Katiba tuitakayo: Kwanini tuujadili Muungano? 4

Kaa la Moto

JF-Expert Member
Apr 24, 2008
7,903
1,053
Monday, 18 June 2012 13:37

Nafasi ya Urais
Urais ndio alama kubwa ya Muungano. Urais unashika nguvu zote za dola na kwa hivyo Mtanzania anaekuwa Rais ndiye mwenye amri ya mwisho katika uteuzi, kutangaza vita na hali ya hatari, kumaliza maisha ya Mtanzania, kumsamehe kifungo chake nk. Rais kwa mujibu wa Katiba hapaswi kufuata ushauri wowote ule.

Nafasi ya Urais hugombewa, lakini sivyo ilivyokuwa hapo mwanzo kabisa ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikuwa kwa njia ya makubaliano chini ya Mkataba wa Muungano, ambapo Makamo wa Rais alikuwa akitoka Zanzibar moja kwa moja.

Kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano hiyo ilikuwa ni mipango ya muda na ilikuwa wananchi waulizwe, kwa njia ya Kura ya Maoni au nyengine yoyote ambayo ingefaa, mwaka uliofuata yaani 1965, lakini tunajua kuwa Rais Julius Nyerere alisogeza au aliindoa fursa hiyo kwa muda usiojulikana na Kura ya Maoni hiyo haikufanyika tena.

Kuanzia mwaka 1970 Wazanzibari wakaanza kushiriki katika chaguzi za Tanzania kuchagua Rais wa Jamhuri ya Muungano huku Makamo wa Rais akiwa moja kwa moja ni Rais wa Zanzibar , kama Mkataba wa Muungano unavyoeleza.

Kupiga kura kwa Wazanzibari katika uchaguzi wa Rais wa Tanzania kuanzia 1970 hadi 1990 hapakuwa na athari yoyote kwa sababu idadi ya Wazanzibari wote ni sehemu ndogo tu ya wapiga kura wote wa Tanzania na kwa kuwa kura ya Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania ni jimbo moja tu la uchaguzi, matokeo ya aina yoyote ya Zanzibar hayangeweza kuathiri taswira ya Urais wa Muungano.

Lakini iwapo kungekua na kifungu cha Katiba kinachotaka idadi fulani ya wapiga kura wa Zanzibar waridhie Urais wa Muungano pengine hali ingekuwa ni nyengine, lakini kwa muda wote ridhaa ya Wazanzibari katika nafasi hii imekuwa haitakiwi kwa njia ya kura na kisanduku.

Urais wa Tanzania ulishikiliwa na Julius Nyerere kutoka 1964 hadi 1985, wakati Ali Hassan Mwinyi akiwa ni Mzanzibari aliposhika nafasi hiyo kwa muda wa miaka 10 na kuanzia hapo Benjamin Mkapa amekaa miaka 10 na Jakaya Mrisho Kikwete yupo katika kipindi chake cha pili kutimiza miaka 10.

Ilikuwa ni mwaka 1995 wakati mfumo mpya wa Mgombea Mwenza ulipoanzishwa sambamba na kusimamishwa mfumo wa vyama vingi vya siasa na kuanzia hapo imekuwa ni lazima Mgombea Urais awe na Mgombea Mwenza kutoka upande tofuati wa Tanzania anaotoka yeye Rais.

Kuna mifano mingi ya nchi zilizoungana ambapo nafasi ya Urais imekuwa ikizunguka ili kuonyesha ushiriki wa sehemu nyengine katika Muungano lakini pia kutoa fursa sawa za kushika nafasi hiyo na sio upande mmoja kuishika kwa ajili ya wingi wake wa wapiga kura.

Hii ni sababu moja ya kujadili Muungano ambapo fikra mpya zinaweza kuja juu ya namna ya kupata kiongozi wa nchi ambapo si lazima atokane na kura za wananchi moja kwa moja, kadri ambavyo mapendekezo yatavyoweza kutolewa wakati wa Mjadala wa Katiba.

Orodha ya mambo ya Muungano
Orodha ya Mambo ya Muungano kwa hali ilivyo sasa hakuna ambaye anaijua. Baadhi ya wataalamu wamekuwa wakitaja idadi inayotofautiana kwa mujibu wa unyumbuaji wa mambo hayo kutokana na orodha ya Mambo 22 yaliyo ndani ya Katiba hivi sasa ambapo awali kabisa yalikuwa ni Mambo 11 kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano.

Dhana ya kuimarisha Muungano siku zote imekuwa ni kumega mambo kutoka mamlaka ya Zanzibar na kuyatia katika Muungano, kwa maana nyengine ni kuongeza nguvu za Muungano na kuidhoofisha Zanzibar ndiko maana halisi za kuimairisha Muungano.

Katika umegaji huo Zanzibar imebakia hivi sasa gamba tupu kwa sababu mambo yaliotiwa katika Orodha ya Mambo ya Muungano ni yale ambayo ndio ya msingi kuiwezesha nchi kusimama na kukosekana kwayo basi nchi hunywea na Zanzibar imenywea kiuchumi kwa kuondoshwa mambo hayo kutoka milki yake.

