Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,890
- 6,898
Kushoto (CAG), Ludovick Utouh Kulia Speaker Anne Makinda
Malipo hewa kwa wabunge yabainishwa
Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, (CAG), Ludovick Utouh, amebaini kulipwa kwa posho ya kujikimu Sh. 6,960,000 wabunge wakati hawakuwa mjini Dodoma.
Hayo yapo katika ripoti ya ukaguzi kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni mwaka jana, iliyowasilishwa katika mkutano wa saba wa Bunge. Pia alisema Sh. 20,915,126 zililipwa kwa wafanyakazi kinyume cha kanuni za Bunge na mwongozo wa utumishi.
Utouh alisema uongozi uliripoti kuwepo kwa madeni katika taarifa ya fedha ambayo ni Sh. 209, 010,235. Alisema madeni hayo ni kinyume cha mfumo wa bajeti ambayo unatumiwa na serikali.
Aidha, malipo yenye thamani ya Sh. 163,195,130.34 hayakuwa na nyaraka zinazostahili kama kanuni ya 94 (4) ya kanuni ya fedha za umma ya mwaka 2001. Pia ukaguzi huo umebaini posho za muda wa ziada wa kazi na posho nyingine zinazofikia Sh. 94,000,000 zililipwa kwa wafanyakazi wa Bunge.
Pia alisema madurufu ya safari (imprests) yenye thamani y a Sh. 65,803,144 hayakurudishwa kwa mwaka mzima kinyume na kanuni namba 103 (1) (7) ya kanuni ya fedha za umma ya mwaka 2001 ambayo inataka madurufu ya awali kurudishwa kabla ya kutoa mapya.Aliongeza kuwa marejesho yanatakiwa kurejeshwa siku 14 tangu mfanyakazi aliporejea kutoka safari ambayo aliombea madurufu. Ripoti hiyo imeonyesha kuwa matumizi ya sh 170,858,030, vocha za malipo zilikosekana.Katika ripoti hiyo kunabainisha kuwa uongozi wa Bunge ulinunua mashine ya kuchapisha kwa gharama ya sh 370,019,894 lakini haikufanya kazi.
Hivyo, ilisababisha uongozi wa Bunge kukodisha mashine nyingine kwa malipo ya Sh. 190,480,496 kwa mwaka. Hali kadhalika uongozi wa Bunge, haukuweka kumbukumbu sahihi kama vile za orodha ya mali zisizohamishika hali inayosababisha mapungufu mbalimbali.Alizitaja kuwa ni magari mawili yaliyosajiliwa kwa namba STK 8590 aina Toyota Land Cruiser Hardtop na STK 3039 Toyota LandCruisser hazikuwekwa katika orodha ya mali zisizohamishika. Magari hayo yalishushwa thamani ya mali kwa kuwekwa katika taarifa ya fedha.