Ningependa kujua haswa nini chanzo cha kutokea kwa bonde la ufa, athari zake ni nini kwa nyakati zilizopita na hizi tulizo nazo na zijazo.
Kama lisingetokea hilo bonde la ufa nini kingetokea na nini kitatokea baada ya kutokea bonde la ufa.
Bonde la ufa ni eneo la ardhi au bahari linalotitia chini baada ya mabamba mawili au matatu ya ardhi kila moja kujivuta upande wake au kupasuka. Bamba maana yake ni pande kubwa la mwamba hasa sehemu ya juu ( Earth's lithosphere) ambalo huelea juu ya bamba lile linalochemka kwa joto kali (asthenosphere). Toka Dunia kuumbwa ina mabamba 7 ambayo ndiyo huunda sehemu ya juu ya dunia
Mabamba haya kila moja lipo kwenye mwendo aidha kujivuta au kusogeleana na bamba mwenzake, na kitendo hiki ndicho husababisha vitu vifuatavyo kutokea: mabonde ya ufa, milima ya volcano, baadhi ya maziwa, chemichemi za maji ya moto, matetemeko ya ardhi nk.
Bonde la ufa hutokea baada ya bamba moja na jingine kuachana, kila mwaka mabamba haya huachana kwa sentimita au milimita kadhaa na kitendo hiki kinapofanyika kwa mamilioni ya miaka matokeo yake ndiyo tunayoyashuhudia hapo juu, milima, mabonde ya ufa, nk. Mabonde ya ufa hutokea pia baharini na wataalamu wanasema kuwa baharini ndiko kulipo na mabonde ya ufa makubwa na milima mikubwa kuliko hata ardhini. Yote yanayotokea juu ya ardhi na baharini pia ni hivyohivyo.
Dunia ina mabonde ya ufa kadhaa lakini lililokuwa maarufu zaidi na ambalo bado lipo hai(active) nikiwa namaanisha linaendelea kuongezeka siku hadi siku ni lile la Afrika ya Mashariki ambalo na sisi ndimo tulipo na mlima wetu wa Kilimanjaro. Bonde hili limeanzia kule Mashariki ya kati nchi za Lebanon na Israel na kuishia nchi ya Msumbiji. Wanajiolojia wanasema miaka mamilioni yajayo bonde hili litasababisha eneo zima la Pembe ya Afrika, zaidi Somalia na Djibout kugeuka kisiwa baada ya maji ya bahari kufurika katika bonde hili litakapokuwa limetanuka vyakutosha.
Ushahidi wa 'theory' hii ni Mabara 7 tunayoyaona leo hii, inasemekana Dunia mamilioni ya miaka huko nyuma lilikuwa ni pande moja tu kubwa la ardhi (PANGAEA) na kweli hata unapojaribu kucheki ramani ya dunia, ukilisogeza bara la Africa karibu na mabara ya Amerika ya Kusini na Kaskazini utagundua yanafiti pamoja kama vile ni mtu aliyakata kwa kisu.
Mamilioni ya miaka nyuma pia Rasi ya Uarabuni ambayo leo hii imetenganishwa na Afrika kwa Red sea zamani ilikuwa kitu kimoja mpaka pale maji yalipofurika katika bonde la ufa lililokuwa kati ya bara Arabu na Afrika pakatokea red sea.
Ukizidi kuja huku nyuma ya red sea ndipo unakutana na Bonde la ufa la Afrika ya Mashariki ambalo nalo kadiri miaka inavyosogea mbele nalo linatanuka polepole na itafika mahali bamba la somalia linalojumuisha pembe nzima ya afrika kutenganishwa kabisa na maji ya bahari na kugeuka kuwa kisiwa mithili ya Madagaska huku kikiacha maeneo mengine ya Afrika yakiwa yenyewe.
Athari za bonde la ufa ndiyo kama nilizotaja na kwa wakati ujao kama unavyoona ni kuendelea kubadilika kwa sura/uso wa dunia tu na wala siyo kupungua au kuongezeka chochote. Ni sawa na mdau mmoja alisema amesikia hata baadhi ya visiwa kama Zanzibar kuna muda huko mbele mamilioni ya miaka yajayo vitatoweka, yaweza kuwa kweli lakini pia kumbuka kinapomezwa kisiwa mahali fulani pia kuna sehemu nyingine patainuka au kuibuka kisiwa kipya.
Mabadiliko haya hutokea taratibu sana na inawezekana tukio kama la kugawanyika Bara likachukua milioni kadhaa za miaka, si leo wala kesho hivyo kama unasoma hapa usije ukakosa usingizi ukiwaza mambo haya. Si ajabu hata vitukuu na vilembekeze vyako visijekuyashuhudia.
Bonde la ufa kubwa zaidi halipo hapa Duniani , lipo kwenye Sayari ya Mars