukweli ni kuwa serikali hii imedhamiria kuvunja maeneo hayo kwa kuwa hakuna mradi kama huu unaofanyika ukaruhusu jirani kuwa na vizuizi kama majengo alisema Askofu Kakobe.
Alisema amesikitishwa na Waziri Ngeleja kutoa maelezo kuwa hata kituo cha televisheni ambacho anatarajia kuanzisha hakitaweza kukidhi vigezo.
Unawezaje kusema eti hatuwezi kukidhi vigezo vya kuomba usajili, inawezekana labda wameshafikia hatua ya kutaka kutunyima kibali maana wanatoa kauli hizo ambazo zinaweza kuwa ni dalili njema, alisema Askofu Kakobe.
Askofu Kakobe alipingana na madai yaliyotolewa na Mshauri Mtaalam wa Kampuni ya BICO, kuwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), linatakiwa kuepukana na kona kali kwenye waya na kutounganisha sehemu yoyote kati ya nguzo namba 18 na 19.
Akitolea mfano, alisema kuna maeneo mbambali yaliyopitishiwa umeme kama huo, ingawa unatofautiana kwa ukubwa wake, ambao umewekwa kona ikiwemo maeneo ya Mwenge na katika kijiji cha Tanangozi kilichoko Iringa karibu na makaburi ya Kiyeyeu.
Huu ni uwongo! Wanafikiri hatuna uelewa wa masuala hayo ya umeme? Si kweli kuwa kunaweza kutokea madhara iwapo kutawekwa kona kama wangepitisha upande wa pili; mbona karibu na kaburi la Kiyeyeu kule Iringa nguzo zimevushwa upande wa pili? alihoji Askofu Kakobe.
Juzi Waziri Ngeleja aliwaambia waandishi wa habari kuwa mgogoro uliodumu kwa siku 77 kati ya serikali na Askofu Kakobe umemaliza kwa askofu huyu kukubali umeme huo kupitishwa eneo la kanisa lake.
SORCE Tanzania Daima.