Hata pale ambapo Zanzibar imejaribu kusimamia mamlaka yake ambayo kwa makosa yametiwa katika Orodha ya Mambo ya Muungano kama suala la Ushirikiano wa Kimataifa, kupitia juhudi za kutaka kujiunga na Jumuia ya Kiislamu ya OIC hapo mwaka 1992, Rais wa Zanzibar Dk Salmin Amour alinyamazishwa.

Jamhuri ya Muungano ilitoa ahadi kujiunga na OIC kama Tanzania na sio kuiachia Zanzibar peke yake, lakini hilo hadi sasa halijaweza kufanyika.

Hali ya Zanzibar kukosa sifa ya kimataifa na hivyo kushindwa kujiunga na taasisi kama Shirika la Soka Duniani FIFA na mifano ambayo kila mara inakumbusha jinsi Zanzibar ilivyosalimisha mamlaka yake hayo ndani ya Muungano.

Kutoka Mambo 11 ya Muungano sasa yapo Mambo 22 ya Muungano na suala kuu hapa linalokuja ni jee uongezwaji wa mambo hayo yametimiza masharti ya uhalali mbali ya kwamba yamekuwa yakipitishwa na Bunge?

Muda mwingi imekuwa ikitolewa hoja kuwa Zanzibar imepoteza sifa ya kuwa dola na kukosa mamlaka ya kujiunga na jumuia za kimataifa na kuingia mikataba ya kimataifa na ambapo inaeleweka kuwa Muungano wa Tanzania uliundwa kwa misingi hiyo na wakati huo Zanzibar ilikuwa na mamlaka hayo, na kutokana na mamlaka hayo ndipo ikasalimisha katika Muungano orodha ya mambo 11 ya Muungano.

Hoja tunayotaka kutoa hapa ni kuwa kama Zanzibar ilishapoteza mamlaka yake ya kimataifa na kuingia kwenye mikataba ya kimataifa, sasa imewezekana vipi Zanzibar kutoa mambo yaliyo ndani ya mamlaka yake na kuyatia katika orodha ya Muungano, ilhali haina tena nguvu hizo?

Kwa hivyo katika mambo yalioyoongezwa likiwemo suala la Mafuta kwa Sheria No 48, 1968 na mengine yote yaliofuatia hayana na hayawezi kuwa na uhalali kwa sababu utaratibu wa kuchukua mamlaka hayo kutoka Zanzibar haungetosha tu kwa kupitisha sheria ya Bunge bali kurudi kwa Zanzibar wenyewe kutaka ridhaa yake, jambo ambalo halikufanywa kwa sababu ya kukosekana utaratibu wa kufanya hivyo ndani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

Uvurugaji wa Mambo ya Muungano unaonekana pia katika suala la Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano katika Mkataba wa Muungano ambapo ametajwa kwa jina kuwa angekuwa Rais wa Zanzibar Abeid Amani Karume. Na akatumikia nafasi hiyo Aboud Jumbe na Ali Hassan Mwinyi, bila ya mabadiliko katika Mkataba wa Muungano ambao ulimtaja Rais Abeid Karume kwa jina.

Katika kipindi cha 1985-1995 ambapo Rais Ali Hassan Mwinyi alikuwa madarakani kwenye nafasi ya Urais wa Tanzania, Zanzibar haikutoa Makamo wa Rais.

Mabadiliko ya kumuondoa Rais wa Zanzibar kuwa Makamo wa Rais wa Tanzania yalifanywa kikatiba mwaka 1992 wakati Tanzania ilipoingia katika Uchaguzi Mkuu wa 1995 ambapo mfumo wa Mgombea Mwenza ulianzishwa kwa kila chama kutakiwa kuwa na Mgombea Mwenza anaetoka pande tofauti na Mgombea Urais wa kila chama.

Mabadiliko hayo yanakosa uhalali wa kisiasa kwa sababu ile ile ambayo tumeitoa hapo juu kwamba kama kulikuwa na haja ya kufanya mabadiliko ya msingi kama hayo ilipaswa kurudi katika Mkataba wa Muungano.

Lakini pili kumuondoa Rais wa Zanzibar kuwa Makamo wa Rais ni kuvunja msingi muhimu wa Muungano na pia ni kuondosha kiungo cha muhimu na lazima cha Zanzibar katika Muungano ambapo hivi sasa Makamo Rais wa Tanzania anaechaguliwa kwa njia ya Mgombea Mwenza hana uhusiano wowote na Mfumo wa Kiserikali wa Zanzibar.

Cha muhimu pia ni kuwa Makamo wa Rais wa Tanzania hana uhalali wa moja kwa moja wa kisiasa na baraka za Wazanzibari kwa sababu hakupigiwa kura na hivyo hawezi kuwa sauti yao katika jambo lolote la Muungano kwa sababu hakuwa na sera zozote juu ya Zanzibar ambazo ametumwa na Wazanzibari akazisimamia. Kosa kubwa ambalo limefanyika na linaendelea kufanyika ni kutouheshimu Mkataba wa Muungano, na badala yake kuipa mamlaka katiba ambayo pia inautata kwa kukosa uhalali katika uundaji wake.

Hii pia ni sababu muhimu sana ya suala la Muungano kujadiliwa kwa undani wakati wa Mjadala wa Katiba utakapokuwa unaendelea.

Makala haya yametolewa katika kitabu kilichoandaliwa na Baraza la Katiba Zanzibar 2012
 
Back
Top Bottom