Lady Whistledown
JF-Expert Member
- Aug 2, 2021
- 1,024
- 1,618
PICHA: MTANDAO
Baadhi ya wanachama wa Chama cha Wajane wakimsikiliza Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum, Dk Doroth Gwajima wakati akizindua chama hicho tawi la Dar es Salaam.
WAJANE wanaongezeka kwa kasi nchini, Chama cha Wanawake Wajane Tanzania (CCWWT) kimebainisha.
Katika mazungumzo na mwandishi wa habari hizi, Katibu wa chama hicho, Sabrina Tenganamba amesema wamebaini kuwapo kasi ya ongezeko la wajane, hali aliyoitafsiri ni ishara ya kuwapo vifo vingi vya wanaume nchini.
Sabrina anasema wameanza utafiti kubaini kiini cha vifo vingi vya wanaume; kwanini kesi za mirathi zinakaa muda mrefu mahakamani na kwanini wajane wanashindwa kujisimamia wenyewe kiuchumi.
Licha ya kushika nafasi ya sita nchini kwa kuwa na idadi kubwa ya watu, ukiwa na watu 2,989,299, Sabrina anautaja Mkoa wa Kagera kuongoza kuwa na wajane wengi walio katika chama hicho.
Matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi 2022 yanaonesha Kagera inazidiwa kwa idadi ya watu na mikoa ya Dar es Salaam (5,383,728), Tabora (3,391,679), Mwanza (3,699,872), Morogoro (3,197,104) na Dodoma (3,085,625).
Katika mazungumzo na Nipashe,
Sabrina anabainisha kuwa Mkoa wa Kagera una wanachama wengi wanaofikia 32,000 kati ya 148,000 wenye kadi maalum za chama chao katika mikoa 16 nchini.
KULIKONI KAGERA?
Sabrina anasema kuna sababu nyingi zinazochangia changamoto hiyo mkoani Kagera, akiutaja umekumbwa na madhila mengi kama magonjwa ya kuambukiza ukiwamo Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI); Virusi vya UKIMWI (VVU) viliingia nchini kupitia mkoa huo na ndio ulioathirika zaidi.
Kuhusu vifo vitokanavyo na UKIMWI kuwa vingi zaidi kwa wanaume kuliko wanawake, Mratibu wa Kudhibiti UKIMWI Mkoa wa Manyara, Dk. Charles Shija, anasema wanaume wanaongoza kwa vifo vitokanavyo na UKIMWI kulinganisha na wanawake kwa sababu si wepesi wa kutaka kujua hali zao kiafya, hivyo wanapofika hospitalini au kituo cha afya hujikuta virusi vimeshaingia kwenye hatua ya pili.
“Kwahiyo, wanaume wengi hugundulika kipindi ambacho virusi vimeingia katika hatua ya UKIMWI. Ndio maana wanawake wanaongoza kwa maambukizi ya VVU, lakini wanaume wanaongoza kwa vifo vitokanavyo na UKIMWI,” anasema.
Ni hoja inayoungwa mkono na Nyangusi Laiser, Ofisa Ufuatiliaji na Tathmini wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS), anayebainisha kwamba, mwaka 2020 Tanzania ilikuwa na maambukizi mapya ya VVU kwa watu 68,000. Kati yao 37,000 ni wanawake (asilimia 54.4) na wanaume 21,000.
Vilevile, Meneja Mfuko wa Udhamini wa Kudhibiti UKIMWI Tanzania (ATF), Peter Kivugo, alikaririwa na Nipashe mwaka juzi akisema, “Vifo vitokanavyo na magonjwa nyemelezi kwa wanawake vimepungua, lakini kwa wanaume vinapanda.
“Wengi wanakufa mapema kutokana na kushindwa kuzingatia maelekezo ya dawa na kujizuia katika tabia hatarishi ambazo zinasababisha kupata maambukizi mapya na magonjwa mengine ya zinaa,” alisema.
Kivugo alirejea takwimu za vifo vitokanavyo na UKIMWI kwa mwaka 2019, akibainisha vilikuwa 21,526 kwa watu wenye umri kuanzia miaka 15, wanaume wakiwa 12,225 (asilimia 56.8) na wanaume 9,304 huku watoto chini ya miaka 15 vilikuwa 5,900 na hivyo kufanya jumla ya vifo 27,429.
Unaporejewa ufafanuzi wa Katibu wa CCWWT, Sabrina, mbali na changamoyo ya VVU na UKIMWI, Mkoa wa Kagera pia unakabiliwa na changamoto za mila na desturi ambazo zinamweka hatarini zaidi mwanamume kulinganisha na mwanamke, ikiwamo kurithi wajane.
Sabrina anataja mikoa mingine yenye wanachama wengi wajane ni Iringa (29,000) na Mbeya (27,000).
Chanzo: Nipashe